STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 28, 2012

MAMA AFRIKA SARAKASI YAFANA


... ilikuwa ni maajabu na kweli.
 
Kijana mwingine alionyesha umahili wake ni huyu kama vile unavyomuona.
Michezo ya kamba nayo ilikuwa ya kuvutia.
 Mchezo mwingine ulikuwa niwa kurushiana vikapu ya kutimia miguu.
 Vijana wakionyesha uhodari wao wa kupaa juu.
 
Vijana wakiaga mara baada ya onyesho kumalizika.

FAINALI ZA MICHUANO YA SAFARI POOL MWANZA YAFUNGULIWA 


Waamuzi wa mchezo wa Pool wakiongoza maandamano ya kuingia ukumbini wakati wa ufunguzi wa mashindano ya Safari Pool Taifa yaliyofunguliwa rasmi jana katika Hoteli ya Monarch jijini Mwanza na Mkuu wa Wilya ya Ilemela, Amina Masenza.

 Meneja wa Bia ya Safari Lager, Oscar Shelukindo akizungumza na wachezaji wa Pool (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa mashindano ya Safari Pool Taifa yaliyofunguliwa rasmi na Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amina Masenza katika Hoteli ya Monarch jijini Mwanza
Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amina Masenza (wapili kulia) akifungua rasmi mashindano ya Safari Pool Taifa .Kulia ni Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Ilemela(OCD),Debora Magiligimba.Wengine kutoka kushoto ni Katibu wa chama cha Pool Mkoa wa Ilala, Mohamed Mwarabu, Mwenyekiti wa kamati ya mashindano, Haji Kapulila na Makamu mwenyekiti wa TAPA, Fred Mushi


Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Amina Masenza akizungumza na wachezaji (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa mashindano ya Safari Pool Taifa katika Hoteli ya Monarch jijini Mwanza.Kushoto ni Meneja wa Bia ya Safari Lager, Oscar Shelukindo na Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Pool Taifa, Fred Mushi.

BONDIA RAJABU MAOJA AELEKEA NAMIBIA


. Ataiwakilisha Tanzania kwenye programu ya “IBF Utalii wa Michezo” (IBF Sports Tourism)

. Anakutana na bingwa wa Namibia kwenye mpambano wa IBF Africa.


Mtanzania Rajabu mtoto wa Jumanne Maoja mkazi wa jiji la Tanga anaondoka na Shirika la Ndege la Afrika ya Kusini (South African Airways) kuelekea jijini Windhoek, Namibia ambako ana kibarua kikali kuiwakilisha Tanzania kwenye IBF Utalii wa Michezo (IBF Sports Tourism).

Maoja atakutana na bingwa wa nchi ya Namibia, Goettlieb Ndokosho kwenye mpambano uliopewa jina la “Vita Vya Jangwa la Kalahari” (The Battle for the Kalahari Desert) na waandaaji wa mpambano huo wa raundi 12 kumpata bingwa wa IBF Afrika katika uzito wa unyoya. Kinda Boxing Promotions inayoongozwa na bwana Simon Nangolo ambaye ni mkaguzi mwandamizi wa ndani wa mahesabu (Senior Internal Auditor) nchini Namibia ndio waandaaji wa mpambano huo wakukata na shoka.

Mshindi wa mpambano huo atakutana na bingwa wa IBF Afrika, Mashariki ya Kati, Ghuba ya Uarabu na Uajemi, Mtanzania Ramadhani Shauri ambaye hivi karibuni alimkung’uta bondia Sande Kizito wa Uganda katika mpambano ulioishia raundi ya 8 baada ya Kizito kushindwa kuendelea.

Huu unakuwa mpambano wa tatu kwa Watanzania mwaka huu kuwania ubingwa wa IBF katika bara la Afrika, Mashariki ya Kati ya Ghuba ya Uajemi ambako tayari mikanda miwili ya IBF iko Tanzania.

Mpambano wa Mtanzania Rajabu Jumanne Maoja na Goettlieb Ndokosho wa Namibia utafanyika katika jiji la Windhoek, mji mkuu wa nchi ya Namibia tarehe 29 Septemba siku ya Jumamosi.

Mtanzania Rajabu Jumanne Maoja atafuatana na Kocha wake Ibrahim Raphael Jorum ambaye naye anatoka katika jiji la Tanga.

Msimamizi mkuu wa mpambano huo ni Mtanzania Onesmo Alfred McBride Ngowi ambaye atalisimamia pambano hilo lililo na upinzania mkubwa!

Mungu mbariki Rajabu Jumanne Maoja, Mungu ibariki nchi nzuri ya Tanzania.

Imetolewa na:
Utawala
KAMISHENI YA NGUMI ZA KULIPWA NCHINI (TPBC)

ESTHER BULAYA AKIKABIDHI JEZI ZA MPIRA KWA VIJANA



 Mbunge wa viti maalumu kundi la vijana mkoa wa Mara, Ester Bulaya akikabidhi jezi na mpira kwa wenyeviti na makatibu wa vijana wa CCM wilaya ya Butiama kwenye hafra fupi iliyofanyika kwenye ukumbi wa Chama cha Mapinduzi mjini Musoma. (Picha na Berensi Alikadi)

Jeshi Stars yaivua Magereza ubingwa wa Wavu


MABINGWA mara tatu mfululizo wa michuano ya wavu ya wanawake, Magereza, wamevuliwa ubingwa huo na maafande wenzao wa Jeshi Stars baada ya kubwagwa kwa seti 3-1 katika mechi ya fainali iliyopigwa kwenye viwanja vya Bwalo la Umwema mjini Morogoro.
Kwa upande wa wanaume, timu ya Magereza ilitetea vyema taji lao baada ya kuwachapa Jeshi Stars kwa seti 3-0 katika mechi nyingine ya fainali iliyochezwa jana.
Nahodha wa Jeshi Stars (Wanawake), Zainab Thabit alisema timu yake imetwaa ubingwa huo kutokana na ujasiri wa kupambana hadi mwisho waliouonyesha dhidi ya mabingwa hao wa muda mrefu huku Ester Noel wa Magereza akiahidi kwamba mwakani watajifua zaidi kuhakikisha wanarejesha taji walilopoteza.
Mgeni rasmi katika fainali hizo, Katibu Mkuu Msaidizi wa Baraza la Michezo Taifa (BMT), Mohamed Kiganja, alisema mwamko wa baadhi ya michezo kama wavu umeendelea kuwa ni mdogo kwa kukosa ufadhili na ndio sababu mikoa mingi imeshindwa kuleta timu.
Aidha, Kiganja alilaumu baadhi ya viongozi kuua michezo kwa kugombea nyadhifa kwenye vyama vya michezo kwa matarajio fulani ambayo wakiyakosa huvitelekeza.
Alishauri zifanyike juhudi za kuibua vipaji vipya kwa kuweka nguvu kwenye ngazi ya shule badala ya kuendelea kutumia wachezaji walioibuliwa zamani kwenye michuano ya Umoja wa Michezo kwa Shule za Msingi (UMISHUMTA), ambao wameendelea kuliwakilisha taifa.
Naye Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Wavu Tanzania, Muarami Msumi, alitaka serikali kupitia kitengo chake cha uwekezaji kuhakikisha wawekezaji wanapewa masharti ya kujenga viwanja vya michezo kama sehemu ya uwekezaji, sambamba na kuendelea kujenga na kuimarisha viwanja vya michezo kuanzia ngazi za shule za awali.
Timu 11 zikiwamo tatu za wanawake zilishiriki michuano hiyo.

AZAM KUIENGUA SIMBA KILELENI LEO?

Kikosi cha Azam kitakachopambana na JKT Ruvu leo usiku

TATIZO la majeruhi limeendelea kuikumba timu ngumu ya JKT Ruvu baada ya nyota wake Credo Mwaipopo, Damas Makwaya na George Minja kuondolewa katika kikosi kitakachoshuka dimbani leo kuivaa Azam katika mechi yao ya Ligi Kuu ya Bara itakayopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kuanzia saa 1:00 usiku na kuonyeshwa ‘live’ kupitia kituo cha televbisheni cha Super Sport.
Azam inasaka pointi tatu zaidi leo kuwapiku vinara Simba na kukwea kileleni mwa msimamo wa Ligi kuu ya Bara.
Akizungumza na NIPASHE jana, kocha wa JKT Ruvu, Charles Kilinda, alisema kuwa Makwaya ataikosa mechi ya leo kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya misuli, Minja jeraha la goti na mwaipopo atakuwa nje akiuguza maumivu ya jeraha paja.
Kilinda amesema kuwa anasikitika kuwakosa wachezaji hao, lakini hana hofu kwa vile ana wachezaji wengine wazuri wa kuziba nafasi zao, wakiwamo Ramadhan Kauogo na Dumba Ramadhan.
"Pamoja na kuwakosa majeruhi hao, bado kikosi changu kina ari kubwa ya kuibuka na ushindi," alisema Kilinda.
Hata hivyo, Kilinda alilalamikia ratiba ya ligi kwa kusema kwamba imewabana mno kwani  wamejikuta wakicheza mechi tatu mfululizo dhidi ya timu tatu zilizokamata nafasi za juu kwenye msimamo wa ligi msimu uliopita,  ambazo ni Simba, Azam na Yanga.
Katika mechi mbili zilizopita kabla ya leo, JKT Ruvu walicheza dhidi ya Simba na kuchapwa 2-0 na kasha wakafungwa tena 4-1 katika mechi iliyopita dhidi ya Yanga.
Endapo Azam itashinda, itakwea kileleni kwenye msimamo wa ligi kwani itafikisha pointi 10, moja zaidi ya vinara wa sasa, Simba.
Coastal Union ya jijini Tanga iliyoshinda nyumbani 3-2 katika mechi yao ya juzi dhidi ya Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani ilikwea hadi katika nafasi ya pili baada ya kufikisha pointi nane.
Ligi hiyo inayoshirikisha timu 14, itaendelea pia kesho wakati Simba itakapocheza dhidi ya Prisons ya Mbeya kwenye uwanja huo huo wa Taifa kuanzia saa 11:00 jioni huku Yanga na African Lyon wakivaana keshokutwa Jumapili, pia kwenye Uwanja wa Taifa.
Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam utachezewa mechi kati ya Ruvu Shooting na Mtibwa Sugar itakayochezwa Oktoba 1 kuanza saa 10.30 jioni na mechi ya mwisho ya 'Super Weekend' itachezwa Oktoba 3 kwenye Uwanja wa Taifa na kuwakutanisha mahasimu wa jadi, Yanga na Simba kuanzia saa 1:00 usiku.
Wakati huo huo, Shirikisho la Soka Nchini (TFF) limesikitishwa na taarifa za kifo cha Katibu Mkuu mstaafu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Erasto Zambi kilichotokea Septemba 26 jijini Dar es Salaam kutokana na maradhi.
Zambi ambaye anatarajiwa kuzikwa keshokutwa Jumapili, kabla ya kuwa kiongozi TOC, kwa muda mrefu alikuwa mwalimu wa michezo katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambapo wanamichezo wengi hasa waliokuwa wanafunzi katika chuo hicho wamepita mikononi mwake.

Kikosi cha JKT Ruvu kikiwa mazoezini


CHANZO:NIPASHE

RAIS TFF AFAANUA SUALA LA UDHAMINI WA LIGI KUU TANZANIA BARA


RAIS wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodgar Tenga ameingilia kati msuguano unaoendelea kati ya klabu zinazoshiriki Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara na mdhamini mkuu wa ligi hiyo, kampuni ya huduma za simu ya Vodacom kuhusiana na kuwapo kwa kipengele cha upekee katika mkataba wa udhamini wa ligi hiyo.
Akizungumza na waandishi wa habari kwenye makao makuu ya TFF jijini Dar es Salaam jana, rais huyo alizionya klabu zinazokiuka makubaliano yaliyomo kwenye mkataba huo na kwamba klabu zitakazoendelea kufanya hivyo zitachukuliwa hatua.
“Tunashukuru kupata mkataba ambao ni mara mbili ya ilivyokuwa awali. Mkataba huu lazima ulindwe na uheshimiwe. Yeyote atayekiuka, atachukuliwa hatua za kisheria na kinidhamu,” alisema Tenga.
Tenga aliyasema hayo wakati mazungumzo kati ya klabu na mdhamini yakiendelea pia jijini Dar es Salaam jana.
Klabu zinalamikia kuwapo kwa vipengele kadhaa katika mkataba huo, vikiwamo vya posho za wachezaji, usafiri na kipengele cha upekee ambacho kinazuia timu kuvaa jezi au kubandika nembo za wapinzani wa kampuni hiyo kibiashara (makampuni ya huduma za simu).
Tenga alisema kuwa kuwapo kwa kipengele cha upekee lazima kiheshimiwe si wakati wa mechi tu, bali hata wakati wa mazoezi ya timu zote 14 zinazoshiriki ligi hiyo kwa kuwa kampuni hiyo ina haki ya matangazo hadi kwenye viwanja vya mazoezi vya timu hizo.
“Klabu zote zinazoshiri Ligi Kuu lazima zielewe hilo. Hata kwenye viwanja vyao vya mazoezi hawaruhusiwi kuvaa jezi au kubandika mabango ya wapinzani wa Vodacom, maana tulikubaliana hivyo na kampuni hiyo kabla ya kusaini mkataba huu,” alisema.
“African Lyon hawakuelewa vizuri vipengele vilivyomo kwenye mkataba huo ndiyo maana tulizungumza nao baada ya kutokea kwa tukio la timu yao kuingia na jezi zenye nembo ya Zantel wakati wa mechi ya Ligi Kuu.
Alidai kuwa mdhamini mkuu wa Ligi ya England ni benki ya Barclays, lakini Liverpool wanavaa jezi zenye nembo ya wadhamini wao ambao ni benki ya Standard Chartered kwa vile benki hizo mbili si wapinzani kibiashara maana kila moja ina aina yake ya wateja.
Alisema kuwa shirikisho hilo liliamua kuondoa kipengele cha upekee katika udhamini kama ilivyokuwa kwenye mkataba wa miaka mitano wa kampuni hiyo uliomalizika mwishoni mwa mwezi uliopita, lakini kipengele hicho kimebaki kwenye bidhaa miongoni mwa wadhamini.
Aidha, Tenga alisema kuwa baadhi ya klabu zinazoshiriki ligi hiyo zinadaiwa kiasi kikubwa cha pesa na shirikisho hilo na kwamba pesa zote zitakazotolewa na wadhamini zitaingizwa kwenye akaunti maalum itakayokuwa chini ya Kamati ya Ligi ya TFF kabla ya kusambazwa kwa klabu husika.
“Klabu zimechelewa kupata fedha kutoka kwa mdhamini mkuu kwa sababu mkataba ulichelewa kusainiwa. Ni kweli kwamba baadhi ya klabu zinadai pesa ya msimu uliopita, lakini klabu nyingi hasa zile kubwa tunazidai kiasi kikubwa sana cha pesa. Safari hii tumefungua akaunti maalum ambapo pesa za wadhamini zitawekwa kabla ya kupelekwa kwa wahusika. Wale wanaodai watalipwa na wale tunaowadai tutakata pesa yetu kwanza kabla ya kuwapatia fungu lao,” alisema.
Alizitaja klabu zinazodaiwa na shirikisho hilo kuwa ni pamoja na Simba, Yanga na Tanzania Prisons na kwamba madeni hayo yalitokana na TFF kuzilipia faini katika nyakati tofauti kwa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), lakini alikataa kutaja kiasi hicho wanachozidai klabu.
Klabu zimekuwa katika mgongano na wadhamini kwa kudai kwamba kiasi wanachotoa cha Sh. bilioni 1.7 kwa mwaka ni kidogo mno kulinganisha na gharama za uendeshaji na kwamba, ili kipengele cha upekee kiendelee kuwapo, ni lazima waongeze fedha hizo na baadhi wamekaririwa wakitaka walau udhamini huo uwe wa Sh. bilioni 4 kwa mwaka.
Wakati ligi kuu ya Bara yenye timu 14 na kuhusisha mechi zaidi ya 180 kwa msimu ikidhaminiwa kwa Sh. bilioni 1.7, timu ya taifa pekee (Taifa Stars) hudhaminiwa na Kampuni ya Bia (TBL) kwa dau la zaidi ya Sh. bilioni 3.5 kwa msimu, bila kujali kwamba mechi zake huwa hazizidi 20 kwa mwaka.

TWIGA STARS
Katika hatua nyingine, Tenga pia aliomba wadhamini wajitokeze kuzisaidia timu za taifa za vijana na timu ya taifa ya wanawake (Twiga Stars) kwa kuwa zina hali mbaya kifedha.
“Tunatumia fedha nyingi sana kuiendesha timu ya Twiga Stars. Kuanzia Januari hadi Juni mwaka huu, tumetumia Sh. milioni 222 kuihudumi timu hiyo wakati wa kambi na mechi ndani na nje ya nchi,” alisema Tenga.
Tenga, ambaye pia ni Rais wa Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), aliushukuru uongozi wa kituo cha televisheni cha Super Sport cha Afrika Kusini kwa kuamua kuonesha baadhi ya mechi za Ligi Kuu msimu huu.

FA YAMFUNGIA NA KUMPIGA FAINI JOHN TERRY KWA UBAGUZI



John Terry na Anton Ferdinand wakigombana katika tukio linalodaiwa Terry kumbagua Ferdinand
Terry akiwasili mahakamani kutoa ushahidi wa tuhuma hizo na kisha kukutwa hana hatia
LONDON, England
Katika sakata hilo ambalo lilifikishwa mahakamani na Terry kukutwa hana hatia, nahodha huyo wa zamani wa England anadaiwa kumbagua beki wa klabu ya QPR, Anton Ferdinand
HATIMAYE Chama cha Soka cha England (FA), leo kimefikisha tamati sakata la ubaguzi wa rangi lililokuwa likimkabili beki na nahodha wa Chelsea, John Terry na kutoa huku iliyotabiriwa na mtuhumiwa huyo mapema wiki hii.
Katika hukumu yake iliyotoka jana, iliyokuja baada ya mfululizo wa siku nne za kuhojiwa kwa nyota huyo na wakili wake kutoa ushahidi wa kumtetea, FA imemfungia nyota huyo mechi nne na faini ya pauni 220,000.
Katika sakata hilo ambalo lilifikishwa mahakamani na Terry kukutwa hana hatia, nahodha huyo wa zamani wa England anadaiwa kumtolea lugha za kibaguzi beki wa kimataifa wa England anayechezea klabu ya Queens Park Rangers, Anton Ferdinand.
Terry tayari alishakana kuhusika na tuhuma hizo anazodaiwa kuzitoa Oktoba mwaka jana wakati wa mechi baina ya Chelsea na QPR na kusema kuwa, FA inajaribu kukwepa ukweli uliomuacha huru kwenye Mahakama ya Westminster Magistrates.
Kutokana na kuhisi kuonewa na kutambua kama FA ilipanga kumhukumu isivyo, Terry mapema wiki hii alitangaza kustaafu kuichezea timu ya taifa ya England, kama sehemu ya kutoa hisia zake kuwa FA kwamba haimtendei haki katika sakata hilo.
Akitangaza uamuzi wa kustaafu soka la kimataifa, Terry, 31, alisema: “Natangaza rasmi leo kuwa nastaafu soka la kimataifa. Napenda kutoa shukrani kwa makocha wote wa England walionichagua mimi kuwamo dimbani na timu hiyo mara 78.
“Nimefanya maamuzi haya mapema kabla hata ya kusikia nini kitaamuliwa juu yangu kwa tuhuma zinazonikabili kwa sababu nahisi FA, imepanga hukumu isiyo ya haki dhidi yangu, licha uamuzi mzuri wa mahakama ulionisafisha na tuhuma hizo.”

Thursday, September 27, 2012

Cheka, Nyilawila kupimwa afya uzito kesho, kuvaana PTA J'mosi

Karama Nyilawila (kushoto) na Francis Cheka wanaotarajia kupima uzito na afya kesho kabla ya kuvaana katika pambano lao lwa kuwania ubingwa wa Mabara wa UBO litakalofanyika siku ya Jumamosi ukumbi wa PTA.

BINGWA wa ngumi za kulipwa anayetambuliwa na  ICB na IBF-Afrika, Francis Cheka na aliyekuwa bingwa wa Dunia wa WBF, Karama Nyilawila wanatarajia kupima uzito na afya zao kesho tayari kwa pambano lao la Jumamosi kuwania ubingwa wa UBO-Mabara.
Mabondia hao wanatarajiwa kupambana katika pambano la uzani wa Super Middle la raundi 12 kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam siku ya Jumamosi.
Mratibu wa pambano hilo, Robert Ekerege wa Afrika Kabisa Entertainment, alisema Cheka na Nyilawila watapimwa uzito na afya zao sambamba na mabondia wengine watakaowasindikiza kwenye pambano lao kwenye ukumbi wa Mawela jijini Dar.
Ekerege, alisema kupimwa kwa afya na uzito wa mabondia hao ni kuashiria kuiva kwa pambano hilo la kimataifa litakalochezewa na mwamuzi toka Malawi.
"Tunatarajia kuwapima afya na uzito wao mabondia wote watakaopigana Jumamosi, karibu mabondia wote wameshatua Dar tayari kwa zoezi hilo litakaloanza kufanyika saa 5 asubuhi ili kujiweka tayari kwa mchezo huo utakaofanyika PTA," alisema.
Aliongeza kuwa, maandalizi ya ujumla wa pambano hilo la Cheka na Nyilawila ambalo ni la tatu kwao kukutana na yale ya utangulizi yamekamilika ikiwemo kubadilisha mgeni rasmi wa siku hiyo kutoka Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo , Amos Makalla hadi kuwa Kamanda wa Kanda Maalum Dar, Afande Suleiman Kova.
Ekerege alisema wamemkosa Waziri Makalla waliokuwa wamempanga awali kwa vile atakuwa safarini na hivyo kumpa jukumu la kumvika mshindi wa pambano hilo la kesho Mlezi wa mchezo wa ngumi nchini, Kamanda Kova aliyethibitisha kushiriki.
Aliongeza kuwa katika mapambano hayo bendi maarufu ya Mashukaa Band 'Wana Kibega' ndio watakaotoa burudani ukumbini.

Mwisho

Arsenal, Man Utd, Liverpool zang'ara Kombe la Ligi

Mchezaji Ignasi Miquel akishangilia bao lake dhidi ya Coventry City
VIGOGO vya Ligi Kuu wa England, Arsenal, Manchester United, Liverpool na Tottenham Hotspurs usiku wa kuamkia zimefanya vema katika michuano ya Kombe la Ligi baada ya kutoa vipigo kwa wapinzani wao na kuvuka raundi nyingine.
Arsenal iliisasambua  Coventry City kwa mabao 6-1 kwenye pambano lililochezwa uwanja wa Emirates mjini London, wakati mahasimu wao Tottenham walipata ushindi wa magoli 3-0 dhidi ya Carlisle United ikiwa ugenini.
Manchester United wenyewe walipata ushindi wa mabao 2-1 wakiwa uwanja wa Old Trafford dhidi ya Newcastle United, wakati Liverpool ilitoka kupokea kichapo katika Ligi Kuu toka kwa wapinzani wao wa jadi Man United iliitafuna West Bromwich Albion kwa idadi kama hiyo ya mabao 2-1.
Mechi nyingine zilizochezwa jana WPR ilijikuta ikinyukwa nyumbani na Readind kwa mabao 3-2 na Norwich City iliilaza kwa bao 1-0 timu ya Doncaster Rovers.
Matokeo kamili ya mechi za michuano hiyo kwa siku ya jana ni kama ifuatavyo:
Norwich City 1-0 Doncaster Rovers
QPR 2-3 Reading
Arsenal 6-1 Coventry City
Celtic 2-1 Benfica
Manchester United 2-2 Newcastle
Carlisle United 0-3 Tottenham
West Brom 1-2 Liverpool
More: Scores | Fixtures | League Cup
 

Coastal yatakata Mkwakwani, Toto ikiendeleza mdudu wa sare

 MABAO mawili toka kwa mshambuliaji nyota na mzoefu, Nsa Job na jingine la Daniel Lyanga jana yaliipaisha timu ya Coastal Union hadi nafasi ya pili mwa msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kuilaza Kagera Sugar goli 3-2.
Coastal  ilipata ushindi huo katika pambano lililochezwa kwenye uwanja wa Mkwakwani Tanga ikiwa chini ya kocha wao wa makipa, Juma Pondamali na kulingana kila kitu na Azam waliokuwa wakiishikilia nafasi hiyo.
Huo ni ushindi wa pili kw atimu hiyo baada ya awali kufanya hivyo katika mechi ya fungua dimba la Ligi Kuu dhidi ya 'majirani' Mgambo Shooting kabla ya kutoka sare mbechi nyingine mbili.
Katika mfululizo wa ligi hiyo timu ya Toto Africans ya Mwanza imeendelea na mdudu wake wa sare baada ya jana kutoka suluhu ya bila kufungana na wenyeji wao Polisi Morogoro.
Hiyo ni sare ya nne kwa Toto Africans baada ya awali kufanya hivyo dhidi ya JKT Oljoro ilitoka sare ya 1-1, Azam 2-2 na kisha Mgambo Shooting mechi yao iliyopita.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea mwishoni mwa wiki kwa michezo kadhaa itakazozihusisha timu za Azam, Yanga na Simba ambazo kwa sasa zinawindana kwa ajili ya pambano lao litakalofanyika Jumatano ijayo jijini Dar. 

Wednesday, September 26, 2012

SHINDALO LA UCHORAJI KWA TAASISI ZA KIELIMU


Shindalo la Uchoraji Kwa Taasisi za Kielimu
Image Profession ikishirikiana na Baraza la Sanaa Tanzania (BASATA) kwa mara nyingine inatangaza kuanza kwa muhula mpya wa pili wa Shindano ya Uchoraji maalumu kwa Taasisi za elimu.
Shindano ambalo pia linajulikana Kama: Educational Drawing Competition au Image Profession Educational Drawing Competition, lina malengo ya kuibua vipaji katika fani ya uchoraji kwa kuzingatia uwekezaji kwa watoto na vijana.
Theme/Wazo kuu la mwaka huu: ART IMITATES LIFE au SANAA HUFUATISHA MAISHA
Makundi ya ushiriki
´ Chekechea,
´ Elimu ya Msingi,
´ Elimu ya Sekondari na  
´ Elimu  ya Juu
Kwa maelezo na taratibu za Shindano tembelea Facebook Page/Group “Tanzania Drawing Competition” au wasiliana na BASATA au
DRAWING COMPETITION – IMAGE PROFESSION,
P O BOX 92 DAR ES SALAAM.
SIMU: +255 222 664 740 / +255 713 484 040
/ +255 714 676 217 / +255 716 430 084
EMAIL: info@imageprofession.com

Kamanda Kova ambadili Waziri Makalla pambano la Cheka, Nyilawila

Kamanda Kova
KAMANDA wa Polisi Kanda Maalum ya Mkoa wa Dar es Salaam, Suleiman Kova, amembadili Naibu waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Amos Makalla katika kuwa mgeni rasmi wa pambano la kimataifa la kuwania ubingwa wa UBO, kati ya Francis Cheka na Karama Nyilawila.
Mratibu wa pambano hilo litakalofanyika siku ya Jumamosi kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam, Robert Ekerege aliiambia MICHARAZO kuwa, kumekuwa na mabadiliko ya mgeni rasmi badala ya Waziri Makalla sasa atakuwa Kova ambaye ni mlezi wa ngumi Tanzania.
Ekerege alisema Kova amechukua nafasi ya Makalla kutokana na waziri huyo kupangiwa safari nje ya nchi ambayo itafanyika wakati pambano la Cheka na Nyilawila likifanyika PTA.
Mratibu huyo alisema kutokana na udhuru huo wameona ni vema nafasi hiyo achukue mlezi wao wa ngumi, Kamanda KOva ambaye ameshaitikia wito huo wa kuwa mgeni rasmi ambapo ndiye atakayemvisha mkanda mshindi wa pambano hilo la uzani wa Supermiddle la raundi 12 litakalochezwa na mwamuzi toka Malawi.
"Kwa sababu zilizo nje ya uwezo wetu, tumeamua kubadili mgeni rasmi wa pambano la jumamosi badala ya kuwa Waziri Makalla sasa ni Kamanda wa Kanda Maalum ya Mkoa wa Dar es Salaam, Suleiman Kova, Waziri atakuwa safarini na hivyo hataweza kuhudhuria kama tulivyotangaza awali," alisema Ekerege.
Aliongeza, ugeni wa Kova katika pambano lao limewaongezea uhakika wa ulinzi wa kutosha siku ya mchezo huo ambao unawakutanisha Cheka na Nyilawila kwa mara ya tatu katika safari yao ya ngumi baina yao.
Ekerege alisema maandalizi mengine yanaendelea kama kawaida ambapo mabondia wote watakaopanda ulingoni wanatarajiwa kupima afya na uzito wao kesho kwenye ukumbi huo tayari kwa pambano la Jumamosi ambalo linadhaminiwa na kinywaji cha Coca Cola na kondomu za Dume na litapambwa na burudani toka kwa Mashujaa Band waliopania kuwachezesha wapenzi wa ngumi mtindo wao wa 'Kibega'.


Manchester City hoi Kombe la Ligi, Chelsea yaua

Wachezaji wa Man City wakiwa hoi baada ya kujifunga moja ya mabao yaliyoizamisha jana mbele ya Aston Villa

MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya England, Manchester City, imeanza vibaya msimu kwa kung'olewa   mapema kwenye michuano ya Kombe la Ligi baada ya kulazwa mabao 4-2 na Aston Villa, huku vinara wa ligi hiyo ya England, Chelsea ikitoa kichapo cha  mabao 6-0 kwa 'Mbweha'.
Kipigo hicho toka kwa Aston Villa, kimempa wakati mgumu kocha wa Man City, Roberto Mancini, kwani ni dalili za kushindwa kurejea mafanikio iliyopata msimu uliopita ilipotwaa taji la Ligi Kuu baada ya miaka 50.
Matokeo mengine ya mechi za jana za michuano hiyo ya Kombe la Ligi ni kama ifuatavyo;
Bradford iliinyuka Burton Abilion mabao 3-2 katika muda wa nyongeza, Chelsea  ilivuna ushindi wa mabao 6-0 kw Wolves, Crawley ilinyukwa mabao 3-2 na Swansea, Leeds United ikainyoa Everton magoli 2-1.


Wachezaji wa Chelsea wakishangilia moja ya mabao yao katika mechi ya Kombe la Ligi jana usiku
Mechi nyingine Manchester City vs Aston Villa baada ya muda wa nyongeza 2-4,MK Dons ikalala mabao 2-0 kwa Sunderland, Preston iliangukia pua mbele ya Middlesbrough kwa kichapo cha mabao 3-1 na Southmpton ilivuna ushindi wa mabao 2-0 kwa Sheffied Wed, Swindon iliinyuka Burnley 3-1 na wagonga nyundo wa West Ham wakalala mabao 4-1 kwa Wigan.

Mgunda afuata nyayo za Saintfiet atimuliwa Coastal Union

Hemed Suleiman 'Morocco' (kushoto) aliyetua Coastal Union
SIKU chake tangu klabu ya Yanga kumtimua kazi aliyekuwa kocha wake mkuu, Tom Saintfiet kutoka Ubelgoji, uongozi wa Coastal Union ya jijini Tanga umemtangaza, Hemed Suleiman 'Morocco' kuwa kocha mpya akichukua nafasi ya aliyekuwa kocha wao, Juma Mgunda.
Morocco, aliyekuwa akiinoa timu ya taifa ya Zanzibar, anatarajiwa kuiangalia Coastal ikicheza pambano  lao dhidi ya Kagera Sugar litakalofanyika kwenye uwanja wa Mkwakwani, chini ya kocha wa makipa, Juma Pondamali aliyekuwa ameachiwa timu baada ya Mgunda na msaidizi wake, Habib Kondo kutimuliwa.
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana jijini, uongozi wa Coastal ulifikia maamuzi hayo katika kikao kilichofanyika jana asubuhi na kwamba wamewatimua kufuatia kutoridhishwa na kiwango cha wachezaji wa timu hiyo licha ya kutofungwa mechi.
"Tayari wameshajulishwa maamuzi haya na Morocco atakuwa jukwaani kesho na ndiye atakayeongoza jahazi," alisema kiongozi mmoja wa juu wa timu hiyo.
Chanzo hicho kilisema kuwa katika mchezo wa leo, kocha wa makipa, Juma Pondamali ndiye atakayeiongoza timu hiyo na wanaamini mabadiliko yatazaa matunda.
Mgunda mwenyewe alinukuliwa jana akidai kuwa ameamua kujiondoa Coastal kwa nia njema na mapenzi mkubwa aliyonayo kwa timu hiyo aliyowahi kuichezea kwa mafanikio enzi zake za uchezaji.
Mgunda alisema aliona ni bora ajiondoe kutokana na shinikizo kubwa lililopo ndani ya Coastal ambayo imejiwekea malengo makubwa katika msimu huu wa ligi na kuwataka mashabiki na viongozi wa timu hiyo kumheshimu na kuyaheshimu maamuzi yake yaliyokuja wakati Coastal ikiwa nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi kutokana na kushinda mechi moja na kupata sare mechi mbili.

Simba yaenda Zenji kuiwinda Yanga, Jangwani wakimbilia Bagamoyo








MABINGWA watetezi wa soka nchini Simba imeondoka jijini jana kuelekea Zanzibar kwa ajili ya kuweka kambi ya kujiwinda na pambano lao na watani zao Yanga litakalochezwa Jumatano ijayo.
Timu hizo mbili zinatarajiwa kukutana katika pambano la kwanza kwa msimu huu litakalochezwa kwenye uwanja wa Taifa na kurushwa 'live' na kituo cha Super Sport, huku Yanga ikiwa na deni kubwa la kipigo cha mabao 5-0 iliyopata katika pambano baiona yao lililofungia msimu uliopita.
Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange 'Kaburu', alinukuliwa jana kuwa wachezaji wote 29 wa timu hiyo wameondoka na wanatarajia kurejea keshokutwa kwa ajili ya kuvaana na Prisons ya Mbeya kabla ya kurejea tena visiwani humo kuweka kambi hadi siku ya mchezo wao na Yanga.
Alisema kuwa wakiwa Zanzibar wataendelea kufanya mazoezi ya ufukweni na ya uwanjani na wanaamini kambi yao itazaa mafanikio kwa kushinda mechi hizo zinazowakabili.


Wakati Simba ikienda kujichimbia Zenji, watani zao walikuwa katika mchakato wa kuelekea mjii Bagamoyo kwa ajili ya kujiandaa na pambano hilo la watani zao na lile la Jumamosi ijayo itakapoumana na African Lyon.


Yanga imepania kulipa kisasi cha mabao hayo 5-0 iliyofungwa na Simba Mei 6, lakini pia wakiwa na deni la miaka zaidi ya 30 ya kipigo cha mabao 6-0 ilichopewa na Simba mwaka 1977.



YANGA HATARINI KUSHUSHWA DARAJA - MADENI YA PAPIC NA NJOROGE YAWAPONZA FIFA

Kikosi cha Yanga kilichopo hatarini kiushushwa daraja
Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Oseah


Tumepokea barua kutoka Kitengo cha Sheria cha Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Mpirawa Miguu (FIFA) likitutaka tuitaarifu Yanga kuhusu mashtaka yaliyowasilishwa na kocha wazamani wa klabu ya Yanga, Kostadin Papic. Katika malalamiko yake, Papic anadai kuwa hajalipwa malimbikizo ya mshahara wake yanayofikia kiasi cha Dola 12,300 za Kimarekani. Katika barua yake, kocha huyo anadai kuwa alikuwa akiwasiliana na maofisa na viongozi wa Yanga, lakini hakupata ushirikiano na hivyo kuamua kwenda FIFA. TFF ilifanya juhudi za kuwasiliana na Yanga kuhusu malalamiko hayo ili kujaribu kumzuia kocha huyo asishtaki FIFA, lakini juhudi hizo hazikuzaa matunda.
Kama chombo kinachosimamia uendeshaji wa mpira wa miguu nchini, TFF imesikitishwa na habari hizo na inaiomba klabu ya Yanga kufanya kila jitihada kuhakikisha kuwa inawasilisha taarifa zote muhimu na nyaraka zinazohusiana na stahiki za kocha huyo ili kama ilishamalizana naye, sifa ya klabu ya Yanga isafishwe. Tayari barua imeshaandikwa kwa klabu ya Yanga kuitaka itekeleze utashi huo mapema iwezekanavyo.
Tukio hilo, si tu linachafua sifa ya klabu ya Yanga, bali soka ya Tanzania kwa ujumla kutokana na ukweli kwamba ikishadhihirika kuwa kuna tatizo la malipo ya makocha nchini, ni dhahiri kuwa itakuwa ni vigumu kwa klabu zetu na hata timu za taifa kupata makocha wazuri kutoka nje kwa kuwa watakuwa wamejengeka hofu ya kufanya kazi nchini.
Hili ni tukio la pili kwa Yanga baada ya mchezaji wake mwingine, John Njoroge kuishtaki klabu hiyo FIFA na kushinda kesi yake iliyoamuliwa mwezi Januari na Kitengo cha Usuluhishi wa Migogoro cha FIFA (DRC). Ushindi wa Njoroge unamaanisha kuwa iwapo Yanga itashindwa kutekeleza kumlipa mchezaji huyo kasi cha Sh milioni 17, inaweza kujikuta katika adhabu ambayo itatulazimisha tuishushe daraja; kuinyang’anya pointi kwa kiwango kitakachotajwa na FIFA; kuipiga faini au adhabu zote kwenda kwa pamoja. Tunaiomba Yanga itekeleze hukumu hiyo kwa wakati uliotajwa kwenye barua ya FIFA ili kuepuka hatua hizo.
Suala la Njoroge ni moja kati ya matukio mengi yanayohusu ukiukwaji wa taratibu za kuvunja mikataba yanayofanywa na klabu zetu. Kuna malalamiko ya wachezaji wengi dhidi ya klabu zao za zamani kuhusu kutolipwa stahiki zao. Hivyo TFF inatoa wito kwa klabu kujiepusha na vitendo hivyo kwa kuwa vinawanyima haki wachezaji, lakini pia vinachafua sifa ya nchi iwapo wachezaji wanachukua hatua za kwenda kwenye vyombo vya juu.
Tumekuwa tukisoma kwenye vyombo vya habari kuhusu kutimuliwa kwa sekretarieti nzima ya Yanga kutokana na kuonekana kuwa ina udhaifu. Taarifa hizo hazijaifikia rasmi TFF. Kiutaratibu, Yanga inatakiwa iwsasilishe majina ya maofisa watakaofanya kazi na TFF kwa sasa na itakapoajiri sekretarieti ya kudumu, basi itume barua nyingine ya kuwatambulisha watendaji wake.
Kama itakuwa imeitimua sekretarieti nzima, basi TFF inapokea taarifa hizo kwa masikitiko makubwa. Si nia ya TFF kutetea watendaji wazembe, lakini klabu hazina budi kufuatilia kwa karibu utendaji wa sekretarieti zao ili isije ikafikia wakati sekretarieti nzima inaondolewa kwa makosa ambayo yangeweza kusahihishwa kama kungekuwa na ufuatiliaji wa karibu. TFF imekuwa ikitoa mafunzo kwa watendaji wa klabu ili waweze kufanya kazi zao vizuri na kwa mintaarafu ya mpira wa miguu na hivyo kuondolewa kwa timu nzima kama hiyo kunamaanisha kuwa ni upotevu wa rasilimali ambayo imetumika kuwapa elimu ya kutenda kazi zao vizuri. TFF ilishafanya kozi ya Event Management kwa ajili ya watendaji wa klabu; semina ya kuangalia upya maazimio ya Bagamoyo kwa watendaji na viongozi na pia kozi ya utawala hivyo haipendi juhudi hizi zipotee kirahisi.
Angetile Osiah
KATIBU MKUU

Monday, September 24, 2012

Vincent Barnabas akiri ligi ngumu msimu huu

Vincent Barnabas (kushoto) akiwa dimbani na timu ya taifa , Taifa Stars

WINGA machachari wa timu ya soka ya Mtibwa Sugar, Vincent Barnabas amesema matokeo ya mechi za awali za Ligi Kuu Tanzania Bara zimeonyesha jinsi gani msimu huu utakuwa na ligi ngumu isiyotabirika kirahisi.
Aidha nyota huyo aliyewahi kutamba na timu za Kagera Sugar, Yanga na African Lyon, ameitabiria klabu yake ya Mtibwa Sugar kufanya vema tofauti na msimu uliopita ilipomaliza ikiwa nafasi ya nne.
Akizungumza na MICHARAZO, Barnabas, alisema kwa mechi za raundi tatu zilizokwisha kucheza mpaka sasa inaonyesha wazi ligi ya msimu huu sio nyepesi kama watu walivyokuwa wakiifikiria.
Nyota huyo alisema kutokana na mwenendo wa ligi hiyo, ni vigumu kutabiri mapema nani anayeweza kuwa bingwa kwa vile ligi bado haijatulia.
"Sio siri msimu huu ligi imeanza kuonyesha ni ngumu kwa aina ya matokeo yaliyopatikana, naamini ugumu huu umetokana na klabu zote kujipanga vema na kusaidia kuongeza ushindani," alisema.
Juu ya Mtibwa ambayo ilianza kwa sare dhidi ya Polisi Moro kabla ya kuilaza Yanga mabao 3-0 na kuzimwa na Azam mwishoni mwa wiki kwa bao 1-0, winga huyo alisema anaamini itafanya vema msimu huu tofauti na ligi iliyopita.
"Kwa namna tulivyo, naamini tutafanya vema, licha ya ugumu unaoonekana kwenye ligi ya msimu huu, wachezaji tumejipanga kuipigania timu ili imalize msimu tukiwa katika nafasi bora zaidi ya msimu uliopita," alisema Barnabas.
Kwa matokeo ya mwishoni mwa wiki, Mtibwa imejikuta ikiachwa nafasi ya sita ya msimamo ikiwa na pointi nne sawa na ndugu zao za Kagera Sugar na Yanga iliyozinduka kwa kuilaza JKT Ruvu mabao 4-1, ikizizidi uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa.

Mwisho

Mashali, Sebyala kumkumuka Mwl Nyerere kwa masumbwi Dar

Med Sebyala wa Uganda akiwa na taji lake la ubingwa wa Uganda
Thomas Mashali wa Tanzania akiwa na ubingwa wake wa TPBO


BONDIA machachari wa ngumi za kulipwa nchini, Thomas Mashali anatarajia kuzidunda na Mganda Med Sebyala katika pambano la kuwania taji la Afrika Mashariki siku ya kumbukumbu ya kifo cha Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere.
Pambano hilo la uzati wa kati la raundi 10 limepangwa kufanyika Oktoba 14 kwenye ukumbi wa Friends Corner, Manzese Dar es Salaam.
Mratibu wa pambano hilo litakalosimamiwa na Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO, Regina Gwae alisema tayari wameshamalizana na mabondia hao kwa ajili ya pambano hilo la kimataifa.
Regina, alisema pambano hilo ni fursa nzuri kwa Mashali anayeshikilia ubingwa wa Taifa wa TPBO kujitangaza kimataifa iwapo atafanikiwa kumnyuka Sebyala.
“Huwezi kwenda nje kama ndani hufanyi vizuri na huwezi kwenda Ulaya, iwapo unashindwa kutamba  Afrika Mashariki, hivyo tumeona tumpe Mashali mchezo huu ili akifanya vyema aweze kuvuka mipaka ya sasa, "alisema Regina.
Regina alisema ana matumaini mpambano huo utakuwa mzuri na utakaovutia kutokana na ukweli mabondia wote wawili wana sifa zinazofanana waking'ara ndani ya nchi zao.
Alisema Sebyala ni mmoja wa bondia wazuri waliowasumbua baadhi ya nyota wa ngumi nchini kama Rashid Matumla na Francis Cheka aliowahi kuja kucheza nao hapa nchi  katika mechi za zisizo za ubingwa.
Mratibu huto aliwaomba wafadhili wajitokeze kwa ajili ya kudhamini mchezo huo unatarajiwa kuwa na mapambano ya utangulizi.

Mwisho

Maugo kuwania ubingwa wa WBF Arusha

Bondia Mada Maugo

BONDIA nyota wa ngumi za kulipwa nchini, Mada Maugo anatarajiwa kupanda ulingoni mjini Arusha kuzichapa na Mustapha Katende kutoka Uganda katika pambano la kuwania ubingwa wa Mabara wa WBF.
Pambano hilo la uzani wa Super Middle la raundi 12 litafanyika Oktoba 28 kwenye ukumbi wa Triple A, jijini humo na kusindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi pamoja na burudani ya muziki wa kizazi kipya.
Akizungumza na MICHARAZO leo asubuhi, Maugo alisema awali pambano hilo litakalosimamiwa na Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Tanzania, PST, lilikuwa limkutanishe na bondia toka Iran, Gavad Zohrenvard.
Maugo alisema hata hivyo bondia huyo wa Iran amepatwa na dharura na hivyo kupangiwa Mganda ili kuonyeshana nae kazi siku ya pambano hilo.
"Natarajia kupanda ulingoni Oktoba 28 kwenye ukumbi wa Triple A mjini Arusha kuzichapa na Mganda, Mustapha Katende, ambapo pia tutasindikizwa na michezo mbalimbali ya utangulizi," alisema.
Alitaja baadhi ya mabondia watakaowasindikiza siku hiyo ni Robert Mrosso wa Arusha atakayepigana na Selemani Said 'Tall' wa Dar na Abbas Ally wa Arusha dhidi ya Joseph Marwa wa Zanzibar.
Bondia huyo aliyepanda mara ya mwisho ulingoni April mwaka huu kuwania ubingwa wa IBF-Mabara dhidi ya Francis Cheka na kupigwa, alisema amejiandaa vya kutosha kuweza kunyakua taji hilo la WBF dhidi ya Mganda.
"Naendelea kujifua kwa ajili ya kuhakikisha natwaa taji hilo, sambamba na kusaidia kutoa hamasa kwa vijana wenye vipaji vya ngumi mkoani Arusha," alisema Maugo.

Mwisho

WAZIRI MAKALLA MGENI RASMI PAMBANO LA CHEKA< NYILAWILA

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo Amos Makalla atakayekuwa mgeni rasmi katika pambano la ngumi la kuwania ubingwa wa UBO Mabara kati ya Francis Cheka na Karama Nyilawila


NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni Vijana na Michezo, Amos Makalla anatarajiwa kuwa mgeni rasmi wa pambano la kimataifa la kuwania ubingwa wa Mabara wa UBO kati ya mabondia Francis Cheka na Karama Nyilawila.
Pambano hilo litafanyika kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam Septemba 29, na waratibu wa mchezo huo, kampuni ya Afrika Kabisa Entertainment wamesema Waziri Makalla ndiye atakayemvisha taji mshindi.
Promota Robert Ekerege, aliiambia MICHARAZO kwamba tayari amehakikishiwa na Waziri Makalla kuwa mgeni rasmi katika pambano hilo la Super Middle la raundi 12 amblo litasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
"Mgeni rasmi katika pambano letu kati ya Cheka na Nyilawila atakuwa Naibu Waziri wa Michezo, Amos Makalla, na kila kitu kimekamilika katika maandalizi ya pambano hilo," alisema Ekerege.
Ekerege alisema mbali na Waziri Makalla, pia siku ya pambano hilo litahudhuriwa na Mlezi wa mchezo wa ngumi nchini, Suleiman Kova ambaye ni Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Mkoa wa Dar es Salaam.
Aliongeza kuwa, katika kunogesha pambano hilo mabondia kadhaa karibu 10 watapanda ulingoni kuwasindikiza akina Cheka kwa kucheza michezo ya raundi sita kila moja na wa watasindikiza na burudani toka Mashujaa Band.
"Mashujaa Band ndio watakaosindikiza michezo hiyo yote ambayo itakuwa na ulinzi wa kutosha ili kudhibiti vitendo vyote vya kihuni ambavyo vinaweza kutuharibia," alisema Ekerege.

Mwisho

VAN PERSIE AIZAMISHA LIVERPOOL, ARSENAL WAISHIKA MANCHESTER CITY, DEMBA BA HASHIKIKI...MILAN, INTER HOI!


LONDON, England
PENATI ya Robin van Persie kuelekea mwishoni mwa mechi iliipa Manchester United iliyocheza chini ya kiwango ushindi wa ugenini wa 2-1 dhidi ya wachezaji 10 wa Liverpool katika mechi yao iliyojaa hisia ya Ligi Kuu ya England kwenye Uwanja wa Anfield huku mabingwa watetezi, Manchester City wakishikiliwa kwa sare ya nyumbani ya 1-1 dhidi ya Arsenal leo.
Mholanzi Van Persie aliwahakikishia ushindi Man U wakati alipopiga penati ya shuti kali iliyomshinda kipa Pepe Reina kufuatia Glen Johnson kumuangusha Antonio Valencia.
Licha ya kucheza chini ya kiwango, Man U walipanda hadi katika nafasi ya pili katika msimamowa ligi wakiwa na pointi 12, wakizidiwa kwa pointi moja tu na vinara Chelsea.
Man City walipata sare ya tatu katika mechi zao tano za mwanzo wa msimu baada ya  Laurent Koscielny kuisawazishia Arsenal kwa bao la 'usiku' kufuatia goli la utangulizi la Joleon Lescott kuwapa wenyeji uongozi hadi mapumziko. Timu zote mbili hazijafungwa na kufikisha pointi tisa.
Tottenham Hotspur wamefikisha pointi nane baada ya Jermain Defoe kuwafungia bao la ushindi wa 2-1 dhidi ya Queens Park Rangers, ukiwa ni ushindi wa kwanza wa nyumbani wa Tottenham chini ya kocha Andre Villas-Boas.
Demba Ba alifunga bao pekee lililowapa Newcastle United ushindi wa 1-0 dhidi ya Norwich City inayonolewa na kocha wao wa zamani, Chris Hughton.
Hiyo ilikuwa ni mechi ya kwanza kwenye Uwanja wa Anfield tangu kutolewa kwa taarifa ya  Hillsborough iliyowasafisha mashabiki wa Liverpool ambao awali walikuwa wakilaumiwa kwa kusababisha vifo vya mashabiki 96 kwenye mechi yao ya nusu fainali ya Kombe la FA mwaka 1989.
Balaa kwa Liverpool lilianza katika dakika ya 39 wakati mchezaji wao Jonjo Shelvey alipotolewa nje kwa kadi nyekundu.
Hata hivyo, Liverpool walipata bao walilostahili baada ya kuanza kipindi cha pili kupitia shuti la Steven Gerrard, lakini Man U wakasawazisha dakika sita baadaye kupitia shuti la "upinde" la beki Rafael.
Bao la 'usiku' la Van Persie, ambalo ni la tano kwake msimu huu, limemuacha kocha Brendan Rodgers akikosa ushindi baada ya mechi tano za mwanzo wa msimu, ikiwa ni rekodi "mbovu" kabisa katika historia ya klabu hiyo kwenye Ligi Kuu ya England.

Yanga kupokwa ushindi dhidi ya JKT Ruvu?

Kikosi cha timu ya Yanga

LICHA ya kuchekelea ushindi wa mabao 4-1 iliyopata dhidi ya JKT Ruvu, mabingwa wa Kombe la Kagame, Yanga huenda wakapokwa ushindi wao huo iliyopata juzi kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar iwapo itabainika wakikiuka kanuni za ligi juu ya idadi ya wachezaji wa kigeni kucheza mechi moja.
Yanga katika mechi yao na JKT iliwachezesha wachezaji wake wote watano wa kigeni, kitu kinachoelezwa ni kinyume na kanuni inayoruhusu klabu kuwatumia wachezaji wasiozidi watatu kucheza mechi moja ya ligi.
Katika pambano hilo la juzi Yanga iliwachezesha mapro wake wote akiwamo kipa Yew Berko, beki Mbuyu Twite, kiungo Haruna Niyonzima, mshambuliaji Didier Kavumbagu na winga Hamis Kiiza.
Micharazo, imedokezwa kwamba uongozi wa Simba tayari unajiandaa kuwasilisha barua ya kupinga kitendo kilichofanywa na watani zao za kuwatumia wachezaji wake hao wa kigeni katika mechi moja, ingawa tunaendelea kufuatilia kuona kama Yanga ilikiuka kanuni ya ligi kuhusu wachezaji au la...
Kama itakuwa imekiuka kuna uwezekano Yanga wakajikuta wakipokwa ushindi huo na kuzidi kuwasononesha baada ya kutoka kwenye machungu ya kushindwa kufurukuta katika mechi zao za awali ambapo ililazimishwa suluhu na Prisons Mbeya kabla ya kulala mabao 3-0 kwa Mtibwa Sugar.


Simba yazidi kupaa Ligi Kuu Tanzania Bara

Amri Kiemba wa Simba ajijaribu kumtoka beki wa Ruvu katika pambano lao la jana
 
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, Simba, wameendeleza wimbi la ushindi wa asilimia 100, baada ya kuibuika na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ruvu Shooting, pambano lililochezwa leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Simba ilipata bao la kuongoza dakika ya 30, likiwekwa nyavuni na nyota wa kimataifa wa Zambia, Sunzu kwa kichwa maridadi akimalizia krosi iliyopigwa baada ya kazi nzuri ya kuwachambua mabeki iliyofanya na Said Nassor ‘Cholo’ aliyepanda kusaidia mashambulizi.

Dakika 38, Kiemba akawachachafya wachezaji wa Ruvu, kabla ya krosi yake kukosa mmaliziaji na kuishia mikononi mwa Benjamin Haule.

Simba iliendelea kushambulia ambapo katika dakika ya 44, beki Mau Bofu wa Ruvu alimwangusha Sunzu ndani ya 18 na mwamuzi Swai kuamuru ipigwe penati. Akuffor akabeba jukumu la kupiga tuta hilo, ambalo mlinda mlango Haule alipangua na kuwa kona tasa.

Hadi mapumziko, Simba ilitoka ikiongoza kwa bao hilo, huku mashabiki waliohudhuria mechi hiyo wakishuhudia maamuzi tata ya mwamuzi Swai, aliyeonekana dhahiri kutowajali vibendera wake Samwel Mpenzu na Godfrey Kihwili wote wa Arusha pindi wanapoashiria madhambi.

Kipindi cha pili kilianza kwa Ruvu kushambulia lango la Wekundu na kama si umakini mdogo miongoni mwa washambuliaji wake Paul Ndauka, Hussein Said na Hassan Dilunga aliyekuwa akipenya kirahisi safu ya ulinzi, wangeweza kupata mabao.

Sunzu akafanya shambuliazi kali dakika ya 55 lililotokana na jitihada binafsi akiwalima chenga mabeki, kabla ya Ruvu nao kurudi langoni mwa Simba na Dilunga (Hassani) nusura aipatie bao timu yake, kabla ya mawasiliano madogo na Abdulrahman Mussa kumgharimu.

Ruvu ikapata bao la kusawazisha mnamo dakika ya 78, lililowekwa nyavuni na mtokea benchi Seif Rashid, akitumia makosa ya beki Juma Nyoso wa Simba, aliyeshindwa kuondoa hatari langoni akiwa peke yake na kuukanyaga mpira huo na kuteleza, ambapo Seif aliunasa na kumchambua Juma Kaseja.

Daniel Akuffor akimtoka beki wa Ruvu Shooting


Wakati wengi wakimiani matokeo ya pambano hilo yangebaki kuwa ni sare ya bao 1-1, mtokea benchi wa Simba, Christopher Edward aliyeingia kuchukua nafasi ya Akuffor, akaipatia timu yake bao la pili dakika ya 87 kwa shuti na kuamsha mamia ya mashabiki wake jukwaani.