STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, June 7, 2012

Bingwa wa karate aililia serikali

BINGWA wa mchezo wa Karate kwa nchi za Afrika Mashariki ngazi ya klabu, Sensei Mikidadi Kilindo, ameiomba serikali iutupie macho mchezo huo na kuupa sapoti kama ilivyo kwa michezo mingine ili kuuhamasisha nchini. Aidha, Kilindo amedai kuwa kutopewa kipaumbele kwa mchezo huo ndio kilichomfanya mara zote awe anaenda na kurudi na medali bila hata kutangazwa au kufahamika kwa wananchi kitu kinachomsikitisha. Akizungumza na MICHARAZO , Sensei Kilindo alisema licha ya mchezo huo kuwa na manufaa makubwa kwa taifa na jamii kwa ujumla umekuwa haupewi kipaumbele kama michezo mingine. Alisema kutokana na hali hiyo ni vema serikali na wadau wa michezo kuutupia macho na kuusaidia ili utangazike na kutumiwa kuiletea sifa Tanzania baada ya michezo mingine kushindwa kufanya hivyo. Bingwa huyo wa miaka minne mfululizo wa Afrika Mashariki tangu 2008 alisema, kutopewa kipaumbele kwa karate ndiko kunakofanya hata wachezaji wanaoenda kuitangaza nchi wasifahamike warudipo na ushindi. "Mimi nimerudi hivi karibuni na medali ya dhahabu baada ya kuwa mshindi wa kwanza Afrika Mashariki, hii ni mara ya nne mfululizo, ila hakuna anayejua wala kiongozi aliyewahi kunipokea na kunipongeza inauma sana," alisema. Pia Kilindo alisema ukimya unaofanywa na viongozi wa Chama cha Karate nchini, TASHOKA katika kuutangaza mchezo huo ni tatizo linalofanya usisikike licha ya mafanikio yake kwa ngazi ya klabu. Alisema ni vema TASHOKA ikafanya utaratibu wa kuandaa michuano ya taifa angalau mara mbili kwa mwaka itakayoshirikisha klabu mbalimbali nchini kwa lengo la kuuhamasisha na kuutangaza mchezo huo.

Zuri Chuchu Anapenda Kuishi bwana!

MUIMBAJI wa zamani wa bendi za Bambino Sound na Double M Sound, Zuri Chuchu ambaye kwa sasa anaimba muziki wa Injili, yupo mbioni kuingiza sokoni albamu yake ya kwanza iitwayo 'Napenda Kuishi', huku akianza kuipika nyingine mpya. Zuri, ambaye majina yake kamili ni Esther Charles Mugabo, alisema albamu hiyo yenye nyimbo 12 ilishakamilika mujda mrefu kiasi baadhi ya nyimbo zake kuchezwa redioni, ila aliichelewa kuingiza sokoni kwa sababu zilizo nje ya uwezo wake. Alisema hata hivyo anashukuru kwa sasa mipango yake ya kuitoa hadharani albamu hiyo inaelekea vema na wakati wowote ataingiza sokoni. Zuri, ambaye alitangaza kuishi na VVU akiendesha kampeni mbalimbali kwa sasa kutoa elimu dhidi ya ugonjwa wa Ukimwi, alisema wakati albamu hiyo ya kwanza ikiandaliwa kutoka, tayari ameanza maandalizi ya albamu yake nyingine ya pili. Alisema mpaka sasa amesharekodi nyimbo sita katika studio za Katra Production iliyompa ofa ya kufyatua albamu hiyo bure kama kuunga mkono juhudi zake za kuendesha neno la Mungu na kutoa elimu ya Ukimwi kwa jamii. "Nashukuru kwa nafasi niliyopewa na Katra Studio kutoa albamu yangu ya pili ambapo mpaka sasa nimesharekodi nyimbo sita, wakati nikitaka kuingiza sokoni kwanza albamu yangu ya kwanza iitwayo Napenda Kuishi yenye nyimnbo 12," alisema. Muimbaji huyo, alisema ameamua kutumia muziki kuhubiri na kutoa elimu ya Ukimwi kutokana na ukweli wanaoathirika na ugonjwa huo ni wengi, licha ya kwamba mambo hayawekwi hadharani hivyo anataka maambukizi mapya yasiendelee kuwepo kwa jamii.

Yanga, Simba 'jino kwa jino' kisa Kelvin Yondani

KLABU za soka za Simba na Yanga zimeingia katika vita mpya kufuatia beki wa kati wa kimataifa nchini, Kelvin Yondani kudaiwa kusaini kwa mpigo ndani ya klabu hizo kwa ajili ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao. Wakati Simba ikiendelea kushikilia msimamo kwamba Yondani ni mali yao baada ya kusaini mkataba mpya, Yanga wenyewe wamesisitiza kuwa beki huyo wameshamilazana nao na kuinyoa Simba iache kutupia vitisho katika suala la mchezaji huyo. Afisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu amesema wameshamalizana na Yondani kwa kumsainisha mkataba wa miaka miwili na kwamba kinachofanywa na watani zao kutaka kuwayumbisha mashabiki na kusisitiza watakula nao sahani moja hadi kieleweke ili kubaini nani mkweli katika hilo. Hata hivyo Mwenyekiti wa Simba Ismail Rage, amesema Yanga inajidanganywa kwa Yondani na huenda ikala kwao kwa hasara waliyoingia juu ya beki huyo wa kimataifa ambaye pia anaichezea timu ya taifa, Taifa Stars.

Wednesday, June 6, 2012

Mwenyekiti Villa Squad ajiuzulu, kisa...!

MAKAMU Mwenyekiti wa klabu ya Villa Sqaud aliyekuwa pia akikaimu nafasi ya Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ramadhani Uledi ametangaza kujiuzulu kuiongoza klabu hiyo kwa kile alichodai kutaka kulinda heshima yake. Habari za kuaminika toka katika klabu hiyo iliyoshuka daraja toka Ligi Kuu na yenye maskani yake eneo la Magomeni Mapipa, jijini Dar na kuthibitishwa na Uledi mwenyewe zinasema mwenyekiti huyo ameamua kubwaga manyanga tangu jana. Sababu zilizomfanya Uledi ajiondoe uongozini ni kutokana na kusakamwa na wanachama na kutengwa na viongozi wenzake baada ya kushindwa kushindwa kuinusuru Villa Squad isishuke daraja. Chanzo cha habari cha awali kilisema kutokana na shinikizo kubwa la wanachama hao, Uledi aliamua kubwaga manyanga akiandika barua ya kujitoa madarakani. Hata hivyo MICHARAZO lilipowasiliana na Uledi kutaka kuthibitisha taarifa hizo, alikiri juu ya kujiuzulu kwake, akidai amefanya hivyo ili kulinda heshima yake kutokana na kuona hali si shwari ndani ya klabu yao. Uledi, alisema tangu alipochaguliwa hakuwahi kupata ushirikiano wa kutosha kwa viongozi na wanachama, ila aliichukulia hali hiyo kama changamoto wake, lakini kwa hali inavyozidi kwenda mrama klabu kwao ameona bora ajiengue ili Villa itulie. "Ni kweli nimejiuzulu kutokana na hali ya mambo iliyopo klabuni, pia nahofia kuvunjiwa heshima, hivyo nimewaachia wanachama klabu yao, ingawa bado nitaendelea kuwa ndani ya timu hiyo kwa hali na mali kama mwanachama hai," alisema. Uledi, aliongeza anadhani chokochoko zote zilizopo Villa Squad kwa sasa zimetokana na timu hiyo kushindwa kubaki ligi kuu, japo alidai yapo mambo mengi yaliyochangia timu hiyo kutohimili ushindani hasa kutokana na hali mbaya ya kifedha iliyokuwa nayo. Mwenyekiti huyo na wenzake walichaguliwa kwenye uchaguzi mkuu uliokuwa umejaa mizengwe Juni 25 mwaka jana, huku nafasi ya Mwenyekiti na wajumbe watatu zikiwa wazi baada ya Kamati ya Uchaguzi wa TFF, kuwaengua waliokuwa wagombea wake kwa kukosa sifa za kuwania nafasi hizo ikiwemo suala la elimu zao.

Muziki wa Dansi walilia nafasi redioni, runingani

BAADHI ya wamiliki wa bendi za muziki wa dansi wameomba nyimbo za muziki huo zipewe nafasi ya kutosha katika vipindi vya televisheni na redio ili zisikike kama ilivyo sasa kwa taarab na bongofleva. Walitoa ombi hilo jana jijini Dar es Salaam katika mkutano wao na waandishi kutoka vyombo mbalimbali vya habari huku wakibainisha kuwa nyimbo za muziki huo kwa sasa hazina nafasi kubwa kama zamani. Mratibu kamati ya muda wa wamiliki wa bendi, Khaleed Chuma 'Chokoraa' alisema kuwa wamefikia kutoa ombi hilo baada ya kuona hali inavyokwenda sivyo ndivyo na hivyo kuwa na hofu muziki huo ukapotea kama hautapewa nafasi ya kutosha kwenye vyombo hivyo vya habari. "Tunachofanya sasa ni kujaribu kuwaunganisha wamiliki wote wa bendi za muziki wa dansi wa ndani na nje ya Dar es Salaam kwa lengo ya kufanya mkutano wa pamoja ili kuzungumzia hali hii," alisema Chokoraa. Alisema kuwa tayari baadhi ya wamiliki hao wameshakubaliana katika hilo na kwamba huenda mkutano huo ukafanyika wiki chache zijazo kama watakuwa wamewasiliana kikamilifu na wamiliki wote. "Lengo letu ni kuwaomba wahusika angalau kuangalia uwezekano wa kuufanya muziki wa dansi uwe na nafasi ya kutosha kwenye redio na televisheni ili kuwaibua wanamuziki wachanga nao wajulikane, p[ia muziki wa dansi uwe na vipindi maalum kama ilivyo kwa Bongofleva na Taarab ambao karibu kila redio na televisheni una vipindi," alisema. Naye Msemaji wa kamati hiyo ya muda, Ally Choki, alisema muziki wa dansi ni muziki wa zama na zama, na umekuwa ukisaidia vijana wengine kupata ajira, kwa wamiliki kama wao kuwaajiri, lakini kama hawapewi nafasi ya kutangazika ni vigumu wamiliki kuendelea kutoa ajira hizo. Choki, alisema kama walivyoweza kupewa nafasi na kutangazika wao wakati wakiibuka ndivyo vijana walioingia katika muziki huo nao wanapaswa kutangazwa kama ilivyo kwa wenzao wa miondoko mingine. "Siombi hili labda kwa kutaka nitangazwe, ila kuna vijana ambao wapo kwenye muziki huo hawapati nafasi na hivyo kuwatia unyonge na kusababisha dansi kufa tukiondoka kizazi chetu," alisema. Aliongeza kuwa, kama bendi wamekuwa wakilipa matangazo katika redio na televisheni kwa gharama, lakini fadhila ya matangazo hayo hawayaoni kwa muziki wao kutopewa nafssi katika vituo hivyo. Pia alidai kwamba muziki wa dansi ni mrefu kwa wimbo mmoja sio ukweli kwani wimbo mmoja wa dansi hauzidi dakika 8, lakini taarab wimbo mmoja huchukua hadi robo saa, lakini wanapewa nafasi, kadhaalika nyimbo za kikongo huwa na muda zaidi lakini nazo pia zinapigwa na vituo hivyo, jambo analohisi kinachofanyika ni kama hujuma kwa dansi. Aidha, alisema kwa uchunguzi wao wamebaini watangazaji wengi wa redio na televisheni wamekuwa na mzuka na miondoko mingine zaidi ya dansi kwa vile baadhi yao ni mameneja wa wasanii wa bongofleva na wengine hutumia vikundi vya taarab kuandaa maonyesho kama waratibu hivyo hutoa upendeleo kwa ajili ya masilahi yao binafsi. Choki alisisitiza kilio chaao sio kama kuvilaumu vituo hivyo, ila wanaombwa nao wapewe nafasi kama miondoko mingine kwa sababu muziki wa dani una historia kubwa ya nchi hii pi ni ajira za watu hivyo kama bendi zinazopiga muziki huo zitasahaulika, basi hata ajira za wanamuziki zitakuwa shakani pia. Mratibu huyo alikiri kwamba muziki wa dansi unachezwa na vituo hivyo vya runinga na redio lakini akadai kuwa si kama ilivyo kwa taarab na bongofleva ambao umekuwa ukipewa nafasi kubwa.

Uchaguzi Mkuu Yanga kumekucha, wanawake waitwa Jangwani

WAKATI zoezi la uchukuaji na urudishaji fomu kwa ajili ya uchaguzi mdogo wa klabu ya Yanga ukitarajiwa kufungwa rasmi leo saa 10:00 jioni, wanachama vibopa wa klabu hiyo wamejitokeza kuwania uongozi na kuonyesha namna gani Jangwani walivyopania kufanya mabadiliko ya kuondokana na viongozi 'ombaomba'. Miongoni mwa waliojitokeza kwa jana kuchukua fomu za kuwania madarakani katika uchaguzi huo utakaofanyika Julai 15 ni pamoja na Yono Kevella wa Yono Auction Mart, Muzzammil Katunzi na Mussa Katabalo wanaowania nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo. Wanachama wengine waliochukua fomu jana kuwania ujumbe wa Kamati ya Utendaji ni Eliakim Mmaswi, Lameck Nyambaya, Ahmed Gao na wachezaji nyota wa zamani wa klabu hiyo ambao ni Edgar Fongo, Ramadhani Kampira, Ally Mayai na Aaron Nyanda. Uchaguzi mdogo wa Yanga unatarajiwa kufanyika Julai 15, hatua inayotokana na idadi kubwa ya viongozi waliokuwa madarakani hapo awali kutangaza kujizulu hivi karibuni, akiwemo Lloyd Nchunga aliyekuwa akishikilia nafasi ya uenyekiti. Tofauti na wagombea wengine, Katunzi na Katabalo wao walichukuliwa fomu na wazee wa klabu hiyo ambao wako chini ya mwenyekiti wao Jabir Katundu na katibu, Ibrahim Akilimali. Akimkabidhi fomu Katunzi, Akilimali alisema kuwa lengo la kumtaka mwanachama huyo wa Yanga kugombea ni kuimarisha safu yao ya uongozi ambayo itakuja na jukumu moja tu la kuiendeleza Yanga na kuokoa jahazi lao ambalo anaamini kwamba lilikuwa likizama. Akilimali alisema kuwa Yanga inahitaji wanachama wenye uwezo wa kuisaidia timu wakati wowote ili ifanye vizuri na kurejesha furaha kwa wanachama wao. "Hatuhitaji waomba dagaa, tunataka kiongozi mwenye uwezo ambapo inapohitajika Sh. 300,000, yeye atatoa Sh. 600,000," alisema Akilimali. Hadi kufikia jana, waliochukua fomu kuwania kutwaa mikoba ya Nchunga ni pamoja na John Lambele, huku Ayuob Nyenzi ambaye katika uchaguzi uliopita alijitoa kuwania nafasi ya Makamu Mwenyekiti, akichukua fomu ya kuomba kuchaguliwa kwenye cheo hicho. Wengine waliochukua fomu wakiwania nafasi za ujumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga ni Jumanne Mwamwenya, Peter Haule, Gaudecius Ishengoma, Abdallah Sheria, Saleh Abdallah, Abdallah Binkleb na Muhingo Rweyemamu. Isack Chanzi amejitokeza kuwania nafasi ya Makamu Mwenyekiti ambayo Davis Mosha alijiuzulu mapema mwaka jana baada ya kudai kwamba ameshindwa kutimiza malengo yake kwa kukosa ushirikiano kutoka kwa viongozi wenzake. Uchaguzi huo unasimamiwa na Kamati ya Uchaguzi ya klabu hiyo iliyoko chini ya Jaji Mstaafu John Mkwawa. Hata hivyo mpaka sasa hakuna mwanachama yeyote wa kike wa klabu hiyo aliyejitokeza kuwania uongozi, hali iliyofanya kamati hiyo kutoa wito kwa wanachama hao kujitokeza kwani milango i wazi kwa wote.

John Kitime ajitosa kwenye utunzi wa vitabu, aja na 'vunja mbavu'

MWANAMUZIKI mkongwe wa muziki wa dansi nchini, John Kitime, amejitosa kwenye utunzi wa vitabu, ambapo kwa sasa yuko hatua za mwisho kukamilisha kitabu chake cha kwanza cha 'vunja mbavu' kiitwacho 'Kucheka ni Muhimu'. Akizungumza na MICHARAZO jana, Kitime ambaye ni mwanamuziki wa bendi ya Kilimanjaro 'Wana Njenje na pia ni mmoja wa wanakamati ya kutetea muziki wa dansi nchini, alisema amepata wazo la kuandika kitabu hicho kutokana na kipaji cha uchekeshaji alichonacho. Kitime ambaye wakati mwingine huwa jaji wa shindano la kusaka vipaji vya kuimba la Bongo Star Search, alisema kitabu hicho kwa sasa kipo katika hatua ya uhariri kabla ya kuanza mipango ya kukichapisha na kukisambaza ili kuwapa burudani wapenzi wa vunja mbavu. "Nipo katika hatua ya mwisho ya kumalizia kitabu changu cha kwanza kiitwacho 'Kucheka ni Muhimu', nadhani muda si mrefu mhakato wake wa kukitoa utafanyika na kuwapa burudani Watanzania," alisema. Aliongeza mbali na kitabu hicho pia ameshaandika vitabu vingine viwili kimoja kiitwacho 'Kilimanjaro Band' ambacho kitakuwa maalum kwa ajili ya kuzungumzia historia ya bendi hiyo ilitoka, ilipo na inapoenda pamoja na wasifu wa wanamuziki wake. "Kitabu kingine cha tatu ni cha 'Haki Miliki'. Nimeamua kuandika hiki kwa nia ya kuwazindua wasanii kufahamu haki zao katika miliki ya kazi zao," alisema mkongwe huo. Kitime anakuwa mwanamuziki wa pili mkongwe kujitosa kwenye fani ya uandishi vitabu, baada ya Tshimanga Kalala Assosa, aliyetunga kitabu cha 'Jifunze Lingala' ambacho kinaendelea kutamba sokoni kwa sasa huku akiandaa kingine cha wasifu wake.

Nassib, Majia kuwania ubingwa wa TPBO

MABONDIA machachari wa ngumi za kulipwa nchini, Nassib Ramadhani na Fadhili Majia wanatarajiwa kupanda ulingoni Juni 9 kuwania taji la taifa la Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBO). Pambano hilo la uzani wa Super Fly (kilo 52) litafanyika kwenye ukumbi wa Friend's Corner, Manzese na litasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi. Rais wa TPBO, Yasin Abdallah 'Ustaadh', aliiambia MICHARAZO jana kuwa pambano hilo limeandaliwa na promota Kaike Siraju na kwamba maandalizi yanaendelea vema. Ustaadh alisema tayari mabondia wote wanaendelea kujifua tayari kwa pambano hilo litakalokuwa la raundi 10 ambapo siku moja ya kupanda ulingoni watapimwa afya na uzito wao. "Mabondia wetu mahiri kabisa nchini, Nassib Ramadhani na Fadhili Majia wanatarajiwa kupigana kuwania ubingwa wa TPBO uzani wa Super Fly, litakalofanyika siku ya Jumamosi kwenye ukumbi wa Friend's Corner," alisema. Katika kuzuia vitendo vyovyote vya kihuni, Ustaadh alisema TPBO imejipanga kuhakikisha ulinzi madhubuti katika pambano hilo kwa kuanza kuwasiliana na mkuu wa polisi kituo cha urafiki ili kuwasaidia siku hiyo. "Tayari tumeshamuandikia barua mkuu wa kituo cha Polisi cha Urafiki, Afande Paparika, ili kutupa ulinzi wa kutosha siku ya pambano," alisema. Ustaadh alisema imani yake pambano hilo litawasisimua wengi kutokana na upinzani mkali uliopo baina ya mabondia hao na wale watakapambana katika michezo ya utangulizi siku hiyo na kuwataka mashabiki kujitokeza kwa wingi.

Bibi Cheka, Dogo Aslay kutambulishwa Kanda ya Ziwa

WASANII wanaokuja juu katika muziki wa kizazi kipya nchini, Asilahi Is'haka 'Dogo Aslay' na Cheka Hija a.k.a 'Bibi Cheka' wanatarajiwa kwenda kutambulishwa rasmi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa wakisindikizwa na wasanii kibao nyota. Meneja wa wasanii hao, Said Hassani 'Mkubwa Fella' aliiambia MICHARAZO kwamba wasanii hao wataenda kutambuliwa katika mikoa ya Mwanza na Mara katika maonyesho yatakayofanyika mwishoni mwa wiki hii. Fella alisema wasanii watakaoenda kuwasindikiza Bibi Cheka anayetamba na wimbo wake wa 'Ni Wewe' alioimba na Mheshimiwa Temba, na Dogo Aslay aliyeachia ngoma mpya ya 'Umbea', ni pamoja na Ferooz, Easy Man, kundi la TMK Wanaume Family na wengine. "Mkubwa tunatarajia kwenda mikoa ya Kanda ya Ziwa kwa ajili ya maonyesho maalum ya kuwatambulisha Dogo Aslay na Bibi Cheka, shoo hizo zitakuwa tatu mfululizo zikianza Juni 8 mpaka 10 na watasindikizwa na 'vichwa' kibao," alisema Fella. Aliongeza kuwa maonyesho yao mawili ya awali yatafanyika jijini Mwanza kabla ya kumalizia burudani yao mkoani Mara na iwapo watapata fursa zaidi wanaweza kuhamishia utambulisho huo mkoani Shinyanga kabla ya kurejea Dar es Salaam. Alisema mbali na 'Ni Wewe', Bibi Cheka msanii wa muziki wa kizazi kipya mwenye umri mkubwa kuliko wote nchini, atatambulisha wimbo wake mwingine mpya aliouimba kwa kushirikiana tena na Mheshimiwa Temba uitwao 'Mario'.

Warembo Miss Bagamoyo kusaka vipaji J'pili Dar

WAREMBO tisa wanaojiandaa na shindano la urembo la 'Redd's Miss Bagamoyo 2012' wanatarajiwa kuonyeshana kazi katika mchuano wa kusaka kipaji 'Miss Talent' Jumapili ijayo. Mratibu wa shindano hilo, Awetu Salim, alisema shindano hilo la vipaji litafanyika kwenye ukumbi wa Club Masai, Kinondoni kabla ya warembo hao kuelekea mjini Bagamoyo kuwania taji la urembo la mji huo litakalofanyika Juni 15. Alisema warembo hao wanaoendelea na mazoezi kwenye ukumbi wa Club Masai chini ya mkufunzi wao, Sadah Salim wameanza kutambiana kila mmoja akidai ana kipaji kitakachompa ushindi kabla ya kwenda kutwaa taji la urembo. "Warembo wetu wanaendelea vizuri na mazoezi yetu na Jumapili wanatarajia kuchuana kwenye shindano la vipaji, litakalofanyikia kwenye ukumbi wa Club Masai na siku chache baadae wataelekea Bagamoyo kuwania taji la urembo litakalofanyika Juni 15 kwenye ukumbi wa TaSUBA," alisema. Awetu aliwataja warembo hao kuwa ni Zuhura Abdallah, Veronica James, Rose Lucas, Beatrice Bahaya, Diana Exavery, Nancy, Flora, Yvonne Steven na Celline Wangusu. Aidha, Awetu alishukuru kuongezeka kwa wadhamini zaidi katika shindano lao ambapo aliitaja kiwanda cha mvinyo cha Dodoma Wines kuwa ni miongoni mwa wadhamini wapya waliojitosa kuwapiga tafu. Mratibu huyo aliongeza kuwa upande wa burudani katika shindano lao watapambwa na bendi ya African Stars 'Twanga Pepeta' na mshehereshaji wa shughuli hiyo anatarajiwa kuwa Khadija Shaibu 'Dida wa G'.

Aurora afariki, azikwa Dar atakumbukwa kwa mengi

MDAU wa michezo na burudani hapa nchini, Ally Suleiman 'Aurora' amefariki usiku wa kuamkia juzi na kuzikwa jana kwenye makaburi ya Kisutu jijini Dar es Salaam. Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana ilieleza kwamba Aurora alifikwa na mauti baada ya kuugua kwa muda mrefu na kulazwa kwenye hospital ya Muhimbili. Enzi za uhai wake Aurora aliweza kufadhili mashindano ya urembo, sambamba na michezo mbalimbali ikiwamo ngumi. Miongoni mwa mabondia waliofanikiwa kwa msaada wa Aurora ni bingwa wa Afrika Mashariki na Kati, Awadh Tamim ambaye alisaidiwa na Aurora kutimiza ndoto hizo. Mbali na Tamim, Aurora aliweza kuisadia timu ya waandishi wa Habari za Michezo nchini 'Taswa FC' katika kufanikisha kufanya vizuri katika mashindano mbalimbali ikiwamo yale ya Media Bonanza yanayofanyika kila mwaka mkoani Arusha. Pia alikuwa akitajwa kama mmoja wa wafadhili wakubwa wa Coastal Union, hivyo kifo chake ni pigo kwa wadau wengi wa michezo na burudani. Mungu Ailaze Roho ya Marehemu Mahali Pema PEPONI Amiin

Monday, June 4, 2012

Kitale: 'Teja' la kwenye runinga lisiloujua 'unga'

KWA jinsi anavyoigiza na muonekano wake kama 'teja' katika baadhi ya kazi zake za filamu za kawaida na vichekesho, ni vigumu kuamini kuwa msanii Mussa Yusuph 'Kitale Rais wa Mateja' sio mtumiaji wa dawa za kulevya. Mwenyewe anadai hatumii kilevi cha aina yoyote zaidi ya kuigiza tu kama muathirika wa dawa hizo haramu za kulevya. Msanii huyo aliyewahi kutamba na makundi ya Kaole Sanaa na Fukuro Arts Professional, alisema watu wachache wanaoamini kama kweli hatumii kilevi. "Situmii kilevi chochote, sio pombe wala bangi, naigiza tu we mwenyewe unaniona bonge la HB au vipi?" Kitale alisema kwa utani alipohojiawa. Kitale alidokeza chanzo cha yeye kupenda kuigiza kama 'teja' aliyeathiriwa na 'unga' kiasi cha kuwa kibaka ni uzoefu alioupata kwa kuishi karibu na 'mateja'. Kitale, alisema jirani na kwao na sehemu kubwa ya Mwananyamala wapo vijana walioathiriwa na dawa hizo za kulevya, hivyo alikuwa akiwachunguza jinsi wanavyoongea, kutembea na maisha yao kwa ujumla na kujifunza mengi. "We unajua Mwananyamala na maeneo mengi ya uswazi kuna mateja wengi na bahati nzuri karibu na home kuna maskani yao ndio walionisaidia kunifanya niigize kama teja la kutupwa," alisema. Alisema mbali na uigizaji huo kuwa kama 'nembo' yake, lengo lake ni kuishtua jamii jinsi ya kuthibiti tatizo la dawa za kulevya, linaloteketeza kizazi na nguvu kazi ya taifa. "Naigiza hivyo, ili kuizindua jamii na kukabiliana na tatizo la dawa za kulevya, dawa hizi zimekuwa zikiharibu na kupoteza nguvu kazi kwa jinsi zinavyoathiri na kuwa na madhara makubwa kwa taifa letu," alisema. Alisema japo wanaibuka wasanii wanaoigiza kama yeye (Kitale), msanii huyo alidai hana hofu kwa kutambua ataendelea kubaki kuwa Kitale na kamwe hajishughulishi na wasanii hao wanaoiga 'nembo' yake. "Kwa kweli wapo baadhi ya wasanii wameanza kuiga uigizaji wangu, ila sina hofu na wala muda wa kuwajadili, mie naendelea kupiga kazi kwani naamini nitaendelea kubaki kuwa Kitale aliye mmoja tu yaani Rais wa Mateja," alisema. Kitale, aliyeanzia sanaa tangu akiwa kinda wakati akisoma Shule ya Msingi, alisema licha ya umaarufu mkubwa alioupata kwa namna ya uigizaji huo wa kama 'teja' hasa alipong'ara katika tamthilia ya 'Jumba la Dhahabu', alidai wakati mwingine hupata usumbufu. "Ukiacha watu kunishangaa, wapo wengine hudhani uigizaji wangu ni uhalisia wa maisha yangu hivyo huniogopa wakidhani ni teja na kibaka, ingawa huwa naamini ujumbe nilioukusidia umefika kwa jamii," alisema. VIPAJI KIBAO Kitale, mchumba wa Fatuma Salum na baba wa mtoto mwenye umri wa miaka karibu miwili aitwae Ahmed, licha ya kuigiza pia ni mahiri kwa utunzi na utayarishaji wa filamu sambamba na akiimba muziki wa kizazi kipya. Kwa sasa mkali huyo anatamba na wimbo uitwao 'Hili Dude Noma' alioimba na kaka yake Mide Zo na Corner, kikiwa ni kibao cha pili kwake baada ya 'Chuma cha Reli' alichokitoa mwaka jana akiimba na mchekeshaji wenzake, Gondo Msambaa. Msanii huyo alisema kwa sasa anaendelea kumalizia kazi yake ya mwisho kabla ya kuhitimisha albamu itakayokuwa na nyimbo nane akizitaja zilizokamilisha kuwa ni 'Anajifanya Msela' alioimba na Juma Nature, 'Hili Toto' ft. Sharo Milionea na Mide Zo, 'Tulianzishe' na 'Kinaunau'. "Nimebakisha wimbo mmoja tu ambao nimeshautunga na kuufanyia mazoezi ila nasubiri kuafikiana na mmoja wa wasanii nyota nchini ili niurekodi," alisema. Hata hivyo Kitale alikiri kuwa, licha ya umaarufu mkubwa aliopata katika uigizaji, bado haridhiki na masilhai anayopata katika fani hiyo akidai hailipi kama ilivyo kwa muziki. Alisema, uigizaji haulipi kama muziki, lakini bado hana mpango wa kuachana na fani hiyo. "Kwenye uigizaji tunaambulia sifa tu, ila masilahi ni madogo mno tofauti na muziki, hata hivyo siwezi kuachana na fani hii kwani nimeshaizoea, na kwa sasa najiandaa kutoa kazi mpya nikishirikiana na Sharo Milionea," alisema. Alizitaja kazi hizo mpya ni; 'Sharo Madimpoz', 'Sharo Crazy', 'Sharo Taxi Driver' na 'Drug Dealer' wanazoziandaa na msanii mwenzake. Kitale alisema hizo ni baadhi ya filamu walizopanga kuzitoa ndani ya mwaka huu, sambamba na kuendelea na masuala ya muziki akidai kila mmoja imekuwa ikimpa mafanikio makubwa. FILAMU Kitale aliyezaliwa miaka kadhaa iliyopita mjini Morogoro ni shabiki mkubwa wa soka, mchezo aliowahi kucheza utotoni kabla ya kutumbukia kwenye uigizaji, akizitaka timu anazoshabikia kuwa ni Yanga na Manchester City. "Aisee katika soka huniambii kitu, licha ya kulicheza pia ni mnazi mkubwa wa Yanga na naipenda mno Manchester City," alisema. Kitale anayependa kula ugali kwa dagaa na kunywa vinywaji laini, alisema mbali na kucheza 'Jumba la Dhahabu' iliyompa umaarufu mkubwa, ameigiza pia filamu kama 30 na kushiriki kipindi cha vichekesho cha 'Vituko Show'. Alizitaja baadhi ya kazi hizo kuwa ni 'Back from Prisons', 'Mtoto wa Mama', 'Alosto', Mbwembwe', 'More than Lion' aliomshirikisha msanii wa muziki wa kizazi kipya wa kundi la Tip Top Connection, Abdulaziz Chende 'Dogo Janja'. Kitale, anayemzimia King Majuto aliyeigiza naye baadhi ya kazi, alisema fani ya sanaa nchini imepiga hatua kubwa, isipokuwa inakwamishwa na wajanja wachache wanaowanyonya wasanii na kuwafanya wasinufaike na fani hiyo. Alisema ni vema juhudi za kupambana na maharamia ikaongezwa, ili wasanii wa Bongo wanufaike na jasho lao na kuishi kama wasanii wa mataifa mengine ambao ni matajiri kuliko hata watu wa kada zingine. Kitale, anayefurahishwa na tukio la kuzaliwa kwa mwanae, akihuzunishwa na kifo cha mjomba wake aliyekufa kwa ajali ya gari, alisema matarajio yake ni kumuomba Mungu ampe umri mrefu na afya njema afike mbali kisanii. Alisema angependa kujikita zaidi katika muziki na kutoa kazi zake binafsi za filamu ili kunufaika na jasho lake baada ya kutumikia watu wengine bila kunufaika zaidi ya kuambulia sifa tu.

Drogba aimwagia sifa Taifa Stars, achekelea kuwatungua

NAHODHA wa timu ya taifa ya Ivory Coast, Didier Drogba, ameisifu timu ya Tanzania kwamba iliwapa wakati mgumu sana katika mechi yao ya raundi ya awali ya kufuzu kwa Kombe la Dunia 2014 kwenye Uwanja wa Felix Houphouet Boigny mjini Abidjan Jumamosi. "Ilikuwa ni mechi ngumu sana, lakini jambo la muhimu ni kwamba tumepata pointi tatu," alisema Drogba baada ya mechi hiyo ambayo wenyeji walishinda 2-0. "Kocha alikuwa na siku tatu za kuwa pamoja nasi, lakini tumeshinda mechi hivyo ni kazi nzuri kwake. Sasa tuna muda wa kufanya kazi pamoja naye na kujaribu kuboresha tulichofanya. Tutajiandaa na mechi ijayo dhidi ya Morocco kisha tuone nini kitatokea." Ivory Coast ilimfukuza kocha wake, Francois Zahoui na kumpa nafasi hiyo nyota wa zamani wa timu ya taifa ya Ufaransa, Sabri Lamouchi, siku tatu kabla ya mechi dhidi ya Stars. Ushindi unaifanya Ivory Coast kuongoza Kundi C la kuwania kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za Brazil 2014 ikiwa na pointi tatu baada ya Gambia na Morocco kutoka sare ya 1-1 katika mechi nyingine ya kundi hilo na kuzifanya kuwa na pointi moja kila moja baada ya mechi hiyo moja. Tanzania imeanza kwa kushika mkia ikiwa haina pointi. Baada ya kuanza vibaya, Stars imedhamiria kumalizia hasira zao kwa ushindi katika mechi yao ya pili dhidi ya Gambia Jumapili 10 jijini Dar es Salaam. Stars haijaonekana kurudishwa nyuma na kipigo kutoka kwa miamba hao wa Afrika na badala yake kikosi kilianza mazoezi jana asubuhi kwenye uwanja wa Shirikisho la Mpira wa Miguu la Ivory Coast (FIF) ambao uko pembezoni mwa jiji la Abidjan. Timu hiyo ilitarajia pia kutafanya tena mazoezi leo asubuhi asubuhi kabla ya kuanza safari ya kurejea nyumbani saa 1:30 usiku kwa ndege ya Kenya Airways kupitia Nairobi ambapo itawasili Dar es Salaam kesho saa 1:40 asubuhi. Kocha Kim ambaye amekuja na wachezaji wote hapa ukiondoa wanne ambao ni majeruhi (Thomas Ulimwengu, Nurdin Bakari, Haruna Moshi na Nassoro Masoud Cholo) amesema hivi sasa wameelekeza akili yao kwenye mechi ijayo dhidi ya Gambia. “Safari ya kujenga timu ndiyo imeanza. Mechi dhidi ya Ivory Coast imepita na ninawashukuru wachezaji kwa kucheza kwa mujibu wa maelekezo na kujituma. Mpira ni mchezo wa makosa, tumefanya makosa yaliyosababisha tuwape Ivory Coast mabao mepesi," alisema kocha wa Stars, Kim Poulsen. “Lakini kama nilivyosema mechi hiyo imepita, hivi sasa tunaangalia mechi ijayo dhidi ya Gambia. Hatuna muda mwingine wa kujipanga na ndio maana niliamua kuja na wachezaji wote Abidjan,” amesema Kim. Mechi dhidi ya Gambia itachezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 jioni. Gambia ilitoka sare ya bao 1-1 na Morocco katika mechi iliyochezwa juzi jijini Banjul. Stars itamkosa nahodha msaidizi Aggrey Morris ambaye alitolewa kwa kadi ya pili ya njano dakika ya 65 baada ya baada ya kumkwatua mchezaji wa Ivory Coast, Gosso Gosso. Morris alipewa njano ya kwanza katika dakika ya 12 baada ya kumkwatua Didier Drogba. Vikosi katika mechi hiyo vilikuwa; Ivory Coast: Boubacary Barry, Kolo Toure, Siaka Tiene, I. Lolo, Emmanuel Eboue, Cheik Tiote/Ya Konan, K. Coulibaly, Jean Gosso Gosso, Didier Drogba, Salomon Kalou/Max Gardel na Gervinho/Kader Keita. Tanzania; Juma Kaseja, Aggrey Morris, Kelvin Yondani, Amir Maftah, Shomari Kapombe, Mrisho Ngassa, Shaban Nditi, Mwinyi Kazimoto, Salum Abubakar/ John Bocco, Mbwana Samatta na Frank Domayo. CHANZO:NIPASHE

Wazee wa Ngwasuma kutumbuiza Miss Kigamboni

BENDI ya muziki wa dansi ya FM Academia maarufu kama 'Wazee wa Ngwasuma' na msanii wa vichekesho, Mpoki, wataburudisha wakati wa shindano la kumsaka mrembo kitongoji cha Kigamboni City 2012 litakalofanyika Juni 15 katika ukumbi wa Navy Beach, Kigamboni jijini Dar es Salaam. Mratibu wa shindano hilo, Somoe Ng'itu alisema kutakuwa na ushindani mkubwa katika shindano hilo kutokana na vimwana wakali waliopo kambini na bendi ya FM inafahamika kwa kutoa burudani nzuri kwa mashabiki wa muziki wa dansi nchini. Somoe alisema kuwa burudani nyingine kali itatoka kwa Mpoki ambaye mbali ya kuwa ni mkazi wa Kigamboni, lakini ukubwa wa kazi yake unafahamika na kwamba mashabiki watapaswa kuandaa mbavu za ziada kutokana na vichekesho vyake. Mratibu huyo kutoka kampuni ya K& L, alisema kuwa jumla ya warembo 15 wanaendelea kujifua katika kambi ya mazoezi chini ya mwalimu wao Miss Temeke, Hawa Ismail, ambaye anashirikiana na mshiriki wa Miss Tanzania mwaka jana Blessing Ngowi. Aliwataja warembo hao kuwa ni pamoja na Carolyne Dandu, Fatina Francis, Edda Slyvester, Aisha Mussa, Rosemary Peter, Doreen Kweka, Caroline Peter, Agnes Goodluck, Sophia Martine, Rosemary Deogratius, Beatrice Boniface, Julieth Philip na Khadija Kombo. "Kigamboni ni zaidi ya kitongoji, tunaamini shindano letu litakuwa na mvuto na hadhi ya kipekee kama eneo lake lilivyo," aliongeza. Somoe alisema kuwa warembo watakaofanya vizuri watapata nafasi ya kuwakilisha kitongoji hicho katika mashindano ya kanda ambayo yatafanyika baadaye mwaka huu. Aliwataja wadhamini ambao tayari wamethibitisha kuwezesha shindano hilo kuwa ni pamoja na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chake cha Redd's, Dodoma Wine na NSSF, Hope Country Motel, Norbro’s Collections, Screen Masters, Global Publishers. Salha Israel kutoka Kanda ya Ilala ndiye mrembo anayeshikilia taji la taifa ambapo mwaka huu ratiba ya mashindano hayo imebadilika. CHANZO:NIPASHE Warembo watakaochuana kwenye shindano la Miss Kigamboni 2012

Masai Nyota Mbofu aachia Rungu na Mukuki

MCHEKESHAJI maarufu nchini, Gilliad Severine 'Masai Nyota Mbofu', ameachia wimbo mpya uitwao 'Rungu na Mukuki' sambamba na video yake akishirikiana na wasanii wa kundi la Vichwa la Zambia, Simple K na G4. Tayari wimbo na video hiyo imeshaanza kurushwa hewani wakati mwenyewe akijiandaa kupakua kazi nyingine mpya. Akizungumza na MICHARAZO, Masai Nyota Mbofu, alisema wimbo huo ameurekodia nchini Zambia katika studio za Hez Sound chini ya Prodyuza, Acknex na video yake amefyatulia nchini humo na kuja kuimalizia Tanzania. Msanii huyo, alisema kazi hiyo mpya ni salamu kwa mashabiki wake waliomzoea kumuona katika filamu na komedi tu, kwamba kwenye muziki naye yumo. Masai Nyota Mbofu, alisema wakati wimbo na video hiyo ikiendelea kutamba ameanza kuandaa wimbo mipango ya kutoa kazi nyingine kwa lengo la kuja kufyatua albamu hapo baadae. "Wakati Rungu na Mukuki, ikiendelea kukimbiza kwa fideo na radio, tayari nimenza kuandaa kazi nyingine nataka onyesha mashabiki angu kwamba mi nawesa," alisema Masai kwa kiswahili kibovu cha kikomedi. Mkali huyo aliyeanza kutamba kwenye michezo ya runinga akiwa na kikundi cha Jakaya Theatre kabla ya kuibukia kwenye filamu chini ya kampuni ya Al Riyamy Production. Baadhi ya kazi zilizowahi kumpa ujiko msanii huyo ni Iny'e Plus, 'Iny'e Gwedegwede', 'Vumba Vimejaa', 'Pedeshee' na sasa anatamba na kipindi cha Vituko Show.

Mosha awachomolea wazee Yanga, fomu zachangamkiwa

HUKU zoezi la uchukuaji fomu za kuwania uongozi kwa ajili ya Uchaguzi wa klabu ya Yanga ukizidi kupambamoto, aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo Davis Mosha amewachomolea wazee wa Yanga waliomtaka awanie tena uongozi akidai hana mpango huo. Aidha, kamati ya uchaguzi imekanusha taarifa kwamba Mfadhili Mkuu wa klabu huyo, Yusuf Manji amejityosa kuchukua fomu za kuwania Uenyekiti, ingawa kamati hiyo imesema milango i wazi kwake kama ana dhamira hiyo ya kuwania uongozi Yanga katika uchaguzi utakaofanyika Julai 15. Mosha, aliyefuatwa na wazee hadi nyumbani kwake Mikocheni juzi jijini Dar es Salaam, akijibu maombi ya baraza wazee lililomuomba kugombea moja ya nafasi katika uchaguzi huo na kusema hana mpango wa kuwania uongozi. Alisema kwa sasa hayuko tayari kugombea uongozi katika klabu lakini yupo tayari kusaidia kitu chochote kinachohitajika kwa maendeleo ya klabu. “NAwashukuru wazee kwa kuja kuniaona na kunipa pole, pia nashukuru kwa kuona umuhimu wa mimi kuwepo Yanga, ila napenda niwaeleze sintoweza kuwania uongozi kwa sasa, bali nipo tayari kuisaidia Yanga kwa lolote litakalokuwa ndani ya uwezo wangu,”alisema. “Mimi ni mpiganaji kweli, naiopenda Yanga na napenda iwe na maendeleo…nitashirikiana na viongozi watakaochaguliwa lakini mimi siwezi kuongoza Yanga kwa sasa nina mambo mengi ya kufganya,”alisema Mosha ambaye alijitoa madarakani miezi michache kabla iongeza kuwa wanachama wa Yanga hawana budi kuchagua viongozi ambao wapo tayari kuisaidia klabu hiyo na si kupata chochote. “Napenda kuwahadharisha wanachama wenzangu nkwamba tusikurupuke, tutafute watu wenye mapenzi ya kweli na si maslahi kwani Yanga ni kwa ajili ya kutumika si kuvuna,”alisema. Awali Katibu wa baraza hilo Ibrahim Akilimali ‘Abramovich’ kwa niaba ya wazee wengine wa Yanga ambao walikwenda nyumbani kwa Mosha kwa ajili ya kumpa pole kutokana na kufiwa na Mkwewe, aliwasilisha ombi la kumtaka Mosha kurejea kundini. Mzee Akilimali alisema kuwa wameamua kumuomba Mosha arejee kuongoza Yanga kutokana na umahiri mkubwa aliouonesha kipindi alichoongoza ambapo alikuwa mstari wa mbele kuisaidia timu hiyo na hatimaye kwa kipindi kifupi iliweza kupata mafanikio. “Mwanetu sisi wazee wako tumekuja kukupa pole lakini pamoja na hilo tunakuomba urejee kuongoza kwani bado tunakumbuka ushupavu wako katika kuongoza…kuna kombe la Kagame linakuja ambalo wewe ulichangia kwa kiasi kikubwa kupatikana, sasa uje ulibakize tena kombe hilo,”alisema Mzee Akilimali. Aidha , Mzee Akilimali aliongeza kuwa wanataka Yanga iingie kwenye mashindano na kushiriki hivyo mchango wa Mosha katika hilo ni muhimu sana. Uuchaguzi huo utajaza nafasi za viongozi waliojiuzulu na ile ya mjumbe mmoja aliyefariki dunia, ambapo viongozi watakaochaguliwa watakaa madarakani kwa muda uliosalia kama katiba inavyoelekeza na kwa mantiki hiyo viongozi hao watamaliza muda wao wa miaka minne mwaka 2014. Uchaguzi huo unafuatia kujiuzulu kwa aliyekuwa Mwenyekiti Lloyd Nchunga baada ya kushinikizwa na baadhi ya wanachama wakiongozwa na baraza la wazee wa klabu hiyo kutokana na kushindwa kuiletea mafanikio klabu hiyo chini ya uongozi wake. Pia nafasi ya Makamu mwenyekiti iliyokuwa inashikiliwa na Davis Mosha ambaye alijitoa miezi michache baada ya kuchaguliwa kutokana na kutoelewana na Nchunga, huku mjumbe Theonest Rutashoborwa akitangulia mbele ya haki. Uchaguzi huo pia utajaza nafasi za Wajumbe walioachia ngazi ambao ni pamoja na Mzee Yusuf, Charles Mgondo na Ally Mayay. Kwa sasa Yanga imebaki na wajumbe wanne, Mohammed Bhinda, Sarah Ramadhan, Tito Osoro na Salum Rupia ambao baada ya uchaguzi wataungana na viongozi wapya na kuteua wajumbe wengine watatu kwa mujibu wa katiba, hiyo inatokana na wajumbe hao wa kuteuliwa Seif Ahmed, Mbaraka Igangula na Pascal Kihanga kujiuzulu. Katika hatua nyingine, wagombea watatu walijitokeza kuchukua fomu za kuwanmia nafasi ya ujumbe katika, wanachama hao ni pamoja na Jumanne Mwamamwenye na Salehe Hassan na Ayoub Nyenzi anayewania nafasi ya Makamu Mwenyekiti. Huku kamati ya uchaguzi ikikanusha taarifa kwamba Manji naye amejitosa kuchukua fomu kuwania Uenyekiti wa klabu hiyo, ingawa umesema milango i wazi kwake na kwa yeyote mwenye sifa kabla ya zoezi la kuchukua na kurudisha fomu kufungwa rasmi Jumatano jioni.

Simba noma, yabebe mzigo wa matibabu ya akina Boban

UONGOZI wa klabu ya Simba umesema kuwa umechukua jukumu la kuwatibu wachezaji wake Haruna Moshi 'Boban' na Nasoro Masoud 'Cholo' walioumia wakiwa na kikosi cha timu ya taifa 'Taifa Stars' baada ya kukatishwa tamaa na kusuasua kwa shirikisho la soka (TFF) kubeba gharama hizo. Akizungumza jijini Dar, Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala alisema kuwa klabu yake haina muda wa kusubiri matibabu ya TFF kwa wachezaji hao kwasababu ya kuzongwa na kalenda ya mashindano. Simba imeanza maandalizi kwa ajili ya mashindano ya klabu bingwa ya Afrika Mashariki na Kati hivyo haiwezi kusubiri mpaka TFF liwatibie 'Boban' na 'Cholo'. Kauli hiyo ya Mtawala imekuja siku moja baada ya katibu mkuu wa TFF, Angetile Osiah, kusema bila kutaja tareeh rasmi kuwa shirikisho litafanya jitihada za kuwatibu wachezaji hao walioumia wakiwa ndani ya kikosi cha Stars. "Sisi ndio tunawalipa mshahara wachezaji hawa, na mtu akigundulika ameumia anatakiwa kutibiwa haraka na hakuna kusubiri," alisema. "Tumeanza kuwatibu ili kocha wetu atakaporudi awakute wachezaji katika hali nzuri na kuendelea na programu zake za mazoezi." Kocha wa timu hiyo Mserbia Milovan Cirkovic atarejea nchini Juni 15, alisema. Kocha huyo ametuma programu ya mazoezi kwa ajili ya maandalizi ya Kombe la Kagame ambayo kwa sasa yanasimamiwa na kocha wa makipa wa timu hiyo James Kisaka. "Timu imeanza maandalizi chini ya Kisaka (James) kwa sababu kocha msaidizi naye ameenda mapumzikoni nchini kwao," alisema zaidi Mtawala. Alisema kocha msaidizi Richard Amatre ataungana na timu Alhamisi baada ya kuwasili nchini Jumatano. Mtawala alisema klabu hiyo imeweka malengo ya kutwaa ubingwa wa Kagame ambao unashikiliwa na watani zao Yanga walioutwaa kwenye mashindano ya mwaka jana kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kuifunga Simba goli 1-0.

Noela ndiye Miss Tabata 2012

MREMBO Noela Michael, 19, usiku wa kuamkia juzi alifanikiwa kutwaa taji la Tabata 'Miss Tabata 2012' katika shindano lililofanyika kwenye ukumbi wa Da’ West Park jijini Dar es Salaam. Noela ambaye awali alibwagwa katika kuwania taji la talent aliweza kuwafunika warembo wengine 18 waliokuwa wanawania taji hilo lililokuwa linashikiwa na Faiza Ally. Noela alizawadiwa shilingi 500,000 na king’amuzi iliyolipiwa miezi sita iliyotolewa na Multichoice. Nafasi ya pili katika shindano hilo ilishikwa na Diana Simon, 20, aliyeshinda Sh 500,000 watatu ni Wilhemina Mvungi, 21, (Sh 350,000), wanne ni Phillos Lemi, 19, na Suzzane Deodatus, 20, alishika nafasi ya tano. Wote wawili walizawadiwa Sh 200,000 kila moja. Warembo hao watano watakiwakilisha Tabata katika mashindano ya Kanda ya Ilala yatakayofanyika baadaye mwaka huu. Warembo wengine waliofanikiwa kuingia hatua ya 10 walikuwa ni Angel Kisanga, Khadija Nurdin, Haika Joseph, Queen Issa na Neema Saleh. Wote walizawadiwa Sh 100,000 kila moja. Queen Issa alifanikiwa kutwaa taji la mrembo mwenye kipaji cha kucheza huku Mercy Mlay akiteuliwa kuwa mrembo aliyekuwa na nidhamu ya juu tangu kuanza kwa shindano hilo. Queen na Mercy kila moja alizawadiwa Sh 100,000. Warembo waliosalia walipata kifuta jasho cha Sh 50,000 kila moja. Shindano hilo lilipambwa na burudani kutoka kwa bendi ya Mashujaa, Mashauzi Classic iliyoko chini ya Isha Ramadhani Mfalme na Costa Sibuka. PICHA Tofauti za matukio ya Miss Tabata 2012, ambapo Noela Michael aliibuka kidedea.

Saturday, June 2, 2012

Mr Blue, Malaki wachanganywa na Msichana Mzuri

Malaki MSANII anayekuja kwa kasi nchini, Sela Myovela 'Malaki' ameachia ngoma mpya iitwayo 'Msichana Mzuri' aliyoimba akishirikiana na mkali wa R&B, Khery Sameer Rajab maarufu kama Mr Blue au 'Kabaysa'. Akizungumza na MICHARAZO, Malaki aliyewahi kufyatua ngoma nyingine kali iitwao 'Maisha' aliyoimba na mkali wa Bongofleva nchini, Juma Kassim Kiroboto 'Sir Juma Nature' alisema wimbo huo mpya ameurekodia katika studio za Fishcrab chini ya prodyuza matata, Lamar. Malaki alisema wimbo huo uliopo katika miondoko ya R&B ni maalum ya ujio wake mpya chini ya usimamizi wa kaka yake, Mfaiswa Myovela 'Mzee wa FilamuCentral'. "Baada ya kimya kirefu cha miaka kama mitano, nimekuja na ngoma mpya kabisa iitwayo 'Msichana Mzuri' niliyopigwa tafu na Mr Blue, ikifanywa chini ya Lamar wa Fishcrabs Studio," alisema. Alisema, tayari wimbo huo ameshausambaza katika vituo vya redio na kuanza kurushwa hewani, huku mwenyewe nakijipanga kwa ajili ya kuitolea video yake. Aliongeza, lengo lake ni kufyatua albamu hapo baadae ingawa alisema kwa sasa ataendelea kudondosha wimbo mmoja mmoja kwa ajili ya kuweza kujitangaza na kupata shoo zitakazomwezesha kupata fedha za kukamilishia albamu hiyo. Malaki alitumbukia kwenye muziki wa kizazi kipya tangu mwaka 2005 na kutoa kazi yake ya kwanza kabisa akiwa na Juma Nature mwaka 2007 kabla ya kuwa kimya hadi mwaka huu alipotoka na 'ngoma' hiyo mpya.
Mr Blue katika pozi zake.

'Maafande' wamnyemelea Ngassa

KLABU nne tofauti zimekuwa zikimnyatia mshambuliaji mahiri wa timu ya Moro United, Benedict Ngassa, kwa ajili ya kutaka kumnasa ili wazichezee timu zao katika msimu moya wa Ligi Kuu Tanzania Bara. Akizungumza na MICHARAZO, Ngassa alizitaja klabu hizo zinazomnyemelea kuwa ni JKT Ruvu, Ruvu Shooting, African Lyon na timu iliyopanda daraja ya Prisons ya Mbeya. Ngassa alisema viongozi wa klabu hizo kwa nyakati tofauti wamekuwa wa kiwasiliana nae na kufanya mazungumzo ingawa alikiri bado hajaafikiana nao mpaka sasa. "Licha ya kufuatwa na viongozi wa klabu hizo, bado sijaamua niende wapi, nitaangalia kwanza masilahi," alisema. Aliongeza kuwa, ingawa anafurahia kunyatiwa na timu hizo, lakini roho yake inamuuma kwa timu yake ya Moro United kushuka daraja akielekeza lawama zake kwa wachezaji walioichezea timu hiyo kwa mkopo. Ngassa, alisema wachezaji waliotua katika timu hiyo kwa mkopo toka klabu mbalimbali nyingine za ligi kuu walikuwa wakiihujumu timu yao ambapo licha ya wachezaji halisi wa Moro kujituma na kuifungia mabao, magoli hayo yalikuwa yakirejeshwa kitatanishi. "sio siri tumeshushwa daraja na wachezaji waliokuja Moro kwa mkopo, inauma sana," alisema. Moro United iliyokuwa imerejea tena Ligi Kuu imejikuta ikishuka daraja ikiungana na timu za Villa Squad na Polisi Dodoma kutokana na kujikusanyia pointi chache katika mechi 26 ilizocheza msimu huu ambapo Simba waliibuka mabingwa.

Bondia Magoma Shaaban afariki, azikwa kwao Tanga

ALIYEKUWA Bingwa wa Dunia wa WBU uzani wa Super Fly, Magoma Shaaban amefariki dunia na kuzikwa kwao mkoani Tanga. Kwa mujibu wa mdau mkubwa wa mchezo wa ngumi ambaye pia ni promota, Ibrahim Kamwe, Magoma alikumbwa na umauti juzi kwenye hospitali ya Bombo mkoani Tanga. Magoma alikuwa amelazwa katika hospitali hiyo siku nne zilizopita kutokana na kuzidiwa na maradhi aliyokuwa nayo siku nyingi na kufariki majira ya jioni na alizikwa jana nyumbani kwao Mabovu Mwembesamaki, mjini Tanga. Marehemu aliyeacha mjane na watoto wawili Sudi,10 na Almasi,7 alizaliwa Oktoba 21, 1980 mjini Tanga na alianza kucheza ngumi tangu akiwa kinda akipitia klabu mbalimbali za ngumi za ridhaa kabla ya kuingia za kulipwa mwaka 1996 alipopanda ulingoni kuzipiga na Athumani Omari na kushinda kwa pointi. Hadi mauti yanamkuta bondia huyo aliyekuwa mfupi lakini machachari, alikuwa amepigana mapambano 16 na kushinda 13 kati ya hayo mapambano manne akishinda kwa KnockOut (KO) na kupigwa matatu pia kwa KO. Mara ya mwisho kupanda ulingoni ilikuwa Julai 21 mwaka 2006 na Eugen Sorin Tanasie mjini Timisoara, Romania katika pambano ambalo alipigwa kwa Technical Knockout (TKO) raundi ya pili. Taji lake la kwanza kutwaa lilikuwa ni la IBF Afrika, Septemba 12, mwaka 1998 akimpiga Mkenya Joseph Waweru kwa KO raundi ya kwanza, Uwanja wa Mkwakwani, Tanga. Mei 11, mwaka 2000 alimpiga bondia ‘matata sana’ Totin Lukunim wa Thailand na kutwaa taji la IBF Intercontinental, uzito wa Super Fly kwenye ukumbi wa PTA, Temeke, Dar es Salaam. Agosti 3, mwaka 2001 ndipo alitwaa ubingwa wa dunia wa WBU baada ya kumpiga Ferid Ben Jeddou wa Tunisia kwa TKO raundi ya sita mjini Avezzano, Abruzzo, Italia, kabla ya kupoteza taji hilo kwa kupigwa na Gabula Vabaza Julai 26, mwaka 2002 katika ukumbi wa Hemingways Casino, East London, Eastern Cape, Afrika Kusini kwa KO raundi ya kwanza. Mei 25, mwaka 2003 alipigwa na Mtanzania mwenzake, Mbwana Matumla kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam kwa TKO raundi ya nne. Wadau mbalimbali wa ngumi wameelezwa kusikitishwa na kifo cha Magoma, wakiitaka familia, ndugu, jamaa na rafiki zake kuwa na subira katika kipindi hiki kigumu wakiwakumbusha kuwa kazi ya Mola huwa haina makosa.

Friday, June 1, 2012

Costa, Jabu, Kago watupiwa virago Simba, wanne wajaza nafasi zao

NYOTA watano wa kikosi cha Simba ambao kwa kiasi kikubwa waliisaidia timu hiyo kung'ara msimu huu wamedaiwa kutupiwa virago, huku nafasi zao zikichukuliwa na wakali wanne waliosajiliwa mpaka sasa ndani ya kikosi hicho. Habari za kuaminika ambazo zimenaswa jijini ni kwamba wachezaji walitupiwa virago ni nyota wa kimataifa toka Jamhuri wa Kati, Gervais Kago, mabeki wa kati Victor Costa na Juma Nyosso, Juma Jabu na Ulimboka Mwakingwe aliyekuwa majeruhi kwa muda mrefu. Aidha kuna taarifa nyingine kwamba naye Uhuru Seleman yupo katika mchakato pia wa kutemwa katika kikosi hicho iwapo atafanikiwa kupata timu, ikidaiwa ananyemelewa na Yanga. Kwa mujibu wa chanzo cha habari toka ndani ya Simba, ni kwamba Costa, Jabu na Kago wametemwa kwa kushuka viwango, huku Nyosso anaysakwa na Yanga pia, ametemwa kutokana na utovu wa nidhamu wa mara kwa mara anaoufanya dimbani na kuigharimu timu, huku Mwakingwe kwa umri na kuwa majeruhi wa muda mrefu. Nafasi za wachezaji hao mpaka sasa zimechukuliwa na wakali wanne walionaswa Msimbazi ambao ni Juma Abdallah, Mussa Mudde Mbongo aliyekuwa akicheza SOFAPAKA, Patrick Nkanu toka Congo na Ibrahim Rajab 'Jebba'. Viongozi wa Simba walinukuliwa jana kwamba, zoezi zima la usajili wa timu yao utaanikwa baada ya kamati zao za ufundi na mashindano kuendesha zoezi hilo kwa maelekezo ya kocha wao, Cirkovic Milovan. Zoezi la usajili nchini kwa timu za Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2012-2013 umefunguliwa rasmi leo Juni Mosi na unatarajiwa kumalizika mwanzoni mwa Julai kabla ya Ligi kuanza Agosti ambapo miongoni mwa timu zitakazoshiriki ni Polisi Moro, Mgambo Shooting ya Tanga na Prisons ya Mbeya zilizopanda daraja toka la Kwanza.

Wema Sepetu afafanua pete aliyovishwa Maisha Club

MSANII nyota wa filamu nchini, Wema Sepetu amefafanua uvumi ulioenea jijini Dar kwamba ameangukia kwenye penzi na mwanamuziki wa bendi ya Machozi, Mwinyi kiasi cha kuvishwa pete ya uchumba kama alivyofanyiwa na aliyekuwa boifrend wake, Naseeb Abdul 'Diamond' kabla ya kumwagana hivi karibuni. Wema alisema pete aliyovishwa mwishoni mwa mwezi uliopita ilikuwa ni igizo la filamu aliyokuwa akiishoot iitwayo 'Super Star' kazi binafsi anayokuja nayo ambayo sehemu kubwa inahusu maisha yake halisi. Mrembo huyo alisema wengi walishindwa kuelewa walipomuona akivishwa pete na Mwinyi na kukumbatiwa huku wakipigana mabusu kwa kuwa kamera zilizokuwa zikitumika kutengenezea filamu hiyo zilikuwa juu na hivyo hazikuonwa na watu. "Sio kweli kama nimechumbiwa na Mwinyi wa Machozi, ila tulikuwa tukiigiza filamu yangu ya kwanza binafsi iitwayo 'SUPER STAR' ambayo ni kama inazungumzia maisha yangu," alisema. Mwinyi amecheza kama Diamond katika filamu hiyo ambapo aliwahi kumvisha pete na kutamka maneno ya kusisimua kabla ya kuja kugeukana. Wema alisema filamu hiyo anatarajia kuizindua Juni 23 baada ya kukamilika na imemgharimu karibu Sh Milioni 30 mpaka sasa. Miss Tanzania huyo wa 2006 amesema filamu hiyo imewashirikisha wasanii kadhaa nyota, na anatarajia itakuwa filamu ya kusisimua kutokana na kuigiza sehemu kubwa katika uhalisi wa maisha yake kama WEMA SEPETU.

YANGA MPO? RATIBA YA UCHAGUZI WENU HII HAPA

Stars yafika salama Abidjan, kuwavaa Tembo wa Ivory Coast kesho

Kikosi cha Taifa Stars kimewasili salama mjini Abidjan mchana wa jana huku Kocha Mkuu wa timu hiyo Kim Poulsen akisema mechi dhidi ya Ivory Coast itakuwa ngumu. Kwa mujibu wa ofisa habari wa TFF Boniface WAmbura ambaye ameambatana na timu, Stars yenye wachezaji 21 ilikuwa iwasili hapa asubuhi, lakini ndege iliyobadilisha Nairobi ilichelewa kuondoka kwa saa tatu. Mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Taifa Stars na wenyeji Ivory Coast (Tembo) itachezwa Juni 2 mwaka huu Uwanja wa Felix Houphouet-Boigny kuanzia saa 11 kamili jioni ambapo Tanzania itakuwa saa 2 kamili usiku. Licha ya kwanza, Stars ililazimika kuacha wachezaji wawili dakika za mwisho (Haruna Moshi na Nassoro Cholo), Kim amesema kikosi chake ambacho kimefikia hoteli ya Ibis bado kimejipanga vizuri kwa ajili ya mechi hiyo. “Tunaiheshimu Ivory Coast kwa vile ni timu ambayo inaundwa na baadhi ya wachezaji nyota wa dunia kama akina Drogba (Didier) na Yaya (Toure), lakini wajiandaa kupata wakati mgumu kutoka kwetu,” amesema Kim ambayo kikosi chake baada ya kuwasili hapa kilipata fursa ya kufanya mazoezi jioni. Kikosi cha Stars kinaongozwa na nahodha wake Juma Kaseja akisaidiwa na Aggrey Morris. Wachezaji wengine waliopo hapa na kikosi hicho ni Mwadini Ally, Deogratius Munishi, Amir Maftah, Erasto Nyoni, Kelvin Yondani, Waziri Salum, Shomari Kapombe na Juma Nyoso. Jonas Mkude, Mwinyi Kazimoto, Salum Abubakar, Shabani Nditi, Edward Christopher, Mrisho Ngasa, Frank Domayo, Mbwana Samata, Ramadhan Singano, Simon Msuva na John Bocco. Mbali ya Kim, Benchi la Ufundi lina Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi), Juma Pondamali (Kocha wa makipa), Leopold Mukebezi (Meneja wa timu), Juma Mwankemwa (Daktari wa timu), Frank Mhonda (Physiotherapist) na Alfred Chimela (Mtunza vifaa).
Msafara wa Stars hapa unaongozwa na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Crescentius Magori lakini pia yupo Mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Dioniz Malinzi ambaye amekuja kushuhudia mechi hiyo.