STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, December 18, 2013

Kumekucha Mapinduzi Cup 2014

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEidHqliFYSZOmDPW5hrFg2PMS_Vb8y2SyA_h5ntdlbc7p_ziipo7RjFOftfcIgjo6ppVjCmYDygeOYsb4S4e8zCpZauYKNhGgDLQsY2aZ-u1Nbeup5fgIxqSQSFzG_RM2M5JukfdvGsIX9u/s1600/1.jpg
Himid Mao kama nahodha wa Azam akipokea kombe la Mapinduzi mwaka huu. Je Azam watalipokjea tena mwakani visiwani Zanzibar?
KAMATI ya mashindano ya Kombe la Mapinduzi, imetangaza makundi na ratiba ya hatua ya awali ya michuano hiyo inayofanyika kuadhimisha miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar Januari mwakani.

Hata hivyo, ratiba hiyo haioneshi uwepo wa timu kutoka nchi za Vietnam, China na Oman ambazo awali ilitangazwa kuwa zimealikwa kushiriki patashika hizo.
Ratiba iliyotolewa na kamati hiyo, inaonesha kuwa jumla ya timu 12 zitaumana kuwania taji hilo, ambazo zimegawiwa katika makundi matatu, kila moja ikiwa na timu nne.


Timu hizo ni Mbeya City, Pemba Combine, Chuoni na URA kutoka Uganda ambazo zinaunda kundi A, huku kundi B likiwa na timu za Simba, KMKM, AFC Leopards ya Kenya pamoja na KCC kutoka Uganda.

Mabingwa watetezi wa michuano hiyo Azam FC watakuwa katika kundi C pamoja na makamu bingwa Tusker ya Kenya, Yanga SC na Unguja Combine.
Kwa mujibu wa ratiba hiyo, pazia la ngarambe hizo litafunguliwa Januari 1, 2014, kwa mechi mbili za kundi B katika uwanja wa Amaan, ambapo wakati wa saa 10:00 mabaharia wa KMKM watapambana na Manispaa ya jiji la Kampala (KCC).
Aidha saa 2:00 usiku, wekundu wa Msimbazi Simba SC, watakuwa kibaruani dhidi ya AFC Leopards.

Januari 2, 2014, kutakuwa na mechi nne, katika kila uwanja, kati ya Amaan Unguja na  Gombani Pemba, kutakuwa na michezo miwili.
Zile za Amaan, ni kati ya Azam FC na Unguja Combine (saa 10:00 jioni) na Yanga dhidi ya Tusker itakayorindima kuanzia saa 2:00 usiku, na huko Gombani shughuli itakuwa kati ya URA na Chuoni (kundi C) watakaovaana saa 8:00 mchana, huku Mbeya City ikitoana jasho na Pemba Combine, saa 10:00 jioni katika mchezo wa kundi A.

Fainali ya ngarambe hizo itapigwa uwanja Amaan Januari 12 wakati wa saa 2:00 usiku, ambayo ndiyo kilele cha maadhimisho ya sherehe za miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Tanzanite watua salama J'burg kuwavaa Wasauzi

Kikosi cha wachezaji 20 na viongozi tisa cha timu ya Tanzania ya wasichana chini ya miaka 20 (Tanzanite) kimewasili leo jijini Johannesburg tayari kwa mechi dhidi ya wenyeji Afrika Kusini (Batsesana).
Mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya pili kuwania tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia kwa wasichana wenye umri chini ya miaka 20 zitakazofanyika mwakani nchini Canada.
Tanzanite imefikia Millpark Garden Court Hotel tayari kwa mechi hiyo itakayochezwa Jumamosi katika Uwanja wa Dobsonville ulioko Soweto, Johannesburg kuanzia saa 9.30 alasiri kwa saa za Afrika Kusini.
Wachezaji wa Tanzanite walioko katika kikosi hicho ni Amina Bilali, Amina Hemed, Amisa Hussein, Anastaz Katunzi, Anna Mwaisula, Belina Nyamwihula, Donisia Minja, Fatuma Maonyo, Happiness Mwaipaja, Latifa Salum, Maimuna Kaimu, Najiat Idrisa, Neema Kiniga, Rehema Rhamia, Sada Hussein, Shelda Mafuru, Stumai Athuman, Tatu Salum, Theresa Kashilim na Vumilia Maarifa.

Viingilio Simba, Yanga vyatajwa

Simba
KIINGILIO cha chini kwenye mechi ya Mtani Jembe kati ya Simba na Yanga itakayochezwa Jumamosi (Desemba 21 mwaka huu) ni sh. 5,000. Kiingilio hicho ni kwa viti vya rangi ya kijani ambavyo ni 19,648.
Kwa upande wa viti vya rangi ya bluu kiingilio ni sh. 7,000, viti vya rangi ya chungwa itakuwa sh. 10,000, VIP C kiingilio ni sh. 15,000, VIP B itakuwa sh. 20,000 wakati VIP A yenye viti 748 tu tiketi moja itapatikana kwa sh. 40,000. 
Tiketi zitaanza kuuzwa siku moja katika vituo mbalimbali, mchezo huo utafanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.
Vituo ambavyo tiketi hizo zitauzwa keshokutwa (Ijumaa) ni Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala, Uwanja wa Uhuru, na BMM Salon iliyoko Sinza Madukani.
Mechi hiyo itachezeshwa na Ramadhan Ibada (Kibo) kutoka Zanzibar, ambapo atasaidiwa na Ferdinand Chacha wa Bukoba, na Simon Charles kutoka Dodoma. Mwamuzi wa akiba ni Israel Nkongo wa Dar es Salaam wakati mtathimini wa waamuzi ni Soud Abdi wa Arusha.

Homa ya mpambano wa Msondo na Sikinde yazidi kupanda

* Sikinde yajichimbia mjini Bagamoyo
* Msondo washindwa kutaja kambi ilipo
Baadhi ya wanamuziki wa Sikinde

Baadhi ya waimbaji wa Msondo Ngoma
HOMA ya pambano la watani wa jadi katika muziki wa dansi nchini kati ya Mlimani Park 'Wana Sikinde' na Msondo Ngoma 'Baba ya Muziki' litakalofanyika siku ya Krismasi imeanza kupanda kwa bendi hizo kujificha kambini na huku wakipigana vijembe.
Bendi hizo kongwe nchini zinatarajiwa kuonyeshana kazi katika onyesho litakalofanyika kwenye viwanja wa TCC Club Chang'ombe, Temeke Dar es Salaam katika kunogesha sikukuu hiyo ya Krismasi.
Katika kuonyesha wamelipania pambano hilo bendi ya Sikinde tayari imeiendea Msondo wilayani Bagamoyo kwa ajili ya kuweka kambi yao na wamewatahadharisha 'mahasimu' wao hao wasije wakatoa visingizio baada ya kugaragazwa kwenye onyesho hilo.
"Sisi tumeamua kuweka kambi yetu mjini Bagamoyo ambako tutatua viwanja vya TCC kutokea huko ili kuisambaratisha Msondo, na tunataka wajipange sawasawa ili wasije wakatoa visingizio tena kwa maana kama vyombo vipya bendi zote imepewa na Konyagi," Katibu wa Sikinde, Hamis Milambo alisema.
Milambo alisema mashabiki wa dansi wajitokeze kwa wingi kushuhudia namna gani wanavyowachachafya wapinzani wao hao, ikizingatiwa hawajakutana kwa muda tangu mwaka jana.
Upande wa Msondo kupitia Meneja wao, Said Kibiriti, alisema hawana haja ya kutaja mahali kambi yao ilipo isipokuwa wamejiandaa kuwatoa nishai wapinzani wao siku ya onyesho hilo litakaloanza saa nane mchana.
"Sisi hatuna mchecheto wowote na mpambano huo, tunaendelea kujifua kimya kimya mahali ambapo siwezi kupataja kwa sasa," alisema Kibiriti.
Naye muimbaji anayekuja juu wa bendi hiyo ya Msondo alitokea Sikinde, Athuman Kambi, alisema amejipanga kuonyesha umahiri wake katika mpambano huo baada ya kufanya hivyo wakati akiwa Sikinde dhidi ya Msondo kwenye ukumbi wa Diamond na kuwawehusha mashabiki wa muziki wa dansi nchini.
"Najua watu watataka kuona nafanya kitu gani dhidi ya bendi yangu ya zamani iliyonitangaza vyema, wasiwe na hofu waje Desemba 25 waone nini nitakachofanya TCC Club Chang'ombe," alisema Kambi.
Mpambano huo wa Sikinde na Msondo umeandaliwa na kampuni ya Bob Entertainment na Keen Arts chini ya udhamini wa Konyagi, gazeti la NIPASHE, Integrated Communications, CXC Africa na Salute5.

Msanii Remmy Williams anayefanya kazi Italia atua Bongo

MSANII wa mziki wa bongo fleva Remmy Williams
MSANII wa mziki wa bongo fleva Remmy Will akiwasili nchini akitokea Italy

MSANII wa mziki wa bongo fleva Remmy Will  (kushoto ) akiwasili nchini akitokea Italy kulia ni meneja wake nchini Italy Wactor Fizio walipowasili nchini Tanzania

MSANII wa mziki wa bongo fleva Remmy Williams
MSANII wa mziki wa bongo fleva Remmy Williams katikati akilakiwa na baadhi ya warembo waliojitokeza kumpokea msanii huyo

MSANII wa mziki wa bongo fleva Remmy Williams akiwa ameshikwa mkono na meneja wake wa Tanzania Mcdennis Mgatha


Na Mwandishi Wetu
MSANII wa muziki wa kizazi kipya, Remmy Williams anayefanya shughuli zake za muziki nchini Italia ameingia nchini jana kwa ajili ya kufanya shughuli na wasanii wenzake wa nyumbani Tanzania.
Akizungumzia ujio wake mara baada ya kutua uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere Dar es salaam, msanii huyo aliyekuwa ameambatana na meneka wake toka Italia, alisema lengo lake ni kutaka kuona kazi za wasanii wa Tanzania zikitamba kimataifa.
"Nataka kazi za wasanii wenzangu zitambe na kuvuka mipaka ya Tanzania na kujitangaza kimataifa, naamini nitafanya nao kazi kwa ufanisi," alisema.
Remmy aliwaomba wasanii na wadau wa muziki nchini wampe ushirikiano wa kutosha kufanikisha lengo hilo ambapo akiwa nchini atarekodi kazi kwa kushirikiana na wasanii wa hapa nchini pamoja na kushirikia maonyesho mbalimbali ya pamoja.
Meneja wake wa hapa nchini, Mcdennis Mgatha, alisema Remmy amekuja pia kutambulisha nyimbo zake mpya pamoja na kutoa nyingine akishirikiana na wasanii wa Tanzania kabla ya kuanza kuzitambulisha katika maonyesho yatakayoandaliwa.

Meshack Abel asikitika kuikosa Simba


BEKI wa kati wa zamani wa Simba, Meshack Abel ameelezea kusikitishwa kwa kuikosa fursa ya kurejea kuchezea klabu hiyo ya Msimbazi.
Abel alikuwa katika mazungumzo na klabu ya Simba ili kurejea kikosini akitokea Bandari ya Kenya anakocheza soka la kulipwa kwa sasa, lakini mipango hiyo ilikufa kutokana na kubanwa na mkataba alionao na klabu yake hiyo ya Mombasa na Simba ikamsajili Donald Musoti kutoka Gor Mahia.
Akizungumza na MICHARAZO kutokea nchini Kenya, Abel anayetarajiwa kurejea nchini leo kwa mapumziko, alisema anasikitika kukosa nafasi ya kurejea tena Msimbazi, kwani alikuwa na hamu ya kuja kucheza soka nyumbani.
Hata hivyo, beki huyo aliyewahi kuzichezea timu za African Lyon, Ashanti United na Moro United, alisema ana matumaini ya kurejea kucheza nyumbani msimu ujao kwani mkataba wake na Bandari unakaribia kumalizika.
Abel alisema mkataba wake umebakisha miezi sita tu kabla ya kuisha na kudai kilikuwa kikwazo kunyakuliwa na Simba iliyokuwa ikisaka beki wa kati ya kuwasaidia mabeki waliopo sasa klabuni hapo, Joseph Owino na Gilbert Kaze.
"Mkataba wangu umesalia miezi sita na ulifanya mambo yasiende kama nilivyotarajia kutua Simba, lakini naamini msimu ujao nitarejea kucheza nyumbani baada ya kucheza nje kitambo tangu nije hapa Kenya," alisema.
Abel alikuwa akikipiga Bandari na Watanzania wengine akiwamo kiungo Mohammed Banka aliyerejea Tanzania na kujiunga Ashanti United, David Naftar na mshambuliaji nyota, Thomas Mourice waliosalia nchini humo.

Coastal Union kwenda Oman kuinolea makali JKT Oljoro

 
MABINGWA wa zamani wa kandanda nchini, Coastal Union ya Tanga wanatarajiwa kuondoka nchini Januari mosi kuelekea Oman kwa ajili ya kuweka kambi ya kuajindaa na duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Aidha kikosi hicho hakikusajili mchezaji yeyote katika dirisha dogo lililofungwa mwishoni mwa wiki badala yake imewapandisha wachezaji watano kutoka kikosi chao cha vijana cha U20 kilichotwaa ubingwa wa Kombe la Uhai.
Ofisa Habari wa klabu hiyo, Hafidh Kido aliiambia MICHARAZO kuwa timu yao itaondoka na msafara wa watu wasiopungua 30 wakiwamo wachezaji 26 na viongozi watano akiwamo kocha wao mkuu mpya, Yusuph Chipo.
Kido alisema Coastal inaenda Oman kwa ajili ya kuweka kambi ya wiki mbili wakiwa chini ya wenyeji wao klabu ya Fanja inayoshiriki Ligi Kuu ya nchini humo.
"Kwa sasa Coastal tupo katika maandalizi ya ziara yetu ya kambi ya wiki mbili nchini Oman kwa mualiko wa klabu ya Fanja na tukiwa huko tutacheza mechi tatu ambazo tutapangiwa na wenyeji wetu," alisema Kido.
Alisema miongoni mwa wachezaji watakaokuwa katika msafara huo ni vijana watano waliopandishwa katika kikosi cha kwanza kutoka timu ya U20 iliyotwaa taji la Uhai 2013 baada ya kuwalaza vijana wa Yanga katika fainali iliyochezwa hivi karibuni.
Kido alisema mara wakirejea nchini moja kwa moja watakuwa wakikabiliana na JKT Oljoro katika pambano la fungua dimba la duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Coastal ambayo ilimaliza duru la kwanza ikiwa katika nafasi ya nane kwa kujikusanyia pointi 16 chini ya kocha Hemed Morocco waliyemtema na kumnyakua Mkenya Yusuf Chipo atakayeanza kibarua akiwa ughaibuni.

Azam Media Tv wazidnua huduma zao


Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Yusuf Bakhresa (kushoto) akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa Jengo la Ofisi za huduma kwa wateja za Azam TV, zilizopo kwenye makutano ya barabara ya Nyerere na Mandela, Tazara jijini Dar es Salaam leo. Kulia ni Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Rhys Torrington.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Yusuf Bakhresa akizungumza na vyombo mbali mbali vya habari vilivyokuwepo kwenye ufunguzi huo wa Jengo la Ofisi za huduma kwa wateja za Azam TV, zilizopo kwenye makutano ya barabara ya Nyerere na Mandela, Tazara jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Yusuf Bakhresa akizungumza.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Rhys Torrington akisisitiza jambo mbele ya waandishu wa habari (hawapo pichani) juu ya huduma mbali mbali wazitoazo kama Azam TV.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Yusuf Bakhresa akisalimiana na baadhi ya waigizaji wa Filamu nchini kutoka kundi la (Bongo Movie) waliokuwepo kwenye Ufunguzi huo uliofanyika leo jijini Dar.


Burudani ya ngoma za asili pia zilikuwepo kwenye Uzinduzi huo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Yusuf Bakhresa (kushoto) akizungumza jambo na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media wa Kampuni ya Azam Media Ltd,Rhys Torrington mara baada ya Ufunguzi wa Jengo la Ofisi za Azam TV jijini Dar es Salaam.Katikati ni Meneja Uzalishaji na Ufundi wa Kampuni hiyo,Mehboob Aladdad.

Wasanii wa Bongo Movie wakiwa kwenye picha ya pamoja.

AzamTV leo imeanza kutoa huduma zake rasmi katika makao makuu yaliyopo barabara ya Nyerere, jijini Dar es Salaam.
Huduma za matangazo ya AzamTV zilianza kupatikana hewani Kuanzia Ijumaa Desemba 6, 2013 kwa kuwawezesha wateja waliounganishwa kwenya kisimbuzi kuangalia bure hadi hii leo ambapo huduma kwa malipo inaanza rasmi kwa ada ya shilingi 12,500 kwa mwezi.
Kwa kuanzia huduma ya AzamTV itahusisha chaneli 50 zinazojumuisha chaneli maarufu za kimataifa, chaneli maarufu za ndani na chaneli tatu maalumu za Azam ambazo ni:

· Azam One – burudani kwa familia kutoka Afrika, sehemu kubwa ya matangazo itakuwa kwa lugha ya Kiswahili.
· Azam Two – vipindi maalum kutoka sehemu mbalimbali za dunia
· SinemaZetu – Chaneli maalumu kwa tamthilia za kitanzania kwa saa 24.



Kwa pamoja, chaneli tajwa zitawapa wateja wigo mpana wa kufaidi matangazo bora ya michezo, tamthilia, watoto na maisha.
Ofisi ilifunguliwa rasmi na Bw. Yusuf Bakhresa: Mkurugenzi Mtendaji wa Azam Media Ltd.
“Ofisi hii ya makao makuu ambayo kwa hakika ni ya kuvutia ni kielelezo cha nia thabiti ya Azam Media kufanya kazi kwa umakini katika shughuli ya utangazaji hapa Tanzania. Dira yetu ni kutoa burudani ya kiwango cha juu kwa familia kwa bei nafuu kote nchini, na baadaye kote barani Afrika. Hili ni jambo ambalo kila mmoja hapa nchini anapaswa kujivunia.” Alisema Bakhresa

Rhys Torrington: Afisa Mtendaji Mkuu wa Azam Media Ltd alisema: “Naona faraja kubwa kwamba leo hii AzamTV ipo sokoni kwa ajili ya kila mtanzania. Tutahabarisha, kuelimisha na zaidi ya yote tutaburudusha watu kote nchini. Huduma yetu inapatikana kwa watu wote – situ katika ofisi hizi lakini pia kupitia mtandao wetu unaohusisha zaidi ya mawakala 50 katika kila mkoa. AzamTV ni ya kudumu”

Azam Media pia inawekeza katika utayarishaji wa vipindi vipya kupitia kampuni yake tanzu, Uhai Productions, kwa kushirikiana na watayarishaji wa vipindi wa hapa Tanzania.

Chelsea yatupwa nje Capital One, Mkorea awanyamazisha, Man City haooo

Kitu Sundeland wakiizamisha Chelsea katika Capital One jana usiku
Edin Dzeko akiifungia Manchester City moja ya mabao yake mawili yaliyoivusha Nusu Fainali
BAO la muda wa nyongeza lililofungwa na nyota wa timu ya taifa ya Korea ya Kaskazini, Sung Yong Ki limeivusha 'vibonde' wa Ligi Kuu ya England Sunderland na kuizuia Chelsea kutinga Nusu Fainali ya Kombe la Ligi 'Capital One'.
Sunderland inavuka hatua hiyo ya nusu fainali ya michuano hiyo baada ya muda mrefu na huku ikiwa katika hali mbaya kwenye ligi kuu, na sasa imeungana na Manchester City waliopata ushindi wa mabao 3-1 usiku wa jana katika mechi nyingine ya Robo Fainali ya michuano hiyo dhidi ya Leicester City.
Katika pambano la Sunderland waliokuwa nyumba dhidi ya vijana wa Jose Mourinho, dakika 90 ziliisha kwa timu hizo kufungana bao 1-1, Chelsea wakizawadiwa bao baada ya kiungo wa wenyeji, Lee Cattermole kujifunga dakika moja baada ya kipindi cha pili kuanza kabla ya Fabio Borini kusawazisha bao hilo dakika ya 88 ya mchezo huo uliokuwa ukionekana kama Chelsea wanaelekea kutinga Nusu Fainali.
Ndipo zikaongezwa dakika 30 za nyongeza na kushuhudia Chelsea wakishindwa kupata mabao mpaka dakika mbili kabla ya muda huo kumalizika Mkorea huyo kuifungia Sunderland bao lililowang'oa vijana wa Darajani nje ya michuano hiyo.
Katika pambano jingine Manchester City waliopo kwenye kiwango kwa sasa walipata ushindi ugenini wa mabao 3-1 na kutiunga nusu fainali dhidi ya wenyeji wao Leichester City.
Mpaka mapumziko wageni walikuwa na mabao 2-0 yaliyofungwa na Aleksandar Kolarov dakika ya 8 na Edin Dzeko aliongeza bao dakika ya 41.
Kipindi cha pili City waliongeza bao jingine dakika ya 53  kupitia tena kwa Dzeko akimalizia kazi ya james Millner kama ilivyokuwa kwa bao lake la kwanza na wenyeji kupata bao la kufutia machozi dakika ya 77 kupitia kwa  Lloyd Dyer.
Michuano hiyo itaendelea tena usiku wa leo kwa mechi nyingine za mwisho wa roboa fainali kati ya Manchester United itakayokuwa ugenini kuwakabili Stoke City na Tottenham kuikaribisha West Ham United.

Tuesday, December 17, 2013

Da! Hemed, Mlela waja kivingine katika I Know U

Hemed (kushoto) akimtishia bastola Mlela
Hemed na Mlela wakiwa wamelazwa hospitalini baada ya kuumizana huku mama yao akiwaangalia kwa huzuni
Kasha la filamu mpya ya bifu la kina Mlela na PHD inayotarajiwa kuingia mtaani keshokutwa Jumatano.
LILE bifu lililowahi kufukuta kwa kasi mithiri ya moto wa kifuu baina ya ‘tozi’ wawili ndani ya tasnia ya filamu, Hemed Suleiman ‘PhD’ na Yusuf Godfrey Willard Mlela ‘Mlela’ linadaiwa kuibuka upya na kuzidisha uhasama baina ya wasanii hao.
Aidha, alisema bifu hilo lilidhihirika hivi karibuni wakati wawili hao walipokutanishwa kuigiza filamu moja, kwani mara kwa mara walijikuta wakifanya kweli kwenye baadhi ya vipande vya ugomvi na mapigano jambo lililompa wakati mgumu muongozaji wa filamu hiyo inayotarajiwa kuingia sokoni kuanzia Desemba 18 mwaka huu iliyopewa jina la I Know You.

“Walikuwa na muda mrefu sana bila kukutana, tukadhani bifu lao halipo tena, lakini hivi karibuni walikutana kwenye filamu iliyoandaliwa na Mtitu Game 1st Quality, wakawa wanafanya kweli kwenye baadhi ya sehemu za majibizano na mapigano huku wakifanyiana fujo mbalimbali huku kupigana vijembe vya wazi,” alisema rafiki huyo.

“Ni kweli tulikuwa na utofauti, ule mvutano wa zamani bado ulikuwepo, kila mmoja hakutaka kuwa dhaifu kwa mwenzake, utaona baadhi ya vipande tulivyofanya kweli,” alisema Mlela ambapo simu ya Hemed iliita bila kupokelewa licha ya mwandishi wetu kuipiga mara kwa mara.

Naye Meneja matayarishi wa Kampuni ya Game st Quality Ltd, Noel Amani ‘Futo’ alisema filamu ya I know You iliwapa wakati mgumu sana kutokana na bifu la wasanii hao kuonekana waziwazi.
“Walitumbua sana, kuna wakati walifokeana kweli, kukunjiana ngumi hata hivyo kuna baadhi ya vipande walivyofanya kweli tumelazimika kuviacha ili kuleta uhalisia zaidi. Kila mmoja anaamini yuko juu ya mwenzake,” alisema Futo.

Tanzanite waagwa kutimka kesho Sauzi

Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, Boniface Wambura akikabidhi bendera kwa madada wa Tanzanite leo (Picha zote: Lenzi ya Michezo)
Wakisikiliza nasaha kabla ya kuondoka kesho kwenda kuiwakilisha Tanzania
Kocha Kaijage (kati) akizungumza huku Kaimu Katibu Mkuu wa TFF, akisikiliza kwa makini
Tunaenda kupigana na lolote linaweza kutokea tuombeeni tu
nahodha wa timu naye akitoa yake
TIMU ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 ‘Tanzanite’ itaondoka kesho kuelekea nchini Afrika Kusini kwa ajili ya mechi ya marudiano ya kufunzu kombe la dunia huku ikiwa na matumaini ya kufanya vizuri.

Katika mechi ya kwanza dhidi ya Afrika Kusini iliyochezwa hivi karibuni kwenye uwanja wa nyumbani wa Taifa wa Dar es Salaam, Tanzanite ilichapwa mabao 4-1, hivyo inahitaji kushinda katika mchezo huo kuanzia mabao 5 ili iweze kusonga mbele. 

Kaimu Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania(TFF) Boniface Wambura alisema jana kuwa timu hiyo wakiongoza na kiongozi mmoja wa msafara wataondoka kuanzia saa nne na nusu kwa ndege ya Fast Jet.

Akizungumzia maandalizi ya mchezo huo wa marudiano Kocha wa Tanzanite Rogasian Kaijage alisema wana matumaini ya kufanya vizuri kwa vile walirekebisha mapungufu yaliyojitokeza katika mechi ya kwanza dhidi ya timu hiyo.

“Mchezo uliopita  ulikuwa na mapungufu kidogo, lakini kwa sasa tumeshayarekebisha na tuna imani ya kufanya vizuri jambo la muhimu ni watanzania kutuombea,”alisema.
Kaijage alisema licha ya kufanya vibaya katika mechi ya kwanza wanahitaji kupewa moyo na sio kulaumiwa kwa kupoteza mchezo mmoja, kwa vile huweza kuwakatisha tamaa wachezaji.

Kwa upande wake, Nahodha wa timu hiyo Fatma Issa aliomba watanzania kuacha kuwakatisha tamaa na badala yake wawape moyo na kuwaombea ili kurudi na ushindi.
Alisema “tunaahidi kufanya vizuri kwasababu tayari Kocha amerekebisha mapungufu, jambo la muhimu nawaomba watuombee,”.

Aliwataka watanzania kutovunjika moyo kwa matokeo mabaya yaliyopita na kuongeza kuwa kutokana na marekebisho makubwa yaliyofanywa wana imani ya kufanya vizuri.

Cheki Extra Bongo wakijifua na Muumin kwa ajili ya maonyesho ya sikukuu ya X-mass, Mwaka Mpya

Muumin akiimba na waimbaji wa Extra Bongo
Kilio ooo ooo Kiliooo Kilio cha Baba yangu.....Ndivtyo wanavyoimba waimbaji Muumi, Adam Mbombole na Kabatabo

Mnaimba hivi...si mnajua mimi ndiye Kocha wa Dunia?

Ephraem Joshua mzee wa Kanyaga Twende akicharaza gitaa mazoezini

Wakionyesha umahiri wao

Mfaume Rhythm akicharaza gita la kati ya Rhythm mazoezni leo
Sebastian Lukandikja akipapasa kinanda huku akiangaliwa na mwanamuziki mwingine
Ephraem Joshua (solo) na mcharaza gitaa la Bass Hosea Mgohache wakifanya mambo mazoezini
Mkaanda Chips, Mpogoro Mashine akifanya mautundu yake huku, msaidizi wake, Sunady Mukinga (kati) akifuatilia kwa makini na mwenzake

Rais JK atuma salamu za Rambirambi kwa Rc Mwanza

Breaking News: Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mwanza (Mabina) auwawa na wananchi wenye hasira kali kwa kupigwa mawe

Taarifa zaidi, soma hapa => http://bit.ly/18O5nYu
Marehemu Mabina enzi za uhai wake
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Eng. Evarist  Ndikilo kufuatia vifo vya watu wawili vilivyotokea tarehe 15 Desemba,2013 katika Kitongoji cha Kanyama Kata ya Kisesa Wilaya ya Magu, Mkoani Mwanza.
Rais ametuma salamu hizo kwa Mkuu wa Mkoa kufuatia vifo vya BW. Clement Mabina na Tenery Malimi vilivyotokea baada vurugu zilizosababishwa na mabishano ya ardhi.
Rais amemuomba Mkuu wa Mkoa kuwatahadharisha wananchi kutokuchukua sheria mikononi mwao na pia kuwa waangalifu na matumizi ya silaha za moto.
“Nimesikitishwa na kufadhaishwa sana na taarifa za vifo vya wananchi hao wawili (2) vilivyosababishwa na mgogoro wa Ardhi ambao ungeweza kupata suluhu kwa njia za amani. Ni vema wananchi kuwa na subira na kuwa waangalifu katika kutatua migogoro yao”. Rais amesema na kuongeza kuwa “ ni vema subira na busara zikawa ndio muongozo wa kutatua migogoro yetu katika jamii badala ya hasira”.
Aidha, Rais Kikwete amemuomba Mkuu wa Mkoa amfikishie salamu zake za dhati kwa familia na ndugu wa Marehemu Mabina pamoja na Wazazi na ndugu wa Marehemu Tenery Malimi, ambao walifariki kutokana na vurugu hizo.
          “Amewaomba familia zote mbili ziwe na subira wakati huu mgumu kwa kuondokewa na wapendwa wao na kuviacha vyombo vya dola kuchukua hatua kwa kufuata taratibu zilizopo”.  Kwa ndugu Mabina, Chama cha Mapinduzi kimepoteza mmoja wa viongozi wake mahiri na wa kutumainiwa.  Aidha, kwa marehemu Tenery taifa limepoteza mmoja wa vijana wake wanaochipukia ambae angejaaliwa kuishi angeweza kutoa mchango muhimu kwa maendeleo ya jamii na nchi yetu.
 Mabina amewahi kushika nyadhifa mbalimbali zikiwemo Diwani na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Magu mwaka 2000 – 2005, Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Mwanza, mwaka 2007 – 2012.
Rais ameziombea nyoyo za marehemu wote Mungu azilaze  mahali pema peponi Amen.

Imetolewa na;
Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais Msaidizi,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
17 Desemba,2013

Uchaguzi wa Simba kufanyika Januari


Mwenyekiti wa Simba, Ismail Rage
MWENYEKITI wa klabu ya soka ya Simba, Ismail Aden Rage ameibuka na kufafanua baadhi ya mambo ambayo yamekuwa yakielekezwa kwake hasa sakata la kusajiliwa kwa Emmanuel Okwi na mahasimu wao Yanga na kuweka bayana ili kuondoa mzozo wa fitina Msimbazi, huenda akautisha uchaguzi mkuu Januari.
Kwa mujibu wa Katiba ya Simba, uchaguzi mkuu wa klabu hiyo unatakiwa kufanyika Mei mwakani, lakini kwa vile hali inaonekana tete ndani ya klabu hiyo Mwenyekiti huyo alisema amekutana na viongozi wa matawi na kuzungumza nao na kutoa pendekezo la kuitiosha uchaguzi mkuu mapema tofauti na unavyotakiwa.
"Nimekutana nao na lengo kuu ni kuzungumza hali iliyopo ndani ya klabu na kama tatizo ni mimi basi nipo tayari kuitisha uchaguzi hata Januari ili Simba iingie duru la pili ikiwa na amani na utulivu na iliyokamilika safui mpya ya uongozi kwa maana ya Mwenyekiti, Makamu na Kamati ya Utendaji mpyam," alinukuliwa Rage.
Rage alisema kuwa tofauti yake na wenzake ni msimamo wake wa kupigania haki za klabu na hasa kutaka kila kitu kifanyike klabu na kwa uwazi.
Kuhusu sakata la Okwi analotupiwa lawama kwamba alisaidia kutua kwake Jangwani, Rage alisema ni kutaka kumbebesha lawama usiomhusu kwani kwa kipindi kirefu akikuwa nje ya nchi na kama Okwi alikuwa ni muhimu Simba Kamati ya usajili ingemsajili kama ilivyofanywa kwa wachezaji wengine watatu.
Kamati hiyo ya Simba imewasajili makipa Ivo Mapunda, Yew Berko na beki wa Gor Mahia, Donald Musoti na Rage alihoji mbona hao walisajiliwa na vipi Okwi asingesajiliwa na badala ya wanachama kumtupia lawama zisizo na maana yoyote.
Wanachama wa Simba wakiongozwa na tawi la Mpira Pesa limekuwa likimshutumu Rage kuhusu suala la Rage kwamba aliwacheza shere na kuapa kwamba wangeenda nyumbani kwake mara baada ya pambano lap na Yanga na Nani Mtani Jembe siku ya jumamosi kushinikiza kujiuzulu au kuzionyesha fedha za usajili za mchezaji huyo aliyeuzwa Etoile du Sahel ya Tunisia kabla ya kurejea kwao Sc Villa Yanga ilipoenda kumnasa.
Kuhusu uchaguzi huo ujao, Rage alisema hana mpango wa kuwania nafasi yoyote katika klabu hiyo na hasa kutokana na kuchoshwa na vurugu ndani ya Simba ambazo zimemlenga yeye binafsi kila mara hasa mtu mmoja tu aliyemtaja kuwa hohehahe.
"Sintagombea uongozi wala kutetea kiti changu, ili kuachia wengine waiongoze Simba iwapo kama mimi ni tatizo," alisema Rage na kusisitiza kuwa fedha za Okwi hazijalipwa na wala hazijalipwa hivyo wanachama wa Simba watulie.

Extra Bongo, Muumini wawarejesha 'Mafahali Watatu' Tanzania

Mwinjuma Muumin 'Kocha wa Dunia' (kushoto) akiwa na waimbaji wa Ectra Bongo kwenye mazoezi ya bendi hiyo kujaindaa na maonyesho maalum ya sikukuu ya Krismasi na Mwaka Mpya
BENDI ya Extra Bongo inatarajia kukumbishia 'Mafahali Watatu' wa muziki wa dansi nchini watakaposhirikiana na Mwinjuma Muumin 'Kocha wa Dunia' katika maonyesho ya sikukuu ya Krismasi na Mwaka Mpya.
Muumini ambaye alikutwa na MICHARAZO mchana wa leo akifanya mazoezi na wanamuziki wa Extra Bongo ataungana na bendi hiyo katika maonyesho hayo yatakayofanyika jijini Dar es Salaam na mikoa ya Kanda ya Ziwa.
Mkurugenzi wa Extra Bongo aliiambia MICHARAZO kujiunga kwa Muumini katika bendi yao kwa maonyesho hayo itawakumhusha watanzania kundi lao la 'Mafahali Watatu' lililokuwa likiundwa na yeye (Ally Choki), Banzastone na Muumini.
Choki alisema onyesho la kwanza la pamoja na Muumini litafanyika Mkesha wa Krismasi na siku ya sikukuu hiyo kwenye ukumbi wa Meeda kabla ya kufanya hivyo mkoani Shinyanga na Bukoba.
"Mkesha wa Krismasi tutakamua Meeda Club. Sinza Mori na siku ya Krismasi yenyewe tutakuwa Chikaz Pub kabla ya kabla ya kuvamia Geita kuzindua ukumbi mpya wa Omega Splended Resort Mkesha na siku ya Mwaka Mpya na Januari 2 kuelekea Kahama, Shinyanga na siku inayofuata kufanya vitu vyetu Bukoba," alisema Choki
Choki alisema katika maonyesho yote hayo watatumia kutambulisha nyimbo zao mpya tatu za 'Mgeni', 'Wanawake Wanapendeza' na 'Hafidh'.
Muumini mwenyewe alisema anajisikia furaha kujumuika pamoja na wana Extra Bongo na hasa Choki akikumbushia enzi zao za Double Extra bendi iliyotisha Tanzania.

Monday, December 16, 2013

Spurs yamtimua AVB, kipigo cha Liver kinauma

Aliyekuwa kocha wa Spurs, AVB alipokuwa wakiajibika kibaruani kabla ya kusitishiwa mkataba wake

KLABU ya Tottenham Hotspur ya England imetangaza kumtimua aliyekuwa kocha wake mkuu, Andre Villa Boas kutokana na matokeo mabaya iliyopata timu hiyo jana kwenye Ligi Kuu ya nchi hiyyo toka kwa Liverpool.
Timu hiyo ilikung'utwa mabao 5-0 na Liverpool ikiwa nyumbani na kukasirisha mabosi na mashabiki wa timu hiyo ambayo imekuwa ikifanywa asuswa kwenye ligi hiyo tofauti na usajili wa kishindo uliofanya msimu huu.
taarifa ya klabu hiyo imesema kuwa wameafikiana na AVB kuachana naye na kwa sasa wanasaka kocha mkuu mpya wa kuinoa timu hiyo ambayo ilimnyakua Mreno huyo miezi 18 iliyopita baada ya kumtema Harry Redknapp aliyeipaisha barani Ulaya.
Miongoni mwa makocha wa awali wanaotajwa kumrithi AVB aliyeishuhudia vijana wake wakinyukwa mabao 6-0 wiki mbili zilizopita na Manchester City ugenini, ni bosi wa zamani wa timu ya taifa ya England, Fabio Capello anayeinoa timu ya taifa ya Russia.
Pia wanatajwa Glenn Hoddle, kocha wa Swansea City Michael Laudrup na mtu anayetajwa haswa kuchukua nafasi hiyo ni Guus Hiddink.

Tanzanite kuagwa kesho, kurudiana na Wasauzi J'mosi

MECHI ya marudiano ya raundi ya pili kuwania tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia kwa wasichana wenye umri chini ya miaka 20 kati ya Tanzania (Tanzanite) na Afrika Kusini (Batsesana) itachezwa Jumamosi, Desemba 21 mwaka huu.
Mechi hiyo itachezwa Uwanja wa Dobsonville ulioko Soweto, Johannesburg kuanzia saa 9.30 alasiri kwa saa za Afrika Kusini. Tanzanite itaondoka Jumatano, Desemba 18 mwaka huu saa 4 asubuhi kwa ndege ya Fastjet ikiwa na msafara wa watu 29 wakiongozwa na mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF, Khalid Abdallah.
Kikosi hicho kitaagwa kesho (Desemba 17 mwaka huu) saa 6 katika ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).
Katika pambano la kwanza lililochezwa jijini Dar es Salaam Tanzanite ilikumbana na kipigo cha mabao 4-1 toka kwa wasichana wenzao hao, hivyo kuwa na kazi ya kupata ushindi usiopungua mabao manne iwapo inataka kufuzu hatua ya mwisho kuwania nafasi mbili ya kucheza fainali za Dunia zitakazofanyika Canada mwakani.

Pambano la Stand, JKT Kanembwa kurudiwa


 
MECHI ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kati ya Stand United na Kanembwa JKT iliyochezwa Novemba 2 mwaka huu Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga na kuvunjika, sasa itarudiwa Februari 1 mwakani.
Uamuzi huo umefanya na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB) katika kikao chake kilichofanyika jana jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine ilipitia ripoti za mchezo huo uliovunika dakika ya 87.
TPLB imefikia uamuzi huo baada ya kujiridhisha kuwa mwamuzi Peter Mjaya alitoa taarifa ambazo si sahihi kuhusu mechi hiyo. Mjaya ameondolewa kuchezesha mechi za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na FDL.
Mechi hiyo itarudiwa katika Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora ambapo timu zote zimetumiwa uamuzi huo kwa maandishi.
Vilevile wachezaji tisa wa Kanembwa JKT waliompiga mwamuzi katika mechi hiyo suala lao linapelekwa Kamati ya Nidhamu ya TFF kwa ajili ya hatua zaidi kwa mujibu wa Ibara ya 27(g)(3) ya Kanuni za FDL.
Wachezaji hao ni Abdallah Mgonja, Baliki Abdul, Mbeke Mbeke, Mkuba Clement, Mrisho Musa, Mtilakigwa Hussein, Nteze Raymond, Philo Ndonde na Uhuru Mwambungu.

Arsenal kuivaa Bavarian, City vs Barca Mtoano Ligi Ulaya


RATIBA ya 16 Bora Ligi ya Mabingwa Ulaya imetoka ambapo Arsenal wametupiwa kuanzia nyumbaji dhidi ya mabingwa watetezi, Bayern Munich ya Ujerumani, huku Manchester City wakipewa Barcelona.
Kwa mujibu wa tariba hiyo, Schalke 04 wenyewe wamepangwa kuikaribisha Real Madrid nyumbani katika mechi ya awali kabla ya kurudiana ugenini kuwania kutinga robo fainali ya ligi hiyo ya mabingwa Ulaya.
Ratiba kamili inaoonyesha Manchester United ikipangiwa mchekea sawa na ilivuo kwa Borussia Dotmund ambao waliicheza fainali za mwaka jana na kunyukwa na Baravian.
Ratiba yenyewe ndiyo hii:
Manchester City Vs Barcelona
Olympiakos Vs Manchester United
AC Milan Vs Atletico Madrid
Bayer Leverkusen Vs Paris Saint-Germain
Galatasaray Vs Chelsea
Schalke 04 Vs Real Madrid
Zenit St. Petersburg Vs Borussia Dortmund
Arsenal Vs Bayern Munich

mechi za awali zitachezwa kuanzia  Februari 18 na Machi 10 kujua zitakazoingia Robo Fainali.