STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, April 15, 2011

Matumla kuzichapa Dodoma




BINGWA wa zamani wa Dunia wa Ngumi za Kulipwa nchini, Rashid Matumla 'Snake Man' anatarajiwa kupanda ulingoni siku ya Pasaka kuzipiga na Mkenya, Joseph Odhiambo katika pambano litakalofanyika mjini Dodoma.
Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO, Yasin Abdallah 'Ustaadh', alisema pambano lisilo la ubingwa la uzani wa Middle, litakuwa la raundi 10.
Ustaadh, alisema lengo la pambano hilo ni kusaidia kuinua mchezo wa ngumi mkoani humo sambamba na kuwapelekea burudani wakazi wa mji huo ambao watakuwa wakisherehekea sikukuu ya Pasaka.
"Dodoma imekuwa ikipelekewa burudani za muziki, mpira na kadhalika, lakini mchezo wa ngumi kwa muda mrefu haujafanyika mjini humo na TPBO tumeamua kuwapelekea pambano hilo kubwa kama njia ya kuhamasisha mchezo huo na kuwaburudisha wakati wa sikukuu," alisema.
Alisema maandalizi ya pambano hilo litakalodhaminiwa na mfanyabiashara maarufu wa mjini humo, Moshi Semayu yamekamilika na watautangazia umma pambano hilo litafanyikia wapi, ingawa alikuwa na hamu lifanyike uwanja wa Jamhuri, mjini humo.
Aliongeza, baada ya pambano hilo la Dodoma, TPBO ilikuwa itafanya mipango ya kuandaa michezo mingine ya ngumi za kulipwa katika mikoa ya Mbeya, Iringa, Singida na kadhalika kwa lengo la kuuhamasisha mchezo huo katika mikoa hiyo.
Matumla, aliyewahi kuwa bingwa wa dunia wa WBU, alisema yupo fiti kumchapa Odhiambo, ili kudhihirisha kuwa yeye bado wamo katikia mchezo huo uliomjengea sifa ndani na nje ya nchi.

No comments:

Post a Comment