STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, March 25, 2013

Madhira amlilia Rais Kikwete




MUIGIZAJI mahiri wa filamu, Mbwana Salim 'Bessa' au Madhira, amemlilia Rais Jakaya Kikwete na kuomba kuonana naye ili aweze kumfikishia kilio chake na cha wasanii wenye ulemavu kama yeye.
Bessa ambaye pia ni mtunzi wa riwayana mchoraji, alisema kutokana na wasanii wenye ulemavu kutothaminika wala kutiwa moyo, angependa kuonana na Rais Kikwete akiamini anaweza kusikia kilio chao na kuwasaidia ili nao wawe na hadhi sawa na wasanii wengine nchini.
"Ningependa nipate nafasi ya kuonana na Rais Kikwete ili nimfikishie kilio tulichonacho sisi wasanii wenye vipaji vya sanaa, lakini tunadhalilika kwa sababu ya ulemavu wetu, tafadhali naomba unifikishie ujumbe wangu kwa mheshimiwa," alisema Bessa.
Msanii huyo ambaye ni mtunzi mkuu wa vichekesho na filamu za kampuni ya Al Riyamy alisema hali wanayotendwa wasanii wenye ulemavu nchini ikiwemo kunyonywa kimasilahi na kutothaminika hata kwa viongozi wanaosimamia sanaa inawakatisha tamaa, ilihali waliamua kujitegemea.
"Wapo watu wenye ulemavu kama sisi walikata tamaa na kuwa tegemezi, sisi tumeamua kutumia vipaji vyetu kujiajiri na kuwatia moyo wengine, lakini bado tunaangaliwa kama watu duni na kukatishwa tamaa, naimba serikali iliangalie hili," alisema msanii huyo.
Aliongeza kuwa, pamoja na juhudi anazozionyesha akiwa pia ni mwalimu wa chekechea, mchoraji na mtengenezaji wa chaki na batiki, alisema kuna haja wasanii waenye vipaji kama yeye watupiwe macho kuwafanya wapige hatua kimaendeleo na kuwahamasisha wengine kujitegemea.

Golden Bush yazidi kutoa dozi ikiisubiri Wahenga FC

Kikosi cha Golden Bush Veterani
SIKU chache kabla ya kuvaana na wapinzani wao, timu ya Golden Bush Veterani imeendelea kutoa dozi baada ya mwishoni mwa wiki kuinyuka Kibangu Veterani kwa mabao 4-1 kabla ya kuwakung'uta tena watoto zao Golden Bush Fc kwa magoli 2-0.
Mechi hizo za kujipima nguvu zilichezwa Jumamosi na Jumapili ikiwa ni maandalizi ya kuvaana na wapinzani wao, Wahenga Fc pambano litakalochezwa kwenye uwanja wa Tp Afrika, Sinza siku ya Pasaka.
Katika mechi yao dhidi ya Kibangu, Golden Bush walipata ushindi wao kupitia mabao ya Sadik Muhimbo aliyefunga mara mbili, Said Swedi 'Panucci' na Di Natale, huku bao la kufutia machozi la Kibangu liliwekwa kimiani na Daudi.
Katika mechi iliyochezwa jana, dhidi ya vijana wao wanaoshiriki Ligi ya TFF- Kinondoni, Wazee wa Golden walipata ushindi wa 2-0 na kuendeleza ubabe kwa watoto hao kwani wiki iliyopita waliwanyuka mabao 2-1.
Katika hatua nyingine, Mlezi wa Golden Bush Veterani, Onesmo Waziri 'Ticotico' ameamua kutangaza dau kwa wapinzani wao iwapo wataibuka na ushindi au kuambulia sare atakuwa tayari kuwapa papo hapo kitita cha Sh 200,000.
Mechi hiyo ya Golden Bush na Wahenga, inatarajiwa kuhudhuriwa na mgeni rasmi, Kamanda Thobias Andengenye na itachezwa majira ya saa 10 jioni ambnapo lineup ya Golden Bush, kwa mujibu wa msemaji wao itakuwa kama ifuatavyo;

Philemon, Said Swedi, Faraji, Majuto Komu, Wisdom Ndlovu, Godfrey Bonny, Onesmo Wazir 'Ticotico' (captain), Waziri Mahadhi  'Mandieta', Athumani Machupa 'Magoli', Herry Morris na Sadik Muhimbo.

Rais TFF kufungua semina Copa Coca Cola








Na Boniface Wambura
RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga atakuwa mgeni rasmi katika ufunguzi wa semina elekezi ya michuano ya Copa Coca Cola itakayofanyika kesho (Machi 26 mwaka huu).

Semina hiyo inayoshirikisha makatibu wakuu wa vyama vya mpira wa miguu mikoa ya Tanzania Bara na Zanzibar itafanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na itafunguliwa na Rais Tenga kuanzia saa 3 kamili asubuhi.

Washiriki wengine katika semina hiyo itakayokuwa na watoa mada kutoka TFF na wadhamini kampuni ya Coca Cola ni waratibu wa michuano ya Umoja wa Michezo wa Shule za Sekondari Tanzania (UMISSETA).

MAPINDUZI SIMBA YALIKUWA BATILI-TFF

Wanachama wa Simba walipokutana Machi 17

Na Boniface Wambura
MKUTANO Mkuu wa Dharura ulioitishwa na wanachama wa Simba, Machi 17 mwaka huu na kuuondoa uongozi wa klabu hiyo si halali kwa vile haukufuata taratibu, na Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) halitambui Kamati za Muda.
Uamuzi huo umefikiwa na Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za
Wachezaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Machi 24 mwaka huu) jijini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa.
Kamati imebaini kuwa kwa mujibu wa Ibara ya 22(2) ya Katiba ya Simba, Mkutano Mkuu wa Dharura unaitishwa na Kamati ya Utendaji baada yawanachama wasiopungua 500 kuwasilisha ombi hilo kwa maandishi na kujiorodhesha. Mkutano huo haukuitishwa na Kamati ya Utendaji ya Simba.
Utaratibu huo haukufuatwa ambapo barua ya Mkutano huo iliandikwa kwa Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo badala ya Kamati ya Utendaji ya Simba ambayo ndiyo matakwa ya Katiba ya Simba.
Kwa mujibu wa Katiba ya Simba, Kamati ya Utendaji ndiyo inayoitisha Mkutano Mkuu wa Dharura baada ya kuhakiki uhai na uhalali wa wanachama waliojiorodhesha kuomba mkutano huo.
Kamati imesisitiza kuwa Katiba za wanachama wote wa TFF hazina
kipengele cha kura ya kutokuwa na imani na uongozi (vote of no
confidence), ndiyo maana uko nyuma wanachama wa Yanga, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Shinyanga (SHIREFA) na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Tabora (TAREFA) walipiga kura hiyo, na TFF kutotambua uamuzi wao.
Hata Katiba ya Simba haitoi mamlaka kwa Mkutano Mkuu wa Dharura kufukuza uongozi uliochaguliwa.
Katiba za wanachama wote wa TFF zimezingatia katiba mfano za
Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) ambazo zinasema
kiongozi ataingia madarakani kwa uchaguzi, na si kuteuliwa (Kamati ya
Muda).
Pia Kamati imesema endapo wanachama wa Simba wangefuata taratibu na uongozi ukakataa kuitisha mkutano, wanachama wangetuma ombi hilo TFF kupitia Kamati ya Sheria ili kutoa mwongozo kwa uongozi wa Simba .
TFF ina mamlaka ya kutoa adhabu kwa viongozi wa wanachama wake wanaokwenda kinyume cha Katiba zao. Pia Kamati imesisitiza kwa wanachama wa TFF kuitisha mikutano yao kwa mujibu wa taratibu na Katiba zao, na wale ambao muda umefika wafanye hivyo haraka.

TENGA APONGEZA WACHEZAJI, SERIKALI USHINDI WA STARS

Na Boniface Wambura
RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga
ameipongeza wachezaji wa Taifa Stars na benchi lao la ufundi, washabiki, mdhamini na Serikali kwa kufanikisha ushindi wa jana.

Tenga amesema ushindi huo umetokana na ushirikiano kutoka kwa wadau wote, na hasa wachezaji walioonesha kiwango kikubwa kulinganisha na mechi zilizopita ikiwemo kiwango cha kujituma uwanjani.

Amesema Serikali ni mdau mkubwa wa mpira wa miguu katika miundombinu, usalama na idara zake mbalimbali ikiwemo Uhamiaji ambayo imefanikisha kwa kiasi kikubwa kuwepo kwa mechi hiyo ambapo Taifa Stars iliifunga Morocco mabao 3-1.

MECHI YA TAIFA STARS YAINGIZA MIL 226/


Na Boniface Wambura
PAMBANO la mchujo la Kombe la Dunia  kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Morocco (Lions of the Atlas) lililochezwa jana (Machi 24 mwaka huu) na Stars kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 imeingiza sh. 226,546,000.

Fedha hizo zimepatikana kutokana na watazamaji 32,614 waliokata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio cha sh. 5,000, sh. 7,000, sh.10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.

Mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh. 34,557,864.41, maandalizi ya mchezo sh. 28,450,000 wakati wa gharama za uchapaji tiketi ni sh.
8,625,641.88.

Nyingine ni bonasi kwa timu ya Taifa Stars sh. 28,798,220.34, asilimia 15 ya uwanja sh. 18,917,141.01, asilimia 20 ya gharama za mechi sh.25,222,854.67 na asilimia 5 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika
(CAF) sh. 6,305,713.67.

Asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) sh.71,885,135.82 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 3,783,428.20 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye mgawo wa TFF.

Friday, March 22, 2013

Niyonzima 'atikisa' kiberiti Jangwani


Haruna Niyonzima
KIUNGO wa kimataifa wa Yanga, Haruna Niyonzima, amesema kuwa atakuwa tayari kusaini mkataba mpya wa kuichezea Yanga katika msimu ujao wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara endapo watampa dola za Marekani 150,000 (Sh. milioni 240).
Mkataba wa Niyonzima aliyejiunga na Yanga mwaka juzi akitokea APR ya Rwanda unamalizika mwezi Juni mwaka huu.
Akizungumza kwa njia ya simu kutoka kwao Kigali, Rwanda ambako amekwenda kuitumikia nchi yake inayokabiliwa na mechi dhidi ya Mali Jumapili, Niyonzima, alisema hataki kurudia makosa aliyofanya mwaka jana.
Niyonzima alisema anaamini kuwa hicho kiwango cha fedha ndiyo dau lake kwa sasa au zaidi na ameamua kuwaambia Yanga kutokana na hatua yao ya kukataa kumruhusu mwaka jana kujiunga na El Mereikh ya Sudan iliyokuwa imekubali kumlipa kiasi hicho.
Kiungo huyo ambaye ni nahodha wa timu ya taifa lake (Amavubi), aliongeza kuwa hivi sasa kazi ya kuzungumzia mkataba wake itafanywa na wakala wake.
"Mambo nahitaji yafanyiwe kazi kabla sijaamua kuendelea kubaki Yanga, ikiwamo kuongezewa mshahara,'' alisema Niyonzima.
Kiungo huyo kipenzi cha mashabiki wa Yanga aliongeza kuwa hataki kupoteza nafasi kama ilivyokuwa miaka ya nyuma wakati alipokuwa akiichezea APR ambao hawakuwa tayari kumruhusu kirahisi kuondoka ndani ya timu hiyo inayotetea ubingwa wake wa ligi Kuu ya Rwanda.
Akizungumzia matakwa hayo ya Niyonzima, Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Seif Ahmed, alisema jana kuwa wako katika mipango ya kuwapa mikataba mipya wachezaji wao wote wanaowahitaji kuendelea kuwa nao kabla ya kumalizika kwa ligi.
Hata hivyo, Ahmed alisema hawawezi kusema ni lini watakamilisha kazi hiyo kwani hiyo ni mipango ya viongozi wa klabu kwa kushirikiana na benchi kao la ufundi.
Niyonzima na Mrisho Ngassa wa Simba waliivutia El Mereikh baada ya kuonyesha kiwango kizuri katika mashindano ya Kombe la Chalenji yaliyofanyika mwaka jana nchini Uganda lakini Ngassa aliamua kuikacha timu hiyo kwa madai kwamba anazingatia maslahi yake na siyo kukimbilia kucheza nje. Nafasi ya nyota hao ilichukuliwa na Selemani Ndikumana kutoka Interclub ya Burundi.


CHANZO:NIPASHE.

Rais Kikwete azindua Complex ya Azam na kuzipiga 'dongo' Simba, Yanga


 Rais Jakaya Kikwete akizindua rasmi Jiwe la Msingi wa Uwanja wa Azam Complex. (Picha na Habari Mseto Blog)
Rais Jakaya Kikwete akiwa kwenye Uwanja mwingine wa Azam ambao bado upo kwenye matengenezo
 Rais Jakaya Kikwete akikata utepe,wakati wa uzinduzi rasmi wa uwanja wa Azam Complex.
 Rais Jakaya Kikwete akiwapungia mkono  mashabiki wa Azam waliokuja kushuhudia uzinduzi rasmi wa uwanja wa Azam Complex,baada ya kuuzindua rasmi uwanja huo.
 Rais Jakaya Kikwete,akiwa kwenye chumba cha kufanyia mazoezi kwenye Uwanja wa Azam Complex,baada ya kuuzindua rasmi.
 Rais Jakaya Kikwete,akiwa kwenye chumba cha kufanyia mazoezi kwenye Uwanja wa Azam Complex,baada ya kuuzindua rasmi.
Rais Jakaya Kikwete akiwa kwenye Uwanja mwingine wa Azam ambao bado upo kwenye matengenezo.
 
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete alipigwa na butwaa baada ya kufika katika makao makuu ya klabu ya Azam yaliyopo Mbande jijini Dar es Salaam jana na kujionea uwekezaji mkubwa uliofanywa katika kujenga miundombinu ya kisasa ya timu hiyo.
Rais Kikwete ambaye alikuwa amefuatana na Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, mkewe Mama Salma Kikwete na viongozi mbalimbali wa serikali, aliweka jiwe la msingi kuashiria kuzinduliwa rasmi kwa uwanja wa klabu hiyo wa uitwao Azam Complex, kisha akatembezwa kuiona miradi mbalimbali ya wawakilishi hao pekee wa Tanzania waliobaki mwaka huu katika michuano ya klabu ya Afrika.
Akizungumza baada ya kuzindua uwanja huo na kuona utekelezaji wa mipango ya Azam ikiwamo ya kulea vijana wenye vipaji vya soka, rais Kikwete aliupongeza uongozi wa klabu hiyo na kuzipa changamoto klabu kongwe za Simba na Yanga kujifunza kutoka kwao.
Kikwete pia aliipongeza Azam kwa kuwa timu pekee ya Tanzania iliyobakik katika michuano ya kimataifa baada ya Simba na Jamhuri kutolewa katika hatua ya kwanza ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika huku timu hiyo iliyokamata mnafasi ya pili msimu uliopita ikifuzu kwa raundi ya tatu ya michuano ya Kombe la Shirikisho.
"Azam wamekuwa na mchango mkubwa katika kuendeleza soka nchini na timu yao sasa ni timu kigogo. Simba na Yanga sasa wanalazimika kujipanga zaidi wanapocheza na timu hii," alisema Kikwete.Akieleza zaidi kuhusu Simba Yanga, rais Kikwete alisema kuwa licha ya kuwa 'mnazi' wa mojawapo miaka iliyopita, klabu hizo zinakabiliwa na matatizo mengi yakiwamo ya tuhuma za ushindi wa kununua, imani za kishirikiana na kukosa viongozi makini.
"Klabu hii (Azam) haina wanachama wengi kama baadhi ya klabu nyingine ambazo wanachama wake wanagombana kila kukicha. Viongozi wa Azam msibweteke kama hawa jamaa kwa kutegemea kamati za ufundi (ushirikina)… hakuna uchawi katika mpira. Kama uchawi ungelikuwa unacheza mpira, Afrika tungelikuwa tumeshatwaa Kombe la Dunia. Ni upuuzi kuwekeza kwenye kamati za ufundi," alisema Kikwete.
"Wapo watu wanawekeza kwenye kusajili wachezaji kila mwaka. Ukifuatilia vizuri, wachezaji wanasajiliwa si kwa sababu wanahitajika, bali wasichukuliwe na timu nyingine, mpira hauko hivyo. Wekeza kwa vijana kwa kuhakikisha wanakula na kulala vizuri. Unakuta kiongozi hajui mchezaji anakula nini na analala wapi.
"Timu hii (Azam) inaendeshwa bila kutegemea wanachama wanaokimbilia kupiga kura kwa kuhongwa. Itakuwa timu kubwa sana, labda mshindwe wenyewe kwa kuamua kutumiwa. Mkikubali kuwa kivuli cha timu yoyote ili kuisaidia, mtashindwa."
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa kampuni za Bakhresa (SBB) wanaomiliki Azam, Aboubakar Bakhresa, alimshukuru rais kwa kukubali kushiriki uzinduzi wa uwanja huo wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 7,000.
Alisema imewagharimu Sh. milioni 800 kulinunua eneo walilojenga uwanja huo, ofisi na hosteli za wachezaji na kwamba awamu ya kwanza ya ujenzi wa miundombinu hiyo tayari imeshawagharimu takriban Sh. bilioni tatu.
Azam ilianzishwa mwaka 2004 ikiwa na muungano wa timu za viwanda vitatu vya SSB. 2005 ilipanda dara la tatu, daraja la pili (2006), la kwanza (2007) na ilitinga Ligi Kuu ya Tanzania Bara 2008.
Hivi sasa, Azam ambayo haijawahi kushuka daraja tangu ipande ligi kuu, inakamata nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, ikiwa na pointi 37 baada ya kucheza mechi 19, pointi 11 nyuma ya vinara Yanga walioshuka dimbani mara 20.
Novemba mwaka jana, mshindi mara tatu wa zamani wa tuzo ya mwanasoka bora wa Afrika, Abedi Pele alipigwa butwaa pia alipofika Mbande na kukiri kuwa amevutiwa mno na jitihada za klabu hiyo katika kukuza soka la vijana.

 

Thursday, March 21, 2013

Mnamibia, Mtswana washindwa kutambiana IBF



LILE Pambano lililokuwa likisubiriwa kwa hamu na watu wengi wa kumpata Mfalme wa  wa bantam wa kimataifa kati ya mabondia Immenuel Naidjala a.k.a Prince kutoka Namibia na Lesley Sekotswe kutoka Botswana haukuweza kutoa mshondi baada ya matokeo ya majaji wawili kumpa kila mmoja ushindi wana jaji wa tatu kutoa draw.
Pambano hili lilikuwa limeandaliwa na kampuni ya Sunshine Promotions ya bwana Nestor Tobias na lilikuwa na kila aina ya hamasa baada ya mabondia wote wawili kuonyesha ufundi wa kurusha makonde. 
Rais wa IBF kutoka Afrika, Ghuba ya Uajemi na mashariki ya Kati Mtanzania Onesmo Ngowi ambaye alikuwa ndiye msimamizi mkuu wa mpambani huu alitangaza kuwa mabondia wote wawili watakutana tena baada ya kipindi cha mapumziko ya mwezi mmoja ili kuweza kumpata mshindi wa mkanda huo ambaoni watatu kwa umaarufu katika mukanda ya ngumi. Mkanda wa kwanza kwa umaarufu ni wa ubingwa wa dunia. Mkanda wa tatu ni wa ubingwa wa mabara na mkanda wa tatu ni wa ubingwa wa kimataifa ambao ndio uliokuwa unagombewa na mabanodia hao. 
Wakazi wengi wa jiji la Widhoek na miji mingine ya jirani pamoja nan chi za jirani walijazana katika hotel ya Widhoek Country Club and Casino kuushughudia mpambani huo ambao ulikuwa na kila aina ya hamasa.

Mumbara aita mashabiki Stars v Morocco


Castor Mumbara alipokuwa akicheza 3 Star ya Nepal
KIUNGO Mshambuliaji wa timu ya Coastal Union, Castor Mumbara amewaomba mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi uwanjani Jumapili ili kuishangilia Taifa Stars itakayocheza dhidi ya Morocco.
Timu hizo zitaumana kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam katika pambano la kuwania kucheza Fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwakani nchini Brazil.
Mumbara aliyewahi kuichezea timu za Moro Utd, Toto African, Yanga na Taifa Stars, alisema kujitokeza kwa wingi kwa mashabiki na kuiunga mkono Stars kuisaidia kupata ushindi dhidi ya wageni.
Alisema mbali na kuwahimiza mashabiki kujitokeza kwa wingi, pia aliwataka wachezaji wa Stars kuhakikisha wanapigana kiume uwanjani kuhakikisha wanaitoa kimasomaso Tanzania.
Mumbara aliyewahi kucheza soka la kulipwa katia klabu za 3 Star na Himalayan Sherpa, alisema kujituma kwa wachezaji uwanjani na mashabiki kuishangilia mwanzo mwisho kutaipa timu ushindi.
"Stars ikipewa sapoti na wachezaji wakijituma uwanjani inaweza kuwa silaha ya ushindi dhidi ya Morocco na kuisaidia kujiweka pazuri katika mbio za kwenda Brazil," alisema.Mumbara alisema Stars ina nafasi ya kwenda kwenye WC2014 iwapo itaungwa mkono mwanzo mwisho kwa mechi zilizosalia za kundi lake la C licha ya kuchuana na timu vigogo.
Stars inayoshika nafasi ya pili kwa sasa ikiwa na pointi tatu inahitaji ushindi Jumapili mbele ya Morocco ili kuzidi kuifukuzia Ivory Coast wanaoongoza kundi hilo kwa pointi nne ambapo Jumamosi itakuwa uwanjani kuumana na wanaoburuza mkia, Gambia.
Kikosi cha Morocco ambacho kitakuja bila nyota wake Marouane Chamakh anayekipiga West Ham kwa mkopo akitokea Arsenal kinatarajiwa kutua nchini kesho tayari kwa pambano hilo.

WASHTAKIWA 52 KESI YA PONDA WAHUKUMIWA KWENDA JELA

Washtakiwa 52 kati ya 54 katika kesi ya kula njama na kufanya maandamano isivyo halali wamehukumiwa kwenda jela kila mmoja baada ya kukutwa na makosa matatu huku mmoja akiachiwa huru baada ya kukutwa hana hatia na mwingine kufariki dunia kabla ya hukumu iliyotolewa leo na hakimu Sundi Fimbo wa Mahakama ya Hamimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam.  
  
Washtakiwa hao walidaiwa kutenda kosa Februari 15 mwaka huu.

Baada ya pande zote kusikilizwa na washtakiwa kutoa hoja za utetezi, hatimaye hakimu Fimbo alitoa hukumu hiyo leo ambapo aliwatia hatiani washtakiwa 52 kwa makosa matatu kati ya manne na kila mmoja akamhukumu kwenda jela mwaka mmoja kwa kila kosa.

Hata hivyo, Fimbo akasema washtakiwa hao watakwenda kutumikia kifungo cha mwaka mmoja jela kwa vile adhabu zote zinakwenda kwa pamoja.

Mshtakiwa aliyeachiwa huru baada ya kukutwa kuwa hana hatia ni Waziri Omari (namba 48), ambaye katika utetezi wake alidai kwamba siku ya tukio alikamatwa wakati akiwa katika shughuli zake za biashara ya kuuza kwa kutembeza barabarani vyombo vya nyumbani ikiwa ni pamoja na mabeseni.

Kabla ya kutolewa kwa hukumu hiyo leo, wakili Mohamed Tibanyendera alimtaka hakimu awapunguzie adhabu wateja wake kwavile wengi wao wanategemewa na familia zao na kwamba, tayari walishakaa mahabusu kwa kipindi cha zaidi ya mwezi mmoja.

Washtakiwa katika kesi hiyo walikuwa ni Salum Makame, Said Idd na Ally Nandumbi, Makame, Idd na Nandumbi, Hussein Athumani, Seif Rwambo, Abdull Ally, Waziri Swed, Naziru Waziri, Ahmad Rashid, Jumanne Kayogola, Hamis Tita, Amri Diyaga, Salum Said, Rajabu Mpita na Haji Sheluhenda.

Wengine ni Abdul Ahmed, Bakari Mwambele, Ramadhani Fadhili, Awadh Juma, Omari Mkwau, Kassim Chobo, Abubakari Bakari, Ramadhani Milambo, Hamis Ndeka, Athuman Juma, Abdallah Salum, Juma Makoti, Bashir Kakatu, Imam Omari, Rashid Lukuta na Bakari Athumani, Mbwana Kassim, Nurdin Ahmed, Mustapha Mide, Rajabu Kifumbo, Zuberi Juma, Omari Mkandi, Idrisa Katulimo, Sawali Mola, Said Dudu, Ramadhani Juma, Musa Sinde, Issa Sobo, Yahaya Salum, Jabil Twahil, Shomari Tarimo, Hashim Bendera, Waziri Toy, Athuman Yahaya, Yasin Seleman, Shaban Malenda, Yasin Mohamed, Khatib Abdallah na Rajabu Rashid wote wakazi wa jijini Dar es Salaam.

Awali, ilidaiwa kuwa katika siku ya tukio, wilaya ya Ilala, jijini Dar es Salaam, washtakiwa wote kwa pamoja walikula njama za kufanya maandamano isivyo halali.

Shitaka la pili, ilidaiwa kuwa siku na eneo la tukio la kwanza, washtakiwa walifanya mkusanyiko usio halali kwa lengo la kusababisha uvunjifu wa amani.

Wakili wa Serikali Mwandamizi, Benard Kongola, alidai katika shitaka la tatu kuwa siku na eneo la tukio la kwanza na la pili, washtakiwa wote kwa pamoja baada ya Jeshi la Polisi kutoa zuio la kufanya maandamano, walikiuka amri hiyo na kufanya mkusanyiko ulisababisha vurugu na uvunjifu wa amani.

Katika shitaka la nne, ilidaiwa kuwa mshtakiwa Makame, Idd na Nandumbi, waliwashawishi wananchi kwa kuwasambazia vipeperushi vya kuhamasisha kufanya maandamano yasiyo halali.

VILIO, SIMANZI
Baada ya kutolewa kwa hukumu hiyo, vilio vilitawala katika viunga vya mahakama vilivyofurika watu kufuatia baadhi ya ndugu na jamaa wa washtakiwa kuangua kilio, wasiamini kile kinachotokea.

Baadaye washtakiwa walipandishwa kwenye karandinga na kupelekwa gerezani.

JANA ILIKUWA NDIYO 'BIRTHDAY' YA MAREHEMU SHARO MILIONEA

Kaburi la marehemu sharo milionea

''Masai Nyotambofu na Na Alex wa machejo A.k.a Ngekewa, wakitazama picha za marehem Sharo milionea kwenye simu.
''Masai Nyotambofu akimbembeleza Shilole Baada ya kulia.

Tunda man akiwa na mama yake marehemu sharo siku ya arobaini tanga muheza

Rais wa TAFF  mwakifamba Pamoja na mwenyekiti wa chama cha comed KITALE wakiongea na wasanii baada ya arobaini ya sharo muheza tanga.
Kushoto ni Kambangwa wa Jakaya thietre akifuatiwa na Asha Boko wa VITUKO SHOW Dogo Janja pamoja na Safina wa MIZENGWE.
RAIS WA TAFF Mwakifamba Akigonga msosi na Masai Nyotambofu Pamoja na Wasanii wengine kibao.
Masai Nyotambofu akigonga msosi.
Camera man wa VITUKO SHOW ''Yosso Komando'' Akigonga msosi na Dogo Janja na wengineo.
Wasanii wakiliangalia kaburi la sharo milionea na kumkumbuka
Mchekeshaji mahiri alieiteka jamii kwa kuigiza lafudhi ya kabila la wamasai nchini, Gilliady Severine ''Masai Nyotambofu'' wa VITUKO SHOW akiwa na mchekeshaji machachari Joti wa ORIGINAL COMEDY wakiwa maeneo ya muheza nyumbani kwao marehem Sharo Milionea siku ya Arobaini.
Shilole akilia kwenye kaburi la marehem sharo milionea

 

Yosso wa Simba wafanya 'Mauaji' Singida

C

Yosso wa Simba (ukiondoa Amri Kiemba kulia) wakishangilia bao lililofungwa na Haroun Chanongo katika mechi dhidi ya Coastal. Picha ya Maktaba.

Na Princess Asia
KATIKA kujiandaa na mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Kagera Sugar mjini Bukoba Jumatano, Wekundu wa Msimbazi, Simba SC leo wamecheza mchezo wa kirafiki mjini SIngida na kutoa adhabu kali ya kipigo cha mabao 4-0 kwa wenyeji, Singida United.
Katika mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida, mabao ya mabingwa hao wa Bara, yalitiwa kimiani na Rama Kipalamoto, Mselemu Salum, Omar Waziri ‘Inzaghi’ na Ramadhani Singano ‘Messi’.
Simba SC ambayo imewapumzisha wachezaji wake wengi wa kikosi cha kwanza na kuamua kutumia chipukizi waliopandishwa kutoka kikosi cha pili, leo ilicheza soka ya kuvutia mno.
Mashabiki wa soka mjini Singida walikuwa wakishangilia kwa nguvu burudani ya soka ya ‘Kibareclona’ na kupiga kelele timu hiyo iachane na magwiji wasio na nidhamu na kuwekeza zaidi kwa yosso hao.
Kocha Mfaransa, Patrick Liewig alitoa pendekezo la kutolewa kwa wachezaji ‘mafaza’ katika kikosi chake, kwa kuwa hawamsikilizi.
Miongoni mwa waliotengwa ni wachezaji hodari na vipenzi vya mashabiki kama Amir Maftah, Juma Nyosso, Haruna Moshi ‘Boban’ na Mwinyi Kazimoto.
Wachezaji hao makinda walicheza mechi ya kwanza ya Ligi Kuu wiki mbili zilizopita dhidi ya Coastal Union ya Tanga na kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Sasa timu hiyo inaelekeza nguvu zake katika mechi mbili za kanda ya Ziwa, ikianza na Kagera na baadaye Toto African mjini Mwanza wiki ijayo, huku wapenzi wengi wakiwa na imani na yosso wao hao. 
Kwa sasa, Simba SC inashika nafasi ya tatu katika Ligi Kuu, ikiwa na pointi 34, tatu nyuma ya Azam FC inayoshika nafasi ya pili wakati Yanga SC wapo jirani kabisa na ubingwa kwa pointi zao 48 ligi ikiwa imebakiza mizunguko sita kutia nanga.
Simba SC inapambana hata kama itapoteza ubingwa, basi iipiku Azam FC katika nafasi ya pili.
Katika mchezo wa leo, kikosi cha Simba kilikuwa; Abuu Hashim, Haruna Shamte, Waziri Omar, Hassan Hassan, Hassan Khatib, Jonas Mkude, William Lucian ‘Gallas’/Said Mangela, Mselem Salum, Christopher Edward, Ramadhani Singano ‘Messi’ na Marcel Kahezya/Haroun Chanongo.

IMEHAMISHWA:BIN ZUBEIRY

Banka ataka TFF ifuatilie nyota waliopo nje ya nchi

Mohmmed Banka (kulia)
KIUNGO wa kimataifa wa Tanzania anayecheza soka la kulipwa nchini Kenya, Mohammed Banka amesema ipo haja ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kufuatilia nyendo za wachezaji wa kitanzania wanaocheza nje ya nchi ili waweze kupata fursa ya kulitumikia taifa lao katika mechi za kimataifa.
Banka anayeichezea timu ya Ligi Kuu ya Kenya, Bandari ya Mombasa, alisema nje ya nchi wapo wachezaji wanaofanya vyema nje ya nchi lakini hawapati nafasi ya kuitwa timu za taifa kwa vile hawafuatiliwi kwa ukaribu na shirikisho la kandanda nchini.
"Nadhani kuna haja TFF ijenge utamaduni wa kuwafutilia wachezaji wao wanaocheza soka nje ya nchi kwa vile wapo wanaoweza kuwa msaada wa timu za taifa, lakini hawapati nafasi kwa vile hawafuatiliwi," alisema.
Alisema utamaduni wa kuwafuatilia wachezaji waliopo nje unaweza kuwa msaada mkubwa wa soka la Tanzania kwa sababu mchanganyiko huo unaweza kufanya Stars kuwa na kikosi imara.
Kwa sasa Stars imekuwa ikiwatumainia mchango wa nyota wanaocheza soka la kulipwa katika klabu ya TP Mazembe ya DR Kongo, Mbwana Samatta na Thomas Ulimwengu, huku wengine wakishindwa kuitwa kwa sababu mbalimbali ikiwemo kucheza ligi zisizo na umaarufu na kutofuatiliwa maendeleo yao.

Kamanda Andengenye kuzishuhudia Golden Bush v Wahenga Pasaka

Kamanda Thobias Andengenye

KAMANDA wa zamani wa Polisi wa Mikoa ya Morogoro na Arusha ambaye kwa sasa amehamishiwa Makao Makuu jijini Dar es Salaam, Afande Thobias Andengenye anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika pambano la soka la 'wazee' kati ya Golden Bush Veterani na Wahenga Fc.
Pambano la wapinzani hao wa jadi linatarajiwa kufanyika siku ya Pasaka kwenye uwanja wa TP Afrika, Sinza, Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Mlezi na Msemaji wa Golden Bush, Onesmo Waziri 'Ticotico', Kamanda Andengenye amethibitisha kuwa mgeni rasmi wa pambano hilo litakalochezwa saa 10 jioni siku hiyo ya Pasaka.
Ticotico, alisema walithibitishwa na kamanda huyo jana na hivyo kupata faraja kubwa ya kuona kamanda huyo kulishuhudia pambano hilo la wapinzani hao wa jadi.
Macocha Mayay wa  Wahenga, akiwaburuza wachezaji wa Golden Bush walipokutana mara ya mwisho Janurai 12, 2013 na Golden Bush kushinda mabao 4-3 na kulipa kisasi cha kipigo kama hicho walichopewa na wapinzani wao Desemba 31, 2012.

"Kamanda Thobias Andengenye ametuthibitishia kuwa mgeni rasmi katika pambano letu dhidi ya Wahenga litakalochezwa siku ya Pasaka," alisema Ticotico.
Ticotico alisema katika kujiweka fiti zaidi kabla ya kuvaana na wapinzani wao hao Jumamosi wanatarajia kushuka dimbani tena kuuvaana na Kijitinyama Veterani katika uwanja wa Bora.
"Katika kujiweka vyema zaidi kabla ya kuwaangushia kipigo Wahenga, Jumamosi tutacheza mechi ya mwisho ya kujipima nguvu dhidi ya Kijitonyama Veterani pale kwenye uwanja wa Bora," alisema Ticotico.
Wahenga inayotambia wachezaji kadhaa nyota kama akina Mengi Matunda, Yona Babadimo na wengine na Golden Bush yenye nyota wa zamani wa Simba na Yanga, kama akina said Swedi, Yahya Issa, Wisdom Ndlovu, Athuman Machuppa na wengine hilo litakuwa pambano lao la nne baada ya awali kuvaana mara tatu na kutambiana mara moja moja na mechi yao nyingine kutoka sare ya bao 1-1.

SERIKALI  SASA YARIDHIA UCHAGUZI WA TFF, KWA KATIBA IPI...SIRI!

Leodegar Tenga, Rais wa TFF

SERIKALI imekubali mchakato wa uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) uendelee kwa sharti la kuhakikisha haki inatendeka kwa wagombea waliofika mbele ya Kamati ya Rufani ya Uchaguzi.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mchana, Rais wa TFF, Leodegar Tenga amesema uamuzi huo umefikiwa kwenye kikao kati ya uongozi wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo chini ya Waziri Dk. Fenella Mukangara, TFF na Baraza la Michezo la Taifa (BMT).

Amesema baada ya maafikiano hayo, TFF italiandikia barua Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) ambalo ndilo lililosimamisha mchakato huo ili litume ujumbe wake kwa ajili ya kusikiliza malalamiko ya wagombea walioenguliwa.

Rais Tenga ambaye ameishukuru Serikali kwa kuruhusu mchakato huo uendelee, pia ameahidi kuwa uchaguzi wa TFF utafanyika kabla ya Mei 25 mwaka huu kama walivyokubaliana na Serikali, na kuwa haki si tu itatendeka bali ionekane imetendeka.

“Serikali imetuelekeza uchaguzi ufanyike kabla ya Mei 25. Tumewaambia kwetu huko ni mbali. FIFA wakija hata kesho wakituambia endeleeni sisi tuko tayari. Hesabu zetu ziko tayari, makabrasha yote yako tayari yanasubiri mkutano tu. Labda itakuwa kutoa muda tu kwa wajumbe walioko mbali waweze kujiandaa, maana wajumbe huwezi kuwaita ghafla,” amesema.

Amesisitiza kuwa TFF ilishapanga tarehe ya uchaguzi, lakini ukasimamishwa na FIFA baada ya baadhi ya walioenguliwa kulalamika huko. Hivyo maneno kuwa TFF hawataki uchaguzi kwa sababu wanataka kuendelea kubaki madarakani haya maana hata kidogo.

Hivyo amewataka wagombea wote waliofika kwenye Kamati ya Rufani ya Uchaguzi na wakaendelea kujiandaa vizuri, kwani FIFA watakapofika watawasikiliza wao na vyombo vilivyowaengua.

Pia amesema TFF ina heshimu Serikali na itaendelea kufanya hivyo, lakini vilevile lazima iheshimu FIFA sababu iko kwenye mpira wa miguu, na FIFA ndiyo wasimamizi wa mchezo huo duniani. 

Amewakumbusha wanachama wa TFF, hasa wajumbe wa Mkutano Mkuu kufahamu kuwa TFF ina katiba, lakini ni lazima pia wafahamu kwanini kuna FIFA.

Rais Tenga amewahadharisha watu wanaopitapita mikoani kuomba saini za wajumbe ili kuita Mkutano Mkuu wa dharura wakati wanajua mkutano ulishaitishwa, lakini ukasimamishwa na FIFA. Jambo hilo kikatiba ni kosa.

TUZO ZA MUZIKI ZA KILI 2013 ZAZINDULIWA

Katikati ni Kushilla Thomas Mkurugenzi wa Masoko wa TBL kulia na Godfrey Mungereza Kaimu Katibu Mtendaji wa BASATA kushoto pamoja na Maofisa wa TBL na BASATA wakifurahia jambo mara baada ya kuzinduliwa rasmi kwa tuzo za Kilimanjaro Tanzania Music Awards 2013 sambamba na nembo ya tuzo hizo. Hafla hiyo imefanyika jijini Dar es salaam  (Picha: Executive Solutions)
Kushilla Thomas Mkurugenzi wa Masoko wa TBL akibadilishana hati na Godfrey Mungereza Kaimu Katibu Mtendaji wa BASATA baada ya kusainiwa kwa mkataba wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager kudhamini tuzo za Kilimanjaro Tanzania Music Awards kwa miaka mingine mitano mpaka 2018 sambamba na uzinduzi wa tuzo hizo kwa mwaka 2013 huku viongozi wengine wa TBL na BASATA wakipiga makofi. Hafla hiyo imefanyika jijini Dar es salaam jana.(Picha: Executive Solutions)

TUZO za muziki maarufu kama Kilimanjaro Tanzania Music Awards 2013 zimezinduliwa jana jijini Dar es Salaam zikiwa na dhumuni kubwa la kutambua wasaniii waliopata mafanikio katika sekta ya muziki kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita.

George Kavishe, Meneja wa  kinywaji cha Kilimanjaro Premium Lager amesema wakati wa uzinduzi huo kuwa, “Kilimanjaro Premium Lager inajivunia kuendelea kudhamini  tuzo hizi kwa mara ya 12 sasa lengo likiwa kukuza muziki nchini Tanzania. Mchakato wa kuwapata wanamuziki bora wa mwaka unaanza leo na utamalizika tarehe 8 Juni ambapo tutakuwa na hafla ya usiku maalum wa kwa ajili ya kutangaza washindi.”

Alisema Kilimanjaro Premium  Lager imejizatiti kuendeleza tasnia ya muziki Tanzania kwa kutambua na kuwapa tuzo wasanii wenye vipaji. ‘Tunataka  wanamuziki  wetu wajisikie wanathaminiwa na kutambuliwa kwa kazi nzuri wanayoifanya  vile vile tunataka Watanzania  waweze kuthamini muziki wa nyumbani na kutambua mchango wa wanamuziki katika kuleta maendeleo ya uchumi katika nchi.

‘’Kilimanjaro Premium Lager inajivunia  kuwa sehemu ya tuzo hizi na ni matumaini yetu kua mwaka huu tukio hili litakua kubwa na zuri zaidi’’

‘’Pia tuna furaha kutangaza  kwamba BASATA imetupatia leseni ya kuendelea kudhamini tuzo hizi kwa kipindi cha miaka mingine mitano. Kusainiwa kwa mkataba mpya na BASATA ni uthibitisho wa azma kubwa tuliyonayo katika kuendeleza muziki wa Tanzania. Mkataba huu utaifanya Kilimanjaro Premium Lager kuwa mdhamini wa tuzo hizi mpaka mwaka 2018.

KILIMANJARO WAHIMIZA MASHABIKI MECHI STARS v MOROCCO

Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager inayodhamini Timu ya Taifa (Taifa Stars), George Kavishe, akibadilishana mawazo na wachezaji wa Taifa Stars wakati wa chakula cha jioni kilichoandaliwa na Kilimanjaro Premium Lager Jumanne usiku.



Na Mwandishi wetu
Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, George Kavishe amesema sasa hivi Timu ya Taifa (Taifa Stars) inauzika na kwamba watanzania wamerudisha imani katika timu hiyo.

Kavishe ambaye Bia yake ndio inadhamini Taifa Stars ameyasema hayo juzi usiku wakati wa chakula cha jioni pamoja na wachezaji wote na benchi la ufundi kilichoandaliwa kwa hisani ya Kilimanjaro Premium Lager ili kuwakaribisha wachezaji kambini.

Alisema wao kama wadhamini wamefarajika na matokeo ya Taifa Stars mpaka sasa na kuwa mwenendo ni mzuri na unaridhisha.

“Watanzania wengi sasa hivi wamerudisha imani katika timu hii kwa hivyo msiwaangushe,” alisema Kavishe na kusisitiza kuwa kwa sasa hivi Taifa Stars inauzika.

Alisema ushindi katika mechi ya Jumapili dhidi ya Morocco kutafuta nafasi ya kufuzu kucheza katika Kombe la Dunia mwakani Brazil ni lazima na ni muhimu pia kupata ushindi katika mechi ya marudiano mwezi Juni.

Aliwaomba watanzania wajitokeze kwa wingi kuishangilia timu yao kama walivyofanya wakati wa mechi  dhidi za Zambia na Cameroon.

Alimpongeza Kocha Kim Poulsen kwa kazi nzuri anayoifanya na kusisitiza kwamba anawapa watanzania burudani kwa kuleta ushindi.

“Kocha ameniambia ameiona Morocco ikicheza na wachezaji wake nyota na bila wachezaji nyota kwa hivyo ana mbinu zote za kuikabili Morocco Jumapili…yeye ameshafanya kazi yake ya intelijensia kwa hivyo tusimuangushe,” alisema Kavishe.

Naye kocha Kim Poulsen alisema wachezaji wako katika hali nzuri na tayari kupambana Jumapili ili kuibuka na ushindi.

Alisema udhamini mkubwa na wa uhakika wa Kilimanajro Premium Lager umekuwa chachu kubwa sana katika mafanikio ya Taifa Stars.

“Sasa hivi tuna uhakika wa kambi, wachezaji wanalipwa kwa wakati na pia tunafarajika kuona kuwa mdhamini yuko karibu sana na timu na anaithamini,” alisema Poulsen.

Wachezaji wote 23 wamesharipoti kambini na wanaendelea na mazoezi kila siku ili kujiandaa na mechi dhici ya Morocco itakayochezwa Jumapili saa tisa katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Taanzania iko katika kundi moja na Ivory Coast, Gambia na Morocco. Kwa sasa Ivory Coast inaongoza kwa pointi 4, Tanzania 3, Morocco 2 na Gambia 1.