STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, July 26, 2013

Suarez ruksa kuteta na Arsenal, ila...!

http://i.telegraph.co.uk/multimedia/archive/02489/luis-suarez_2489623b.jpg
LONDON, Uingereza
LUIS Suarez ataruhusiwa kufanya mazungumzo na Arsenal baada ya klabu hiyo ya London kufikisha ofa ya paundi milioni 40 lakini Liverpool haiko tayari kumuuza mshambuliaji huyo hadi bei ya paundi milioni 50 itakapofikiwa.
Ofa iliyoweka rekodi ya Arsenal ya paundi milioni 40 jumlisha paundi moja ilikataliwa na Liverpool lakini Suarez sasa anataka kufanya mazungumzo na klabu hiyo ya London.
Ripoti nyingine zinasema mshambuliaji huyo amewaambia maafisa wa Liverpool kwamba anataka kujiunga na Arsenal na anajiandaa kuwasilisha barua ya kuomba kuondoka Anfield.
Ofa ya paundi milioni 40 inamaanisha kwamba kipengele cha kuvunjia mkataba wake kimefikiwa na hivyo ni lazima Liverpool imfahamishe kuhusu ofa hiyo na sasa yuko huru kuzungumza na Arsenal.
Arsenal wanajiandaa kumlipa Suarez mshahara wa paundi 150,000 (Sh. milioni 364) kwa wiki kwa mkataba wa miaka mitano.
Lakini Liverpool haiko tayari kumuuza hadi Arsenal watakapoongeza ofa yao.
Juzi Jumatano, Suarez aliichezea Liverpool kwa mara ya kwanza tangu tukio maarufu la kumng'ata mkononi beki wa Chelsea, Branislav Ivanovic msimu uliopita, akiingia kutokea benchi katika dakika 18 za mwisho za mechi yao ya kirafiki waliyoshinda 2-0 dhidi ya Melbourne Victory kwenye Uwanja wa MCG.
Huku Liverpool ikiongoza kwa goli 1-0, Suarez alipika goli la pili la timu hiyo wakati alipomtengea mchezaji mpya Iago Aspas katika dakika za lala salama.
Baada ya mechi hiyo kocha wa Liverpool, Brendan Rodgers alisema: "Hakuna kipya cha kueleza, yeye (Suarez) ni mchezaji wa Liverpool na ndani ya wiki chache zijazo tunahitaji kumrejeshea kasi yake."
Rodgers hata hivyo, alimkumbusha Suarez deni alilonalo kwa mashabiki wa Liverpool ambao walisimama upande wake kwa misimu miwili ambayo ametawaliwa na matukio ya utata.
"Sapoti aliyopata kutoka kwa mashabiki na watu wa mji wa Liverpool haipimiki," Rodgers aliongeza.
"Katika kipindi hicho alikosa mechi nyingi za timu kutokana na sababu mbalimbali. Watu walisimama upande wake kama mtoto wao na hakika walikuwa wakimtetea. Chochote kitakachotokea katika wiki zijazo jambo hilo litabaki akilini mwake kwa sababu ni mambo ambayo huwezi kuyasahau."
Liverpool sasa wamekataa ofa mbili kutoka Arsenal, ambao wamedhamiria kuimarisha safu yao ya ushambuliaji, wakati Real Madrid, ambao tayari wamemuuza Gonzalo Higuain kwa Napoli, bado pia wanamhitaji nyota huyo wa Uruguay licha ya kwamba hawajapeleka ofa yoyote.
Kufuatia ofa mpya ya Arsenal, mmiliki wa Liverpool, John Henry aliwakebehi katika ukurasa wake wa Twitter kwa kuandika: "Unadhani wanavuta/puliza nini kule Emirates?"
Haijawa wazi kama kama Henry anazungumzia majaribio ya Arsenal kutaka kumsajili Suarez au kiasi cha ofa wanazotuma.
Wakati Liverpool wanadhamiria kumbakisha Suarez, ambaye alifunga magoli 30 katika mechi 44 za klabu hiyo msimu uliopita, ugumu wao unatarajiwa kulegea kama kama ofa hiyo itazidi kuongezwa. Kama ofa ya Arsenal itakubaliwa, itakuwa ni zaidi ya mara mbili ya kiwango cha juu cha pesa walichotoa kumnunua mchezaji.
Arsenal, ambao ofa yao ya kwanza kwa Suarez ilikuwa ni paundi milioni 30, walilipa paundi milioni 17.5 kumnunua winga wa Sevilla, Jose Antonio Reyes mwaka 2004.
Suarez anataka kuondoka Anfield ili akacheze soka la Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya licha ya kwamba alisaini kurefusha mkataba wake Liverpool mwaka jana tu.
Uvumi ulianza kukua kuhusu hatma ya Suarez tangu alipofungiwa mechi 10 mwishoni mwa Aprili kwa kumng'ata Ivanovic.
Mshambuliaji huyo amebakisha mechi sita za kutumikia katika kifungo chake na pia alifungiwa mwaka 2011 baada ya kukutwa na hatia ya kumfanyia vitendo vya kibaguzi beki wa Manchester United, Patrice Evra.
Suarez alijiunga na Liverpool akitokea Ajax Januari 2011 kwa ada ya uhamisho ya paundi milioni 22.7.
Wachezaji walionunuliwa na Arsenal kwa pesa nyingi zaidi ni Jose Antonio Reyes (paundi milioni 17.5 kutoka Sevilla), Santi Cazorla (paundi milioni 16, Malaga), Andrey Arshavin (paundi milioni 15, Zenit St Petersburg), Sylvain Wiltord (paundi milioni 13, Bordeaux) na Thierry Henry (paundi milioni 11, Juventus).

Simba, Coastal kuvaana Mkwakwani J2


TIMU ya soka ya Simba ya jijini Dar es Salaam inatarajiwa kuvaana na 'ndugu' zao, Coastal Union ya Tanga katika pambano la kirafiki na kujiandaa na Ligi Kuu Tanzania Bara itakayoanza Agosti 24 litakalochezwa kwenye uwanja wa Mkwakwani siku ya Jumapili.
Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga alisema lengo la mechi hiyo ni pamoja na kuwaandaa wachezaji wao kabla ya kuanza kampeni ya kuwania kurejesha taji lao walilolipoteza kwa mahasimu wa jadi, Yanga.
Alisema mechi hiyo itatoa nafasi kwa mashabiki wa Simba waliopo jijini Tanga kuwafahamu wachezaji wapya waliosajiliwa kwa ajili ya msimu mpya.
Alisema mara baada ya mechi hiyo wachezaji wa Simba watarejea jijini Dar es Salaam kujiandaa na mechi nyingine dhidi ya timu ya Kombaini ya Majeshi itakayopigwa Agosti 3 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Coastal itavaana na Simba ikiwa na kumbukumbu ya kuinyuka URA kwa bao 1-0, huku Simba ikiwa inauguza kipigo toka kwa Wakusanya ushuru hao wa Uganda waliowadungua mabao 2-1.

Tanzania yaanza vibaya michuano ya Wavu Uganda


Athuman Rupia (kulia) akiwa na mchezaji mwenzake wa timu ya taifa ya wavu
TIMU ya taifa ya mchezo wa Wavu ya Wanaume ya Tanzania jana ilianza vibaya michuano ya Kanda ya Tano kuwania kufuzu fainali za kimataifa za mchezo huo FIVB World Cup 2014 zitakazofanyika Poland baada ya kutandikwa na Wakenya kwa seti 3-0.
Michuano hiyo ya Kanda ya Tano Afrika, inafanyika nchini Uganda kwenye uwanja wa MTN Sports uliopo Lugogo jijini Kampala ikishirikisha timu nne wakiwamo wenyeji Uganda.
Kwa mujibu wa mmoja wa wachezaji wa timu hiyo, Athuman Rupia aliyezungumza na MICHARAZO kwa njia ya simu asubuhi hii kutoka Uganda, ni kwamba Tanzania ilishindwa kufuruka kwa Wakenya kutokana na hali ya uchovu waliokuwa nao baada ya kutua nchini humo majira ya asubuhi na jioni kushuka dimbani.
"Tumeanza vibaya michuano ya Kanda ya Tano kuwania Fainali za Kombe la Dunia baada ya kufungwa sti 3-0 na Wakenya, ila tunaamini uchovu umechangia kipigo chetu na tunajipanga kwa mechi zilizosalia dhidi ya Burundi na wenyeji Uganda," alisema Rupia anayeichezea pia timu ya Jeshi Stars.
Jumla ya timu za taifa za nchi nne tu kati ya sita zilizotarajiwa kushiriki michuano hiyo ndizo zinazochuana jiji Kampala baada ya  wakali kutoka Sudan na Rwanda kujioengua dakika za lala salama na kuziacha Kenya, Uganda, Tanzania na Burundi zikionyeshana kazi kuwania nafasi tatu za Kanda hiyo ya Tano.

Thursday, July 25, 2013

Hatimaye Javu atua rasmi Jangwani

Mshambuliaji mpya wa timu ya Yanga Hussein Javu














HATIMAYE klabu ya soka ya Yanga imekamilisha usajili wa mshambuliaji nyota wa timu ya Mtibwa Sugar, Hussein Javu ambapo mchezaji huyo asubuhi ya leo alianza mazoezi Jangwani.
Javu ambaye alikuwa akisisitiza kuwa alikuwa hajasaini kokote licha ya kutangazwa alishasajiliwa na klabu hiyo, zoezi lake la kutua Jangwani lilikamilika leo na kuungana na wenzake katika  mazoezi kwenye uwanja wa shule ya sekondari Loyola Mabibo jijini Dar es salaam.
Hussein Javu amesajili Young Africans kwa mkataba wa miaka miwili ambapo atavaa jezi za watoto wa Jangwani mpaka mwishoni mwa msimu wa 2014/2015.
Usajili wa Javu unafikisha idadi ya washambuliaji sita mpaka sasa wakiwemo Didier Kavumbagu, Jerson Tegete, Said Bahanuzi, Shaban Kondo (mpya - Msumbiji) na Realintus Lusajo (mpya kutoka Machava FC - Moshi).
Kikosi cha Mholanzi Ernie Brandts kinaendelea na mazoezi kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom unaotarajiwa kuanza agosti 24 kwa kufungua dimba na timu ya Ashanti United iliyopanda msimu huu.
Agosti 17-2013  Young Africans itacheza mchezo wa Ngao ya Hisani na timu ya Azam FC katika uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam ikiwa ni ishara ya ufunguzi wa pazia la Ligi Kuu kwa msimu wa 2013/2014.
Mpaka sasa klabu ya Yanga imekamilisha usajili wa wachezaji saba (7) wapya ambao ni:
1. Deogratius Munishi 'Dida' -  Huru Azam FC (Golikipa)
2.Rajab Zahir -  Huru Mtibwa Sugar  (Mlinzi wa kati)
3.Hamis Thabit - Huru Ureno (Kiungo)
4.Shaban Kondo - Huru Msumbiji (Mshambuliaji)
5.Mrisho Ngassa - Huru Azam FC (Kiungo mshambuliaji)
6.Reanlintus Lusajo - Huru Machava FC (mshambuliaji)
7. Hussein Javu - Mtibwa Sugar (mshambuliaji)
Kikosi kinaendelea na mazoezi katika uwanja wa shule ya sekondari Loyola kila siku saa 2 asubuhi na wachezaji waliopo katika timu ya Taifa Tanzania (Taifa Stars) wanatarajiwa kuungana na wenzao katika mazoezi siku ya jumatatu.

Young SC

Hivi ndivyo ilivyokuwa Siku ya Mashujaa Tanzania

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akiweka ngao na sime katika mnara wakati wa maadhimisho ya kumbukumbu ya Mashujaa katika kambi ya jeshi ya Kaboya, Bukoba, mkoani Kagera leo Julai 25, 2013


Viongozi wa dini wakisoma dua kwenye maadhimisho hayo. Pembeni ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Mohamed Ali Shein, Makamu wa Rais Dkt Mohamed Gharib Bilali, Jaji Mkuu Mheshimiwa Chande Othman na Jaji Mkuu wa Zanzibar Mhe Othman Makungu




Rais Jakaya Kikwete akitembelea makaburi ya mashujaa waliopoteza maisha wakati wa vita na Nduli Iddi Amini wa Uganda

                                  Rais JK akisalimiana na askari wastaafu




Maskini Kibosile wa Home Shopping Centre!


MFANYABIASHARA maarufu na Mmiliki wa maduka ya Home Shopping Center (HSC), Said Mohamed Saad, ambaye wiki iliyopita alimwagiwa tindikali maeneo ya Msasani City Mall, jijini Dar es Salaam, sasa yuko Afrika Kusini kwa matibabu zaidi .

Wiki iliyopita majira ya saa moja jioni, mfanyabiashara huyo alimwagiwa tindikali na mtu mmoja ambaye hakufahamika na mara baada ya kutenda tukio hilo, mhusika alikimbia huku mlinzi wa eneo hilo akijaribu kumkimbiza pasipo mafanikio baada ya kuteleza na kuanguka.

Hatua hiyo ilitoa mwanya kwa mtuhumiwa kutoroka eneo la tukio kwa kutumia usafiri aina ya pikipiki.

Hapo awali ilidaiwa kuwa Saad alikuwa anaweza kuzungumza japo amefungwa mashine sehemu ya pua kwa ajili ya kumsaidia kupumua.  Matukio ya watu kumwagiwa tindikali yameonekana kushamiri nchini katika siku za hivi karibuni.

Tukio la kumwagiwa tindikali mmiliki huyo wa Home Shopping Centre, limekuja ikiwa ni takribani wiki mbili tangu Sheikh Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha, Said Juma Makamba naye ajeruhiwe vibaya usoni kwa kumwagiwa maji maji yanayosadikiwa kuwa ni tindikali majira ya usiku akiwa nyumbani kwake.SOURCE BOFYA HAPA

Vialli kuwakosa Uganda The Cranes Jumamosi?

Vialli (kati) anayeweza kuikosa Uganda Jumamosi

Na Boniface Wambura
TIMU ya taifa, Taifa Stars imewasili salama hapa Kampala tayari kwa mechi ya marudiano ya mchujo dhidi ya Uganda (The Cranes) kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Tatu za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.

Stars ambayo iliwasili ikitokea jijini Mwanza ilipokuwa imepiga kambi ya siku kumi kujiandaa kwa mechi hiyo itakayoamua ni timu ipi kati ya hizo mbili itakwenda Afrika Kusini mwakani imefikia hoteli ya Mt. Zion iliyoko eneo la Kisseka katikati ya Jiji la Kampala.

Kocha Mkuu wa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager, Kim Poulsen ameridhishwa na kiwango cha hoteli hiyo, kwani ndiyo ambayo timu ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) ilifikia Novemba mwaka jana ilipokuja Kampala kushiriki michuano ya Kombe la Chalenji inayoandaliwa na Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).

Stars ambayo ilitiwa chachu na Rais Jakaya Kikwete alipokutana nayo Uwanja wa Ndege wa Mwanza wakati ikiondoka kuja Kampala, na kuitakia kila la kheri itafanya mazoezi yake ya mwisho kesho (Julai 26 mwaka huu) Uwanja wa Mandela kujiandaa kwa mechi ya Jumamosi.

Kocha Kim amesema ingawa mechi hiyo ni ngumu, lakini kikosi chake kimejiandaa kuikabili Uganda kwani wachezaji wako wako vizuri na ari kwa ajili ya mechi iko juu.

Wachezaji wote wako katika hali nzuri, isipokuwa Khamis Mcha aliyekuwa na maumivu ya goti, lakini kwa mujibu wa madaktari wa timu anaendelea vizuri kwani tayari wanampa mazoezi mepesi.

Kikosi cha kamili cha Stars ilichoko hapa kinaundwa na makipa Juma Kaseja, Mwadini Ali na Ali Mustafa. Mabeki ni Aggrey Morris, David Luhende, Erasto Nyoni, Kelvin Yondani, Nadir Haroub na Vincent Barnabas.

Viungo ni Amri Kiemba, Athuman Idd, Frank Domayo, Haruni Chanongo, Khamis Mcha, Mudhathir Yahya, Salum Abubakar na Simon Msuva. Washambuliaji ni John Boko, Juma Luizio na Mrisho Ngasa.

Wakati huo huo, Kocha Kim Poulsen atakuwa na Mkutano na Waandishi wa Habari siku ya Jumatatu (Julai 29 mwaka huu). Mkutano huo utafanyika saa 5 kamili asubuhi katika ukumbi wa mikutano wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

JUma Fundi, Nasibu Ramadhani hapatoshi Idd Pili

IMG_4971
Mabondia Juma Fundi (kushoto) na Nasibu Ramadhani (kulia) wakinyakuliwa mikono na mratibu wa pambano lao la Idd Pili

BONDIA Nassibu Ramadhani na Juma Fundi ambao ni wapinzani wa jadi wanatarajiwa kuvaana kayika pambano litakalofanyika siku ya Idd Pili, huku wakitambiana.
Mabondia hao watavaana kwenye ukumbi wa Friends Corners katika pambano la kumaliza ubishi baina yao baada ya kutambiana kwa muda mrefu kila mmoja akijinasibu kuwa ni mkali zaidi ya mwenzake.
Pambano hilo litakalokuwa la raundi 10 linaratibiwa na Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Tanzania (PST).
Bondia Nasibu Ramadhani amesema hana hofu na mpinzani wake kwa sababu anamuona mwepesi kwa vile alishampinga na kutwaa ubingwa wa Dunia wa WB-Forum.
"Anayeniumiza kichwa katika uzito wa Bantam ni Francis Miyeyusho pekee, wengine nawaona wa kawaida tu," alisema Nasibu.
Bondia huyo alisema Fundi atarajie kipigo kikali toka kwake kwani amejiandaa vyema ili kuendeleza rekodi ya ubabe kwa mpinzani wake huyo.
Hata hivyo Fundi alisema yeye hana maneno mengi anasubiri kwa hamu siku ya pambani lifike ili aweze kuzima kilimilimi cha Nasibu.
"Tunaandikia mate ya nini wakati wino upo, tusubiri Idd Pili kisha tujue nani mbabe kati yangu na Nasibu, nimejiandaa kufanya vyema siku hiyo," alisema.

Falcao akana kuwa 'kijeba'

Falcao (kushoto) alipokuwa Atletico Madrid
PARIS, Ufaransa
MSHAMBULIAJI mpya wa klabu iliyorejea Ligi Kuu nchini Ufaransa ya Monaco, Radamel Falcao amekanusha ripoti zinazodai kwamba alidanganya kuhusu umri wake, huku vyombo mbalimbali vya habari vikidai mfumania nyavu huyo ni 'kijeba' akiwa kazaliwa mwaka 1984 tofauti na unaofahamika wa 1986.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Colombia, ambaye alikamilisha uhamisho wa kutua Monaco katika kipindi hiki cha usajili kwa ada ya uhamisho ya euro milioni 60 mwezi Juni, anatuhumiwa kudanganya tarehe yake ya kuzaliwa kufuatia kutolewa kwa rekodi zake za shule ambazo zinaonyesha kwamba mshambuliaji huyo ana umri wa miaka 29.
Kwa mujibu wa rekodi za usajili za mshambuliaji huyo za Fifa, Falcao alizaliwa Februari 10, 1986 lakini kituo cha televisheni cha Noticias Uno cha Colombia kimedai kuwa nyota huyo alizaliwa miaka miwili kabla.
Hata hivyo, nyota huyo wa zamani wa Atletico Madrid alitumia ukurasa wake wa Twitter kukanusha uvumi huo, ambao aliuelezea kuwa ni "upuuzi mtupu".
Aliandika: "Nimeshangazwa na ripoti hizi mpya zilizozunguka umri wangu, na madai haya ni upuuzi mtupu."
"Napenda kukanusha madai haya na naufunga rasmi mjadala huu."
Falcao alipata uhamisho wake wa pesa nyingi wa kutua Monaco baada ya kufunga magoli 70 katika mechi 90 akiwa na Atletico aliyodumu nayo kwa misimu miwili tu.

Joseph Owino 'aota' mbawa Msimbazi


Joseph Owino alipokuwa akiichezea Simba
JUHUDI za viongozi wa klabu ya Simba kutaka kumrejesha beki wa zamani wa timu hiyo, Joseph Owino kutoka Mamlaka ya Mapato ya Uganda (URA), zimegonga mwamba baada ya kukosekana pesa za kumlipa.
Mbali ya kukosekana kwa pesa anazotaka mchezaji huyo, uongozi wa URA  umegoma kumuuza Owino kwa Simba kwa vile amepata ofa nzuri ya kwenda kucheza soka ya kulipwa Qatar, Vietnam na China.
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hanspope alisema mjini Dar es Salaam jana kuwa, wameshafanya mazungumzo na Owino na kukubaliana naye mambo kadhaa, lakini dau analotaka ni kubwa.
Hata hivyo, Hanspope hakuwa tayari kutaja dau hilo, lakini alisisitiza kuwa bado wanaendelea na juhudi za kutafuta pesa ili waweze kukamilisha usajili wa mchezaji huyo.
Owino aliichezea Simba msimu wa 2009/2010 akiwa na Emmanuel Okwi na Hilaly Echessa kutoka Kenya na kuiletea mafanikio makubwa, lakini aliachwa msimu uliofuata baada ya kuumia goti.
Baada ya kuumia, beki huyo mahiri alipelekwa India kupatiwa matibabu na aliporea nchini alijiunga na Azam FC, lakini alishindwa kuichezea kutokana na kukosa namba na kuamua kurejea Uganda.
Owino alionyesha umahiri mkubwa katika mechi mbili za kirafiki za kimataifa, ambazo URA ilicheza dhidi ya Simba na Yanga. Katika mechi hizo zilizochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, URA iliichapa Simba mabao 2-1 kabla ya kutoka sare ya mabao 2-2 na Yanga.
"Kimsingi tumeshazungumza na Owino na ameikubali ofa tuliyompa ili aweze kurudi tena Simba, lakini bado kuna masuala yanayohusu pesa, ambayo hatujayakamilisha,"alisema Hanspope.
Mwenyekiti huyo wa kamati ya usajili ya Simba alisema, kutokana na benchi la ufundi kuvutiwa na kiwango cha beki huyo, watafanya kila wanaloweza kuhakikisha anarejea Msimbazi na kucheza katika ligi kuu msimu ujao.
Wakati Simba ikiwa katika mikakati hiyo, Meneja wa URA, Sam Okabo amesema hawawezi kumruhusu Owino arejee Simba kwa sababu ampata ofa nzuri Marekani na Asia.
Okabo alisema jana kuwa, si rahisi kwa Owino kurejea Simba kama viongozi wa klabu hiyo wanavyotaka kwa vile mchezaji huyo ni lulu kwa sasa na anawindwa na klabu nyingi.
Kwa sasa, Simba imesaliwa na wachezaji wawili wa kigeni, Abel Dhaira na Hamis Tambwe baada ya uongozi kuvunja mkataba wa Mussa Mudde na pia kusitisha mpango wa kumsajili Robert Ssenkoom kutokana na benchi la ufundi kutoridhishwa na kiwango chake.
Katika hatua nyingine, Hanspope amesema mshambuliaji mpya wa timu hiyo, Hamis Tambwe kutoka Burundi anatarajiwa kuwasili nchini Jumanne na kujiunga na timu hiyo kwenye kambi yake iliyopo Mbamba Beach, Kigamboni, Dar es Salaam.

LIWAZO

Ajali ya treni yaua 78, wengine 140 Hispania

Watu 20 wamepoteza maisha


WATU zaidi ya 70 wamefariki na wengine 140  katika ajali mbaya ya treni inayoenda kasi ilitokea Kaskazini Magharibi ya Hispania.
Abiria hao walifariki wakati wakisafiri na treni hiyo kabla ya kupata ajali na kwamba baadhi ya majeruhi hali zao ni mbaya.
Moja ya mabehewa limeonekana likiwa linawaka moto na jingine kukatika katikati kwenye eneo la ajali hiyo karibu na Santiago De Compostela ambapo treni hiyo ilikuwa ikisafiri kuelekea Ferrol Northwest nchini humo.

Msondo yaingia studio, kula Idd Dar, Zenji

Baadhi ya wanamuziki wa Msondo Ngoma wakiwajibika
BENDI kongwe ya muziki wa dansi nchini Msondo Ngoma 'Baba ya Muziki' imetumia muda wake wa mapumziko kuingia studio kurekodi nyimbo zilizosalia za albamu yao, huku ikiweka bayana ratiba nzima ya Sikukuu za Idd el Fitri.
Msemaji wa bendi hiyo, Rajabu Mhamila 'Super D' aliiambia MICHARAZO kuwa, wameona ni vyema kuutupia muda wa likizo ya mfungo wa Ramadhani kurekodi nyimbo za albamu yao ambayo inasubiriwa kwa muda mrefu na mashabiki wao.
Super D, alisema nyimbo zinazorekodiwa kwa sasa katika studio moja ya jijini Dar es Salaam ni Lipi Jema na Baba Kibebe zilizotungwa na Eddo Sanga, Kwa Mjomba Hakuna Urithi wa Huruka Uvuruge, Nadhiri ya Mapenzi wa Juma Katundu na Machimbo.
Wimbo wa Machimbo umeingia kwenye albamu hiyo baada ya kuondolewa kwa kibao kilichokuwa kimetungwa na aliyekuwa muimbaji wao, Isihaka Katima 'Papa Upanga' uitwao 'Dawa ya Deni' na kibao cha mwisho cha albamu hiyo kilichobeba jina wa Suluhu wenyewe ulishakamilika kitambo.
Aidha Super D aliweka wazi kwamba bendi yao katika shamrashamra za Sikukuu za Idd el Fitri, watatambulisha baadhi ya nyimbo mpya katika maonyesho yatakayofanyika kwenye ukumbi wa  DDC Kariakoo kwa onyesho la Idd Mosi na Idd Pili watakamua TCC Chang'ombe kabla ya kuvuka bahari kuelekea Zanzibar kwa onyesho la Idd Tatu pale Gymkhan.
"Idd Mosi tutakamua ngome ya zamani ya wapinzani wetu, DDC Kariakoo na siku inayofuata tutaila Idd viwanja vya TCC Chang'ombe kisha kwenda Zanzibar kumalizia sikukuu," alisema Super.

Kikosi kuweka Zogo lao videoni

Karama Masoud 'Kalapina'
KUNDI la Kikosi cha Mizinga kilichoadhimisha miaka 13 tangu kuanzishwa kwake hivi karibuni, kimekamilisha video ya wimbo wao unaotamba hewani wa 'Zogo la Mtaa'.
Kiongozi wa kundi hilo linalopiga muziki wake katika miondoko ya Hip Hop, Karama Masoud 'Kalapina' aliiambia MICHARAZO kuwa, video hiyo ipo mbioni kuachiwa wakati wowote.
Kalapina alisema mashabiki wa kikosi waliokuwa na hamu ya kuona video hiyo wajiandae kupata burudani.
"Kikosi kimekamilisha video ya wimbo wa 'Zogo la Mtaa' na hivi karibuni itaachiwa hewani, ikiwa ni muendelezo wa maadhimisho ya miaka 13 ya Kikosi," alisema Kalapina.
Msanii huyo alisema mbali na video hiyo, pia kundi lao lenye maskani yake Kinondoni Block 41, linaendelea pia kuuza fulani na vifaa vingine vyenye nembo yao ya Kikosi.
"Pia tumefufua duka letu la Kikosi lililopo Block 41 ambapo tunauza t-sheti, na vifaa vingine," alisema Kalapina.
Kundi hilo la Kikosi cha Mizinga, lilianzishwa rasmi mnamo mwaka 1997 baada ya kusambaratika kwa kundi lililomuibua Kalapina liitwalo School Face Gangster lililokuwa likiundwa na wasanii watatu.

Wednesday, July 24, 2013

Ofisi ya Msajili wa Vyama yaionya CHADEMA


MSAJILI wa vyama vya Siasa nchini amewaasa wanachama na viongozi wa Chama Cha Democrasia na Maendeleo (CHADEMA) kutumia muda wao kufanya shughuli za siasa ili kuchangia maendeleo ya nchi badala ya kutumia uwezo na muda wao kubuni mambo yanayoleta mtafaruku na kuhatarisha amani ya nchi.

Pia amepinga tamko la chama hicho la kuanzisha mafunzo ya kujilinda kwa vijana wake nchi nzima.Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa  leo jijini Dar es Salaam na kusainiwa kwa niaba ya Msajili wa vyama vya siasa Sisty Nyahoza alisema  kuwa hajawahi kuruhusu CHADEMA au chama chochote cha siasa kufanya mafunzo ya ukakamavu au mafunzo ya kutumia nguvu  ya aina yoyote kwa wanachama wake au mtu yeyote yule.

Anaongeza kuwa CHADEMA wanaruhusiwa kuanzisha vikundi vya kujilinda lakini hawaruhusiwi kuanzisha mafunzo ya kutumia nguvu kwaajili ya kujilinda kama walivyo tangaza katika mikutano yao ya hadhara kwani ni kinyume na Demokrasia na Katiba ya Jamuhuri ya Muungano.

Nyahozo ametoa ufafanuzi kuhusu vikundi vya ulinzi na usalama vilivyopo katika Katiba ya Vyama vya Siasa kwamba vikundi hivyo haviruhusiwi kufanya mafunzo ya kutumia nguvu ya aina yoyote katika kutekeleza majukumu yao.
 
Bali wajibu wao ni kutoa taarifa wa vyombo vya Dola pale wanapo sikia au kuona uhalifu ukitokea na wala sio kupambana na wahalifu au watu wanaotaka kuwadhuru kama tamko la CHADEMA  la tarehe 9 mwezi huu linavyo sema.

“Hakuna maelezo yoyote katika Katiba ya CHADEMA yanayoruhusu kutumia nguvu kufanikisha shughuli za kulinda mali na Viongozi wa Chama.Ni vyema wananchi wote waelewe kuwa Sheria za Nchi zimeweka masharti maalumu kwa Vyama Vya Siasa kutokana na umuhimu wa vyama hivi katika kudumisha aman utulivu na umoja wa Kitaifa”, alisema Nyahoza.

Alisema kuwa kutokana na Ibara ya20(2)C ya Katiba ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1997 inasema kuwa “Bila kujali masharti ya ibara ya (1) na (4),haitakuwa halali kwa chama chochote cha siasa kuandikishwa ambapo kutokana na katiba au sera yake:-kinakubali au kunapigani matumizi ya nguvu au mapambano kama njia za kufikia malengo yake ya kisiasa.

Nyahoza alimaliza kwa kuwataka CHADEMA kuacha kutekeleza mpango walio tangaza wa kuanzisha makambi ya kufanya mafunzo ya kujilinda kwa vijana wao nchi nzima,kwani kufanya hivyo ni kukiuka sheria za nchi na endapo  watashindwa kutii agizo hilo  hatua za Kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Ukatili! Mwanamke anyongwa kwa wivu wa mapenzi

MWANAMKE mmoja aitwaye Nyamizi Elias Salamba mwenye umri wa miaka 28 mkazi wa kijiji cha Ilomelo kata ya Ulowa wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, ameuawa kwa kunyongwa shingo na mwanamme anayedaiwa kuwa ni Mwenyekiti wa kijiji cha Kasela wilaya ya Nzega mkoani Tabora.

Taarifa ya jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga imesema tukio hilo limetokea Jumapili ya wiki iliyopita katika kijiji cha Ilomelo wilayani Kahama majira ya saa nne usiku ambapo mwanamke huyo alinyongwa shingo na hawara yake aliyejulikana kwa jina la Kashindye Abeid Sheni mwenye umri wa miaka 45 ambaye ni Mwenyekiti wa kijiji cha Kasela kilichopo mkoani Tabora.

Kamanda wa polisi mkoani Shinyanga, Evarist Mangalla alikitaja chanzo cha mauaji hayo kuwa ni wivu wa mapenzi baada ya marehemu kuwa na uhusiano wa kimapenzi na mwanamme mwingine ambaye hajafahamika, kitendo ambacho kilimuudhi Mwenyekiti huyo.

Kamanda Mangalla alisema mtuhumiwa anashikiliwa na polisi kwa uchunguzi na atafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.

Polisi 117 watimuliwa kambini kisa...!


ASKARI Polisi 117 waliokuwa mafunzoni mjini Moshi katika Chuo cha Taaluma na Mafunzo ya Polisi (MPA), wametimuliwa.


Waliotupiwa virago na kufutwa kwenye kozi hiyo ni wale waliopoteza sifa za kuendelea na mafunzo ya kijeshi baada ya kukutwa na makosa ya utovu wa nidhamu, utoro na matatizo ya kiafya.

Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Matanga Mbushi, ambaye ni mkuu wa chuo hicho alisema katika mahojiano maalumu kwamba, waliotimuliwa chuoni ni kati ya askari wanafunzi 3,189 waliokuwa wamesajiliwa kuanza mafunzo ya kijeshi katika chuo hicho, Oktoba 25 mwaka jana.
 

Kati yao askari 115 ni wale wa Polisi na askari wawili wanatoka katika Idara ya Uhamiaji iliyopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani.

Kufukuzwa kwa wanafunzi hao , kuna akisi moja kwa moja jinsi menejimenti ya chuo hicho ilivyojipanga upya kupunguza wimbi la baadhi ya askari walioko kazini na ambao wanalipaka matope jeshi hilo kutokana na kupotoka kimaadili kwa kutaka kujinufaisha kimaslahi.

Askari hao walikuwa waungane na wenzao ambao wanatarajiwa kuhitimu mafunzo ya awali ya polisi na uhamiaji, Julai 26 mwaka huu baada ya kupatiwa mafunzo ya medani za kivita. Mgeni wa heshima atakayeshuhudia kuagwa kwa askari 3,092 ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi.


Kamishna Mbushi alisema askari hao pamoja na mambo mengine wamepatiwa mafunzo maalumu ya utunzaji wa amani ya nchi iliyopo, Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT), Haki za Binadamu, Masuala ya mtambuka (Cross cutting issues), Usimamizi wa majanga na Usimamizi wa kazi za Polisi.

Mafunzo mengine ni pamoja na Polisi Jamii, Sheria ya ushahidi, Sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai, Upelelezi wa makosa ya jinai, Usalama barabarani na stadi za kazi.

Taarifa za awali kutoka ndani ya chuo hicho, zinaeleza kuwa mahafali hayo ya Polisi yatatanguliwa na medani za kivita yatakayofanyika Julai 25 huko katika Kijiji cha Kilele-Pori, Wilaya ya Siha.

Stars yatua salama kuivaa Uganda The Cranes J'mosi

Baadhi ya wachezaji wa timu ya taifa, Taifa Stars na benchi la ufundi wakiwasili katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebe nchini Uganda jana tayari kwa mchezo wa marudiano na timu ya Taifa ya Uganda Jumamosi hii.
Timu ya Taifa (Taifa Stars) imewasili Uganda jioni hii Jumatano tayari kuikabili Uganda Cranes kwa mechi ya marudiano kutafuta tiketi ya kucheza katika mashindano ya CHAN.
 
Kikosi hicho chichi nye wachezaji 20, kiliwasili muda mfupi baada ya saa kumi alasiri huku wachezaji na benchi la ufundi wakiwa na matumaini makubwa.
 
Akiongea mara baada ya kuwasili Kocha wa Timu ya Taifa Kim Poulsen alisema wamejiandaa vizuri wakiwa Mwanza na ana imanikikosi hiki kitabadili atokeo ya awali ambapo Stars ilifungwa 1-0 na Cranes Jijini Dar es Salaam.
 
Alisema licha ya kuwakosa wachezaji Shomari kapombe na Mwinyi Kazimoto, ana imani na kikosi chake hiki kuwa kitafanya makubwa Kampala.
 
“Tumekuja kubadilisha mahesabu kwani tumejiandaa vizuri kabisa,” alisema Poulsen.
 
Wadhamini wa Stars, Kilimanjaro Premium Lager wamewaomba watanzania wasikate tama kwani Stars bado ina nafasi kubwa ya kupindua meza.
 
“Sisi kama wadhamini bado tuna imani na Stars na tunajua watatuwakilisha vizuri ni vyema watanzania wawe na imani na kuiombea dua timu iibuke na ushindi mnono katika mechi hii ya marudiano,” alisema Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, george Kavishe.
 
Mechi hii ni gumzo kubwa Jijini Kampala kwani baadhi ya waganda wana hofu kuwa henda wakafungwa nyumbani kwao.
 
Mechi hii itapigwa katika Uwanja wa Nambole Jijini Kampala JUmamosi hii saa kumi jioni.
 
Mashindano ya CHAN yanatarajiwa kufanyika Januari mwakani nchini Afrika Kusini.
 
 

Coastal Union yatafuna 'fupa' lililozishinda Simba, Yanga

Coastal Union
MABINGWA wa zamani wa kandanda nchini, Coastal Union ya Tanga jioni ya leo imekifanya kile kilichowashinda vigogo Simba na Yanga kwa kuidungua URA ya Uganda kwa bao 1-0.
URA iliyoikwanyua Simba kwa mabao 2-1 na kusalia kidogo kuiangusha Yanga baada ya wanajangwani hao kuchomoa jioni na kupata sare ya 2-2, waliduwazwa na wagosi wa kaya kwenye uwanja wa Mkwakwani, jijini Tanga.
Coastal ikiwa na sura mchanganyiko katika kikosi chake inaelezwa iliwakimbiza Waganda hao kabla ya Kenneth Masumbuko kuwalaza mapema kwa bao tamu.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa pambano hilo, Coastal iliwazima kabisa wageni hao waliopo nchini kwa michezo ya klirafiki ya kimataifa kwa pasi murua za Haruna Moshi Boban, Uhuru Seleman, Jerry Santo, Caspian Odula na Daniel Lyanga.
Kikosi hicho ca Coastal ambacho0 ukuta wake ulikuwa chini ya Juma Nyosso, kipo katika maandalizi ya Ligi Kuu Tanzania Bara itakayoanza Agosti 24 ambapo yenyewe itaanzia ugenini dhidi ya maafande wa JKT Oljoro.

Kesho ni Siku ya Mashujaa wa Tanzania waliokufa vitani kukumbukwa

 

KESHO ni siku ya kuwakumbuka Mashujaa wa Tanzania, ambapo kitaifa itafanyika mkoani Kagera, japo kila mkoa nao upo katika maandalizi ya kuadhimisha siku hiyo ya kuwakumbuka wale wote waliojitolea kupotea uhai wao kwa ajili ya taifa lao.
Rais Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwaongoza Watanzania katika maadhimisho hayo ya kesho.
Kwa mkoa wa Morogoro shughuli na maandalizi ya siku hiyo ziliendelea leo kama zinavyoonekana pichani ambapo hapo juu Askari wa jeshi la wananchi Tanzania (JWTZ) kikosi cha maombolezi kikiwa katika mazoezi ya kutoa heshima za mwisho kwa  mashujaa waliofariki dunia katika vita ya Kagera mwaka 1978 na 1979 wakati wa gwalide la pamoja la jeshi la magereza, Polisi na JWTZ katika maandalizi ya mwisho ya kilele cha maadhimisho ya siku kuwakubuka mashujaa hao ambayo yataadhimishwa kimkoa kwenye mnara wa kumbukumbu wa Posta julai 25 mkoani Morogoro. PICHA JUMAMTANDA.BLOG

 Askari wa jeshi la polisi wakiwa katika gwalide
 Askari wa jeshi la wananchi Tanzania (JWTZ) nao wakiwa katika gwalide la pamoja.
 Hapa ni askari wa jeshi la magereza wakiwajibika kwa ajili ya maandalizi hayo.
Askari wa jeshi la wananchi Tanzania (JWTZ) Mteule daraja la kwanza, Jonas Philipo kulia akitoa maelekezo eneo la barabara ya Stesheni.
Hapa Aande Philipo kulia akifafanua jambo kwa viongozi wakuu wa mkoa ndani ya jeshi na serikali.
 Moshi ukiwa umezagaa baada ya kulipuliwa kwa mizinga mitatu katika maandalizi hayo.
Hapa vikosi vyote vya JWTZ, Polisi na Magereza vikiingia katika eneo la mzunguko wa posta ambapo ndiko kutaadhimishwa sherehe hizo kimkoa julai 25/ 2013.

Liverpool bado yaidengulia Arsenal juu ya Suarez

Suarez

LONDON, Uingereza
LIVERPOOL imekataa ofa iliyoboreshwa ya Arsenal ya paundi milioni 40 kwa ajili ya kutaka kumsajili mshambuliaji wa Uruguay, Luis Suarez.

Ofa hiyo isiyo ya kawaida, inayofahamika kuwa ni paundi 40,000,001, iliandaliwa maalum kuvuka kidogo bei ya kipengele cha kuvunjia mkataba wa mchezaji huyo, lakini Liverpool wamekataa.

Chini ya vipengele vya mkataba wa Suarez, klabu hiyo inabanwa kutafakari ofa yoyote kwa ajili yake inayozidi paundi milioni 40 na ni lazima imfahamishe mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 26 kuhusu ofa hiyo.

Lakini Liverpool hawataki kumuuza na sasa wamekataa ofa mbili kutoka Arsenal. Ofa ya kwanza ilikuwa ni paundi milioni 30.

Simba kumpeleka Kiggy Makassy India Agosti 18

KLABU ya Simba inapenda kutoa taarifa zifuatazo kwa umma kupitia vyombo vyenu.
KUHUSU MCHEZAJI KIGGI MAKASSY
UONGOZI wa Simba SC umefanikisha miadi (appointment) na madaktari nchini India kwa ajili ya matibabu ya mchezaji wake, Kiggi Makassy.
Mchezaji huyo atakutana na madaktari nchini India Agosti 18 mwaka huu tayari kwa ajili ya kuanza matibabu ya matatizo yake ya goti aliyoyapata wakati akiichezea Simba.
Ikumbukwe kwamba Simba SC ilikuwa klabu ya kwanza ya soka ya Tanzania kupeleka mchezaji nchi za nje kutibiwa takribani miaka minne iliyopita wakati ilipompeleka Uhuru Selemani Mwambungu nchini India.
Kwa taarifa hii, uongozi unapenda kuwahakikishia wapenzi na wanachama wake kwamba dhamira ya klabu ni kuhakikisha wachezaji wanapewa kipaumbele katika afya zao za kimwili na kiakili.
SIMBA DAY
Kama ilivyo ada, mwaka huu Simba itafanya maadhimisho ya Siku ya Simba (SIMBA DAY). Siku hiyo itatanguliwa na WIKI YA SIMBA ambapo wachezaji na viongozi wa klabu watatembelea vyombo vya habari, vituo vya kulelea yatima na hospitali kwa ajili ya kutekeleza wajibu wake kwa jamii (Social Responsibility).
MAANDALIZI YA LIGI KUU
SIMBA imeingia kambini kwa ajili ya mazoezi makali (intensive training) katika eneo la Bamba Beach jijini Dar es Salaam. Kocha Mkuu wa Simba, Abdallah Kibadeni, ameomba kambi hiyo ili kuwatengeneza wachezaji kimwili, kiakili na kisaikolojia.
Kabla ya mechi ya Simba Day, timu itacheza mechi moja ya kirafiki katika tarehe itayotangazwa baadaye.
Miongoni mwa wachezaji walio kambini ni Ramadhani Chomboh (Redondo).
Imetolewa na
Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
Simba SC

Chelsea bado yamng'ang'ania Rooney

Wayne Rooney
KLABU ya Chelsea inajiandaa kuongeza dau la kumnasa mshambuliaji wa Manchester United, Wayne Rooney licha ya United kusisitiza kuwa nyota wao huyo HAUZWI.
Kwa mujibu wa duru za kimichezo toka nchini England zinasema kuwa Chelsea wanajiandaa kuweka mezani Pauni Milioni 40 ili kumnasa mchezaji huyo.
Mchezaji huyo amekuwa hana furaha ndani ya United na imedaiwa kuwa anataka auzwe, lakini uongozi unaweka ngumu.
Chelsea chini ya kocha wake Jose Mourinho imekuwa ikimmezea mate mshambuliaji huyo tegemeo wa England na imeendelea  kusisitiza kuwa inahitaji saini yake kwa sasa.
Arsenal pia ilitajwa kuwa katika mbio za kumnasa mkali huyo wa mabao, ikijitapa wana uwezo wa kumlipa mshahara wake wa pauni 250,000 kwa wiki.
Kuna uwezekano mdogo kwa United kulegeza msimamo wake licha kwamba huenda dau hilo litawavutia baada ya timu yao kuandamwa na majeruhi kabla ya kuanza kwa Ligi.
Mfungaji Bora wa EPL, Robin van Persie aliumia wakati United ikilala Asia kwa mabao 3-2 huku Danny Welbeck akitajwa kuwa majeruhi hali inayomtisha kocha David Moyes.

Kocha Liverpool amcharukia Suarez

Kocha Brendan Rodgers

KOCHA wa Liverpool, Brendan Rodgers amesisitiza kwamba Luis Suarez hataweza kulazimisha kuondoka klabuni hapo katika kipindi hiki cha usajili.
Mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 26 ameweka wazi nia yake ya kuhama Anfield akieleza hadharani anavyoipenda Real Madrid na akazungumzia furaha yake baada ya kusikia anatakiwa na Arsenal, huku klabu hiyo ya London kaskazini ikijiandaa kupeleka ofa ya pili ya paundi milioni 40 baada ya ofa ya kwanza kukataliwa na Liverpool.
Lakini Rodgers amesema Liverpool watakuwa na kauli ya mwisho juu ya uwezekano wa kuhama kwa Suarez, huku akisema hakuna mchezaji anayepaswa kutoiheshimu klabu hiyo.
"Hili ni jambo ambalo liko mikononi mwetu," Rodgers aliwaambia waandishi wa habari. "Jambo hili haliko mikononi mwa mchezaji. Niko makini na thamani ya klabu, mahala tulipo na tunavyojiendesha.
"Soka na jamii ni tofauti siku hizi, soko la uhamisho ni tofauti kabisa na wachezaji wanaweza kuzua njia tofauti za kulifungua.
"Lakini daima nimekuwa nikisema kwamba hakuna mchezaji ambaye ni mkubwa kuliko Liverpool na kwamba hilo ni jambo ambalo tuko makini nalo sana.
"Je, namtarajia abaki? Sana kabisa. Mengi yamesemwa mwisho wa msimu, lakini ukweli ni kwamba yeye ni mchezaji muhimu sana. Kila mchezaji ana thamani yake, lakini haimaniishi kwamba tutamuuza."
Suarez alijiunga na wachezaji wenzake nchini Australia Jumapili baada ya kupewa muda wa ziada wa kupumzika kutokana na kushiriki michuano ya Mabingwa wa Mabara mwezi Juni.
Rodgers, ambaye awali alisema mshambuliaji huyo atacheza mechi ya kirafiki ya kujiandaa na msimu leo dhidi ya timu ya Melbourne Victory, anapanga kuzungumza na nyota huyo wa zamani wa Ajax huko huko ziarani.
"Nitafanya kama nilichofanya na wachezaji wengine kwa kukaa naye chini kuzungumza," Rodgers alisema. "Ukweli ni kwamba tuna jambo moja ama mawili ya kukamilisha, lakini hilo litafanyika na tutaendelea na kazi.
"Luis na mimi tumekuwa tukiwasiliana mara kwa mara, lakini tulipokuja hapa Jumapili usiku na kupata mlo, ulikuwa muda umeenda sana. Tuna aina hiyo ya mahusiano, ambayo mawasiliano yako wazi. daima huwa namueleza ninachojisikia.
"Luis yuko hapa kama ilivyotarajiwa, yeye ni sehemu muhimu ya kikosi na tutazungumza wakati fulani. Kubwa zaidi yeye ni mchezaji wa Liverpool. Tuliletewa ofa moja tu kutoka timu inayomtaka na ilikuwa haikaribii thamani yake na hakuna ofa nyingine tangu wakati huo."

Miaka 13 ya Jide kuhamia Arusha wakati wa Idd el Fitri

Lady Jaydee

MWANADADA mkali wa muziki wa kizazi kipya nchini, Judith Wambura Mbibo 'Lady Jaydee' a.k.a Anaconda, anatarajia kuendeleza shamrashamra za maadhimisho ya miaka 13 ya uwepo wake kwenye fani hiyo katika mkoa wa Arusha wakati wa sikukuu ya Idd el Fitri.

Kwa mujibu wa Meneja wa msanii huyo, Gadna G. Habash maonyesho hayo yafanyika kwa siku mbili mfululizo kuanzia Idd Mosi na Idd Pili na atashirikiana na wasanii kadhaa wakongwe akiwamo Joseph Haule 'Profesa Jay wa Mitulinga a.k.a Big Daddy ambaye ni mkongwe mwenzake katika tasnia hiyo nchini.

Onyesho la kwanza la Binti Machozi litafanyika kwenye ukumbi wa  'Triple A' siku ya Idd Mosi na siku inayofuata atawapa shangwe wakazi wa jiji hilo katika ukumbi wa Botaniko Garden ambapo shughuli nzima ya burudani itaanza majira ya mchana kwa kushirikisha watoto kuonyesha vipaji vyao.

Watoto haao watashindana kucheza, kuimba na vipaji vingine mradi nao kujumuika na Anaconda kabla ya kuwapisha wazee wao kuadhimisha miaka hiyo 13 na mkali huyo asiye na mpinzani nchini miongoni mwa wasanii wa kike.

Hayo yatakuwa maadhimisho ya pili kwa Jide baada ya awali kufanya kama hivyo jijini Dar es Salaam Juni 14 ambapo alifunika mbaya kiasi kwamba ukumbi haukutosha kwa jinsi ulivyofurika watu waliojitokeza Nyumbani Lounge.

Mara baada ya maadhimisho hayo ya Arusha, Jide anatarajiwa kufanya ziara mikoa mbalimbali ili kuwapelekea burudani mashabiki wake katika kuadhimisha miaka hiyo 13 ambapo mwanamuziki huyo amekuwa akizifanya shughuli za muziki bila kutetereka akitajwa kama mmoja wa wanamuziki matarajiri Afrika Mashariki, lakini asiye na makeke.

Katika mipindi chote cha miaka 13 katika ulimwengu wa muziki, Jide ameshatoa albamu sita ambazo ni Machozi (2000), Binti (2003), Moto (2005), Shukrani (2007), The Best of Lady Jay dee(2012) na ya sasa ya Nothing but the Truth akiwa pia anamiliki bendi ya Machozi, Hoteli na miradi mingine ya kiuchumi.

Taifa Stars kuifuata Uganda the Cranes leo

Vijana wa taifa Stars
TIMU ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inatarajiwa kuondoka mchana wa leo ikitokea Mwanza kwenda Kampala, Uganda kwa ajili ya mechi ya marudiano ya Kombe la CHAN itakayochezwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Mandela kuanzia saa 10 kamili jioni.
Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ilikuwa kambini jijini Mwanza chini ya Kocha Kim Poulsen tangu Julai 14 mwaka huu kujiandaa kwa mechi hiyo itakayoamua ni timu ipi kati ya hizo mbili itakayocheza fainali za CHAN zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) Stars itaondoka Uwanja wa Ndege wa Mwanza saa 7.25 mchana kwa ndege ya PrecisionAir, na inatarajiwa kutua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe saa 10.15 jioni.
Stars inahitaji ushindi wa mabao yasiyopungua mawili ili kusonga mbele kwenye fainali hizo baada ya kupoteza ya kwanza iliyochezwa nyumbani wiki mbili zilizopita kwa kufungwa bao 1-0.
Kocha wa timu hiyo jana alizungumza na wanahabari jijini humo na kutamba kwamba vijana wake wapo tayari kwa pambano hilo la Jumamosi na kuahidi watafia uwanjani, mradi kuipa nafasi Stars kurejea ilichokifanya mwaka 2009 iliposhiriki fainali hizo za CHAN zilipofanyika Ivory Coast.