STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, July 22, 2013

Hatimaye ratiba Ligi Kuu yatoka, Simba, Yanga kuanza na wageni zenyewe kuumana Okt. 20

http://blog.pesatimes.com/wp-content/uploads/2013/06/kochaaa.jpg
Yanga itaendelea kubebana kama hivi katika ligi ya msimu huu itakayoanza Agosti 24?
Na Boniface Wambura
LIGI Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara msimu wa 2013/2014 inatarajiwa kuanza  kutimua vumbi rasmi Agosti 24 mwaka huu kwa timu zote 14 kuwa viwanjani katika miji saba tofauti, ambapo mabingwa watetezi Yanga wataanza kibarua dhidi ya Ashanti United, jijini Dar..

Hata hivyo, kabla ya ligi hiyo kuanza kutakuwa na mechi ya kufungua msimu (Ngao ya Jamii- Community Shield) kati ya bingwa mtetezi Yanga na Makamu bingwa Azam itakayochezwa Agosti 17 mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mbali na pambano la Yanga na Ashanti litakalopigwa kwenye uwanja wa Taifa, siku hiyo ya ufunguzi wa ligi hiyo, Mtibwa Sugar na Azam zitaonyeshana kazi kwenye Uwanja wa Manungu, Morogoro huku JKT Oljoro na Coastal Union zitapepetana mjini Arusha kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid.

Simba wenyewe wataanzia ugenini mjini Tabora kuumana na 'wageni' Rhino Rangers, kwenye uwanja wa Ally Hassani Mwinyi, wakati  Mgambo Shooting itaialika JKT Ruvu katika Uwanja wa Mkwakwani, mjini Tanga huku wageni wengine wa ligi hiyo Mbeya City watakuwa nyumbani mjini Mbeya kuikaribisha Kagera Sugar katika uwanja wa Soikoine na Ruvu Shooting na Tanzania Prisons zitaumana Mabatini, Mlandizi.

Pambano la watani wa jadi nchini lenyewe kwa raundi ya kwanza litachezwa Oktoba 20 ambapo Simba watakuwa wenyeji kabla ya kurudiana mwakani April 27, katika moja ya mechi za kufungia msimu Yanga wakiwa ndiyo wenyeji wa pambano hilo.

Mzunguko wa kwanza wa ligi hiyo utamalizika Novemba 3 mwaka huu wakati wa pili utamalizika Aprili 27 mwakani. (Ratiba kamili ya ligi hiyo itatupiwa hapa MICHARAZO muda si mrefu)

Taifa Stars kuifuata Uganda The Cranes keshokutwa

Stars na The Craned walipoumana katika mechi ya kwanza jijini Dar es Salaam
Na Boniface Wambura
Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inaondoka Mwanza keshokutwa (Julai 24 mwaka huu) kwenda Kampala, Uganda kwa ajili ya mechi ya marudiano ya Kombe la CHAN itakayochezwa Jumamosi (Julai 27 mwaka huu) Uwanja wa Mandela kuanzia saa 10 kamili jioni.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iko kambini jijini Mwanza chini ya Kocha Kim Poulsen tangu Julai 14 mwaka huu kujiandaa kwa mechi hiyo itakayoamua ni timu ipi kati ya hizo mbili itacheza Fainali za CHAN zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.

Timu hiyo itaondoka Uwanja wa Ndege wa Mwanza saa 7.25 mchana kwa ndege ya PrecisionAir, na inatarajiwa kutua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Entebbe saa 10.15 jioni.

Wakati huo huo, Kocha Kim Poulsen kesho (Julai 23 mwaka huu) atakuwa na mkutano na waandishi wa habari kuzungumzia maandalizi ya kikosi chake. Mkutano huo utafanyika saa 5 kamili asubuhi kwenye hoteli ya La Kairo jijini Mwanza.

Pepe Reina kutimkia Napoli kumfuata kocha Rafa Benitez

http://i.telegraph.co.uk/multimedia/archive/02622/pepe_reina_2622933b.jpg
  GOLIKIPA wa klabu ya Liverpool, Pepe Reina anatarajiwa kujiunga na timu ya Napoli ya Italia kwa mkopo wa muda mrefu.
Kocha wa Napoli Rafael Benitez amekuwa akimkufukuzia Mhispania mwenzake huyo ambaye alikuwa nambari moja kipindi chake Anfield, baada ya kushindwa kumnasa mlinda mlango wa QPR Julio Cesar.
Reina mwenye umri wa miaka 30, alitarajiwa kurejea mazoezini katika klabu yake jana Jumapili kwa kujiunga na wachezaji wenzake huko katika ziara ya maandalizi ya msimu.
Liverpool ilimsainisha mlinda mlango Simon Mignolet raia wa Ubelgiji kutoka katika klabu ya Sunderland kwa ada ya uhamisho ya pauni milioni £9 mwezi uliopita.
Reina alijunga na Liverpool akitokea Villarreal mwaka 2005.

JK kuongoza watanzania kuwaaga wanajeshi waliouwawa Darfur


 

RAIS wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dk Jakaya Kikwete anatarajiwa kuwaongoza Watanzania kuiaga miili ya askari saba wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), waliouawa katika jimbo la Darfur nchini Sudan.
 
Shughuli ya kuiaga miili hiyo iliyowasili nchini juzi, itafanyika leo kwenye viwanja vya makao makuu ya jeshi hilo, Upanga jijini Dar es Salaam.

Miili ya wanajeshi hao iliwasili nchini juzi kwa ndege maalumu katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu J. K Nyerere, Terminal One na kwenda kuhifadhiwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Lugalo jijini Dar es Salaam.

Wanajeshi waliouawa ni Sajenti Shaibu Othuman, Koplo Oswald Chaula, Koplo Mohamed Juma, Koplo Mohamed Chikilizo, Rodney Ndunguru, Peter Werema na Fortunatus Msofe.

Taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na Kurugenzi ya Habari na Uhusiano, Makao Makuu ya JWTZ, ilieleza kuwa askari hao wataagwa leo na shughuli hiyo itahudhuriwa na familia, makamanda wa jeshi na viongozi wa Serikali.
 

“Shughuli ya kuaga kwa heshima za kijeshi itaanza saa tatu kamili asubuhi katika viwanja vya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Upanga na itaendelea mpaka mchana kabla ya kusafirishwa,” ilisema taarifa hiyo.
 

Wanajeshi hao ambao ni miongoni mwa askari wa kikosi cha Umoja wa Mataifa cha Kulinda Amani katika Jimbo la Darfur nchini Sudan, waliuawa kutokana na mashambulizi ya kushtukiza yaliyofanywa na waasi wanaopigana na Serikali, hivyo kuwa ni mara ya kwanza kwa idadi kubwa ya wanajeshi wa Tanzania wanaolinda amani katika nchi mbalimbali kuuawa kwa wakati mmoja.
 

Mwili wa Mr Bomba kuagwa muda huu Muhimbili rariba kamili hiko hivi

REV. John Makanyagana
Msanii John Makanyaga enzi za uhai wake
MWILI wa muigizaji mkongwe nchini, Mchungaji John Makanyaga unatarajiwa kuagwa asubuhi hii katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kabla ya saa 8 kufanyiwa misa kwenye Kanisa la Anglicana tayari kwa ajili ya kusafirishwa kwenye kuzikwa kwao Mpwapwa.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa hivi punde na Adam Malele' Swebe', mmoja wa waigizaji wenzake wa zamani wa Kaole Sanaa Group, mwili wa msanii hiyo aliyefahamika zaidi kama Mr Bomba utafanyiwa misa ya maombezi kanisa la Ilala Sharifu Shamba
Swebe alisema baada ya ibada hiyo ya mazishi kanisani hapo, mwili huo utasafirishwa kwenda Mpwapwa Dodoma kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika kesho Jumanne.
Marehemu Mr Bomba alifariki juzi hospitali ya Muhimbi kwa tatizo la uvimbe wa kansa katika ini na enzi za uhai wake alitamba na tamthilia mbalimbali kupitia kituo cha ITV kabla ya kuhamia kwenye filamu.
Pia alikuwa ni mwalimu na Mcghungaji wa kanisa la Anglakana mpaka mauti yalipomkumba, ambapo yamekuja huku watanzania wakiendelea kuuguza machungu ya vifo vya wasanii wengine wa uigizaji na muziki vilivyotokea mfululizo tangu mwaka jana.

Mwakyembe, Maugo kupaa kesho kwenda Russia

Mada Maugo

Benson Mwakyembe (kushoto)
MABONDIA watanzania wanaocheza ngumi za kulipwa, Mada Maugo 'King Maugo Jr' na Benson Mwakyembe wanatarajia kuondoka nchini kesho (Jumanne) kuelekea Russia kwa ajili michezo yao ya kimataifa dhidi ya wenyeji wao.
Wanamasumbwi hao wataondoka majira ya saa 10 jioni na watapanda ulingoni Jumamosi ya wiki hii katika mipambano yao ya uzito wa kati wa Kilo 75 (Super Middle).
Rais wa TPBO-Limited, Yasin Abdallah 'Ustaadh', aliiambia MICHARAZO kuwa, Maugo yeye ataenda kupigana na Movsur Yusupov  wakati Mwakyembe ataonyeshana kazi na Apti Ustarkhanov kwenye michezo itakayochezwa kwenye ukumbi wa Trade &Intertainment uliopo mjini Kasiysk, nchini Russia.
Ustaadh alisema mapambano yote hayo yatakuwa na raundi 8 kila mmoja na kwamba Watanzania hao wataungana na wakala wao kutoka Kenya, Thomas Mutua katika mji wa Dubai.
Rais huyo wa TPBO alisema mpinzani wa Maugo rekodi yake inaonyesha amecheza mapambano matatu na yote ameshindwa moja likiwa kwa KO wakati mpinzani wa Mwakyemba amecheza mechi mbili na kushinda moja na kuchapwa moja.
Hata hivyo, alisema pamoja na rekodi hizo zisizovutia kwa wapinzani wao, bado Maugo na Mwakyembe wanapaswa kwenda nchini humo na tahadhari kubwa kwani Warusi huwa hawaruhusu mabondia wa ngumi za kulipwa kucheza mpaka wawe wamepitia ngumi za ridhaa na kushiriki michezo ya Olimpiki.
Akizungumza safari hiyo, Mwakyembe aliiambia MICHARAZO asubuhi hii kwamba licha ya kutomfahamu vyema mpinzani wake, lakini anawaahidi Watanzania kwenda kuwawakilisha vyema katika mchezo huo wa kimataifa ambao ni wa pili kwake nje ya nchi.
"Naahidi sintowaangusha watanzania katika mechi hiyo ya Jumamosi, naenda nikiwa na imani ya kutaka kuweka rekodi kwa kumtwanga mwenyeji wangu na kurejea nchini kwa heshima zote, najiamini kwa mazoezi niliyofanya," alisema.
Kuhusu safari hiyo, Mwakyembe alisema kila kitu kimekaa vyema na kwamba panapo majaliwa ataondoka na mwenzake (Mada Maugo) kesho saa 10 jioni.

Suarez aitamani Arsenal, apanga kuiambia Liverpool

 http://images.dailystar-uk.co.uk/dynamic/58/photos/888000/620x/4888.jpg
MSHAMBULIAJI Luis Suarez anajiandaa kuiambia Liverpool kwamba anataka kuhamia Arsenal.
Gazeti la Sunday Mirror limesema kuwa Liverpool wanamsubiri Suarez aombe rasmi kuondoka ndiyo wamruhusu wakati mshambuliaji huyo wa Uruguay atakapowasili kutoka mapumzikoni mjini Montevideo na kujiunga na kambi ya mazoezi mjini Melbourne.
Arsenal wameongeza matumaini ya kumpata mchezaji huyo na wanatarajiwa kurejea Anfield na ofa nono zaidi baada ya ofa yao ya awali kukataliwa.
Suarez aliweka moyo wake kujiunga na Real Madrid lakini miamba hao wa Hispania hawajajitokeza tena kutaka kumsajili baada ya kuweka wazi kwamba ofa yao ya mwisho wanayoweza kutoa ni paundi milioni 25.
Kocha wa Liverpool, Brendan Rodgers, alisema kuwa thamani ya Suarez ni sawa na ya Muuruguay mwenzake, Edinson Cavani aliyeuzwa kwa paundi milioni 55 kutoka Napoli kwenda PSG. 
Arsenal wameripotiwa kuwa tayari kutoa paundi milioni 40.
Kocha Arsene Wenger anaona Suarez hana shida licha ya kuadhibiwa kwa kumfanyia vitendo vya kibaguzi Patrice Evra na kumng'ata Branislav Ivanovic kwa vile nyota huyo wa Uruguay ni mchapakazi.

Shasta ahairisha kugawa utamu wa penzi

http://thumbp4-ne1.thumb.mail.yahoo.com/tn?sid=2126005954&mid=ACbkimIAAAlPUdQbXwAAAJWB87w&midoffset=2_0_0_1_35347&partid=2&f=1215&fid=Inbox&w=480&h=297
Shasta akiwa katika pozi nyumbani kwake

MSANII wa filamu aliyejitosa pia katika muziki, Leah Mussa 'Shasta' amesitisha kwa muda harakati za kusambaza wimbo wake uitwao 'Utamu wa Penzi' ili kupisha mwezi mtukufu wa Ramadhani, imeelezwa.
Akizungumza mwishoni mwa wiki, Shasta alisema kuwa wimbo huo alioimba na H-Mbizo umeshakamilika na kilichobaki ni mambo madogo tu na kwamba, baada ya kumalizika kwa mfungo na sikukuu ya Idd ataendelea na kazi ya kuusambaza.
"Sasa wimbo huu utatoka baada ya Sikukuu ya Idd El Fitri," alisema Shasta ambaye amejitosa katika muziki baada ya kuvutiwa na wimbo 'Majanga' wa shoga yake na msanii mwenzake katika  filamu, Snura Mushi.
Baadhi ya filamu alizoshiriki Shasta ni 'Ong'wana', 'Julia', 'Kisasi za Mzimu', 'Siri za Majini' na 'Deception'.

Golden Bush Fc yazinduka Ligi ya Kinondoni

Vijana wa Golden Bush wakiwa mazoezini na kocha wao Shija Katina (kushoto) wakipeana mikakati ya kusaka ushindi katika Ligi daraja la Nne wanayoicheza kwa mara ya kwanza
BAADA ya wiki iliyopita kutibuiliwa rekodi yake ya ushindi mfululizo kwa kulazwa na Kijitonyama, timu ya Golden Bush Fc jana ilizinduka katika Ligi Daraja la Nne wilayani Kinondoni kwa kufanya 'mauaji' ya kutisha dhidi ya Shein Rangers kwa kuinyuka mabao 4-1.
Pambano hilo lililochezwa kwenye uwanja wa Mwananyamala, jijini Dar es Salaam lilishuhudia vijana wa Golden Bush inayonolewa na kocha Shija Katina na Madaraka Seleman 'Mzee wa Kiminyio' wakicharuka tangu mwanzo wa mchezo ili kurejesha heshima yake katiika lig hiyo.
Vijana hao walipata mabao yao yaliyotosha kuwafanya wafikishe pointi 15 katika kundi lake baada ya kucheza mechi 6 yalitumbukizwa kimiani na aliyekuwa nyota wa mchezo, Adilu aliyefunga mawili, Said na Kenan.
Timu hiyo inatarajiwa kushuka tena dimbani siku ya alhamis, ambapo uongozi wa timu hiyo umesema vijana wao watashuka wakiwa na lengo moja tu la kuendeleza vipigo ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kufuzu hatua ya pili na hatimaye kuipanda Ligi Daraja la Tatu.

Washindi shindano la kusoma Qur'an wapatikana

Msomaji wa Quran tukufu katika mashindano ya kitaifa, Abdallah Abdulkadri akisoma wakati wa fainali zake jana.

Msomaji wa Quran tukufu katika mashindano ya kitaifa, Seif Salim Said ambaye ni mremavu wa macho akisoma wakati wa fainali zake jana

Baadhi ya viongoza wa Dini wakifatilia mashindano hayo katika ukumbi wa Diamond Jubilee
Baadhi ya wanafunzi walioshiliki katika kusoma

Qur'an tukufu

Msomaji wa Quran tukufu katika mashindano ya kitaifa, Ummy Swaleh Said ambaye ni mlemavu wa macho akisoma wakati wa fainali hizo.

Baadhi ya waumini wa Dini Ya Kislam wakiongozwa na mratibu wa mashindano ya usomaji wa Qur'an Bi. Aisha Sururu wakifuatilia fainali hizo.
Bi Aisha Sururu akifuatilia mashindano hayo yaliyomalizika jana
Zawadi walizopewa washindi

Mgeni Rasmi wa Mashindano ya kuifadhi Quran tukufu kitaifa Dk, Suleiman Ally Yussuf katikati na Mkurugenzi wa Kituo cha Utamaduni cha Ubalozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ,Morteza Sabouri wakimkabidhi zawadi wa cherehani mshindi wa kusoma juzuu 20

Mgeni Rasmi wa Mashindano ya kuifadhi Quran tukufu kitaifa Dk Suleiman Ally Yussuf kulia na Mkurugenzi wa Kituo cha Utamaduni cha Ubalozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ,Morteza Sabouri wakimkabidhi zawadi ya bajaj  pamoja na pesa taslmu laki tano mshindi wa kuhifadhi Quran tukufu, Suria Ally Bakari.

Mgeni Rasmi wa Mashindano ya kuifadhi Quran tukufu kitaifa Dk Suleiman Ally Yussuf (kulia) akimkabidhi mshindi Abdul Hamid zawadi yake ya bajaj na pesa taslimu.


Baadhi ya washindi wa kuhifadhi Quran Tukufu wakiomba Dua baada ya kumalizika mashindano hayo

Afande Sele kuweka Dini videoni


Afande Sele akiwajibika jukwaani
MKONGWE wa muziki wa hip hop nchini, Seleman Msindi 'Afande Sele' yupo katika harakati za kufyatua video ya wimbo wake mpya unaoendelea kutamba kwenye vituo vya redio uitwao 'Dini Tumeletewa'.
Afande Sele aliiambia MICHARAZO kuwa ijapokuwa hivi sasa yupo mapumzikoni kuupisha mfungo wa mwezi wa Ramadhani, lakini bado anaendelea na mipango ya kukamilisha video ya wimbo huo ili kukata kiu ya mashabiki wake ambao wengi wamekuwa wakiiulizia mara kwa mara.
"Niko mbioni kutoa video ya wimbo Dini Tumeletewa nilioimba na Belle 9. Ikikamilika itasambazwa ili mashabiki wa muziki washuhudie kile nilichoimba,"alisema Afande.
Katika hatua nyingine, Afande Sele alisema kuwa tangu atoe wimbo huo amekuwa akipokea pongezi nyingi na kuombwa atoe video yake.
Msanii huyo amekuwa akijizolea sifa kemkem kutokana na nyimbo zake nyingi kuwa na mashairi yenye kugusa hali halisi ya maisha ya Mtanzania.

TMK Wanaume Family Sasa Tufurahie


KUNDI la muziki wa kizazi kipya la TMK Wanaume Family 'Mapanga Shaa', linatarajiwa kuuachia hewani wimbo wao mpya uitwao 'Tufurahie'.
Wimbo huo uliokamilika wiki iliyopita ni kati ya kazi mpya za kundi hilo baada ya kutamba na 'Kichwa Kinauma' na 'Tutaonekanaje'.
Akizungumza na MICHARAZO, Meneja wa TMK, Said Fella alisema wimbo huo ulirekodiwa katika studio za Tuddy Thomas wa Ngoma Records na utaachiwa leo Jumatatu.
Fella alisema katika wimbo huo, kazi kubwa imefanywa na YP, Mheshimiwa Temba na Said Chegge, na kwamba wanatumai utafanya vizuri kama ilivyokuwa kwa nyimbo zao nyingine.
"Umeandaliwa vizuri na hivyo tunaamini kwamba nao utatamba," alisema Fella.
Katika hatua nyingine, Fella alisema video ya wimbo wa msanii Is'haka Aslay 'Dogo Aslay' uitwao 'Bado Mdogo' alioimba kwa kushirikiana na Linnah wa THT imekalimika.
Wimbo huo umeelezewa na Dogo Aslay kuwa ni kisa cha kweli, akidai kwamba yupo mama mwenye umri mkubwa aliyekuwa akimghasi kwa kumtaka kimapenzi licha ya yeye kumkatalia kwa kumwambia kuwa yeye (Aslay) bado mdogo na hivyo asingependa kujihusisha na masuala hayo ya mapenzi.

Mbwana Samatta azidi kung'ara Afrika

Mbwana Samatta alipokuwa akiitumikia Stars dhidi ya Morocco

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Tanzania, Mbwana Ally Samatta ameendelea kung’ara katika michuano ya Afrika, baada ya mwishoni mwa wiki kuifungia timu yake ya TP Mazembe ya DR Congo bao lililoipa sare ya 1-1 ugenini dhidi ya ESS ya Algeria.
Katika pambano hilo lililochezwa Ijumaa kwenye uwanja wa Mei 8, 1945 la ufunguzi wa hatua ya Makundi Kombe la Shirikisho Afrika kwa kundi B, wenyeji walilazimika kulichomoa bao hilo la Samatta.
Samatta alifunga bao hilo katika dakika ya 81 , lakini hata hivyo dakika mbili baadaye wenyeji walichomoa kupitia kwa beki wao Mourad Delhoum.
TP ya Samatta sasa itarejea nyumbani kuisubiri FUS Rabat ya Morocco katika pambano lao litakalochezwa mjini Lubumbashi Agosti 4.

Sunday, July 21, 2013

Maskini! Papii Kocha alilia tena Rais Kikwete

MUIMBAJI Nyota wa zamani wa bendi ya FM Academia, Papii Kocha amemuandikia ombi jingine maalum Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete kumuomba MSAMAHA wa kufutiwa adhabu yake ya kifungo cha maisha jela alichopewa yeye na wanafamilia yake kwa kesi ya kubaka.
Ujumbe huo unaelezwa ni wa mara nyingine tena kwa msanii huyo aliyepo gerezani na baba yake, japo hakujawa na hakika kama barua hizo zinamfikia Mheshimiwa na kuzisoma au la. Ebu isome mwenyewe barua hiyo ya 'Mwana Mfalme' Papii Kocha kwenda kwa Rais Jakaya Kikwete...inaumiza!
MF/NA: 836'04 Johnson Nguza
(Papii Kocha) Gereza Kuu Ukonga
S.L.P 9091
Dar es Salaam
Mh. Rais Jamuhuri ya Muungano Tanzania

YAH: MAOMBI YA KUPEWA MSAADA (MSAMAHA) WA KUFUTIWA ADHABU YA KIFUNGO NILIYOPEWA NA MAHAKAMA YA HAKIMU MKAZI KISUTU.

Husika na somo hilo hapo juu. Mimi ni mfungwa katika gereza kuu Ukonga. Kwa heshma na taadhima na kwa kutambua utu na huruma yako ya kiMUNGU ulionayo dhidi ya binadamu wenzako pamoja na mamlaka uliokabidhiwa na Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Naanguka na kushika miguu yako mitukufu muheshimiwa rais....Nakuomba msaada (msamaha) kwako muheshimiwa rais, kwa njia hii ya maandishi kusudi niweze kuondolewa adhabu ya kifungo cha maisha gerezani, niliyohukumiwa na mahakama tajwa hapo juu. Mh.Rais mimi nimefungwa nikiwa bado kijana mwenye umri mdogo, na ukweli kutoka moyoni sikufanya kosa hilo.

Si mimi, baba yangu Nguza wala ndugu yangu yeyote aliyefanya kitendo kile. Lakini wenye mamlaka wakatuona tuna hatia na kuamua kuteketeza kizazi chetu gerezani.

Natamani kiama ifike ili mwenyezi Mungu aweke wazi ukweli wote uliojificha nyuma ya pazia. Mpaka sasa natambua wazi hatima pamoja na dhamana ya maisha yangu ipo katika mikono yako mitukufu Mh. Rais Naomba huruma yako muheshimiwa Rais maana mimi ni mtoto wako ninaehitaji huruma yako wewe mzazi. Lakini pia sisi ni binadamu wenye nafsi na miili kama wengine. Waliotumia mamlaka yao kutuweka gerezani nao ni binadamu pia, wenye miili na nafsi.

Ipo siku nafsi zetu zitapaswa kutoa hesabu ya tuliyoyafanya hapa duniani. wakati huo miili yetu tunayoitumia kunyanyasa wanyonge itakuwa imeoza mavumbini.

Natumaini kauli yako ya mwisho ndio itakayoleta pumzi ya uhai nafsini mwangu. Nakutakia kazi njema, afya njema na maisha marefu. Mungu akubariki. Wako mtiifu

Mfungwa NO:836'04 JOHNSON NGUZA (PAPII KOCHA)
 
Udaku Specially

Kumbe Msajili wa Vyama alibariki CHADEMA kuunda 'jeshi'?!


  Nakala za majibu ya Ofisi ya Tendwa kwa CHADEMA zilipelekwa kwa
  • Waziri wa Mambo ya Ndani wakati huo, Omar Mapuri,
  • Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, aliyekuwa anashughulikia Habari na Siasa, Muhammed    Seif Khatib;
  • Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu;
  • Inspekta Jenerali wa Polisi na
  • Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai

LICHA ya kuwapo kwa shutuma mbalimbali zinazopinga mpango wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kuanzisha kikundi cha, kujihami cha Red Brigade kitakachotoa ulinzi kwa viongozi wao, imebainika kuwa msajili wa vyama vya siasa nchini, John Tendwa alitoa baraka za kuanzishwa kwake.

Tanzania Daima imeona nakala ya barua ya mwaka 2005 kutoka katika ofisi ya Tendwa, ikionyesha kubariki jambo hilo ambalo katika siku za hivi karibuni limezua gumzo kubwa na kusababisha Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, kuhojiwa na polisi kuhusiana na kauli zake.

Uchunguzi wa kina uliofanywa na Tanzania Daima umebaini kuwa Desemba 30, 2004 ofisi ya msajili wa vyama siasa ilimwandikia Katibu Mkuu wa CHADEMA barua yenye kumbukumbu Na. RPP/CHADEMA/72/29 ikitaka ufafanuzi baada ya kusikia kupitia vyombo vya habari kuwa chama hicho kinataka kuanzisha kikundi cha kujihami (Red Brigade). “Kulingana na Ibara ya 9 (2) (c) ya Sheria Na. 5 ya Vyama vya Siasa 1992, ibara ya 147 na 148 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Sheria ya Jeshi la Polisi, kuanzishwa kwa kikundi hicho ni kinyume cha sheria hizo,” imeeleza sehemu ya barua hiyo.

Barua hiyo ambayo Tanzania Daima inayo iliyosainiwa na Hilda Lugembe kwa niaba ya msajili wa vyama vya siasa, inaeleza kuwa kuvunjwa kwa sheria hizo kutasababisha CHADEMA kufutwa. CHADEMA baada ya kupata barua hiyo, Januari 6 mwaka 2005 iliijibu kuwa kikundi kinachozungumziwa ni walinzi wa ndani ya chama, vijana wa kike na wa kiume, wanachama wa CHADEMA, watu wasio na silaha, chini ya usimamizi wa kurugenzi ya ulinzi na usalama ya chama hicho. “Kikundi kinachokusudiwa kuundwa ni kutokana na Katiba ya CHADEMA ambayo inaruhusu uundwaji wa Kurugenzi ya Ulinzi na Usalama chini ya Katiba ya CHADEMA, kifungu cha 7.6.4 (h),” inaeleza barua ya CHADEMA yenye kumbukumbu Na. C/HQ/ADM/64 iliyosainiwa na Suzan Kiwanga kwa niaba ya Katibu Mkuu wa CHADEMA. Chama hicho kiliilaumu serikali kwa vitisho ilivyotoa vya kutaka kukifuta endapo kingeendelea na kusudio la kuanzisha kikundi hicho.

Barua ya ofisi ya Msajili wa vyama vya siasa nchini ya kuithinisha uanzishwaji

Hata hivyo, baada ya ufafanuzi huo, Januari 11 mwaka 2005, ofisi ya msajili wa vyama vya siasa, ilipopata majibu hayo ya CHADEMA, ilieleza kuwa kwa madhumuni yaliyoelezwa na chama hicho inakubaliana na malengo ya kuanzisha kikundi cha ulinzi kwa ajili ya usalama wa ndani ya chama. “Ofisi ya msajili wa vyama vya siasa, kwa madhumuni mliyoyatoa kwenye barua yenu C/HQ/ADM/62 inakubaliana na maelezo yenu ya kuanzishwa kwa kikundi cha ulinzi kwa ajili ya usalama wa ndani ya chama ingawa Katiba ya CHADEMA haijatoa ufafanuzi huo, vinginevyo tunawatakia kila la heri kwenye matayarisho ya uundwaji wa kikundi hicho,” ilisema barua ya msajili wa vyama vya siasa nchini.

Barua hiyo yenye kumbukumbu Na. RPP/CHADEMA/72/32 iliyosainiwa na Hilda Lugembe kwa niaba ya msajili wa vyama vya siasa nchini, pia iliwatakia kila la heri CHADEMA kwenye matayarisho ya uundwaji wa kikundi hicho.

Nakala za majibu ya Ofisi ya Tendwa kwa CHADEMA zilipelekwa kwa Waziri wa Mambo ya Ndani wakati huo, Omar Mapuri, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, aliyekuwa anashughulikia Habari na Siasa, Muhammed Seif Khatib; Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu; Inspekta Jenerali wa Polisi na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai

TANZANIA DAIMA

Golden Bush Veterani waikwanyua Faru Dume x3

Golden Bush Veterani a.k.a 'Wazee wa Dozi' katika moja ya mechi zao
WAKALI wa soka la maveterani jijini Dar es Salaam, Golden Bush Veterani jana asubuhi wameikwanyua bila huruma, Faru Dume ya Manzese kwa kuicharaza mabao 3-1 katika pambano la kirafiki lililochezwa kwenye uwanja wa Kinesi, Ubungo jijini Dar es Salaam.
Golden Bush ilipata ushindi wake huo mnono kupitia mabao ya Waziri Mahadhi 'Mandieta', Kudra Omar na Ally Chuo yaliyotosha kuizima Faru katika pambano hilo.
Uongozi wa Golden Bush ulisema umeridhishwa na kiwango cha timu yake na kwa sasa wanaendelea kujipanga kwa ajili ya mechi nyingine za kirafiki ili kugawa 'dozi' kwa wapinzani wao watakaoshuka mbele yao.

Mr Bomba kuagwa kesho kuzikwa kwao Mpwapwa

REV. John Makanyagana
Msanii John Makanyaga (Mchungaji) 'Mr Bomba' enzi za uhai wake


http://www.bongocinema.com/images/products/dangerous_deal.jpg
Moja ya kazi za mwisho mwisho za marehemu Mr Bomba

MWILI wa msanii nyota wa zamani wa Kaole Sanaa, John Makanyanga maarufu kama Mr Bomba unatarajiwa kuagwa kesho jijini Dar es Salaam kabla ya kusafirishwa Mpwapwani, Dodoma kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika siku ya Jumanne.
Kwa mujibu wa mmoja wa wasanii wenzake ambaye hivi karibuni walitoka na filamu mpya iitwayo 'Dangerous Deal', Adam Malele 'Swebe Santana' ni kwamba mwili wa msanii huyo aliyerafiki jana katika Hospitali ya Taifa Muhimbili utaagwa kesho Jumatatu kabla ya kusafirishwa jioni kuepekwa Mpwapwa.
Swebe, ambaye anayemlilia Mr Bomba na kudai ni mtu aliyekuwa naye karibu tangu wakiwa wote Kaole, alisema mwili huo utaagwa nyumbani kwa marehemu Buguruni Malapa karibu na Kanisa la Anglikana, jijini Dar.
"Kwa taarifa ambazo mpaka muda huu nilizonazo ni kwamba marehemu ataagwa kesho kabla ya kusafirishwa kwao Mpwapwa Dodoma kwa ajili ya mazishi ambayo yatafanyika siku ijayofuata," alisema.
Mr Bomba, ambaye kitaaluma alikuwa ni mwalimu aliyewahi kufundisha Shule ya Sekondari Makongo na nyingine binafsi eneo la Mbezi, alifariki jana baada ya kusumbuliwa kwa muda mrefu na kansa ya uvimbe wa kwenye ini mbali na sanaa na ualimu pia alikuwa Mtumishi wa Mungu akiwa kama Mchungaji wa Kanisa la Anglikana.
Enzi za uhai wake msanii huyo aliyejaliwa mwili mkubwa alitamba na tamthilia mbalimbali akiwa na kundi la Kaole Sanaa iliyokuwa ikirushwa na kituo cha ITV, akimudu zaidi nafasi ya 'kibosile' na wakati mwingine kama 'mafia' anayehusika na biashara ya dawa za kulevya na alicheza filamu kadhaa ikiwamo 'Kidole Tumbo', iliyozuiwa kuingizwa sokoni.
Mbali na uigizaji, pia marewhemu alikuwa mtunzi, mwandishi wa miswada ya filamu na kazi ya karibu kuiandaa ni Dangerous Deal ambayo aliitunga na kuiandikia mswada mwenyewe na kuongoza na Swebe ambapo mbali na kuichezea yeye mwenyewe, pia aliigiza na Swebe, Chuchu Hans, Hashim Kambi, Sebastian Mwanangulo, Mama Sonia na wengine.

Mungu aiweke mahali pema roho ya marehemu Mr Bomba.

Waamuzi wa Madagascar kuzihukumu Stars, The Cranes

Stars na Uganda the Cranes walipoumana wiki iliyopita katika pambano lao la kwanza la CHAN na Stars kulala kwa bao 1-0
Na Boniface Wambura
SHIRKISHO la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi kutoka Madagascar kuchezesha mechi kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Uganda (The Cranes) itakayochezwa Jumamosi (Julai 27 mwaka huu) Uwanja wa Mandela ulioko Namboole nje kidogo ya Jiji la Kampala.

Waamuzi wataongozwa na Kanoso Abdoul Ohabee wakati mwamuzi msaidizi namba moja ni Andirvoavonjy Pierre Jean Eric. Mwamuzi msaidizi namba mbili ni Jinoro Velomanana Ferdinand huku Andriamiharisoa Hubert Marie Bruno akiwa mwamuzi wa mezani (fourth official).

Kamishna wa mechi hiyo ya marudiano ya raundi ya mwisho kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ndani (CHAN) ni Ismail Kamal kutoka Ethiopia.

Mechi hiyo namba 38 itachezwa kuanzia saa 10 kamili jioni kwa saa za Afrika Mashariki. Taifa Stars ilipoteza mechi ya kwanza iliyochezwa Julai 13 mwaka huu jijini Dar es Salaam kwa bao 1-0.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iko kambini jijini Mwanza ikijiandaa kwa mechi hiyo itakayoamua ni timu ipi kati ya hizo mbili itacheza Fainali za CHAN mwakani nchini Afrika Kusini.

Mmiliki wa Home Shopping Centre amwagiwa tindikali


Duka moja wapo la Home Shopping Centre lililopo jijini Dar es Salaam 

MTU asiyejulikana juzi usiku alimvamia mmiliki wa maduka ya Home Shopping Centre, Said Mohammed Saad  na kumwagia maji usoni yanayodhaniwa kuwa ni tindikali.
Tukio hilo lililotokea juzi saa 1 usiku karibu na kituo cha Polisi cha Oysterbay, lilithibitishwa na Kaimu Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Ally Mlege kwa kusema kuwa bado polisi wanaendelea na uchunguzi wao ili kuwabaini waliohusika.
“Ni kweli tukio hili limetokea ila polisi wanaendelea na uchunguzi. Tukikamilisha uchunguzi tunatarajia kutoa taarifa kamili za tukio zima,” alisema na kuongeza;
“Hatuna haja ya kuficha ukweli wa tukio hili, uchunguzi wetu ukikamilika na watuhumiwa wakikamatwa kila mtu atajua.”
Taarifa za uhakika kutoka ndani ya Jeshi la Polisi zilizolifikia gazeti hili zilieleza kuwa mtu huyo, alimkuta Saad akiwa anazungumza na mmoja wa wafanyakazi wake katika duka lake jipya lililopo karibu na Kituo cha Polisi cha Oysterbay.
“Wakati akizungumza na mfanyakazi wake, huyo mtu alikuwa kama anapita na alichomoa kitu fulani na kummwagia Saad usoni na kisha kukimbia,” zilieleza taarifa hizo na kuongeza;
“Baada ya tukio hilo alipelekwa katika Hospitali ya AMI, sasa hatujui kama bado yupo hapo au ameondoka, ila sisi tulizungumza naye na alitueleza mwonekano wa mtu aliyemwagia tindikali.”
Taarifa hizo zilifafanua kwamba polisi wanazitumia taarifa hizo walizopewa na Saad, ili kuweza kumkamata mhusika.
Taarifa hizo zilifafanua kuwa polisi wanapanga tena siku ya kumhoji kwa mara ya pili Saad, kwamba watataka kufahamu kama mfanyabiashara huyo alikuwa akipewa vitisho au ujumbe wowote, kabla ya kukutwa na tukio hilo.
Hata hivyo, habari nyingine zilizolifikia Mwananchi Jumapili zilieleza kuwa mtu huyo baada ya kummwagia Saad tindikali, alipanda pikipiki na kutokomea eneo hilo.
“Walikuwa wawili, mmoja alikwenda kufanya unyama na mwingine alibakia katika pikipiki, baada tu ya kumwagia tindikali mtu yule alikimbia mpaka pale alipokuwa imesimama pikipiki, alipanda na kuondoka kwa kasi,” zilieleza habari hizo.
Taarifa zilizopatikana jana asubuhi zilieleza kuwa ndugu na marafiki wa mfanyabiashara huyo, walikuwa katika mipango ya kumpeleka nje ya nchi kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi.

MWANANCHI

Picha za matukio ya miili ya wanajeshi waliouwawa Darfur


MKUU WA MAJESHI GENERALI DAVIS MWAMUNYANGE AKISUBIRI KUPOKEA MIILI YA VIJANA WAKE WALIOUAWA SUDAN
BAADHI YA VIONGOZI WA SERIKALI WAKIONGOZWA NA MAKAMU WA RAIS DR MOHAMMED GHARIB BILAL

MAMA SALMA KIKWETE NA MKUU WA MKOA WA DAR ES SALAAM NAO WALIKUWEPO


NDEGE ILIYOBEBA MIILI YA WANAJESHI MARA BAADA YA KUWASILI KUTOKA SUDAN


MIILI YA WANAJESHI 7 WALIOUAWA SUDAN IKIONEKANA KWENYE NDEGE MARA BAADA YA KUWASILI
WANAJESHI WA JWTZ WAKIBEBA MIILI YA WENZAO WALIOUAWA HUKO SUDAN
NDUGU JAMAA NA MARAFIKI WAKISUBIRI KUWASILI KWA MIILI YA WANAJESHI WALIOUAWA SUDAN
ILIKUWA NI VIGUMU KUVUMILIA HALI HII BAADA YA KUONA MIILI YA WAPENDWA WAO
HALI ILIKUWA YA MACHUNGU KWA NDUGU WA KARIBU
WANAJESHI WA JWTZ WAKIPOKEA MIILI YA WENZAO
MIILI IKITOLEWA KWENYE NDEGE
MMOJA KATI YA MIILI YA MAREHEMU UKIINGIZWA KWENYE GARI
MOJA KATI YA FAMILIA ZA MAREHEM WALIOUAWA SUDAN
FAMILIA ZA MAREHEM WAKISUBIRI KUWAPOKEA WAPENDWA WAO
Miili ya wanajeshi saba mashujaa wa Tanzania waliofariki wakiwa kazini wakitekeleza ulinzi wa amani wa kimataifa katika mkoa wa Darfur nchini Sudan, iliwasilia jana ndege maalumu ya Umoja wa Mataifa.

Kaimu Mkurugenzi wa habari wa JWTZ, Meja Joseph Masanja amesema miili hiyo iliwasili Jumamosi majira ya saa 9.45 alasiri katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa JNIA na imehifadhiwa katika hospitali ya jeshi ya Lugalo hadi Julai 22 ambapo itaagwa rasmi.

Miili iliyowasili ni ya Sajenti Shaibu Othuman, Koplo Oswald Chaula, Koplo Mohamed Juma, Koplo Mohamed Chikilizo, Pte. Rodney Ndunguru, Pte. Peter Werema na Pte. Fortunatus Msofe.

Shughuli za kuagwa miili ya wanajeshi hao zitafanyika katika viwanja vya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la kujenga taifa vilivyoko Upanga jijini Dar es salaam.

Kuwapoteza wanajeshi hawa ni la kwanza na kubwa kwa nchi ya Tanzania tangu Tanzania ilipoanza kuchangia walinzi wa amani chini ya Umoja wa Mataifa mwaka 2007. Wanajeshi wengine watatu wa Tanzania walifariki dunia mwezi uliopita baada ya chombo chao cha kusafiria kusombwa na maji ya mto uliokuwa umefurika huko nchini Sudan. 

 
BONGOCLAN