STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, February 14, 2014

Twiga Stars yalala 2-1 Zambia

Na Boniface Wambura, Lusaka
TWIGA Stars imepoteza mechi ya kwanza ya raundi ya kwanza kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) baada ya leo kufungwa mabao 2-1 na Zambia (Shepolopolo) kwenye Uwanja wa Nkoloma jijini Lusaka.
Hadi dakika 45 za kwanza zinamalizika katika mechi hiyo iliyochezeshwa na mwamuzi Salma Mukansanga timu hizo zilikuwa suluhu.
Wenyeji ndiyo walianza kupata bao lililofungwa na Hellen Mubanga dakika ya 75. Mfungaji huyo aliyeingia kipindi cha pili nchini alimalizia wavuni mpira uliotemwa na kipa Fatuma Omari.
Dakika nne baadaye Zambia ambao walikuwa wakishangiliwa kwa nguvu na washabiki wao baada ya kufunga la kwanza, walipata bao la pili ambalo nahodha wa Twiga Stars, Sophia Mwasikili alijifunga mwenyewe.
Mwasikili alikuwa akijaribu kutoa nje mpira uliopigwa na nahodha wa Shepolopolo, Mupopo Kabange ambapo ulipishana na kipa Fatuma Omari kabla ya kujaa wavuni.
Bao la Twiga Stars lilifungwa na Donisia Daniel dakika ya 90. Beki huyo wa kushoto ambaye pia ni mchezaji wa Tanzanite alipanda mbele kuongeza mashambulizi ambapo akiwa nje ya eneo la hatari alipiga shuti lililomshinda kipa Hazel Nali.
Akizungumza baada ya mechi, Kocha wa Twiga Stars, Rogasian Kaijage alisema amebaini upungufu katika kikosi chake ambao ataufanyia kazi kabla ya mechi ya marudiano ili timu yake iweze kusonga mbele.
“Kwa matokeo haya bado tuna nafasi ya kufanya vizuri kwenye mechi ya marudiano nyumbani na kusonga mbele,” alisema Kaijage.
Twiga Stars iliwakilishwa na Fatuma Omari, Fatuma Bashiru, Donisia Daniel, Fatuma Issa, Evelyn Sekikubo, Sophia Mwasikili, Vumilia Maarifa, Mwapewa Mtumwa/Amina Ali, Asha Rashid, Etoe Mlenzi/Zena Khamis na Shelida Boniface.
Timu hiyo inarejea nyumbani kesho kwa ndege ya Fastjet ambapo itatua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 7 kamili mchana.

Juan Mata afunguka kuhusu Mashetani Wekundu


368919_heroa
Mchezaji ghali zaidi kuwahi kununuliwa na klabu ya Manchester  United, Juan Mata amesisitiza kwamba ana furaha kucheza kwenye sehemu wowote uwanjani atakayopangwa na mwalimu wake na amebakia mtu mwenye furaha tangu alipojiunga na klabu hiyo mwezi uliopita.

Mhispania huyo ambaye amecheza mechi zote nne tangu alipojiunga na timu, na ameiwezesha timu yake kufunga mabao matatu na kuhakikisha inapata pointi 5, huku akichezeshwa kwenye namba tofauti na kocha David Moyes.
Moyes ameshamchezesha Mata kwenye winga zote mbili, amecheza nyuma ya mshambuliaji, lakini kiungo huyo mwenye miaka 25 hana chaguo lolote la sehemu ya kuchezeshwa anachojali ni kuisadia timu yake kushinda.
“Maisha yangu yote ya soka nimekuwa nikicheza upande wa kushoto, kulia na nyuma ya mshambuliaji,” Mata aliwaambia waandishi wa habari.
“Sijali wapi nachezeshwa na kocha wangu. Nina furaha nipo kwenye klabu kubwa sana na nina matumaini tutamaliza msimu vizuri.
“David de Gea amenisaidia kupazoea hapa, pia Chicharito, [Antonio] Valencia, na Rafael, wote wanaongea kihispania na wamenisaidia.”

TFF ya Jamal Malinzi yarejesha Kombe la Taifa kivingine

Rais wa TFF, Jamal Malinzi aliyetangaza mikakati ya kuikwamua Tanzania soka la kimataifa
MASHINDANO maalumu ya mikoa ya kuunda kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ yanatarajiwa kuanza kutimua vumbi Februari 22 hadi Machi 5 mwaka huu, huku ikiigharimu Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) takribani Sh. Milioni 360.
Michuano hiyo maalumu itashirikisha mikoa wanachama ya TFF na itakuwa ikichezwa kwa mfumo wa nyumbani na ugenini kwa timu mbili za kanda moja kuchuana na inatarajiwa kutoa wachezaji bora 60 wataoweka kambi ya siku 30 Tukuyu, Rungwe mkoani Mbeya.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Rais wa TFF Jamal Malinzi amesema michuano hiyo ni maalumu kwa ajili ya kuuunda upya kikosi bora cha Stars, ili kiweze kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) yatakayofanyika mwakani nchini Morocco.
Malinzi alisema jumla ya timu 32 za Tanzania nzima zitashiriki michuano hiyo, kila mechi moja watakuwepo wasaka vipaji watano ‘Scouts’ kwa ajili ya kumulika wachezaji bora, pia mechi zote zitakuwa zikirekodiwa.
Baada ya zoezi la kuibua vipaji kwenye michuano hiyo, wasaka vipaji wote watajifungia (retreat) kwa muda wiki moja mjini Lushoto, Tanga kupitia rekodi zote za mechi na kuchagua wachezaji 60 bora, ambao watapelekwa Tukuyu, Mbeya kwa ajili ya mazoezi makali na wataalamu mbalimbali.
Wachezaji hao 60 watachujwa baada ya mwezi mmoja na kubaki 30, ambao watachanganywa na wachezaji wa sasa wa Taifa Stars na baadaye kupatikana kikosi bora kwa ajili ya mapambano ya kuwania kufuzu kwa AFCON.
Malinzi alisema wachezaji wa sasa wa Stars nao watakwenda kwenye kambi hiyo mkoani Mbeya mara baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) mwezi Aprili.
“Tunaamini mfumo huo utasaidia kupata vijana wapya wa kuboresha kikosi cha Stars, hatutachagua majina wala kuangalia umri kwa kuwa hiki ni kipindi cha mpito na ni muda mchache umebakia kuelekea kwenye michuano hiyo,” alisema Malinzi.
Machi 5 mwaka huu Stars itashuka dimbani kuumana na Namibia katika mechi ya kirafiki inayotambuliwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).

Rais wa TFF, Jamal Malinzi akikabidhi sehemu ya vifaa vya michezo kwa ajili ya michuano maalum ya kusaka kikosi cha Stars leo (Picha kwa hisani ya Lenzi ya Michezo)

Wakati huo huo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limeanza rasmi mikakati ya kuiwezesha timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kufuzu kwa Fainali za mataifa ya Afrika (AFCON) mwakani baada ya kupanga mpango wa timu hiyo kuweka kambi nchini Uholanzi.
Kambi hiyo itakuwa ni maalumu kwa timu hiyo kuweza kujiandaa na hatua ya kufuzu kwa fainali hizo zitakazofanyika mwakani nchini Morocco na kushirikisha jumla ya mataifa 16 yatakayofuzu.

Akizungumza na Waandishi wa Habari leo mjini Dar es Salaam, Rais wa TFF, Jamal Malinzi amesema endapo Stars itafanikiwa kupita katika hatua ya awali ya mchujo ikiwa itapangwa kwenye hatua hiyo, wamepanga kuweka kambi nchini Uholanzi ya timu hiyo, ili kujiandaa na hatua ya pili ya makundi.
Malinzi alisema wameamua kufanya hivyo ili kurudia historia ya mwaka 1980 ya Stars kufuzu kwa mara ya mwisho michuano ya AFCON, iliyofanyika nchini Nigeria, ambapo Stars iliweka kambi Uholanzi mwaka 1979 na kufanikiwa kufuzu kwa fainali hizo.
“Tumepokea barua ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) inayotueleza kuwa mechi zetu za mchujo zitaanza kati ya mwezi Mei hadi Agosti kutokana na kiwango chetu kuwa chini ya nchi 21 bora za bara hili, hivyo muda si mrefu tunafikiria kurekebisha benchi lote la ufundi kwa pamoja na kuanza mikakati ya timu hiyo.
“Huenda timu yetu ikaanzia hatua ya mchujo kama CAF walivyotuandikia, ikifanikiwa kufuzu katika hatua ya makundi ttumepanga kuweka kambi nje ya nchi katika nchi ya Uholanzi, na huko timu itapata mafunzo ya kisasa ili kufanya vizuri kwenye hatua ya makundi,” alisema Malinzi.
Katika hatua nyingine alisema kwa sasa wameshazungumza na Balozi wa Uholanzi hapa nchini kwa ajili ya mipango yao hiyo, pia wamewataarifu wadhamini wakuu wa Stars, Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kupitia kinywaji chao cha Kilimanjaro Premier Lager ili kuandaa bajeti ya ziara hiyo. 

MECHI YA TWIGA STARS, ZAMBIA ‘LIVE’ ZNBC

Na Boniface Wambura, Lusaka
KIKOSI cha Twiga Stars kinashuka Uwanja wa Nkoloma, Lusaka nchini Zambia leo kuwavaa wenyeji Zambia (Shepolopolo) katika mechi ya mchujo ya Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) itakayooneshwa moja moja ‘live’ na televisheni ya Shirika la Taifa la Utangazaji la Zambia (ZNBC).

Mechi hiyo itaanza saa 9 kamili mchana kwa saa za Zambia ambapo Tanzania itakuwa saa 10 kamili jioni huku Kocha Mkuu wa Twiga Stars, Rogasian Kaijage akiwa tayari ametangaza ‘silaha’ zake kwa mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya kwanza.

Watakaoanza kupeperusha bendera ya Tanzania katika mechi hiyo ambayo kiingilio ni bure kwa majukwaa yote isipokuwa lile kuu ni; Fatuma Omari 1, Fatuma Bashiru 17, Donisia Daniel 2, Fatuma Issa 5, Evelyn Sekikubo 15, Sophia Mwasikili 16, Vumilia Maarifa 10, Mwapewa Mtumwa 9, Asha Rashid 14, Etoe Mlenzi 13 na Shelida Boniface 7.

Wachezaji wa akiba ni Maimuna Said 18, Fatuma Hassan 12, Zena Khamis 6, Esther Chabruma 8, Amina Ally 4, Therese Yona 11 na Happiness Hezron 3.

Sikinde yapiga mbizi baharini na kuibukia Kigamboni

Baadhi ya wapiga wa Sikinde wakiwajibika

BENDI kongwe ya muziki wa dansi, Mlimani Park 'Wana Sikinde' leo inatarajia kuvuka bahari ya Hindi na kwenda kufanya onyesho maalum la Siku ya Wapendanao 'Valentine Day' eneo la Mji Mwema Kigamboni.
Onyesho hilo litafanyika kufcuatia maombi ya wadau wa muziki wa dansi wa eneo hilo ambao wanataka kuishuhudia bendi hiyo ikifanya vitu vyake huko kwenye siku hiyo ambayo husherehekewa kote duniani Februari 14 ya kila mwaka.
Mratibu wa onyesho hilo, Michael Yona alisema kuwa amesikia maombi ya wakazi wa Kigamboni na sasa anawapelekea bendi hiyo kongwe ambayo ana uhakika itawaburudisha vya kutosha kwenye siku hiyo maarufu duniani.
"Sikinde wana nyimbo zao mpya kama Kiboyo, Nundu ya Ng'ombe, Kukatika kwa Dole Gumba, Jinamizi la Talaka, Tabasamu Tamu, Deni Nitalipa na nyingine nyingi ambazo nina uhakika itakuwa ni nafasi ya pekee kwa wakazi wa Kigamboni kuburudishwa na nyimbo hizo," alisema Yona.
Alisema kuwa nyimbo hizo ndizo zinazoandaliwa kwa ajili ya albamu mpya baada ya ile ya 'Supu Imetiwa Nazi' ambayo hadi sasa bado iko sokoni wakati wanamuziki wakiendelea kukuna vichwa ili kukamilisha vitu vipya.
Naye katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo alisema Sikinde alisema kuwa kwa muda mrefu haijafanya onyesho Kigamboni na kwamba ana uhakika wakazi wa eneo hilo wana hamu ya kuwaona Sikinde wakiwaburudisha.
"Kwanza kabisa ieleke kwamba Mlimani Park ni bendi ya watu wote wakiwamo wakubwa na vijana wadogo ambao naamini watakuja kuishuhudia kwenye onyesho hili la Siku ya Wapendanao," alisema Milambo.
Bendi hiyo ilirudia jina lake la zamani la Mlimani Parbk kutoka DDC Mlimani Parik baada ya kuachwa na Shirika la DDC na sasa inajitegemea.

Hassan Vocha kuwa Surprise mashabiki leo

 
MUIMBAJI mpya wa kundi la taarab lililorejea upya la Dar Modern 'Wana wa Jiji', Hassan Vocha, amewaahidi kuwafanyia 'mshangao' mashabiki wa kundi hilo watakaohudhuria utambulisho wake na wasanii wenzake unaofanyika leo jijini Dar es Salaam.
Vocha na waimbaji wenzake kadhaa walionyakuliwa na kundi hilo lililowahi kutamba na vibao kama 'Pembe la Ng'ombe', 'Kitu Mapenzi' na 'Malavidavi' watatambulishwa leo 'Valantine Day' eneo la Magomeni.
Akizungumza na MICHARAZO, msanii huyo alisema ameandaa kitu 'spesho' kwa mashabiki wa muziki wa taarab katika onyesho hilo maalum.
"Kuna kitu maalum nimewaandalia mashabiki kwa ajili ya utambulisho huo ikizingatiwa onyesho litafanyika Siku ya Wapendanao', naomba waje ukumbini kujua kitu gani hicho," alisema Vocha.
Vocha aliyejipatia umaarufu mkubwa kupitia wimbo wake wenye jina hilo la 'Vocha' alichoimba na Dogo Aslay wakati akiwa Mkubwa na Wanae, alisema jukumu alililopewa kuvaa 'viatu' vya Hammer Q ni changamoto kwake.
"Najua ni changamoto kwangu, lakini kwa vile mimi ni msanii mwenye kipaji nitawapa burudani mashabiki wenye imani nami," alisema Vocha ambaye katika onyesho hilo ataimba karibu nyimbo zote alizoimba Hammer Q.
Uzinduzi huo wa Dar Modern utafanyika Travertine Hotel na kusindikizwa na makundi ya Kibao Kata na Baikoko ambapo Vocha atatambulisha nyimbo mbili alizorekodi katika albamu za kundi hilo za 'Oh My Sweet' na 'Ngoma Inapasuka'.

Thursday, February 13, 2014

News Alert! Imamu-Arusha amwagiwa 'tindikali'

IMAMU wa Msikiti wa Sawiyatu Qadiria, Hassan Bashir, akiwa amelazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru, baada ya kumwagiwa inayodaiwa kuwa ni tindikali jana na mtu asiyefahamika baada ya mtu huyo kumwita kwa jina anayedaiwa alikuwa amevalia koti na kanzu. Inaelezwa wakati Imamu huyo anageuka ghafla ndipo alipomwagia bahati nzuri ilimpata tutawaletea habari baadae 

Tanzania, Ureno, Algeria zapaa orodha ya FIFA, Hispania bado kinara

TANZANIA imepanda kwa nafasi mbili katika orodha ya ubora wa viwango vya soka duniani kutoka nafasi ya 118 hadi nafasi ya 116, huku Hispania, Ujerumani na Argentina zikiendelea kubaki katika nazo za Tatu Bora kama ilivyokuwa katika orodha ya mwisho.
Kwa mujibu wa orodha mpya iliytotolewa leo la Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) inaonyesha Ureno imepanda kwa nafasi moja toka nafasi ya tano hadi ya nne wakiporomosha Colombia, na Uswisi imepanda kwa nafasi mbili hadi nafasi ya 6 na Uruguay ikiangukwa kwa nafasi moja na kushika nafasi ya 7 juu ya Italia iliyoporomoka kwa nafasi moja pia.
Wenyeji wa michuano ya Fainali za Kombe la Dunia Brazil ilipanda kwa nafasi moja hadi namba 9 na timu inayofungia 10 Bora ya orodha hiyo mpya ni Uholanzi. Timu zilizopo kwenye 20 Bora ukiondoa 10 za kwanza ni pamoja na Belgium,Ugiriki,  Marekani, Chile, Engalnd, Croatia, Bosnia and Herzegovina, Ukraine, Ufaransa na Denmark imefunga dimba.
Kwa upande wa Afrika, Ivory Coast imeendelea kuongoza ikishika nafasi ya 23, huku Algeria ikipanda hadi nafasi ya pili Afrika kwa kukamata nafasi ya 26 na Cape Verde ikiweka rekodi ikikamata nafasi ya 27 na nafasi ya tatu barani Afrika, huku Ghana waliokuwa nafasi ya pili kwa muda mrefu nyuma ya Ivory Coast imeporomoka hadi nafasi ya 4 Afrika na Dunia ya 37.
Misri, inakamata nafasi ya 38 duniani na Afrika ikikamata nafasi ya 5 ikifuatiwa na Tunisia, kisha Cameroon, Nigeria, Mali na Burkina Faso    ikifunga dimba la 10 Bora.
Tanzania wenyewe wamepanda kwa nafasi mbili duniani kwa kushika nafasi ya 116 toka 118 iliyokuwa ikikamata awali na kwa Afrika inakamata nafasi ya 33.
Kwa upande wa CECAFA, Uganda inaendelea kuongoza ikifuatiwa na Ethiopia kisha Kenya ndipo Tanzania , Sudan, Burundi, Rwanda, Eritrea, Sudan Kusini, Somalia na Djibout

Extra Bongo yaibomoa Twanga Pepeta

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEi_thGkmsIrUaJZWJqet-LSegNzvnbsCbEG3Jit2hZQ_xSn2L7PSe0RzFpOjQHOlexM2dfpT-CY4xNZSJNvTSOiAY-j31q0A5lPppz310NhtGlGN5rptXa5P_dpG_6a-t_BOyGnsdHpPo0/s640/EXTRA5.jpg
'Mtoto karudi nyumbani' Rapa Grayson Semsekwa
UONGOZI wa wakali wa muziki wa dansi nchini Extra Bongo ‘Next Level Wazee wa Kimbembe’ umemrejesha kundini aliyewahi kuwa rapa bendi hiyo Greyson Semsekwa sambammba na kumnyakuwa mnenguaji Asha Sharapova kutoka bendi ya African Stars Twanga Pepeta.

Akizungumza jijini Dar es Salaam leo, Msemaji wa bendi hiyo Juma Kasesa, alisema, kurejea kwa Semsekwa mmoja ya wanamuziki waasisi wa Extra Bongo kutaimarisha safu ya 'kufokafoka' kuelekea kwenye uzinduzi wa albamu yao mpya ya 'Mtenda Akitendewa.'

Kwa mujibu wa Kasesa, Mtenda Akitendewa inatarajiwa kuzinduliwa Februari 22 mwaka huu kwenye Ukumbi wa Dar Live, uliopo Mbagala Zakhiem  jijini Dares Salaam.

Semsekwa alishiriki kwa kiwango katika albamu ya 'Mjini Mipango' mwaka 2009 kabla ya baadae kutimkia Twanga Pepeta na sasa amerejea kundini akiwa na rapu mpya ambazo atazimbulisha Jumamosi hii katika onyesho maalumu la Utambulisho wao litakalofanyika katika Ukumbi wa Meeda Sinza.

Alisema, wameamua kumchukua Sharapova baada ya kutambua kipaji alichonacho katika unenguaji hivyo kukidhi vigezo vya kunengua kwenye bendi hiyo inayoundwa na wanenguaji wakongwe kama Maria Salome na Otilia Boniface chini ya ukufunzi wa Super Nyamwela.

"Tunaendelea na mikakati ya kujiimarisha kwakuwa kila maboresho tunayofanya kwenye bendi pia tunazingatia maoni na ushauri wa wapenzi na wadau wa Extra Bongo ili kuendelea kuwapa burudani inayowasuuza nyoyo zao,"alisema Kasesa.

Aliwataka mashabiki kujitokeza kwa wingi Jumamosi hii kwenye onyesho la bendi hiyo Meeda kuona muonekano mpya wa Semsekwa na Sharapova baada ya kutoka Twanga Pepeta.

Yanga watua Comoro tayari kwa vita

baadhi ya wachezaji wa Yanga wakishangilia moja ya mabao yao
MABINGWA watetezi wa Ligi kuu Tanzania Bara, Yanga wamefika salama mjini Demoni, nchini Comoro tayari kwa mchezo wa marudiano Raundi ya Awali Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya wenyeji Komorozine siku ya Jumamosi.
Taarifa kutoka nchini humo inasema kuwa kikosi hicho chenye wachezaji 19 wamefika salama tayari kwa mechi hiyo ya mkondo wa pili.
Yanga iliyoondoka mapema leo, imetua nchini humo ikiwa na matumaini makubwa ya kusonga mbele, baada ya kuichapa Komorozine mabao 7-0 katika mchezo wa kwanza uliofanyika Dar es Salaam Jumamosi iliyopita.
Iwapo Yanga itahitimisha vyema kampeni yake hiyo, itakutana na mabingwa watetezi, Al Ahly mwezi ujao.  

Twiga Stars yatua salama yaahidi mapambano

Twiga Stars
KIKOSI cha wachezaji 19 wa Twiga Stars kimetua salama mjini Lukasa, Zambia (Februari 13 mwaka huu) huku Kocha Mkuu Rogasian akiahidi ushindani kwenye mechi dhidi ya wenyeji itakayochezwa Uwanja wa Nkoloma.

Kocha Kaijage aliwaambia waandishi wa habari kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kenneth Kaunda mara baada ya kikosi chake kutua kwa ndege ya Fastjet saa 3.30 asubuhi kwa saa za Zambia kuwa wamekuja kushindana, na si kushiriki.

Twiga Stars ambayo mara ya mwisho ilikutana na Zambia kwenye michuano ya COSAFA miaka miwili iliyopita na kuibuka na ushindi imefikia hoteli ya
Golden Peacock, na katika uwanja wa ndege ilipokewa na viongozi wa Chama cha Mpira wa Miguu Zambia (FAZ) na Ofisa Ubalozi wa Tanzania nchini Zambia, Jeswald Majuva.

Timu hiyo leo saa 9 alasiri kwa saa za Zambia ambapo Tanzania ni saa 10 jioni itafanya mazoezi kwenye Uwanja wa Nkoloma ambao ndiyo utakaotumika
kwa mechi hiyo ya mchujo ya Kombe la Afrika kwa Wanawake (AWC) itakayochezwa kesho.

Wachezaji waliopo kwenye kikosi hicho ni Amina Ali, Anastazia Katunzi, Asha Rashid, Donisia Minja, Esther Chabruma, Etoe Mlenzi, Everine Sekikubo, Fatuma Issa, Fatuma Makusanya, Fatuma Mwisendi, Fatuma Omari, Happiness Mwaipaja, Maimuna Mkane, Mwapewa Mtumwa, Sherida Boniface, Sophia Mwasikili, Therese Yona, Vumilia Maarifa na Zena Said.

RAIS MALINZI KUZUNGUMZA NA WAANDISHI WA HABARI
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi kesho
(Februari 14 mwaka huu) atakuwa na mkutano na waaandishi wa habari za
michezo.

Mkutano huo utafanyika saa 5 kamili asubuhi kwenye ofisi za TFF zilizopo
ghorofa ya tatu katika jengo la PPF Tower, mtaa wa Garden na Ohio jijini
Dar es Salaam.

Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari na Mawasiliano
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
+260 976375482
Lusaka, Zambia

FIFA yamruhusu Okwi kukipiga Yanga, kuanza na Ruvu Shooting

E-mail Print PDF

Emmanuel Okwi (katikati) akiwa na Juma Kaseja na Hamis Kiiza
Mshambuliaji wa kimataifa wa timu ya Uganda na timu ya Young Africans leo ameruhiswa ramsi kuanza kuitumikia timu yake katika michezo ya Ligi Kuu na Mashindano ya klabu Bingwa Barani Afrika kufuatia shirikisho la soka nchini TFF kuiandikia barua klabu ya Young Africans.
Okwi ambaye alisajiliw aa Young Africans mwishoni mwa mwaka jana na kucheza michezo ya kirafiki ya kujiandaa na msimu mpya, alisimamishwa na Shirikisho la Soka la Nchini TFF wakati wakisubiria kupata udhibitisho wa usajili wake kutoka FIFA.
Mara baada ya barua hiyo, Okwi anatarajiwa kuungana na wenzake mwishoni mwa wiki mara timu itakaporejea kutoka Visiwa vya Comoro na ataanza kuonekana katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom dhidi ya Ruvu Shooting siku ya jumamosi Februari 22 mwaka huu.
Uongozi wa Young Africans unawashukuru wanachama, wapenzi na wadau kwa ujumla kwa kuwa wavumilivu wakati wa suala na hili na hatimaye limepatiwa ufumbuzi.
Young Africans

Twanga Pepeta kuinogesha Valentine Day kesho Mzalendo Pub


BENDI ya muziki wa dansi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’ wanatarajia kuwapagawisha wapendanao watakapofanya onyesho maalum siku ya ‘Valentine Day’, kesho Ijumaa.
Onyesho hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Mzalendo Pub, Kijitonyama jijini Dar es Salaam, litajulikana kama 'Dodoma Wine Valentine Show'.
Mratibu wa onyesho hilo Joseph Kapinga amesema onyesho hilo limeandaliwa na Bob Entertainment na Keen Arts chini ya udhamini wa Dodoma Wine, Freditto Entertainment na Saluti5.
Kapinga alisema siku hiyo Twanga Pepeta watatambulisha nyimbo na staili mpya ya uchezaji.
Mratibu huyo alisema kuwa siku hiyo Twanga Pepeta pia itapiga nyimbo zao za zamani zilizowapatia umaarufu.
Baadhi ya nyimbo hizo ni Kisa Cha Mpemba, Fainali Uzeeni, Mtu Pesa, Safari 2005, Aminata, Busu  2000 na nyinginezo.
Bendi hiyo inayotamba kwa staili ya Kisigono pia itapiga nyimbo zao za kisasa kama 'Nyumbani ni Nyumbani', 'Dunia Daraja',  ‘Mwana Dar es Salaam’, ‘Shida ni Darasa’, ‘Rafiki Adui’, ‘Mwisho wa Ubaya ni Aibu’, ‘Nazi Haivunji Jiwe’ na ‘Sitaki Tena’.
Bendi hiyo inaundwa na wanamuziki kama Kalala Junior, Dogo Rama, Saleh Kupaza, Luiza Mbutu, Badi Bakule, Greyson Semsekwa, Rama Pentagon, Mirinda Nyeusi, Kala Junior, na Janet Isinika katika safu ya uimbaji.
Kwa upande wa upigaji vyombo wapo James  Kibosho, Jojo Jumanne, Moshi Kinanda, Miraji Shakashia, Gody Kanuti, Kaposho, huku safu ya unenguaji ikiwa, Saidi Matongee, Mandela, Abdilah Zungu,  Sabrina Pazi, Vicky, Hamida na Grace.

Azam Fc watua salama Beira, waanza kujifua kuikabili Ferroviario

Kikosi cha Azam kilichoinyoa Ferroviario ya Msumbiji Jumapili iliyopita
Msafara wa Azam ukifungfua kinywa
Na Patrick Kahemele, Beira Msumbiji
MSAFARA wa timu ya Azam upo katika hali nzuri hapa Beira Msumbiji ukijiandaa na mchezo wa marudiano wa Kombe la Shirikisho Afrika utakaopigwa Jumapili hii dhidi ya wenyeji Ferroviario da Beira.
 
Ujumbe mzima unaojumuisha watu 39 wakiwemo wachezaji 21, viongozi wa jopo la ufundi na maofisa wengine umefikia katika hoteli ya Rainbow Mozambique iliyopo Mtaa wa Bagamoyo hapa Beira ambayo ni hadhi ya nyota tatu.
 
Safari ya kutoka Dar es Salaam hadi Beira ilikamilika majira ya saa 1 usiku kwa saa za Msumbiji (Saa 2 usiku Tanzania) jana Jumatano baada ya kuunganisha ndege Johannesburg Afrika Kusini na kuruka kwa muda wa saa mbili hadi Beira.  

Mapema safari ya Dar es Salaam hadi Afrika Kusini ilichukua saa 3. Wachezaji wote wako katika hali nzuri kiafya na kisaiklojia
 
 Asubuhi leo timu imefanya mazoezi ya kwanza tangu kuwasili kwenye uwanja unaomilikiwa na klabu mwenyeji katika harakati za kusaka matokeo mazuri kuelekea hatua ya kwanza ya michuano ya Kombe la Shirikisho.
 
Azam inahitaji ushindi au sare ili iweze kusonga mbele kufuatia ushindi wa nyumbani wa 1-0 katika mchezo wa kwanza uliopigwa Azam Complex Dar es Slaam Jumapili iliyopita.
 
Ikiwa itafaulu kuwatoa Ferroviarrio Azam itapambana na washindi wa pili wa ligi ya Zambia, Zesco mwishoni mwanzoni mwa mwezi Machi.

Simba kuifuata Mbeya City kesho, kuvuna nini Sokoine?

Wachezaji wa Simba watashangilia kama hivi kwa Mbeya City au....!

Kinara wa mabao, Amissi Tambwe atawanyamazisha mashabiki wa Mbeya City Jumamosi uwanja wa Sokoine?
WEKUNDU wa Msimbazi, Simba inatarajiwa kuondoka kesho kwenda Mbeya kwa ajili ya kuwahi pambano lao dhidi ya wenyeji wao Mbeya City, ambayo imekuwa ikielezwa inajifua mchana wa jua kali ili kutafuta mbinu za kuendelea kuwatia machungu vijana wa Zdrakov Lugarusic.
Simba iliyotota kwa Mgambo JKT Jumapili iliyopita uwanja wa Mkwakwani kwa kufungwa bao 1-0, ilirejea jijini kwa ajili ya wachezaji kupata wasaa wa kukutana na Mwenyekiti wao, Ismail Aden Rage ili kuweka mambo sawa kabla ya kuondoka kesho kwa ndege kuwa ajili ya mechi hiyo na Mbeya City.
Mbeya City inayonolewa na kocha Juma Mwambusi, ilitoshana nguvu na Simba kwa kytoka sare ya 2-2 katika pambano lililochezwa jijini Dar es Salaam mwaka jana, itaikaribisha Simba Jumamosi kwenye uwanja wa Sokoine Mbeya ambayo umekuwa 'machinjio' kwa timu wapinzani.
Pambano hilo la Simba na Mbeya City linatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na nafasi ilizokuwa timu hizo ambapo Mbeya wameitangulia Simba kwa pointi tatu ikiwa nafasi ya tatu, nyuma yao 'mnyama' anafuata akiwa na pointi 31.
Vijana wa Msimbazi ambao tangu waanze kucheza mechi za ugenini kwenye duru la pili wamekuwa wakiyumba baada ya kunusurika kulala kwa Mtibwa Sugar waliotoka nao sare ya 1-1 kisha kwenda kuzama Mkwakwani, watalazimika kupata ushindi kwa Mbeya City ili kurejea nafasi ya tatu na kuwapumulia  watani zao Yanga. wanaoakamta nafasi ya pili nyuma ya Azam wanaoongoza ligi hiyo.
Simba ikiongozwa na kinara wa mabao katika ligi kwa msimu huu Amissi Tambwe na wakali wengine kama Ramadhani Singano 'Messi', Haruna Chanongo, Ali Badru, Awadh Juma, Jonas Mkude na kipa Ivo Mapunda hawatapenda kuona wakiteleza Jumamosi kwa Mbeya City iliyopanda ligi msimu huu.
Mbali na mechi hiyo inayosubiriwa kwa hamu siku hiyo pia kutakuwa na mechi nyingine kadhaa ikiwamo ya Mgambo JKT kuvaana na Rhino Rangers mjini Tabora, Ashanti United itaumana na Kagera Sugar uwanja wa Chamazi, jijini Dar na Oljoro JKT iliyokimbiwa na kocha wake Hemed Morocco itaikaribisha JKT Ruvu ambao jana waliteleza kwa ndugu zao wa Ruvu Shooting kwa kufungwa mabao 2-1.
Mechi nyingine siku hiyo ni Ruvu Shooting dhidi ya Coastal Union pambano litakalochezwa uwanja wa Mabatini-Mlandizi  mkoani Pwani.

Yanga kupaa leo bila Kaseja wala Tegete


Mabingwa wa Tanzania, Yanga wanaotarajiwa kuondoka leo mchana kwenda Comoro
KIKOSI cha wachezaji 19 wa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara wanaondoka nchini leo mchana kuelekea Comoro kwa ajili ya mechi ya marudiano ya mashindano ya Ligi ya Mabingwa wa Afrika dhidi ya Komorozine huku nyota kadhaa wakiachwa akiwamo kipa Juma Kaseja na mshambuliaji Jerryson Tegete.
Kaseja, ambaye mwanzoni mwa wiki alifanya mazoezi na wenzake na kisha kubaki kuendelea kujifua na timu ya taifa ya wanawake (Twiga Stars), ameachwa kwa sababu ni mgonjwa na tangu juzi hajafanya mazoezi na wachezaji wenzake, wakati Tegete anauguliwa na mama yake mzazi ambaye yuko jijini Mwanza.
Habari ambazo zimepatikana jijini Dar es Salaam zinaeleza kwamba kipa huyo aliyedaka dakika 90 katika mechi ya kwanza iliyofanyika Jumamosi iliyopita ana matatizo ambayo hawakutaka kuyaweka wazi.
Kwa mujibu wa chanzo cha gazeti hili, wachezaji wengine watakaoachwa katika safari hiyo ni pamoja na Nizar Khalfan, Salum Telela, Hussein Javu, Renatus Lusajo, Shabani Kondo, Bakari Masoud, Ibrahim Job na Emmanuel Okwi ambaye bado amesimamishwa na Shirikisho la Soka Nchini (TFF).
Wachezaji wanaotarajiwa kuondoka leo ni pamoja na Deogratius Munishi 'Dida', Ally Mustapha 'Barthez', Juma Abdul, Oscar Joshua, David Luhende, Nadir Haroub 'Cannavaro', Haruna Niyonzima 'Fabregas', Simon Msuva, Didier Kavumbagu,  Hamis Kizza, Mrisho Ngasa, Kelvin Yondani, Mbuyu Twite, Frank Domayo, Athumani Iddi 'Chuji' na Hassan Dilunga.
Benchi la Ufundi linaongozwa na Pluijm na msaidizi wake, Charles Mkwasa, kocha wa makipa, Juma Pondamali, daktari wa timu, Suphian Juma, meneja wa timu, Hafidh Saleh, mtunza vifaa, Mahmoud Omar 'Mpogolo' na mchua misuli, Jacob Onyango.
Viongozi ni Aaron Nyanda na Mohamed Bhinda (Kamati ya Utendaji), Ofisa Habari, Kizuguto na Ramadhan Nassib ambaye ni mkuu wa msafara kutoka Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Soka (TFF).
Afisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, alisema jana kuwa maandalizi ya safari yamekamilika na timu hiyo itaondoka leo alfajiri kwa ndege ya Shirika la Ndege la Precession.
Hadi jana mchana Kizuguto alisema kuwa taratibu zote za safari zimekamilika ila idadi ya wachezaji wanaondoka bado hawajaipokea kutoka benchi la ufundi.
Wawakilishi hao wa Bara wanaondoka nchini wakiwa na nafasi nzuri ya kusonga mbele kutokana na ushindi mnono wa mabao 7-0 walioupata kwenye mchezo wa kwanza uliofanyika Jumamosi iliyopita kwenye uwanja wa Taifa.
Kocha wa Yanga, Hans van der Pluijm, amesema kwamba wanakwenda Comoro kusaka ushindi wa pili na hawatabweteka na matokeo waliyopata hapa nyumbani.
Alisema pia wanapaswa kusaka mbinu kali za kuikabili Al Ahly katika raundi ya pili ya mashindano hayo.
Baada ya mazoezi ya timu yake kwenye Uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam jana asubuhi, Pluijm alisema anaamini timu yake itavuka hatua ya awali kwani iliibuka na ushindi mnono wa kutosha katika mechi yao ya kwanza, hivyo kazi iliyopo mbele yao kwa sasa ni kutafuta mbinu za kuwaua mabingwa hao wa Afrika, Al Ahly ambao watakutana nao baada ya kuing'oa Komorozine.
Raia huyo wa Uholanzi alisema timu yake kwa sasa iko vizuri na ilionyesha kiwango cha juu katika mechi iliyopita lakini bado inahitaji kupikwa zaidi kabla ya kuwavaa Al Ahly ambao walituma mashushushu katika mechi ya Jumamosi kwa ajili ya kuzisoma mbinu za Yanga.
Alisema wapinzani wao katika hatua ya pili ya mashindano hayo, Al Ahly ya Misri wana kikosi kizuri na wana uzoefu mkubwa wa mashindano hayo.
“Tumeonyesha kiwango kizuri katika mechi ya nyumbani, ingawa bado tunatakiwa kwenda Comoro kurudiana na baada ya hapo tunakutana na Al Ahly ya Misri. Naifahamu vizuri timu hiyo maana niliwahi kukutana nayo, lazima ujipange vizuri kabla ya kucheza nao," alisema Pluijm.
“Timu yetu kwa sasa ni nzuri na tunandelea kujipanga vizuri kwa ajili ya mchezo huo kwa sababu lengo letu kubwa ni timu kufika mbali katika mashindano hayo. Nafikiri hayo ndiyo matarajio ya wapenzi wa Yanga na Watanzania kwa ujumla.
“Lakini kwa sasa nafikiri tunapaswa kuelekeza nguvu zetu katika mchezo uliopo mbele yetu dhidi ya Komorozine na baada ya hapo tutawageukia Al Ahly," alisema zaidi kocha huyo ambaye aliwahi kuvaana na Al Ahly wakati akikinoa kikosi cha timu ya Berekum Chelsea ya Ghana.
Endapo Yanga itasonga mbele itakutana na mabingwa wa zamani wa michuano hiyo, Al Ahly ya Misri mapema mwezi ujao.
NIPASHE

Hizi ndizo kamati za TFF ya Jamal Malinzi

BOARD OF TRUSTEE; Said Hamad El-Maamry, Stephen Mashishanga, Dr Ramadhan Dau, Joel Bendera, Mohamed Abdul Aziz

Kamati ya Nidhamu; Tarimba Abbas (Mwenyekiti), Advocate Jerome Msemwa (Makamu Mwenyekiti), Kassim Dau, Nassoro Duduma, Kitwana Manara.
Kamati ya Rufani ya Nidhamu; Profesa Mgongo Fimbo (Mwenyekiti), Advocate Hamidu Mbwezeleni (Makamu Mwenyekiti), Titus Bandawe, Twaha Mtengera, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP) mstaafu Boniface Mpaze.
Kamati ya Maadili; William Erio (Mwenyekiti), Advocate Ezekiel Maganja (Makamu Mwenyekiti), Advocate Victoria Mandari, Kanali mstaafu Enos Mfuru na Said Mtanda.
Kamati ya Rufani ya Maadili; Jaji mstaafu Stephen Ihema (Mwenyekiti), Wakili Alesia Mbuya (Makamu Mwenyekiti), Lilian Kitomari, Jabir Shekimweri na Chabanga Hassan Dyamwale.
Kamati ya Uchaguzi; Advocate Melchesedeck Lutema (Mwenyekiti), Advocate Walter Chipeta (Makamu Mwenyekiti), Hamidu Mahmoud Omar, Jeremiah John Wambura, Hassan Dalali.
Kamati ya Rufani ya Uchaguzi; Advocate Julius Lugaziya (Mwenyekiti), Advocate Mwita Waissaka (Makamu Mwenyekiti), Juma Abeid Khamis, Rashid Dilunga, Masoud Issangu.
Kamati ya Fedha na Mipango; Wallace Karia (Mwenyekiti), Francis Ndulane (Makamu Mwenyekiti), Omari Walii, Eliud Mvella, Said Muhammad, Geofrey Nyange, Kidao Wilfred, Ayoub Nyenzi, Lina Kessy, Cyprian Kuhyava.
Kamati ya Mashindano; Geofrey Nyange (Mwenyekiti), Clement Sanga (Makamu Mwenyekiti), Msafiri Mgoyi, James Mhagama, Mohamed Nassoro, Moses Katabaro, Seif Ahmed, Gerald Ambi, Davis Mosha, Said George, Nassoro Idrissa (Mshauri wa Rais Ufundi- Pelegrinius Rutayuga).
Kamati ya Ufundi; Kidao Wilfred (Mwenyekiti), Athumani Kambi (Makamu Mwenyekiti), Vedastus Lufano, Blassy Kiondo, Rahim Kangezi, Patrick Kahemele, Daud Yassin, Nicholas Mihayo, Dk. Cyprian Maro (Mshauri wa Rais Ufundi- Pelegrinius Rutayuga).
Kamati ya Mpira wa Miguu wa Vijana; Ayoub Nyenzi (Mwenyekiti), Khalid Abdallah (Makamu Mwenyekiti), Ali Mayay, Mulamu Ng’hambi, Apollo Kayungi, Said Tully, Luteni Kanali Charles Mbuge, Lameck Nyambaya, Ibrahim Masoud (Mshauri wa Ufundi wa Rais- Pelegrinius Rutayuga).
Kamati ya Mpira wa Miguu wa Wanawake; Lina Kessy (Mwenyekiti), Shyrose Bhanji (Makamu Mwenyekiti), Zena Chande, Amina Karuma, Dk. Cecilia Makafu, Zafarani Damoder, Beatrice Mgaya, Sofia Tigalyoma, Martin Mung’ong’o, Ingridy Kimaro.
Kamati ya Waamuzi; Saloum Umande Chama (Mwenyekiti), Nassoro Said (Makamu Mwenyekiti), Charles Ndagala (Katibu), Riziki Majala, Kanali Isaro Chacha, Paschal Chiganga, Victor Mwandike, Soud Abdi, Zahra Mohamed.
Kamati ya Habari na Masoko; Hamad Yahya Juma (Mwenyekiti), Naibu Waziri January Makamba (Makamu Mwenyekiti), Tido Mhando, Yusuf Manji, Yusuf Bakhresa, Samwel Nyalla, Jack Gotham, Fredrick Mwakalebela, Juma Pinto.
Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji; Advocate Richard Sinamtwa (Mwenyekiti), Advocate Moses Kaluwa (Makamu Mwenyekiti), Zacharia Hans Poppe, Hussein Mwamba, Philemon Ntahilaja, Abdul Sauko, Imani Madega.
Kamati ya Ukaguzi wa Fedha; Ramadhan Nassib (Mwenyekiti), Zitto Kabwe (Makamu Mwenyekiti), Nicholas Magarinza, Jackson Songora, Epaphra Swai, Kalilo Samson, Goodluck Moshi, Golden Sanga, Elias Mwanjala.
Kamati ya Tiba; Dk. Paul Marealle (Mwenyekiti), Dk. Fred Limbanga (Makamu Mwenyekiti), Dk. Mwanandi Mwankemwa, Dk. Nassoro Matuzya, Dk. Eliezer Ndelema, Asha Sadick.
Kamati ya Mpira wa Miguu wa Ufukweni; Ahmed Idd Mgoyi (Mwenyekiti), Shaffih Kajuna Dauda (Makamu Mwenyekiti), Boniface Pawasa, Deo Lucas, Juma Mgunda, John Kanakamfumu, John Mwansasu.
AD HOC COMMITTEES
Kamati ya Kutathimini Muundo wa Ligi; Dk. Mshindo Msolla (Mwenyekiti),Idd Mshangama (Katibu), Rahim Kangezi, Amri Said, Sunday Manara, Salim Bawazir, Lucas Kisasa.
Kamati ya Kutathimini Muundo wa Bodi ya Ligi; David Nchimbi (Mwenyekiti), Edwin Kidifu, Jones Paul, Evans Aveva, John Jambele, Masoud Sanani, Pelegrinius Rutayuga.

Moto waleta kizaazaa Chuo cha Polisi (CCP)- Moshi

Wanafunzi wa chuo cha taaluma ya polisi Moshi wakijaribu kuzima moto na kuokoa mali zilizokuwa zikiungua katika moja ya stoo ya kuhifadhia vitu mbalimbali zikiwemo nguo baada ya kuzuka kwa moto katika jengo hilo.
Hakuna mtu aliyeripotiwa kudhurika na Mkuu wa Chuo hicho Kamishana Msaidizi wa Polisi Matanga Mbushi ameahidi kutoa taarifa kamili baadaye.
 


Askari wanafunzi wakipambana na moto kwa kila jinsi


Mapambano na moto yanaendelea


Baadhi ya vitu vikiokolewa kutoka katika jengo lililowaka moto.


Juhudi za kuondoa vifaa vilivyookolewa kabla ya kuteketea kwa moto


Wanafunzi wakipambana na moto







Sare za askari zikiwa zimeokolewa toka katika jengo hilo.

Moja ya kifaa kilichopo chuoni hapo ambacho pia kilikuwa kikitumika kwa shughuli za kuzima moto katika jengo hilo .Mkuu wa chuo hicho Matanga Mbushi amesema taarifa kamili ya moto huo itatolewa baadae.


Kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro Robert Boaz akiwa na mkuu wa Chuo cha taaluma ya Polisi kamishana msaidizi wa polisi Matanga Mbushi wakishuhudia zoezi la uzimaji moto katika jengo hilo.






CHANZO MATUKIO ISSA MICHUZI
Wanafunzi wa chuo cha taaluma ya polisi Moshi wakijaribu kuzima moto na kuokoa mali zilizokuwa zikiungua katika moja ya stoo ya kuhifadhia vitu mbalimbali zikiwemo nguo baada ya kuzuka kwa moto katika jengo hilo.
Hakuna mtu aliyeripotiwa kudhurika na Mkuu wa Chuo hicho Kamishana Msaidizi wa Polisi Matanga Mbushi ameahidi kutoa taarifa kamili baadaye.
 


Askari wanafunzi wakipambana na moto kwa kila jinsi


Mapambano na moto yanaendelea


Baadhi ya vitu vikiokolewa kutoka katika jengo lililowaka moto.


Juhudi za kuondoa vifaa vilivyookolewa kabla ya kuteketea kwa moto


Wanafunzi wakipambana na moto







Sare za askari zikiwa zimeokolewa toka katika jengo hilo.

Moja ya kifaa kilichopo chuoni hapo ambacho pia kilikuwa kikitumika kwa shughuli za kuzima moto katika jengo hilo .Mkuu wa chuo hicho Matanga Mbushi amesema taarifa kamili ya moto huo itatolewa baadae.


Kamanda wa polisi mkoa wa Kilimanjaro Robert Boaz akiwa na mkuu wa Chuo cha taaluma ya Polisi kamishana msaidizi wa polisi Matanga Mbushi wakishuhudia zoezi la uzimaji moto katika jengo hilo.






CHANZO MATUKIO ISSA MICHUZI