 |
| Tabu :ley akiwa na Mbilia Bel |
BRUSSELS, Ubelgiji
MWANAMUZIKI mkongwe wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Pascal Tabu Ley
Rochereau, amefariki katika hospitali moja ya mjini Brussels.
Tabu Ley, alifariki juzi saa mbili usiku baada ya kuugua kwa muda mrefu
ugonjwa wa kiharusi. Alianza kuugua ugonjwa huo tangu 2008.
Meneja wa zamani wa mwanamuziki huyo, Mekansi Modero, ambaye kwa sasa
anaishi nchini Marekani, amethibitisha taarifa za kifo cha Tabu Ley,
baada ya kuthibitishiwa na ndugu wa karibu wa mkongwe huyo.
Mwanamuziki Nyboma Mwandido, anayeishi mjini Paris, Ufaransa pia amethibitisha taarifa za kifo cha mwanamuziki huyo mkongwe.
Tabu Ley alikuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa huo kwa muda mrefu na
alikuwa akitembea kwa kutumia baiskeli maalumu kutokana na kushindwa
kutembea kwa miguu.
Kifo cha Tabu Ley kimewapa simanzi kubwa mashabiki wa muziki barani
Afrika, kutokana na kuwa mmoja wa watu mahiri, ambaye nyimbo zake
zilikuwa na mvuto wa aina yake.
Katika miaka ya hivi karibuni, Tabu Ley aliamua kuachana na muziki na
kujitosa katika masuala ya siasa, baada ya kuteuliwa kuwa waziri katika
serikali ya Rais wa zamani wa DRC, Laurent Kabila mwaka 1997
Awali, Tabu Ley alilazimika kuikimbia DRC na kwenda kuishi uhamishoni
nchini Ubelgiji kutokana na kutoelewana na rais wa zamani wa nchi hiyo,
marehemu Mobutu Sese Seko.
Kabla ya kwenda Ubelgiji, Tabu Ley aliishi kwa muda nchini Ufaransa
akipatiwa matibabu ya ugonjwa huo. Baada ya hali kuanza kuwa mbaya,
alihamishiwa Ubelgiji kwa ajili ya kupatiwa matibabu maalumu.
Enza za uhai wake, Tabu Ley alikuwa akichuana vikali na wakati nyota wa
DRC wa wakati huo kama vile Joseph Kabasele, Nicolas Kasanda na Rwambo
Lwanzo Makiadi 'Franco'.
Alianza kujihusisha na muziki 1959 akiwa mtunzi, mwimbaji na mcheza shoo
akiwa katika bendi ya African azz, iliyokuwa ikiongozwa na Kabasele.
Mkongwe huyo amerekodi na kuimba nyimbo zaidi ya 2,000 na kutoa albamu
250.
Alizaliwa 1940 katika mji wa Bandundu nchini DRC. Alianza
maisha akiitwa Pascal Tabu. Akiwa na umri wa miaka 14, aliandika wimbo
wake wa kwanza Bessama Muchacha, ambao aliurekodi na kundi maarufu la
African Jazz, lililokuwa chini ya Kasebele, (asichanganywe na Pepe
Kalle).
Aliendelea na shule na hatimae alipomaliza sekondari 1959, ndipo alipojiunga rasmi na African Jazz.
Alikuwa mmoja wa wanamuziki walioimba wimbo Independence Cha Cha, wa
Grande Kalle, uliotikisa anga la Afrika miaka ya 1960. Wimbo huo ukawa
rasmi wa kusherehekea uhuru wa DRC.
Baada ya miaka minne, alijiengua katika kundi la African Jazz. Akiwa na
mpiga gita mahiri, Nicholaus Kassanda, wakaanzisha kundi la African
Fiesta, ambalo alidumu nalo hadi 1965.
Wakati DRC ikiwaka moto kimuziki na ushindani kuwa mkali, aliamua
kuachana na Nico na kuanzisha kundi lake la African Fiesta National au
mara nyingine ikiitwa Africa Fiesta Flash na kurekodi kibao maarufu cha
Afrika Mokili Mobimba, ambacho kilivuka mauzo ya nakala milioni moja
miaka ya 1970 na kuiingiza bendi hiyo kuwa kati ya bendi zilizopata
mafanikio ya juu katika Afrika kwa wakati huo.
Wanamuziki kama Papa Wemba na Sam Mangwana ni miongoni mwa wakongwe waliowahi kupitia katika kundi hili tishio.
Mwaka 1970, Tabu Ley alianzisha bendi ya Orchestre Afrisa International.
Wakati huo Afrisa na TPOK Jazz, ndizo zilizokuwa bendi maarufu zaidi
Afrika. Afrisa waliteremsha vibao kama Sorozo, Kaful Mayay, Aon Aon na
Mose Konzo.
Kutokana na umahiri wake, Tabu Ley aliweza kupata tuzo kutoka serikali
za nchi kama Chad, iliyompa heshima ya 'Officer of The National Order'
wakati Senegal ilimpa heshima ya 'Knight of Senegal' na akawa sasa
anaitwa Siegneur Rochereau.
Katikati ya miaka ya 1980, Tabu Ley aligundua kipaji cha mwanamama
aliyekuja kutikisa anga za Afrika, Mbilia Bel. Baadae Tabu Ley alimuoa
Mbilia, wakapata mtoto mmoja.
Nyimbo kama Nadina, Nakei Nairobi zinaonyesha kipaji gani alikuwa nacho
mwanamama huyo, aliyekuwa mzuri kwa sura, aliyejua pia kucheza na
kutawala jukwaa vizuri.
Mwaka 1988, Tabu Ley akagundua kipaji cha mwimbaji mwingine wa kike,
Faya Tess. Hapo Mbilia akaacha bendi na kuendelea na maisha yake ya
muziki peke yake. Katika kipindi hicho, mtindo wa Soukus uliokuwa na
mapigo yenye mwendokasi zaidi ya ile ya rumba ya Afrisa na TP OK Jazz,
ulianza kuzishika nyoyo za vijana, bendi hizi kubwa zikaanza kufifia.
Mwanzoni mwa miaka ya 1990, Tabu Ley, alihamia Marekani, akawa anaishi
Kusini mwa California na kubadili muziki wake katika kujaribu kujikita
zaidi katika soko la kimataifa.Akatunga nyimbo kama Muzina, Exil Ley na
Babeti Soukous.
Mwaka 1996, Tabu Ley, alishiriki katika album ya kundi la Africando,
akiimba wimbo wa Paquita, ambao aliurekodi miaka ya 1960, akiwa na
African Fiesta.
Tabu Ley alipata cheo cha uwaziri katika utawala wa Kabila baada ya
kuondolewa kwa Mobutu. Hata baada ya kifo cha Kabila, 2005, alipewa cheo
cha gavana.
Mwaka 2006, Tabu Ley, alishirikiana na rafiki yake wa muda mrefu,
Maika Munah na kurekodi album yake ya mwisho, iliyoitwa Tempelo. Katika
albumu hiyo, binti yake, Melodie aliimba nyimbo kadhaa.
Inaelezwa kuwa mkongwe huyo ameacha zaidi 54 kutoka kwa wanawake 36 aliozaa nao kwa nyakati tofauti.