STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, November 29, 2012

Sharomilionea azikwa
*Waliomuibia kusakwa nyumba kwa nyumba
*Serikali yamlilia pamoja na Mlopelo, Maganga
mwili wa Sharo Milionea ukiingizwa kaburini jana










Na Lulu George na Steven William, Muheza
MAELFU ya waombolezaji walijitokeza jana kushiriki mazishi ya msanii muigizaji na mwimbaji Hussein Ramadhani Mkiety (Sharomilionea) yaliyofanyika kwenye kijiji cha Lusanga wilayani hapa huku baadhi yao wakipoteza fahamu.
Mazishi hayo yaliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali na vyama vya siasa, wakiwamo Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Subira Mgalu na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, yalifanyika saa 7:00 mchana katika makaburi yaliyopo nyumbani kwa mama wa msanii huyo, kitongoji cha Jibandeni katika kijiji cha Lusanga wilayani Muheza, Tanga.
Wasanii mbalimbali nyota walihudhuria pia mazishi ya msanii mwenzao, baadhi wakiwa ni Amiri Athumani ‘King Majuto’, Singo Mtambalike ‘Richie’, Jacob Steven ‘JB’, Claudi, Wema Sepetu, Jacqueline Wolper, Hamisi Mwinjuma Mwana-FA, Muhogo Mchungu, Kingwedu na Dude.
Wengine waliofika kwenye msiba huo ni Mbunge wa Jimbo la Muheza, Herbert Mntangi, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Muheza, Amiri Kiroboto na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Muheza, Ibrahimu Matovu na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM aliyekuwa akimwakilisha Rais Kikwete, Nape Nnauye .
Waombolezaji kutoka nje ya Muheza walianza kumiminika kijijini Lusanga tangu juzi jioni na shughuli za mazishi zilikuwa zikiongozwa na kamati iliyokuwa chini ya uenyekiti wa Mkuu wa Wilaya, Mgalu.
Shughuli za ibada ya mazishi ziliongozwa na Sheikh Twaha Juma ambapo baada ya jeneza kutolewa ndani ya nyumba ya mama wa msanii huyo, liliwekwa uwanjani na kuswaliwa na waumini kutoka maeneo mbalimbali nchini kabla ya kupelekwa makaburini, eneo la umbali wa
mita 100 kutoka nyumbani kwao.
Mamia ya waombolezaji waliojitokeza walionekana kujawa na simanzi kubwa na baadhi yao, wakiwamo ndugu wa marehemu, walipoteza fahamu na kukimbiziwa katika Hospitali Teule ya Wilaya ya Muheza.

DC ATOA SIKU MBILI
Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Subira Mgalu, aliwapa siku mbili (kuanzia jana) watu waliopora vitu vya marehemu Sharomilionea wakati alipopata ajali ya gari na kufariki dunia katika Kijiji cha Maguzoni wilayani hapa kuvirejesha mara moja kabla ya kuchukuliwa hatua kali za kisheria.
Mgalu aliyasema hayo wakati akizungumza mbele ya umati wa watu waliofika kushiriki mazishi ya msanii huyo yaliyofanyika katika Kijiji cha Lusanga ambako ni nyumbani kwa marehemu.
Mgalu alilaani kitendo hicho na kusema kwamba hakikubaliki hata kidogo kwani ni cha aibu na si cha kiungwana, hivyo wote waliohusika na wizi huo wajitokeze na kurejesha vitu vya marehemu.
Alisema kuwa Wilaya ya Muheza inapitiwa na barabara kuu na hivyo, wakazi wake wote wanapaswa kuwa wakarimu na kusaidia kwa upendo watu wanaopata ajali badala ya kujihusisha vitendo vya wizi dhidi ya wanaopatwa na ajali.
Alisema kuwa baada ya siku mbili, polisi wataendesha msako mkali wa nyumba kwa nyumba katika kijiji cha Maguzoni na kwamba, ni lazima wahusika wote watajulikana na kutiwa nguvuni.
Mgalu alitangaza hatua hiyo kutokana na taarifa kuwa mara tu baada ya Sharomilionea kupata ajali saa 3:00 usiku juzi na kufariki dunia, watu wasiojulikana waliuvamia mwili wake na kumuibia vitu vyote ikiwa ni pamoja na nguo alizovaa kabla ya kumuacha na soksi na nguo yake ya ndani tu.

SALAMU ZA RAIS KIKWETE
Nape aliyekuwa akimwakilisha Rais Jakaya Kikwete, alisema Serikali imeguswa na msiba huo na kwamba iko pamoja na wasanii katika kuomboleza kifo cha Sharomilionea.
Alisema Serikali inathamini kwa kiasi kikubwa mchango wa wasanii wakiwamo wa filamu, na kwamba iko nao katika kuwaendeleza.
“Rais amenituma nimwakilishe katika msiba huu… anasema binafsi ameguswa sana na msiba huu wa Sharomilionea kwani ni msanii ambaye alikuwa mbunifu na alikuwa akichipukia kwa hali ya juu katika fani ya uigizaji,” alisema Nape.
Alisema sasa ni wakati muafaka kwa wasanii hao kuungana na kuhakikisha kwamba jasho lao halipotei wala kunyonywa na wajanja wachache wa kati ambao kila siku wamekuwa wakinufaika huku wasanii wakiendelea kurudi nyuma.
Nnauye alisema mbali ya wasanii wa filamu pia wasanii wa fani nyingine nao wanastahili kuungana kuhakikisha jasho lao linawanufaisha na siyo mtu mwingine ili kujiletea maendeleo wao binafsi na familia zao kwa ujumla.
Nape alimkabidhi bahasha ya rambirambi ya msiba huo Rais wa Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF), Simon Mwakifwamba.
Mkuu wa Wilaya ya Muheza, Mgalu, pia alisoma salamu za rambirambi kutoka kwa mke wa Rais, Mama Salma Kikwete, ambaye Mwenyekiti wa Taasisi ya Wanawake na Maendeleo (WAMA).

SERIKALI YAWALILIA
Wakati huo huo, Serikali imeelezea kusikitishwa na vifo vya wasanii watatu wa filamu nchini vilivyotokea mwezi huu vya waigizaji John Maganga, Halid Hemed ‘Mlopelo’ na Hussein Ramadhani Mkiety 'Sharomilionea'.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Waziri ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, misiba hiyo mitatu imeleta simanzi kubwa kwa serikali, familia, wasanii wenzao na wapenzi wa filamu na muziki kwa ujumla.
"Wasanii wote hawa ndiyo kwanza wameanza kung'ara katika tasnia ya filamu na sote tu mashahidi kwamba walianza kuleta matumaini makubwa katika kukuza na kuendeleza tasnia ya filamu na muziki, hususan muziki wa kizazi kipya. Lakini Ghafla wametutoka. tunasikitika sana kwa kuwa vifo hivi vimekuwa ni vya ghafla mno," alisema Dk. Mukangara katika taarifa hiyo.
"Hili ni pigo kubwa kwa taifa na jamii nzima, hasa wakati huu ambao serikali inafanya juhudi kubwa za kuhakikisha tasnia ya filamu na muziki zinakuwa rasmi.
"Serikali inatoa pole nyingi kwa familia, ndugu, jamaa na wote walioguswa na misiba hii. Ni imani ya Serikali kuwa wasanii wa tasnia hizi wataendeleza yote mazuri waliyoyafanya wenzao ili kuendelea kuwaenzi. 
"Serikali inaungana na familia na wapenzi wa tasnia yza filamu na muziki katika kipindi hiki kigumu.
"Kwa pamoja tuungani katika kuwaombea marehemu John Maganga, Halidi Mohamed na Hussein Mkieti wapumziko kwa amani. Mungu azilaze roho zao mahali pema Peponi. Amina," ilimaliza taarifa hiyo.



Baadhi ya waombolezaji katika msiba huo

King Majuto akiwa katika sura ya huzuni makaburini
Chanzo: NIPASHE

Wednesday, November 28, 2012

JB M'PIANA ATUA DAR, AAHIDI SHOO KALI IJUMAA LEADERS


JB Mpiana akizungumza mna Waandishi Dar es Salaam leo

MWANAMUZIKI nguli wa dansi Afrika, JB Mpiana ametua jijini Dar es Salaam juzi tayari kwa maonyesho kadhaa, likiwamo lile la uzinduzi wa albamu ya Mashujaa Band inayokwenda kwa jina la Risasi Kidole, litakalofanyika Ijumaa katika viwanja vya Leaders Club, Dar es Salaam.
Kabla ya shoo hiyo ya Ijumaa, JB Mpiana ambaye amekuja na kundi lake zima la Wenge Musica BCBG, likiwahusisha wanamuziki wake za zamani na wapya, atauwasha moto jijini Arusha kesho kabla ya kufanya kweli jijini Mwanza Jumapili.
Akizungumza katika Hoteli ya Double Tree iliyopo Masaki, Dar es Salaam, JB Mpiana ameahidi kutoa shoo ya aina yake ambayo anaamini itakonga nyoyo za Watanzania.
Alisema kuwa amefurahisa sana kuja Tanzania kwa mara nyingine, ikiwa ni pamoja na mapokezi aliyoyapata, akiahidi kutoa burudani ya nguvu kwa Watanzania kuwalipa mapokezi waliyomwonesha.
 “Nina imani waandaaji wamefanya maandalizi ya kutosha, nimekuja na wanamuziki wangu wote 25, nimekuja na vifaa vyangu vyote vilivyopo katika kundi langu, ili kutoa burudani ya kutosha kwa Watanzania.
 “Nimewaletea albamu inayojulikana kwa jina la Biloko (chakula), watanzania wajiandae kula, yaani kupata burudani ya nguvu kutoka kwangu na kundi langu,” alisema JB Mpiana.
Kati ya wasanii aliokuja nao, alisema wapo wale wa zamani aliokuwa nao enzi hizo ndani ya kundi lake hilo lilipoanza kutamba katika anga ya muziki, na wengine wapya ambao wapo fiti.
Katika programu yake hapa nchini, amesema atapiga nyimbo zake za zamani na mpya ili kuwapa watanzania fursa ya kupata vionjo vya zamani na vipya, kuweza kupima ubora wa kazi hizo.
Akizungumzia muziki wa Tanzania, amewataka wasanii wa hapa nchini kujituma na kuzipenda kazi zao na kuiheshimu waweze kufanikiwa katika kazi zao hizo.
Juu ya kiongozi wa safu ya unenguaji, alisema safari hii inaongozwa na mwanadada Zambrota, ikiwa ni baada ya kufariki kwa aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo, Monica.
 “Nimefurahi sana kuja Tanzania kwa mara nyingine, wapenzi wa burudani wajiandae kupata shoo ya nguvu kutoka kwa JB Mpiana,” alisema mkali huyo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa kampuni ya QS Muhonda, Joseph Muhonda, waratibu wa maonesho hayo, amesema kuwa ni matarajio yao wakazi wa Dar es Salaam, Arusha na Mwanza, watafurahia shoo hiyo kutoka kwa JB Mpiana na Mashujaa kutokana na maandalizi ya nguvu waliyofanya, akiwataka wakazi wa maeneo hayo, kujitokeza kwa wingi.
Alisema kuwa katoka onesho la JB Mpiana jijini Arusha, atatumbuiza katika ukumbi wa Triple A kuanzia saa tatu usiku, wakati Desemba Mosi atakuwa katika ukumbi wa Villa Park kuanzia saa tatu usiku.
 “Maandalizi yote yapo sawa, kila kitu kimekamilika, tuliahidi JB Mpiana anakuja na kweli amekuja kama mlivyomuona,” alisema na kuongeza kuwa JB Mpiana atasindikizwa na wasanii wa Bongo Fleva kama H Baba, MB Doggy, Ney wa Mitego na wengineo.

TENGA ASEMA TFF, SERIKALI KUKUTANA KUMALIZA UTATA WA TRA

Tenga


SHIRIKISHO la soka Tanzania (TFF) pamoja na Wizara ya Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, wanatarajiwa kukutana na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa ajili ya kuzungumzia mustakabali mzima wa suala la makato katika michezo mbalimbali.
Hatua hiyo inafuatia TRA kuzifunga akaunti za udhamini wa ligi hiyo kama shinikizo kwa TFF  kulipa makato ya kodi kwenye mishahara ya timu ya taifa ‘Taifa Stars’ tangu kipindi cha kocha Mbrazil Marcio Maximo kwa madai kwamba imekuwa haikatwi kodi za mishahara ya makocha na hivyo kufikia sh milioni 157,407.968.00.
Rais wa TFF, Leodger Tenga amesema leo kwamba kitendo walichokifanya TRA ni jambo la heri kwani kinaonyesha majukumu ya Serikali katika soka.
Alisema ukaribu uliopo sasa baina ya Serikali chini ya Rais Kikwete na soka ni mkubwa kutokana na ukweli kwamba  inachangia kwa kiasi kikubwa kulipa mishahara ya makocha wa timu za Taifa.
Alisema suala hilo linahitaji mazungumzo baina ya pande hizo ili kuweza kulipatia ufumbuzi na hakuna haja ya kuilaumu TRA kwa sababu inafuata taratibu zilinazostahili kwa mujibu wa kanuni.
 “Hawana njia nyingine ya kufanya hivyo ufumbuzi ni sisi ni kukutana na Wizara na TRA ili kulizungumza hili na katika siku mbili hizi tunarajiwa kukutana,”alisema
Tenga aliongeza kuwa TFF haina uwezo wa kulipa fedha hizo na kwamba hela zilizochuliwa si za Shirikisho hilo bali ni za ligi kuu Bara ambazo zimetolewa na wadhamini wake, kampuni ya simu za mkononi,Vodacom kwa maelekezo maalum.
 “Ni jambo nyeti na lazima lifanyiwe kazi, hatuwezi kumlamu mtu na nimatumaini tutakapoketi pamoja tutapata ufumbuzi,”alisema.
Aidha, Tenga alisema wanatarajia kuzungumzia suala la makato ya michezo mbalimbali ambayo yamekuwa yakilalamikiwa na vilabu kwa muda mrefu.
 “Changamoto za namna hiyo tumekuwa tukizifanyia kazi kwa muda mrefu na ndiyo maana tangu mwaka 2005 asilimia ya makato ya TFF imekuwa ikipunguzwa, nadhani ni kuendelea kuwa na subira.

SIMBA WAMLILIA SHARO MILIONEA


Na Ezekiel Kamwaga
MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Mhe; Ismail Aden Rage, amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa aliyekuwa msanii maarufu wa muziki na filamu, Hussein Ramadhani Mkiety, maarufu kwa jina la Sharo Milionea, kilichotokea jana usiku mkoani Tanga.

Kwa niaba ya klabu ya Simba na kwa niaba yake binafsi, Mwenyekiti anapenda kutuma salamu za pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki wote wa marehemu kutokana na msiba huu mkubwa sana si kwao pekee bali kwa taifa zima la Tanzania.

Sharo Milionea hakuwa msanii wa kawaida. Yeye ni miongoni mwa kizazi kipya cha vijana wa Kitanzania walioamua kutafuta maisha kwa kutumia vipaji walivyopewa na Mungu. Yeye alijitumbukiza zaidi katika uchekeshaji na baadaye akaonyesha uwezo mkubwa katika fani ya muziki.

Sharo alikuwa maarufu kiasi kwamba makampuni makubwa yalikuwa yameanza kumtumia kwenye matangazo yao ya kibiashara. Hii ilionyesha kwamba makampuni yalibaini faida itakayopatikana kwao kwa kumtumia msanii huyu ambaye bado alikuwa na heshima kubwa kwenye jamii kutokana na haiba yake na uwezo wake kwenye kazi alizokuwa akifanya.

Msiba huu umekuwa pigo kubwa kwa tasnia ya filamu ambayo bado inaomboleza vifo vya wasanii kama Steven Kanumba, Mlopelo na John Steven Maganga, waliofariki dunia mwaka huu pia.

"Ifahamike kwamba Sharo Milionea alikuwa miongoni mwa wasanii wa Kitanzania waliotuma maombi Simba ya kutaka kushiriki kwenye mchakato wa kutengeneza wimbo rasmi wa klabu ya Simba. Yeye alikuwa miongoni mwa wasanii waliokuwa wakiumizwa na ukweli kwamba klabu kama Simba inashindwa kufanya biashara ya kuuza nyimbo zake ilhali wanunuaji wapo," alisema Rage.

Kwa klabu ya Simba, namna pekee ya kumuenzi marehemu ni kufanyia kazi mambo ambayo alikuwa akitushauri kwenye eneo la biashara. Ni matumaini yetu kwamba iwapo tutafanya lile alilokuwa akitushauri, atakuwa mwenye amani huko alikotangulia mbele ya haki.

Rage amewaomba wasanii wa tasnia ya filamu na muziki kuwa watulivu na wenye subra kwenye kipindi hiki kigumu kwao. Kila kitu katika maisha ya wanadamu kinapangwa na Mwenyezi Mungu na ndiyo maana Waswahili wana msemo kuwa Kazi ya Mungu haina makosa.

Mola na ailaze mahali pema peponi roho ya marehemu Hussein Ramadhani Mkeity

(Kamwaga ni Ofisa Habari wa Simba SC).

SUPER D APANIA KUPELEKA VIJANA WAKE OLIMPIKI 2016

Kocha wa Kimataifa wa Mchezo wa Masumbwi nchini Rajabu Mhamila 'Super D' akiwa katika picha ya pamoja na vijana waliojitokeza katika mazoezi ya ngumi ufukwe wa GYKHANA Dar es salaam jana Picha na www.superdboxingcoach.blogspot.com


KLABU ya ngumi ya Ashanti Ilala imeota kuwa moja ya klabu itakayotoa wawakilishi katika michezo ya Olimpiki itakayofanyika mwaka 2016  nchini Brazil.

Klabu hiyo ambayo kwa sasa inaundwa na chipkizi 18 pamoja na mabondia wakongwe imepania kufanya hivyo huku ikijitapa kuwa itaanza kufanya maajabu kupitia mashindano ya taifa ya mchezo huo yatakayofanyika Januari mwakani.

Akizungumza na gaazeti hili Dar es Salaam jana, Kocha wa ngumi wa klabu ya Ashanti  pamoja na timu ya Mkoa wa Ilala Kimichezo Rajabu Mhamila 'Super D' alisema kwa sasa klabu yake imejikita katika maandalizi kabambe kuhakikisha inaingiza mabondia wengi katika timu ya taifa ambao baadaye wataingia kwenye kinyang'anyiro cha kuwania nafasi za kufuzu kucheza Olimpiki.


Alisema tayari jumla ya vijana 18 wanajifua katika Ufukwe wa Gymkhana Dar es Salaam kwa ajili ya mapambano mbalimbali ikiwemo ya ubingwa wa taifa ambayo yanaandaliwa na Shirikisho la Ngumi Tanzania (BFT).


Alisema vijana wengi waliopo kwenye klabu hiyo ni wenye umri chini ya miaka 12 na chini ya miaka 20 ambapo amewataja kuwa umri huo ni mzuri kwani kijana atakuwa mwepesi wa kuelewa kile ambacho atakuwa anafundishwa na makocha wake
Super D ambaye anafundisha kwa kutumia mbinu mbalimbali zikiwemo kwa njia ya DVD ambazo zinatoa mwanga kwa mchezaji kujua mchezo na kufahamu zaidi mbinu mpya zitumiwazo na mataifa mbali mbali Duniani.
Wakiwemo mabondia bingwa wa dunia kama Manny Paquaio,Floyd Maywether,Amir Khani, Mohamed Ali ,Mike Tayson na wengine wengi wanaotamba na waliotamba katika mchezo huo wa masumbwi Duniani
Super D ametoa wito kwa makampuni mbalimbali kujitokeza kutoa sapoti ya mchezo wa masumbwi kwani ndio mchezo pekee unaoweza kututoa kimasomaso watanzania tukafurahi

YOMBAYOMBA KUPAMBANA NA 'GOGO POA' KUCHANGIA WAGOJWA WA MOYO

 Saidi Omari 'Gogo Poa' .kushoto na Rajabu Mhamila'Super D' 
MABONDIA wa zamani walioiletea nchi Medali katika mashindano ya All Africa Games na Jumuiya ya Madola miaka ya 1998, Michael Yombayomba na Said Omari 'Gogo Poa' wamejitolea kupanda ulingoni na kutwangana kwa ajili ya kuchangia watoto wenye matatizo ya Moyo.





Yombayomba ambaye alitwaa medali ya dhahabu katika mashindano ya Jumuia ya Madola katika miaka hiyo ya 1998 na Gogo Poa wameamua kutwangana ikiwa ni sehemu ya mchango wao kwa watoto hao huku wakisisitiza wadau kuunga mkono tukio hilo.


Akizungumza na gaazeti hili Gogo Poa alisema pambano hilo litafanyika Januari 25 mwakani ambapo pia litasindikizwa na mapambano ya mabondia mbalimbali wenye viwango vya juu nchini.


"Tumeguswa sana na tatizo hili la watoto wanaougua ugonjwa wa moyo ambao wengi wao hukosa fedha kwa ajili ya matibabu hivyo sisi kama sehemu ya jamii tutahamasisha uchagiaji wa fedha kwa kujitolea kupanda ulingoni na chochote kitakachopatikana itakuwa ni sehemu ya mchango wetu,"alisema Gogo Poa.

Aliwaomba wadhamini na wadau mbalimbali kujitokeza kuzamini mchezo huo ambao una tija ya kuchangia watoto hawo kwani ata wao walikuwa watoto ndio mana wamekuwa katika afya nzuri na kucheza mchezo huo na kuiletea sifa taifa hili kwa kuleta Medali

Hivyo na watoto hawo wanatakiwa wawe na AFya njema ili wapate kuja kurithi nyayo zetu bila afya ya mtoto michezo yote akuna kwa kuwa vipaji vingi vinangaliwa ukiwa mtoto

Zahoro Pazi amfagilia Kim kuchezesha vijana Kili Stars

Zahoro Pazi (kushoto) akiwa uwanjani akichuana na Jerry Santo aliyekuwa Simba enzi hizo
MSHAMBULIAJI mkali wa Azam, Zahoro Pazi, amemfagilia kocha mkuu wa timu ya taifa, Taifa Stars, Kim Poulsen anayeinoa timu ya Tanzania Bara Kilimanjaro Stars katika michuano ya Kombe la Chalenji inayoendelea nchini Uganda, kwa uamuzi wake wa kuwaamini vijana katika kikosi cha timu hiyo.
Pazi, anayefahamika kwa jina la utani kama 'Cristiano Ronaldo', alisema kitendo kilichofanywa na Kim kuwapanga wachezaji karibu wote vijana ndio chachu ya ushindi wa mabao 2-0 iliyopata mbele ya Sudan na kuwataka watanzania wamuunge mkono kwani jambo hilo litailetea manufaa Tanzania siku za baadae.
Alisema kupewa nafasi kwa vijana kunawapa nafasi ya kupata uzoefu na kuondoka woga na hivyo kuweza kulitumikia taifa wakiwa Taifa Stars kama mashujaa wa Tanzania jambo ambalo limekuwa likililiwa kwa muda mrefu.
"Kwa kweli nimefurahishwa na uamuzi wa kocha Kim kuwapanga karibu vijana wote katika kikosi cha Kili Stars, kwani nadhani ndio chachu ya ushindi na pia italisaidia taifa kuweza kufanya vema zaidi kwani vijana hao ndio wanaoweza kuivusha Tanzania katika michuano mikubwa zaidi ya kimataifa," alisema.
Pazi, mtoto wa kipa wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Idd Pazi 'Father' alisema kilichofanywa na Kim kinawatia moyo wachezaji vijana kama yeye ambao walikuwa wakipuuzwa Stars ilipokuwa chini ya Jen Poulsen aliyetimuliwa na nafasi yake kuchukuliwa na Kim.
"Hata mimi ambaye nimekuwa nje ya timu ya taifa tangu Maximo alipoondoka nimepata moyo na kuamini nikijibidiisha naweza kurejea tena Stars," alisema.
Aliongeza kwa kuwataka Watanzania wamuunge mkono kocha huyo toka Denmark kwa madai anaonekana ni kocha mwenye mipango na maendeleo ya mbali kaa alivyokuwa Maximo hivyo aachiwe afanye kazi kwa raha zake na kwa muda mrefu ili Tanzania ivune matunda yanayoanza kuonekana.
Kilimanjaro Stars leo inatarajiwa kutupa karata yake ya pili katika michuano hiyo ya Chalenji kwa kuvaana na Burundi, ikiwa inachekelea ushindi iliyopata dhidi ya Sudan kwa mabao ya John Bocco 'Adebayor'.

Kivumbi cha Ligi ya England kuendelea leo, Aston Villa yaizamisha Reading

WAKATI vinara wa Ligi Kuu ya England, Manchester United ikitarajiwa kushuka dimbani leo kuvaana na West Ham ili kujihakikishia ufalme wa kileleni, Aston Villa yenyewe jana iliizamisha Reading kwa bao 1-0 huku kocha Harry Redknapp akianza kibarua chake QPR kwa kuambulia suluhu dhidi ya Sunderland.
Manchester itaavana na wagoinga nyundo hao kwenye dimba lao la nyumbani la Old Trafford, ikiwa ni siku chache tangu ilipoiizamisha QPR mabao 3-1.
Mashetani hao wekundu wapo kileleni mwa msimamo wakiwa na pointi 30, moja dhidi ya mabingwa watetezi, Manchester City ambao nao leo watashuka dimbani ugenini kuvaana na Wigan, huku LIverpool itakaribishwa na Tottenham na Arsenal kupambana na Eveton.
 Mechi nyingine zinazochezwa leo ni pambano la Southampton itakayovaana na Norwich City, Stoke City dhidi ya Newcastle United, Swansea City itakayopambana na West Bromwich na Clesea itakayoikaribisha Fulham.
Katika mechi zilizochezwa jana kwenye mfululizo wa ligi hiyo maarufu, Aston Villa iliizamisha Reading kwa kuilaza bao 1-0 lililotupiwa kambani na mshambuliaji wake, Christian Banteke katika dakika ya 80 kwa pasi ya Westwood.
Nayo QPR ikiwa chini ya kocha wake mpya, Harry Redknapp ililazimisha suluhu ugenini dhidi ya wenyeji wao Sunderland na kuifanya timu hiyo inayoburuza mkia katika msimamo wa ligi hiyo kufikisha pointi tano.
ratiba kamili ya mechi zinazochezwa leo katiika ligi hiyo ya England ni kama ifuatavyo:

 Chelsea v Fulham 19:45

  • Everton v Arsenal 19:45
  • Southampton v Norwich 19:45
  • Stoke v Newcastle 19:45
  • Swansea v West Brom 19:45
  • Tottenham v Liverpool 19:45
  • Man Utd v West Ham 20:00
  • Wigan v Man City
  • Wachezaji  Nathan Baker wa Aston Villa (kulia) na Jason Robert wakichuana katika pambano lao la jana.



Stars vitani na Burundi leo, Uganda yafuzu

Wachezaji wa timu ya Kilimanjaro wakitania kwenye mazoezi ya timu yao, ambapo jioni ya leo inavaana na Burundi

Na Somoe Ng'itu, Kampala
WAKATI wenyeji Uganda jana walikuwa wa kwanza kutinga hatua ya robo fainali ya Kombe la Chalenji baada ya kushinda 1-0 dhidi ya Ethiopia, timu ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) itatupa karata yake ya pili katika mechi ya kundi B dhidi ya Burundi leo.
Goli pekee kutoka kwa Brian Umony liliwafanya Uganda kufuzu baada ya kufikisha pointi sita katika kundi A, huku Kenya ambayo ilishinda 2-0 mapema jana dhidi ya Sudan Kusini ikishika nafasi ya pili baada ya mechi mbili. Ethiopia pia ina pointi tatu lakini iko katika nafasi ya tatu kutokana na tofauti ya magoli. Katika mechi ya kwanza Uganda ilishinda 1-0 dhidi ya Kenya, wakati Ethiopia iliifunga Sudan Kusini 1-0 katika siku ya ufunzi wa michuano hiyo inayofanyika kwenye Uwanja wa Namboole hapa Kampala.
Baada ya kushinda 2-0 dhidi ya Sudan katika mechi ya ufunguzi, Kilimanjaro Stars itashuka dimbani leo kuikabili Burundi kuanzia 12:00 jioni.
Burundi ndio kinara wa kundi hilo kutokana na kuwa na magoli mengi ya kufunga ambapo alipata ushindi wa 5-1 dhidi ya Somalia.
Akizungumza na gazeti hili jana baada ya mazoezi kwenye Uwanja wa Chuo Kikuu cha Makerere, Kocha Mkuu wa Kilimanjaro Stars, Kim Poulsen, alisema kwamba wachezaji wake wako vizuri na amejipanga kuikabili Burundi na hatimaye kuibuka na ushindi.
Kim alisema kwamba Burundi ni timu inayotumia nguvu lakini wachezaji wake wamejiandaa kutumia kasi waliyonayo kuwatoka wapinzani wao ambao wengi wana miili mikubwa wakiongozwa na mshambuliaji wa zamani wa Simba, Selemani Ndikumana.
Alisema kuwa mashindano ni magumu na hakuna timu ya kuidharau hivyo amewaandaa wachezaji wake kupambana kuanzia mwanzo hadi mwisho wa mchezo.
"Kila mchezo tutaingia na mbinu tofauti, nimewasoma Burundi wakati walipokuwa wanacheza na Somalia...naamini tutawafunga ili tuongoze kundi letu," alisema Kim ambaye hii ni mara yake ya kwanza kufika Uganda na kuongoza timu kwenye michuano ya Kombe la Chalenji inayoendelea.
Aliongeza kwamba anafurahishwa na kikosi chake kucheza kwa kuelewana na anaamini kitafanya vizuri mechi zote zinazofuata na kutimiza malengo ya kurejea nyumbani na ubingwa.
Nahodha wa timu hiyo, Juma Kaseja, aliliambia gazeti hili kwamba jitihada za kila mchezaji ndiyo zinafanikisha matokeo mazuri na anaamini watasonga mbele katika hatua inayofuata.
Kaseja alisema kwamba mashindano haya yana upinzani na wao wamejiandaa kukabiliana na changamoto hiyo.
"Ni mashindano ambayo tunakutana wachezaji tunaofahamiana hasa Rwanda, Burundi, Kenya na Uganda, yana ushindani na yanatufanya tujifunze zaidi kila mara, mwalimu aliiangalia Burundi hivyo ametupa maelekezo ya nini cha kufanya ili tufanye vizuri," alisema Kaseja.
Aliongeza kwamba ushindi walioupata katika mechi ya kwanza haukuwa wa kubahatisha na wanaamini mwaka huu watafika mbali.
Aliwataka mashabiki wa Tanzania waendelee kuwaombea ili wao wafanye kile walichotarajia na kurudi nyumbani na heshima.
Kilimanjaro Stars inayodhaminiwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) itakamilisha mechi za hatua ya makundi Jumapili kwa kuivaa Somalia kuanzia saa nane mchana kwenye uwanja utakaotajwa hapo baadaye.
Mchezo mwingine utakaochezwa leo mchana ni kati ya Somalia na Sudan ambazo zote zilipoteza mechi zao za kwanza.

SHARO KUZIKWA LEO, NCHI NZIMA NI MAJONZI MATUPU

Sharo Milionea enzi za uhai wake
WAKATI salamu za rambirambi zikiendelea kumiminika kufuatia kifo cha msanii wa vichekesho nchini, Hussein Mkiety maarufu kama Sharomilionea, aliyefariki dunia katika ajali ya gari juzi usiku, nyota huyo atazikwa leo saa 10:00 jioni.
Kwa mujibu mjomba wa marehemu, Omar Fundikira, Sharo atazikwa nyumbani kwao katika kijiji cha Lusanga wilayani Muheza mkoani Tanga.
Sharo alifariki dunia alifariki kufuatia ajali ya gari iliyotokea eneo la Maguzoni, Songa, Muheza.
Kwa mujibu wa kamanda wa polisi wa mkoa wa Tanga, Constatine Masawe, Sharo alikuwa peke yake garini wakati ajali hiyo ikitokea na mwili wake uko katika hospitali ya Teule, Muheza.
Kamanda Masawe alisema Sharo akiwa anaendesha gari namba T478 BVR Toyota Harrier akitokea Dar es Salaam kwenda Muheza na alipofika eneo hilo gari lake liliacha njia na kupinduka mara kadhaa na kusababisha kifo chake.
Taarifa za kifo chake kilianza kuzagaa kwa watu kutumiana ujumbe wa simu kabla ya kuthibitishwa na Kamanda Constantine.
Umati wa watu ulikusanyika katika hospitali Teule ya Wilaya ya Muheza kujaribu kuushuhudia mwili wa muigizaji huyo aliyepata umaarufu mkubwa kutokana na vibwagizo vyake vya "Umebugi meen!", "kamata mwizi meen!" na "Ooh mamma!"
Mwandishi wetu ambaye alifika katika chumba cha maiti katika hospitali hiyo alishuhudia umati wa watu ukisubiri kuingia ndani ya chumba hicho kuuona mwili wa msanii huyo aliyeumia vibaya kichwani na kifuani.
Kutokana na hali hiyo mhudumu wa chumba cha maiti aliyejitaja kwa jina la Mhusa na daktari wa hospitali hiyo aliyejitaja kwa Kibaja walipata wakati mgumu kuwazuia watu waliofurika wakiwamo wanafunzi wanaosomea udaktari katika hospitali hiyo.
Baadaye mwandishi wetu alifika nyumbani kwa marehemu katika kijiji cha Lusanga ambapo alikuta vilio kutoka kwa ndugu na jamaa huku umati wa watu ukiwa umefurika nyumbani hapo pia.
Miongoni mwa wasanii waliokuwapo nyumbani hapo akiwamo mkongwe aliyekuwa akifanya naye kazi nyingi, Amri Athuman maarufu King Majuto, alisema kuwa amesikitishwa mno na msiba huo.
Majuto alisema anakosa maneno ya kusema kutokana na ukubwa wa msiba huo kwake kwa kumpoteza kijana aliyemsifu kuwa ni mchapakazi aliyekuwa na usongo wa mafanikio.
Mkogwe huyo huyo alisema kifo cha Sharo ni pigo kwa wasanii wote hususan yeye mwenyewe ambaye alikuwa ni meneja wake katika kazi zao za kila siku.
“Kusema kweli sioni wa kuziba pengo hili… ni mtu ambaye nilimzoea sana na sijui ni kipi cha kusema ila Mwenyezi Mungu anajua zaidi yetu,” alisema Majuto.
Rambirambi pia zilitoka katika serikali wilayani Muheza ambapo ilisema imeshtushwa mno na kifo cha Sharo kutokana na umahiri wake na kuifanya kazi ya usanii kuwa ajira kama zilivyo ajira nyingine.
Mkuu wa wilaya ya Muheza, Subira Mgalu alisema kuwa kimsingi msanii huyo amekuwa mfano wa kuigwa na wasanii wengine nchini kutokana na kuithamini na kuipenda  kazi yake na hivyo kuwa mbunifu siku hadi siku.
"Kwa kweli marehemu Sharo alikuwa ni mbunifu katika kazi yake na aliifanya sanaa kuwa ni ajira kama zilivyo ajira nyingine, kweli huu ni mfano wa kuigwa na vijana na kupitia yeye wengi wameweza na wanaweza kujitambua kuwa wana vipaji ambavyo wakivitumia vitawaondoa katika umasikini. Inasikitisha kwamba ametutoka mapema sana kipindi ambacho wapenzi wa sanaa na watoto walishamzoea kumwona na kumsikia," alisema Mgalu.
Naye mwenyekiti wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage, alisema amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa msanii huyo.
Katika taarifa yake iliyotolewa na afisa habari wa klabu hiyo, Ezekiel Kamwaga, Rage alisema kwa niaba ya klabu ya Simba na kwa niaba yake binafsi, anapenda kutuma salamu za pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa na marafiki wote wa marehemu kwa kuwa na msiba huu ni mkubwa sana si kwao pekee bali kwa taifa zima la Tanzania.
Taarifa hiyo ilisema: "Sharo Milionea hakuwa msanii wa kawaida. Yeye ni miongoni mwa kizazi kipya cha vijana wa Kitanzania walioamua kutafuta maisha kwa kutumia vipaji walivyopewa na Mungu. Yeye alijitumbukiza zaidi katika uchekeshaji na baadaye akaonyesha uwezo mkubwa katika fani ya muziki.
"Sharo alikuwa maarufu kiasi kwamba makampuni makubwa yalikuwa yameanza kumtumia kwenye matangazo yao ya kibiashara. Hii ilionyesha kwamba makampuni yalibaini faida itakayopatikana kwao kwa kumtumia msanii huyu ambaye bado alikuwa na heshima kubwa kwenye jamii kutokana na haiba yake na uwezo wake kwenye kazi alizokuwa akifanya.
"Msiba huu umekuwa pigo kubwa kwa tasnia ya filamu ambayo bado inaomboleza vifo vya wasanii kama Steven Kanumba, Mlopelo na John Steven Maganga, waliofariki dunia mwaka huu pia.
"Ifahamike kwamba Sharomilionea alikuwa miongoni mwa wasanii wa Kitanzania waliotuma maombi Simba ya kutaka kushiriki kwenye mchakato wa kutengeneza wimbo rasmi wa klabu ya Simba. Yeye alikuwa miongoni mwa wasanii waliokuwa wakiumizwa na ukweli kwamba klabu kama Simba inashindwa kufanya biashara ya kuuza nyimbo zake ilhali wanunuaji wapo."
Taarifa hiyo iliendelea: "Kwa klabu ya Simba, namna pekee ya kumuenzi marehemu ni kufanyia kazi mambo ambayo alikuwa akitushauri kwenye eneo la biashara. Ni matumaini yetu kwamba iwapo tutafanya lile alilokuwa akitushauri, atakuwa mwenye amani huko alikotangulia mbele ya haki."
Aidha, Rage amewaomba wasanii wa tasnia ya filamu na muziki kuwa watulivu na wenye subra kwenye kipindi hiki kigumu kwao akisema kila kitu katika maisha ya wanadamu kinapangwa na Mwenyezi Mungu na ndiyo maana Waswahili wana msemo kuwa Kazi ya Mungu haina makosa.

ALIIBIWA KILA KITU
Watu wasiojulika waliiba kila kitu kutoka kwa msanii huyo baada ya kupata ajali ya gari na kufariki papo hapo.
Wezi hao walimuibia msanii huyo vitu vyote na kumbakisha na pensi ya ndani ambayo alikutwa nayo na polisi katika sehemu ya tukio akiwa tayari ameshakufa.
Ripoti zinasema kuwa baada ya kufa, vibaka wa eneo hilo la kijiji cha Maguzoni walimuibia viatu, mkufu, nguo, fedha.
Wakizungumza na NIPASHE mashuhuda katika eneo la tukio walisema kuwa walisikia kishindo kikubwa cha gari hiyo kuanguka kabla ya vijana ambao hawakutambulika kulivamia na kuanza kupora bila ya kutoa msaada kwa msanii huyo hadi watu walipojaa na kusaidia.
Hii ni ajali ya pili kwa Sharo kupata mwaka huu baada ya Januari 5 kunusurika katika ajali ya basi alilokuwa amepanda likitokea Burundi kuelekea Dar es Salaam kupinduka katika eneo Mikese, Morogoro saa 2:30 asubuhi.
Sharo ambaye alikuwa amekaa kwenye siti ya mbele kabisa alipoteza simu tu katika ajali hiyo ambayo ilijeruhi abiria wengine vibaya.
Kifo cha Sharo kinafuatia vifo vya wasanii wengine wawili wa filamu nchini ndani ya wiki moja, Mlopelo aliyetamba na kundi la Kaole na John Maganga aliyetamba na filamu ya 'Mrembo Kikojozi' aliyocheza na Aunt Ezekiel. John Maganga alizikwa jana mchana kwenye makaburi ya Kinondoni. Vifo hivyo pia vinakumbushia msiba wa Steven Kanumba, ambaye pia alifariki ghafla mwaka huu pia katika kilichodaiwa kuwa ni ugomvi wa kimapenzi.
Sharo atakumbukwa kwa ubunifu wake katika uigizaji akitoka kama mchekeshaji msafi tofauti na wachekeshaji wengi waliomtangulia ambao waliamini vichekesho ni lazima kuvaa kama katuni, kujaza nguo tumboni ili kuonekana na matumbo makubwa ama kujipaka masizi.
Akipendeza kwa mavazi nadhifu, Sharo Milionea alipata umaarufu kwa msemo wake wa "kamata mwizi meeen" na "Ooooh mamma!" huku akijipangusa mabega katika pozi za 'kibrazameni'.
Katika siku za karibuni amekuwa akitawala vioo vya televisheni kutokana na kushiriki tangazo la kampuni ya huduma za simu ya Airtel akiwa na mchekeshaji mkongwe King Majuto, ambapo msemo wake mwingine wa "umebugi meen!" umetawala hasa midomoni mwa watoto.
Meneja Uhusiano wa Airtel, Jackson Mbando, alisema jana kuwa wameshtushwa na kusikitishwa na kifo cha ghafla cha Sharo ambaye waliingia naye mkataba hivi karibuni ili kutangaza huduma za kampuni hiyo.
"Tunaungana na familia, ndugu na jamaa na wadau wa burudani kutokana na kifo cha Sharomilionea. Alikuwa ni kijana mdogo, mchangamfu na aliyekitumia vema kipaji chake cha sanaa na tulikuwa bado tunamtegemea," alisema Mbando.
Wasanii wengine waliowahi kufanya kazi na msanii huyo walisema kuwa wanashindwa kuamini kama amefariki.
Mchekeshaji mwenzake maarufu kwa jina la Kitale alisema siku tatu zilizopita alipigiwa simu na Sharo akimtaka aende nyumbani kwake.
"Nilipofika akaniambia hii ni 'suprise' huku akinionyesha ufunguo wa gari, aliniambia amenunua gari mpya na akanipa Sh.200,000 huku akiniambia kwamba kuna 'dili' ameniunganishia ya kwenda naye nje ya nchi kufanya kazi ya sanaa," alisema Kitale.
Muigizaji Masai Nyota Mbofu alisema itamchukua muda mrefu kumsahau Sharo aliyetamba naye kwenye filamu na kipindi cha 'Vituko Show' wakati wakiwa katika kampuni ya Al Riyamy.
Naye mtayarishaji wa filamu nchini Mustafa Wazir 'West' alisema atamkumbuka daima kwa kipaji Sharo wakati mchekeshaji mwingine aliyekuwa akiigiza na Sharo, Ally Boffu 'Man Bizo', alisema hadi sasa haamini kama amefariki.

VIPAJI TELE
Sharo alikuwa ni msanii mwenye vipaji vingi na aliyejitambulisha pia kama "bonge la rapa" na muimbaji wa Bongofleva.
Baada ya kukosa mafanikio kwa nyimbo zake za awali za awali kabisa za 'Nahesabu Namba' na 'Tusigombane', Sharo ambaye alianza sanaa ya kikazi kipya tangu mwaka 2004, alirekodi nyimbo nyingine za 'Tembea Kisharobaro', aliurekodi katika studio ya Andrew Music ya jijini Tanga na 'Sondela' alioupika katika studio ya Ally's Records ya Tanga pia.
Aliiambia NIPASHE katika mahojiano enzi za uhai wake kwamba pamoja na kumudu miondoko mbalimbali ya muziki kama kwaito, hip hop, na kadhalika, aliamua kugeukia kuimba.
"Nimeamua niimbe kwa sababu naona wengi wananikubali zaidi ninapoimba," alisema msanii huyo ambaye aliliacha jina la Sharobaro na kuhamia Sharomilionea.

CHANZO CHA SHARO-MILIONEA
Wakati akianza sanaa yake ya ucheshi, msanii huyu alijiita Sharobaro, jina ambalo pia ni la studio ya kurekodi muziki inayomilikiwa na msanii na mtayarishaji wa muziki, Bob Junior, aliyemtoa msanii Diamond Platinumz.
Lakini baada ya kilichoripotiwa kuwa ni bifu baina yake na Bob Junior, msanii huyo aliliacha jina la "Sharobaro" na kuanza kujiita "Sharo Milionea".
"Sina ugomvi na Bob Junior, ila watu wa pembeni ndio waliokuwa wakiongea vibaya kutaka kutugombanisha, ndio maana nikamweleza kwamba ni vyema nibadili jina, ndo nikaanza kutumia Sharomilionea, lakini hatuna ugomvi," alisema Mkieti katika mahojiano na NIPASHE wakati wa uhai wake.
Alitamba katika filamu kadhaa za ucheshi ikiwamo ya 'Sharobaro' na 'Mtoto wa Mama', ambamo alitoa msemo wake uliompa umaarufu mkubwa wa "kamata mwizi meeen" pale alipoibiwa simu na kibaka, ambapo badala ya kumkimbiza alionyesha kwamba yeye "brazameni" hawezi kukimbiza mwizi hiyo akiwataka wengine wamsaidie huku akitoa msemo huo.
Baadaye alitamba katika filamu ya kampeni ya kupambana na malaria ya 'Chumo' akiigiza pamoja na Yusuph Mlela na Jokate Mwegelo ambayo ilikuja baada ya filamu yake nyingine ya ucheshi ya 'Back From New York', ambamo aliigiza kama kijana aliyerejea kutoka Marekani na kujumuika na baba yake (wa maigizo) King Majuto, ambaye naye akamgeuza kuwa 'mzee Sharobaro' anayevaa 'kibrazameni' na anayetemba huku akidunda kama vijana wa mjini.
Sharo Milionea enzi za uhai wake akiwa kapigilia kanzu
Hussein Mkiety 'Sharomilionea', alizaliwa Machi 20, 1987 Muheza, akiwa mtoto wa mwisho kati ya watoto watatu na amefariki akiwa mbioni kufyatua video za nyimbo zake mbili zilizokamilika hivi karibuni za 'Vululuvululu' alioimba na Tundaman na 'Changanya Changanya' alioimba na Ally Kiba.

PICHA ZA GARI ALILOPATA NALO AJALI SHARO MILIONEA NA WANANCHI NJE YA CHUMBA CHA MAITI



Gari aina ya Toyota Harrier lenye namba za usajili T 478 BVR alilokuwa akiendesha msanii wa filamu na muziki Hussein Ramadhani Mkieti ‘Sharo Millionea’ kutoka jijini Dar es salaam kuelekea Kijijini kwao Lusanga Wilaya ya Muheza  mkoa wa Tanga. Sharo Millionea alikufa papo hapo na mwili wake kuhifadhiwa Hospitali ya Teule Muheza Tanga.

Baadhi ya watu wakiliangalia gari aina ya Toyota Harrier lenye namba za usajili T 478 BVR alilokuwa akiendesha msanii wa filamu na muziki Hussein Ramadhani Mkieti ‘Sharo Millionea’ kutoka jijini Dar es salaam kuelekea Kijijini kwao Lusanga Wilaya ya Muheza  mkoa wa Tanga. Sharo Millionea alikufa papo hapo na mwili wake kuhifadhiwa Hospitali ya Teule Muheza Tanga.

Gari aina ya Toyota Harrier lenye namba za usajili T 478 BVR alilokuwa akiendesha msanii wa filamu na muziki Hussein Ramadhani Mkieti ‘Sharo Millionea’ kutoka jijini Dar es salaam kuelekea Kijijini kwao Lusanga Wilaya ya Muheza  mkoa wa Tanga. Sharo Millionea alikufa papo hapo na mwili wake kuhifadhiwa Hospitali ya Teule Muheza Tanga.

Mbunge wa Jimbo la Muheza Hebert Mtangi akiwasili nje ya jengo la Chumba cha Kuhifadhia Maiti cha Hospitali ya Teule Muheza kwa ajili ya kushuhudia mwili wa msaniii Sharo Millionea aliyekufa katika ajali ya gari wakati akitoka Dar es Salaam kwenda Lusanga, Muheza mkoani Tanga, ajali hiyo imetokea katika kijiji cha Kijiji cha Songa Kibaoni jana usiku.

Wakazi wa wilaya ya Muheza na maeneo mengine wakiwa wamefurika nje ya Chumba cha Maiti cha Hospitali Teule Muheza, kusubiri kushuhudia mwili wa Sharo Millionea, aliyefariki kwa ajali ya gari usiku wa jana. (Picha Zote na Ahmed Khatib, Tanga).

Sharo Milionea enzi za uhai wake. Anatarajiwa kuzikwa leo kwao

Chanzo:Francis Dande

Tuesday, November 27, 2012

Sharo Milione: Nyota iliyozimika ghafla ikielekea kilele cha mafanikio

NAMNA ya uigizaji wake katika hali ya kitanashati na mikogo ya kipekee inayoendana  na lugha ya kisharobaro, imemfanya msanii Husseni Ramadhani Mkiety kulipoteza jina lake halisi.
Ilikuwa vigumu kumsaka msanii huyo kwa jina lake halisi na kumpata kirahisi tofauti na kama ungemtafuta kwa jina la Sharoi Milionea.
Msani huu alibadilisha jina lake la awali na Sharobaro na kuwa Sharo Milionea baada ya kuingia mzozo na msanii mwenzake, Bob Junior na kuhofua wasikosane aliamua kutumia jina hilo jipya lililomnganda kuliko maelezo.
Nakumbuka katika mahojiano baina yetu mwishoni mwa mwaka juzi, alisema alipenda kuigiza alivyoigiza kama brazameni, ili kujitofautisha na wasanii wengine nchini akiiga staili ya msanii aliyekuwa akimhusudu mno, Will Smith.
Sharo Milionea, aliyekuwa mahiri kwa kuigiza filamu na uimbaji wa muziki wa kizazi kipya, alikiri kwamba karibu kila jambo katika sanaa yake, ina chembe cha nyota huyo wa Kimarekani anayetamba kwenye muziki na filamu ulimwenguni.
Pia, alidai ndoto yake ni kuona siku moja anakuja kuwa kama msanii huyo, mbali na kuanzisha biashara binafsi za kumuingizia pato la kutosha litakalomsaidia maishani mwake.
"Sio siri mambo mengi nayaiga kwa Smith. Nampenda mno huyu mtu, natamani siku moja niwe kama yeye," aliniambia katika mahojiano hayo yaliyofanyika eneo la Magomeni Mikumi.
Mkali huyo aliyewahi kutamba na nyimbo kama 'Nahesabu Namba','Tusigombane', 'Chuki Bure', 'Hawataki', 'Sondela', 'Tembea Kisharobaro' na aliyekuwa mbioni kuachia kazi nyingine za 'Vululuvululu' na 'Changanyachanganya', hatunaye tena.
Msanii huyo amefariki usiku wa kuamkia jana katika ajali ya gari wakati akielekea mjini Muheza, mji aliozaliwa miaka 25 iliyopita.
Sharo, ambaye nilizungumza naye mara ya mwisho jioni ya siku ya Ijumaa na kunieleza mipango yake ya kufyatua video za nyimbo hizo mbili mpya alizoimba na Ally Kiba na Tundaman, aliwahi kudai pamoja na kipaji cha kuzaliwa, lakini kukunwa na Smith na King Majuto kumemfanya afike hapo alipokuwa amefikia.
"King Majuto niliyeigiza nae filamu kadhaa ikiwemo  'Back to New York' na Smith ni kati ya waliochangia mie kuingia kwenye sanaa, navutiwa nao kwa kila wanalofanya," alisema.
Sharo Milionea, alinidokeza kuwa yeye alizaliwa katika kijiji cha Lusanga, kilichopo Muheza mkoani Tanga, Machi 20, 1987 akiwa mtoto wa mwisho wa familia yenye watoto watatu, alisema licha ya mafanikio aliyokuwa nayo tangu atumbukie kwenye fani akisoma Shule ya Msingi Luisanga na baadae Sekondari Kabuta, alikuwa hajaridhika.
Mkali huyo alianza kung'ara kupitia kundi la Chanya na Hasi kabla ya kutua Dar na kuungana na wasanii wenzake katika kundi la Jamaa Arts lililoongozwa na mtayarishaji Gumbo Kihorota alipokuwa na Mac Regan, Masanja Mkandamizaji, Snura na wengine.
Filamu ya kwanza kuigiza ilikuwa ni Itunyama na baadae Zindua akiwa na kundi hilo kuangukia Jumba Arts lililoundwa na wasanii waliojiengua Fukuto Arts Professional wanaotamba na filamu ya Elikanza.
Kazi yake ya kwanza ya vichekesho kwake ni 'Mbwembwe', iliyofuatiwa na 'Vichwa Vitatu', 'Sharobaro', iliyokuwa kazi yake binafsi, pia amecheza 'Nazi Koroma', 'Kuku wa Kichina', 'Muuza Sura', 'Sharo Milionea'.
Mwaka 2009 alitua kundi la Bongo Super Stars Comedy chini ya kampuni ya Al Riyamy Production ambapo walifyatua filamu ya 'Sharo Milionea', 'Mtoto wa Mama' alipoibuka na maneno ya 'Kamata Mwizi Meeen' na kabla ya kufuatiwa na kazi nyingine kadhaa ikiwemo Back From New York'.
Hata hivyo mapema mwaka huu alinidokeza kwa simu kuwa alikuwa amejiondoa Al Riyamy na kufanya kazi chini ya usimamizi wa meneja Ustaadh Juma Namusoma.
Mwenyewe alikiri kwamba sanaa ilimmsaidia mengi ikiwemo kiuchumi na kufahamika, licha ya kutopenda mengi yaanikwe gazetini kwa madai ni mambo yake binafsi.
"Sanaa imenisaidia mambo mengi, ila sipendi kuyaanika gazetini," nilimnukuu.
Msanii huyo aliyekuwa akipenda kula hasa vyakula vinono kuliko kitu kingine maishani mwake na kunywa juisi ya Parachichi, alisema angekutana na Rais angemuomba asaidia kuinua uchumi na kuboresha huduma za kijamii ili kila Mtanzania aifurahie nchi yake.
"Pia ningemuomba asaidie fani za michezo na sanaa, ziwe na nguvu ya kulikomboa taifa hususan katika tatizo la ajira," alisema.
Ila , alidai kaka yeye angekuwa ni Rais, angetoa kipaumbele katika huduma za kijamii hasa elimu na afya, pia angepigania sanaa na michezo ziwe sehemu ya nguzo za uchumi nchini.
Sharo Milionea aliyetaja tukio la furaha ni siku alipofahamishwa kwamba kazi zake zinaonwa nje na kuwavutia wengi kiasi cha vijana wanazoziangalia kumuiga, alisema ili kutimiza ndoto za kung'ara kimataifa amekuwa akigeuka kuwa 'Kinyonga'.
"Ukinyonga wangu kuigiza vichekesho, filamu 'seriuos' na muziki," alisema.
Sharo Milionea, alikuwa shabiki wa klabu ya Real Madrid, ingawa alinidokeza hakuwa anamjua hata moja la nyota wa kikosi hicho, huku akidai katika matukio ya huzuni kwake ni kifo cha babu yake aliyekuwa mlezi baada ya kumlea tangu baba yake afe akiwa kinda.
"Alikuwa mlezi na muongozo wangu kimaisha, alinipenda na nilimpenda mno." aliniambia kwa huzuni
Mkali huyo aliyetamba na filamu ya 'Chumo' aliyoigiza na Yusuph Mlela na Jokate Mwegelo, alikuwa hajaoa wala kuwa na mtoto, ingawa alikuwa na mchumba aliyekuwa akidai angemuoa muda muafaka ungefika..
Sharo Milionea aliyekunwa na Joti na Kanumba kwa hapa nchini, alisema kama msanii nyota amekuwa akipata usumbufu toka kwa wanawake wanaomtaka kimapenzi, ila alidai hutumia busara kuwaepa akitambua kuwa sio wote wanampenda, pia kuwepo Ukimwi.
"Hili la Ukimwi, kila mtu analitambua, ni wajibu wa kila mtu ndani ya jamii kuepukana nao, ili kutimiza ndoto za maisha yao, kama ninavyofanya mimi," alisema.
Kuhusu wasanii nyota kujitumbukiza kwenye skondo na matendo maovu, Sharo Milionea, alisema ni vigumu kuwazuia wanaofanya, ila aliwataka watambue kuwa wao ni vioo vya jamii na wenye familia nyuma zao, hivyo wajiheshimu na wajithamini kusudi nao wathaminiwe na jamii.
"Kama mtu hajiheshimu au kujithamini ni vigumu kuheshimiwa na jamii, kitu hicho ndicho kinachochangia fani yetu kuonekana ya kihuni wakati sivyo ilivyo," alisema.
Wakati mauti yanamkumba msanii huyo alikuwa ametoka kuingia mkataba wa kutangaza huduma za simu za mkononi za Airtel na kuuza sura katika matangazo ya bidhaa za kampuni za Bakhresa hasa soda za Azam akishirikiana na King Majuto.
Sharo atakumbukwa daima kwa ucheshi wake na kujichanganya na watu licha ya umaarufu alionao, hakuwahi kunata au kujiona kama baadhi ya watu wa kariba yake.
Kifo cha Shario Milionea kimekuja wakati wadau wa sanaa wakiendelea kuomboleza vifo wa wakali wengine waliofariki hivi karibuni, kuanzia Steven Kanumba, Mlopelo, Mariam Khamis, John Maganga.
Kwa hakika tuliwapenda wenzetu, lakini Mwenyezi Mungu aliwapenda zaidi. Jina la Allah Lihimidiwe kwani kazi yake haina makosa.

Wasanii, Airtel wamlilia Sharo Milionea

Meneja Uhusiano wa kampuni ya Airtel, Jackson Mbando

Sharo Milionea enzi za uhai wake
KAMPUNI ya simu za mkononi ya Airtel imeungana na watanzania wengine kumlilia msanii nyota wa filamu na mwanamuziki wa kizazi kipya, Husseni Ramadhani Mkiety 'Sharo Milionea' aliyefariki usiku wa kuamkia jana kwa ajali ya gari.
Meneja Uhusiano wa Airtel, Jackson Mbando, alisema wameshtushwa na kusikitishwa na kifo cha ghafla cha Sharo Milionea ambaye waliingia naye mkataba hivi karibuni ili kutangaza huduma za kampuni hiyo.
Alizungumza asubuhi hii na kituo cha Cloud FM, Mbando alisema kifo cha Sharo Milionea, kimewatia simanzi kutokana na ukweli kimekuja ghafla mno na huku akiwa bado anahitajika katika kuitangaza kampuni yao.
"Tunaungana na familia, ndugu na jamaa na wadau wote wa burudani kutokana na kifo cha Sharo Milionea, alikuwa kijana mdogo, mchangamfu na aliyekitumia vema kipaji chake cha sanaa, Airtel tumeguswa na msiba huu kwani tulikuwa bado tunamtegemea kutangaza huduma zetu," alisema Mbando.
Wasanii wengine waliowahi kufanya kazi na msanii huiyo aliyefariki jana saa mbili usiku baada ya gari alilokuwa akiliendesha kwenda kwao Muheza Tanga, kupinduka na kusababisha kifo chake wamedai wanashindwa kuamini kama amefariki.
Masai Nyota Mbofu, amedai itamchukua muda mrefu kumsahau Sharo aliyewahi kutamba naye keenye filamu na kipindi cha 'Vituko Show' wakati kampuni ya Al Riyamy.
Naye mtayarishaji wa filamu nchini Mustafa Wazir 'West' alisema atamkumbuka daima Sharo Milionea kwa kipaji alichokuwa nacho.
Mchekeshaji mwingine aliyekuwa akiigiza na Sharo, Ally Boffu 'Man Bizo', alidai mpaka sasa haamini kama Sharo Milionea amemtoka kwa jinsi ilivyokuwa ghafla.
Kifo cha Sharo Milione kimekuja huku wadau wa sanaa wakiendelea kuwaomboleza muimbaji wa TOT-Taarab Mariam Khamis 'Paka Mapepe' aliyefariki wiki mbili zilizopita na waigizaji Mlopero na John Maganga waliokufa wiki iliyopita.
Hussein Mkiety 'Sharo Milionea, aliyezaliwa Machi 20, 1987 Muheza, akiwa mtoto wa mwisho kati ya watoto watatu na amefariki akiwa mbioni kufyatua video za nyimbo zake mbili zilizokamilika hivi karibuni za 'Vululuvululu' alioimba na Tundaman na 'Changanya Changanya' alioimba na Ally Kiba.
Taarifa tulizozipata hivi tunde zinasema kwamba huenda marehemu Sharo Milionea akazikwa leo mjini Muheza, Tanga ingawa tunaendelea kufuatilia taarifa zaidi juu ya msiba huo.

Mashindano ya ngumi yaota mbawa mpaka mwakani

MASHINDANO ya ngumi za ridhaa ya klabu bingwa ya taifa yaliyopangwa kuanza kufanyika jana Novemba 26 hadi Novemba -30 mwaka huu yamesogezwa mbele hadi Januari 29 hadi Februari 3 mwakani.
Katiku Mkuu wa Shirikisho la Ngumi za Ridhaa nchini (BFT), Makore Mashaga alisema juzi kuwa, wamelazimika kusogeza mbele mashindano hayo hadi mwakani kutokana na sababu mbalimbali.
Alizitaja baadhi ya sababu hizo kuwa ni pamoja na timu shiriki kushindwa kukamilisha taratibu, ikiwa ni pamoja na kutothibitisha ushiriki wake katika tarehe iliyopangwa.
Kwa mujibu wa Mashaga, sababu zingine ni timu shiriki kushindwa kuwasilisha majina na picha za mabondia wake pamoja na kulipa ada ya ushiriki ya sh. 200,000.
"Hadi leo hakuna hata timu moja iliyokamilisha utaratibu huo kwa nia ya kupanga mashindano vizuri ili yawe na hadhi ya taifa kwa kuzingatia sheria za Chama cha Ngumi za Ridhaa cha Dunia (AIBA)," alisema.
"Sababu kama hizi mara nyingi zimesababisha mashindano mengi kuendeshwa kwa kiwango cha chini na lawama nyingi kuelekezwa kwa BFT bila ya kufahamu sababu za msingi," aliongeza.
Mashaga alisema pia kuwa, kozi ya waamuzi iliyopangwa kuanza Novemba 11-30 mwaka huu ilishindwa kufanyika kutokana na washiriki kushindwa kukamilisha taratibu za ushiriki ikiwa ni pamoja na kulipa ada kwa wakati.
Kutokana na BFT kuwa na majukumu mengine, Mashaga alisema kozi hiyo sasa imepangwa kufanyika Januari 15 hadi Februari 4 mwakani na mazoezi ya vitendo yatafanyika wakati wa mashindano ya klabu bingwa.
Mashaga alisema kwa sasa, BFT imeweka nguvu kubwa katika usajili wa makocha, waamuzi, mabondia na madaktari ili waweze kutambulika kwa ajili ya kujiunga na mashirikisho ya ngumi za kulipwa.

Uncle D kuziba pengo la Uncle JJ Bongo Movie?

Uncle JJ (kushoto) na Uncle D anayejaribu kuvaa viatu vyake
Uncle D

BADO mashabiki wa filamu nchini wanaendelea kuumizwa na kifo cha aliyekuwa nyota wa fani hiyo, Steven Kanumba 'Uncle JJ' ama lile maarufu la 'The Great Pioneer' aliyefariki ghafla Aprili mwaka huu.
Tangu alipofariki dunia, mashabiki wake wamekuwa wakisikilizia na kutaka kuona nani atakayeweza kuvaa viatu vya mkali huyo aliyekuwa na kiu kubwa ya maendeleo katika fani yake tangu alipokuwa Kaole Sanaa.
Wengi wamekuwa wakijiuliza ni msanii gani atakayeweza kuwaburudisha kwa kiwango alichokuwa akikifanya Kanumba hasa kupitia filamu zake mchanganyiko zikiwemo za kiutu uzima, watoto, kidini na masuala mengi ya kijamii.
Japo wapo wasanii kibao waliowahi kufanya kazi pamoja na Kanumba wamekuwa wakiaminiwa huenda wakasimama na kuziba pengo hilo la msanii huyo, hata hivyo hali inaonekana kuwa ngumu.
Hii inatokana na ukweli kwamba marehemu Kanumba, aliiteka mioyo ya mashabiki wengi kiasi imekuwa vigumu kwa mashabiki hao kuruhusu mioyo hiyo kutoa nafasi kwa mtu mwingine kuingia.
Ndio maana hata soko la filamu lilionekana kuyumba tangu Kanumba alipofariki kwa kazi za watu wengine kusahauliwa kwa muda na kukimbiliwa kazi za nyuma za mkali huyo, ingawa kwa sasa hali inaendelea kubadilika kwa watu kuzoea hali halisi iliyotokea.
Hata hivyo, huenda mashabiki wa filamu wakasuuzwa roho zao, baada ya Jacklyne Wolper kuamua kutengeneza filamu mpya iitwayo 'After Death' ambayo imemshirikisha msanii asiye na jina, lakini aliyeshabihiana na marehemu Kanumba.
Msanii huyo si mwingine bali ni Philemon Latwaza ambaye ndani ya filamu hiyo mpya atafahamika kwa jina la 'Uncle D'.
Uncle D, ameigiza na 'watoto wa Kanumba', Jennifer na Patrick, walioibuliwa na filamu za 'Uncle JJ' na 'This is It', sambamba na waigizaji wengine wenye majina waliowahi kucheza pamoja na marehemu Kanumba enzi za uhai wake.
Muongozaji wa filamu hiyo, Leah Richard Mwendamseke 'Lamata' alisema ujio wa Uncle D unaweza kuziba pengo la Kanumba kwa kiasi fulani na pengine kuwarudisha mashabiki wa marehemu huko katika 'sononi' mpya ya kumkumbuka.
Lamata, alisema wamefyatua filamu hiyo kama njia ya kumuenzi Kanumba na pia kuendelezaa juhudi zake za kuibua na kukuza vipaji vya akina Jennier na Patrick.
"Nadhani After Death, itawakumbusha mbali mashabiki wa filamu kwa namna Uncle D alivyomudu kumuigiza Kanumba na hasa kutokana na kufanana naye kwa sura kwa kiasi kikubwa," alisema.
Mbali na Uncle D na watoto Jennifer na Patrick katika filamu hiyo pia wameigiza akina Mainda, Mayasa Mrisho, Ben Blanco, Wolper mwenyewe, Irene Paul, Shamsa Ford na Patcho Mwamba.
Swali la kujiuliza je, Uncle D atamudu kuvaa viatu vya Kanumba kama Lamata anavyodai? Ni suala la kusubiri kuona mara filamu hiyo itakapoachiwa mtaani.


Golden Bush: Klabu ya 'mastaa' wa soka iliyopania makubwa nchini * Yajipanga kuuza wachezaji wao barani Afrika kwanza kabla ya Ulaya


Nembo ya klabu ya Golden Bush






Kocha wa Golden Bush, Shija Katina akiwaelekeza wachezaji wake katika mazoezi ya timu hiyo

Kikosi kamili cha Golden Bush (wa kwanza kulia) ni kocha Shija Katina



KIU kubwa ya kutaka kuinua na kuendeleza vipaji vya soka kwa vijana pamoja na kutoa ajira kwa vijana hao kupitia soka ndiko kulikofanya baadhi ya nyota wa zamani wa soka nchini kuungana na kuanzisha timu yao ya Golden Bush.
Nyota hao wa zamani wakiongozwa na Ally Mayay, Wazir Mahadhi 'Mandieta' , Abuu Ntiro, Said Swedi 'Panucci', Salum Swedi 'Kussi', chini ya makocha Shija Katina na Madaraka Selemani waliungana na kuiasisi timu hiyo mpya.
Wakiwa wamepeana majukumu ndani ya timu hiyo iliyo chini ya muasisi na

mlezi wao, Onesmo Wazir 'Ticotico', kiu yao kubwa ni kuifanya klabu hiyo kuwa ya mfano nchini kutokana na malengo na mikakati waliyoijiwekea.
Moja ya malengo ya timu hiyo inayojiandaa na ushiriki wa Ligi ya TFF wilaya ya Kinondoni ni kuendeleza vipaji na kuwawezesha vijana wenye uwezo wa kucheza soka la kulipwa nje ya nchi wakitimiza ndoto zao.
Uongozi wa timu hiyo yenye maskani yake Sinza, Dar es Salaam japo iliasisiwa

Mabibo, ulisema haitakimbilia kuwapeleka wachezaji wao kucheza soka Ulaya badala yake wataanzia kuwapeleka nchi za barani Afrika kwanza.
Meneja wa timu, Wazir Mahadhi alisema wanaamini kucheza soka la kulipwa

barani Afrika ni njia nzuri ya kuwapa nafasi wachezaji wao kupata uzoefu wa kuhimili mikikimikiki kabla ya kusonga mbele kwenye ushindani zaidi kisoka.
Mahadhi alisema ndiyo maana katika timu yao wamejumuisha wachezaji wa umri wa miaka 17-23 tu, kwa kuamini umri huo ni sahihi kwa wachezaji kupata nafasi ya kucheza soka la kulipwa.
Naye mlezi wa klabu hiyo, Onesmo Wazir 'Ticotico' alisema tayari wameanza mipango ya kujenga uhusiano na klabu kadhaa za barani Afrika ili kurahisisha mipango yao wakianzia na nchi ya Msumbiji.
"Tayari tumeshaanza kutekeleza mikakati yetu, tunatarajia kupeleka wachezaji wetu nchini Msumbiji, tunatarajia miezi sita ijayo tutapanua wigo zaidi katika mahusiano na klabu nyingine za nje," alisema Ticotico.
Ticotico, 'membaz' wa zamani wa Friends of Simba na mjumbe wa zamani wa Kamati ya Fedha na Uchumi ya Simba chini ya uongozi wa akina ismail Rage,

alisema wamepanga miaka miwili ijayo Golden Bush iwe mbali kimaendeleo.
"Tumelenga kuja kuanzisha 'academy' ya soka itakayohusisha vijana wenye umri kati ya miaka 14-17,  pia tuweze kuwalipa wachezaji wetu mishahara tofauti na posho tunazowapa kwa sasa," alisema.

KWA NINI?
Ticotico alisema saababu kuu ya kuasisiwa kwa timu hiyo ilitokana na yeye na wachezaji hao nyota wa zamani kukerwa kuona vipaji vya soka vya vijana vikipotea mitaani bila kutumiwa wala kunufaisha taifa na wachezaji wenyewe.
Japo alikiri wanatambua changamoto kubwa zilizopo mbele yao ili kuifikisha

Golden Bush mahali walikokusudia, bado anaamini timu yao itafika mbali kutokana na walivyojipanga hasa  kuifanya timu yao iwe yenye ushindani.
Ticotico, Mahadhi na kocha Shija Katina walisema kwa nyakati tofauti wakati ilipoanzishwa klabu hiyo ilikuwa kwa ajili ya kushiriki mabonanza, lakini kule kuona vijana wengi wakijitokeza kucheza pamoja nao iliwapa wazo la kuiboresha.
Walisema ilipoanzishwa timu hiyo ilikuwa na wachezaji wasiozidi 20, ila kwa sasa wamesajiliwa 28 kwa ajili ya Ligi ya TFF inayotarajiwa kuanza hivi karibuni.

MATARAJIO
Mbali na kuifanya iwe klabu ya mfano, Mahadhi alidai wanataka kuipandisha timu hiyo daraja sambamba na kutoa ajira kwa vijana kama alivyofafanua mlezi wao juu ya mipango ya kuanzisha 'chuo' na kuuza wachezaji nje ya nchi.
Hata hivyo, Mahadhi wenzake walisema kitu cha muhimu wanachoomba ni kupata sapoti kwa wadau wa soka nchini wakiwamo wafadhili kujitokeza kuwapiga tafu ili kutimiza malengo yao.
"Hatuwezi kufanikiwa kama hatutaungwa mkono na wadau kuanzia watu binafsi hadi makampuni kwa ajili ya udhamini," alisema.
Aliongeza kuwepo kwa wadhamini wa kutosha na sapoti toka kwa wadau wa

soka kutaiwezesha Golden Bush kutimiza ndoto za kuwa klabu ya mfano sawia na kuwapa faraja wachezaji wanaotegemea vipaji vya kuwanufaisha.

NIDHAMU
Katika moja ya vitu ambavyo uongozi na benchi la ufundi la timu hiyo inavyoviangalia ni suala la nidhamu ndani na nje ya uwanja.
Makocha, Shija Katina na Madaraka Seleman 'Mzee wa Kiminyio', walisema suala la nidhamu ndicho kipaumbele cha kuchukuliwa kwa vijana kuichezea timu hiyo na suala hilo linaendelea kuzingatiwa hata sasa timu ikiwa inazidi kuimarika.
Katina, alisema bahati nzuri wachezaji walionao ni waelewa na wenye malengo ya kweli ya kufika mbali kisoka na hivyo wanazingatia nidhamu na kujituma kwa moyo bila kusukumwa.
Alisema nidhamu hiyo ya wachezaji na ushirikiano uliopo baina yao na uongozi mzima wa Golden Bush ndiyo iliyowawezesha katika mechi 15 walizokwishacheza moja sasa kushinda mara saba ikiwamo kuzilaza Mtibwa Sugar, 94 KJ na kuisimamisha Kagera Sugar waliotoka nao sare miongoni mwa sare mbili walizopata.
"Tumecheza mechi 15 tuimeshinda saba na kupoteza sita na sare mbili baadhi ya timu tulizocheza nazo ni za Ligi Kuu na Daraja la Kwanza, na tuliweza kuzisimamisha kwa vile wachezaji wana nidhamu ndani na nje ya dimba hata kwa mechi za kirafiki."

SAFU YAKE
Klabu hiyo ya Golden Bush iliyoasisiwa April mwaka jana kabla ya kupata usajili kamili mwishoni mwa mwaka jana, ina safu kamili ya uongozi ambapo Mwenyekiti wake ni Ally Mayay akisaidiwa na Salum Swedi.
Katibu Mkuu wa klabu hiyo ni Majaliwa Mwaigaga akisaidiwa na Henry Morris, huku Meneja akiwa ni Wazir Mahadhi, na makocha wake ni Shija Katina na Madaraka Seleman.
Mlezi wa timu hiyo ambayo imekuwa ikifanya mazoezi yake kwenye uwanja wa Kinesi Ubungo na wakati mwingine Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni Onesmo Wazir na ikipata sapoti kubwa na nyota wa zamani akina Abuu Ntiro, Yahya Issa, Said Swedi, Shaaban Kisiga na waasisi wengine baadhi wakiendelea kucheza soka ngazi ya ligi kuu na daraja la kwanza.
Add caption

Wolper amkumbuka marehemu Kanumba

Jacklyne Wolper alipoigiza na Kanumba katika filamu ya Ndoa Yangu


NYOTA wa filamu nchini, Jacklyne Wolper, amemkumbuka marehemu Steven Kanumba na kumtungia filamu iitwayo 'After Death' aliyowashirikisha baadhi ya wasanii chipukizi walioibuliwa na Kanumba enzi za uhai wake.
Muongozaji wa filamu hiyo, Leah Richard, aliiambia MICHARAZO kuwa  filamu hiyo ni maalum kwa ajili ya kuenzi mchango wa mkali huyo wa filamu aliyefariki ghafla na kuzikwa Aprili mwaka huu.
Leah alisema filamu hiyo imetungwa na Jacklyne Wolper aliyewahi kucheza na Kanumba filamu mbalimbali ikiwemo 'Ndoa Yangu' na imeongozwa na yeye.
"Imetungwa na Wolper na kuongozwa na mimi mwenyewe na mpaka sasa imekamilika na inasubiriwa kufanyiwa uzinduzi rasmi hapo baadae," alisema Leah.
Mwanadada huyo alisema anaamini filamu hiyo itakapoingia sokoni itawarejeshea kumbukumbu wapenzi wa filamu juu ya Kanumba na watoto wake kwa namna mtu aliyeigiza kama Kanumba kushabihiana naye kwa sura kwa kiasi kikubwa.
"Yaani ni kama Kanumba amerejea upya ulimwengu kupitia 'After Death' kwa namna aliyemuigiza kufanana naye na namna alivyoigiza na watoto hao wa Kanumba," alisema.
Kanumba, aliyekuwa akifahamika kama The Great', aliwaibua watoto wenye vipaji  na kuigiza nao katika filamu kadhaa kama 'Uncle JJ', 'This is It' na 'Big Daddy', alifariki dunia Aprili 6 mwaka huu.

Tutegemee vipaji sio miili yetu-Salha

Salha Abdallah katika pozi


MUIMBAJI wa kundi la taarab la Dar Modern 'Wana wa Jiji', Salha Abdallah, amewataka wasanii wenzake wa kike kujiheshimu, kujiamini na kutumia vipaji vyao kuwakomboa kiuchumi badala ya kuitegemea miili yao kujitajirisha.
Salha anayetamba kwa sasa na kibao alichokitunga na kukiimba cha 'Nauvua Ushoga', alisema msanii anayetegemea kipaji chake, kujiheshimu na kujiamini hawezi kukubali kukudhalilishwa na watu wachache wanaowaozunguka katika fani na ndani ya jamii.
Alisema wasiojiamini na siyo na vipaji vya kweli ndio wamekuwa wepesi kujidhalilisha kwa kuitegemea miili yao kuwapa mafanikio na mwishowe kuachwa wakiwa hawana thamani mbele ya watu waliowachezea na jamii kwa ujumla.
"Lazima niseme ukweli wapo baadhi ya wasanii wenzetu wanaitegemea miili yao kuwainua kisanii na kimaisha, ila hawatambui waavyojishushia hadhi, mwanamke wa kweli ni yule anayejiamini, kujiheshimu na kutegemea kipawa alichojaliwa," alisema.
Alisema kama msanii mrembo amekuwa akikutana na vishawishi vingi toka kwa wanaume wakware, ila amekuwa akiwakwepa kistaarabu huku akifichua wengi wa wanaume wa hivyo huandika namba zao za simu katika fedha wanaozoenda kuwatunza.
Muimbaji, aliyezaliwa pacha na mwenzake, alisema binafsi huwa anakerwa na wasanii wa kike wanaojihusisha na skendo na kukubali kutolewa picha za ovyo magazetini.

Ruvu Shooting wamsubiri Mkwasa



UONGOZI wa klabu ya soka ya Ruvu Shooting ya Pwani, umesema wiki hii utaweka hadharani mikakati yao kwa ajili ya maandalizi ya duru lijalo la Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kupokea taarifa na mapendekezo ya kocha wao.
Afisa Habari wa Ruvu, Masau Bwire aliiambia MICHARAZO kwamba panga pangua ya kikosi chao inatarajiwa kufahamika wiki hii baada ya kumaliza kucheza mechi zao za duru la kwanza kwa kuilaza Prisons-Mbeya mabao 2-0.
Bwire, alisema uongozi unasubiri ripoti ya bnchi lao la ufundi chini ya kocha Charles Boniface Mkwasa, ili kujua wapi pa kuanzia katika maandalizi ya duru hilo walilodai wamelipania ili wamalize msimu katika nafasi nzuri.
"Baada ya kumalizika kwa pambano letu na Prisons tukishukuru kushinda kwa mabao 2-0, kwa sasa tunasubiri taarifa na mapendekezo ya mwalimu wetu kwa ajili ya kujipanga kwa duru lijalo," alisema Bwire.
Bwire, alisema wangependa kuona duru lijalo wakifanya vizuri zaidi na duru lao la kwanza lililowaacha wakiwa nafasi ya saba wakijikusanyia jumla ya pointi 20 kutokana na mechi 13 ilizocheza katika duru hilo.
Afisa Habari huyo, alisema yapo baadhi ya mapungufu yaliyoonekana katika kikosi chao yanayohitajika kurekebishwa, lakini uongozi hauwezi kusema lolote mpaka waipate ripoti ya kocha Charles Boniface.
***

Kipa wa zamani Yanga kwenda Msumbiji


KIPA wa zamani wa timu za Yanga na Moro United, Steven Marashi, anatarajiwa kuondoka nchini mwishoni mwa wiki kwenda nchini Msumbiji kujaribu kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Ligi Kuu nchini humo.
Akizungumza na MICHARAZO, Marashi, aliyeachwa kitatanishi misimu miwili iliyopita pamoja na akina Wisdom Ndhlovu na John Njoroge, alisema mipango ya safari yake inafanya mmoja wa mawakala waliopo nchini Msumbiji aliyewahi kumuona akicheza.
Marashi, alisema japo jina la timu anayoenda kufanyiwa majaribio haikumbuki kwa jina, lakini amedai ni ya Ligi Kuu ya Msumbiji na imani yake ni kufanya vema.
"Kaka nipo katika maandalizi ya safari ya kwenda Msumbiji kwa ajili ya kujaribu kucheza soka la kulipwa baada ya kupatiwa na nafasi na mmoja wa mawakala wa nchini humo aliyevutiwa nami wakati nikiwa Moro United," alisema.
Kipa huyo ambaye aliamua kujiengua Moro United mara baada ya kushuka daraja toka Ligi Kuu Tanzania Bara msimu uliopita, alisema kama mambo yataenda yalivyopangwa basi ataondoka nchini Jumamosi au Jumapili.

ZANZIBAR WAANZA NA SARE CHALLENJI - NIYONZIMA AKIING'ARISHA RWANDA

Beki wa timu ya Zanzibar Heroes, Said Chollo akimiliki mpira wakati wa
mchezo dhidi ya timu ya Eritrea wakati wa michuano ya Cecafa Challenge
2012 uliochezwa katika Uwanja wa Mandela nchini Uganda

Wachezaji wa timu za Zanzibar na Eritrea wakiwania mpira wakati wa
mchezo dhidi ya timu ya Eritrea wakati wa michuano ya Cecafa Challenge
2012 uliochezwa katika Uwanja wa Mandela nchini Uganda.



Haruna Niyonzima akishangilia goli lake aliloifungia Rwanda dhidi ya Malawi na kufanya matokeo kuwa 2-0 mpaka kipenga cha mwisho kilipopulizwa - kufuatia goli la kwanza lilofungwa na Jean Baptiste Muginereza katika dakika ya 38 ya kipindi cha kwanza.   

SHARO MILIONEA ATUNAYE TENA!



MCHEKESHAJI mahiri ambaye pia ni msanii wa muziki wa kizazi kipya nchini, Hussein Mkiety ‘Sharo Milionea’amefariki papo hapo usiku wa kuamkia leo baada ya kupatwa ajali akielekea nyumbani kwao Muheza, mkoani Tanga.

.

Hussein Mkiety
Msanii Husseni Mkiety 'Sharo Milionea'  enzi za uhai wake

Taarifa za awali ambazo MICHARAZO ilizipata jana usiku zilisema kuwa, marehemu alifariki wakati gari alililokuwa akiendeza kupinduka mara kadhaa na kumsababishiaa kifo chake ikiwa ni siku tatu tangu alipozungumza na mwandishi wa habari hizi akielezea mipango ya kupakua avideo zake mbili za nyimbo za 'Vululuvululu' na 'Changanya Changanya' alizoimba na Tundaman na Ally Kiba.
Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Tanga, Constantine Massawe alinukuliwa na kituo kimoja cha redio na kuthibutisha taariofa za kifo cha msanii huyo machachari.
“Leo majira ya saa mbili usiku kwenye barabara ya Segera Muheza Tanga mtu mmoja aliyetambulika kwa jina la Hussein Ramadhani au Sharo Milionea akiwa anaendesha gari namba T478 BVR Toyota Harrier akitokea Dar es salaam kwenda Muheza alipofika eneo hilo gari lake liliacha njia na kupinduka mara kadhaa na kusababisha kifo chake.
Mwili wa marehemu umehifadhiwa kwenye hospitali Teule ya wilaya ya Muheza” Kamanda amesema hakuna kona kali sana wala ubovu wa barabara kwenye sehemu aliyopata ajali Sharo Milionea, katikati ya Segera na Muheza ambapo gari imehifadhiwa mahali salama kwa sababu haitembei.
Taarifa hii imetolewa na Kamanda wa Polisi Mkoa Tanga Constantine Massawe,
Hadi mauti inamkuta alikuwa ni mwanamuziki wa muziki wa kizazi kipya wimbo wake wa Chuki Bure alioimba na Dully Sykes mbali na kibao chake cha 'Hawataki'.
taarifa zaidi kuhusu taratibu za mazishi tutaendelea kuwajulisha
ingawa inaelezwa msiba wake upo nyumbani kwao Muheza Tanga.
MICHARAZO inawapa pole  familia, ndugu, jamii na rafiki wote wa  msanii huyo Mungu aipokee Roho ya