STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, March 9, 2014

Simba katika mtihani mgumu Mbeya leo

Simba
Wenyeji Prisons
SIMBA ambayo haijashinda katika mechi nne mfululizo, inatakiwa kuifunga Prisons kwenye Uwanja wa Sokoine leo ili kubakiza hai matumaini yake ya kutokosa mara mbili mfululizo kwa mara ya kwanza, moja ya nafasi mbili za juu kwenye msimamo wa ligi kuu ya Bara.
Simba ambayo ilishika nafasi ya tatu msimu uliopita nyuma ya Yanga na viongozi wa ligi kuu msimu huu Azam, ipo hatarini kukosa tena moja ya nafasi mbili za juu kutokana na kuachwa na Azam kwa tofauti ya pointi tano zikiwa zimebakiwa mechi sita.
Wekundu wa Msimbazi pia wameachwa kwa tofauti ya pointi tatu na Yanga ambayo ina mechi tatu mkononi katika nafasi ya pili. Azam ina mechi mbili za ziada.
Hivyo ni ushindi tu ambao utaendeleza ndoto ya Simba ya kucheza angalau Kombe la Shirikisho la klabu za Afrika mwakani, lakini inakutana na Prisons ambayo imeshinda mechi tatu mfululizo zilizopita. 
Kocha wa Prisons, David Mwamaja alinukuliwa toka Mbeya akisema kuwa amekiandaa vyema kikosi chake kuhakikisha kinaibuka na ushindi dhidi ya Simba ili kiendelee kusalia kwenye ligi kuu msimu ujao.
Licha ya kutopoteza mchezo wowote katika mechi sita za duru la pili, Prisons ipo pointi nne tu juu ya janga la kushuka daraja na ushindi dhidi ya Simba leo utaisaidia kupiga hatua kubwa katika kutimiza lengo la klabu na Mwamaja.
“Tunaiheshimu Simba kwa sababu ni klabu kongwe nchini lakini hatuiogopi na kamwe wasitarajie mteremko katika mechi yetu ya kesho (leo).," alisema Mwamaja.
"Tunazihitaji pointi tatu muhimu dhidi yao ili tujiweke sehemu nzuri katika msimamo wa ligi.”
Naye Zdravko Logarusic, kocha mkuu wa Simba, alisema ana matumaini makubwa ya kushinda mechi ya leo.
Alisema kuifunga Prisons ni sehemu ya mikakati ya kushinda mechi zao zote sita zilizobaki ili kuwa katika nafasi za juu kadri iwezekanavyo katika msimamo wa ligi hiyo.
Mechi nyingine itakayopigwa leo ni kati ya JKT Ruvu itakayoikaribisha Mtibwa Sugar kwenye uwanja wa Chamazi ikiwakosa wachezaji wake kadhaa akiwamo Mussa Mgosi na Salvatory Ntebe walioadhibiwa na TFF

No comments:

Post a Comment