STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, July 19, 2013

Deo Lyatto atoa Shukrani kwa wadau wa soka nchini

Deo Lyatto, alipokuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF
HAPO chini ni Maelezo ya Shurani ya Mwenyekiti Aliyemaliza muda wake wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Deo Lyatto kwa wadau wa soka nchini.

1. Kama wote tunavyofahamu jana uongozi wangu wa Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ulifikia tamati kama mlivyotangaziwa na Rais wa TFF. Kwa heshima kubwa naomba kutumia fursa hii kuwashukuru viongozi na wadau wa soka kwa ushirikiano mkubwa nilioupata kutoka kwao wakati nikitekeleza majukumu mbalimbali ya TFF.

2.  Kwa kushirikiana na viongozi wa mpira wa miguu katika TFF na mikoa yote Tanzania Bara, pamoja na wadau wa soka, nimepata fursa kulitumikia soka la nchi yetu kwa nafasi mbalimbali. Kwa pamoja tumetekeleza majukumu ya ujenzi wa misingi ya uongozi bora katika TFF na wanachama wake.

3.  Naishukuru Kamati ya Utendaji ya TFF:

(i)kwa kuniteua kuwa mjumbe wa Kamati ya Nidhamu ya TFF, (Jan 2005 - Jan 2007). Nawashukuru pia wajumbe wa Kamati hiyo chini ya Mhe. Said El-Maamry kwa kunichagua kuwa Katibu wa Kamati hiyo. Ushirikiano mlionipatia ulioniwezesha kulitumikia taifa katika soka na kwa pamoja kurejesha nidhamu kwa kiwango kikubwa.

(ii)kwa kuniteua kuwa mjumbe wa Kamati Maalumu, iliyochunguza mkasa wa timu yetu ya Taifa ya wachezaji wa umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) mwezi Juni 2005. Nawashukuru wajumbe wa kamati  hiyo chini ya Dr. Hamad Ndee Mkuu wa Idara ya Michezo ya Chuo kikuu cha Dar es salaam, kwa kunichagua kuwa Katibu wa kamati hiyo iliyoandaa taratibu za mashindano ya vijana  ambazo ni msingi  wa mashindano ya vijana wa umri chini ya miaka 17  hapa nchini.

(iii)kwa kuniteua kuwa Mjumbe wa Kamati Maalumu iliyotayarisha Programu ya kuendeleza Timu ya Taifa kwa kipindi cha miezi 15 (April 2006 hadi Juni 2007). Progamu iliyochangia Tanzania kiinua kiwango cha ubora wa soka kutoka nafasi ya 165 duniani mwezi Februari 2006 hadi nafasi ya 89 mwezi Desemba 2007.

(iv)kwa kunipa fursa ya kuwa mjumbe wa Kamati Maalumu ya kuboresha mapato ya TFF mwaka 2009. Nikiwa mjumbe na Katibu wa Kamati hiyo nilipata ushurikiano mkubwa kutoka kwa wadau wa soka nchini  na nje ya nchi.  Nina imani kuwa TFF itakamilisha utekelezaji wa mapendekezo ya Kamati na ya wadau wa soka ikiwa ni pamoja na kuanza kutumia tiketi za elektroniki.

(v)kwa kuniteua kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF  kwa  vipindi viwili; Februari 2009 - Machi 2011 na kuniteua tena kuiongoza Kamati hiyo kwa kipindi cha pili Machi 2011 hadi jana tarehe 18 Julai 2013. Naishukuru Kamati ya Utendaji ya TFF kwa imani kubwa iliyoonyesha kwangu na wanakamati wenzangu.
4.  Nawashukuru wajumbe wote wa wa Mkutano Mkuu wa TFF, kwa ushirikiano mkubwa mliotoa kwangu na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kushiriki kwa amani na utulivu na kuzingatia Katiba za vyama vyenu, Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi na hivyo kufanikisha zoezi la chaguzi za viongozi katika wilaya zote na Mikoa yote ya Tanzania Bara na hivyo kuwezesha kuwa na wajumbe wa Mkutano Mkuu, ambao  katika kikao chake cha kwanza baada ya chaguzi hizo kimefanya jambo la kihistoria kuweka nguzo za  Mwenendo, Maadili  na Miiko ya uongozi wa soka la nchi yetu. Nilifarijika kuwa sehemu ya Mkutano Mkuu huo nikiwa mwalikwa.

5. Nawashukuru viongozi na wafanyakazi wote wa Sekretarieti ya TFF, wajumbe wa Kamati zote za TFF, Wajumbe wa Kamati zote za Uchaguzi za wanachama wa TFF na wanachama wao, kwa ushirikiano mkubwa na wa dhati uliowezesha kuwatumikia wadau wa soka kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa.

6. Nawashukuru sana wajumbe wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa ushirikiano niliopata kutoka kwao kwa muda tuliofanya kazi pamoja. Si jambo rahisi kusimamia chaguzi za mikoa yote na klabu zenye wanachama za Ligi Kuu, hata hivyo kwa kushirikiana na wadau mbalimali wa soka ambao nachukua fursa hii kuwashukuru, kwa pamoja tumeweza kutimiza jukumu hilo kikamilifu.  

7. Nawashukuru sana Waandishi na Wahariri wa habari za michezo na pia Wahariri Watendaji wa vyombo vya habari, kwa ushirikiano mzuri nanyi, ushirikiano na uhusiano wa uwazi ambao haukuwa na mikwaruzo ya aina yoyote kwa kipindi chote (Jan 2005-Jul 2013) tulichoshirikiana kwa pamoja kulitumikia soka la nchi yetu.

8. Namshukuru sana Rais wa TFF Ndg. Leodegar Tenga kwa imani kubwa aliyonayo kwangu na kwa wanakamati niliokuwa nao katika kutekeleza majukumu ya umma. Miaka ishirini na tisa (29) iliyopita nilipata fursa ya kufanya kazi ya mpira miguu kwa mara ya kwanza na Ndg. Tenga, nikiwa nahodha wa Timu ya Mpira wa Miguu ya Chuo kikuu cha Dar es salaam, Desemba 1984, wakati Ndg. Tenga alipojitolea kuifundisha timu ya Chuo Kikuu cha DSM. Tangu wakati huo hadi sasa imani  na  ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya umma niliopata kutoka kwa Ndg. Tenga haujawai kutetereka hata kwa siku moja. Ni faraja kubwa kwangu kufanya kazi hizi za umma chini ya kiongozi anayeheshimika na kuaminika na wadau wa soka hapa nchini, Afrika Mashariki na Kati, Afrika na familia ya soka Duniani kwa ujumla.

9. Mwisho, kwa viongozi na wadau wote wa mpira wa miguu, nawashukuru na nawatakia kheri, baraka  na mafanikio katika Uchaguzi Mkuu wa TFF na  ujenzi wa  soka la nchi yetu..

Asanteni.
 
Deogratias J. Lyatto
19 Julai 2013, Dar es salaam, Tanzania.

Yanga wamegeuzia kibao Kiiza, kisa...!

Na Dina Ismail
BAADA ya kuipiga danadana kwa muda mrefu, hatimaye klabu ya soka ya Yanga imemgeuzia kibao aliyekuwa kiungo mshambuliaji wake wa kimataifa,Hamis Kiiza. 
Hivi karibuni nyota huyo kutoka nchini Uganda, amekuwa katika mvutano na uongozi wa klabu hiyo juu ya kusaini mkataba mpya wa kuendelea kutumikia klabu hiyo. 
Kwamba, Kiiza alitaka kuongezwa ofa ya aliyopewa na uongozi kutoka dola 35,000 hadi dola 50, 000 ambazo amesisitiza kupewa na baadaye kumuongeza hadi dola 40,000. 
Hata hivyo, habari kutoka ndani ya uongozi wa Yanga zinaeleza kwamba wameamua kuachana kwanza na suala la Kiiza kutokana na nafasi yake kutokuwa na umuhimu katika kikosi hicho. 
Kiongozi mmoja aliliambia gazeti hili kwamba kwa sasa Yanga inahitaji mshambuliaji halisi mmoja ambaye atashirikiana na mshambuliaji aliyepo sasa, Didier Kavumbagu. 
“Kwa sasa suala la Kiiza tumeliweka kando kwani nafasi yake haina umuhimu katika kikosi chetu, tunatafuta mshambuliaji halisi, ila tukikosa ndo tutarudi kwake,”alisema 
Akienda mbali zaidi, kiongozi huyo alisema kwamba mshambuliaji huyo anafahamu kila kitu juu ya mustakabali wake ndani ya klabu hiyo na hata hilo suala la kumpa fedha anayoitaka yeye halipo. 
Aliongeza kuwa baada ya kumleta mshambuliaji kutoka Nigeria Ogbu Brendan  kwa ajili ya majaribio, hivi karibuni tena wanataleta washambuliaji wengine kuja kujaribiwa. 
Katika hatua nyingine, kikosi cha Yanga kimeendelea na mazoezi yake ya kujiandaa na ligi kuu soka Tanzania Bara ambapo keshokutwa itacheza mechi ya kirafiki na URA ya Uganda. 

Mchezo huo utakaopigwa kwenye dimba la Taifa jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya kukipima kikosi hicho.

Mtwara kumekucha! Lori lenye shehena ya mabomba lashambuliwa mawe dereva hoi


Habari zilizotufikia kutoka mjini Mtwara zinasema kuwa Gari lililokuwa limebeba Shehena ya Mabomba ya Kusafirishia gesi kutoka Mjini Mtwara kuelekea Dar limeshambuliwa na mawe na kupelekea dereva wa lori hilo Kujeruhiwa Vibaya. 
Lori hilo lilianza kushambuliwa mara baada ya kuingia katika eneo la Mikindani Manispaa ya Mtwara Mjini na sababu ya kushambulia gari hilo ni katika kile kinachodhihirisha kuwa wana Mtwara bado hawajakubaliana na hoja ya Serikali ya kutaka Kusafirisha Gesi hiyo kwa ajili ya Manufaa ya Nchi. Lori hilo kwa sasa lipo kituo kikubwa cha polisi  Mtwara.
Tukio hilo linatokea ikiwa ni wiki moja tu imepita tokea watu kadhaa kukamatwa na jeshi la polisi mkoani Mtwara kwa kile kinachodaiwa kusambaza waraka wa kuhujumu miundombinu yote ya gesi mara tu serikali itakapoanza utekelezaji wake wa ujenzi wa bomba hilo kupeleka Dar.

Source: Jamii Forum

Miili ya wanajeshi waliouwawa Darfur kurejeshwa nchini kesho

http://www.raiamwema.co.tz/sites/default/files/styles/slideshow/public/field/image/307_jwtz.jpg?itok=8L3GOhTM
Miili ya wanajeshi hao ilipokuwa ikiagwa na askari wenzao nchini Sudan

MIILI ya wanajeshi waliouwawa katika mji wa Darfur, nchini Sudan inatarajiwa kuwasili nchini kesho kuanzia majira ya saa 4 asubuhi kwa ajili ya mazishi yake.
Wanajeshi hao waliokuwa kwenye jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa, walishambuliwa asubuhi ya Jumamosi iliyopita na waasi wanaopigana na serikali ya Sudan katika jimbo hilo la Darfur wakati wakisindikiza msafara ambaopo askari wengine akiwemo Polisi wa Tanzania walijeruhiwa.
Taarifa zinasema miili hiyo itapokelewa kesho kwa heshima zote kabla ya kufanyiwa taratibu za kuagwa kitaifa kisha kuzikwa kwa kushirikiana na familia zao.

Wenger amkatia tamaa Fabregas

http://gossip.ladyarse.com/wp-content/uploads/2012/07/wenger-arsene.jpg
Kocha Arsene Wenger

KOCHA wa Arsenal, Arsene Wenger amesema kwamba kuwa hatarajii kumsajili Cesc Fabregas katika kipindi hiki cha usajili wa majira ya kiangazi kwani kiungo huyo wa timu ya taifa ya Hispania ameamua kubaki kwa "mwaka mmoja zaidi " kwenye klabu yake ya Barcelona.
Arsenal wamesisitiza kuwapo kwa kipengele kinachowaruhusu kumnunua tena Fabregas kwa paundi za England milioni 25 ambacho kiliwekwa wakati wa mkataba wao wa kumuuza Mhispania huyo kwa Barca miaka miwili iliyopita.
Hata hivyo, licha ya Manchester United kujaribu kumtwaa kwa kuwasilisha ofa ya euro milioni 30 Jumatatu iliyopita, Mfaransa Wenger anaamini kwamba wao hawahitaji kutuma ofa yoyote kwa nia ya kumzuia nahodha wao huyo wa zamani kwenda Man U.
Iliripotiwa mwishoni mwa mwezi uliopita kuwa Wenger amekuwa akiwasiliana kila mara na nahodha wake huyo wa zamani, na sasa amedai kuwa anafahamu msimamo wa Mhispania huyo kuhusiana na hatma yake msimu ujao.
"Hivi sasa, Fabregas ameamua kubaki Barcelona kwa mwaka mmoja zaidi," Wenger aliwaambia waandishi wa habari.
Nahodha huyo wa zamani wa Arsenal amekuwa akihaha kupata nafasi ya uhakika katika kikosi cha kwanza tangu arejee katika timu yake ya utotoni lakini kuondoka kwa Thiago Alcantara kwenda Bayern Munich kunamaanisha kuwa sasa ana nafasi kubwa ya kucheza katika kiungo cha kocha Tito Vilanova.
Vilanova alisisitiza mwanzoni mwa wiki hii kwamba kiungo huyo mwenye miaka 26 anataka kubaki Barca na kuigania namba.
Alisema: "Natambua kwamba tumepokea ofa kadhaa kutoka klabu nyingine. Nilizungumza naye na ameniambia anataka kubaki.
"Cesc hafikirii kuhamia katika klabu nyingine. Anajua kwamba ushindani hapa ni mkubwa. Ndoto zake ni kuona anafanikiwa akiwa hapa."
Katika hatua nyingine kocha huyo amesema klabu yake inamudu mshahara wa kumlipa mshambuliaji wa Manchester United, Wayne Rooney anayetajwa kutaka kuhama Old Trafford licha ya klabu kudai HAUZWI.
Wenger alisema kama mchezaji huyo ataamua kukubali kutua kwao hawatakuwa na tabu ya kumlipa mshahara ambao kwa wiki hulipwa pauni 250,000.
"Rooney ana mkataba na amebakisha miaka miwili uishe, hivyo ni Man U wenye maamuzi. Lakini hatutakuwa na shida kulipa mshahara wa Rooney." alinukuliwa kocha huyo kutoka Ufaransa.

Mama atelekeza kichanga kisa wivu wa mapenzi

http://www.varbak.com/images/photos-of-black-babies-nb17527.jpg
Picha hii haihusiani na tukio hilo la kutelekezwa mtoto mjini Tanga
MWANAMKE mmoja mkazi wa eneo la Mtakuja jijini Tanga, aliyetajwa kwa jina la Asha Muhidini, amedaiwa kumtekeleza mtoto wake mchanga wa miezi miwili na kutokomea kusikojulikana kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni wivu wa mapenzi dhidi ya mumewe.
Mtonyaji wa habari hizi, Mariam Victor aliyejitambulisha kama mpwa wa mume wa mwanamke huyo, aliiambia MICHARAZO kuwa, mama huyo amekuwa na mzozo kwa muda mrefu na mumewe aliyetajwa kwa jina la Muhidini Mohammed baada ya mwanaume kuzaa nje ya ndoa mtoto mwenye miaka mitano.
Mariam alisema mwanamke huyo alimtelekeza kichanga hicho kwa kumfungia ndani ya chumba wanachoishi na mumewe tangu saa 1 usiku na walikuja kushtuka saa 5 usiku mtoto akilia na mjomba aliporejea kazini.

Aliongeza kuwa Asha amekuwa akipinga mtoto huyo aliyezaliwa kuja kuishi katia familia yao, lakini mumewe alikuwa akipinga akidai hawezi kuiacha damu yake kwa msimamo wa mkewe huyo.
"Mzozo uliosababisha hili jambo ni mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa na Mjomba ambapo kwa muda mrefu amekuwa akipinga na mkazamjomba (Asha) na jana alikuja kumtembelea baba yake na mke akapinga lakini mjomba alishikilia msimamo wake," alidokeza Mariam.
Alisema hawakujua kinachoendelea mpaka walipobaini kuwa mtoto kaachwa pekee yake na mama wa mtoto katoweka na kuanza kumsaka asubuhi hii bila ya mafanikio na kukimbilia ofisi ya serikali ya mtaa wao kuripoti ambapo wameombwa kuwa na subira kuona kama mwanamke huyo atarudi au la.
"Mwenyekiti katuambia tuvute subira na tumlishe mtoto maziwa na ng'ombe wakati tunasubiri mama yake arejee na kama vipi tuangalie ustaarabu mwingine ikiwemo kuripoti Polisi au kuendelea kumtunza mtoto kwa sababu pia hasumbui zaidi ya anapotaka kunyonya tu," alisema Mariam.
Juu ya mjomba wake na tukio hilo alilofanyiwa na mkewe, Mariam alidai hana la kusema kwa vile ni mpole kupita maelezo na kwamba amekubali kilichotokea kwa sababu kichanga hicho ni mwanae na ana wajibu wa kumtunza hasa ikizingatiwa wanapoishi ni nyuma ya familia hivyo kichanga kitaangaliwa.

Salha atua King's Modern Taarab


MUIMBAJI wa zamani wa kundi la Dar Modern Salha Abdallah 'Salha wa Hammer' aliyetimuliwa katika kundi hilo kwa kutoa wimbo binafsi na mumewe, amejiunga na la King's Modern Taarab na ameanza kuijifua kwa ajili ya maonyesho ya sikukuu ya Idd el Fitri.
Salha aliyetamba na vibao kadhaa akiwa na Dar Modern ukiwamo utunzi wake uliobeba jina la albamu ya 'Nauvua Ushoga' amelamba ajira King's Modern Julai 4 mwaka huu na anaendelea kujifua nao kwa ajili shoo za Idd na maandalizi ya albamu mpya ya kundi hilo.
Akizungumza na MICHARAZO, Salha alisema amesaini mkataba wa kulifanyia kazi kundi hilo linalotamba na kibwagizo cha 'Kijoka chazima taa' na hakuona sababu ya kuvunga huku akiwa ameshatimuliwa katika kundi lake la zamani.
"Baada ya kutemeshwa mzigo Dar Modern hivi karibuni, kundi la King's Modern limenifuata na kuniomba kujiunga nalo na kwa sasa mimi ni muimbaji wa kundi hilo, tunajiandaa kwa shoo za sikukuu ya Idd," alisema Salha.
Alisema hana cha kuahidi kwa mashabiki wa kundi hilo lakini wajiandae kupata burudani kabambe akishirikiana na wanamuziki wenzake ambao wamempokea kwa mikono miwili.
Uongozi wa Dar Modern unadaiwa kumtimua Salha baada ya muimbaji huyo na mumewe kutoa wimbo wa 'Mapenzi Matamu' (Wapendanao) kinyume na utaratibu uliopo ndani ya kundi hilo, japo Salha alilia kwamba hakutendewa haki kwa vile aliyeimba naye katika kazi hiyo ni mumewe na siyo kundi au msanii mwingine wa nje.

JAJI KORTI YA RUFANI KUONGOZA KAMATI TFF

Na Boniface Wambura
SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemteua Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bernard Luanda kuongoza Kamati ya Rufani ya Uchaguzi kufuatia mabadiliko ya Katiba yaliyofanywa Jumamosi (Julai 13 mwaka huu) na kuingiza kamati nyingine mpya.

Rais wa TFF, Leodegar Tenga ametangaza wajumbe wa kamati hizo jana (Julai 18 mwaka huu) mara baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji ya TFF kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Amesema uteuzi wa wajumbe hao umezingatia maoni ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF, lakini vilevile amewashukuru wajumbe walioteuliwa kwa kukubali kutoa mchango wao katika maendeleo ya mpira wa miguu nchini.

Mbali ya Jaji Luanda ambaye ni Mwenyekiti wa kamati hiyo, wajumbe ni Francis Kiwanga (Makamu Mwenyekiti), Anney Semu, Yohane Masalla na Allen Kasamala. Kamati ya Uchaguzi inaongozwa na Hamidu Mbwezeleni, Moses Kaluwa (Makamu Mwenyekiti), Mustafa Siyani, Hassan Dyamwale na Kitwana Manara.

Mwenyekiti Kamati ya Rufani ya Maadili ni Jaji Steven Ihema, Bi. Victoria Makani (Makamu Mwenyekiti), Mheshimiwa Mohamed Missanga, Henry Tandau na Mheshimiwa Murtaza Mangungu. Kamati ya Maadili inaundwa na Bi. Jesse Mguto (Mwenyekiti), Francis Kabwe (Makamu Mwenyekiti), Profesa Mtambo Madundo, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Mohamed Mpinga na Evod Mmanda.

Profesa Mgongo Fimbo anaongoza Kamati ya Rufani ya Nidhamu wakati Makamu wake ni Ong’wanuhama Kibuta na wajumbe ni Kanali Mstaafu Idd Kipingu, Dk. Mshindo Msolla na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Mstaafu Jamal Rwambow. Kamati ya Nidhamu inaongozwa na Kamishna wa Polisi (CP) Mstaafu Alfred Tibaigana, Mustafa Kambona (Makamu Mwenyekiti), Mheshimiwa Azzan Zungu, Yusuf Nzowa na Mohamed Msomali.
Pia Kamati ya Utendaji imefanya mabadiliko katika Kamati ya Waamuzi ambapo Said Nassoro na Charles Ndagala kutoka Chama cha Waamuzi wanachukua nafasi za Joan Minja na Riziki Majala. Kamati hiyo inaendelea kuongozwa na Kapteni Mstaafu Stanley Lugenge, Omar Kasinde (Makamu Mwenyekiti) wakati mjumbe mwingine ni Mohamed Nyama.

Kamati ya Tiba inaongozwa na Dk. Paul Marealle wakati nafasi ya Makamu Mwenyekiti itajazwa baadaye na Rais Tenga. Wajumbe ni Mwanandi Mwankemwa, Anthony Ngome, Frank Mhonda, Kapteni Joakim Mshanga na Helen Semu.

Rais Tenga alisema mabadiliko mengine yamefanyika kutokana na waliokuwa wajumbe kuomba kupumzika. Wajumbe walioomba kupumzika ni Dk. Sylvester Faya, Idd Mtiginjola na Deo Lyatto

Thursday, July 18, 2013

Ajali tena! Basi la Princess Muro lawaka moto abiria chupuchupu


Abiria zaidi ya 50 wilayani Nzega mkoani Tabora wamenusurika kupoteza maisha baada ya basi walilokuwa wakisafiria kuungua moto kutokana na hitilafu ya kiufundi.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora, Peter Ouma alisema moto huo ulioteketeza mizigo yote ya abiria, ulitokea juzi saa 4 usiku katika kijiji cha Nata kwenye basi la Princess Muro.

Alisema gari hilo aina ya Scania lenye namba za usajili T 6766 CEH, lilikuwa likitoka Dar es Salaam kwenda Mwanza likiwa linaendeshwa na dereva Boniface Francis.

Alisema likiwa na mwendo wa kawaida, lilianza kuwaka moto ndipo kondakta pamoja na dereva waligundua na kulisimamisha.

Abiria walifanikiwa kushuka wakiwa salama isipokuwa mizigo yao iliteketea kwa moto. Jitihada za kuuzima zilishindikana kutokana na eneo ilikotokea ajali hiyo kukosa kikosi cha zima moto na uokozi.
Kwa mujibu wa kamanda, kulitokea hitilafu kwenye injini ya gari hilo hali iliyosababisha moto. Hakuna mtu alijeruhiwa.

Kamanda amewataka wamiliki wa vyombo vya usafiri hususani vya kusafirisha abiria, kufanya ukaguzi na kuvikarabati kwa nyakati tofauti kuepusha ajali.

Inauma! Bi Harusi mtarajiwa ateketezwa na moto

 
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ernest Mangu,
FAMILIA moja ya watu wanne, akiwemo bi harusi mtarajiwa, Bushrati Bushiri (23) aliyetarajia kufunga ndoa Julai 13, mwaka huu, wamepoteza maisha baada ya nyumba walimokuwa wamelala kuteketea kwa moto.

Tukio hilo la kusikitisha lilitokea saa 6:00 usiku wa  Julai 10, mwaka huu eneo la Lumala, Kata ya Pasiansi, Manispaa ya Ilemela, jijini hapa ikiwa ni siku mbili tu kabla ya ndoa ya Bushrati.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ernest Mangu, nyumba iliyoteketea kwa moto ni ya Nuru Fadhili (46) mkazi wa Lumala, Pasiansi.

Mbali na Bushrati, Kamanda Mangu aliwataja marehemu wengine waliotokana na moto huo uliotokea usiku kuwa ni Amina Musa (75), Mariam Musa (72) na mtoto Janetha Abdul ambaye umri wake haukujulikana mara moja.

Alisema mwanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kiseke, Doto Twaha (17) alinusurika katika ajali hiyo kwa kupata majeraha mwilini na amelazwa katika Hospitali ya Rufaa Bugando (BMC) akipata matibabu.

Kamanda Mangu alisema chanzo cha moto huo ni jiko la mkaa ambalo lilikuwa sebuleni kwa ajili ya kupasha chakula cha mwezi mtukufu (daku) usiku.

Alisema kwamba mkaa ulidondokea kwenye zulia kisha kushika masofa na pikipiki iliyokuwa imeegeshwa sebuleni na kusambaa nyumba nzima huku marehemu wakiwa usingizini.

GPL

Mzee Mandela atimiza miaka 95 hospitalini

RAIS wa zamani wa Afrika Kusini, Mzee Nelson Mandela leo ametimiza miaka 95, lakini tofauti na mwaka uliopita alipotimiza miaka 94 safari hii ameshindwa kuisherekea kwa vile yupo mahututi hospitalini.
Siku ya Mandela huadhimishwa kuenzi kazi za kiongozi huyo alizozifanya kwa miaka 67 akiutumikia umma wa wananchi wa Afrika Kusini, zikiwamo vita dhidi ya ubaguzi wa rangi na hatimaye kuwa Rais wa kwanza mzalendo kwa miaka mitano, kisha kustaafu.


 “Happy birthday Mzee Madiba.” Rais wa kwanza na mzalendo wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, leo anatimiza umri wa miaka 95, pia anatimiza siku ya 40 tangu alipolazwa katika Hospitali ya Medclinic, Pretoria kwa ajili ya matibabu.

Nelson Rolihlahla Mandela, alizaliwa Julai 18, 1918 katika Kijiji cha Mvezo, eneo la Mthatha, Transkei Mkoa wa Eastern Cape na ametumia zaidi ya asilimia 70 ya maisha yake akipigania haki na usawa wa wananchi wa Afrika Kusini.


Maadhimisho ya miaka 95 tangu kuzaliwa kwa Mandela yanabeba uzito mkubwa kuliko maadhimisho mengine yaliyotangulia kwani kwa siku 40, wananchi wa Afrika Kusini wamekuwa katika wasiwasi mkubwa hasa kutokana na kuzorota kwa afya ya kiongozi huyo.
Mandela alilazwa katika hospitali hiyo Juni 8, mwaka huu akiugua magonjwa ya figo na afya yake imeelezwa kuwa ni mbaya.

UCHAWI TAZARA: NJIA ATUA NA BARUA YA VITISHO MBEYA

Njiwa akiwa na ujumbe wa barua kama inavyo onekana 


 Njiwa akiwa amedhoofu kwa Baridi akiwa katika choo cha wanaume 
 Hii ni sehemu alipokutwa Njiwa huyo 
 Majengo nje ya Ofisi ya Afisa Mwajiri 
 Baadhi ya wafanyakazi wakielekea eneo la  tukio 
 Afisa Mwajiri (Mwenye shati ya bluu) Na baadhi ya wafanyakazi wakishuhudia tukio 
 Mashuhuda wakitoka eneo la tukio 

 Barua iliyoletwa na Njiwa maeneo ya Ofisi ya Mwajiri upande wa mbele na nyuma 
 Jengo la Ofisi ya Afisa Mwajiri 
Stesheni ya TAZARA kituo  cha Mbeya 


MAKUBWA YAIBUKA TAZARA MBEYA : NJIWA ATUA NA BARUA YA VITISHO .

Njiwa akiwa na ujumbe wa barua kama inavyo onekana 


 Njiwa akiwa amedhoofu kwa Baridi akiwa katika choo cha wanaume 
 Hii ni sehemu alipokutwa Njiwa huyo 
 Majengo nje ya Ofisi ya Afisa Mwajiri 
 Baadhi ya wafanyakazi wakielekea eneo la  tukio 
 Afisa Mwajiri (Mwenye shati ya bluu) Na baadhi ya wafanyakazi wakishuhudia tukio 
 Mashuhuda wakitoka eneo la tukio 

 Barua iliyoletwa na Njiwa maeneo ya Ofisi ya Mwajiri upande wa mbele na nyuma 
 Jengo la Ofisi ya Afisa Mwajiri 
Stesheni ya TAZARA kituo  cha Mbeya 


*******************************************************
WAFANYAKAZI wa Mamlaka ya Reli, kati ya Tanzania na Zambia(TAZARA) jana walijikuta katika wakati mgumu na baadhi yao kulazimika kuzikimbia ofisi zao, baada ya ndege aina ya njiwa kukutuwa katika moja ya choo cha ofisi hiyo akiwa amefungwa hirizi shingoni, huku akiwa na barua yenye ujumbe wa onyo kali.
Tukio hilo la aina yake, lilitokea mapema leo   saa mbili asubuhi katika ofisi za mamlaka hiyo zilizopo eneo la Iyunga Mkoani hapa, hali ambayo mbali na baadhi ya wafanyakazi wake kuzikimbia ofisi, ilisababisha kuibuka kwa mjadala mkubwa dhidi ya tukio hilo.
Mtandao huu ulifanikiwa  kushudia njiwa huyo  mweusi akiwa nyuma ya choo cha kiume katika eneo hilo la ofisi ya mwajiri, huku akiwa amefungwa hirizi shingoni iliyozungushiwa shanga mchanganyiko wa rangi tatu, ambazo ni Nyekundu, Njano  na Nyeupe.
Mbali ya kuwa na hirizi hiyo, pia njiwa huyo alikuwa amebeba barua inayodaiwa kuwa ni ya mmoja wa wafanyakazi wa Mamlaka hiyo (jina limehifadhiwa kwa sababu maalumu) ambaye anadaiwa hivi karibuni kufukuzwa kazi kwa makosa ya ubadhirifu.
Barua hiyo ilikuwa na maandishi mekundu yenye ujumbe ulioandikwa kwa lugha mbili za Kiswahili na kiarabu, ambapo katika maandishi ya Kiswahili yalisomeka “ Naomba majibu haraka kama mtarudisha binti huyu kazini” ilisema sehemu ya ujumbe huo, huku ikiwa na orodha ya majina matatu ya viongozi wa shirika hilo.
Mbali na ujumbe huo ukiwa umeandikwa kwa maandishi ya mkono yaliyokolezwa kwa wino mwekundu upande wa nyuma, lakini upande wa mbele kulikuwa na maandishi yakiwa ni barua ya kutaarifiwa kufukuzwa kazi kwa mfanyakazi huyo.
Akizungumzia tukio hilo, Mwajiri wa mamlaka hiyo kanda ya Mbeya, aliyejitambulisha kwa jina la Mchaba Mgweno, alikiri kutokea kwa tukio hilo na kwamba waliobaini ni wahudumu wa usafi.
Aliongeza kuwa baada ya kupokea taarifa hiyo aliwaarifu na wafanyakazi wenzake ambao walikusanyika na kumshuhudia Njiwa huyo mweusi akiwa amedhoofika huku akiwa na barua hiyo yenye vitisho.
Alisema baada ya kushuhudia hali hiyo waliamua kutoa taarifa kituo cha polisi kilichopo ndani ya shirika hilo, ambapo waliichukua barua hiyo na baadhi ya wafanyakazi hao wakienda kutoa maelezo kituoni hapo.
“Kwa kweli hali hii si ya kawaida, ila kwa sasa siwezizungumzia chochote kwa kuwa hata mimi tukio hili limeniweka katika wakati mgumu na nimeshindwa kuendelea na majukumu yangu ” alisema Mgweno.
Hata hivyo kuliibuka malumbano makali kati ya wafanyakazi wa shirika hilo walioshuhudia tukio hilo, ambapo baadhi yao wakidai kuwa tukio hilo ni la kutengenezwa kwa lengo la kuchafuana.
“Hebu angalia hiyo barua yenyewe mbona ni kivuli (Photocopy), kama ingekuwa ni ya ….wanamtaja mfanyakazi aliyefukuzwa jina limehifadhiwa ingekuwa ni nakala halisi….haiwezekani mambo haya ni kutaka kuchafuana tu” alisema mmoja wa wafanyakazi hao.
Lakini baadhi yao wakiamini kweli kuwa barua hiyo ilitumwa ili itoe vitisho kwa viongozi wa shirika hilo.
Baadhi ya askari polisi wa kituo cha Tazara walikiri kutokea kwa tukio hilo na kwamba wanaendelea na uchunguzi ili kubaini ukweli wake.
“Ndugu zangu nyie mnajua taratibu za utoaji wa taarifa kwa jeshi hili, maana wapo wahusika, lakini kwa kifupi sisi tulipokea taarifa na tunaendelea kuzifanyia kazi” alisema mmoja wa askari hao.
Hata hivyo, hadi tunapoondoka eneo la tukio majira ya saa sita mchana Njiwa huyo alikuwa bado yupo eneo la tukio. ANGALIZO: UNAPOTUMIA HABARI HIZI USIPOTOSHE UKWELI WASILIANA NASI KWA NAMBA 0787-490 752 Au 0654-221465

PICHA ZOTE NA MBEYA YETU 


Watano wajeruhiwa, mmoja vibaya katika ajali Tanga

Picha haihusiani na taarifa hiyo hapo juu
HABARI zilizotufikia muda huu zinasema kuwa watu watano wamejeruhiwa mmoja vibaya baada ya kutrokea ajali eneo la Usagara, mkoani Tanga.
Kwa mujibu wa chanzo chetu cha habari ni  kwamba watu hao walijeruhiwa baada ya gari dogo lililokuwa likiendeshwa na mtu ambaye siye dereva kuwagonga.
"Mtu ambaye siye dereva alijaribu kuendesha gari na kwa bahati mbaya akawavamia na kuwajeruhi watu watano, mmoja akiwa katika hali mbaya na wote wamekimbizwa hospitali ya Bombo kwa matibabu.
MICHARAZO inaendelea kufuatilia ikiwemo kujua kama kuna madhara zaidi ya taarifa hiyo, kadhalika inawaombea kila la heri majeruhi hao ili wapone haraka.

Cheka aidindia TPBO, adai atacheza mechi zake mbili iwe isiwe


Bondia Francis Cheka (kulia)
BONDIA Francis Cheka 'SMG' ametaka mzizi wa fitina kwa kusema wazi kuwa yupo tayari kupanda ulingoni kupigana katika mapambano yake mawili aliyopangiwa kuyacheza ndani ya mwezi ujao.
Msimamo huo wa Cheka unatofautiana na mkwara uliotolewa na Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBO-Limited) iliyomtaka asidhubutu kucheza mechi yake isiyo na ubingwa dhidi la Mmalawi Chiotcha Chimwemwe.
TPBO kupitia Rais wake, Yasin Abdallah 'Ustaadh' ilionya kuwa Cheka hapaswi kupigana ndani ya siku 30 kabla ya pambano lake na Mmarekani Findley Derrick litakalokuwa la kuwania ubingwa wa WBF, litakalochezwa Agosti 30 jijini Dar.
Kabla ya pambano hilo Cheka alishasaini pigano jingine dhidi ya Mmalawi Chiotcha Chimwemwe litakalofanyika Agosti 10 kwenye uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro katika shamrashamra za sikukuu ya Idd el Fitri.
Hata hivyo akizungumza na MICHARAZO kwa njia ya simu jana toka kambini kwake mjini Morogoro, Cheka alisema hawezi kukacha kupigana na Mmalawi kwa madai ni sehemu ya maandalizi ya pambano lake dhidi ya Mmarekani.
Cheka alisema alishasaini mikataba na waratibu wa michezo hiyo na hivyo ni vigumu kusitisha pigano lake la Chimwemwe hata kama silo la ubingwa wowote.
"Mimi nitacheza mapambano yote, lile la Mmalawi ni kama sehemu ya maandalizi ya pigano lake dhidi ya Derrick, pia waratibu wa pambano la pili wenyewe ndiyo waliochelewa kumalizana nami na kujikuta nasaini mechi ya Chimwemwe," alisema Cheka.
Aliongeza haoni ubaya wa yeye kupigana na Mmalawi kabla ya kuvaana na Derrick, licha ya kukiri anapaswa kuwa makini ili asijeruhiwe kama ilivyotokea walipoumana na bondia huyo mjini Arusha na kutetea taji la IBF Afrika.
"Chimwemwe ni bondia nzuri na hatari ulingoni, hivyo nitacheza pambano langu la Idd Pili kwa umakini ili nisishindwe kupigana na Mmarekani, pia muda wa kujiandaa na pigano la pili unatosha kabisa sioni sababu ya kuibuka kwa malumbano wakati huu," alisema Cheka.
Hata hivyo TPBO-Limited kupitia rais wake, imeendelea kusisitiza kuwa Cheka anapaswa kuzingatia ushauri wake ili asije akavuruga pambano hilo la kimataifa la WBF ambalo litazidi kumjengea jina kuliko mechi ya 'ndondo' isiyo na tija.
Pia amesema taarifa walizonazo ni kwamba Chimwemwe ana pambano atakalopigana na Mkenya Agosti 10 na siyo Cheka na kudai huenda ni mbinu zinafanyika kulivuruga pambano hilo la Cheka na Mmarekani.

Mtibwa Javu haendi kokote, bado ni mali yetu- Mtibwa Sugar

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhdEulqye6NB2gXsPi5nX52ruKNuZkwLExeKIBZx9YhfvRv9i-1GRUvXwcGWe-uVRRKZzgwsiMkZgmzbo80RFdgxlHnANAjRcCAnSAEfyBFFwRCrJPMxsv_FBRuFjUHKP11ERryy3d8XlE/s640/Javu.jpg
Husseni Javu
KLABU ya soka ya Mtibwa Sugar imevunja ukimya na kusema wazi kuwa, mshambuliaji wao nyota Hussein Javu bado ni mchezaji wao kwa vile Yanga iliyokuwa ikimhitaji kushindwa kwenda kumalizana nao ili ajiunge Jangwani.
Javu amekuwa akitajwa kuwa ameshasaini mkataba wa miaka miwili wa kuichezea Yanga kwa msimu ujao, lakini uongozi wa Mtibwa Sugar umesema taarifa hizo siyo za kweli kwa sababu hakuna maafikiano yoyote yaliyofanyika.
Mkurugenzi wa klabu hiyo, Jamal Bayser aliiambia MICHARAZO kuwa, ni kweli Yanga waliwafuata wakionyesha nia ya kumsajili mfungaji wao huyo hodari, lakini baada ya kuwapa masharti yao hawakurejea tena kwao.
Bayser alisema kutokana na ukimya huo wa mabingwa hao wa soka nchini, ni wazi huenda wameachana na wazo la kumsajili mchezaji huyo ambaye bado wana mkataba naye wa kuichezea klabu hiyo mpaka mwakani.
"Javu bali ni mali yetu tuna mkataba naye, pia tangu Yanga walipokuwa kwa mara ya kwanza wakionyesha nia ya kutaka kumsajili hawajarudi tena, na kunashangaa kwamba mchezaji huyo akielezwa kasajiliwa Jangwani," anasema.
Anasema anadhani taarifa za Javu kutua Jangwani ni za kuuzia magazeti tu kwa vile hakuna makubaliano yoyote na wenzao wa Yanga, akiamini pia nyota huyo aliyeanza kuichezea Mtibwa kupitia timu ya vijana tangu mwaka 2007 atasalia Manungu kwa msimu ujao.
Javu mwenyewe aliliambia MICHARAZO kwamba bado anajitambua ni mchezaji wa Mtibwa Sugar, licha ya kukiri kuwahi kufuatwa na viongozi wa Simba na Yanga kwa nia ya kumshawishi kujiunga na klabu zao.
"Walinifuata kwa nyakati tofauti ili kunishawishi nitue katika klabu zao, ila niliwaeleza mimi bado nina mkataba na Mtibwa hivyo wakazungumze na mabosi wangu wakiafikiana sintakuwa na tatizo, ila mpaka sasa sijui kinachoendelea," alisema Javu aliyepo pia kwenye kikosi cha pili ya taifa 'Young Taifa Stars.

Mwisho

Kiungo Simba akiri Kibadeni zaidi ya Liewig

Abdallah 'Dullah' Seseme (kushoto) akiwajibika uwanjani
KIUNGO mkabaji chipukizi wa Simba, Abdallah Seseme, amemwagia sifa kocha mkuu mpya wa klabu hiyo, Abdallah Kibadeni 'King' akisema ni bonge la kocha na ana imani ataipa mafanikio klabu hiyo katika msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Seseme alisema kuondoka kwa makocha Milovan Cirkovic na 'Babu' Patrick Liewig kulimpa hofu kwamba huenda Simba ingeyumba, lakini kwa kipindi kifupi alichokaa na kocha wake wa sasa amemstaajabisha kwa umahiri huku akisema ni zaidi ya waliomtangulia.
Mchezaji huyo alisema kwa staili anazofundisha kocha Kibadeni na wasaidizi wake anaimani kubwa ya Simba kurejesha heshima yake baada ya kuyumba msimu uliopita kiasi cha kuingia kwenye kinyang'anyiro cha kuwania nafasi ya tatu.
"Simsifii labda kwa kujipendekeza, ila ukweli sijawahi kuona kocha bomba kama Kibadeni. Kwa mtazamo wangu huenda ni zaidi ya watangulizi wake na kama Simba itamng'ang'ania itafika mbali na kurejesha heshima yake kitaifa na kimataifa," alisema Seseme.
Seseme anayemudu nafasi nyingine za mbele na aliyekuwa mmoja wa mhimili walioisaidia Simba kushika nafasi ya tatu msimu uliopita, alisema kwa kuangalia maandalizi ya timu zitakazoshiriki ligi ijayo anadhani msimu ujao kutakuwa na ligi ngumu sana.
"Nadhani msimu ujao kutakuwa na ligi ngumu pengine kuliko iliyopita japo ninaipa nafasi kubwa ya Simba kurejesha heshima yake, pia unaweza kuwa msimu wa kuwika kwa vijana wazawa tofauti na msimu uliopita wageni kuonyesha viwango vya juu," alisema.
Katika msimu uliopita wachezaji wa kigeni waling'ara hasa kwa nafasi ya ushambuliaji na haikuwa ajabu Kipre Tchetche wa Azam kunyakua kiatu cha dhahabu akifuatiwa na Mrundi, Didier Kavumbagu wa Yanga.

Wawakilishi wa WB, TSCP wakagua mradi wa mifereji Mwanza

Wawakilishi wa Benki ya Dunia na Timu ya Mradi wa Kuendeleza Miji Tanzania (TSCP) ulio chini ya OWM-TAMISEMI, wakikagua ujenzi wa Mifereji jijini Mwanza wakati walipokuwa na ziara ya kutembelea miradi hio na kuona maendeleo yake.
 
Standi mpya ya Mabasi ya Dala dala iliyopo katikati ya mji wa Kigoma, Ni moja kati ya matunda ya Mradi wa Kuendeleza Miji hapa nchini  (TSCP) chini ya OWM-TAMISEMI. 
 

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda (wa pili kulia), Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI, Hawa Ghasia (wa pili kushoto), Mkurugenzi wa Benki ya Dunia – Tanzania, Philippe Dongier (kulia), pamoja na Mkurugenzi wa Uendelezaji wa Miji (OWM-TAMISEMI), Anna Mtani (kushoto) katika tukio la Uzinduzi wa mradi wa kuboresha Miji wa ULGSP, mradi uliozaliwa na mradi Mkakati wa Undelezaji Miji (TSCP) chini ya OWM-TAMISEMI kwa mkopo wa Banki ya Dunia

Ujenzi wa Dampo Jijini Arusha, wa TSCP, mradi chini ya OWM-TAMISEMI, ukikaguliwa na wawakilishi wa Banki ya Dunia na timu ya TSCP.

Rais Kikwete ateta na Rais wa Sudan kuhusu vifo wa wanajeshi wa JW


                                THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS



TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais Jakaya Mrisho Kikwete amefanya mazungumzo kwa njia ya simu na Rais wa Sudan Mheshimiwa Omar Bashir kufuatia kuuawa na kujeruhiwa kwa askari wa Tanzania, walioko katika ulinzi wa kimataifa wa amani katika jimbo la Darfur na kumtaka Rais Bashir kuchukua hatua za haraka kuwasaka na kuwakamata waliohusika na kitendo hicho kiovu na kuwafikisha mbele ya sheria haraka iwezekanavyo
Katika mazungumzo yao, Rais Omar Bashir amekubaliana na Rais Kikwete na kumuahidi kuwasaka  hadi kuwakamata wale wote waliohusika na kuwachukulia hatua za kisheria.
Rais Bashir amemueleza Rais Kikwete kuwa binafsi anaamini kuwa waliohusika ni wahalifu na hivyo kuahidi kuwa lazima watasakwa hadi kukamatwa kwa ajili ya kuchukuliwa hatua.
Rais Bashir amempa pole Rais Kikwete kwa tukio hilo la kusikitisha ambapo wanajeshi wa Tanzania wameenda nchini Sudan kulinda Amani na Usalama wa wananchi wa Sudan.
Mapema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa(UN) Bw. Ban Ki Moon alimpigia Rais Kikwete na kumpa pole kwa mkasa huo mkubwa na wa kusikitisha ambao umewatokea wa Tanzania hao wakati wakiwa katika kutekeleza jukumu lao la kulinda amani nchini Sudan.
Hadi sasa hakuna kikundi chochote ambacho kimekiri kuhusika na shambulio hilo ingawaje kumekua na  kutupiana lawama baina ya vikundi vya kiserikali na  vya waasi katika jimbo la Darfur.
Mapigano baina ya vikundi vya kikabila na koo mbalimbali zimesababisha mapigano na uvunjifu mkubwa wa amani na usalama katika jimbo la Darfur kwa muda wa miaka 10 sasa, na mara nyingi mapigano  na tofauti zao hizo zimesababisha vifo na uvunjifu wa amani kwa wananchi wa Sudan na wageni pia.
Mwishoni mwa mwaka jana  Wanajeshi wanne kutoka Nigeria waliuawa karibu na El Geneina , Magharibi mwa Darfur ambapo pia inaelezwa na Umoja wa Mataifa kuwa wanajeshi wapatao 50 wameuawa tangu kikosi hiki cha Umoja wa Afrika kinachoundwa kwa  pamoja chini ya Umoja wa Mataifa (UNAMID) kianze operesheni yake mwishoni mwa mwaka 2007.
Taarifa za Umoja wa Mataifa pia zinaeleza kuwa kabla ya mashambulizi yaliyofanyika dhidi ya kikosi cha Tanzania jumamosi iliyopita, wanajeshi 6 wanaolinda Amani wameuawa tangu oktoba mwaka huu ambapo pia inasadikiwa kuwa watu wapatao 300,000 wameyakimbia makazi yao.
Hata hivyo kiini cha mgogoro huo unaosadikiwa kuwa ni ugomvi wa ardhi na rasilimali zilizoko katika jimbo hilo nchini Sudan.
Miili ya maaskari hao saba wa Tanzania inatarajiwa kuwasili nchini ijumaa tarehe 19, Julai kwa ajili ya maziko.
Imetolewa na:
Premi Kibanga,
Mwandishi wa Habari wa Rais, Msaidizi,
Ikulu
Dar-Es-Salaam, Tanzania
16 Julai, 2013

Wednesday, July 17, 2013

Ajali nyingine tena, Air Bus lapinduka Maseyu

Photo: Basi la Airbus likielekea Dar-es-salaam kutokea Tabora
Basi la Airbus likiwa safarini. Moja ya mabasi hayo limepata ajali jioni hii

ABIRIA 23 waliokuwa wakisafiri na basi la Air Bus linalofanya safari zake kati ya Tabora na Dar wamejeruhiwa wanne kati yao vibaya baada ya basi hilo kupinduka eneo la Maseyu, mjini Morogoro.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotangazwa na Radio One hivi punde ni kwamba basi hilo lilipinduka kutokana na mwendo kasi wakati likijaribu kuyapita malori na kupoteza muelekeo kabla ya kupinduka.
Taarifa hizo zinasema kuwa, majeruhi wameumia vibaya maeneo ya kichwani, kifuani na miguuni na wamekimbizwa hospitali ya Mkoa wa Morogoro, huku wanne akiwemo dereva wa basi hilo wenyewe wakiwahishwa jijini Dar es Salaam katika hospitali ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.
Kati ya abiria haop waliojeruhiwa 13 wamelazwa hospitali hiyo ya mkoa wa Morogoro, na kwamba taarifa zaidi zinaendelea kufuatiliwa ili kujua kinachoendelea, ingawa mpaka sasa hakuna kifo chochote kilichoripotiwa.