STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, February 19, 2014

Yanga yaingia kambini kuiwinda Ruvu Shooting

Ruvu Shooting
Yanga
KIKOSI cha mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara leo imeingia kambini mjini Bagamoyo kwa ajili ya pambano lao lijalo dhidi ya Ruvu Shooting litakalochezwa siku ya Jumamosi kwenye uwanja wa Taifa.
Wachezaji 28 bila Hussen Javu anayesumbuliwa na Malaria ndiyo walioingia kambini kwa ajili ya mechi hiyo ambayo Ruvu wametamba kuinyoa vijana wa Jangwani kama anavyotamba Msemaji wa klabu hiyo, Masau Bwire.
Kambi hiyo pia inaelezwa itakuwa ikitumiwa na Yanga kwa ajili ya mechi yao ya kimataifa ya Ligi ya Mabingwa ya Afrika, dhidi ya Al Ahly ya Misri mechi itakayochezwa Machi Mosi kwenye uwanja wa Taifa.
Afisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, alinukuliwa hivi punde na Radio One Stereo, amekiri timu yake kuingia kambini kwa ajili ya mechi ya Ruvu na ile ya Ligi ya Mabingwa ya Afrika.
Kizuguto alisema wachezaji wote wana ari ya ushindi, huku msemaji mwenzake, Masau Bwire amesema kuwa Yanga lazima waanze kuchagua mapema aina ya mnyoo watakaonyolewa Jumamosi kama ni Kiduku au kipara kwani hawatapona Jumamosi wakitambia kocha wao Tom Oloba na wachezaji wake mahiri.
Katika mechi ya mkondo wa kwanza Yanga ikiwa wenyeji, Ruvu walikaa kwa kulala bao 1-0, kitu ambacho Bwire ametamba ni lazima walipize kisasi kwa vijana hao wa Johannes van der Pluijm. Ngoja tuone inakuwaje

Breaking News! Ajali yaua wanne Sekenke

Wananchi wakiangalia Lori baada ya kuteketea kwa moto baada ya kuporomoka korongoni
 Mabaki ya Lori hilo bada ya kuteketea kabisa na moto jioni hii
 Baadhi ya wasafiri wakitazama lori lililongua jioni hii

 Bonde la mlima sekenke linavyoonekana na baadhi ya miti imeunguaa
 Hii ni njia ya mlima sekenke

AJALI mbaya imetokea jioni hii baada ya Lori la Mafuta kuanguka na kuteketea katika eneo la Milima ya Sekenke mkoani Singida na kuua watu wanne hapohapo.Chanzo cha ajali hiyo ni breki kufeli kukamata wakati lori hilo lilipokuwa linashuka mlima huo. Shuhda wa ajali hiyo bwana Julius chacha alipoongea na mtandao wetu wa Dj sek blog amesema kwamba Lori hilo lilipoacha njia lilipinduka na kuingia bondeni na kushika moto. Akiendelea kuongea shuhuda huyo alisema walishindwa kutoa msaada wowote kwa kwa moto uliposhika ulikuwa mkubwa na hawakuwa na vifaa vya kuokolea.Watu wanne wamekuufa papo hapo kutokana na ajali hiyo.Polisi walikuwa bado hawajafika eneoo la tukio mpaka tunaondoka eneo la tukio.

Prisons yaigagadua JKT Ruvu 6-0


Prisons
MABINGWA wa zamani wa Tanzania, Prisons ya Mbeya jioni ya leo imetoa kisago cha aina yake kwa maafande wenzao wa JKT Ruvu kwa kuitandika mabao 6-0 katika pambano pekee la Ligi Kuu Tanzania Bara lililochezwa nchini leo.
Pambano hilo limechezwa kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya ambapo mechi hiyo ya 'kiporo' ilishuhudia wenyeji wakipata mabo yao kupitia kwa Peter Michael aliyefunga mabao mawili, Omega Seme, Nurdin Chona, Lugano Mwangama na Frank William na kuiwezesha timu hiyo kuchupa hadi nafasi ya 9 ikiwa na pointi 19 sawa na JKT wanaoshuka hadi nafasi ya 10 kuipisha Prisons kwa tofauti na mabao ya kufunga na kufungwa.
Kipigo hicho kinaweza kuwa mwanzo mbaya kwa JKT inayojiandaa kushuka dimbani Jumapili dhidi ya Simba, ikiwa chini ya kocha mpya Fred Minziro baada ya aliyekuwa kocha wao Mbwana Makatta kubwaga manyanga wiki chache zilizopita.
Timu hiyo katika mechi nne zilizopita imeambulia pointi moja tu baada ya kufungwa mechi tatu na kupata sare mchezo mmoja dhidi ya Oljoro JKT.

Msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara:
                          P    W     D     L      F     A   GD  PTS
01.Azam            16   10    06   00   29   10   19  36
02.Yanga           16   10    05   01   34   12   22  35
03.Mbeya City    18   09    08   01   24   14   10  35
04.Simba           18   08    08   02   33   16   17  32
05.Ruvu Sh.       18   06    07   05   20   19   01  25
06.Kagera Sugar 18  05    08   05   15    15   00  23
07.Coastal Union18   04    10    04  12    09   03  22
08.Mtibwa Sugar 18   05    07    06  21   22  -01  22
09.Prisons          17   04    07    05   15   16  -01 19
10. JKT Ruvu      18   06    01    11   13   27  -14 19
11.Mgambo        18   04    05    09    10  26 -16  17
12.Oljoro            19   02    09    08    14  28 -14  15
13.Ashanti          17   03    05    09   14   28 -16  14
14.Rhino Rangers18   02    07    09   12  22 -10  13
Wafungaji:14- Tambwe Amisi (Simba)
09- Elias Maguri (Ruvu Shooting), Kipre Tchetche (Azam)
08- Hamis Kiiza (Yanga), Juma Luizio (Mtibwa Sugar)
06- Themi Felix (Kagera Sugar), Mrisho Ngassa, Didier Kavumbagu (Yanga), Peter Michael (Prisons)
05- Tumba Sued (Ashanti Utd), Jerry Santo (Coastal Union), Jerome Lambele (Ruvu Shooting)
04- Jerry Tegete (Yanga), Jonas Mkude, Betram Mombeki (Simba), Bakar Kondo, Salum Machaku (JKT Ruvu),
03- Haruna Chanongo, Ramadhani Singano (Simba), Paul Nonga (Mbeya City), Salum Machaku (JKT Ruvu), Humphrey Mieno, Mcha Khamis (Azam), Amir Omary (Oljoro), Jeremia John (Mbeya City), Said Dilunga (Ruvu Shooting)


Mechi zijazo za Ligi hiyo wikiendi hii;
Feb 22, 2014
Ruvu Shooting  vs Yanga SC
Kagera Sugar  vs Rhino
Mtibwa Sugar  vs Ashanti Utd
Coastal Union vs Mbeya City
JKT Oljoro  vs Mgambo
Azam   vs Prisons
 

Feb 23, 2014
Simba SC    vs JKT Ruvu

SOMA SIMULIZI HILI LA MSANII AT

Msanii Ali Ramadhan 'AT'
SIMULIZI la kusikitisha ambalo ni la kweli na tunaweza kulitaja kama ‘simulizi la kusikitisha zaidi
la uhalisia lililowahi kusimuliwa kwenye media na msanii mkubwa wa Tanzania. Hata hivyo msanii
huyo aliiambia tovuti ya Times Fm Dar es salaam, kuwa hakuwahi hata siku moja kuyaweka masimulizi haya kwenye media wala kumsimulia mtu asiye wa familia yao.
Hii ni kwa ajili yako msomaji,


''Mimi nina kitu ambacho nadhani watanzania wengi hawakijui na ni kwa sababu sijawahi kukizungumza kokote ila tu ni kwa heshima yenu na heshima ya watanzania. Mimi nimeanza kutembea nikiwa na umri wa miaka mitano.''

Tangu nilipozaliwa nilikuwa tu nipo, natambaa kama kawaida lakini baada ya miaka mitano ndio
nikaanza kutembea kwa sababu nilikuja nikaumwa mpaka hakuna aliyeweza kufikiria kama ningepona katika familia na mwili wangu ulikuwa una usaha mwili mzima. Mfano, ukichukua wembe ukichinja kwenye mwili haitoki damu inatoka usaha, kwa hiyo kitu ambacho kilikuwa kinapelekea watu wanashindwa kukaa kwa sababu ya harufu, ulikuwa unatoa harufu sana.

Mama yangu mwenyewe siku moja aliwasikia watu wanazungumza kuwa huyu mtoto hawezi kupona,
kama sio kesho basi kesho kutwa tunaenda kuzika. Kitu ambacho wamekuja kushangaa baada ya kuja kuniona mimi mzima na nakwenda. Lakini nimeanza kutembea nina miaka 5, watoto walikuwa wananishangaa jitu zima najifundisha kwenda. Wenyewe watoto wadogo wanaenda nawekwa nichezeze nao lakini siwezi nalia, inabidi watoke watu waje kunichukua.

Yaani hakuna mtu hata mmoja anaamini kwamba yule mtoto ambaye alikuwa anaumwa tukawa
tunafikiria marehemu, leo hii atajulikana Tanzania nzima na atakuwa mtu maarufu na anafanya
shughuli zake anaruka na kucheza.

Na ilikuwa inafikiria kipindi, kama mvua inataka kunyesha wiki moja kabla watu wanatizama majira
kupitia mimi, miguu yangu kwanza lazima ivimbe, na ukibonyeza hivi kama umebonyeza mkate
halafu inakuja juu taratibu. Kwa hiyo watu walikuwa wakiniona niko hivyo wanajua kuwa mvua inataka kunyesha. Kwa hiyo nilikuwa kama mtoto wa ajabu ajabu.

Lakini alikuja doctor mmoja mpaka leo yu hai anaitwa ‘Makwetu’ ndio aliweza kunitibia,
tungekuwa tuna imani kama hizi za sasa hivi tunazungumzia za kishirikina basi mimi ningeweza
kufa. Nilichanwa kwenye mguu kwenye miguu mpaka leo niko na kovu, nikatiwa vyuma, ikapanuliwa mifupa ya miguu, ulitoka usaa naambiwa unaweza kufika hata ndoo, yaani mwili mzima mpaka mikononi nikawa natiwa mautambi….mpaka watu wanaulizana kulikoni, karogwa au vipi. Lakini mwenyezi Mungu ndio ana
mipango yake, hakuna mtu anaweza kujua.

Kwa hiyo iliwapa ugumu sana wazazi wangu, lakini baba yangu kipindi hicho alikuwa nje (Ugiriki), na
alikuwa amekata tamaa kabisa, anajua huyu mtoto ni marehemu.

AT anaamini kutokana na simulizi la maisha yake, Mungu alikuwa amemuandaa kuwa mshindi tangu
mapema. Huyu ndiye AT, mshindi wa tuzo ya Kili aliyejizolea mashabiki wengi kwa wimbo wake
‘Nipigie’ akiwa na Stara Thomas.


Times Fm Dar es salaam

Msanii Tiko Hassan atawaka wasanii 'mapepe' kubadilika

Msanii Tiko Hassan
MUIGIZAJI filamu maarufu nchini, Tiko Hassan amewataka wasanii wenzake wa kike wabadilike na waepuke matendo machafu ili kulinda hadhi na heshima yao pamoja na kujiweka katika nafasi nzuri ya kulamba tenda za matangazo.
Tiko aliyeanza kutamba tangu akiwa kundi la Shirikisho Msanii Afrika, alisema baadhi ya wasanii wanajisahau na kujikita kwenye mambo ya upuuzi na kupoteza mvuto na heshima mbele ya jamii na hata taasisi zilizopo nchini.
Alisema taasisi hizo zikiwemo mashirika na makampuni ya umma na yale ya watu binafsi yamekuwa yakishindwa kuwatumia kutangaza bidhaa zao kama ilivyo kwa baadhi ya wenzao wa kiume kwa sababu 'hawajatulia'.
"Hakuna kampuni au taasisi itakayotaka kumtumia msanii asiyejiheshimu kutangaza bidhaa zao kwa sababu itavunja murua na hadhi ya bidhaa na kampuni husika, lazima wasanii wa kike tubadilike na tutulie," alisema.
Alisema, tenda za matangazo zinasaidia kuvuna pato la ziada ambalo lingewafanya wasanii waishi kulingana na hadhi zao kama ilivyo kwa wasanii wa mataifa mengine wanaokimbiza kwa utajiri kwa tenda nje ya sanaa zao.
"Wito wangu wasanii wa kike wajitambue ni nani ndani ya jamii, wajiheshimu na kuwa mfano mbele ya jamii ili kusaidia kushawishi taasisi kuwatumia kwa matangazo na kuwaingizia pato la ziada," alisisitiza.
Staa huyo wa filamu za 'The Living Ghost', 'Devil's Soul', 'Limbwata',' Check in the Bible', 'Melvin' na nyingine alisema kama msanii wa kike havutiwi na vitendo vya wenzake, lakini hana cha kufanya kwa vile vyombo vya kuweza kuwashughulikia wasanii wa aina hiyo vyenyewe vimekaa kimya.
"Wanatuaibisha na kututia aibu, lakini utafanyaje kama vyombo vyenye jukumu la kuwashughulikia vimenyamaza, ila wanakera sana," alisema Tiko.

Arsenal, Bayern Munich hapatoshi, Milan, Atlerico Madrid mh!

Arsenal watashangilia kama hivi kwa Bayern Munich leo

Baadhi ya wachezaji wa Bayern  Munich wakijifua tayari kwa mechi ya leo
KIVUMBI cha Ligi ya Mabingwa Ulaya kinatarajiwa kuendelea tena leo kwa mechi mbili kali zitakazowakutanisha mabingwa watetezi, Bayern Munich itakayuokuwa ugenini kuvaana na Arsenal, huiku Am Milan wakiwaalika Atletico Madrid katika mechi za mkondo wa kwanza za 16 Bora.
Tayari mechi mbili za awali za hatua hiyo ziliochezwa usiku wa kuamkia leo na kushuhudia matokeo ya kusisimua ambayo yamewafanya mashabiki wa kandanda ulimwenguni kuote kutaka kuona mechi ya leo nazo zitakuwa na matokeo ya aina gani.
Arsenal wanaoongoza Ligi Kuu ya England, wanakumbuka kipigo walichopewa na watetezi hao kwenye uwanja wao wa Emirates katika mechi baina yao kulala 3-1 kabla ya kwenda kushinda ugenini 2-0 lakini ikang'oka michuanoni wa Bavarian hao.
Hata hivyo vijana wa Gunners wameapa kupata ushindi leo nyumbani na kwenda kufanya kweli ugenini ili kuvuka hatua hiyo ya 16 Bora ilityokwama kwa karibu misimu minne.
Gunners wanapaswa kupigana kiume mbele ya vijana wa Pep Guardiola kwa sababu Bavarian wapo katika kiwango bora msimu huu kama ilivyokuwa misimu miwili mfululizo iliyopita.
Ikiwa imetoka kuing'oa mashindanoni Liverpool waliowapopoa kwenye ligi mabao 5-1 katika mbio za kuwania kombe la FA, Arsenal wameapa kufa na Bayern katika mechi ya leo kaa alivyonukuliwa beki wake wa kati anayetoka Ujerumani Per Mertesacker aliyedai kuwa itawakuwa "mechi mbili sahihi" kwa Arsenal kusonga mbele, lakini hilo ndilo muhimu na si kuonyesha kuikubali sana Bayern.
"Tunatakiwa kwenda kucheza mechi mbili sahihi dhidi yao," alinukuliwa
"Tunajua tunaweza kuwafunga kwa sasa, hivyo labda kiakili tupo  katika hali nzuri kuliko mwaka jana.
"Tuliwakubali sana katika mchezo wa kwanza baada ya hapo, ilikuwa kazi rahisi kwao.
"Ladba tumejifunza kitu fulani kutokana na somo hilo na tutafanya vizuri wakati huu.
"Sasa tunayo nafasi nyingine na fursa ya kuwafunga mabingwa. Tunataka kupata mafanikio ya kipekee msimu huu, hivyo tunapaswa kuwafunga walio bora.
"Hilo si kwa Manchester City na Chelsea tu, pia na Bayern Munich kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya."
Hata hivyo Arsenal itamkosa kiungo Mikel Arteta anayetumikia  adhabu ya kadi nyekundu aliyozawadiwa katika hatua ya makundi dhidi ya Napoli, wakati Jack Wilshere na Bacary Sagna, ambao walikuwa katika benchi dhidi ya Liverpool wakitarajiwa kuwamo, huku Kieran Gibbs na Santi Cazorla, waliocheza kipindi cha pili na Tomas Rosicky, aliyekuwa amepumzishwa wote wakirejeshwa katika mechi ya leo.
Kwa upande wa Kiungo Mathieu Flamini anaamini kuwa ushindi dhidi ya Liverpool utawahamasisha kufanya vizuri dhidi ya Bayern.
Flamini alisema kukichapa kikosi cha Brendan Rodgers ambacho kipo katika kiwango cha juu ni changamoto kwao kufanya vizuri katika mechi hiyo ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na kwamba kufungwa na Bayern msimu uliopita haiwezi kuwa sababu ya Arsenal kufanya vibaya tena.
Wapinzani wao Bayern imeendelea kuongoza katika ligi ya ndani baada ya Jumamosi kushinda 4-0 dhidi ya Freiburg licha ya kuwapumzisha Jerome Boateng, David Alaba, Thiago na Mario Goetze.
Ushindi huo unaifanya Bayern kushinda mechi 13 mfululizo za Bundesliga huku ikiwa imeshuka dimbani mara 46 bila kufungwa. Mechi pekee iliyopoteza msimu huu ni ya Ligi ya Mabingwa Ulaya nyumbani dhidi ya Manchester City, ikiwa tayari imejihakikishia kusonga mbele hatua ya 16 bora.
Itashuka uwanjani leo bila winga wa Kifaransa Franck Ribery, ambaye ni majeruhi, na Xherdan Shaqiri aliyekuwa akipewa nafasi kubwa ya kuzipa pengo lake na aliyefunga mara mbili dhidi ya Freiburg, lakini atakuwa nje kutokana na kuwa majeruhi wa paja.
Pamoja na hali ya ushindi wa msimu uliopita jijini London, walipopata ushindi wa mapema kupitia kwa Toni Kroos na Thomas Mueller hivyo kuwa mbele kwa mabao 2-0 ndani ya dakika ya 21, nahodha wa Bayern Philipp Lahm bado anaihofia Arsenal.
"Mechi ni tahadhari kwetu," Lahm alisema. "Tulikuwa wazuri sana jijini London, tulifikiri hakuna lolote linaweza kutokea kwetu katika mchezo wa marudiano. Yote kwa yote ghafla tukawa tumechapwa 2-0 na kulikuwa bado na dakika chache za kucheza. Ukweli inaonyesha kuwa mambo yanaweza kwenda haraka katika Ligi ya Mabingwa Ulaya. Tutakuwa na kukumkumbu ya hilo katika akili zetu."
Lahm alisema anaitupia macho ya karibu Arsenal huku angalizo lake likiwa kwa Wajerumani wenzake Mertesacker, Mesut Ozil na Lukas Podolski, pamoja na Kinda ambaye hajaichezea timu ya taifa Serge Gnabry.
Mechi ya marudiano kwa timu hizo itachezwa Ujerumani Machi 11, mwaka huu na katika pambano jingine la leoAC Milan itakuwa uwanja wa nyumbani wa San Siro nchini Italia kuikaribisha  Atletico Madrid.
Pambano hilo linatarajiwa kuwa kali kutokana na uborwa wa Atletico kwa sasa ikiongozwa na 'muuaji' wao Diego Costa, huku Milan ikipigana kurejesha heshima yake chini ya Clarence Seedorf  baada ya kuwa na msimu mbaya katia Seria A safari hii.
Barcelona, PSG wenyewe wameshamaliza kazi zao na kusubiri michezo ya marudiano, je  Arsenal au Bayern Munich itakayomliza mwenzake, au Milani kukubali kuendelea kudorora kwa Madrid tusubiri.

Barcelona, PSG zaua ugenini Ligi ya Mabingwa Ulaya


Messi akifunga penati iliyolalamikiwa na kocha  Pellegrini
Ibrahimovic akifunga moja ya mabao yake, chini akishangilia bao lake la kwanza

Add caption
KIPIGO cha kustukiza cha mabao 2-0 walichopewa Manchester City ikiwa nyumbani kwao na Barcelona kimemtibua kocha wa timu hiyo Manuel Pellegrini kumtupia lawama refa wa pambano hilo la awali la mtoano kuwania kucheza Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya akidai aliwabeba na kuwatengenezea ushindi wapinzani wao.
Pellegrini anailalamikia penati iliyotolewa kwa wapinzani  iliyosababishwa na kufungwa na Lionel Messi dakika tisa baada ya kuanza kwa kipindi cha pili.
Messi aliangushwa nje kidogo na eneo la penati na Martin Demichelis na refa Jonas Eriksson kuamuru ipigwe adhabu hiyo na Messi kuifungia Barcelona bao la kuongoza kabla ya beki Dani Alves kuongeza la pili dakika ya 90 na kuiweka Barca katika nafasi nzuri ya kutinga robo watakapoikaribisha Manchester City kwenye mechi ya marudiano Machi 11.
Pellegrini amenukuliwa akisema anashangaa ni vipi UEFA hata ikamteua mwamuzi huyo kutoka Sweden kuchezesha pambano kubwa kama hilo, huku akidai mara kadhaa amekuwa wakiionea timu yake.
Hata hivyo matamshi hayo ya kocha huyo kutoka Chile yanaweza kumweka matatani kwa 'mabosi' wa UEFA.
Katia mechi nyingine ya michuano hiyo hatua ya 16 Bora, mabingwa wa Ufaransa, PSG ikiongozwa na Zlatan Ibrahimovic, iliisasambua Bayer Liverkusen nyumbani kwao kwa kuichabanga mabao 4-0.
Wanafainali hao wa michuano ya mwaka jana wakiwa kwenye uwanja wao wa BayArena mjini Leverkusen, nchini Ujerumani walishindwa kuamini kipigo walichopewa na Wafaransa hao ambao ni kama wamejihakikishia hatua ya robo fainali kwa vile Leverkusen watalazimika kuifunga PSG mabao 5-0 jijini Paris ili kuiondosha kitu kinachoonekana kuwa kigumu, japo soka lolote linaweza kutokea.
Mabao ya wababe hao wa Ufaransa yalifungwa na Blaise Matuidi dakika ya tatu kwa pasi ya Verratti, kabla ya Ibrahimovic kuongeza la pili dakika ya 39 kwa mkwaju wa penati na kisha kufunga jingine dakika 42 akimaliza pasi Matuidi.
Bao la nne lililoikata maini Wajerumani nyumbani kwao liliwekwa kimiani na mchezaji mpya wa timu hiyo kutoka Newcastle United, Yohan Cabaye aliyefunga katika dakika ya 88 akimaliza pasi ya Lucas.

Tuesday, February 18, 2014

UWF yahimiza wanawake kushiriki Siku ya Wanawake Dunia


  MENEJA wa Tuzo ya Mwanamakuka ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Marafiki (UWF) Mariam Shamo akifafanua jambo mbele ya washindi wa tuzo hiyo wa mwaka juzi na jana pamoja na wanahabari kuhusiana na hafla yao wanayoitarajia kuifanya siku ya Familia 'Family Day' Machi 15 mwaka huu,ambayo imepangwa kufanyika ndani ya kiota kipya cha maraha na burudani Escape One Mikocheni jijini Dar, pembeni yake ni  Mdau mkubwa wa tuzo hizo na Mkurugenzi wa Benki ya Wanawake Tanzania Margareth Chacha.

Mjumbe wa Mradi wa Mwanamakuka (Mwanamakuka Awards) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Wanawake Tanzania,Bi. Margareth Chacha akisisitiza jambo mbele ya washindi wa Mwanamakuka mwaka 2012 na 2013 alipokuwa akiongelea siku ya Familia  Duniani tarehe 15 mwezi ujao mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki. Kushoto ni Meneja wa Mradi wa Mwanamakuka ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kituo cha Wanawake Marafiki (Unit of Women Friends),Bi Maryam Shamo.
WASHINDI wa Tuzo ya Mwanamakuka mwaka 2012 na 2013 wakiwa pamoja wakati walipokutana na waratibu wa shindano hilo kwa ajili ya kujipanga na Siku ya Wanawake Duniani inayotarajiwa kufanyika mnamo Machi 8 na kufuatiwa na Family Day Machi 15 mwaka huu.
WANAWAKE nchini wamehamasishwa kushiriki Siku ya Wanawake Duniani itakayofanyika Machi 8, na kufuatiwa na Family Day Machi 15, mwaka huu jijini Dar es Salaam na kujadili masuala mbalimbali ya kumwezesha mwanamke.
Mjumbe wa mradi wa Mwanamakuka (Mwanamakuka Award) na Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Wanawake Tanzania, Margareth Chacha, aliwaambia waandishi wa habari mwishoni mwa wiki kuwa siku hiyo ni ya muhimu kwa wanawake kwa vile itawaleta pamoja na kujadili masuala mbalimbali.
“Tutakutana Siku ya Wanawake Duniani na kujadili namna bora zaidi ya kumuwezesha mwanamke kujiinua kiuchumi,” alisema.
Alisema benki yake inafadhili washindi wanawake wajasiriamali kupitia mradi huo na inafanya hivyo kwa ajili ya kumwinua mwanawake kupitia benki yao ya wanawake.
Alisema benki hiyo inataka kuona wanawake wengi wanaingia katika shughuli za kijasiriamali na pia imejipanga kutumia matawi yake nchini kupanua wigo wa zawadi ya Mwanamakuka.
Alisema mpaka sasa ni asilimia mbili tu ya wanawake wanaotumia huduma za kibenki kati ya asilimia nane ya Watanzania wote wanaotumia huduma hizo, na sasa wakati umefika kuongeza idadi ya wanawake.
“Hali hiyo ni ya kihistoria lakini kwa sasa wanawake tunashukuru hali imebadilika tunaweza kufanyakazi mbalimbali zikiwamo za biashara,”aliongeza.
Alisisitiza umuhimu wa wanawake kujiunga katika vikundi kwa ajili ya kupata mikopo kutoka katika benki yao kufanyia shughuli zao za kijasiriamali.
Naye Meneja wa mradi wa Mwanamakuka ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kituo cha Wanawake Marafiki (UWF),  Maryam Shamo, alisema Siku ya Wanawake Duniani kutakuwa na maonyesho ya kazi za kijasiriamali za wanawake na michezo mbalimbali.
“Siku hiyo washindi wa mwaka huu watapatiwa zawadi zao, na pia mshindi wa jumla wa mwaka 2012 na 2013 atapatiwa zawadi kati ya washindi kumi waliokwisha pata zawadi,'' alisema.
Alifafanua kuwa katika kusherehekea ya siku hiyo, watu wengi wamealikwa wakiwamo akinamama wajasiriamali na wanasiasa wanawake.
Kwa upande wake, mjasiriamali mkazi wa Dar es Salaam na mshindi wa nyuma wa mradi huo, Tatu Ngao, alisema alishinda Shilingi  milioni sita ambazo zimemwezesha kufanya biashara yake kwa ufanisi.
“Nilishinda kupitia biashara yangu ya kutengeneza keki...nimepanuka kwa kiwango cha kuridhisha hadi sasa,” alisema.
Zawadi ya Mwanamakuka ni mradi uliobuniwa na Kituo cha Wanawake Marafiki kwa ajili ya kuwawezesha wajasiriamali wanawake kwa ufadhili wa Benki ya Wanawake Tanzania na wadau wengine.

Naye mshindi wa pili wa mwaka jana , Leila Mwambungu alisema anashukuru mradi huo umemfanya apanuke kiakili katika ujasiriamali pamoja na kuweza kuwasaidia wanawake wenzake na kiu yake kubwa kuzidi kusonge mbele ili kuwa mfano kwa wengine.
"Nashukuru waandaji wa tuzo hii, shukrani zangu za pekee ziende kwa Mariam Shamo, Mama Margareth Chacha kwa namna wanavyowasaidia wanawake wenzao, najisikia furaha na fahari kuwa Mwanamakuka namba mbili wa mwaka 2013 na kiu yangu nifike mbali zaidi baada ya kuwezeshwa na mradi huu," alisema Leila. 


Yanga imepania, yamtuma Mkwasa Cairo kuifanyia ushushushu Al Ahly

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiyhILGXEPzcg08Ou6VWhyphenhyphenGQ_bEGVRsjHkUwM-95WMFyKgoa3AmSEp0pQFl7LDHsP8AUvz0B1SdcA1_DqHCjiLzsmNFvGJVgE7hf4UYU6HgdkrfVXUq4_nOTvCDcVKeGrucIGKzxSSwSOHl/s640/Charles-Boniface-Mkwasa1.jpg
Charles Boniface Mkwasa aliyeondoka nchini leo mchana
Yanga watakaowavaa Al Ahly ya Misri Machi mwaka huu kwenye raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika
KATIKA kuhakikisha kwamba Wamisri hawaponi kwa vijana wa Jangwani, Kocha Msaidizi wa Yanga, Charles Boniface Mkwasa 'Master' ameondoka nchini mchana wa leo kuelekea Cairo nchini Misri ili kwenda kuipeleleza Al Ahly katika mechi yake ya fainali ya Super Cup dhidi ya Cs Sfaxien ya Tunisia.
Mechi hiyo itachezwa Alhamisi na Mkwasa ataenda kuwafanyia ushushushu Al Ahly watakaovaana nao kwenye mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika mapema mwezi ujao.
Kwa mujibu wa tovuti ya klabu Yanga, imesema kuwa Mkwasa ataenda kushuhudia mchezo huo Super Cup inayozikutanisha Bingwa wa Ligi ya Mabingwa Afrika na wale wa Kombe la Shirikisho Afrika, mchezo utakaochezwa katika dimba la Cairo International Stadium.
Mkwasa ameondoka kwa usafiri wa Shirika la Ndege la Ethiopia Airline ambapo atapitia jijini Adis Ababa kabla ya kuunganisha kuelekea Cairo ambapo atatua Uwanja wa Ndege majira ya saa 7 usiku na kupokelewa na wenyeji kutoka ofisi za Ubalozi wa Tanzania nchini Misri.
Kutokana na umuhimu wa mchezo huo Uongozi wa Young Africans kwa pamoja na Benchi la Ufundi walikaa na kukubaliana kuwa kocha msaidizi Mkwasa aende kushuhudia mchezo huo wa fainali ambao utaweza kusaidia kupata picha ya wapinzani Al Ahly ambao watacheza na Young Africans mwishoni mwa mwezi huu.
Lengo la safari ni kuweza kuwaona Al Ahly wanavyocheza katika mchezo huo wa fainali, pili ni kujua wanayocheza wakiwa katika uwanja wao wa nyumbani na tatu ni kuijua timu nzima kiufundi inachezaje.
Kwa upande wake Kocha Mkwasa amesema anaamini ataitumia vizuri nafasi hiyo ya kuutazama mchezo wa Super Cup kwa kuwasoma wapinzani na pindi atakaporejea atasaidiana na kocha mkuu kuwaandaa vijana tayari kwa mchezo huo.
Mkwasa mara baada ya kuutazama mchezo huo dhidi ya CS SFaxien siku ya Alhamis jioni saa 11 kamili kwa saa za Afrika Mashariki atarejea nchini siku ya ijumaa n akuungana na kikosi kwa ajili ya mchezo wa siku ya jumamosi dhidi ya timu ya Ruvu Shooting.
Al Ahly Mabingwa watetezi wa klabu Bingwa Barani Afrika watacheza na Young Africans Tarehe 1 Machi 2014 katika mchezo wa kwanza wa kuwania kuingia katika 16 bora kisha kurudiana jijini Cairo wiki moja baadae.
Rekodi inaonyesha kuwa Yanga haijawahi kuifunga achilia mbali kuitoa timu yoyote ya Afrika Kaskazini katika michuano ya kimataifa na safari hii wana jangwani wameapa ni lazima mzizi wa futina ukatwe kwa kuwaondosha na kuwavua taji Al Ahly katika mechi zao za raundi ya kwanza.

STAND UNITED YAIKATIA RUFANI KANEMBWA JKT

Vurugu  za mechi ya awali baina ya Stand Utd na Kanembwa JKT

TIMU ya soka ya Stand United ya Shinyanga imekata rufani Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ikipinga Kanembwa JKT ya Kigoma kuchezesha wachezaji waliosajiliwa katika dirisha dogo kwenye mechi ya kiporo iliyozikutanisha timu hizo.
Mechi hiyo namba 22 ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) ilichezwa juzi (Februari 16 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora ambapo Kanembwa JKT iliibuka na ushindi wa bao 1-0.
Katika rufani yake, Stand United inadai kwenye mechi hiyo Kanembwa JKT ilichezesha wachezaji wanane waliosajiliwa katika dirisha kidogo kinyume na maelekezo kutoka TFF kwa timu hizo kuwa wachezaji waliosajiliwa katika dirisha dogo hawawezi kucheza mechi hiyo.
Wachezaji wanaodaiwa kusajiliwa dirisha dogo na kucheza mechi hiyo ni Hamidu Juma, Ibrahim Shaban Issa, Joseph Mlary, Lucas Charles Karanga, Raji Ismail, Salvatory Kulia Raphael, Seif Ibrahim Zaid na Yonathan David Sabugowiga.
Dirisha dogo lilifunguliwa Novemba 15 na kufungwa Desemba 15 mwaka jana, hivyo Stand United katika rufani yake inaombwa ipewe pointi tatu na mabao matatu kwa Kanembwa JKT kuchezesha wachezaji wasiostahili.
Awali mechi hiyo ilichezwa Novemba 2 mwaka jana Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga, na kuvunjwa na mwamuzi dakika ya 87 baada ya Kanembwa JKT kugomea pigo la penalti dhidi yao.

Twiga Stars kurudiana na Zambia Machi 2

 Na Boniface Wambura
MECHI ya pili ya raundi ya kwanza kuwania Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) kati ya Tanzania (Twiga Stars) na Zambia (Shepolopolo) itachezwa Machi 2 mwaka huu Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi, Dar es Salaam.

Twiga Stars tayari imeingia kambini kujiandaa kwa mechi hiyo itakayochezwa kuanzia saa 10 kamili jioni. Twiga Stars chini ya Kocha Rogasian Kaijage inafanya mazoezi yake kwenye Uwanja wa Karume ambao ni wa nyasi za bandia kama ulivyo ule wa Azam Complex.

Shepolopolo iliibuka na ushindi wa mabao 2-1 katika mechi ya kwanza iliyochezwa Februari 14 mwaka huu kwenye Uwanja wa Nkoloma jijini Lusaka.

Iwapo Twiga Stars itafanikiwa kuiondoa Shepolopolo itacheza na mshindi wa mechi kati ya Botswana na Zimbabwe. Zimbabwe ilishinda mechi ya kwanza ugenini.

Wachezaji wa Twiga Stars waliopo kambini ni Amina Ali, Anastazia Katunzi, Asha Rashid, Donisia Minja, Esther Chabruma, Etoe Mlenzi, Everine Sekikubo, Fatuma Issa, Fatuma Makusanya na Fatuma Mustafa.
Wengine ni, Fatuma Mwisendi, Fatuma Omari, Flora Kayanda, Happiness Mwaipaja, Maimuna Mkane, Mwajuma Abdallah, Mwapewa Mtumwa, Pulkeria Charaji, Sherida Boniface, Sophia Mwasikili, Therese Yona, Vumilia Maarifa na Zena Said.

Wa3 waombewa ITC kucheza Thailand, Ujerumani



WACHEZAJI watatu wanaocheza mpira wa miguu nchini Tanzania wameombewa Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC) ili wakacheze katika nchi za Thailand na Ujerumani.



Mchezaji Khamis Mroki Jamal aliyekuwa na timu ya Daraja la Kwanza ya Polisi Dar es Salaam ameombewa ITC na Chama cha Mpira wa Miguu Thailand (FAT) ili akajiunge na Kabinburi ya nchini humo.



Said Ali Nassor aliyekuwa akichezea FC Turkey ya Zanzibar na Samuel Chuonyo wameombewa na ITC na Chama cha Mpira wa Miguu Ujerumani (DFB) kwa ajili ya kujiunga na klabu ya VfB Eichstatt.



Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linafanyia kazi maombi hayo na mara taratibu zote zitakapokamilika ikiwemo ridhaa ya klabu zao za hapa Tanzania itatoa ITC hizo.

Wadanganyifu TFF washtakiwa Kamati ya Maadili

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limewalalamikia wana familia watano wa mpira wa miguu kwa Kamati ya Maadili kuhusiana na udanganyifu katika mtihani wa utimamu wa mwili wa waamuzi na usajili wa mchezaji Emmanuel Okwi.

Riziki Majala na Army Sentimea ambao ni wakufunzi wa waamuzi, na Oden Mbaga na Samwel Mpenzu ambao ni waamuzi wanadaiwa kughushi nyaraka kuhalalisha mtihani huo kinyume cha taratibu.

Naye Sabri Mtulla analalamikiwa na TFF kwa madai ya kuidanganya Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji kuwa hakukuwa na pingamizi lolote juu ya usajili wa mchezaji Emmanuel Okwi huku akijua wazi kuwa jambo hilo si kweli.

Kwa mujibu wa kanuni, malalamiko hayo yamefikishwa kwenye Kamati ya Maadili ambayo itachunguza ili kujiridhisha kama yana msingi au la. Ikibaini kuna kesi ndipo walalamikiwa watafika mbele ya kamati hiyo.

CCM yawaonya vikali Lowassa na wenzake


https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjTt29nQDhgvo4aSwRstqcg9niRSVdsUPKCplQaZqwKxhMtoltV8TO3YuTwgV7VyC54dDsO4Hwl5onj7IXeagLMkN9ReHe73OIfKg6nNThzTzD5rSEcLu9xrW1u-a6p0VjLxg_itDR65gC-/s1600/nec13.jpg
Kati ya tarehe 13/02/2014  na tarehe 18/02/2014 kumekuwa na mfululizo wa vikao kadhaa vya Chama kitaifa vilivyoshughulikia suala la maadili ndani ya Chama.



Vikao hivyo ni pamoja na Kamati Ndogo ya Udhibiti tarehe 13-14/02/2014, Tume ya Udhibiti na Nidhamu 18/02/2014 na Kamati Kuu tarehe 18/02/2013.



Waliohojiwa katika mfululizo wa vikao hivi ni wafuatao:-



1.            Ndg. Frederick Sumaye

2.            Ndugu Edward Lowasa

3.            Ndugu Bernard Membe

4.            Ndugu Stephen Wassira

5.            Ndugu January Makamba

6.            Ndugu William Ngeleja



Baada ya kuwahoji ilithibitika kuwa baadhi ya tuhuma dhidi yao ni za kweli na hivyo kupendekeza adhabu.  Mapendekezo hayo yalipelekwa kwenye Tume ya Udhibiti na Nidhamu na hatimaye Kamati Kuu ya CCM ambayo ilitoa adhabu kwa wahusika.



Kwa ujumla waliohojiwa wamethibitika kuwa na makosa yafuatayo:-



1.        Walithibitika kuanza kampeni za kutafuta kuteuliwa kugombea Urais kabla ya wakati kinyume na Kanuni za Uongozi na Maadili za CCM Toleo la Februari 2010, Ibara 6(7)(i).



2.       Wamethibitika kufanya vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya Chama na baadhi yao kufanya vitendo vinavyokiuka maadili ndani ya jamii.  Kosa hili nalo ni kwa mujibu wa Kanuni za Uongozi na Maadili za CCM Toleo la Februari 2010, Ibara kadhaa za kanuni hizo.

 

Kamati Kuu baada ya kuthibitisha makosa hayo imewapa watu wote sita waliohojiwa adhabu ya ONYO KALI na kuwataka wajiepushe na vitendo vinavyokiuka maadili na iwapo wataendelea na vitendo hivyo Chama kitawachukulia hatua kali zaidi.



Tafsiri ya adhabu ya ONYO KALI kwa mujibu wa Kanuni za Uongozi na Maadili za CCM Toleo la Februari 2010, Ibara ya 8(ii) (b) ni:-



“Mwanachama aliyepewa adhabu ya ONYO KALI atakuwa katika hali ya kuchunguzwa kwa muda usiopungua miezi 12, ili kumsaidia katika jitihada zake za kujirekebisha.”



Kamati Kuu imeitaka pia Kamati Ndogo ya Udhibiti kuwachunguza na kuchukua hatua kwa wote waliohusika kwa namna moja au nyingine (mawakala na wapambe) kufanyika kwa vitendo hivyo vilivyovunja Kanuni za Chama.



Aidha, Kamati Kuu imewaonya vikali Viongozi na Watendaji wa Chama na kuwataka kujiepusha kujihusisha na matendo ya wanawania Urais yanayovunja na kukiuka maadili ya Chama, wametakiwa kuzingatia Kanuni na taratibu za Chama.




Imetolewa na:-




Nape Moses Nnauye,

KATIBU WA HALMASHAURI KUU YA TAIFA,

ITIKADI NA UENEZI,

18/02/2014

KUMEKUCHA KILI MUSIC AWARDS 2014


Mwaka 2009, wazo jipya lilizaliwa. Wazo la kuwa na tuzo zitakazopatikana kwa mchakato wa wazi utakaotokana na mapendekezo ya watu wenyewe ya kuchagua mastaa wa michezo, muziki, filamu au vipindi na watangazaji wanaopendwa zaidi. Wazo hilo liliendelea kuboreshwa na mwaka huu (2014), limeiva na liko tayari kutoka kwenye hatua ya wazo la kichwani, na kuwa tukio lenyewe.

"Nilizisajili na kuanzisha mwaka 2009 ila kutokana na mipango na malengo ya kampuni niliamua kuziweka kwanza hadi sasa," anasema Mwenyekiti wa Bongo5 Media Group, Luca Neghesti.

"Sasa hivi tumeshuhudia ukuaji katika tasnia mbalimbali na tumeona ni wakati muafaka wa kuwatunuku wale wanaopendwa na wananchi, kuwapatia tuzo pamoja na zawadi ya fedha taslimu milioni 1" ameongeza.

Tofauti na tuzo zingine, tuzo za watu hazitafuti ubora bali zinalenga wanaopendwa zaidi na tuzo hizi hazitajikita katika tasnia moja peke yake.

Kwa kuanzia, tuzo hizi zitatolewa katika tasnia ya burudani inayojumuisha filamu na muziki. Pia zitaiangazia sekta ya utangazaji kwa kuwatunuku watangazaji na vipindi vinavyopendwa zaidi na watu nchini huku pia mwanamichezo bora (soka, basketball, ndondi na michezo mingine) naye akipewa nafasi.

Tuzo za watu si tuzo za vijana peke yake, zipo kuwakilisha watu wa rika zote.

Tofauti nyingine kubwa ni kuwa tuzo za watu zitalenga kuwatunuku watu kutokana na umaarufu ama kupendwa kwao na si ubora. "Tuzo hizi hazileti ushindani na tuzo zingine kwasababu hazilengi tasnia moja tu," anafafanua Neghesti.

"Tanzania imesifiwa kwa uhuru wa vyombo vya habari na tuzo hizi zinalenga kujumuika na tuzo zingine kuhakikisha watanzania wanaopendwa na kufanya vizuri wanatambuliwa."

Upigaji kura unaanza wiki hii katika vipengele 11 ambapo wananchi wenyewe watachagua majina ya washiriki watakaoshindana kwenye vipengele hivyo. Awamu ya kwanza ya upigaji kura itafungwa baada ya wiki mbili kutoka siku ya kwanza ya upigaji kura na majina ya watu watano waliotajwa zaidi kutoka kwenye kila kipengele watachaguliwa kama watajwa wa mwisho.

Kuanzia hapo, upigaji kura wa wananchi utajikita tu katika orodha ya majina hayo matano kwenye kila kipengele kinachoshindaniwa. Wiki moja baada ya majina ya washiriki kutangazwa, mchujo wa kwanza utafanyika katika kila kipengele na mtu mmoja ataondolewa.

Wiki moja baadaye, mchujo wa pili utafanyika na kuwabakiza washiriki watatu kwenye ila kipengele.

Washiriki wote 33 (watatu katika kila kipengele) waliosalia baada ya kufanyika mchujo wa mwisho, watakuwa wageni wa heshima kwenye utoaji wa tuzo hizo, utakaofanyika wiki moja baada ya mchujo huo wa mwisho.

Katika hafla hiyo, washindi watatangazwa na kila mshindi atapokea zawadi ya fedha taslimu, shilingi 1,000,000 za Kitanzania pamoja na tuzo ya thamani iliyotengenezwa kwa mkono kutoka kwenye mali ghafi asili za Kitanzania.

Tuzo za watu mwaka 2014 zitajumuisha vipengele 11 ambavyo ni pamoja na:

1. MTANGAZAJI WA REDIO ANAYEPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW1 na jina' kwenda 15678)
2. KIPINDI CHA REDIO KINACHOPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW2 na jina' kwenda 15678)
3. MTANGAZAJI WA TV ANAYEPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW3 na jina' kwenda 15678)
4. KIPINDI CHA TV KINACHOPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW4 na jina' kwenda 15678)
5. MWANAMICHEZO ANAYEPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW5 na jina' kwenda 15678)
6. MWANAMUZIKI WA KIUME ANAYEPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW6 na jina' kwenda 15678)
7. MWANAMUZIKI WA KIKE ANAYEPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW7 na jina' kwenda 15678)
8. WIMBO UNAOPENDWA (2013) (tuma SMS yenye 'TZW8 na jina' kwenda 15678)
9. MUIGIZAJI WA FILAMU WA KIUME ANAYEPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW9 na jina' kwenda 15678)
10. MUIGIZAJI WA FILAMU WA KIKE ANAYEPENDWA (tuma SMS yenye 'TZW10 na jina' kwenda 15678)
11. FILAMU INAYOPENDWA (2013) (tuma SMS yenye 'TZW11 na jina' kwenda 15678) JINSI YA YA KUPIGA KURA

Mchakato wa kupendekeza majina ya washiriki katika tuzo hizi utafanyika kwa njia kuu mbili. Ya kwanza ni kwa kutumia tovuti ya tuzo hizi ambayo ni www.tuzozetu.com ambapo utakutana na hatua rahisi ya kupendekeza na kutaja majina katika vipengele vyote 11. Jinsi ya kupiga kura, bofya palipoandikwa Piga Kura na ufuate hatua rahisi kabisa ambayo haikuhitaji kujiandikisha jina wala email yako.

Njia ya pili ni kwa njia ya ujumbe mfupi wa simu ambapo utaandika neno ‘Tuzo’ kwenda namba 15678. Ukishafanya hivyo utaletewa Menu yenye vipengele vyote 11 vikiwa na code number zake. Kutaja ama kupendekeza jina, tuma code husika na jina kwenye namba hiyo hiyo; kwa mfano Justin Bieber. Gharama ya sms ni ile ile inayotozwa sms ya kawaida.