STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, June 2, 2012

Bondia Magoma Shaaban afariki, azikwa kwao Tanga

ALIYEKUWA Bingwa wa Dunia wa WBU uzani wa Super Fly, Magoma Shaaban amefariki dunia na kuzikwa kwao mkoani Tanga. Kwa mujibu wa mdau mkubwa wa mchezo wa ngumi ambaye pia ni promota, Ibrahim Kamwe, Magoma alikumbwa na umauti juzi kwenye hospitali ya Bombo mkoani Tanga. Magoma alikuwa amelazwa katika hospitali hiyo siku nne zilizopita kutokana na kuzidiwa na maradhi aliyokuwa nayo siku nyingi na kufariki majira ya jioni na alizikwa jana nyumbani kwao Mabovu Mwembesamaki, mjini Tanga. Marehemu aliyeacha mjane na watoto wawili Sudi,10 na Almasi,7 alizaliwa Oktoba 21, 1980 mjini Tanga na alianza kucheza ngumi tangu akiwa kinda akipitia klabu mbalimbali za ngumi za ridhaa kabla ya kuingia za kulipwa mwaka 1996 alipopanda ulingoni kuzipiga na Athumani Omari na kushinda kwa pointi. Hadi mauti yanamkuta bondia huyo aliyekuwa mfupi lakini machachari, alikuwa amepigana mapambano 16 na kushinda 13 kati ya hayo mapambano manne akishinda kwa KnockOut (KO) na kupigwa matatu pia kwa KO. Mara ya mwisho kupanda ulingoni ilikuwa Julai 21 mwaka 2006 na Eugen Sorin Tanasie mjini Timisoara, Romania katika pambano ambalo alipigwa kwa Technical Knockout (TKO) raundi ya pili. Taji lake la kwanza kutwaa lilikuwa ni la IBF Afrika, Septemba 12, mwaka 1998 akimpiga Mkenya Joseph Waweru kwa KO raundi ya kwanza, Uwanja wa Mkwakwani, Tanga. Mei 11, mwaka 2000 alimpiga bondia ‘matata sana’ Totin Lukunim wa Thailand na kutwaa taji la IBF Intercontinental, uzito wa Super Fly kwenye ukumbi wa PTA, Temeke, Dar es Salaam. Agosti 3, mwaka 2001 ndipo alitwaa ubingwa wa dunia wa WBU baada ya kumpiga Ferid Ben Jeddou wa Tunisia kwa TKO raundi ya sita mjini Avezzano, Abruzzo, Italia, kabla ya kupoteza taji hilo kwa kupigwa na Gabula Vabaza Julai 26, mwaka 2002 katika ukumbi wa Hemingways Casino, East London, Eastern Cape, Afrika Kusini kwa KO raundi ya kwanza. Mei 25, mwaka 2003 alipigwa na Mtanzania mwenzake, Mbwana Matumla kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam kwa TKO raundi ya nne. Wadau mbalimbali wa ngumi wameelezwa kusikitishwa na kifo cha Magoma, wakiitaka familia, ndugu, jamaa na rafiki zake kuwa na subira katika kipindi hiki kigumu wakiwakumbusha kuwa kazi ya Mola huwa haina makosa.

Friday, June 1, 2012

Costa, Jabu, Kago watupiwa virago Simba, wanne wajaza nafasi zao

NYOTA watano wa kikosi cha Simba ambao kwa kiasi kikubwa waliisaidia timu hiyo kung'ara msimu huu wamedaiwa kutupiwa virago, huku nafasi zao zikichukuliwa na wakali wanne waliosajiliwa mpaka sasa ndani ya kikosi hicho. Habari za kuaminika ambazo zimenaswa jijini ni kwamba wachezaji walitupiwa virago ni nyota wa kimataifa toka Jamhuri wa Kati, Gervais Kago, mabeki wa kati Victor Costa na Juma Nyosso, Juma Jabu na Ulimboka Mwakingwe aliyekuwa majeruhi kwa muda mrefu. Aidha kuna taarifa nyingine kwamba naye Uhuru Seleman yupo katika mchakato pia wa kutemwa katika kikosi hicho iwapo atafanikiwa kupata timu, ikidaiwa ananyemelewa na Yanga. Kwa mujibu wa chanzo cha habari toka ndani ya Simba, ni kwamba Costa, Jabu na Kago wametemwa kwa kushuka viwango, huku Nyosso anaysakwa na Yanga pia, ametemwa kutokana na utovu wa nidhamu wa mara kwa mara anaoufanya dimbani na kuigharimu timu, huku Mwakingwe kwa umri na kuwa majeruhi wa muda mrefu. Nafasi za wachezaji hao mpaka sasa zimechukuliwa na wakali wanne walionaswa Msimbazi ambao ni Juma Abdallah, Mussa Mudde Mbongo aliyekuwa akicheza SOFAPAKA, Patrick Nkanu toka Congo na Ibrahim Rajab 'Jebba'. Viongozi wa Simba walinukuliwa jana kwamba, zoezi zima la usajili wa timu yao utaanikwa baada ya kamati zao za ufundi na mashindano kuendesha zoezi hilo kwa maelekezo ya kocha wao, Cirkovic Milovan. Zoezi la usajili nchini kwa timu za Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2012-2013 umefunguliwa rasmi leo Juni Mosi na unatarajiwa kumalizika mwanzoni mwa Julai kabla ya Ligi kuanza Agosti ambapo miongoni mwa timu zitakazoshiriki ni Polisi Moro, Mgambo Shooting ya Tanga na Prisons ya Mbeya zilizopanda daraja toka la Kwanza.

Wema Sepetu afafanua pete aliyovishwa Maisha Club

MSANII nyota wa filamu nchini, Wema Sepetu amefafanua uvumi ulioenea jijini Dar kwamba ameangukia kwenye penzi na mwanamuziki wa bendi ya Machozi, Mwinyi kiasi cha kuvishwa pete ya uchumba kama alivyofanyiwa na aliyekuwa boifrend wake, Naseeb Abdul 'Diamond' kabla ya kumwagana hivi karibuni. Wema alisema pete aliyovishwa mwishoni mwa mwezi uliopita ilikuwa ni igizo la filamu aliyokuwa akiishoot iitwayo 'Super Star' kazi binafsi anayokuja nayo ambayo sehemu kubwa inahusu maisha yake halisi. Mrembo huyo alisema wengi walishindwa kuelewa walipomuona akivishwa pete na Mwinyi na kukumbatiwa huku wakipigana mabusu kwa kuwa kamera zilizokuwa zikitumika kutengenezea filamu hiyo zilikuwa juu na hivyo hazikuonwa na watu. "Sio kweli kama nimechumbiwa na Mwinyi wa Machozi, ila tulikuwa tukiigiza filamu yangu ya kwanza binafsi iitwayo 'SUPER STAR' ambayo ni kama inazungumzia maisha yangu," alisema. Mwinyi amecheza kama Diamond katika filamu hiyo ambapo aliwahi kumvisha pete na kutamka maneno ya kusisimua kabla ya kuja kugeukana. Wema alisema filamu hiyo anatarajia kuizindua Juni 23 baada ya kukamilika na imemgharimu karibu Sh Milioni 30 mpaka sasa. Miss Tanzania huyo wa 2006 amesema filamu hiyo imewashirikisha wasanii kadhaa nyota, na anatarajia itakuwa filamu ya kusisimua kutokana na kuigiza sehemu kubwa katika uhalisi wa maisha yake kama WEMA SEPETU.

YANGA MPO? RATIBA YA UCHAGUZI WENU HII HAPA

Stars yafika salama Abidjan, kuwavaa Tembo wa Ivory Coast kesho

Kikosi cha Taifa Stars kimewasili salama mjini Abidjan mchana wa jana huku Kocha Mkuu wa timu hiyo Kim Poulsen akisema mechi dhidi ya Ivory Coast itakuwa ngumu. Kwa mujibu wa ofisa habari wa TFF Boniface WAmbura ambaye ameambatana na timu, Stars yenye wachezaji 21 ilikuwa iwasili hapa asubuhi, lakini ndege iliyobadilisha Nairobi ilichelewa kuondoka kwa saa tatu. Mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Taifa Stars na wenyeji Ivory Coast (Tembo) itachezwa Juni 2 mwaka huu Uwanja wa Felix Houphouet-Boigny kuanzia saa 11 kamili jioni ambapo Tanzania itakuwa saa 2 kamili usiku. Licha ya kwanza, Stars ililazimika kuacha wachezaji wawili dakika za mwisho (Haruna Moshi na Nassoro Cholo), Kim amesema kikosi chake ambacho kimefikia hoteli ya Ibis bado kimejipanga vizuri kwa ajili ya mechi hiyo. “Tunaiheshimu Ivory Coast kwa vile ni timu ambayo inaundwa na baadhi ya wachezaji nyota wa dunia kama akina Drogba (Didier) na Yaya (Toure), lakini wajiandaa kupata wakati mgumu kutoka kwetu,” amesema Kim ambayo kikosi chake baada ya kuwasili hapa kilipata fursa ya kufanya mazoezi jioni. Kikosi cha Stars kinaongozwa na nahodha wake Juma Kaseja akisaidiwa na Aggrey Morris. Wachezaji wengine waliopo hapa na kikosi hicho ni Mwadini Ally, Deogratius Munishi, Amir Maftah, Erasto Nyoni, Kelvin Yondani, Waziri Salum, Shomari Kapombe na Juma Nyoso. Jonas Mkude, Mwinyi Kazimoto, Salum Abubakar, Shabani Nditi, Edward Christopher, Mrisho Ngasa, Frank Domayo, Mbwana Samata, Ramadhan Singano, Simon Msuva na John Bocco. Mbali ya Kim, Benchi la Ufundi lina Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi), Juma Pondamali (Kocha wa makipa), Leopold Mukebezi (Meneja wa timu), Juma Mwankemwa (Daktari wa timu), Frank Mhonda (Physiotherapist) na Alfred Chimela (Mtunza vifaa).
Msafara wa Stars hapa unaongozwa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Crescentius Magori lakini pia yupo Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Dioniz Malinzi ambaye amekuja kushuhudia mechi hiyo.

Kipa Lyon akiri udhaifu, ajipanga

MLINDA mlango wa kutumainiwa wa timu ya African Lyon, Noel Lucas, amekiri kuwa msimu uliopita timu yao haikuwa katika ubora wake, huku mwenyewe akishuka kiwango jambo lililosababisha timu yao kunusurika kushuka daraja. Hata hivyo, alisema yeye binafsi amekuwa akitumia muda wake wa mapumziko kwao Kigoma kujifua ili kurejesha kiwango chake na akiamini pia usukwaji upya wa kikosi chao unaweza kutoa ushindani mkubwa katika msimu ujao. Akizungumza na MICHARAZO
kwa njia ya simu kutoka Kigoma, Lucas alisema Lyon kwa msimu uliopita ilicheza chini ya kiwango na kusababisha kuwa na wakati mgumu kabla ya kunusurika kushuka daraja dakika za mwisho. Kipa huyo aliyepoteza namba kwa kipa mwenzake Abdul Seif, alisema hata hivyo anashukuru timu yao kupona kurudi Ligi Daraja la Kwanza, akiamini msimu ujao itakuwa timu tishio huku mwenyewe akidai anajipanga upya. "Najipanga kurejesha makali yangu, sio siri msimu uliopita sikuwa katika kiwango kabisa na ndio maana nilipoteza namba," alisema Lucas. Kipa huyo ambaye kabla ya kutua Lyon alitamba timu za Small Boys ya Singida, FC Congo ya Kigoma na Toto Afrika ya Mwanza na mwaka jana kuipa Kombe la Taifa mkoa wa Singida 'Kindai Shooting' kwa mara ya kwanza mkoa huo kufanya hivyo.

Coastal yamng'ang'ania Nsa Job

UONGOZI wa klabu ya Coastal Union ya Tanga, umesisitiza kuwa umeshamalizana na mshambuliaji wa Villa Squad, Nsa Job, aliyedai bado hajasaini kwao. Aidha, uongozi huo umetangaza kuwanasa nyota wengine wawili, Selemain Kassim 'Selembi' aliyekuwa akiichezea African Lyon kwa mkopo akitokea Azam na Mohammed Soud wa Toto Afrika ya Mwanza. Afisa Habari wa Coastal Union, Eddo Kumwembe, aliiambia MICHARAZO kuwa, Nsa aliyenukuliwa hajasaini kokote, ameshamwaga wino kwao tangu wiki iliyopita hivyo ni mali yao kwa ajili ya msimu ujao. Kumwembe alisema, Nsa ni mmoja kati ya wachezaji watatu ambao wameshamalizana nao mpaka sasa kwa ajili ya kusuka kikosi chao kwa msimu ujao, wengine wakiwa ni Selembi. "Nsa ni mmoja wa wachezaji wetu wapya ameshasaini fomu za usajili tangu karibu wiki sasa, tunashangaa akituruka, ila huenda hakupenda watu wajue mapema, lakini ukweli ndio huo msimu ujao ni wetu," alisema. Msemaji huyo aliongeza kuwa mbali na wachezaji hao watatu, pia wanakaribia kumnasa kinda wa timu ya taifa, (Taifa Stars), Simon Msuva aliyekuwa katika timu iliyoshuka daraja ya Moro United akitokea kikosi cha U-20. "Kwa sasa tunamfukuzia Msuva ambapo tunakaribia kumnasa," alisema Kumwembe. Coastal Union iliyorejea Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu na kumaliza katika nafasi ya tano, tayari imetangaza kuwatema wachezaji wake tisa akiwemo Ally Ahmed Shiboli aliyemwaga wino Polisi Moro iliyopanda daraja msimu huu. Wengine waliotemwa sambamba na Shiboli ni Ramadhani Wasso, Ben Mwalala, Samuel Temi, Enock John, Laurent Mugia, Bakari Mohamed, Daudi Changula na Francis Busungu.

Malipo kiduchu yamkimbiza bondia ulingoni

BONDIA machachari wa ngumi za kulipwa nchini, Saleh Mkalekwa, amesema malipo madogo wanayolipwa mabondia wengi akiwemo yeye yamefanya wengi wao kufa maskini, jambo linalomfanya afikirie kuachana na mchezo huo kabla ya kutimiza ndoto zake. Akizungumza na MICHARAZO
, Mkalekwa mwenye rekodi ya kucheza mara saba, akishinda sita na kupoteza moja, alisema alipotumbukia katika ngumi alikuwa na ndoto nyingi ikiwemo kutamba kimataifa, ila amekatishwa tamaa na malipo kiduchu anayolipwa. Alisema hali ya kulipwa kidogo haipo kwake tu, bali karibu mabondia wote ambao licha ya kuhatarisha maisha yao wamekuwa hawathaminiwi zaidi ya kuwanufaisha wasimamizi wa mchezo huo wakiwemo mapromota. Mkalekwa alisema kutokana na hali hiyo anafikiria kuachana na mchezo huo kwani haoni faida anayopata zaidi ya kuhatarisha maisha yake na kuwanufaisha waandaaji ambao wamekuwa wakiweka mbele masilahi yao kuliko ya mabondia na ngumi kwa ujumla. "Kwa kweli nilitamani mno kufika mbali kama walivyofika wakali wengine, lakini kwa jinsi tunavyonyonywa na kutumiwa kuwaneemesha wengine, ngumi zimenitumbukia nyongo," alisema. Alisema tangu alipoanza kupanda ulingoni mwaka 2008 hajawahi kulipwa pigano lolote malipo yanayozidi Sh 100,000, licha ya gharama kubwa za kuajiandaa na michezo hiyo kitu ambacho akihoji anaambiwa acheze kwanza ili akuze jina lake. "Wenzetu katika soka, hata kama ni chipukizi, wanalipwa fedha ambazo zinawatia nguvu kuendelea kuufurahia mchezo huo sio sisi, ndio maana unaona nimejiweka kando nikijifanyia mazoezi mwenyewe nikishughulisha na biashara ya spea za magari," alisema. Hata hivyo bondia huyo alisema iwapo atafanikiwa kupata mtu wa kumsaidia kumtafutia michezo yenye malipo ya kuridhisha na hasa ile ya kimataifa atakuwa tayari kuendelea na ngumi.

Hili Dude la Kitale videoni

VIDEO ya wimbo mpya wa mchekeshaji maarufu nchini, Mussa Yusuf 'Kitale' uitwao 'Hili Dude' inatarajiwa kuanza kurekodiwa wiki hii. Kitale, alisema atarekodi video hiyo baada ya kuona wapenzi wa muziki wameupokea vizuri wimbo wake huo ulioanza kushika chati katika vituo mbalimbali vya redio. Wakati msanii huyo akimalizia wimbo wa mwisho kuhitimisha albamu yake ya kwanza, alisema, wakati akianza kurekodi video hiyo, pia anajipanga kumalizia wimbo wa mwisho kwa ajili ya albamu yake itakayokuwa na jumla ya nyimbo nane. "Najiandaa kurekodi video ya wimbo wangu mpya wa 'Hili Dude' wakati pia nikijipanga kumalizia wimbo wa mwisho kwa ajili ya albamu yangu ya kwanza," alisema. Alisema mpaka sasa amekamilikisha nyimbo saba alizoshirikiana na wasanii mbalimbali akiwemo Sir Juma Nature na kuzitaja baadhi yake kuwa ni 'Chuma cha Reli', 'Kama Vipi Tulianzishe', 'Anajifanya Msela', 'Kinaunau' na 'Hili Dude'. Kitale, alisema amepanga hadi Julai awe ameikamilisha albamu yake itakayofahamika kwa jina la 'Kama Vipi Tulianzishe' sambamba na video ya nyimbo zote za albamu hiyo.

Loveness apika nyingine mpya

MSANII na mtayarishaji wa filamu anayekuja juu nchini, Loveness Watson 'Love' yupo jikoni akipika kazi nyingine mpya baada ya filamu yake ya 'Impossible Promise' kufanya vema sokoni. Akizungumza na MICHARAZO, Loveness alisema kama ilivyokuwa kwa kazi ya awali ya 'Impossible Promise, filamu hiyo nyingine ameitunga kuiandika na atatayarisha yeye mwenyewe. Loveness alisema, kazi hiyo mpya itakuwa na simulizi la mapenzi ambapo atashirikiana na wakali kadhaa nchini kuicheza filamu hiyo. "Baada ya kuitoa filamu yangu ya 'Impossible Promise' inayofanya vema sokoni kwa sasa nipo jikoni napika kazi hiyo ambayo natarajia kuiachia kabla ya Agosti," alisema. Aidha msanii huyo alisema pia yupo katika maandalizi ya kutumbukia kwenye muziki, akidai fani hiyo aliifanya siku za nyuma kabla ya kuingia kwenye uigizaji wa filamu kwa ushawishi wa kaka yake aliyemtaja kwa jina la Yokania Watson. Alisema tofauti na wasanii wenzake kuimba miondoko mchanganyiko, yeye atajikita zaidi katika mirindimo ya R&B.

Miss Tabata kufanyika leo, Mashauzi na Mashujaa Band kunogesha uhondo

Shindano la kusaka Miss Tabata 2012 linafanyika leo (Ijumaa) katika ukumbi wa Da’ West Park, Tabata. Mratibu wa shindano hilo Joseph Kapinga alisema jana kuwa bendi za Mashauzi Classic na Mashujaa zitawasindikiza warembo 19 watakaopanda jukwaani kuwania taji hilo. Mratibu wa shindano hilo lililoandaliwa na Bob Entertainment na Keen Arts alisema kuwa mshindi wa kwanza atazawadiwa Sh 500,000/- na king’amuzi ambayo imelipia miezi sita yenye thamani ya sh 800,000 iliyotolewa na Multichoice. Mshindi wa pili atapata sh 500,000, mshindi wa tatu sh 350,000 wakati washindi wa nne na watano kila moja atapata sh 200,000. Kapinga alisema warembo watano watawakilisha Tabata kwenye shindano la Miss Ilala. Warembo wengine watakaoingia 10 bora kila moja atapata sh 100,000 wakati waliyosalia watapata Sh 50,000 kila moja. Kapinga alisema shindano hilo pia litatumika kwa ajili ya kusherehekea miaka 10 tangu kuasisiwa kwa shindano la Miss Tabata. “Shindano la mwaka huu sio la kukosa kwani litakuwa ni la aina yake ukizingatia kuwa litatumika kusherekea miaka 10 tangua kuanza kuandaa Miss Tabata,” alisema Kapinga. Alisema warembo waliyowahi kushinda mataji mbalimbali ya shindano hilo, pia wamealikwa kusherehekea miaka 10 ya Miss Tabata. Shindano hili limedhaminiwa na Dodoma Wine, Redds, Integrated Communications, Fredito Entertainment, Multichoice Tanzania, Screen Masters, Kitwe General Traders, Step In Electronics, Brake Point, Atriums Hotel na Lady Pepeta. Mrembo anayeshikilia taji la Tabata kwa sasa ni Faiza Ally. Warembo wa Tabata wamekuwa wakifanya vizuri katika mashindano ya Miss Tanzania ambapo mwaka juzi Consolata Lukosi alishinda nafasi ya tatu kabla ya kutangazwa kuwa balozi wa kinywaji cha Redds. Katika shindano la mwaka juzi Juliet William pia alishinda nafasi ya tatu katika ngazi hiyo ya taifa. Juliet ndiye anayeshikilia taji la dunia la Miss Progressive International.
Washiriki wa Miss Tabata

Monday, May 28, 2012

Uigizaji haulipi kama muziki-Kitale

MSANII KITALE AKTIKA KATIKA POZI TOFAUTI
MSANII nyota wa filamu cha vichekesho nchini, Mussa Yusuf 'Kitale' amedai licha ya fani ya uchekeshaji kutolipa kama muziki, lakini katu hawezi kuachana na fani hiyo. Akizungumza na MICHARAZO, Kitale alisema ndio maana kwa sasa akishirikiana na Husseni Mkiety 'Sharo Milionea' wameandaa filamu zao binafsi zaidi ya tano. Alisema katika muziki msanii ananufaika kwa vile huwa ni kazi yake binafsi tofauti na filamu ambapo mabosi ndio wanaoneemeka na msanii hutumika tu kama kibarua. "Kwenye filamu na uchekeshaji tunaambulia sifa tu, lakini kimasilahi ni kidogo tofauti na muzikio, hata hivyo siwezi kuachana na fani hii kwani nimeshaizoea na kwa sasa kuna kazi mpya ninazoandaa na Sharo Milionea," alisema. Alizitaja kazi hizo kuwa, "Sharo Madimpoz', 'Sharo Crazy', 'Sharo Taxi Driver' na 'Drug Dealer' ambazo anaziandaa kwa kushirikiana na Sharo Milionea ambaye wamekuwa wakiendana katika uigizaji wao. "Hizi ni baadhi ya filamu tutakazotoa ndani ya mwaka huu, sambamba na kazi zetu za muziki ambazo kila mmoja anaifanya na kumpa mafanikio makubwa," alisema. Kitale anayeigiza kama 'teja', alisema amepanga kabla ya kumalizika kwa mwaka huu albamu yake binafsi iwe imeshaingia sokoni.

Manyika avunja ukimya na Wololowololo

NYOTA wa zamani wa Yanga aliyetumbukia kwenye muziki, Manyika Peter, ameachia wimbo mpya uitwao 'Wolowolo', akijiandaa kutolea video yake. Akizungumza na MICHARAZO, kipa huyo aliywahi kung'ara na timu za Mtibwa Sugar, Sigara, Yanga na klabu kadhaa za kimataifa alisema kazi hiyo ni ya pili tangu alipotoa albamu yake mwaka 2004. Manyika, alisema 'Wololowololo' umetoka ikiwa ni miaka minne tangu atoe wimbo wake wake wa mwisho mwaka 2007 uitwao 'Manabii'. "Baada ya kimya kirefu nimetoka na wimbo wa 'Wololowololo' ninaouandalia video yake, hiki ni kibao cha pili baada ya albamu yangu ya 'Unanipeleka Puta' ilitoka mwaka 2004," alisema. Manyika, alisema tofauti na alipotumbukia kwenye fani hiyo mwaka 2001 wakati akiwa anaichezea Yanga, kwa kutoa albamu, safari hii hana mpango huo kwa madai utoaji wa albamu haulipi kama kutoa 'singo'. "Sina mpango wa kutoa albamu, nitaendelea kutoa wimbo mmoja mmoja kwa lengo la kupata shoo ambazo ndizo zinazolipa vema," alisema. Alisema wakati akihangaikia kuitolea video wimbo huo wa 'Wololowololo', tayari kuna nyimbo nyingine mbili ameshaziandika ambazo atazirekodi baadae ili kudhihirisha nia yake ya kujikita jumla kwenye muziki.
MANYIKA PETER KATIKA POZI TOFAUTI KAMA MSANII WA MUZIKI WA KIZAZI KIPYA

Mpeni muda Kim atufikishe mbali kimataifa-Manyika

NYOTA wa zamani wa kimataifa aliyewahi kuzichezea timu za Mtibwa, Sigara na Yanga, Manyika Peter, amewataka wadau wa soka nchini kumpa muda kocha Kim Poulsen, ili afanye kazi zake kwa manufaa ya soka la Tanzania. Pia, aliwataka wadau hao kutoweka matumaini makubwa ya timu yao ya taifa, Taifa Stars kufuzu fainali za Afrika 2013 au Kombe la Dunia 2014, ila nguvu ziwekezwe kwa fainali za mbele zaidi akiamini timu itakuwa imewiva. Manyika, alisema Tanzania imekuwa ikikwama kufika mbali kwa vile makocha wanaozifundisha timu za taifa na hata klabu hawapewi muda mrefu wa kukaa na timu husika, kitu alichotaka kisitokee tena kwa kocha wa sasa wa Stars. "Tumpeni nafasi Kim aweze kufanya kazi zake na naamini kwa uwezo alionao tunaweza kufika mbali zaidi na hapa tulipo, ila kama tutaendelea na tabia ya kulaumu kisha aondolewe tutadumaa hapa hapa kisoka," alisema. Alisema Kim, ni mmoja wa makocha wazuri kutokana na kufanya nae kazi akiwa kama Mkufunzi wa FIFA wa makipa wa timu za taifa za vijana, hivyo aliwataka wadau wa soka wasimbughudhi ili afanye kazi zake kwa ufanisi. Aliongeza, licha ya kuwataka wadau wawe na subira pia wasiweke tumaini kubwa la Tanzania kufuzu fainali zijazo za Afrika zitakazofanyika Afrika Kusini au Kumbe la Dunia la Brazil, ingawa alikiri lolote linaweza kutokea. "Tukifuzu itakuwa ni bahati, lakini nadhani tunapaswa kuweka nguvu kwa ajili ya fainali za mbele, tumechelewa mno kujipanga hivyo lolote litakalotokea tulichukulie poa na kujipanga zaidi ili tufuzu michuano ijayo," alisema. Tanzania ipo kwenye mbio za kuwania kufuzu fainali za Afrika ikitarajiwa kuvaana na Msumbiji katika mechi ya marudiano Juni 15 baada ya awali kutoka sare. Pia ipo kundi C na timu za Ivory Coast, Morocco na Gambia katika mbio za kuwania kucheza fainali za Kombe la Dunia za 2014 zitakazofanyika nchini Brazil, ikianza kibarua Juni 2 kwa kuumana na Ivory Coast.

Sijasaini kokote-Nsa Job

MSHAMBULIAJI nyota wa timu ya Villa Squad, Nsa Job, amesema licha ya kuzungumza na watu wa Coastal Union ya Tanga, bado hajasaini fomu yoyote ya kujiunga kuichezea timu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara. Kutokana na kutosaini, Nsa alisema milango i wazi kwa klabu yoyote ambayo imevutiwa naye, mradi aridhishwe na dau watakalokubaliana. Akizungumza na MICHARAZO, Nsa alisema ni kweli amefanya mazungumzo na Coastal Union, ila hawaafikiana na ndio maana hajasaini fomu na hivyo kutoa ruksa kwa timu nyingine kuweza kuzungumza nae. "Sijasaini kokote ndugu yangu, ingawa ni kweli nilishafuatwa na kuzungumza na watu wa Coastal Union," alisema. Nsa, alisema yeye kama mchezaji anaangalia masilahi hivyo timu yenye dau kubwa la kuvutia ndio atakayoichezea kwa msimu huo ujao. Nyota huyo aliyewahi kuzichezea timu za Moro United, Simba, Yanga na Azam, alisema hawezi kukurupuka kusaini timu bila kuangalia masilahi yake ikizingatiwa soka kwake ndio ajira inayomuingizia kipato. "Soka la sasa sio la kuchezea sifa, naangalia masilahi kwanza timu baadae," alisema.

Boxer Johnny Tapia has died at the age of 45

Tapia, whose career was marked by cocaine addiction, alcohol, depression and run-ins with the law, was found dead on Sunday in his hometown of Albuquerque, New Mexico. He won the WBO super-flyweight title in 1994, two belts at bantamweight and the IBF featherweight belt in 2002. Police spokesman Robert Gibbs said the death "did not appear to be suspicious". His tragic start in life - both parents were murdered, several stints in jail and numerous rivalries, garnered him a cult following in the sport. Tapia was orphaned at eight when his mother was murdered in brutal circumstances and, despite his successes in the ring, trouble stalked him for the rest of his life. Having been banned from boxing for three and a half years in the early 1990s because of his cocaine addiction, he beat Henry Martinez to become a world champion for the first time. Tapia went 11 years unbeaten as a professional before Paulie Ayala defeated him in 1999 in The Ring magazine's Fight of the Year, taking his WBA bantamweight title. Tapia lost a rematch with Ayala in 2000. In 2002 he beat Manuel Medina to secure the IBF featherweight crown and was good enough to take Mexican great Marco Antonio Barrera the distance later that same year. In 2007, he was hospitalised after an apparent cocaine overdose. Several days later, his brother-in-law and his nephew were killed in car accident on their way to Albuquerque to see the ailing boxer. In his 2006 autobiography, Tapia described how he had been declared clinically dead five times, each time due to a drug overdose. He also survived shootings, a bus crash and a near-drowning. Tapia last fought in June, outpointing Mauricio Pastrana. He finished with a 59-5-2 record.

Friday, May 25, 2012

Jackson Chove ajipigia debe

KIPA wa timu iliyoshuka daraja ya Moro United, Jackson Chove, amesema yupo tayari kujiunga na timu yoyote itakayomhitaji kwa sababukiwango chake kipo juu licha ya timu yake kuporomoka. Chove, ambaye aliwahi kuzidakia Yanga, Prisons-Mbeya, JKT Ruvu na Azam kabla ya kutua Moro United, alisema kama mchezaji anatambua soka ndio ajira yake, hivyo kila siku anaendelea kujivua kujiweka fiti ili aendelee kutesa. Alisema, timu yoyote ambayo itaridhiana nae atakuwa tayari kujiunga nayo kwa ajili ya msimu ujao, ingawa alisisitiza kuwa yupo katika maandalizi ya kwenda Msumbiji kucheza soka la kulipwa. "Kwa kweli nipo tayari kutua timu yoyote baada ya timu yangu ya Moro Utd kushuka daraja, soka ndio kazi yangu hivyo kokote mie nacheza," alisema. Chove, aliyewahi kucheza soka la kulipwa nchini DR Congo na Rwanda kwa nyakati tofauti baada ya kutemwa Yanga, alisema anaamini yeye ni miongoni mwa makipa mahiri nchini, ila hajapata sehemu ya kuonyesha makali yake. Kipa huyo anayefahamika kama Mandanda, alisema kwa kuwa msimu mpya ndio unaanza sasa kwa klabu kusajili wachezaji wapya na kuacha wa zamani, naye anasubiri mahali atakapoangukia kwa ajili ya msimu ujao. Chove, alikuwa miongoni mwa makipa tegemeo wa Moro Utd iliyoshindwa kuhimili vishindo vya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu iliyoirejea toka daraja la kwanza na kuteremka pamoja na Polisi Dodoma na Villa Squad. Mwisho

TPBO yamlilia Mafisango, yaasa wachezaji Simba

OGANAIZESHENI ya Ngumi za Kulipwa nchini, TPBO, imetuma salamu za rambirambi kwa klabu ya soka ya Simba kutokana na msiba wa kiungo wao nyota, Patrick Mutesa Mafisango aliyefariki wiki iliyopita kwa ajali ya gari. Rais wa TPBO, Yasin 'Ustaadh' Abdallah, alisema wameshtushwa na kifo cha ghafla cha mchezaji huyo aliyekuwa kiigizo chema kwa wachezaji vijana nchini na kuungana na ndugu, jamaa na wadau wa klabu ya Simba kwa msiba huo. Ustaadh, alisema wadau wa ngumi hasa wanaopenda kuhudhuria michezo mbalimbali ya soka, wanajua namna gani Simba imepata pigo kwa kufiwa na kiungo huyo rais wa Rwanda ingawa mwenyeji wa DR Kongo. "TPBO tunaupa pole uongozi wa Simba na wadau wote wa klabu hiyo na soka kwa ujumla kwa kuondokewa na Patrick Mafisango, kama wadau tunaungana nao katika majonzi na kuwatakia moyo wa subira," Ustaadh alisema. Aliongeza kwa kuwataka wachezaji wenzake ambao anafahamu itawachukua muda mrefu kusahau kifo cha Mafisango kumuenzi mwenzao kwa kuiheshimu kazi yake aliyoifanya enzi za uhai wake kwa kuipa Simba mafanikio zaidi. "Najua ni vigumu wadau wa Simba kusahau msiba wa Mafisango, lakini TPBO tunaamini nnia pekee ni kumshukuru Mungu kwani kazi yake haina makosa na pia kumuenzi kwa kuipa Simba mafanikio zaidi," alisema. Patrick Mutesa Mafisango, aliyezikwa Jumapili iliyopita nyumbani kwao, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, alifariki usiku wa kuamkia Alhamisi iliyopita kwa kupata ajali ya gari akitokea Maisha Club 'kujirusha'. Kiungo huyo aliyewahi kung'ara na timu za TP Mazembe, APR, Azam kabla ya kutua Simba akiichezeapia timu ya taifa ya Rwanda 'Amavubi', amefariki akitokea kuisaidia Simba kutwaa taji la Ligi Kuu Tanzania Bara 2011-2012.

ZFA yaifungulia milango Yanga kutua Zenji

MSEMAJI WA ZFA, Munir Zakaria CHAMA cha Soka cha Zanzibar, ZFA, kimesema kipo tayari kuipokea klabu ya Yanga, iliyotishia kutaka kuhamia visiwani humo, mradi wafuate taratibu zinazokubalika. Wazee wa klabu ya Yanga walinukuliwa wiki iliyopita kwamba wanafanya mpango wa kuihamishia Yanga visiwani Zanzibar kutokana na kukerwa na maamuzi ya uongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania, TFF 'kumbeba' Mwenyekiti wao, Llyod Nchunga. Wanachama hao wa Yanga wamekuwa na mgogoro na Nchunga kiasi cha kuitisha mkutano na kuung'oa uongozi huo, jambo lililopingwa na TFF kwa madai ya kutozingatia katiba inayoiongoza klabu hiyo. Jambo hilo lilionyesha kuwakewa wazee hao ambapo kupitia Katibu wake, Ibrahim Akilimali alinukuliwa akitishia kuihamisha Yanga Zanzibar kama njia ya kuikomoa TFF na Nchunga, kitu kilichoufanya uongozi wa ZFA kusema upo tayari kuwapokea. Msemaji wa ZFA, Munir Zakaria alinukuliwa na kituo kimoja cha redio alisema wao wanaisubiri Yanga kutua visiwani humo wakiamini itasaidia kuinua soka la Zanzibar. Zakaria, alisema pia kuhamia kwa Yanga visiwani humo kutaifanya Zanzibar itambe kimataifa na hivyo wanafungua milango kwa klabu hiyo, ila wakiitaka kuzingatia taratibu za kuweza kucheza ligi ya visiwani humo. "Tunawasubiri waje, hatuna vikwazo kwao kwa vile tunaamini watasaidia kuinua soka la visiwani humo, ila wafuate taratibu ikiwemo kama wanaweza wainunue klabu yoyote ya ligi kuu kisha waibadilishe jina kwa kuiita Yanga ili waweze kucheza ligi yetu," alisema. Msemaji huyo ambaye pioa ni Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya ZFA, alisema wao hawaoni tatizo kwa Yanga kujiunga katika ligi yao kwani ni moja ya timu yenye mashabiki wengi visiwani humo na ina jina kubwa katika anga la kimataifa. Hata hivyo, tishio hilo la wazee wa Yanga kutaka kuhamia Zanzibar linaonekana kama 'danganya toto' kwani baadhi ya wanachama wake wamewapuuza wazee hao wakiona kama wanaotapatapa katika kuubana uongozi wa Yanga. "Hatudhani kama hilo linaweza kufanyika, nadhani wazee wanatafuta njia ya kutaka kuungwa mkono katika kile walichokifanya ambacho kinaendana kinyume na katiba hata kama ni kweli viongozi wa Yanga wanakosa," alisema mmoja wa wanachama wa klabu hiyo aliyekataa kutajwa jina la kwa madai ya uhusiano wake wa karibu na wazee. Klabu ya Yanga imekuwa katika hali tete tangu walipopoteza taji lao la ubingwa wa Ligi Kuu kwa watani zao, na pia kupokea kichapo cha aibu cha mabao 5-0 mbele ya Simba katika mechi ya kufungia msimu wa ligi Tanzania Bara. Hata hivyo tayari Nchunga ameshatangaza kuachia ngazi mwenyewe kwa hiari yake, na hivyo suala au tisho la Yanga kuhamia Zenji huenda lisiwepo tena. TUSUBIRI TUONE!

Watanzania zidini kuniombea, tumaini la kupona lipo-Sajuki

NYOTA wa filamu ambaye yupo nchini India kwa matibabu, Juma Kilowoko 'Sajuki' amewataka Watanzania kuzidi kumuombea kwa Mungu ili aweze kupona matatizo yake, akisema wakati akituoa nchini humo kwa matibabu hali yake ilikuwa tete. Akizungumza toka India, Sajuki alisema hali yake ilikuwa mbaya alipofika nchini humo ambapo alipimwa na kukutwa hana damu na huku akiwa kadhoofika kiasi cha kushindwa kufanyiwa chochote. Alisema hata hivyo uangalizi aliopewa katika siku chache zilizopita hali yake imeimarika na sasa anasubiri kupimwa tena kuona kama anaweza kufanyiwa upasuaji kuondoa uvimbe ambao alidai umeongezeka sehemu nyingine ya tumbo lake. "kwa kweli mpaka nazungumza hivi ujue nimeimarika, nilikuwa na hali mbaya hasa baada ya kubainika kuwa kulikuwa na vivimbe vingine vilivyodhoofisha afya yangu na pia nilikuwa na upungufu wa damu, hivyo nikawa katika uangalizi maalum, ila nashukuru mno na ninawaomba Watanzania waniombee," alisema. Sajuki, alisema wakati wowote kuanzia sasa huenda akafanyiwa upasuaji ambao ndio unaoelezwa ni salama ya maisha yake. Wakati akiondoka nchini, Sajuki aliwaliza watu kutokana na kushindwa kutembea mwenyewe na pia alionekana kadhoofu maradufu tofauti na siku za nyuma kabla ya kusafiri kwenda kufanyiwa matibabu nchini humo. Msanii huyo anatibiwa katika hospitali ya Saifee iliyopo Mumbai na sio Apollo kama ilivyokuwa ikiripitiwa awali na vyombo vya habari.

Hili Dude la Kitale ni nouma!

MCHEKESHAJI maarufu nchini, Mussa Yusuf 'Kitale' ameachia wimbo mpya uitwao 'Hili Dude' ukiwa miongoni mwa nyimbo anazoziandaa kwa ajili ya albamu ya kwanza. Akizungumza na MICHARAZO, Kitale ambaye amepata umaarufu mkubwa kwa kuigiza kama 'teja', alisema tayari ameshausambaza wimbo huo mpya katika vituo vya radio huku video yake ikiwa katika hatua za mwisho kabla ya kuachiwa. Kitale alisema kibao hicho ni cha pili kwake baada ya awali kufyatua 'Chuma cha Reli' alichokiimba na Gondo Msambaa. "Nimekamilisha dude jipya, linaitwa 'Hili Dude' ambalo limeshaanza kurushwa hewani ikiwa ni utambulisho wa albamu yangu ambayo tayari nyimbo saba kati ya nane zimeshakamilika," alisema. Alisema katika wimbo huo mpya, ameimba kwa kushirikiana na Mide Zo na Corner ambaye pia ndiye prodyuza wa wimbo huo kutoka studio za Kwanza Records ya mjini Morogoro. Msanii huyo alizitaja nyimbo nyingine zitakazokuwa katika albamu hiyo kuwa ni 'Anajifanya Msela' alioimba na Juma Nature, 'Hili Toto' alioimba na Sharo Milionea na Mide Zo, ' Tulianzishe', 'Kinaunau' na 'Chuma cha Reli'. "Wimbo wa mwisho nimeshautunga, ila sijaurekodi kwa sababu bado naendelea kufanya mazungumzo na mmoja wa wasanii kwa ajili ya kuimba nae," alisema. Aliongeza, ameamua kutumbukia kwenye muziki baada ya kuona fani ya uchekeshaji ikiwa haimlipi kwa vile kazi nyingi hufanya chini ya watu ambao ndio hunufaika.

Dogo Aslay kupagawisha Dodoma

DKAMPUNI ya Ruhazi Promotion ya jijini Dar es Salaam, inatarajia kumtambulisha msanii chipukizi anayetamba hivi sasa katika muziki wa kizazi kipya nchini Aslahi Isihaka ‘Dogo Aslay’ kwa mashaki wa mjini Dodoma . Akizungumza na mwandishi wa habari hizi jijini Dar es Salaam jana mratibu wa onesho hilo Jackline Masano, alisema kuwa onesho hilo litafanyika Jumamosi Juni 9 kwenye uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma . Alisema kuwa wasanii wengine kutoka kituo cha Mkubwa na Wanawe watamsindikiza na kuwa mazungumzo na wasanii wengine watakaopamba onesho hilo yanaendelea na kwamba watawatangaza pindi watakapomalizana nao. “Tumeamua kuwaletea wapenzi wa burudani wa Dodoma burudani ya uhakika Jumamosi ya Juni 9, litaanza saa 6:00 mchana na litamalizika saa 12:00 jioni ambapo Dogo Aslay akisindikizwa na wasanii kutoka mkubwa na Wanawe na wasanii nyota nchini ambao tutawatangaza majina yao tukishamaliza makubaliano nao,” alisema Jackline. Alisema pamoja na kwamba onesho hilo litapambwa na wasanii wengi lakini wameamua kiingilio kiwe cha shilingi 5,000 tu kwa wakubwa na shilingi 1000 kwa watoto ili kuwawezesha wapenzi wengi zaidi waweze kukimudu na kushuhudia burudani hiyo.

Steve Nyerere kusomesha yatima kwa miaka 7

MSANII wa filamu nchini ambaye pia huiga sauti za viongozi mbalimbali, Steve Mengele 'Steve Nyerere' jana amezindua filamu yake mpya inayojulikana kama 'Mwalimu Nyerere', huku akiahidi kuwasomesha watoto wawili yatima wa kituo cha Maunga Centre ulipofanyikia uzinduzi wa filamu hiyo. Akizungumza mara baada ya kuzindua filamu hiyo akiwa pamoja na watoto yatima wa kituo hicho, Steve Nyerere alisema ameamua kufanya hivyo kutokana na ukweli kwamba Baba wa Taifa Mwali Nyerere hakubagua watu. Alisema ujio wa filamu hiyo ni kama azma yake aliyoipanga tangu awali kuhakikisha anamuenzi Baba wa Taifa kwa kutoa filamu itakayokuwa inaonesha mambo mbalimbali aliyowahi kuyafanya Baba wa Taifa. "Jina lililonibeba zaidi katika tasnia hii ya filamu ni jina la Steve Nyerere kiasi ambacho hata jina la Baba yangu halijanizoea, hivyo kutokana na ukubwa wa jina hili limenifanya mimi kutambulika na jamii nzima ya Tanzania hivyo ili kulienzi jina hili nimeamua kutoa filamu hii ya Mwalim Nyerere,"alisema Steve. Alisema msaada alioutoa kwa watoto yatima hautaishia kwao bali ataendelea kutoa kile atakachokipata kupitia filamu hiyo kuwasaidia na wale wasiojiweza. Alisema filam ya Mwalimu Nyerere ameifanyia Butiama alipozaliwa Baba wa Taifa ili kujenga uhalisia wa kile alichodhamiria na kwamba ameitengeneza filamu hiyo kwa kipindi cha miezi mitatu huku akishirikiana vema na mke wa Hayati Baba wa Taifa Mama Maria Nyerere. Alisema jumla ya sh. milioni 25 ametumia katika kuikamilisha filam hiyo ambayo itaanza kuingia sokoni leo ikiwa chini ya usambazaji wa Steps Entertaiment. Kabla ya kutoa filam hiyo Steve Nyerere alitamba na filam ya 'Mr President' aliyoitunga kwa kuvaa uhusika wa Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania Dkt.Jakaya Kikwete ambayo aliitaja kama zawadi kwa Rais Kikwete katika kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika

Twiga yapaa kuwafuata wahabeshi, wamwagiwa 'mihela'

TIMU ya taifa ya soka ya wanawake Tanzania, Twiga Stars imeondoka jana jioni kwa ndege ya Ethiopian Airlines kuelekea Ethiopia ikiwa imekabidhiwa Bendera ya Taifa na Naibu Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Amos Makalla. Twiga Stars yenye msafara wa watu 24 wakiwemo wachezaji, benchi la ufundi na viongozi itacheza na Ethiopia katika mechi ya kwanza ya raundi ya pili ya michuano ya mchujo kwa ajili ya Fainali za Nane za Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) zitakazofanyika Novemba mwaka huu Equatorial Guinea. Mechi hiyo itafanyika Mei 27 mwaka huu kwenye Uwanja wa Addis Ababa wakati ile ya marudiano itachezwa Juni 16 mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Twiga Stars ikifanikiwa kuitoa Ethiopia itakuwa imepeta tiketi ya kwenda Equatorial Guinea. Wachezaji walioondoka na kikosi hicho ni Amina Ally, Asha Rashid (nahodha), Ester Chabruma, Ettoe Mlenzi, Evelyn Sekikubo, Fadhila Hamad, Fatuma Bashiri, Fatuma Khatib, Fatuma Mustafa, Fatuma Omari, Maimuna Said, Mwajuma Abdallah, Mwanahamisi Omari, Mwanaidi Tamba, Mwapewa Mtumwa, Rukia Hamis, Semeni Abeid na Zena Khamis. Kwa upande wa Benchi la Ufundi ni Charles Mkwasa (Kocha Mkuu), Nasra Mohamed (Kocha Msaidizi), Furaha Francis (Meneja wa Timu), Mwanahamisi Abdallah (Mtunza Vifaa) na Christina Luambano (Daktari wa Timu). Twiga Stars ambayo msafara wake unaongozwa na Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu kwa Wanawake Tanzania (TWFA) ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) itarejea nyumbani Mei 28 mwaka huu saa 6 mchana kwa ndege ya Ethiopian Airlines. Timu hiyo imeondoka ikiwa imemwagiwa posho toka serikalini na wadhamini wengine kama motisha ya kufanya vema katika mechio yao dhidi ya wahabeshi watakaoumana nao kesho Jumamosi. Katika hatua nyingine, Ligi ya Taifa inayoshirikisha mabingwa wa mikoa sasa itaanza Mei 27 mwaka huu badala ya Mei 26 mwaka huu kama ilivyokuwa imepangwa awali. Uamuzi wa kusogeza mbele kwa siku kuanza kwa ligi hiyo uliofanywa na Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Mei 23 mwaka huu). Timu 23 zitachuana katika kinyang’anyiro hicho kitakachofanyika katika vituo vya Kigoma (Uwanja wa Lake Tanganyika), Musoma (Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume) na Mtwara (Uwanja wa Umoja) ambapo kinatarajia kumalizika Juni 13 mwaka huu. Kituo cha Kigoma kina timu za Aston Villa ya Singida, Bandari (Kagera), CDA (Dodoma), JKT Kanembwa (Kigoma), Majimaji (Tabora), Mwadui (Shinyanga) na Pamba (Mwanza). Ashanti United ya Ilala, Flamingo (Arusha), Forest (Kilimanjaro), Korogwe United (Tanga), Nangwa VTC (Manyara), Polisi (Mara), Red Coast (Kinondoni) na Tessema ya Temeke ziko kituo cha Musoma. Kituo cha Mtwara kina timu za Kurugenzi ya Iringa, Lindi SC (Lindi), Mighty Elephant (Ruvuma), Mkamba Rangers (Morogoro), Mpanda Stars (Rukwa), Ndanda (Mtwara), Super Star (Pwani) na Tenende (Mbeya)

Nchunga aachia ngazi baada ya 'kutishwa'

Mwenyekiti wa Yanga, Lloyd Nchunga akisoma taarifa yake mbele ya waandishi wa Habari (hawapo pichani)jana jijini Dar, kutangaza kujiuzulu uongozi ndani ya klabu ya Yanga. MWENYEKITI wa Yanga, Wakili Lloyd Baharagu Nchunga ametangaza kujiuzulu wadhifa wake jioni hii ofisini kwake, jengo la NSSF, barabara ya Bibi Biti, Dar es Salaam, siku moja baada ya kuvamiwa na kundi la watu nyumbani kwake, Mbezi, Jijini usiku wa wa manane. Hata hivyo, Nchunga amekataa kulihusisha tukio la kuvamiwa kwake usiku wa juzi na kujiuzulu kwake, akisema kwamba amefikia uamuzi huo kuinusuru Yanga, kwa sababu wapo watu wako tayari Yanga ife, lakini wamng'oe yeye madarakani, kitu ambacho yeye hapendi kitokee. Nchunga alisema kwamba majira ya saa nane usiku wa jana, alivamiwa na kundi la watu takribani 15, lakini hawakufanikiwa kufanya chochote kutokana na ulinzi mkali uliopo katika nnyumba hiyo. "Kwanza mbwa walianza kubweka, walinzi wakashituka wakaomba msaada kwa walinzi wenzao, nasi tukapuga simu polisi, wakaja haraka sana na kukuta watu hao wamekwishakimbia,"alisema ISOME TAARIFA RASMI YA KUJIUZULU KWA NCHUNGA: LLOYD NCHUNGA BIHARAGU C/O LLOYD ADVOCATES, Morogoro/Bibi TIti Mohamed Rd,7th Floor, J.K. Nyerere Pension towers P.BOX 75111, Dar-Es- Salaam,Tanzania. TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU KUJIUZULU NAFASI YA UENYEKITI WA KLAB YA YANGA. Ndugu wana Habari, najua kwamba taarifa hii itawafedhehesha wajumbe na wanayanga wanaotuunga mkono,hasa ukizingatia maamuzi ya pamoja ya vikao vyetu vya kamati ya utendaji vilivyopita kwamba hakuna wa kujiuzulu kati yetu mpaka tujue hatma ya mkutano mkuu ambao tulipanga ufanyike tarehe 15 Julai 2012, ukiachia mbali shinikizo la kujiuzulu linalotolewa na baadhi ya wazee na wanaojiita vijana wa klab, kwa wajumbe wa kamati ya utendaji, na hasa mimi kama mwenyekiti. Nawashukuru wajumbe kwamba tulifanya kazi kwa pamoja na kwa ushirikiano mzuri, na hata pale tulipotofautiana tulifanya hivyo kwa hoja na kufikia maazimio ambayo wote tulikuwa tunawajibika nayo. Tangu tumeingia madarakani tumeweza kushirikiana na kupata mataji matatu katika kipindi cha mwaka mmoja, yaani; Ngao ya Hisani 2010, Ubingwa wa ligi kuu ya Vodacom 2010/2011, na Ubingwa wa Afrika Mashariki na Kati (Kagame Cup), 2011. Zaidi ni kwamba tuliuwa uteja kwa watani wetu wa jadi kila tulipokutana katika ligi ukiachia mbali mechi ya tarehe 6 Mei 2012, ambayo tulifungwa goli 5 bila, na kuleta mtafaruku mkubwa katika klab yetu. Hali kadhalika tumeshirikiana mpaka tumeweza kuboresha mkataba kati yetu na TBL kupitia Kilimanjaro Premium Lager, tumeingia mkataba na kampuni ya NEDCO kuendeleza mali zetu katika mtaa wa mafia na uwanja wetu wa KAUNDA baada ya kufikia hatua nzuri katika kupata hati miliki za maeneo yote mawili. Nafahamu kwamba kampuni hiyo iko katika hatua za mwisho za kumalizia michoro. Hali kadhalika tuliingia mkataba wa kuzalisha na kuuza bidhaa zenye nembo yetu na hasa baada ya kufanya marekebisho yatokanayo na matakwa ya sheria kule BRELA na pia mkataba na kampuni ya NEXUS LTD, ambayo itakuwa inatutafutia wadhamini wa nje na ndani, kufanya promosheni zetu na kampeni kwa njia ya electronic kupitia mitandao mbalimbali na kukusanya data za wanachama na kusajili wapya tukiwa na malengo ya kukusanya shilingi 300,000,000/= hadi 800,000,000/= kwa mwaka katika kipindi cha miaka mitatu. Haya yote tuliyafanya tukilenga kujitegemea kujazia mapengo yaliyokuwa yakitokana na kutegemea ufadhili wa mtu mmoja mmoja. Kwa ridhaa yenu tumekua tukiendelea na mazungumzo na makampuni mbali mbali kwa ajili ya udhamini na kwa sababu maalum, nitazitaja katika hati ya makabidhiano kwa kiongozi ajaye. Aidha, tumeshirikiana katika kufanya mambo mbali mbali ya kijamii, ikiwa ni pamoja na sikukuu ya kuadhimisha miaka 77 ya Yanga, sikukuu za pasaka, kuchangia jamii na waliokumbwa na maafa, na kongamano la vijana lililolenga kuwaamsha vijana kuitambua nafasi yao katika Yanga ikiwa ni pamoja na kupata azimio la kuanzisha SACCOSS ya Yanga, ambapo maombi yapo kwa msajili Manispaa ya Ilala. Haya yote nayataja ikiwa ni kuwashukuru kwa ushirikiano na ikiwezekana muweze kuyakamilisha yaliyobaki ambayo mtaona yalikuwa mazuri. Lakini pia tulipopata matatizo tulikuwa pamoja. Nichelee kusema tu kwamba tulisimama pamoja baada ya kujiuzulu Makamu Mwenyekiti wetu Ndugu Davis Mosha na mjumbe wetu ndugu Seif A. Seif, Ali Mayayi, na wengineo, kwani tulifungwa na katiba.Tulisimama pamoja pia katika suala la kujiuzulu ndugu Yusuf M. Manji, aliyekuwa mdhamini mteule na mfadhili mkuu ambaye sasa ameonyesha nia ya kurudi nanyi mkaridhia mkutane naye. Awali, tulitumia kila jitihada za kumrejesha lakini ikashindikana. Hata hivyo doa limetupata baada ya kufungwa na watani wetu goli 5 bila, ambapo kuna wanachama wanaoelewa na wasioelewa kabisa. Ninachokiona mimi ni usaliti wa hali ya juu uliombatana na matukio mbalimbali yaliyopita na yanayoendelea hadi kujaribu kupindua uongozi wa halali wa kidemokrasia. SIWATUHUMU WACHEZAJI MOJA KWA MOJA, isipokuwa mfululizo wa matukio wiki tatu kabla ya mchezo ule na sasa, inaonyesha kwamba kulikuwa na usaliti mkubwa ambao sisi hatukuweza kuubaini mapema. Sioni mantiki katika hoja kwamba wachezaji walikuwa wakidai mishahara, posho n.k. Au ati mtendaji wetu alishikiliwa Arusha kwa deni la hoteli, ndiyo tuvune bao 5! Kwa wanaoijua Yanga, imewahi kuwa na madeni makubwa katika Hoteli mbali mbali, mawakala wa ndege n.k, na baadhi tumeyakuta na sisi tumekuja tukayalipa. Hii imewahi kutokea kabla na wakati akiwepo mfadhili, sembuse sisi tulioachwa baki, na bado wachezaji walicheza kwa morali. Hata hivyo, utamaduni wa kutimuana baada ya matokeo mabaya ni dhambi ambayo itatula kama hatutaiacha, kwani wenye hila na uchu wa madaraka wataendelea kutumia mbinu hiyo ili kuuondoa uongozi wa kidemokrasia. Baada ya mapinduzi kushindikana na TFF kuonya kuhusu mapinduzi hayo, wazee kupitia msemaji wao , Mzee Akilimali wamesikika katika kipindi cha Michezo cha Redio moja maarufu hapa nchini wakidai kwamba ni bora Yanga ishushwe daraja au kufungiwa kuliko mimi kuendelea kuongoza! Hii imenikumbusha HEKMA ZA MFALME SELEMANI akiamulia ugomvi wa wanawake wawili waliokuwa wakigombea mtoto naye akaamuru wamgawane nusu kwa nusu. Yule mwenye mtoto kweli alimuomba Mfalme amuachie mwenzie kuliko kumkata nusu. Kwa hekma hiyo nimeamua kujiuzulu nafasi yangu katika Uenyekiti wa Yanga kwani ni klab ninayoipenda hata kama sio kiongozi kwa mujibu wa ibara ya 28 ya katiba yetu. Vile vile siko tayari kuona klab yangu ikisalitiwa au kuhujumiwa eti kwa sababu tu mimi ni kiongozi. Natumaini kamati ya utendaji kwa pamoja na wale tuliowateua chini ya ibara ya 29(3) ya katiba ya Yanga pamoja na bodi ya wadhamini, itawaongoza wanachama mpaka kufikia mkutano mkuu kwa mafanikio zaidi. Nitaendelea kuwa mwanachama mwadilifu na nitatoa mchango wangu wa hali na mali pale nitakapo hitajika na nikiwa na uwezo wa kufanya hivyo. YANGA DAIMA MBELE, NYUMA MWIKO. Wasalaam, LLOYD NCHUNGA BIHARAGU. Nakala kwa:- Mama Fatma Karume,Mdhamini Francis Kifukwe, Mdhamini Bwana Yusuf Manji – Kwa taarifa