STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, July 29, 2012

UBALOZI WA UAE WAFUTURISHA WAUMINI DAR

UBALOZI wa Nchi ya Falme za Kiarabu, UAE nchini kupitia taasisi ya kutoa huduma za kijamii ya Khalifa Bin Zaayid Al Nahyaan, umeamua kuwafuturisha waumini wa dini ya kiislam wa Msikiti wa Al Rahman wa Dar es Salaam kwa mwezi mzima wa mfungo wa Ramadhani. Msaada huo wa futari ulianza kutolewa tangu kuanza kwa mfungo wa mwezi huo siku 10 zilizopita na juzi MICHARAZO lilishuhudia ugawaji wake kwa waumini hao ambao imewafanya wapate fursa ya kuwa na uhakika wa kula baada ya funga zao. Imamu wa Msikiti huo wa Al Rahman uliopo eneo la Kinondoni, Sheikh Abdullah Salim Bahssany, akiwahutubia waumini wake wakati wakigawiwa futari hiyo, alisema huo ni msaada toka ubalozi wa UAE na utakuwa ukitolewa hapo kila siku hadi mwezi mtukufu wa Ramadhani utakapomalizika mwishoni mwa mwezi ujao. Imamu huyo aliwaambia waumini hao kuwa wale waliokuwa na shaka na kupata futari katika funga zao, waondoe hofu kwani sasa watakuwa wakipata chakula hicho, huku akiushukuru ubalozi huo kwa ukarimu iliyouonyesha kwa waumini hao. "Jamani futari mnayokula leo imetolewa na ubalozi wa nchi za Falme za Kiarabu na msaada huu utakuwa ukitolewa kwa mwezi mzima katika mfungo huu wa Ramadhani hivyo msiwe na hofu katika funga zenu,"alisema Sheikh Bahssany. Nao baadhi ya waumini waliofuturishwa msikiti hapo waliushukuru ubalozi huo na kuomba watu wengine wenye uwezo kuiga mfano huo wakidai mwezi huu ndio wa waumini wa kweli kuonyesha upendo, ukarimu na kuhurumiana katika kutekeleza nguzo ya nne kati ya tano za Imani za Kiislam. "Wengine wetu tunafunga lakini hatuna hakika ya kupata futari, lakini kwa hili linalofanywa na ubalozi huu ambao hata mwaka jana walitusaidia tunashukuru na kuomba wengine wawe wanatukumbuka wanyonge kama sisi," alisema muumini mmoja aliyekataa kutajwa jina lake gazetini. Mwisho

Monday, July 2, 2012

Yanga yakubali kwenda Zenji kushiriki Kombe la Urafiki

HATIMAYE timu ya soka ya Yanga imeamua kubadili msimamo wake wa kushiriki michuano ya Urafiki kwa kukubali kwenda visiwani Zanzibar kushiriki, ambapo inatarajiwa kuondoka leo sambamba na watani zao Simba. Awali uongozi wa Yanga 'ulichomoa' kushiriki michuano hiyo, lakini baada ya 'vikao' na waandaji wake, uongozi huo umelegea na kukubali kwenda kushiriki. Katibu Mkuu wa Yanga, Celestine Mwesigwa, alisema wamekubali baada ya kuridhiana na waandaaji na pia kwa vile michuano hiyo ina lengo la kudumisha urafiki baina ya timu za Tanzania Bara na Visiwani, hawakuona sababu ya kuigomea. "Tunaenda kushiriki, tutaondoka kesho asubuhi kuwahi michuano hiyo na tunaamini tutafanya vema na tutaaitumia kwa ajili ya fainali za Kombe la Kagame," alisema Mwesigwa. Mwesigwa alisema Yanga itaenda Zanzibar ikiwa na kikosi chake kamili ambacho Jumamosi iliitoa nishai Mabingwa wa Uganda, Express kwa kuilaza mabao 2-1 kwenye mechi ya kirafiki ya kimataifa iliyochezwa jijini Dar. Yanga ndio mabingwa watetezi wa michuano hiyo ya Kagame na itafungua dimba Julai 14 kwa kuumana na Atletico ya Burundi. Timu nyingine za Tanzania Bara zitakazoshiriki michuano hiyo ya Urafiki ni Simba ambao jioni ya leo inatarajiwa kushuka dimba la Amaan kuumana na Mafunzo.

Hispania wabeba tena ubingwa wa Ulaya

WAFALME wa soka wa Dunia, Hispania usiku wa kuamkia leo iliweka rekodi ya aina yake kwa kutwaa ubingwa wa Ulaya kwa mara ya pili mfululizo baada ya kuisambaratisha Italia kwa mabao 4-0. Ushindi katika mechi hiyo ya kusisimua iliyokuwa ya kushambuliana mwanzo mwisho , imeifanya mabingwa hao wapya wa Ulaya kuwa timu ya kwanza katika historia kutwaa mataji mawili mfululizo, huku ikiwa pia na taji la Dunia iliyotwaa katika fainali za mwaka 2010 zilizochezwa barani Afrika. Hispania imefuata nyayo za Argentina iliyowahi kutwaa mataji matatu mfululizo kwa kutwaa ubingwa wa Copa Amerika wakati michuano hiyo ikichezwa kila mwaka kati ya a 1945 hadi 1947. Ikiwa na kiu ya kutaka kudhihirisha kuwa wao ni wababe wa kweli wa soka duniani kwa sasa, Hispania iliucheza mchezo huo kwa kushambulia mwanzo mwisho na kujiandikia bao la kwanza katika dakika ya 14 kupitia kwa David Silva aliyefunga kwa kichwa. Bao la pili la wakali hao wanaonolewa na Vicente del Bosque liliingizwa kimiani na dakika nne kabla ya mapumziko kupitia beki wa kushoto Jordi Alba baada ya kuwatambuka walinzi wa Italia na kumtungua kipa Gianluigi Buffon. Italia iliyokuwa ikijaribu kurejea tukio lililowashtua mashabiki wengi wa soka kwa kuikwamisha Ujerumani katika mechi ya nusu fainali, kwa kuilaza mabao 2-1 ilishindwa katika kufurukuta Kwa Hispania hasa baada ya kuumia kwa Thiago Motta wakati wakiwa wameshamaliza orodha ya wachezaji wa akiba na kucheza pungufu dimbani. Wengi wakiamini huenda mechi ingeisha kwa idadi ya mabao 2-0, Fernando Torres 'El Nino' alikuwa mchezaji wa kwanza kufunga goli katika mechi mbili za fainali za Euro wakati alipopachika bao la tatu dakika ya 84. Torres, pia alifunga goli la ushindi katika fainali mwaka 2008 wakati walipotwaa ubingwa. Dakika mbili kabla ya kumalizika kwa pambano hilo kiungo matata wa Chelsea, Juan Mata aliifungia Hispania bao la nne lililoikatisha tamaa kabisa Italia ambao walitawala mchezo huo dakika za mwanzoni kabla ya kupoteana na kukimbizwa.

Sunday, July 1, 2012

Azam Marine yaleta meli ya kisasa, abiria kusafiri na magari yao

Kampuni za meli za Azam Marine, imeamua kufanya kweli ambapo hivi karibuni inatarajia kuzindua meli kubwa ya kisasa ambayo itawawezesha abiria wake kwenda na magari yao visiwani Zanzibar. Meneja Mkuu wa kampuni hiyo Hussein Mohammed Said, amesema Julai 15 mwaka huu meli hiyo yenye urefu wa mita 100 itazinduliwa. Mohamedi alisema shida ya usafiri itapungua kwa asilimia kubwa kutokana na meli hiyo kuwa na uwezo wa kubeba abiria 1500, Mizigo tani 500 na magari 200 ambapo abiria atakae jisikia kwenda na gari lake Zanzibar, Pemba au Dar es Salaam ataweza kufanya hivyo. Waziri Mwenye dhamana ya Mawasiliano na Miundombinu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Hamadi Masoud, alithibitisha kwamba ana taaarifa za ujio wa meli hiyo ambayo alisema kwa kiasi kikubwa itakuwa ni ya kutoa huduma tu na siyakutengeneza faida. Meli hiyo inauwezo wa kwenda kasi ya notkomail 20.
MELI HIYO INAVYOONEKANA NDANI NA NJE

Lamata: Muongozaji anayeota kuwafunika 'madume' kimataifa

HUENDA akawa ndiye muongozaji pekee wa kike anayewapeleka puta waongozaji wengine wa kiume waliojaza nchini kwa namna anavyoifanya kazi yake kwa ufanisi wa hali ya juu. Wengi wanamfahamu kwa jina la 'Lamata', ingawa majina yake halisi ni Leah Richard Mwendamseke, mmoja wa waandishi wa miswada na waongozaji mahiri wa filamu nchini. Lamata, alisema aliipenda kazi hiyo tangu akiwa mtotoni na ndio maana alitumia muda mfupi kama muigizaji akiwa na kundi la Amka Sanaa lililorusha michezo yake katika kituo cha ITV kabla ya kugeukia uongozaji wa filamu. Mwanadada huyo alisema, mara alipoosha 'nyota' kwa kushiriki igizo la 'Ndoano' alijiunga na kampuni ya RJ chini ya Vincent Kigosi 'Ray' na Blandina Chagula 'Johari' kuandaa filamu huku akijifunza uongozaji kabla ya kuianza rasmi kazi hiyo mwaka 2010. Lamata, anayemiliki kampuni yake binafsi iitwayo 'Lamata Enterteinment, alisema kupenda kwake kuangalia filamu na kusoma vitabu vimechangia kuwa 'malkia' wa uandishi miswada na kuongoza filamu kazi aliyodai imemsaidia kwa mengi kimaisha. Alisema mbali na Ray, pia hawezi kuwasahau Salles Mapunda na Adam Kuambiana waliomnoa sambamba na kujifunza uongozaji wa filamu kupitia njia ya mtandao kiasi cha kuwa muongozaji pekee wa kike anayeifanya kazi hiyo kama ajira rasmi. Baadhi ya kazi alizoziandika na kuziongoza ni pamoja na Candy, All about Love, My Angel, Rude, My Princess, Tears Forever, Time After Time, Dunia Nyingine, Mke Mwema, Mr President, Chocolate, Life to Life, The Avenger, Family War na kazi zilizopo njiani kutoka za House Maid na Injinia. Lamata anayependa kula pilau na chips kwa kuku na kunywa vinywaji laini, alisema kati ya kazi zote alizoziandika na kuziongoza zilizo bomba kwake na kujivunia ni Candy na Rude. Mwanadada huyo anayechizishwa na nguo za rangi ya zambarau na pinki, alisema kabla ya kuingia kwenye filamu aliwazimia mno Desire Washington, Mel Gibson na James Canon, Juu ya filamu Bongo, Lamata ambaye hajaolewa wala kuwa na mtoto ingawa anatamani kuja kuzaa watoto watatu atakapoolewa, alisema imepiga hatua kubwa kulinganisha na miaka ya nyuma ila alisema wapo watu wachache wanaoikwamisha kuvuka mipaka ya kimataifa. Alisema ni watayarishaji wabishi wasiokubali kukosolewa na kugawa majukumu ya kazi kwa wengine na wasanii wasiotambua wapo katika fani hiyo kwa ajili ya kitu gani. Pia alisema wizi na uharamia uliokithiri katika fani hiyo na kukosekana kwa wasambazaji wengi wa kutosha ni tatizo ambalo aliiomba serikali kujaribu kuwasaidia ili wasanii wainuke kimaisha. Lamata mwenye ndoto za kuja kuwa muongozaji wa kimataifa na kujikita kwenye biashara, alimtaja msanii Jacklyne Wolper kama msanii anayemkubali na kumuona yupo makini katika fani hiyo nchini na anayefurahia kufanya nae kazi kama ilivyo kwa Jennifer Kyaka 'Odama'. Muongozaji huyo aliyewaasa wasanii na wadau wote wa filamu kupendana na kushikiana, alisema ukimuondoa Mungu na Yesu Kristo wengine anawashukuru kumfikisha alipo ni Ray, Wolper na Daniel Basila. Leah Richards Mwendamseke 'Lamata' alizaliwa miaka kadhaa iliyopita mjini Mbeya akiwa mtoto wa mwisho wa familia ya watoto sita na alisoma Shule za Msingi Ikuti na Karobe kabla ya kujiunga na Shule ya Sekondari za Arage Mbeya aliyosoma hadi kidato cha pili. Alimalizia masomo yake ya sekondari katika shule ya Wanging'ombe ya mjini Iringa na kisha kuendelea na masomo ya juu ya Sekondari Shule ya Perfect Vision kabla ya mwaka 2008 kujitosa kwenye sanaa akianzia kundi la Amka Sanaa lililotamba katika kituo cha ITV.

LEO NDIO LEO FAINALI ZA UERO 2012

MABINGWA watetezi wa Kombe la nchi za Ulaya, Hispania leo inatarajiwa kushuka dimbani kujaribu kuendeleza rekodi yake katika michuano ya kimataifa kwa kuvaana na Waitalia. Timu hizo mbili zilizofuzu fainali za mwaka huu za barani humo, zitaavanaa kila moja ikitaka kudhihirisha ubabe wake baada ya mechi yao ya awali ya makundi kuisha 1-1. Baina ya nchi hizo Hispania na Italia zimetoa mabingwa 25 wa Ulaya katika ngazi ya klabu lakini hii itakuwa mara ya kwanza kwa timu zao za taifa kukutana katika fainali ya kombe la Mataifa ya Ulaya. Ni wachache watahoji uhalali wa timu hizo kufika fainali. "Mshindi atakuwa bingwa anayestahili," alisema kiungo wa Hispania Cesc Fabregas. "Nadhani timu hizi mbili ndiyo zimekuwa na matokeo mazuri mfululizo katika michuano hii." Italia ni mabingwa mara nne wa Kombe la Dunia, mara ya mwisho 2006, wakati Hispania inajaribu kufanya kitu cha kipekee kwa kuwa timu ya kwanza kutwaa mfululizo vikombe vitatu vikubwa baada ya Euro 2008 na Kombe la Dunia miaka miwili iliyopita. Wakati mafanikio ya Vicente Del Bosque na Hispania yamejengwa katika safu imara ya ulinzi na kukaa muda mrefu na mpira, Italia imefika fainali kutokana na kufanya mashambulizi mfululizo yakiongozwa na mtukutu Mario Balotelli ambayo yaliiwezesha kuitoa Ujerumani katika nusufainali. Mfumo wa Hispania, wa pasi fupi-fupi 'Tiki Taka' umewapa mafanikio ya kujivunia - hakuna timu ya Ulaya tangu Ujerumani Magharibi mwanzoni mwa miaka ya 1970 imefanikiwa kucheza fainali tatu mfululizo za michuano mikubwa. Lakini 'enzi ya Hispania' kwa namna nyingi itaelezewa na jinsi itakavyokabiliana na timu iliyoshangaza kwa kucheza soka la kuvutia ya Italia leo. Kuweka historia ya kutwaa taji la tatu mfululizo, huku vigogo Ujerumani na Uholanzi vikiwa vilishafunga virago kwenye fainali hizi, kutaiweka Hispania kama moja ya timu kabambe zaidi zilizowahi kutokea. Lakini kipigo, mwishoni mwa fainali ambazo wameshindwa kuchengua mashabiki, kutaendelea kuitambulisha 'La Roja' kama moja ya timu za kawaida miongoni mwa vigogo vya soka. Hispania imefika hatua hiyo ya fainali kwa kuiondosha kwa mikwaju ya penati 4-2 wareno wakiongozwa na nahodha wao Cristiano Ronaldo, huku Waitalia maarufu kama 'Azzurri' waliwanyamazisha waliokuwa wakipewa nafasi kubwa ya kuwa mabingwa wa mwaka huu, Ujerumani kwa mabao 2-1, magoli yaliyofungwa na 'mtukutu' Mario 'Super Mario' Balotelli ambaye ana asili ya Afrika hususani nchini Ghana.

Ratiba ya Kagame Cup 2012 hadharani

Release No. 102 TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI Juni 29, 2012 YANGA KUANZIA KWA ATLETICO KOMBE LA KAGAME Mabingwa watetezi wa Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame) wataanza kutetea ubingwa wao Julai 14 mwaka huu dhidi ya Atletico ya Burundi kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), Nicholas Musonye ametangaza ratiba ya michuano hiyo leo (Juni 29 mwaka huu) katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Timu 11 zitashiriki katika michuano hiyo itakayoanza Julai 14 hadi 28 mwaka huu ambapo kwa siku zitachezwa mechi mbili (saa 8 mchana na saa 10 jioni) huku Tanzania Bara ikiwakilishwa na Yanga, Simba na Azam. Mechi ya kwanza siku ya ufunguzi (saa 8 mchana) itakuwa kati ya APR ya Rwanda na Wau Salaam ya Sudan Kusini. Kundi A lina timu za Simba, URA ya Uganda, Vita Club ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) na Ports ya Djibouti. Azam, Mafunzo ya Zanzibar na Tusker ya Kenya ziko kundi B. Yanga inaunda kundi C lenye timu za APR ya Rwanda, Wau Salaam ya Sudan Kusini na Atletico ya Burundi. Timu nane zitaingia robo fainali itakayochezwa Julai 23 na 24 mwaka huu. Kundi A na C kila moja litatoa timu tatu kwenda robo fainali wakati B litatoa timu mbili. El Merreikh ya Sudan, Red Sea ya Eritrea, Coffee ya Ethiopia na Elman ya Somalia hazitashiriki katika mashindano ya mwaka huu ambayo yanafanyika Tanzania Bara kwa mwaka wa tatu mfululizo kutokana na sababu mbalimbali. Coffee haitashiriki kwa vile ligi ya Ethiopia inaanza Julai 14 mwaka huu wakati El Merreikh wikiend ya Julai 13-15 mwaka huu itakuwa na mechi ya michuano ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF). Bingwa wa michuano hiyo atapata dola 30,000, makamu bingwa dola 20,000 na mshindi wa tatu dola 10,000. Michuano hiyo itaoneshwa moja kwa moja (live) na Televisheni ya SuperSport. KAGAME CUP 2012 FIXTURE Sat. 14th July 1 APR vs WAU SALAAM Uwanja wa Taifa 2pm 2 YANGA vs ATLETICO Uwanja wa Taifa 4pm Sun. 15th July 3 AZAM vs MAFUNZO Chamazi 4pm Mon. 16th July 4 VITA CLUB vs PORTS Uwanja wa Taifa 2pm 5 SIMBA vs URA Uwanja wa Taifa 4pm Tue. 17th July 6 ATLETICO vs APR Uwanja wa Taifa 2pm 7 WAU SALAAM vs YANGA Uwanja wa Taifa 4pm Wed. 18th July 8 VITA CLUB vs URA Uwanja wa Taifa 2pm 9 PORTS vs SIMBA Uwanja wa Taifa 4pm Thu. 19th July 10 ATLETICO vs WAU SALAAM Uwanja wa Taifa 2pm 11 MAFUNZO vs TUSKER Uwanja wa Taifa 4pm Fri. 20th July 12 PORTS vs URA Uwanja wa Taifa 2pm 13 YANGA vs APR Uwanja wa Taifa 4pm Sat. 21st July 14 AZAM vs TUSKER Uwanja wa Taifa 2pm 15 SIMBA vs VITA CLUB Uwanja wa Taifa 4pm Sun. 22nd July REST DAY QUARTER FINALS Mon. 23rd July 16 B2 vs C2 17 A1 vs C3 Tue. 24th July 18 C1 vs A2 19 B1 vs A3 Wed. 25th July REST DAY SEMI FINALS Thu. 26th July 20 Winner 16 vs Winner 17 21 Winner 18 vs Winner 19 Fri. 27th July REST DAY FINALS AND 3rd PLACE PLAY OFFS Sat. 28th July 22 Loser 20 vs Loser 21 23 Winner 20 vs Winner 21 Boniface Wambura Ofisa Habari Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Licha ya mafanikio, Diamond hajamsahau Mungu wake

NYOTA wa muziki wa kizazi kipya nchini, Naseeb Abdul 'Diamond' amesema licha ya mafanikio makubwa aliyonayo katika sanaa hiyo, bado haachi kufanya ibada kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa kumfikisha hapo alipo. Akizungumza na MICHARAZO, Diamond anayetamba na nyimbo kama 'Moyo Wangu', Lala Salama' na Nimepende Nani, alisema ni vigumu kumsahau Mungu kwani anaamini ndiye aliyemnyanyua hapo alipo kisanii. Diamond, alisema jambo la kumkumbuka Mungu na kufanya ibada ni kitu kinachopaswa kufanywa na kila mtu hususani wasanii ambao hutumia muda wao mwingine katika kufanya shughuli zao kiasi cha kubanwa kufanya ibada. "Kaka huwezi amini sijamsahau Mungu, naendelea kufanya ibada kama kawaida kwa sababu najua bila ya uwezo na mapenzi yake Mungu, nisingefika kokote," alisema. Mkali huyo alisema, kumtanguliza Mungu katika kila analofanya pamoja na kujibidiisha kufanya mazoezi na kuumiza kichwa kuandaa kazi makini, zimemfanya awe mmoja wa wasanii wenye majina makubwa kwa sasa nchini na ukanda mzima wa Afrika Mashariki. Aliongeza kwa sasa anajiandaa kupakua kazi mpya ambazo zitazidi kumweka katika matawi ya juu nchini. "Nipo katika maandalizi ya kupakua kazi mpya, hivyo mashabiki wangu wakae mkao wa kula," alisema.

Watayarishaji wengi wa filamu wabishi- Lamata

MMOJA wa waongozaji wa filamu wa kike nchini, Leah Richard Mwendamseke 'Lamata' amesema baadhi ya watayarishaji wa filamu hawataki kukosolewa katika kazi zao na kufanya filamu nyingi kukosa ubora wa kimataifa. Pia, alisema kama watayarishaji hao hawatawadharau waongozaji na kuwathamini wasanii wanaozicheza filamu zao, huenda soko la filamu katika anga la kimataifa likapanuka na kuchuana na zile za nchi za Nigeria, Ghana na kwingineko. Lamata, aliyasema hayo alipozungumza na MICHARAZO na kusema, licha ya kwamba waongozaji ndio wenye nafasi kubwa ya kubebeshwa lawama kazi ikiwa mbaya, ila ukweli wengi wao wanaangushwa na ubishi walionao watayarishaji wa filamu wasiopenda kuelekezwa. Muongozaji na mwandishi huyo wa filamu, alisema wapo watayarishaji hata wakielekezwa kufanya mabadiliko katika kazi zao ili kuziboresha hukataa na kuamini wapo sahihi na kusababisha kazi nyingi kulipuliwa na kushindwa kutamba sokoni. "Pia wamekuwa wakiwadharau waongozaji na kuwathamini zaidi wasanii bila kujua injini ya filamu kuwa nzuri ni muongozaji makini anayeweza kupangilia kazi kulingana na hadithi ilivyo na namna ya kuiboresha ili iendane na uhalisi unaosisimua," alisema. Alisema kama watayarishaji na baadhi ya wasanii wataamua kubadilika na kufanya kazi kwa lengo la kuiinua sanaa hiyo ni wazi filamu za Tanzania zinaweza kutamba kimataifa na kuchuana na kazi za mataifa mengine ambayo wamekuwa vinara kwa miaka mingi iliyopita. Mwanadada huyo aliyeziongoza filamu kadhaa kama 'My Princess', 'Candy', 'Mr President', 'Rude' na sasa akimalizia kazi mpya ya 'Injinia', alisema wapo baadhi ya wasanii hawajui wapo katika sanaa hiyo kwa sababu ipi kwa mambo wanayoyafanya.

Okwi kupaa kwenda Parma ya Italia

MSHAMBULIAJI wa kutumaini wa kimataifa wa timu ya soka ya Simba, Emmanuel Okwi anatarajiwa kutua nchini Italia kwa ajili ya kufanyiwa majaribio katika klabu ya Parma inayoshiriki Ligi ya Seria A, baada ya kuzitosa ofa za timu za Afika Kusini. Mganda huyo ambaye amekuwa chachu kubwa ya Simba kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu msimu uliopita, anatarajiwa kwenda nchini humo, keshokutwa. Habari za kuaminika toka ndani ya Simba na kuthibitishwa na mmoja wa wajumbe wa kamati ya Utendaji aliyekataa kutajwa jina lake, zinasema kuwa Okwi anaenda huko kwa ajili ya kufanya mazungumzo na Parma. "Ni kweli Okwi anatarajiwa kutua Italia Julai 4 kwa ajili ya kufanya mazungumzo na klabu ya Seria A ya Parma kwa ajili ya kujiunga nao kwa msimu ujao baada ya kuachana na ofa za klabu za Orlando Pirates, Mamelodi Sundowns na Super Sports zilizokuwa zikimtaka," chanzo hicho kilidokeza. Chanzo hicho kilidokeza kuwa, iwapo Mganda huyo atafanikuwa kunyakuliwa na Parma huenda Simba ikavuna mamilioni ya fedha kwa usajili huo. Hata hivyo Simba italazimika kugawana mgao huo unaokadiriwa kufikia Sh Bilioni 2 na klabu ya Sc Villa ya Uganda iliyowauzia nyota huyo ambaye aliidhalilisha Yanga kwenye mechi ya kufungia msimu kwa kufunga mabao mawili na kusaidia jingine moja. Hiyo haitakuwa mara ya kwanza Simba kuuza wachezaji wake na kuvuna fedha, kwani mwaka jana iliwauza Mbwana Samatta na Patr
ick Ochan kwa TP Mazembe na kuvuna fedha za kutosha hiyo ni mbali na zile za akina Danny Mrwanda, Henry Joseph na wengineo.

Yanga yatamba 'MTATUKOMA' safari hii

UONGOZI wa
klabu ya soka ya Yanga umetamka neno moja tu 'Mtatukoma' wakitambia kikosi chao katika ushiriki wao wa michuano ya Kombe la Kagame. Yanga watashiriki michuano hiyo itakayoanza Julai 14 na kumalizika mwishoni mwa mwezi huu kama mabingwa watetezi, michuano itakayofanyika kwenye ardhi ya Tanzania Bara. Afisa habari wa Yanga, Louis Sendeu alisema kwa namna kikosi chao kilivyoimarishwa na kujifua wana hakika ya kutetea taji hilo, na pia kufanya vema kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao. Sendeu, alisema kwa halili yoyote wapinzani wao watakaopambana kwenye michuano hiyo ya Kagame na Ligi Kuu wanapaswa kujipanga kwani vinginevyo watakiona cha moto. "Kwa kweli Watatukona kwa namna tunavyoendelea vema na maandalizi yetu ya michuano ya Kagame na kujipanga kwa Ligi Kuu msimu ujao kama unavyojua tumeshaanza kujifua na tumeimarisha kikosi kwa kunasa wachezaji kadhaa," alisema. Sendeu alisema, anaamini wachezaji wapya waliosajiliwa kwa ajili ya michuano hiyo na ligi ijayo wataisaidia Yanga kurejesha makali yake baada ya kumaliza msimu wakiambulia patupu wakipoteza ubingwa na kukosa hata nafasi ya kuiwakilisha nchini katika michuano ya kimataifa. Yanga ilimaliza ligi ikiwa nafasi ya tatu, ikiziacha Simba iliyotwaa ubingwa na Azam walioshika nafasi ya pili wakiwatambia na kupata fursa ya uwakilishi wa nchini katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho. Kikosi hicho cha Yanga kinaendelea kunolewa kwa sasa na Kocha Msaidizi ambaye ndiye Kaimu Kocha Mkuu, Fred Felix Minziro baada ya aliyekuwa kocha mkuu, Kostadin Papic kutimika kwao baada ya kutoongezewa mkataba mwingine na klabu hiyo. Tayari uongozi wa juu ya Yanga umesema wakati wowote utalitangaza jina la kocha mkuu wa timu hiyo baada ya kupitia maombi ya makocha bora watano waliopita katika orodha ndefu ingawa majina ya makocha hao haijawekwa bayana zaidi ya tetesi wapo wa ndani ya Afrika na Ulaya. Timu hiyo jana ilikitambulisha kikosi chake kwa mashabiki wa soka jijini Dar kwa kuumanana na Express ya Uganda na kuikandamiza mabao 2-1, mabao yote ya Yanga yakitupiwa nyavuni Jerry Tegete kwa pasi murua za kinda la Stars, Simon Msuvah na Bahanuzi.

Monday, June 25, 2012

Ngassa atamani kucheza Simba

ACHANA na Mrisho Ngassa. Mshambuliaji nyota wa timu ya Moro United iliyoshuka kwenye ligi kuu ya Bara, Benedict Ngassa, amesema anatamani kuichezea Simba. Kama hatopata nafasi ya kucheza Simba, mabingwa wa mwaka jana, Ngassa amesema anatamani kusajiliwa Yanga. Akizungumza na MICHARAZO, Ngassa, alisema kati ya ndoto anazoota kila siku ni ile ya kuja kuichezea ama Simba au Yanga, klabu anazozihusudu na anazoamini zitaweza kumfikisha mbali kisoka. Ngassa, alisema yeye hatakuwa mchezaji wa kwanza nchini kuziota timu hizo kubwa, ingawa alisema ni vigumu kupata fursa hiyo kirahisi kama hufanyi vitu vya kuzivutia. "Kwa kweli natamani kuichezea timu moja kati ya Simba au Yanga, ni klabu kubwa na zenye mafanikio makubwa nchini na zinazoweza kumfikisha mbali mchezaji kama ana malengo na kila kijana anatamani kuzichezea," alisema. Ngassa, alisema mpaka sasa wakati usajili ukiendelea bado hajasaini kokote licha ya kufuatwa na timu kadhaa. Ngassa ni mmoja wa nyota wa timu ya Moro iliyokuwa imerejea ligi kuu na kushuka msimu uliopita sambamba na Villa Squad na Polisi Dodoma. Nafasi za timu hizo tatu, mbili zikiwa za uraiani, zimechukuliwa na Mgambo Shooting, Polisi Moro na Mbeya Prisons.

Niombeeni kwa Mungu, naumwa-Omar Kapera 'Mwamba'

Kapera (wa tatu kushoto waliochuchumaa) akiwa na wachezaji wenzake wa Yanga
NYOTA wa zamani wa kimataifa wa klabu za Yanga, Pan Afrika na Taifa Stars, Omar Kapera 'Mwamba' ni mgonjwa na amewaomba mashabiki wa soka kumuombea kwa Mungu. Beki huyo aliyewahi kuwa Afisa Michezo na Utamaduni wilayani Kinondoni na Temeke kabla ya kuiongoza Pan Afrika kama Katibu Mkuu, alisema hali yake si njema baada ya kupatwa na maradhi ya kiharusi. MICHARAZO ilimtembelea mchezaji huyo nyumbani kwake Temeke na kukumkuta katika hali isiyoridhisha, ingawa mwenyewe (Kapera) na mkewe Rukia Rashid walisema ni tofauti na alivyokuwa siku za nyuma. Kapera alisema alianza kuugua ghafla Oktoba mwaka jana kabla ya kuzidiwa hasa alipoanza kupinda mdomo na kupoteza hisia upande wake wa kulia kutokana na kiharusi. "Namshukuru Mungu naendelea vema kulinganisha na siku za nyuma, lakini bado naumwa kama unavyoniona na ninaomba watanzania waniombee nipate nafuu," alisema. "Japo kuugua ni ibada bado nawaomba wenzangu msinisahau kwa maombi na dua zenu." Kapera ambaye alikuwa mmoja wa waasisi wa Pan Afrika mwaka 1976 baada ya mgogoro ulioikumba Yanga mwaka 1975, pia aliwataka mashabiki watakaopenda kumjulia hali wawasiliane nae nyumbani kwake au kumpa pole kupitia simu yake ya mkononi ya 0713 636255. 

Hassani Kumbi: Kiungo mkabaji anayetesa na miondoko ya Mduara

AWALI ndoto zake tangu akiwa shuleni ilikuwa kuja kuwa nyota wa soka akimudu nafasi ya kiungo mkabaji na nafasi nyingine za mbele akitamba na timu kadhaa ikiwemo Ajax Mzamba ya Temeke alioshiriki nao Ligi ya Taifa. Hata hivyo kitendo cha kupigwa bisibisi katika mechi ya 'mchangani' ya Ligi ya kuwania Ng'ombe, Kiwalani, lilisitisha ndoto za Hassani Kumbi ' H-Kumbi au 'H-Kilakitu' na kujikuta akihamia kwenye fani ya muziki. Kumbi, alisema baba yake alimpiga marufuku kucheza soka baada ya tukio hilo lilomfanya alazwe hospitalini na alipopona aliamua kuingia katika muziki kwa vile alishawahi kuimba kaswida alipokuwa madrasa. Msanii huyo anayetamba baada ya kuibuliwa na kituo cha Mkubwa na Wanae kinachoendeshwa na Said Fella, alisema alipigwa bisibisi hiyo mbavuni na mmoja wa mashabiki wa timu pinzani iliyocheza na timu yake ya Young Stars. "Baba alinizuia kucheza soka baada ya kitendo cha kujeruhiwa uwanjani ndipo nikahamishia makali yangu kwenye muziki baada ya kupita usaili wa Mkubwa na Wanae," alisema. Kumbi alisema baadhi ya nyota aliocheza nao shuleni na kwenye timu kadhaa ni Abuu Ubwa, Nizar Khalfan, Adam Kingwande, Ramadhani Chombo, Juma Jabu na Ally Mustafa 'Barthez'. Mkali huyo anayetamba kwa sasa na kibao cha 'Vocha' alichoimba na Dogo Aslay waliopo naye kituo cha Mkubwa na Wanae, alisema licha ya kuimba kaswida, pia aliwapenda mno Banzastone na Zahiri Ally Zorro. "Nilivutiwa na Banzastone na Zahir Ally ambao hata leo wanawafuatilia ndio maana nimeweza kuinuka haraka kisanii," alisema. Msanii huyo, anayetarajia kuachia kazi mpya iitwayo 'Sindano' akiwa na video yake huku akikamilisha pia kibao cha Deni alichoimba na AT, alisema muziki kwa sasa nchini unalipa na una mafanikio makubwa. Alisema zamani ilikuwa vigumu msanii wa muziki wa kizazi kipya kuandaa shoo ya kiingilio cha Sh 20,000 au 50,000 lakini sasa inawezekana akitolea mfano tukio la Diamond alipofanya onyesho lake la 'Diamond Are Forever'. Kumbi, anayetamani kuja kuwa mfanyabiashara mkubwa mara 'kijiwe' cha muziki kitakampomchanganyia, alisema licha ya muziki kulipa bado vipo vikwazo ikiwemo uharamia na unyonyaji unaofanywa dhidi ya kazi za wasanii. Alisema ni vema serikali ikawasaidia wasanii kwa kutunga sheria kali ili kuwatia adabu wezi wa kazi za wasanii, sambamba na kuvuna mapato yaliyopo katika fani hiyo, akidai fedha nyingi zinapotea mikononi mwa 'wahuni'. Msanii huyo anayependa kula wali kwa maharage au ugali kwa samaki wa kukangaa na mlenda pamoja na kunywa juisi ya Embe, alisema kama angekutana na Rais angemweleza jambo hilo sambamba na kumsihi aboreshe maisha ya watanzania hasa huduma za kijamii na kudhibiti mfumuko mkubwa wa bei za vyakula na bidhaa nyingine. Kumbi anayeishabikia Simba na Manchester United na kuwazimia wachezaji nyota wa timu hizo, Haruna Moshi 'Boban' na Javier Hernandez 'Chicharito', alisema kati ya matukio ya furaha kwake ni kukubalika kwa kazi yake ya kwanza ya 'Vocha' na pia kukutana kwa mara ya kwanza na kuzungumza na Zahir Ally Zorro anayemhusudu na kumsifia uwezo alionao. "Nilisisimka mno nilipokutana uso kwa uso na Zahir Ally na kujisikia faraja aliponieleza kwamba naweza, pia nilipoachia kazi yangu ya Vocha na kupokelewa vema na kwa huzuni ni msiba wa baba yangu Ally Kumbi na kuuguliwa na mama yangu hadi leo," alisema Kumbi. Mkali huyo aliyeoana na Aisha Soud na kuzaa nae mtoto mmoja aitwae Hawa (2), alisema matarajio yake ni kuhakikisha anafika mbali katika muziki, pia akiweka wazi kwamba yeye ni H Kila Kitu akimaanisha anaimba miondoko yote ya muziki ikiwemo taarab na dansi. Kumbi anayemshukuru Mungu na watu waliomsaidia katika muziki kama Said Fella, Yusuf Chambuso, Suleiman Daud 'Sulesh' na wasanii wenzake wa Mkubwa na Wanae, alisema kitu cha thamani anachokumbuka kununua kwa fedha zake za muziki ni kumuugizia mwanae. "Nakumbuka nilienda kufanya shoo Iringa na kupata fedha nyingi kwa mara ya kwanza katika maisha yangu bya muziki na niliporejaea Dar nilikuwa mwanangu Hawa mgonjwa hivyo nikatumia kumtibia pamoja na kumnunulia nguo za bei mbaya," alisema. Msanii mwenye ndoto za kuja kujitolea kuwasaidia wengine kama anavyofanya Mkubwa Fella, alitoa ushauri kwa watu matajiri kuwasaidia wasanii kuwaibua na kuwaendeleza badala ya kusubiri watu wengine wawaibue kisha kuwarubuni wasanii hao bila kujua walikotokea. "Wapo watu wenye fedha zao wamekuwa wakifanya hila kuwarubuni wasanii chipukizi baada ya kuona wameanza kutoka kwa kuinuliwa na watu kama THT, Mkubwa na Wanae au Tip Top Connection, hii sio haki kwanini wasitumie fedha zao kufanya kama wenzao?" Alihoji. Hassani Ally Kumbi, alizaliwa Juni 16, 1987 akiwa mtoto wa mwisho kati ya watoto wanne na kusoma Shule ya Msingi Mabatini -Tandika Dar es Salaam kabla ya kuendelea na masomo ya Sekondari alipohitimu kidato cha nne mwaka 2006 Shule ya Twaybat pia ya Temeke. Alienda kusomea ufundi umeme wa magari mjini Morogoro kabla ya kuzama kwenye soka aliloanza kucheza tangu akisoma shule ya msingi, timu yake ya chandimu ikiwa ni Santiago Chile maarufu kama G Stiva akimudu namba 6 na nyingine zote za mbele. Timu nyingine alizozichezea kabla ya kutua kwenye muziki ni Good Hope, TMK Kids, DYOC na Ajax Mzamba aliyoitoa daraja la tatu hadi Ligi ya Taifa ya TFF. Mwisho

Kingwendu ajipanga kuachana na soka, kisa...!

MSHAMBULIAJI nyota wa timu ya African Lyon aliyewahi kutamba na timu za Ashanti Utd na Simba, Adam Kingwande amesema anatarajiwa kupumzika kwa muda kucheza soka ili arejee darasani kusoma. Kingwande, aliiambia MICHARAZO kama mipango yake ya kwenda darasani itatimia hivi karibuni, basi huenda asionekane tena dimbani hadi atakapomaliza masomo yake baada yaa miaka mitatu. Mchezaji huyo aliyekuwa msaada mkubwa kwa Lyon kabla ya kuumia na kuwa nje ya dimba hadi aliporejea mwishoni mwa msimu uliopita, alisema ameona ni bora arejee darasani kusoma kisha ndipo aendelee kucheza soka. Kingwande alisema anatarajia kwenda kusomea Sheria katika Chuo kimoja kilichopo hapa nchini na hivyo itamuwia vigumu kwake kuchanganya mambo mawili kwa wakati mmoja. "Kaka huenda nisionekane tena dimbani kwa muda kidogo kwani natarajia kurudi darasani kusoma, si unajua soka la Bongo lilivyo kama mtu hujiwekei mipango mizuri unaweza kuumbuka mbeleni," alisema. Mkali huyo, aliyeibuliwa na kituo cha kukuza soka la vijana cha DYOC, alisema masomo yake yatachukua muda wa miaka mitatu na hivyo kipindi chote cha masomo hayo hataweza kucheza timu yoyote labda ya chuoni tu. Kingwande alisema mbali na chuo hicho, pia ameomba nafasi ya kusoma pia katika chuo kimoja kilichopo nje ya nchi hivyo anasikilizia kama akikubaliwa anaweza kuamua kujiunga na chuo kimojawapo kati ya hivyo. "Nimeomba pia katika chuo kimoja nje ya nchi, lakini ningependa kusoma hapa nchini, mradi tu nitimize ndoto zangu za kuwa mwanasheria," alisema. Mchezaji huyo anayemudu nafasi zote za mbele ikiwemo kiungo alisema anaamini kusoma kutamwezesha kulicheza soka lake kwa uhakika sambamba na kuwa na uhakika wa maisha baada ya kutundika daluga zake. Mwisho

Theresia Ojade, mshindi wa tuzo ya TASWA anaizimia Simba

MWENYEWE anakiri kuwa kiu aliyokuwa nayo tangu utotoni ya kutaka kuwa nyota wa michezo nchini, ndiyo iliyomfanya ajibidiishe, kujituma na kujifunza kwa wengine waliomtangulia na katika kipindi kifupi ameanza kuona matunda yake bila ya kutarajia. Moja ya matunda yanayomfanya mchezaji huyo mkali wa timu ya mpira wa wavu ya Jeshi Stars, Theresia Ojade kujivunia ni Tuzo ya Mchezaji Bora wa Kike wa Wavu aliyotwaa iliyotolewa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo nchini, TASWA. Theresia, alisema tuzo hiyo ambayo hakutarajia kuipata licha ya kuwa mmoja wa nyota watatu walioteuliwa kuiwania sambamba na mchezaji wenzake wa Jeshi Stars, Zuhura Hassani na Evelyne Albert wa Magereza, imempa faraja kubwa na kumtia nguvu ya kujibidiisha zaidi. Mkali huyo aliyeanza kung'ara katika michezo tangu akisoma Shule ya Msingi akicheza netiboli, wavu na kikapu, alisema hakutarajia kama ndoto zake za kung'ara katika michezo zingeanza kutimia mapema kiasi hicho. "Kwa kweli namshukuru Mungu kwa kuniwezesha kuanza kutimiza ndoto zangu za utotoni za kutamba katika michezo baada ya kutwaa tuzo ya TASWA," alisema. Aliongeza tuzo hiyo haimvimbishi kichwa badala yake imemuongezea morali wa kuongeza juhudi ili aje kutamba kimataifa ikiwezekana kucheza mpira wa wavu wa kulipwa kama nyota wa nchi jirani za Rwanda na Kenya. "Natamani nifike mbali katika mchezo huu, hasa kucheza wavu wa kulipwa sambamba na kuisaidia timu yangu ya Jeshi Stars itambe kimataifa," alisema. MAFANIKIO Theresia, aliyeingia kwenye wavu kwa kuvutiwa na umahiri wa dada yake, Maria Daniel na Fausta Paul aliyestaafu kwa sasa, alisema mbali na heshima ya tuzo hiyo na kitita cha Sh. Mil. Moja, pia anashukuru wavu kumsaidia mengi. Alisema, mchezo huo umemfanya hafahamike, kutembea sehemu mbalimbali na kumwezesha kumudu maisha yake na kuisaidia familia yake licha ya kupata mafunzo ya kijeshi kama askariu wa kujitolea wa JKT. "Japo mchezo huu haulipi sana nchini kutokana na kutopewa kipaumbele na kudodora kwake, ukweli umenisaidia kwa mengi kiasi najivunia kuucheza," alisema. Alidokeza kuzimika kwa mchezo huo nchini kumechangiwa na Chama chao cha TAVA kukosa ubunifu na kuandaa mashindano mara kwa mara kuuhamaisha mchezo huo na kuutaka uongozi wake kuzinduka usingizini. Theresia alisema, pia 'ubaguzi' unaofanywa na serikali na wadhamini kwa kutupia macho soka tu, ni tatizo linalodidimiza wavu na michezo mingine na kudai angekutana na Rais angemlilia atupie macho michezo yote ili kuwasaidia wenye vipaji kunufaika nayo. "Ningemuomba Rais aitupie na kuiwezesha michezo mingine ili tunayoicheza tunufaike nayo kama kwa wanasoka na kama ningekuwa Rais ningewekeza katika michezo sambamba na kuboresha huduma za kijamii hasa Afya na Elimu," alisema. FURAHA Nyota huyo anayependa kula ugali kwa samaki na kunywa juisi ya Embe, alisema hakuna kitu cha furaha kwake kama kutwaa tuzo hiyo ya TASWA na kuhuzunishwa na kifo cha mjomba wake kipenzi, Ojade aliyefariki mwaka jana. Theresia aliyejaliwa umbo la kike na sura ya kuvutia, alisema licha ya kucheza mechi nyingi, hawezi kuisahau pambano kati ya Jeshi Stars dhidi ya Prisons ya Kenya katika fainali za michuano ya ubingwa wa nchi za Afrika Mashariki. "Naikumbuka kwa namna wapinzani wetu walivyotuzidi maarifa na namna tulivyocheza na kuambulia kipigo cha aibu cha seti 3-0," alisema. Theresia ambaye hajaolewa wala kuzaa mtoto, akitamani atakapoolewa awe na watoto watatu, ni shabiki mkubwa wa Simba na Manchester United akimzimia mchezaji mwenzake wa Jeshi Stars, Yasinta Remmy. Mkali huyo anayechishwa na nguo za rangi nyeupe na nyeusi na kupenda kutumia muda wake wa mapumziko kusikiliza muziki na kufuatilia maambo ya urembo na mitindo, aliwashukuru familia yake hasa wazazi, dada yake Maria Daniel na marehemu mjomba wake Ojade. ALIPOTOKA Theresia Sylvanus Abwao Ojade, alizaliwa Januari 8, 1988 Shirati mkoani Mara akiwa ni mtoto wa kwanza kati ya wawili wa familia yao. Alisoma Shule ya Msingi Mbagala Kuu jijini Dar kabla ya kujiunga na masomo ya Sekondari katika Shule ya Mwanga na kukwamia kidato cha pili kutokana na matatizo ya kifamilia na kujikita katika michezo aliyoicheza tangu kinda. Klabu yake ya kwanza kujiunga kuichezea ni JKT Mgulani alipokuwa mmoja wa askari wa kujitolea wa Jeshi la Kujenga Taifa kwa mkataba wa miaka mitatu. Baada ya kung'ara na timu hiyo na kumalizika kwa mkataba wake alijiunga na Jeshi Stars mwaka juzi na kufanikiwa kutwaa nao mataji mbalimbali ukiwemo ubingwa wa Ligi ya Muungano wa mwaka huu. Theresia anayewazimia wasanii Lady Jaydee na Ally Kiba wanaotamba katika muziki nchini, alisema atakuwa mchoyo wa fadhila kama hatawashukuru wachezaji wenzake na makocha waliomnoa na kumfikisha hapo alipo. Mwanadada huyo alikiri kwamba amekuwa akipata usumbufu mkubwa kwa wanaume wakware, lakini kwa kujithamini na kutambua kuwa Ukimwi upo na unaua huepuka vishawishi jambo alilotaka wachezaji wenzake na jamii kwa ujumla nao kuwa makini kwa kuepuka tamaa. Pia aliwasihi wachezaji wenzake kupendana, kushirikiana na kujibidiisha na kujituma katika mazoezi na michuano mbalimbali ili wafike mbali. Mwisho

Tuesday, June 19, 2012

Waislam wadai hawahitaji upendeleo serikali, ila...!

AMIRI wa Vijana wa Dini ya Kiislam Tanzania, Sheikh Shaaban Mapeyo, amesema malalamiko wanayotoa waumini wa dini hiyo dhidi ya serikali haina maana ya waislam kutaka upendeleo bali kutaka haki na uadilifu utendwe kwa raia wote nchini. Aidha alisisitiza kuwa msimamo wa viongozi wa dini hiyo juu ya Sensa ya mwaka huu ni ule ule wa kuigomea mpaka kipengele cha dini kilichoondolewa kirejeshwe ili kuondoa utata uliopo na kusaidia kujua idadi ya wanadini nchini. Akiwahutubia waumini wa msikiti wa Mwenge, jijini Dar es Salaam, Sheikh Mapeyo ambye pi ni Imamu Mkuu wa msikiti huo, alisema waislam hawahitaji upendeleo wa aina yoyote, isipokuwa wanapenda kuona haki na uadilifu unatendwa kwa raia wote. Sheikh Mapeyo alisema madai wanayoyatoa kila mara dhidi ya dhuluma na hujuma wanaofanyiwa ni kama njia ya kuikumbusha serikali ifanye shughuli zake kwa uadilifu ikiwatendea haki raia wake wote badala ya kupendelea kundi fulani na kuwapuuza wengine. "Waislam tunapolalamika na kupiga kelele kila mara hatuna maana ya kutaka upendeleo, tunachotaka ni kuona serikali inaendesha shughuli zake za usawa, haki na uadilifu kwa vile taifa hili ni la watanzania wote," alisema. Aliongeza, waislam wamekuwa wavumilivu kwa muda mrefu nchini licha ya kutambua kuna baadhi ya mambo hawatendewi haki, lakini kwa kupuuzwa kwao imewafanya wafikie kikomo na kuitahadharisha serikali iwe makini. "Kwa mfano kwa muda mrefu tumekuwa tukilalamika hujuma tunayofanyiwa katika elimu, ila majuzi imebainika hatulii ovyo baada ya kubainika madudu ya matokeo ya Baraza la Taifa la Mitihani, ambapo wenyewe wamekiri makosa." Alisema ni vema serikali ikazinduka na kuliona tatizo lililopo nchini ni kubwa kuliko wanavyofikiria, huku akisisitiza kuwa bila kuyrejeshwa kwa kipengele cha dini kwenye zoezi la Sensa waislam hawatashiriki. "Huu ni msimamo wetu na tumeanza kuwahimiza waumini wetu kuwa kama kipengele hicho hakirejeshwi basi wasishiriki Sensa na tumeshaiandikia barua serikali juu ya msimamo huo," alisema Sheikh Mapeyo. Alisema serikali iliwaita viongozi wa kidini mjini Dodoma kuzungumzia jambo hilo na kusisitiza hawaterejesha kipengele hicho na wao kuieleza wazi kwamba kama ni hivyo basi wapo radhi wahesabiwe watu wengine na sio waislam. Mwisho

Mcheza filamu wa Marekani kukimbia Mount Kilimanjaro

MCHEZA sinema maarufu duniani kutoka nchini Marekani Deidre Lorenz, anatarajiwa kushiriki mbio za kila mwaka za Mount Kilimanjaro Marathon zitakazofanyika Jumapili ijayo mjini Moshi. Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na waratibu wa mbio hizo zilizoanzishwa na Marie France wa mji wa Bethesda, Maryland nchini Marekani mwaka 1991 na zitakazojulikana kama 7 Continental Races, muigizaji huyo wa filamu naye atakimbia katika mbio hizo. Taarifa hiyo iliyotumwa MICHARAZO na Afisa Habari Uhusiano wa mbio hizo, Grace Soka ni kwamba mcheza sinema huyu aliyecheza sinema kama Santorini Blue, Perfect Strangers, The Great Fight, ujio wake utaitangaza Tanzania katika macho ya dunia na kuwavutia watalii. Lorenz aliyewahi kuteuliwa mara tatu kuwania tuzo za Grammy, ataambana na wamarekani wengine na anatarajiwa kutua nchini Juni 21. Mbio hizo za Mount Kilimanajaro zitawashirikisha wakimbiaji wengine wa kimataifa pamoja na wa nyumbani na zitakuwa za umbali wa Kilomita 42 na washindi wake wakiwemo watoto watazawadiwa zawadi mbalimbali. Pia mbizo zitahusisha mbio za umabli wa kilometa 21, kilometa 10 na kilometa 5 kwa watoto na kwamba washiriki wake hawahitaji ujuzi wa kukimbia bali mradi mtu anayeweza kufanya hivyo. Deidre Lorenz alizaliwa katika jiji la Oregon nchini Marekani lakini alihamia katika jiji la New York City linalijulikana kama "The Big Apple" nchini Marekani akiwa na kampuni yake ya kutengeneza sinema inayoitwa Thira Films LLS. Lorenz alipatikana kushiriki mbio hizo katika bahati nasibu iliyochezwa wakati wa mbio za New York Marathon za mwaka jana.

Coastal Union yanasa vifaa vipya yumo Atupele

KLABU ya soka ya Coastal Union ya Tanga, imetangaza kuwanyakua wachezaji kadhaa wapya akiwemo kipa wa zamani wa Yanga na Azam, Jackson Chove. Afisa Habari wa Coastal, Eddo Kumwembe, aliiambia MICHARAZO, Chove ni miongoni mwa makipa wawili wapya iliyowasajili kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara. Kumwembe alimtaja kipa mwingine iliyomnyakua ni Juma Mpongo aliyekuwa akiidakia Kiyovu Sports ya Rwanda. Afisa Habari huyo aliwataja wachezaji wengine iliyowanasa mpaka sasa kuwa ni mshambuliaji Nsa Job toka Villa Squad, mlinzi wa kushoto wa JKT Oljoro, Othman Omary, Atupele Green aliyekuwa Yanga na nyota wa timu ya taifa ya U20. Kumwembe aliwatraja wachezaji wengine kuwa ni Soud Mohamed kutoka Toto Afrika, Seleman Kassim 'Selembi' na Raraq Khalfan waliokuwa African Lyon. "Hao ni baadhi ya wachezaji tuliowanyakua na tunaendelea na usajili wetu kwa ajili ya kuziba nafasi za wachezaji tisa tuliowatema katika kikosi cha msimu uliopita," alisema Kumwembe. Aliongeza kuwa, mbali na wachezaji hao pia timu yao imeshamalizana na kocha wao wa zamani Rashid Shedu kutoka Kenya ambaye amechukua nafasi ya Jamhuri Kihwelu 'Julio' waliyeachana nae mara baada ya kuiwesha Coastal kumaliza ligi ikiwa nafasi ya tano. "Pia tumeimarisha benchi letu la ufundi kwa kumnyakua Rashid Shedu kuziba nafasi ya Julio tuliyeachana nae," alisema. Kumwembe alisema pia kwa sasa wanafanya mazungumzo na kiungo wa zamani wa Simba, Jerry Santo ili zweze kuichezea timu yao kwa msimu ujao. Mwisho

Friday, June 8, 2012

Zuri Chuchu: Muimbaji wa zamani Double M anayeishi na VVU

HUENDA mashabiki wa muziki wa dansi na ule wa kizazi kipya, bado wanalikumbuka jina Zuri Chuchu, mmoja wa waimbaji mahiri wa kike waliowahi kutamba nchini na bendi mbalimbali pamoja na kazi zake binafsi. Moja ya kazi binafsi zilizomtambulisha muimbaji huyo wa zamani wa Bambino Sound na Double M Sound ni kibao kilichokimbiza kwenye vituo vya runinga kiitwacho 'Channel ya Mapenzi' alichokitoa mwaka 2005 kuelekea 2006 kikiwa katika miondoko ya zouk. Ila wakati mashabiki walipokuwa wakisubiri vitu zaidi kutoka kwake, ghafla alitoweka kitambo kirefu na kuja kuibuka akijitangaza kwamba ni muathirika wa ugonjwa wa Ukimwi. Wapo baadhi ya wanamuziki wenzake, mashabiki wa muziki na hata ndugu, jamaa na rafiki zake walishindwa kumuamini wakidhani labda 'amedata' au alikuwa akitafuta mbinu za kurejea upya kwenye game kwa njia hiyo. Hata hivyo, mwenyewe alikuwa akisisitiza hajitangazi kutafuta sifa au 'promo' bali ni kweli yeye anaishi na VVU kabla ya kuanza kuendesha kampeni za kuelimisha watu wengi kujikinga na maambukizo ya VVU na Ukimwi. Baada ya kuendelea na msimamo wake, jamii ilikubali ukweli hasa alipomuona akiendesha kampeni zake shuleni na ndani ya jamii bila ya hofu yoyote, huku mwenyewe akitoa ushuhuda jinsi anavyoendelea kutumia vidonge vya ARV. Msanii huyo anayejishughulisha kwa sasa na muziki wa Injili akijiandaa kutoa albamu yake ya kwanza iitwayo 'Napenda Kuishi' yenye nyimbo 12, alisema hata yeye awali alipopewa taarifa kuwa ameathirika hakuamini kirahisi. "Hata mimi jambo hili awali lilinitesa kabla ya kukubali ukweli na kujitangaza hadharani nikibeba jukumu la kuwaelimisha wengine juu ya ugonjwa huo." Zuri Chuchu ambaye majina yake kamili ni Esther Charles Mugabo, alisema kumtumainia Mungu na ushauri aliopewa na wataalamu wa afya umemfanya leo ajione mtu wa kawaida akiendelea na shughuli zake kuelimisha wengine. ALIPOTOKEA Zuri Chuchu alizaliwa Septemba 8, 1974 mkoani Mara akiwa mtoto wa tano kati ya saba wa familia yao na alisoma Shule ya Msingi Nyamboto na kuishia kidato cha pili kwa masomo katika Shule ya Sekondari Tarime. Alisema tatizo la kifedha la kifamilia ndilo yaliyomkwaza na kukimbilia kusaka maisha katika machimbo ya Dhahabu ya Nyamongo kabla ya mwaka 1994 kwenda Kenya kufanya shughuli zake binafsi na kutamani kuingia kwenye muziki. Zuri alisema ingawa kipaji cha sanaa hasa uimbaji alizaliwa nacho na kuimba shuleni na kanisani, kupenda uimbaji wa Ally Choki aliyekutana nae Kenya akiwa bendi ya Extra Kimwa, ndiko kulikomfanya atamani nae kuingia katika fani hiyo. Ndipo alipoanza kujifunza taratibu fani hiyo na aliporejea nchini mwaka 2000 alienda kunolewa na Nyoshi El Saadat kabla ya baadae kutua Bambino Sound. Baadae alitoka Bambino kwenda Stono Musica alioenda nao umangani mwaka 2004 na aliporejea alitua Tango Stars na kusafiri na Patcheko kwenda Oman chini ya kundi la Kampiosa Sonare. Alirejea nchini na kujiunga Double M Sound akiwa miongoni mwa walioshiriki kupika albamu ya 'Titanic' kabla ya kujiunga African Beats na kusafiri nao 2006 kwenda Arabuni ambapo alirejeshwa nchini kwa madai hati yake ina tatizo. "Sikujua chochote niliporudishwa, ila nikiwa nchini nilitumiwa ujumbe wa simu na mwanamuziki mwenzangu mmoja aliyenieleza kwamba nijiandae kufa kwani nimerudishwa kwa vile nilikuwa muathirika, nilistuka mno," alisema. Katika wiki kadhaa za mateso ya moyo akijifungia ndani, Zuri alisema alijiwa na nguvu za kiroho na kwenda kupima Muhimbili alikothibitishwa kuwa ni kweli alikuwa na VVU, jambo lililozidi kumchanganya na akakata tamaa. "Nilikuwa najifungia ndani tu nikiwakimbia watu kwa jinsi nilivyoshtushwa na hali hiyo, ila nikajiuliza rohoni nitaendelea kujifungia ndani hadi lini, ndipo nikajitokeza hadharani, ingawa nilipokewa tofauti," alisema. Zuri alikiri alipokuwa kwenye muziki wa kidunia alijirusha na kujiachia kwa raha zake, pia akiwahi kuishi na wanaume watatu bila ya ndoa, lakini hana hakika alivipatia wapi virusi hivyo na hataki kumnyooshea mtu kidole. "Siwezi kumlaumu mtu kwani sikuishi kwa utulivu enzi za nyuma, ila najua kila limpatalo mtu ni mipango ya Mungu, nimejikubali na nasonga mbele kuwasaidia wengine waweze kubadili maisha yao," alisema. MLOKOLE Zuri ambaye sasa ameolewa na Dennis Ignas Mhala ambaye naye ni muathirika, alisema kabla ya kujigundua ni muathirika na kuingia kwenye muziki wa injili, alishaokoka kitambo. Alisema aliokoka mwaka 2005 kutokana na kusumbuliwa na mizimu ya upande wa mama yao iliyomtaka awe Mganga wa Kienyeji. "Nilikuwa nalazimishwa kuwa mganga, sikutaka, nikasumbuliwa sana. Ndipo nilipopata uponyaji na kuokoka hata kabla ya kugundulika kwa tatizo langu," alisema. Alisema anashukuru tangu alipokabidhi maisha yake kwa Mungu na kujitolea kuendesha kampeni dhidi ya Ukimwi amefarijika akiishi kwa amani na utulivu kuliko ilivyokuwa zamani. Zuri anashukuru muziki kumsaidia kwa mengi ikiwemo kujenga nyumba kwao Mara, kuanzisha miradi yake ya biashara ya vyakula akitengeza na kuuza maandazi, kazi anayoifanya kwa sasa. "Sio siri muziki wa kidunia ulinisaidia mengi tofauti na muziki wa Injili kwa vile muziki ninaoufanya sasa siufanyi kibiashara zaidi ya kujitolea kueneza neno la Mungu ila nashukuru sapoti ninayopata kwa watu mbalimbali." Zuri anayependa kula ugali kwa mbogamboga na matunda na kunywa maji na juisi, alisema hakuna tukio la furaha kwake kama kuvishinda VVU kwa kujikubali, amesema mambo yanayomsikitisha ni kusikia waathirika wenzake wanasambaza virusi kwa makusudi. Pia alisema tabia ya unyanyapaa ni tatizo kubwa linalofanya jamii kushindwa kuwa wazi katika ugonjwa huo na kufanya walioathirika kujificha na kuendelea kuwaumiza wengine. HARAKATI Msanii huyo anayewashukuru wakuu wa shule kwa namna wanavyomuunga mkono katika harakati zake, alikiri amekuwa na wakati mgumu kuendesha kampeni zake kwa kutokuwa na fedha na kutopigwa tafu na serikali. "Nilidhani kwa nilivyokuwa muwazi na kipaji cha sanaa nilichokuwa nacho ningetumiwa na serikali kuendesha kampeni za kutokomeza Ukimwi kwa ufanisi zaidi, lakini ukweli sina sapoti yoyote najitolea mwenyewe tu," alisema. Alisema anachoshukuru ni kwamba juhudi zake zimesaidia kuwaokoa wengi na wale walioathirika kujikubali akishirikiana nao kuendesha maisha yao kupitia mashamba ya kilimo cha mboga waliyoyaanzisha ili kujikimu. Alidai mashamba hayo yapo Gongolamboto na Kisarawe, ambayo yamekuwa wakiwawezesha waathirika kumudu maisha bila ya kuwa ombaomba. Zuri aliitaka jamii ibadilike na kukubali kuwa Ukimwi ni tatizo linalohitaji vita ya kila mmoja anakawataka wanandoa kuheshimu ndoa zao na wale wasio na ndoa kuwa waaminifu. "Wengi wameumizwa na Ukimwi, hivyo jukumu letu kila mmoja kuchukua jukumu la kuwa makini nao ili kuepusha au kupunguza maambukizo mapya, kubwa watu wawe waaminifu katika ndoa zao, tusirukeruke ovyo," alisema. Alisema yeyote anayetaka kumuunga mkono katika harakati zake awasiliane nae kwa 0656-756356 au kumtupia mchango wa kuendesha shughuli zake katika akaunti ya Benki ya Posta 01000294431 kwa jina la Esther A. Mugabo.

Thursday, June 7, 2012

Mchumiatumbo atamba hana mpinzani Bongo

BONDIA wa ngumi za kulipwa wa uzito wa juu, Alphonce Joseph 'Mchumiatumbo' ametamba kuwa, haoni bondia wa kupigana nae nchini kutokana na karibu mabondia wote wa uzito wake kuwachapa na wengine kuingia mitini kukacha kupigana nae. Aidha, amewaomba mapromota na wafadhili wa ngumi nchini kumsaidia kumtafutia mapambano ya kimataifa na mabondia wa nje ili awe kutimiza ndoto za kutwaa na kulitangaza jina lake katika anga hizo. Akizungumza na MICHARAZO kwenye mahojiano maalum, Mchumiatumbo alisema kutokana na kuwapiga karibu mabondia wote wa uzani wake na wengine kumkacha ulingoni anahisi hana bondia wa kupigana nchini hivyo kuwataka mabondia wa nje. Bondia huyo aliyepigana mapambano sita na kushinda matano, manne kati ya haayo kwa KO na kupata sare moja dhidi ya Ashraf Suleiman, alisema bondia aliyekuwa akidhani angeweza kumpa upinzani Amur Zungu alishaawahi kumkacha ulingoni. "Kwa kweli kama kila bondia ninayepigana nae naamshinda na wengine kunikacha ulingoni, sidhani kama kuna wa kupigana nami kwa sasa, hivyo nilikuwa naomba nitafutiwe michezo ya kimataifa kujitangaza zaidi na kuwania mikanda," alisema. Bingwa huyo wa zamani wa Mkoa wa Dar es Salaam wa ngumi za ridhaa, alisema mabondia wengi wa Tanzania wanaishia kutamba nchini tu kwa vile mapromota na waandaaji wa michezo ya ngumi hawawatafutii michezo ya kimataifa kama nchi nyingine. Mara ya mwisho Mchumiatumbo kupata ushindi ni wiki mbili zilizopita alipomtwanga kwa KO Bahati Mwafyale katika pambano lililofanyika kwenye ukumbi wa DDC Keko.

Madega awaonya Yanga kuhusu uchaguzi

WANACHAMA wa klabu ya soka ya Yanga wameonywa na kutakiwa kuwa makini katika uchaguzi wao mdogo utakaofanyika Julai 15, kwa kuhakikisha wanachagua viongozi wenye uchungu na nia ya dhati ya kuipeleka mbele klabu hiyo. Wito huo ulitolewa hivi karibuni na aliyekuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo, Imani Madega ambapo alisema uchaguzi huo unapaswa kutumiwa vema na wanachama wa Yanga kuhakikisha wanachagua viongozi wenye sifa na wataoikwamua klabu yao. Madega, alisema pupa yoyote watakayofanya wanachama hao kwa kuchagua viongozi wasiokuwa makini maana yake ni kuiweka pabaya Yanga na huenda watu wakaanza kunyoosheana vidole kama ilivyotokea katika uongozi uliopita. Mwenyekiti huyo wa zamani aliyeondoka madarakani kwa heshima kubwa ikiwemo kuiachia klabu hiyo akaunti iliyokuwa na fedha za kutosha, alisema ingawa katika kipindi kama hiki wanachama hunufaika, lakini waikumbuke klabu yao. "Ni vema wanayanga wakawa makini katika uchaguzi huu kwa kuhakikisha wanachangua watu wa mpira, wenye upeo na uwezo wa kuiongoza Yanga ili itoke mahali ilipo na kuweza kuwa klabu yenye hadhi kimtaifa," alisema. Kauli ya Madega imekuja wakati mchakato wa uchaguzi huo wa kuziba nafasi zilizoachwa wazi na waliokuwa viongozi wa Yanga, ambapo wagombea 28 kati ya 33 walirudisha fomu za kuwania uongozi katika kinyang'anyiro hicho. Kwa mujibu wa Katibu wa Kamati ya Uchaguzi wa Yanga, Francis Kaswahili waliojitokeza kuwania nafasi ya Uenyekiti ni wagombea wanne ambao ni pamoja na Sarah Ramadhan, Edger Chibura na John Jambele. Katika nafasi ya Makamu Mwenyekiti pia ina wagombea wanne ambao ni meneja wa zamani wa klabu hiyo, Ayoub Nyenzi, Ali Mayay, Yono Kevela na Clement Sanga huku kwenye Ujumbe wa Kamati ya Utendaji ina wagombea 20. Wagombea hao ni nyota wa zamani wa timu hiyo akiwemo aliyekuwa nahodha Shaaban Katwila, Aaron Nyanda, Edger Fongo na Ramadhan Kampira. Wengine wanaowania nafasi nne za ujumbe huo wa kamati ya utendaji ni Lameck Nyambaya, Mohammed Mbaraka, Ramadhani Saidi, Beda Tindwa, Ahmed Gao, Mussa Katabalo, George Manyama, Omary Ndula na Jumanne Mwamwenya. Wagombea wengine ni Abdallah 'Binkleb' Mbaraka, Peter Haule, Justine Baruti, Abdallah Sheria, Jamal Kisongo, Gaudecius Ishengoma na Yona Kevela.

Bingwa wa karate aililia serikali

BINGWA wa mchezo wa Karate kwa nchi za Afrika Mashariki ngazi ya klabu, Sensei Mikidadi Kilindo, ameiomba serikali iutupie macho mchezo huo na kuupa sapoti kama ilivyo kwa michezo mingine ili kuuhamasisha nchini. Aidha, Kilindo amedai kuwa kutopewa kipaumbele kwa mchezo huo ndio kilichomfanya mara zote awe anaenda na kurudi na medali bila hata kutangazwa au kufahamika kwa wananchi kitu kinachomsikitisha. Akizungumza na MICHARAZO , Sensei Kilindo alisema licha ya mchezo huo kuwa na manufaa makubwa kwa taifa na jamii kwa ujumla umekuwa haupewi kipaumbele kama michezo mingine. Alisema kutokana na hali hiyo ni vema serikali na wadau wa michezo kuutupia macho na kuusaidia ili utangazike na kutumiwa kuiletea sifa Tanzania baada ya michezo mingine kushindwa kufanya hivyo. Bingwa huyo wa miaka minne mfululizo wa Afrika Mashariki tangu 2008 alisema, kutopewa kipaumbele kwa karate ndiko kunakofanya hata wachezaji wanaoenda kuitangaza nchi wasifahamike warudipo na ushindi. "Mimi nimerudi hivi karibuni na medali ya dhahabu baada ya kuwa mshindi wa kwanza Afrika Mashariki, hii ni mara ya nne mfululizo, ila hakuna anayejua wala kiongozi aliyewahi kunipokea na kunipongeza inauma sana," alisema. Pia Kilindo alisema ukimya unaofanywa na viongozi wa Chama cha Karate nchini, TASHOKA katika kuutangaza mchezo huo ni tatizo linalofanya usisikike licha ya mafanikio yake kwa ngazi ya klabu. Alisema ni vema TASHOKA ikafanya utaratibu wa kuandaa michuano ya taifa angalau mara mbili kwa mwaka itakayoshirikisha klabu mbalimbali nchini kwa lengo la kuuhamasisha na kuutangaza mchezo huo.

Zuri Chuchu Anapenda Kuishi bwana!

MUIMBAJI wa zamani wa bendi za Bambino Sound na Double M Sound, Zuri Chuchu ambaye kwa sasa anaimba muziki wa Injili, yupo mbioni kuingiza sokoni albamu yake ya kwanza iitwayo 'Napenda Kuishi', huku akianza kuipika nyingine mpya. Zuri, ambaye majina yake kamili ni Esther Charles Mugabo, alisema albamu hiyo yenye nyimbo 12 ilishakamilika mujda mrefu kiasi baadhi ya nyimbo zake kuchezwa redioni, ila aliichelewa kuingiza sokoni kwa sababu zilizo nje ya uwezo wake. Alisema hata hivyo anashukuru kwa sasa mipango yake ya kuitoa hadharani albamu hiyo inaelekea vema na wakati wowote ataingiza sokoni. Zuri, ambaye alitangaza kuishi na VVU akiendesha kampeni mbalimbali kwa sasa kutoa elimu dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi, alisema wakati albamu hiyo ya kwanza ikiandaliwa kutoka, tayari ameanza maandalizi ya albamu yake nyingine ya pili. Alisema mpaka sasa amesharekodi nyimbo sita katika studio za Katra Production iliyompa ofa ya kufyatua albamu hiyo bure kama kuunga mkono juhudi zake za kuendesha neno la Mungu na kutoa elimu ya Ukimwi kwa jamii. "Nashukuru kwa nafasi niliyopewa na Katra Studio kutoa albamu yangu ya pili ambapo mpaka sasa nimesharekodi nyimbo sita, wakati nikitaka kuingiza sokoni kwanza albamu yangu ya kwanza iitwayo Napenda Kuishi yenye nyimnbo 12," alisema. Muimbaji huyo, alisema ameamua kutumia muziki kuhubiri na kutoa elimu ya Ukimwi kutokana na ukweli wanaoathirika na ugonjwa huo ni wengi, licha ya kwamba mambo hayawekwi hadharani hivyo anataka maambukizi mapya yasiendelee kuwepo kwa jamii.

Yanga, Simba 'jino kwa jino' kisa Kelvin Yondani

KLABU za soka za Simba na Yanga zimeingia katika vita mpya kufuatia beki wa kati wa kimataifa nchini, Kelvin Yondani kudaiwa kusaini kwa mpigo ndani ya klabu hizo kwa ajili ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao. Wakati Simba ikiendelea kushikilia msimamo kwamba Yondani ni mali yao baada ya kusaini mkataba mpya, Yanga wenyewe wamesisitiza kuwa beki huyo wameshamilazana nao na kuinyoa Simba iache kutupia vitisho katika suala la mchezaji huyo. Afisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu amesema wameshamalizana na Yondani kwa kumsainisha mkataba wa miaka miwili na kwamba kinachofanywa na watani zao kutaka kuwayumbisha mashabiki na kusisitiza watakula nao sahani moja hadi kieleweke ili kubaini nani mkweli katika hilo. Hata hivyo Mwenyekiti wa Simba Ismail Rage, amesema Yanga inajidanganywa kwa Yondani na huenda ikala kwao kwa hasara waliyoingia juu ya beki huyo wa kimataifa ambaye pia anaichezea timu ya taifa, Taifa Stars.