STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, November 1, 2013

Azam, Mbeya City kuendeleza rekodi zao Bara kesho

Azam


Mbeya City
MECHI za raundi ya 12 ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) zinatarajiwa kuendelea tena kesho kwenye viwanja vinne tofauti, huku mashabiki wa soka wakitaka kujua kama Azam na Mbeya City ambazo ndizo pekee hazijapoteza mchezo mpaka sasa zitavuna nini?
Mbali na kuendeleza rekodi pia iwapo timu hizo zitashinda mechi zake hizo zitaiengua Yanga kileleni na kuiporomosha hadi nafasi ya tatu na zenyewe kurejea kwenye uongozi huo wakisubiri mechi za kufungia dimba la duru la pili katikati ya wiki ijayo.
Azam waliokuwa wakiongoza msimamo wa ligi hiyo mpaka jioni hii kabla ya Yanga kuwashusha yenyewe itaikaribisha Ruvu Shooting kwenye uwanja wa Chamazi, huku wapinzani wao, Mbeya City nao watakuwa dimba la nyumbani Sokoine kuialika Ashanti United.
Michezo hiyo ni migumu kwa timu zote nne, lakini kwa kasi ya Azam na Mbeya City ni wazi Ashanti na Ruvu watakuwa na kibarua kizito cha kuweza kudhibitisha kuwa wao nao ni kiboko iwapo watazisimamisha timu hiyo katika viwanja hivyo.
Afisa Habari wa Ruvu Shooting, Masau Bwire aliiambia MICHARAZO kwamba kesho wanataka kuweka rekodi ya kuwa timu ya kwanza msimu huu 'kuwatengua udhu' Azam kwenye uwanja wa Chamazi, kwa madai wamejiandaa vya kutosha kupata ushindi.
Bwire alisema kikosi chao kipo imara japo itaendelea kumkosa kiungo mkabaji wao, Juma Seif Kijiko ambaye alionyeshwa kadi nyekundu katika pambano baina ya timu yao na Ashanti United lililoisha kwa sare.
Ruvu imesema wakali wao kama Elias Maguri, Cosmas Ader, Stephen Mwasyika, Said Dilunga na wengine wapo tayari kuwazima Azam ambao wenyewe wamenukuliwa kupiotia meneja wao Jemedari Said kwamba wanataka kumaliza mechi za duru la kwanza wakiwa kileleni mwa msimamo ili kutimiza ndoto za kuja kuwa mabingwa wapya nchini.
Mechi nyingine za kesho ni kati ya Mgambo JKT itakayoumana na 'majirani' zao Coastal Union katika pambano linalosubiriwa kwa hamu litakalochezwa kwenye uwanja wa  Mkwakwani, Tanga huku Mtibwa Sugar ya Morogoro itaialika Rhino Rangers ya Tabora katika dimba la Manungu, Morogoro.
Siku ya Jumapili kutakuwa na mechi moja tu itakayowakutanisha 'Wajelajela' Prisons ya Mbeya itakayoikaribisha timu ya Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.
Katika mechi zao mwisho, Prisons ililala mabao 2-0 mbele ya Mbeya City wakati Oljoro ililazimishwa suluhu na Ashanti United.
Mechi za kufungia duru la kwanza zitaanza kuchezwa Novemba 6 kwa pambano kati ya Jkt Ruvu dhidi ya Coastal Union, Ashanti United dhidi ya Simba, Kagera Sugar kuwa wenyeji wa Mgambo JKT na Ruvu Shooting kuumana na Mtibwa Sugar.
Siku inayofuata yaani Novemba 7, Azam itacheza na Mbeya City uwanja wa Chamazi, huku mabingwa watetezi Yanga itaikaribisha Oljoro JKT na Rhino Rangers itakuwa dimba la nyumbani kuikaribisha Prisons ya Mbeya.

Simba, Kagera Sugar zavuna Mil 32 Taifa

Na Boniface Wambura
MECHI ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Simba na Kagera iliyochezwa jana (Oktoba 31 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 32,726,000.

Washabiki waliohudhuria mechi hiyo namba 81 iliyomalizika kwa timu hizo kutoka sare ya bao 1-1 walikuwa 5,541 ambapo viingilio vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000.

Mgawo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) sh. 4,992,101.69, gharama za kuchapa tiketi sh. 3,183,890 wakati kila klabu ilipata sh. 7,242,252.45.

Wamiliki wa uwanja walipata sh. 3,682,501.25, gharama za mchezo sh. 2,209,500.75, Bodi ya Ligi sh. 2,209,500.75, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 1,104,750.37, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 859,250.29.

Yanga 'yachinja' tena maafande Taifa, Ngassa dah!


 Mfungaji wa mabao mawili ya timu ya Yanga dhidi ya JKT Ruvu katika mchezo wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara, Mrisho Ngasa akishangilia bao lake la kwanza katika mchezo uliofanyika leo kwenye Uwanjawa Taifa jijini Dar es Salaam.
 Mshambulijia wa Yanga, Hamis Kiiza akiwa katika harakati za kufunga.
Wachezaji wa Yanga wakishangilia.
Beki wa JKT Ruvu akiokoa moja ya hatari langoni mwake.
Kiungo wa JKT Ruvu, Nashon Naftal akimtoka Mrisho Ngasa.
Simon Msuva akichuana na Kessy Mapande wa JKT Ruvu.
Mashabiki wa Yanga wakishangilia timu yao.
Wachezaji wa Yanga wakishangilia bao la tatu lililofungwa na Oscar Joshua. (Picha zote: Francis Dande)
JANGWANI wanacheka! Ndivyo unavyoweza kusema kutokana na Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga kuendelea kutoa dozi kwa timu za majeshi baada ya jioni hii kuivurumusha JKT Ruvu kwa mabao 4-0 na kukalia kiti cha uongozi wa ligi hiyo.
Mabao mawili ya mapema ya Mrisho Ngassa 'Uncle' na mengine ya kipindi cha pili yaliyofungwa na beki wa kushoto, Oscar Joshua na jingine la Jerry Tegete yameifanya Yanga kufikisha pointi 25 kutokana na kucheza mechi 12, huku Ngassa akifikisha jumla ya mabao matano katika orodha ya wafungaji na Tegete kufikisha manne.
Ushindi huo wa Yanga ni wa tatu mfululizo kwa maafande wa Jeshi baada ya awali kuitafuna Mgambo mabao 3-0 kisha kuisulubu Rhino Rangers kwa idadi kaka hiyo kabla ya leo kuisasambua JKT Ruvu.
Mabingwa hao watetezi watamaliza mechi zao za duru la kwanza kwa kuvaana tena na maafande wengine Oljoro JKT pambano lityakalochezwa Alhamis ijayo kwenye uwanja wa Taifa.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena wikiendi hii katika viwanja viwanja vitano kuamliza mechi za raundi ya 12 kabla ya Jumatano na Alhamis kuhitimishwa kwa ligi hiyo ambayo msimu huu imekuwa na msisimko na ushindani mkubwa.


Msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2013-2014                                         P    W   D   L    F    A   GD  PTS
01. Yanga                   12    7    4    1   28  11   17    25
02. Azam                    11    6    5    0   17   7    10    23
03. Mbeya City           11    6    5    0   15   7     8     23
04. Simba                   12    5    6    1   22  11    11    21
05. Kagera Sugar        12    4    5    3   12    9    3     17
06. Ruvu Shooting       11    4    4    3   13   10   3     16
07. Mtibwa Sugar        11    4    4    3   16  15    1     16
08. Coastal Union        11    3    6     2   10   6    4     15
09. JKT Ruvu              12    4    0    8    9   16  -7     12
10.Rhino Rangers         11    2    4    5    9   15  -6     10
11.Ashanti                    11    2    4    5    10  19 -9     10
12.Prisons                    11    1    5    5     5   14 -9      8
13.Oljoro                     11    1    4    6     8    16 -8     7
14.Mgambo                 11    1    2    8     3    21 -18   5

Wafungaji:
9- Tambwe Amisi (Simba)
8- Hamis Kiiza (Yanga)
7- Elias Maguri (Ruvu Shooting), Juma Luizio (Mtibwa Sugar)
6- Kipre Tchetche (Azam)
5- Tumba Sued (Ashanti Utd), Themi Felix (Kagera), Didier Kavumbagu, Mrisho Ngassa (Yanga)
4-Peter Michael (Prisons), Jerry Santo (Coastal Union), Jerry Tegete (Yanga)
3- Haruna Chanongo, Jonas Mkude (Simba), Bakar Kondo (JKT Ruvu), Themi Felix (Kagera), Paul Nonga (Mbeya City), Salum Machaku (JKT Ruvu), Jerry Santo (Coastal Union),
2- Haruna Moshi, Crispian Odulla (Coastal Union), Saady Kipanga (Rhino Rangers), Mwagani Yeya, Jeremiah John, Peter Mapunda,(Mbeya City), Godfrey Wambura (Kagera Sugar), Shaibu Nayopa, Amir Omary (JKT Oljoro), Khamis Mcha (Azam), Shaaban Nditti (Mtibwa Sugar), Betram Mombeki, Ramadhani Singano (Simba), Said Dilunga (Ruvu Shooting)
1- Abdi Banda, Danny Lyanga (Coastal Union), Henry Joseph, Joseph Owino, Gilbert Kazze (Simba), Haruna Niyonzima, Nizar Khalfan, Simon Msuva, Frank Dumayo, Mbuyi Twitte, Oscar Joshua (Yanga), Iman Joel, Salum Majid, Mwalimu Musuku, Kamana Salum, Hussein Abdallah, Abbas Mohammed (Rhino Rangers), Gaudence Mwaikimba, Seif Abdallah,  Aggrey Morris,  John Bocco, Joseph Kimwaga, Faridi Maliki, Hamphrey Mieno, Salum Abubakar, Erasto Nyoni (Azam), Steven Mazanda, Richard Peter, Deo Deus  (Mbeya City), Laurian Mpalile (Prisons-OG), Shaaban Susan, Jerome Lembeli, Cosmas Ader  (Ruvu Shooting), Masoud Ally, Shaaban Kisiga (Mtibwa Sugar), Shaaban Juma, Anthony Matangalu, Paul Maono(OG), John Matei, Mwinyi Ally (Ashanti Utd), Abdallah Bunu, Emmanuel Switta, Amos Mgisa (JKT Ruvu), Fully Maganga, Hamis Msafiri (Mgambo JKT), Seleman Kibuta, Daud Jumanne, Maregesi Marwa, Clement Douglas, Salum Kanoni (Kagera Sugar), Paul Malipesa, Expedito Kidulo, Nurdin Mohammed, Fikiri Mohammed (Oljoro JKT)

Yanga kurejea kileleni kwa mgongo wa JKT Ruvu?

Yanga wataendelea kushangilia leo kama hivi
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga leo ina nafasi kubwa ya kurejea kileleni iwapo itapata ushindi mbele ya JKT Ruvu katika mfululizo wa mechi za raundi ya 12 itakayochezwa uwanja wa Taifa.
Yanga yenye pointi 22 kutokana na kucshuka dimbani mara 11, iwapo itaiangusha JKT ambayo imepoteza yale makali yake iliyopanza nayo ligi ilipoanza miezi mitatu iliyopita, itafikisha jumla ya pointi 25 na kuziengua Azam na Mbeya City waliotangulia kileleni ambao wana piinti 23.
Hata hivyo Yanga, haipaswi kuwadharau JKT Ruvu inayonolewa na kocha mahiri, Mbwana Makatta kwani huenda isikubali kugeuzwa ngazi na mabingwa hao kwenye uwanja wa Taifa.
Kocha Msaidizi wa Yanga, Fred Felix Minziro, alisema kikosi chao kipo imara kwa ajili ya pambano hilo japo kuna baadhi ya majeruhi na kiungo wao nyota, Haruna Niyonzima aliyeenda kwao Rwanda kwa matatizo ya kifamilia watakosekana kwenye pambano hilo la leo.
Wachezaji watakaoungana na Niyonzima kulikosa pambano hilo kutokana na kuwa majeruhi ni beki wa kushoto, David Luhende na kiungo mshambuliaji Nizar Khalfan'.
Minziro alisema pamoja na kuwakosa wachezaji hao, lakini wamejiandaa kuendeleza wimbi la ushindi kwa sababu wachezaji waliosalia bado ni imara na wana ari kubwa ya kuipa ushindi Yanga iliyopo nafasi ya tatu kwa sasa ikitangulia watani zao Simba ambao jana walilazimishwa sare ya 1-1 na Kagera Sugar.
Upande wa JKT Ruvu, kocha wake Mbwana Makatta alinukuliwa na kituo cha redio kwamba wanahisi uchovu wa safari waliokuwa nao ukawagharimu baada ya gari lao kuharibika njiani juzi wakirejea jijini toka mjini Tabora walipoenda kucheza na Rhino Rangers na kunyukwa bao 1-0.
Mbwana alisema hata hivyo watapigana kiume kuhakikisha hawapotezi pambano hilo, japo maafande hao kwa siku za karibuni wamekuwa mdebwedo kwa kufungwa mfululizo baada ya awali kushinda mechi tatu mfululizo.
Vijana hao wa JKT kwa sasa wana pointi 12 tu baada ya kucheza mechi 11, wakishinda nne na kufungwa saba na kuleta hisia kilichoikumba msimu uliopita iliponusurika kushuka daraja huenda ikarejea tena msimu huu japo ni mapema wakati duru la kwanza likiisha wiki ijayo.

Thursday, October 31, 2013

Je wewe ni msomi jisome uende kwenye usaili wa Polisi


Jeshi la Polisi Tanzania linawaita kwenye usaili wahitimu walioorodheshwa hapa chini wa vyuo vya Elimu ya Juu na  vya Ufundi  Stadi. 
Usaili utafanyika kuanzia tarehe 11/11/2003 hadi tarehe 15/11/2013 saa mbili asubuhi hadi saa kumi jioni kila siku kwa taaluma na maeneo yafuatayo;
  •  Fani za Menejimenti  ya Rasilimali Watu, Utawala, Uchumi, Usimamizi wa Sheria na Utekelezaji(BaLe), Ualimu, Sosholojia, Saikolojia na Ushauri Nasihi, Sheria, Takwimu, Lugha, Uhusiano wa Kimataifa, Uandishi wa habari na Mawasiliano ya Umma, Maendeleo ya Jamii, Ukutubi na Utunzaji Kumbukumbu. Usaili  wa fani hizi  utafanyika katika chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam(DPA) kilichopo kando kando ya barabara ya Kilwa Kurasini Dar es salaam .
  • Fani ya Udereva ,Ufundi rangi za magari(spray and Painting /Panel Beating ), Ufundi wa matengenezo ya Magari Makubwa(Auto-Mechanics-Heavy Duty) na Ufundi wa Matengenezo ya Umeme wa Magari(Auto Elecrical ). Usaili wa  fani hizi utafanyika Kikosi cha Polisi Ufundi kilichopo kando kando ya barabara ya Kilwa Kurasini Dar es salaam.
  • Fani za Kompyuta. Usaili wao utafanyika nyuma ya kikosi cha Ufundi yaani  TEHAMA KEKO chini.
  • Fani ya Uhandisi Mitambo(Mechanical Engineering ). Usaili wao utafanyika Kikosi cha Polisi Anga kilichopo Uwanja wa Ndege JK Nyerere DSM.
  • Waataalam wa masuala ya Afya/Wauguzi usaili wao utafanyika katika kikosi cha afya kilichopo kando kando ya barabara ya Kilwa Kurasini Dar es salaam.
  • Orodha  ya majina inapatikana  pia katika Gazeti la habari Leo la tarehe  04/11/2013.
   Muhimu: 
  1. (i)Mwombaji afike kwenyeakiwa na nakala  halisi  pamoja na kivuli cha  vyeti vyote vya masomo/Taaluma [Academic Transcript (s)/Certificate(s)]yaani  kidato cha nne, sita ,Chuo na cheti cha kuzaliwa.Hati ya kiapo cha kuzaliwa haitakubalika. 
  1. (ii)Mwombaji aliyeitwa kwenye usaili atalipia gharamaupimaji afya  shilingi elfu kumi(10,000), usafiri, chakula na malazi kwa muda wote wa zoezi la usaili.
 (iii)Kwa kuwa  muda ni mchache  anaekuja kwa usaili ajiandae baada ya usaili atakaechaguliwa  atapelekwa katika Chuo cha Taaluma ya Polisi Moshi siku nne baada ya usaili kwisha yaani tarehe 19/11/2013.
 Orodha ni kama ifuatavyo;

BOFYA HAPO CHINI UDOWNLOAD MAJINA

SOURCE: http://www.policeforce.go.tz

Maskini Mzee huyu afa ghafla mahakamani

Tiger Mwaigomole (70) Mkazi wa kata ya Masukulu wilayani Rungwe amefariki dunia ghafla akiwa katika chumba cha Mahakama ya Wilaya ya Rungwe akifuatilia mwenendo wa kesi inayomkabili mtoto wake wakati Mahakama ikiendelea.

MTU mmoja aliyefahamika kwa jina la Tiger Mwaigomole (70) Mkazi wa kata ya Masukulu wilayani Rungwe amefariki dunia ghafla akiwa katika chumba cha Mahakama ya Wilaya ya Rungwe akifuatilia mwenendo wa kesi inayomkabili mtoto wake wakati Mahakama ikiendelea.
Tukio hilo la aina yake lilitokea hivi karibuni majira ya saa 9 alasiri ndani ya Mahakama hiyo ambapo Marehemu alifika mahakamani hapo akiwa na mwanaye aliyejulikana kwa jina la Lusajo Tiger (40) wakiwa na lengo la kumwekea dhamana ndugu yao Gwakisa Tiger ambaye alifikishwa mahakamani hapo akituhumiwa kwa kosa la kupigana na kujeruhi katika ugomvi uliotokea kijijini kwao.
Kwa mujibu wa mtoto wa Marehemu aliyekuwa ameongozana nae Mahakamani hapo Lusajo Tiger alisema wakati kesi ikiendelea chini ya Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Rungwe, Kingwele, ndugu yao alipandishwa kizimbani kusomewa mashtaka yanayomkabili ndipo marehemu alipoanza kutetemeka kwa madai kuwa anajisikia baridi kali sana.
Alisema kutokana na marehemu kulalamikia baridi aliamua kumnunulia chai ya moto ili anywe na kupunguza baridi ambapo baada ya kufanya hivyo marehemu alikata roho muda mfupi baada ya kumaliza kunywa chai aliyokuwa amepelekewa huku akiwa amekaa ndani ya chumba cha mahakama hiyo.
Kutokana na tukio hilo Askari polisi waliokuwepo mahakamani hapo waliuchukua mwili wa marehemu na kuukimbiza katika Hospitali ya Wilaya ya Rungwe Makandana kwa ajili ya vipimo lakini hata hivyo mwili ulikabidhiwa kwa ndugu kwa ajili ya taratibu za mazishi ingawa ripoti ya kifo chake haikutolewa mapema.
Wakati huo huo Hukumu ya kesi ya mauaji dhidi ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Rungwe, John Mwankenja inayowakabili Hakimu Mwakalinga na wenzie watatu huenda ikatolewa Novemba 11 mwaka huu baada ya Mahakama kuu kanda ya Mbeya chini ya Jaji Samwel Karua kumaliza kusikiliza ushahidi wa upande wa mashtaka pamoja na utetezi kwa upande wa watuhumiwa.
Kwa mujibu wa Jaji Karua alisema baada ya kumaliza kusikiliza pande zote mbili atatumia muda wa siku mbili kwa ajili ya kuandika hukumu ambayo itaitoa Novemba 11, Mwaka huu, kesi ambayo inasimamiwa na Mwanasheria wa Serikali Archiles Mulisa huku watuhumiwa wakitetewa na Mawakili wawili wa kujitegemea ambao ni Simon Mwakolo na Victor Mkumbe.

Na Mbeya yetu

Simba yavutwa mkia jioni, mashabiki wang'oa viti FFU yawafurumusha kwa mabomu ya machozi

Kagera walioinyima raha Simba leo Taifa
BAO la mkwaju wa penati lililofungwa dakika za majeruhi na beki Salum Kanoni limeisaidia Kagera Sugar kunusurika kipigo toka kwa Simba baada ya kulazimisha sare ya 1-1 katika pambano la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Mwamuzi Mohammed Theophile wa Morogoro alitoa penati hiyo baada ya mabeki wa Simba kumuangusha Jumanne Daudi katika lango lao na kusababisha vurugu kubwa kutoka kwa mashabiki wa Simba ambao wanadaiwa walikuwa waking'oa viti na kulazimisha FFU kuvurumusha mabomu ya machozi.
Kabla ya penati, Simba ilionekana kuelekea kuibuka washindi katika pambano hilo lililokuwa kali kwa bao la dakika za majeruhi ya kipindi cha kwanza lililofungwa na Mrundi Amissi Tambwe.
Tambwe alifunga bao hilo kwa shuti kali na kuifanya Simba iende mapumziko ikiwa mbele kwa bao 1-0 ambalo liliendelea mpaka ilipofika dakika nne za nyongeza wakati Kagera waliposhambulia lango na wekundu hao wa msimbazi na kumchezea vibaya Daud.
Kitendo cha kutolewa kwa penati hiyo ilionekana kuwakera benchi nzima la Simba pamoja na mashabiki wao, lakini mwamuzi alisimamia msimamo wake na Kanoni aliyewahi kuichezea Simba kufunga bao hilo na kufanya mashabiki wa Msimbazi kuanza kung'oa viti kwa hasira.
Kwa matokeo hayo ya sare hiyo, Simba imeshindwa kurejea kileleni kwa kufikisha pointi 21 inayowafanya wasalie katika nafasi yao ya nne waliokuwa wakiishikilia nyuma ya Yanga ambayo kesho itashuka kwenye uwanja huo kuvaana na JKT Ruvu.
Azam na Mbeya City zinaendelea kubaki kileleni zikiwa na pointi 23 na Yanga wakifuatia nafasi ya tatu wakiwa na pointi 22 na kama kesho watashinda wanaweza kukaa kileleni mpaka Jumamosi wakati Azam itakaposhuka dimbani kuvaana na Ruvu Shooting.

Gareth Bale aanza mambo Real Madrid, Ronaldo aweka rekodi

Bale na Ronaldo wakipongezana
Bale akishangilia moja ya mabao yake ya jana
 WINGA nyota wa Wales, Gareth Bale ameanza kuonyesha cheche zake baada ya usiku wa kuamkia leo kufunga mabao mawili na kutengeneza mengine wakati Real Madrid wakishinda mabao 7-3 dhidi ya Sevilla.
Wakati Bale akionyesha uhalisia wa thamani ya donge nono alilosajiliwa na klabu hiyo ya Hispania, Mreno Cristiano Ronaldo alitupia kambani mabao matatu na kuweke rekodi.
Kocha Carlo Ancelotti aliwachezesha kwa pamoja washambuliaji hao na kuifanyia maafa makubwa Sevilla iliyomaliza mchezo ikiwa pungufu.
Bale lilikuwa pambano lake la kwanza kucheza kwa muda wote wa dakika 90 tangu aliposajiliwa na timu hiyo hivi karibuni.
Winga huyo alifunga mabao yake katika dakika za 13 na 27, huku Ronaldo akifunga hat trick yake kwa mabao ya dakika ya 32 lililokuwa la penati na mengine ya dakika za 60 na 71,\ na kumfanya awe mchezaji wa nne aliyefunga mabao mengi katika La Liga kwa wachezaji wa Real Madrid alimpiku gwiji Ferenc Puskas.
Ronaldo amefikisha jumla ya mabao 157 moja zaidi la Puskas, nyota wa zamani wa klabu hiyo na nchi ya Hungary.
Mabao mengine wa washindi hao yaliwekwa kimiani na Mfaransa, Karim Benzema katika dakika za 53 na 80.
Wageni wa Real Madrid walipata mabao yao matatu kupitia kwa Rakitic  aliyefunga mawili moja likiwa la penati katika dakika ya 38 na lingine dk ya 63 huku Bacca akifunga pia.
Katika mechi nyingine ya ligi hiyo ya Hispania, Ososuna iliishindilia Rayo Vallecano kwa mabao 3-1 na usiku wa leo kutakuwa na michezo miwili itakayozikutanisha timu za Villarreal dhidi ya Gitafe na Granada itakayovaana na Atletico Madrid.














Hii ndiyo ratiba ya 8 Bora Capital One


MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya England Manchester United imepangiwa kucheza ugenini dhidi ya Stoke City katika pambano lake la Robo Fainali ya Kombe la Ligi (Capital One) baada ya FA kutangaza ratiba ya Nane Bora.
Kwa mujibu wa ratiba hiyo ilivyo ni kwamba Manchester City nayo itacheza ugenini dhidi ya timu ya Daraja la Kwanza Leichester City, huku Tottenham Hotspur watakuwa nyumbani kuvaana na 'Wagonga Nyundo wa London' West Ham United.
Chelsea wenyewe wamepangiwa kuumana na mshindi wa mechi ya mwisho ya hatua ya nne ya michuano hiyo kati ya Sunderland na Southampton.

Tottenham, Manchester City zaifuata Chelsea, Man Utd Capital One League

Manchester City wakipongezana

Wachezaji wa Spurs wakipongeza baada ya kufuzu Roibo Fainali ya Capital One L:eague jana
TIMU za Tottenham Hotspur na Manchester City usiku wa kuamkia leo nazo zimefanikiwa kutinga hatua ya Robo Fainbaliu ya Kombe la League (Capital One) baada ya kupata ushindi kwa mbinde dhidi ya wapinzani wao kwenye mechi za raundi ya nne ya michuano hiyo.
Spurs ililazimika kusubiri mikwaju ya penati kuwavusha hatua hiyo mbele ya Hull City baada ya kumaliza dakika 120 zikiwa nguvu sawa ya kufungana mabao 2-2.
Ikicheza nyumba Spurs ilitangulia kupata bao la kuongoza dakika ya 16 kupitia kwa Gylfi Sigurdsson na kudumu hadi kipindi cha kwanza kinamalizika.
Kipindi cha pili kilianza kwa kipa wa Spurs, 'Babu' Brad Friedel kujifunga bao dakika ya 53 na kuisafanya Hull kupumua na kumaliza dakika 90 zikiwa bao 1-1 na katika dakika za 30 za nyongeza, McShane aliiandikia wageni bao dakika ya 99 kabla ya wenyeji kuchomoa dakika ya 108 baada ya Harry Kane kufunga bao na kuingia kwenye matuta ya penati.
Katika hatua hiyo Spurs ilifanikiwa kutumbukiza penati 8 na Hull City 7 na kufanya Spurs kuungana na vigogo vya Manchester United, Chelsea na Manchester City iliyopata ushindi wa mbinde ugenini dhidi ya  Newcastle United kucheza hatua ya Robo Fainali.
Man City iliishinda Newcastle 2-0 katika muda wa nyongeza baada ya awali kumaliza dakika 90 zikiwa nguvu sawa kwa kutofunagana.
Katika muda huo wa nyongeza mabingwa hao wa zamani wa Ligi Kuu ya England walipata mabao yao dakikka za 99 na 105 kupitia kwa Negredo na Eden Dzeko.
Timu nyingine zilizofuzu hatua hiyo ya Robo Fainali ya Capital One ni Stoke City, West Ham United na Leicester City, huku timu ya mwisho kumalizia nafasi moja iliyosalia itasubiri matokeo ya wiki ijayo kati ya Sunderland dhidi ya Southampton itakayochezwa Novemba 6.

Serikali kuondoa kodi vifaa vya michezo


Waziri Makalla
SERIKALI imeahidi kulifanyia kazi suala la kuondolewa kodi kwa vifaa vya michezo vinavyoingizwa nchini, hususani kwa matumizi ya shule na taasisi ya michezo.
Kauli hiyo ilitolewa juzi bungeni na Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amosi Makalla alipokuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Tabora Mjini, Ismail Rage (CCM).
Mbunge huyo alitaka kujua serikali ina mpango gani wa kuhakikisha vifaa vya michezo vinafutiwa kodi.
Akijibu swali hilo, Makalla alisema serikali imechukua hoja hiyo kama changamoto na kwamba itawasilishwa kwa wanahusika, ili ione kama vifaa hivyo vinavyoagizwa kutoka nje ya nchi kama vinaweza kufutiwa kodi, wakati wa kuingizwa kwake.
Awali, katika swali la msingi Mbunge wa Singida Magharibi, Mohamed Missanga (CCM), alitaka kujua serikali imefikia hatua ipi katika kuendeleza mchezo wa riadha nchini, ikiwa ni pamoja na kupelekwa kwa wataalamu kwenye nchi za Ethiopia na Kenya ili kujifunza mchezo huo.
"Nchi za Kenya na Ethiopia zinafanya vizuri katika mchezo wa riadha wakati Tanzania haifanyi vizuri, je, serikali imefikia wapi katika kutekeleza ushauri wangu niliotoa mwaka 2011 wa kupeleka wataalamu katika nchi hizo hili kujifunza mbinu na mikakati ya kukuza mchezo huu nchini?" alihoji Missanga
Akijibu swali hilo, Makalla alisema wizara hiyo imebaini kuwa nchi hizo zina mafanikio katika mchezo huo kwasababu ya kuzingatia mambo mbalimbali muhimu.
Makalla alisema miongoni mwa mambo hayo ni uhamasishaji na msingi wa kushiriki mchezo huo kuanzia katika umri mdogo katika ngazi za shule za msingi ikiwa ni pamoja na serikali sekta binafsi kuwekezaji katika mchezo huo.
Aliongeza kuwa mambo mengine muhimu yafanywayo na nchi hiyo katika kukuza mchezo huo ni uwapo wa vituo na shule maalum za kuendeleza mchezo huo, pamoja na uongozi thabiti wa mashirika ya mchezo huo.
Makalla alisema kwa kuzingatia mambo hayo, serikali imeanza kuyafanyia kazi kwa kadri ya uwezo wake kwa kushirikiana na Chama cha Riadha Tanzania.

Rais JK kushiriki mbio za Uhuru Marathon

Rais Jakaya Kikwete

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Jakaya Kikwete anatarajiwa kushiriki katika mbio maalum za Uhuru (Uhuru Marathon) zitakazofanyika Desemba 8 jijini Dar es Salaam imefahamika.
Mshindi wa jumla wa mbio hizo za marathoni (kilomita 42) atakabidhiwa zawadi ya Sh. milioni 3.5.
Akizungumza jana kwenye ukumbi wa Idara ya Habari (MAELEZO), Katibu Mkuu wa kamati ya maandalizi ya mbio hizo, Innocent Melleck, alisema kuwa Rais Kikwete atakabidhiwa fomu namba moja ya kujisajili katika ushiriki wa mbio hizo huku akimtaja Spika wa Bunge, Anne Makinda kuwa atapewa fomu namba mbili.
Melleck alisema kuwa viongozi hao watashiriki mbio za kilomita tatu na kumtaja mshiriki mwingine wa mbio hizo ni Kiongozi wa Kambi ya Upinzani bungeni na Mbunge wa Jimbo la Hai, Freeman Mbowe.
Alisema kuwa tayari fomu za kujiandikisha zimeanza kutolewa katika vituo mbalimbali nchini jana huku zoezi hilo likitarajiwa kufanyika kwenye viwanja vya Bunge mkoani Dodoma Jumanne na Jumatano wiki ijayo.
Alisema ada ya fomu hizo kwa mbio za marathoni ni Sh. 6,000 huku za kilomita tano zikiwa ni Sh. 2,000 na zitashirikisha pia wanariadha kutoka nje ya nchi.
Alieleza kuwa lengo la kuanzisha mbio hizo ni kutaka kuenzi na kudumisha amani iliyopo nchini na kukumbushana kutochezea thamani hiyo.
"Kupitia mbio hizi tutaweka tofauti zetu pembeni, Tanzania kwanza, Amani Kwanza," alisema katibu huyo wa kamati ya maandalizi.
Aliwataka wadau na taasisi mbalimbali kujitokeza kudhamini mbio hizo zitakazokuwa zinafanyika kila mwaka nchini.