STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, August 1, 2013

Watu 7 wanusurika kufa ajali ya Ndege Longido

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEj1DmrEfl1anJUzU-aq9ZKrxtChtAM8ILw5c0EHEak7ECequsrmy29HWPXmMZNPDJXbucKkDbGvTUoWDUMGpujXOW5EwFxYaW5Hop0RhIDE_GbqWx51fQ1sCNL73rjzBO-CJLGm2Kf4fqBN/s320/Catalina+Aircraft+-+Canadian+Vickers+PBY-5A+Canso+-+G-PBYA+-+5242+NET.jpgWATU 7 wamenusurika kupoteza maisha baada ya ndege waliyokuwa wakisafiria kuanguka na maeneo ya Longido Mkoani Arusha juzi Jumanne.

Duru za Jeshi la Polisi mkoa wa Arusha zimesema majira ya saa 8 za mchana katika kijiji cha Merugwayi ndege aina ya CESS iliyokuwa na namba za usajili TN/4206 ikiwa na marubani wawili ilipata ajali.

Taarifa hiyo ya Jeshi la Polisi imetaja chanzo cha ajili hiyo kuwa ni upepo mkali uliosababisha ishindwe kupaa katika uwanja wa ndege wa Merugwayi umbali wa mita 120 na kuanguka.

Habari zaidi zinasema ndege hiyo iliondoka Arusha majira ya saa 2 za asubuhi kuelekea wilayani Ngorongoro na baadaye ilirudi tena Arusha ikiwa na Abiria watano ilipofika katika uwanja huo ilishuka kwa ajili ya kuchukua mgonjwa na ilipojaribu kuruka ilishindwa, na kupoteza mwelekeo.

Marubani waliokuwemo katika ndege hiyo ni Jaffer Shakir (23) na Patten Patrick (65).

Hata hivyo Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha ACP Japhet Lusingu amewataja majeruhi kuwa Nalepo MamaSita (38), Anna Laizer (21), Naninkoi Laizer (7), Benson Mukoya (28), Krizosto Malima (30).

Rubani wa ndege hiyo Jaffer Shakir ameumia  vibaya sehemu za usoni na amelazwa katika Hospitali ya Selian, Jijini Arusha kwa matibabu zaidi huku wengine wakiruhusiwa.  
 
Jaizmalaleo

Polisi wauwa jambazi mkoani Iringa, yanasa wahamiaji haramu toka Ethiopia

MTU anayeshukiwa kuwa jambazi ameuawa na mwingine akikamatwa wakati wakivamia duka la Santino Mdesa katika kijiji cha Mkonge kilichopo katika Wilaya ya Mufindi mkoani Iringa.
Aidha wahamiaji haramu watano kutoka nchini Ethiopia wametiwa mbaroni kwa kosa la kuingia nchini kinyemelea ikiwa siku chache tangu Rais Jakaya Kikwete kuchimba mkwara juu ya wahamiaji haramu kuzidi kuongeza nchini.
Akizungumzia tukio hilo ujambazi, Kamanda wa Polisi mkoa wa Iringa ACP Ramadhani Mungi amesema majambazi hao walifyatua risasi hewani ambapo wananchi walipobaini uwepo wa tukio hilo la Uharifu walizingira eneo hilo ambapo majambazi walitambua mbinu hizo na kukimbia.
Aidha kamanda Mungi amesema wananchi kwa kushirikiana na askari polisi waliwakimbiza majambazi hao na baada ya kuzidiwa nguvu, majambazi walitupa bunduki aina ya SMG iliyokuwa na Lisasi 21, na kisha kutelekeza usafiri wao wa Pikipiki, huku askari wakifanikiwa kumpiga kwa risasi mguuni jambazi mmoja aliyekufa wakati akipelekwa kupata matibabu.
Mungi amesema pia Polisi wamefanikiwa kumkamata mwananchi wa kijiji cha Kitayawa katika Wilaya ya Iringa ambaye amekuwa akitengeneza Bunduki za kienyeji.
Katika tukio lingine kamanda Mungi amesema, wamewakamata wahamiaji haramu watano kutoka nchi ya Ethiopia ambao walikuwa wamejificha katika poli la mashamba ya kijiji cha Mazombe, katika Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa, na kuwa wahamiaji hao walikuwa wanaelekea nchini Afrika Kusini.
Akithibitisha kukamatwa kwa wahamiaji hao haramu, ofisa uhamiaji mkoa wa Iringa Ali Nassor amesema wahamiaji hao haramu wakiethiopi wapo chini ya ulinzi kwa hatua zaidi.

Bondia Mtanzania alivyomchakaza Mthailand


 Bondia Mtanzania Omari Kimweri  anayefanya shughuli zake Australia kulia akinyooshwa mkono juu kuashira ushindi wake baada ya kumtwanga  Ekkalak Saenchan  wa Thailand kwa KO raundi ya kwanza.

Bondia Mtanzania Omari Kimweri  (kulia) akimsukumia makonde mazito mfululizi bondia Ekkalak Saenchan  wa Thailand na kufanikiwa kumtwanga kwa kwa KO raundi ya kwanza mwishoni mwa wiki iliyopita.
Bondia Mtanzania Omari Kimweri  anayefanya shughuli zake Australia akimsikilizia mpinzani wake baada ya kumtwanga kumi nzito na kuhesabiwa wakati wa mpambano wake ambapo mpinzani wake toka Thailand alishindwa kuendelea na hivyo kutangazwa mshindi wa KO ya raundi ya kwanza

Tuesday, July 30, 2013

Mwandi kuwakutanisha wadau wa Majimaji

Add caption
Kampuni ya Tanzania Mwandi ikishirikiana na Majimaji FC, imeandaa mkutano wa wadau wote wa soka mkoani Ruvuma chini ya Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Mh. Said Mwambungu, mkutano utakaofanyika katika ukumbi wa Centenary tarehe 10. 08. 2013, kuanzia saa 2 asubuhi.

Lengo kubwa la mkutano ni kurejesha makali ya 1985, 1986 na 1998 kwa klabu ya soka ya Majimaji kwa kuiunda upya kiuchumi chini ya mfumo wa Kampuni, kuijengea uwezo wa kimkakati na kiuendeshaji ili iweze kushiriki kwa mafanikio Ligi Daraja la Kwanza na hatimaye kurejea Ligi Kuu msimu ujao.

Itakumbukwa kuwa Majimaji FC ni klabu ambayo imezalisha magwiji wengi wa soka Tanzania kama Abdala Kibadeni 'Mputa', Madaraka Suleimani 'Mzee wa Kiminyio', Peter Tino, Steven Mapunda 'Garincha', Hamis Gaga, Idd Pazi, Omary Hussein 'Machinga' na Mdachi Kombo na ni klabu ambayo ilikuwa na ushindani mkubwa kwa Simba na Yanga.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotumwa kwa vyombo vya Habari na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Tanzania Mwandi, Bwana Teonas Aswile amewaalika wafadhili na wadau wote wenye mapenzi mema na Majimaji FC kujitokeza na kushiriki katika zoezi la mjadala wa muundo mpya wa Majimaji na hata kununua hisa kwani sasa Majimaji Kampuni haitakuwa na longolongo zozote.

“Binafsi nawahimiza wafadhili wa soka kwamba hii ni fursa adimu nyingine ya kuwekeza fedha zao mahali salama. Majimaji itakuwa ikiendeshwa kikampuni na miradi mbalimbali itaanzishwa na klabu ikiwemo upande wa ukandarasi na kuuza wachezaji nje ya nchi. Kwahiyo atakayenunua hisa atafaidika mara mbili.” alisema Teonas Aswile.

Akizungumzia wachokoza mada wakuu wa Majimaji Revival Conference, Aswile amesema kuwa Wakala wa Kimataifa wa FIFA na Mwanasheria Maarufu nchini, Dkt Damas Ndumbaro pamoja na Bwana Silas Mwakibinga, mhasibu na mdau mkubwa wa michezo ambaye ameshashika nafasi mbalimbali.

Kwa sasa maandalizi kwaajili ya Mkutano wa Wadau wa Majimaji FC “Wanalizombe” yanaendelea vyema na wanaohitaji taarifa wanaweza kuwasiliana na Bwana Nasib Mahinya kwa 0655 468800.

Pia viongozi wa Majimaji FC kama Katibu Mkuu Majimaji FC 0752 622887

TFF kuwataini Mawakala wa wachezaji, waamuzi nao kupimwa


Na Boniface Wambura

MTIHANI wa uwakala wa wachezaji (players agent) na uwakala wa mechi (match agent) wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) utafanyika Alhamisi ya Septemba 26 mwaka huu saa 4 kamili asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Kutakuwa na jumla ya maswali 20 kwenye mtihani huo, 15 yanatoka FIFA kuhusiana na kanuni za kimataifa za mpira wa miguu na matano yatatoka TFF kuhusiana na kanuni mbalimbali zinazotawala mchezo huo nchini.

Kwa ambao wangependa kufanya mtihani huo utakaokuwa katika lugha ya Kiingereza ambayo ni moja kati ya lugha nne rasmi za FIFA wanatakiwa kujisajili TFF kwa ada ya dola 50 za Marekani ambapo watapewa utaratibu na maeneo ambapo mtihani huo unalenga.

Mtihani huo utafanyika saa 4 kamili asubuhi, na muda wa kufanya mtihani hautazidi dakika 90.

Mpaka sasa Tanzania ina mawakala watano wa wachezaji wanaotambuliwa na FIFA. Mawakala hao ni John Ndumbaro, Mehdi Remtulla, Ally Saleh, Yusuf Bakhresa na Said Tully.

Wakati huo huo Waamuzi wote wa daraja la kwanza (Class I) wanaotaka kuchezesha Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu wa 2013/2014 wanatakiwa kuhudhuria mtihani wa utimamu wa mwili (physical fitness test) utakaofanyika katika vituo viwili.

Mtihani huo utafanyika Agosti 12,13 na14 mwaka huu katika vituo vya Dar es Salaam na Morogoro. Kituo cha Mwanza kitahusisha waamuzi kutoka mikoa ya Geita, Kagera, Katavi, Kigoma, Manyara, Mara, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Singida na Tabora.

Kituo cha Dar es Salaam kitahusisha waamuzi kutoka mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Kilimanjaro, Lindi, Mbeya, Morogoro, Mtwara, Njombe, Pwani, Ruvuma na Tanga.

Washiriki wote wanakumbushwa kuwa ni lazima wafuate utaratibu huo wa vituo, na si vinginevyo. Pia waamuzi waliofungiwa (sio maisha) wanatakiwa kushiriki katika mtihani huo.

Makundi ya FDL haya hapa, ratiba kutoka Agosti 14


Na Boniface Wambura
Ratiba ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu wa 2013/2014 inayoshirikisha timu 24 zilizo katika makundi matatu zikicheza kwa mikondo miwili (nyumbani na ugenini) inatarajiwa kutolewa Agosti 14 mwaka huu.

Kundi A linaundwa na timu za Burkina Moro ya Morogoro, JKT Mlale (Ruvuma), Kimondo SC (Mbeya), Kurugenzi Mufindi (Iringa), Majimaji (Ruvuma), Mkamba Rangers (Morogoro), Polisi (Iringa) na Polisi (Morogoro).

African Lyon (Dar es Salaam), Friends Rangers (Dar es Salaam), Green Warriors (Dar es Salaam), Ndanda (Mtwara), Polisi (Dar es Salaam), Tessema (Dar es Salaam), Transit Camp (Dar es Salaam) na Villa Squad (Dar es Salaam) zinaunda kundi B.

Timu za kundi C ni JKT Kanembwa (Kigoma), Mwadui (Shinyanga), Pamba (Mwanza), Polisi (Dodoma), Polisi (Mara), Polisi (Tabora), Stand United (Shinyanga) na Toto Africans (Mwanza).

Tunapenda kukumbusha kuwa dirisha la usajili kwa madaraja yote ni moja ambapo usajili wa hatua ya kwanza ni kuanzia Juni 15 hadi Agosti 3 mwaka huu wakati hatua ya pili ni Agosti 14 hadi 29 mwaka huu. Dirisha dogo litafunguliwa Novemba 15 hadi Desemba 15 mwaka huu.

Hizi ndizo sababu zilizoifanya Yanga kuidindia Azam Media



















Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji (katikati) akiongea na waanidishi wa habari, Makamu mwenyekiti Clement Sanga (kushoto) na mjumbe wa kamati ya utendaji Mark Anthony (kulia)



















UONGOZI wa klabu ya Yanga jana umefanya mkutano na waandishi wa habari juu ya urushwaji wa michezo yake ya Ligi Kuu katika kituo cha luninga cha Azam ambacho kimeingia makubaliano na kamati ya Ligi Kuu  kuonyeshwa michezo yote ya ligi kwa kipindi cha miaka miatatu (3).
Akiongea na waandishi wa habari mwenyekiti wa klabu ya Yanga Yusuf Manji amesema uamuzi wa kamati ya ligi kuingia mkataba na kituo cha Azam Tv bila ya kuwashirikisha wahusika wenyewe ambao ni vilabu vishiriki haukuwa sawa.
Sisi kama klabu ya Yanga tulikaa kikao cha kamati ya utendaji na kuona taratibu za kupewa haki ya matangazo kwa kampuni ya Azam haikua sawa, sisi viongozi wa kalbu ya Yanga hatukushirikishwa katika mchakato huo hivyo tukaona ni vema tuje kwa vyombo vya habari tuulezee umma juu ya maazimio ya kamati ya utendaji.
Ifuatayo ni taarifa kamili kwa vyombo vya habari: 
YAH: URUSHWAJI KATIKA TELEVISHENI MICHEZO YA YANGA.

Hivi karibuni, Tanzania Football Federation (TFF)  iliunda Tanzania Premier League chini ya Bodi ya mpito Bodi ya TPL ambayo ni msimamizi mpaka hapo Bodi itakayokuwa imechaguliwa kidemokrasia. Bodi hii imeamua peke yake kuingia katika mkataba wa miaka 3 (mitatu) na kampuni inayoitwa Azam Television (ambayo ina  mapromota wale wale wanaomiliki Azam Football Club). Makubaliano ambayo Bodi ya TPL inatarajia kuingia na Azam Television, Kamati ya Utendaji ya YANGA inalipinga kwa nguvu zote katika misingi ifuatayo:

1. BODI YA TPL

1.1 Bodi iliyoko sasa hivi ni ya mpito ambayo ilitakiwa kutenguliwa na Bodi iliyochaguliwa kidemokrasia kwa kupitia uchaguzi wa tarehe  ……….. mwaka huu na haitakiwi kuingia katika mikataba a miaka mingi wakati inakaribia kuondoka katika ofisi.

1.2 Bodi ya TPL iliyoko sasa hivi haikuchaguliwa kidemokrasia.

1.3 Bodi ya TPL iliyoko sasa hivi haina mjumbe hata mmoja aliyeteuliwa kutoka YANGA.

2. UTARATIBU WA DUNIA NZIMA

2.1 Haijawahi kutokea katika ligi ya mpira wa miguu ya kisasa kulazimishwa kwa Klabu inayoshindana katika ligi kuachia haki zake za urushwaji wa michezo zichukuliwe na chombo cha habari cha Klabu ya upinzani. 

2.2 Mfumo (undertaking) ambao TPL inataka kuanzisha kwa njia ya kulazimisha mkataba kwa YANGA iachie  urushwaji wa michezo yake ya soka yarushwe na Azam TV unatishia sana uwepo wa msingi wa ushindani katika soka ya Tanzania.

2.3 Makubalianokati ya TPL na Azam Television kuhusu utaratibu wa malipo yanasemakwamba Klabu ya YANGA na Klabu zingine zitakazoshiriki katika Ligi Kuu ya Tanzania  watapata mgao sawa wa mapato ya urushwaji wa michezo hii, ambayo YANGA inapinga kwa sababu kama inavyofanyika duniani kote kwenye ligi zilizofanikiwa (angalau) kutofautisha mgawanyo wa mapato kati ya timu kufuatana na matokeo ya mwisho wa ligi.

2.4 Kamati ya Utendaji ya YANGA siyo tu haikubaliani na mgawanyo sawa wa mapato ambao hautofautishi kati ya timu ya kwanza katika ligi na timu ya mwisho katika ligi, lakini pia ukosefu wa viwango (premiums) vitakavyolipwa: 

2.4.1 Vilabu vya mpira vyenye ufuasi wa washabiki wengi; 

2.4.2 Vilabu vya mpira vinavyoendeshwa na Wanachama; 

2.4.3 Vilabu vya mpira visivyopata ruzuku kutoka Serikalini n.k.

3. MIGOGORO YA MASLAHI

3.1 Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Mpito ya TPL ni Mkurugenzi mwandamizi wa Makampuni ya Azam na  kwa hivyo mazungumzo ya siri kati ya Bodi ya TPL na Azam ni ya kutiliwa mashaka.

3.2 Makampuni ya Azam yana yanashindana kibiashara na makapuni mengi yakiwemo ya utengenezaji wa vinywaji baridi na imeonyesha huko awali inaweka “matakwa maalum” muhimu zaidi kuliko mprira  wa miguu, kama vile Azam F.C. hawashiriki katika Kombe la Tusker na kwa hiyo YANGA inakuwa na msimamo kwamba kwa Azam Television kupewa leseni ya kurusha matangazo ya mpira wa miguu inatishia biashara za washiriki wa sasa na wa baadaye wa YANGA.

3.3 Azam na YANGA wana uadui wa kimichezo. Kumbuka, wakati MRISHO NGASSA alipotaka kwenda YANGA, Azam F.C. walimkopesha kwa nguvu kwa Klabu ya Simba! Kwa hiyo YANGA itahatarika kwa matangazo yenye upendeleo kama Azam Television itarusha hewani michezo yake n.k.

4. KUTOKUWA NA UWAZI

4.1 Mkataba wa utangazaji wa miaka mingi unaotaka kuingiwa kati ya TPL na ambao badohaujarushwa Television ya Azam haukushindanishwa na vyombo vingi vya habari,  na vyombo ambayo wako tayari kwenye soka havikujulishwa kuhusu fursa hii au walizuiliwa kufikisha mapendekezo yao ya maombi ya haki za kurusha matangazo katika Ligi Kuu (Tanzania Premier League).

4.2 Ukosefu wa uwazi wa TPL unanonyesha kuwa MoU iliyokusudiwa kuwekewa saini na TPL haikufikishwa YANGA kwa ajili ya mapitio ya kisheria, licha ya YANGA kufanya ombi hilo kwaTPL.

5. MAZINGATIO YA KIBIASHARA 

5.1 Mamlaka ya kuamua mzozo wowote wa mkataba wa leseni ya utangazaji wa Ligi Kuu (Tanzania Premier Leagu) itakuwa ni Mahakama ya kisheria na siyo FIFA. TPL inasingizia  kwamba leseni ya matangazo ambayo inakusudia kufanya kuwa ni maagizo ya FIFA na kwa hiyo YANGA inapaswa kuukubali "lock, stock and barrel."

5.2 TPL inaelezea kimakosa makubaliano ya leseni ya urushaji  wa mchezo ya mpira inayotarajia kuingia na Television ya Azam kama "makubaliano ya udhamini" (“sponsorship agreement”) ambayo siyo sahihi, kwa sababu urushaji wa michezo ya mpira wa miguu ni biashara inayotokana na maslahi ya uhusiano na hivyo 
wahusika wote ni lazima wazingatie maslahi yao ya kifedha.

Kwa mfano, moja ya vyanzo muhimu vya mapato ya YANGA ni mapato ya kiingilio ya mlangoni yatokanayo na michezo ya mpira wa miguu ambayo urushwaji wa michezo hii itapunguza mapato haya. Kwa wastani michezo ya YANGA  Dar es Salaam huingiza makusanyo ya mlangoni shilingi milioni 50 kwa kila mchezo na hata kushuka kidogo kwa 25% katika mahudhurio ya mechi za YANGA zinafikia mara mbili ya mapendekezo ya mapato takribani Sh milioni 8.3 kwa mwezi kupokelewa na YANGA kutoka mradi wa kibiashara kati ya TPL na Azam Television. Kwa kuzingatia haya, kwamba hata siku za nyuma kama kulikutokea fursa ya kurusha mchuano wa mpira unapochezwa, wadau wote (Timu za mpira wa miguu, TFF na Mtangazaji)  walikuwa wanaafikiana kwanza kwa pamoja kuhusu mapato na mgawanyo wake.

Kamati ya Utendaji ya YANGA ina maoni kwamba makubaliano yoyote ya kibiashara yanayoihusu ni lazima iyalinde maslahi kifendha ya Klabu yake ambapo makubaliano ya TPL / Azam Television hayaangalii na kwa hiyo, Kamati ya Utendaji ya YANGA haitaki mchezo wake urushwe hewani na Azam Television.

Msisitizo wa TPL kuwa lazima Azam Television irushe hewani michezo ya YANGA linasikitisha. Kamati ya Utendaji ya YANGA haina tatizo na Vilabu vingine vya mpira wa miguu zikiruhusu michezo yao kurushwa na Azam Television ila haifurahii kuwa TPL inalazimisha YANGA kuonyesha mchezo wake wa Vodacom Premier League katika Azam Television.
......................
(YUSUF MANJI)
MWENYEKITI
YOUNG AFRICANS SPORTS CLUB
29 JULAI, 2013

Lionel Mess awafunika, Ribery, Ronaldo tuzo za Goal 50



 http://www.goolfm.net/wp-content/uploads/2013/07/messi-goal-50.jpg
MADRID, Hispania
LIONEL Messi ameshinda Tuzo ya Mwanasoka Bora wa Dunia ya ‘Goal 50’ inayotolewa na tovuti maarufu ya soka duniani ya goal.com baada ya kumaliza msimu mwingine huku akiandika rekodi mpya.
Mshambuliaji huyo wa kimataifa wa Argentina alitwaa tuzo hiyo kwa mara ya tatu baada ya kuandika rekodi ya mabao katika msimu ambao alivunja rekodi ya Gerd Muller iliyodumu kwa miaka 40 ya kufunga magoli 85 katika mwaka wa kalenda.
Messi mwenye miaka 26, alifunga magoli 91 mwaka wa 2012 na kuongeza jumla ya mabao yake akiwa ndiye mfungaji kinara mwenye mabao mengi zaidi katika historia ya Barcelona baada ya kufikisha magoli 313 katika michuano yote kufikia mwisho wa msimu uliopita.
Messi alifunga katika mechi ya 19 mfululizo kwenye mechi za La Liga, Ligi Kuu ya Hispania Machi 2013, hivyo kuwa mwanasoka wa kwanza katika historia kufunga mfululizo dhidi ya wapinzani wao wote katika ligi kuu ya soka la kulipwa.
Baada ya kupokea tuzo yake kutoka kwa mwakilishi wa Goal mjini Barcelona, Pilar Suarez, wakiwa kwenye uwanja wa mazoezi wa timu hiyo, Messi alisema: "Nimevutiwa sana na tuzo. Kama wachezaji, tunafanya kazi mwaka mzima ili kutwaa mataji kwa ajili ya timu, hatutafuti tuzo binafsi, lakini wakati zinapokuja huwa zinatutia moyo na kutuongezea nguvu ya kuendeleza kiwango."
Tuzo ya ‘Goal 50’ inachukuliwa kuwa moja ya tuzo zinazoheshimiwa sana katika michezo kwa sababu uteuzi wake hufanywa na tovuti kubwa zaidi ya soka duniani.
Kura hupigwa mwishoni mwa msimu wa ligi za nyumbani za nchi nyingi duniani na pia wa mechi za kimataifa.
Zaidi ya waandishi 500 wa tovuti ya Goal kutoka maeneo mbalimbali duniani hupiga kura kuchagua nyota 50-bora, hivyo kutoa nafasi kwa wachezaji wengi zaidi.
Messi ameibuka kinara wa orodha ya mwaka huu dhidi ya Franck Ribery aliyemaliza katika nafasi ya pili baada ya kuisaidia Bayern Munich kutwaa mataji matatu msimu uliopita likiwamo la Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya. Mshindi wa mwaka jana, Cristiano Ronaldo ametwaa nafasi ya tatu.

WASHINDI WOTE TUZO ‘GOAL 50’
2008     Cristiano Ronaldo
2009     Lionel Messi
2010     Wesley Sneijder
2011     Lionel Messi
2012     Cristiano Ronaldo
2013     Lionel Messi
----------

Mbunge Idd Azan ajisalimisha Polisi sakata la dawa za kulevya

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiqo_UzUC7Oj3-U_F2CfmGpkmKqrZGdPDockhjVaHNAiImTnm3jNqPIeSNi-p0PaFJPIhIaGEdiRQVC4IZ2lKgcTKWIakZ7YP-9KguLJWmkyOJRtvfE4V_0nWie2ZH_LhgpoKyaRZorsM-5/s320/Idd-Azan.jpg
Mbunge wa Kinondoni, Idd Azan
BAADA ya kutuhumiwa kuhusika na biashara ya dawa ya kulevya na barua iliyosambazwa mitandaoni inayodaiwa kuandikwa na mmoja wa wafungwa waliopo jela nchini Hongkong, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni kwa tiketi ya CCM, Idd Mohammed  Azan amejisalimisha Polisi.
Mbunge huyo ameamua kujisalimisha ofisi za Polisi kwa lengo la kutaka jeshi hilo lifanye uchunguzi ili kubaini ukweli wa tuhuma dhidi yake na iwapo atabainika ni kweli ni 'zungu la unga' basi sheria zichukuwe mkondo wake.
Azan alisema aliamua kwenda mwenyewe kutoa taarifa katika Kituo Kikuu cha Polisi Kati, jijini Dar es Salaam kutokana na ukweli tuhuma hizo zimemshtua mno.
"Nimeamua kwenda kituo cha polisi kwa ajili ya kutoa taarifa ili ufanyike uchunguzi wa jambo hilo na ukweli ubainike na hatua za kisheria zifuate juu yangu,"alisema Azan.
"Mimi sipo juu ya sheria , itakapobainika najihusisha na tatizo hilo, nichukuliwe hatua mara moja, na nitajiuzulu ubunge wangu,"alisisitiza Azan na kuongeza:
"Wapiga kura wangu wa Kinondoni pamoja na wananchi kwa ujumla inatakiwa waelewe kuwa barua hizo zina nia mbaya zenye lengo la kunichafua na kama kweli wana ushahidi wangetaja majina yao,"alinukuliwa Mbunge huyo.
Katika barua hiyo ambayo mwandishi wake hajitaji jina, wala kuwataja wafungwa wenzake kuonyesha ni kweli anawawakilisha wala kulitaja jina la mtu aliyemuingiza kwenye biashara hiyo au 'bosi' wake aliyembebesha dawa hizo kwenda nazo Hongkong, alimtaja Mbunge huyo na watu wengine kadhaa.
Hata hivyo baadhi ya watu walioiona barua hiyo yenye kurasa tano zilizotumwa nakala zake kwa vyombo vya habari wamekuwa na shaka nayo kwa vile inaacha maswali mengi ambayo yalipaswa kujibiwa na mfungwa huyo ikiwamo yeye ni nani, aliyemuingiza ni nani na bosi wake anaitwa nani ili iwe rahisi kuendana na uhalisi wa mantiki yake kwamba amejitoa mhanga kupiga vita dhidi ya dawa hizo haramu.

Aibu! Njemba lafungwa miaka 30 kwa kumlawiti, kumzalisha bintie

Yusufu Amani (39) aliyembaka mwanaye wa kumzaa kisha kumzalisha baada ya kutengana na mkewe Afungwa miaka 30
Hapa akijifunika sipigwe picha baada ya hukumu
Kulia ni mtoto aliyebakwa na baba yake kisha kuzalishwa akiwa na mtoto wake wakitoka mahakamani kulia ni mama mzazi wa binti aliyebakwa na kuzalishwa


MAHAKAMA ya wilaya ya Mbeya imemhukumu kwenda jela miaka 30 mkazi wa Isanga Mkoani hapa baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kumlawiti na kumzalisha binti yake wa kumzaa akiwa na miaka 15( jina linahifadhiwa).



Mwendesha mashitaka wa serikali  Archiles Mulisa  aliiambia mahakamani hiyo Mbele ya Hakimu Gilbert Ndeuruo kuwa Mshtakiwa huyo ni Yusufu Amani (39) anayedaiwa kumbaka mwanaye wa kumzaa kisha kumzalisha baada ya kutengana na mkewe.



Alisema kosa hilo ni kinyume cha sheria kifungu cha 154 (1)a na 155 sura ya 16 iliyofanyiwa marekebisho  mwaka 2002, pamoja na kifungu cha 158(a) cha makosa ya kuzini.


akisoma Hukumu hiyo Hakimu Ndeuruo alidai kuwa Mtuhumiwa alianza kujihusisha kimapenzi na mwanaye Mwaka 2008 baada ya kutengana na mkewe ambapo Mtuhumiwa aliachiwa watoto wote.
Aliongeza kuwa wakati huo binti huyo alikuwa na umri wa miaka 12 na alikuwa akisoma shule ya msingi darasa la Tano jambo ambalo wamedumu nalo kwa Miaka mine hadi ilipogundulika kuwa binti alikuwa mjamzito Mei, 2012.
Alisema mbinu aliyokuwa akiitumia ni kumtishia binti asitoe taarifa kwa mtu yoyote na kwamba baada ya kugundulika kuwa na ujauzito alimwambia amsingizie kijana yoyote mtaani kwao.
Hakimu Ndeuruo alisema Mahakama ilimtia hatiani Mtuhumiwa kutokana na ushahidi wa Mhanga wa tukio hilo ambaye ni binti pamoja na ushahidi wa kitaalamu kutoka kwa Mkemia mkuu wa Serikali.
Alisema ushahidi wa Mkemia Mkuu wa Serikali baada ya kupima Vinasaba kutoka Mtuhumiwa, Mhanga na Mtoto aliyezaliwa ulidai kuwa  Mshtakiwa ndiye baba halali wa Mtoto kutokana na Maeneo 15 ya vipimo vya Vinasaba kati ya Baba na Mtoto aliyezaliwa kufungana kwa asilimia 99.9.
Aidha kabla ya kutoa hukumu Hakimu alimpa nafasi mtuhumiwa kujitetea ili apunguziwe adhabu au asiweze kuhukumiwa kabisa lakini hali ikawa tofauti baada ya Mtuhumiwa kujibu kuwa hana la kujitetea vyovyote itakavyokuwa anachotaka ni nakala ya hukumu.
Kutokana na kushindwa kujitetea Hakimu Ndeuruo alimhukumu kwenda jela miaka 30 na kwamba ana haki ya kukata rufaa katika Mahakama kuu endapo hakuridhika na hukumu hiyo.
Awali katika ushahidi wake Mahakamani hapo Mtuhumiwa huyo alidai kuwa hakutenda kosa hilo bali alitengenezewa na Mkewe ambaye aliapa kumkomesha baada ya kukosana na kumpata mume mwingine jambo ambalo lilipingwa vikali na hakimu na kudai kuwa “ mfa maji haachi kutapatapa”

Na Mbeya yetu

Mabondia wa Tanzania huuza mechi zao Ulaya?

http://www.thehabari.com/wp-content/uploads/2011/11/Rashid-matumla.png
Rashid Matumla 'Snake Man'

Benson Mwakyembe
 

http://www.ibn-tv.com/wp-content/uploads/2012/02/Nyilawila.jpg
Karama Nyilawila aliyetwaa ubingwa wa WBF Ulaya

MABONDIA Mada Maugo na Benson Mwakyembe Jumamosi walipokea vipigo nchini Russia katika mapambano yao ya kimataifa, huku kukiwa na tuhuma kwamba mabondia wengi wa Kitanzania wanaoenda kupigana nje ya nchi 'huuza' mechi zao.
Maugo alipokea kichapo cha TKO ya raundi ya 5 katika pambano la raundi 8 dhidi ya bondia asiye na uzoefu Movsur Yusupov aliyecheza mapambano manne tu kulinganisha na Mtanzania huyo aliyepigana michezo 25.
Mtanzania mwingine, Mwakyembe alidundwa kwa KO ya raundi ya 7 ya pambano lake la raundi 8 dhidi ya bondia mwingine asiye na uzoefu Apti Ustarkhanov, ambaye hilo lilikuwa ni pambano lake la tatu na la pili kushinda tangu aingie kwenye ngumi za kulipwa.
Kina Maugo walipambana dhidi ya wenyeji wao katika mapambano ya uzito wa Super Middle ya raundi nane yaliyofanyika katika ukumbi wa Trade & Entertainment Centre 'Moskva', Kaspiysk chini ya wakala Mkenya Thomas Mutua.
Vipigo vya mabondia hao vimekuja wakati wadau wa ngumi za kulipwa wakihoji sababu zinazofanya mabondia wa Kitanzania kushindwa kutamba kila waendapo nje huku ripoti mbalimbali zikiwatuhumu mabondia wa majuu kuwatumia mabondia kutoka Afrika kupandisha chati zao katika viwango vya ubora kwa kuwanunua wawaachie washinde.
Ripoti za kuuzwa mechi au kuwapo kwa mchezo mchafu ziliwahi kutolewa na baadhi ya mabondia akiwamo Pascal Ndomba na Francis Cheka aliyepokea kichapo cha kushangaza mapema mwaka huu nchini Ujerumani.

Ndomba anayepigana uzito wa juu wa (Cruiserweight), alisema baadhi ya mawakala wa nje hutaka mabondia dhaifu wa kwenda kupigana na mabondia wao ili kupata ushindi kirahisi na kuboresha rekodi zao.
"Hili ndilo linalofanyika, bondia mkali mara chache sana kupelekwa nje na hata akienda basi atahujumiwa ili apoteze mchezo kwa manufaa ya mabondia wanaoenda kupigana nao," Ndomba alisema hivi karibuni.
Naye Cheka alitoa maelezo ya kufanyiwa 'hila' katika pambano lake dhidi ya Uensal Arik aliloongoza kwa raundi sita za mwanzo kabla ya kurushiwa kitaulo katika raundi ya saba na kupoteza mchezo kwa TKO.

Pascal Ndomba
"Sikupoteza pambano lile, ila mwenyeji alibebwa na mwamuzi aliyemaliza pambano kana kwamba nimesalimu amri, ni vigumu mabondia wa Tanzania kushinda nje," alisema Cheka mara alipotua nchini.
Cheka alisema kambi ya mpinzani wake walimfuata hadi hotelini alipofikia kuelekea pambano lao kumshawishi awaachie pambano hilo kwa ahadi ya pesa lakini alipokataa ndipo alipokuja kuhujumiwa ulingoni kwa mtu aliyekuwa upande wa kona yake kurusha taulo ulingoni ilhali alikuwa akiongoza kwa pointi.
Bondia huyo anayeaminika kuwa bora zaidi nchini kwa sasa katika uzito wake, alisema hakuambatana na kocha wake wakati akienda katika pambano hilo hivyo hata kwenye kona yake walikuwa wenyeji wake na ndiyo waliorusha taulo ulingoni.
Hata hivyo, wapo waliomtuhumu kwamba huenda Cheka alicheza 'dili' na wakala wa pambano hilo ili kutotibua rekodi ya mpinzani wake ambaye alikuwa amepoteza pambano moja tu ya 18 aliyokuwa amecheza.
NIPASHE ilizungumza na Marais wa Mashirikisho ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, Emmanuel Mlundwa wa PST na Yasin Abdallah 'Ustaadh' wa TPBO kutaka kujua ukweli kuhusu tuhuma hizo, ambapo walikuwa na maoni tofauti .
Mlundwa alisema kinachowaponza mabondia wa Tanzania siyo hujuma wala nini ila maandalizi duni wanayofanya kabla ya mapambano yao pia kuwa na viwango duni kulinganisha na wapinzani wao wanaoenda kucheza nao.

"Ngumi za kulipwa ni biashara, mabondia wa ngumi hizo wanapotafutiwa mechi wanapaswa kujiandaa, lakini hilo halifanyiki na hivyo kwenda kulitia aibu taifa na kujiharibia soko wao wenyewe bila kujua," alisema Mlundwa.
Nyota huyo wa zamani wa kimataifa wa ngumi, alisema siyo kweli kama kuna rushwa zinazofanyika bali Watanzania wanaopewa nafasi kulingana na rekodi zao nchini huenda kupigana kichovu kwa kukosa maandalizi mazuri.
Ustaadh yeye alisema
Francis Cheka
linalowaangusha mabondia wa Tanzania nje ya nchi ni maisha wanayoishi kuwa kinyume na nidhamu ya ngumi za kulipwa na kwamba kutokuwa na mameneja ni tatizo jingine linalowakwaza.
"Mabondia wengi hawafanyi mazoezi mpaka wakati wa pambano, hapo unatarajia afanye vizuri? Pia hawaishi kwa kuzingatia miiko ya ngumi na hivyo wanapoenda nje ni rahisi kupigwa na kuhisiwa labda wanauza," anasema.

Alisema ni vyema mabondia wakafanya kazi chini ya mameneja kama ilivyokuwa kwa Rashid Matumla kwani itafanya ajikite kwenye mazoezi tu na mambo mengine kuwaachia meneja zao.
Ustaadh alisema majukumu wanayobeba mabondia ya kufanya kila kitu wakati mwingine huwafanya washindwe kujikita kwenye mazoezi na hivyo kujikuta muda wa pambano ukifika hawajajiandaa vizuri.
Rais huyo wa TPBO-Limited, alisema pia mabondia wengi hutoa visingizio kila wanapopigwa nje ya nchi bila kuangalia kama sheria za ngumi zinasemaje wanapokuwa kwenye ulingo na kutolea mfano pigano la Cheka na Arik.
"Cheka alipolalamika nilimuuliza vipi katika pambano lake na Arik, hakutupa ngumi yoyote katika raundi ya 7 na kupigwa makonde mfululizo na kunieleza mkono wa kulia ulimzingua, sheria zinasema bondia asipojibu mapigo kwa zaidi ya ngumi 10 alizorushiwa refa anaweza kuvunja pambano au wasaidizi wa bondia kuingilia kati kwa kurusha kitaulo na ndivyo ilivyotokea," alisema.
Mada Maugo