STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, October 18, 2013

Miss Universe Tz 2013 akabidhiwa bendera

MREMBO wa Miss Universe Tanzania 2013 Betty Boniface Omara amekabidhiwa bendera leo na Waziri wa Maliasili na Utalii Dk Khamis Kagasheki.

Zoezi hili limefanyika katika ukumbi wa mkutano wa wizara hiyo tayari kwa safari yake ya kwenda kwenye mashindano ya Miss Universe yatakayofanyika Moscow nchini Urusi mapema mwezi Novemba.

Akimkabidhi bendera huku akimpongeza waziri Kagasheki pia amemtakia mafanikio mema huko aendako.

Betty pia aliwaahidi watanzania kuwa mbali na kurudi na ushindi lakini pia ataenda kuitangazia dunia kuacha kutumia nakshi(Mapambo) yanayotumia pembe za ndovu ili kumaliza tatizo la ujangili nchini.

Zoezi la kukabidhiwa bendera lilifanyika likishuhudiwa na Mkurugenzi wa Kitaifa Miss Universe Tanzania Maria Sarungi Tsehai.

Mashindano ya Miss Universe Tanzania 2013 yamedhaminiwa na hifadhi ya Taifa Tanapa na Mrembo Betty Boniface ameshaanza kutangaza hifadhi hizi kwa njia mbalimbali hapa nchini na nje ya nchi.
 Mrembo wa Miss Universe Tanzania 2013 Betty Boniface Omara akipokea bendera ya taifa leo kutoka Waziri Maliasili na Utalii, Hamisi Kagasheki.

Mbeya City, Azam kuing'oa Simba kileleni VPL?

Vijana wa Mbeya City
Na Boniface Wambura
LIGI Kuu ya Vodacom (VPL) inaendelea kutimua vumbo kesho (Oktoba 19 mwaka huu) kwa mechi tano huku Mbeya City ikiikaribisha JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya, ambapo ushindi wowote unaweza kukwea kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo kwa mara ya kwanza.
 

Timu hiyo iliyopanda daraja msimu huu ina pointi 17 sawa na Azam ambayo nayo ina nafasi ya kuing'oa Simba kama itaifunga Oljoro JKT wanaoumana nao jijini Arusha.

Simba wanaoongoza msimamo wa ligi hiyo kwa sasa ikiwa na pointi 18 na yenyewe itashuka dimbani Jumapili kuwakaribisha watani zao Yanga katika uwanja wa Taifa.


Mbali na mechi ya Mbeya City na JKT Ruvu na ile ya Oljoro dhidi ya Azam mechi nyingine zitazkazochezwa kesho ni Mtibwa Sugar na Mgambo Shooting (Uwanja wa Manungu, Turiani), Ashanti United na Ruvu Shooting (Azam Complex Chamazi, Dar es Salaam) na Kagera Sugar dhidi ya Coastal Union (Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba).

Wakati huo huo, Ligi Daraja la Kwanza (FDL) nayo inaendelea katika viwanja nane kesho (Oktoba 19 mwaka huu) huku Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam ukiwa mwenyeji wa mchezo kati ya African Lyon na Friends Rangers.

Nayo Villa Squad itacheza na Green Warriors katika Uwanja wa Mabatini, Mlandizi, Polisi Morogoro na Kimondo (Uwanja wa Jamhuri, Morogoro), Lipuli na Kurugenzi (Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora mjini Iringa) na Mkamba Rangers dhidi ya Majimaji (Uwanja wa CCM Mkamba, Morogoro).

Toto Africans na Mwadui (Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza), Polisi Dodoma na Polisi Tabora (Uwanja wa Jamhuri, Dodoma), wakati Polisi Mara na pamba zitacheza kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.

Magari Maalum tu, pambano la Simba na Yanga J2

Afisa Habari wa TFF, Boniface Wambura
MAGARI yenye shughuli maalumu tu ndiyo yatakayoruhusiwa kuingia uwanja wakati wa mechi ya Simba na Yanga itakayochezwa keshokutwa (Jumapili) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mechi itaanza saa 10 kamili jioni, na kila timu inaruhusiwa kuingia na magari matatu tu; gari la timu na mengine mawili ya viongozi. Ukaguzi wa kuingia uwanjani ni kwa watu wote, kwani utaratibu huo si wa kumdhalilisha mtu bali lengo lake ni kuhakikisha usalama.
Vilevile watu hawataruhusiwa kuingia uwanjani na mifuko ya aina yoyote ikiwemo mabegi, isipokuwa kwa waandishi wa habari wanaotumia mabegi hayo kwa ajili ya kubebea kamera zao. Pia hakuna wafanyabishara watakaoruhusiwa kufanya biashara katika maeneo yanayozunguka uwanja.
Kwa washabiki watakaokuwa katika mazingira ya kuwa kero kwa wenzao wakiwemo walevi hawataruhusiwa kuingia uwanjani, pamoja na wale wenye silaha kama bastola ambapo wakikamatwa wafikishwa polisi na baadaye kufunguliwa mashtaka kortini.
Barabara ya Uwanja wa Taifa itafungwa kuanzia saa 2 asubuhi upande wa Chang’ombe, hivyo washabiki wanatakiwa kununua tiketi zao mapema kesho (Jumamosi) ambapo zitaanza kuuzwa katika vituo mbalimbali kuanzia saa 4 asubuhi.
Vituo hivyo ni mgahawa wa City Sports Lounge, Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala, Uwanja wa Uhuru, mgahawa wa Brake Point uliopo Kijitonyama na BMM Salon iliyoko Sinza Madukani.

TFF bado ina kinyongo na Shafii Dauda yamchinja, ikitangaza majina wagombea uchaguzi mkuu, mwenyewe adai hakubali

Shafii Dauda 'Tishio' akiwa kwenye shughuli zake za habari
 KAMATI ya Uchaguzi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imetangaza orodha ya mwisho ya wagombea wa uchaguzi wa TFF na wa Bodi ya Ligi (TPL Board) utakaofanyika baadaye mwezi huu, 'ikimchinja' tena Shafii Dauda katika kinyang'anyiro hicho.
Uchaguzi wa Bodi ya TPL utafanyika Oktoba 25 mwaka huu wakati ule wa TFF utafanyika Oktoba 27 mwaka huu. Kampeni kwa ajili ya uchaguzi wa TPL Board na ule wa TFF zimeanza leo (Oktoba 18 mwaka huu)  zitamalizika siku moja kabla ya uchaguzi saa 10 kamili alasiri. Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Hamidu Mbwezeleni amewataja wagombea kwa upande wa TPL Board kugombea uenyekiti ni Hamad Yahya Juma (Mtibwa Sugar), Makamu Mwenyekiti ni Said Muhammad Said Abeid (Azam). Wanaowania ujumbe wa Bodi ya Uendeshaji ni Kazimoto Miraji Muzo (Pamba) na Omary Khatibu Mwindadi (Mwadui).
Wagombea kwenye uchaguzi wa TFF ni Athuman Jumanne Nyamlani na Jamal Emily Malinzi (Rais), Imani Omari Madega, Ramadhan Omar Nassib na Wallace Karia (Makamu wa Rais).
Kwa upande wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ni Kalilo Samson (Kanda namba 1- Geita na Kagera), Jumbe Odessa Magati, Mugisha Galibona, Samwel Nyalla na Vedastus Lufano (Kanda namba 2- Mara na Mwanza), Epaphra Swai na Mbasha Matutu (Kanda namba 3- Shinyanga na Simiyu).
Ali Mtumwa, Elley Simon Mbise na Omar Walii Ali (Kanda namba 4- Arusha na Manyara), Ahmed Idd Mgoyi na Yusuf Hamis Kitumbo (Kanda namba 5- Kigoma na Tabora), Ayubu Nyaulingo na Blassy Mghube Kiondo (Kanda namba 6- Katavi na Rukwa), Ayoub Shaibu Nyenzi, David Samson Lugenge, John Exavery Kiteve, Lusekelo Elias Mwanjala (Kanda namba 7- Iringa na Mbeya).
James Patrick Mhagama na Stanley William Lugenge (Kanda namba 8- Njombe na Ruvuma), Athuman Kingombe Kambi, Francis Kumba Ndulane na Zafarani Mzee Damoder (Kanda namba 9- Lindi na Mtwara), Hussein Zuberi Mwamba, Stewart Ernest Masima, Charles Komba (Kanda namba 10- Dodoma na Singida), Farid Nahdi, Geofrey Irick Nyange, Juma Abbas Pinto, Riziki Juma Majala) na Twahil Twaha Njoki (Kanda namba 11- Morogoro na Pwani).
Davis Elisa Mosha, Khalid Abdallah Mohamed (Kanda namba 12- Kilimanjaro na Pwani), Alex Crispine Kamuzelya, Kidao Wilfred Mzigama, Muhsin Said Balhabou na Omary Isack Abdulkadir (Kanda namba 13- Dar es Salaam).
Mbwezeleni amewataka wagombea kufanya kampeni bila kukashfu wenzao, kwani Kanuni ya Uchaguzi za TFF toleo la 2013 inatoa fursa kwa Kamati ya Uchaguzi kuwaondoa wagombea wa aina hiyo kwenye uchaguzi.
Aliyekuwa mgombea wa Ujumbe wa Kanda ya 13, Shafii Dauda ametoswa licha ya kulipa faini aliyotakiwa kulipa ndani ya siku tatu na Kamati ya Maadili ya Rufaa.
Akihojiwa muda mfupi uliopita na kituo cha Uhuru Fm, Shafii amesema hakubali hata kidogo na ameshaanza mchakato wa kupeleka malalamiko yake FIFA kwa madai kuna mchezo mchafu amefanyiwa na kamati hiyo ya uchaguzi ya TFF.
Shafii alisema tangu awali kulikuwa na zengwe kwa lengo la kuwabeba wagombea fulani kutetea nafasi zao na dai kwamba hana uzoefu ni sababu tu, lakini alisema hakubali haki yake ipotee bure na Jumapili atakwea pipa kwenda Zurich makao makuu ya FIFA kupeleka mashtaka yake.
Baadhi ya wadau wa soka waliozungumza na MICHARAZO wamedai kushtushwa na maamuzi ya Kamati ya Uchaguzi ya TFF wakidai ni kama kutaka kuleta malumbano yasiyokuwa na sababu yoyote.

Thursday, October 17, 2013

Simba yapumua, Mombeki arejea dimbani kuivaa Yanga J'2

Hii ndiyo kazi ya Mombeki kuwaokotesha mipira mabeki na kipa
KLABU ya soka ya Simba imepumua na kuwa na matumaini makubwa ya kumtumia mshambuliaji wake mrefu na mwenye nguvu, Betram Mombeki aliyekuwa akitajwa huenda asiwepo kwenye pambano lao na watani za Yanga.
Mombeki alitajwa yupo katika hatihati ya kulikosa pambano hilo la watani wa jadi litakalochezwa kwenue uwanja wa Taifa siku ya Jumapili baada ya kujiumiza mazoezi katika kambi ya timu hiyo iliyopo Bagamoyo.
Hata hivyo habari njema kwa wanachama na mashabiki wa Simba ni kwamba mshambuliaji huyo aliyesajiliwa na Simba akitokea Pamba ya Mwanza, amerejea tena uwanjani na kuna uwezekano mkubwa Jumapili atashirikiana na mfumani nyavu mahiri, Amissi Tambwe kuichachafya ngome ya Yanga.
Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga aliiambia MICHARAZO kuwa, Mombeki amerejea tena uwanjani baada ya hali yake kutengemaa na kuwapa matumaini makubwa ya kushuka dimbani Jumapili kuiangamiza Yanga.
Kamwaga alisema hata hivyo kikosi chao bado kitaendelea kukosa huduma za wachezaji wao nyota kama Henry Joseph, Issa Rashid 'Baba Ubaya' na Miraj Adam.
"Tunashukuru hofu ya kumkosa Mombeki imeondoka baada ya mshambuliaji huyo kurejea tena dimbani, japo Simba itawakosa Henry Joseph ambaye hayupo kambini, Baba Ubaya, Miraj Adam na Abdallah Seseme ambao ni majeruhi," alisema Kamwaga.
Kamwaga alisema kikosi chao kina morali na ari kubwa ya kushinda mechi ya Jumapili, licha ya kudai litakuwa pambano gumu.
Pia alisema katika kuwatia motisha wachezaji ili kuigaragaza Yanga kwenye uwanja wa Taifa, viongozi na 'matajiri' wa Simba wanatarajia kuteta na wachezaji siku ya Jumamosi kwa lengo la kuwaweka sawa kisaikolojia pamoja na kuwatia morali zaidi ili kuwashinda Yanga.
"Viongozi na matajiri wa Simba wataitembelea kambi na kuzungumza na wachezaji kati ya Ijumaa na Jumamosi ili kuwaweka sawa na kuhakikisha Yanga anakufa Jumapili Taifa," alisema Kamwaga.
Simba na Yanga zitakutana katika mchezo huo, huku Simba ikiwa na deni la kulipa kisasi cha kipigo walichopewa katika mechi yao ya mwisho ya ligi iliyopita iliyochezwa Mei mwaka huu ambapo Yanga ilishinda mabao 2-0.

Wednesday, October 16, 2013

Wanachama Yanga kupiga kura uundwaji wa kampuni

Afisa Habari wa klabu ya Yanga SC Baraka Kizuguto (kushoto) akiongea na waandishi wa habari, kulia ni Lawrence Mwalusako -Kaimu Katibu Mkuu
UONGOZI wa klabu ya Young Africans leo umetangaza rasmi kuanza kwa zoezi la kupiga kura ya NDIYO  juu ya uundwaji wa kampuni au kura ya  HAPANA kwa kutoridhia klabu kuwa kampuni maazimio yaliyofikiwa katika mkutano mkuu uliofanyika Januari 16, 2013.
Akiongea na waandishi wa habari makao makuu ya klabu ya Yanga kaimu katibu mkuu Lawrence Mwalusako amesema zoezi hilo linanza leo kwa wanachama hai kufika makao makuu ya klabu na kupiga kura ya NDIYO au HAPANA na zoezi hilo litaendelea mpaka novemba 10, 2013.
Ifuatayo ni Taarifa kwa Wanachama na Waandishi wa Habari
 MAONI YA WANACHAMA YA KUUNDA KAMPUNI
Katika Mkutano wa Kawaida wa Wanachama wa YANGA uliofanyika tarehe 16 Januari 2013 Mwenyekiti kwa niaba ya Kamati ya Utendaji aliwapa Wanachama wafikirie mapendekezo ya YANGA kuwa Kampuni ama kutokuwa Kampuni kisha kuyawasilisha kwa Katibu Mkuu wa YANGA.
Nachukua nafasi hii kuwaambia Wanachama wa YANGA kuwa kuanzia leo tarehe 16 Oktoba 2013 mpaka tarehe 10 Novemba 2013, kutakuwa na sanduku moja (1) hapa Klabuni kwa ajili ya kukusanya kura za maoni ya Wanachama ya kuanzisha Kampuni (NDIYO) au kutokuwa Kampuni (HAPANA)
Kila Mwanachama hai atakuwa na uhuru wa kupiga kura na atalazimika kuja na Kadi yake ambapo itamzuia kupiga kura mara mbili au zaidi.
Zoezi hili ni muhimu kwa ajili ya maendeleo ya YANGA.

YANGA DAIMA MBELE NYUMA MWIKO
LAWRENCE MWALUSAKO

Mazito yaibuka kupigwa risasi kwa Ufoo Saro


MAZITO yameibuka kufuatia kupigwa risasi kwa Mtangazaji wa Independent Television (ITV), Ufoo Saro na mtu anayedaiwa ni mzazi mwenzake, Ateri Mushi, Risasi Mchanganyiko lina mkanda mzima.
Ufoo Saro akitolewa chumba cha upasuaji.
Ufoo alipigwa risasi na mwanaume huyo na kujeruhiwa tumboni na mguuni katika tukio lililotokea Oktoba 13, mwaka huu nyumbani kwa mama yake mzazi, Anastazia Saro, Kibamba, Dar es Salaam kufuatia kutoelewana kati ya wawili hao.
Katika tukio hilo la kutisha, Ateri pia alimuua kwa risasi mama wa Ufoo na kujiua mwenyewe na maiti zao kupelekwa Muhimbili.

MAZITO YALIYOIBUKA
Juzi, Shekilango, Ubungo jijini Dar, Risasi Mchanganyiko lilizungumza na rafiki mmoja wa marehemu Ateri aliyejitambulisha kwa jina moja la Urassa ambaye aliweka wazi mambo anayoyajua kuhusu marehemu kabla ya kujiua kwa risasi.
Alisema tangu mwaka huu (2013) uanze, marehemu Ateri alikuwa akilalamika kwamba, anampenda sana Ufoo lakini hamuelewielewi.


“Tangu mwaka huu ulipoanza nimekuwa nikiwasiliana na Ateri. Alikuwa akisema anampenda sana Ufoo lakini kama hamuelewielewi katika mambo fulani ya uhusiano.
“Alisema kukaa kwake mbali (Sudan) na mchumba wake huyo anahisi kama mambo yanakwenda kufikia mwisho wa uchumba wao. Kwa jumla Ateri alishajua nini atakifanya mwaka huu kuhusu uhusiano wake na yule mtangazaji maana maneno yake mengi yalikuwa ni malalamiko tu,” alisema Urassa.

MAREHEMU ALISEMA AMECHOKA KUISHI
Akienda mbele zaidi, Urassa alisema Septemba, mwaka huu marehemu alimpigia simu na kumwambia anahisi amechoka kuishi kwenye dunia hii yenye maumivu ya mapenzi kila kukicha.
“Nilimuuliza amechoka kuishi kivipi? Akanijibu anaona kuna mambo hayaendi sawa kama anavyotaka yeye kwa huyo mchumba wake. Lakini kwenye simu hakuniambia kama hayo mambo ni yapi? Ila nahisi ni mapenzi yao,” Urassa alizidi kutoboa.
 
Ufoo Saro.
ALIIBUA TABIA YA KUPENDA KUSALI
Katika mazungumzo na Urassa, pia alimgusia marehemu kwamba kwa siku za karibuni aliibua tabia ya kusali kila wakati kuliko siku za nyuma.
“Siku moja akiwa Sudan alinipigia simu, akasema anapenda kama mahali anapoishi kule pangekuwa na kanisa karibu ili awe anasali alfajiri, mchana na jioni lakini akaniambia kule hakuna makanisa.
“Nilimuuliza mbona amepanga kusali mara tatu zote hizo kwa siku, akanijibu binadamu tunatakiwa kujiandaa kwani saa yoyote roho inaweza kutoka,” alisema Urassa.

Baadhi ya wananchi na wanahabari wakiwa hospitalini kujua hali ya Ufoo.
MAREHEMU ALIKUWA AKILIA WIVU
Risasi Mchanganyiko: Kwa hiyo unawaza nini kuhusu marehemu kumuua mama mkwe wake na kumjeruhi mchumba wake kisha na yeye kujimaliza?
Urassa: Kwa kweli ninavyojua mimi ni wivu tu. Unajua yule alikuwa yuko kikazi Sudan, mchumba wake yupo Dar. Mfano siku moja aliniambia anatamani apate mtu wa kumfuatilia Ufoo kwenye nyendo zake za kila siku kwani anahisi anaibiwa japo hakuniambia kama ana uhakika.
DALILI ZA MAUAJI ZILIONEKANA MAPEMA
Kwa mujibu wa ndugu, licha ya kwamba hawakujua litakalotokea mbele, lakini baada ya kutokea ndiyo wamebaini kwamba marehemu Mushi alishabadilika roho muda mrefu.
Walisema uchangamfu na utani aliokuwa nao siku za nyuma alipokuwa akienda kuwatambelea viliisha ghafla kwani hivi karibuni alikuwa akienda, baada ya salamu hakuwa akiongeza neno.

LENGO LA MAREHEMU
Kwa mujibu wa watu waliofika nyumbani kwa mama Ufoo mapema, marehemu alionesha dalili za kuteketeza familia hiyo.
“Huyu bwana (marehemu) nahisi alitaka kutekeza familia, maana kabla ya kujiua yeye, alipiga risasi mtungi wa gesi ukiwa na nguo, ukalipuka. Sasa hapo unadhani lengo lake lilikuwa nini kama si kuiangamiza familia yote ya mzee Peter Saro?” alisema jirani mmoja kwa mtindo wa kuhoji.

UFOO ALILIJUA HILO
Habari zinasema baada ya Ufoo kupigwa risasi, akiwa anatambaa na damu zake tumboni aliwataka ndugu zake kutotoka kwani shemeji yao alikusudia kuwaua wote. Kauli ya Ufoo inakwenda sambamba na madai ya mzee aliyesema dhamira ilikuwa kuiangamiza familia hiyo.

ALIKUWA HAELEWANI NA BABA WA UFOO
Godluck Saro ni mdogo wa Ufoo, yeye akizungumza na gazeti hili juzi, nyumbani kwao, Kibamba, Dar alisema marehemu shemeji yake alikuwa haelewani kabisa na baba wa Ufoo, marehemu mzee Peter Saro aliyefariki dunia Julai 16, 2011 kwa shinikizo la damu.
“Kwanza shemeji alianza kufika hapa nyumbani baada ya baba kufariki, kabla ya hapo alikuwa hafiki maana walikuwa hawaelewani kabisa. Baba alikuwa anasema shemeji ni mkorofi, hawezi kuwa mume wa dada,” alisema kijana huyo.  

MAJIRANI WA KWA UFOO
Juzi, Risasi Mchanganyiko lilipata bahati ya kuzungumza na baadhi ya majirani wa kwa Ufoo, Mbezi jijini Dar es Salaam ambapo karibu wote walidai kusikia majibizano ya muda mrefu usiku wa kuamkia siku ya tukio.
“Tulisikia majibizano kwa muda mrefu ule usiku, lakini si ya wazi sana kiasi cha kumfanya mtu ajue nini kilikuwa kinaongelewa,” alisema jirani mmoja.
“Mimi alfajiri wakati wanaondoka niliwasikia, lakini sikujua wanakwenda wapi na nilijua wapo na amani tu kwani hakukuwa na mazungumzo ya ugomvi,” alisema jirani mwingine.

UFOO NA MAREHEMU
Ufoo yeye bado amelazwa Hospitali ya Muhimbili kwa matibabu. Yeye na marehemu walibahatika kupata mtoto mmoja wa kiume, Alvin Ateri Mushi.

MAZISHI YA WOTE
Juzi, ndugu wa marehemu Mushi walikutana katika kikao cha ratiba ya mazishi pale 92 Hotel, Shekilango - Ubungo, Dar ambapo walisema mwili wa marehemu utasafirishwa kabla ya Ijumaa kwenda kijijini kwao Uru, Moshi kwa mazishi.
Mwili wa marehemu Anastazia ulisafirishwa jana kwenda Machame, Moshi ambapo mazishi yake yalipangwa kufanyika leo katika eneo hilo.
Mwenyezi Mungu aziweke pema peponi roho za marehemu. Amina.


GPL

Hili siyo mchina?! Ni kati ya waliojaliwa bambataa!


Kama unaringia mchina, hapa je?

Ashanti United yaifumua Prisons, beki Tumba Sued azidi kumfukuzia Tambwe

Na Mahmoud Zubeiry, Chamazi
BAO la dakika ya 90 na ushei la Mwinyi Ally limeipa ushindi wa 2-1 Ashanti United dhidi ya Tanzania Prisons katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jioni hii Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
Mchezaji huyo aliyetokea benchi dakika ya 83 kuchukua nafasi ya Fakhi Hakika, alifunga bao baada ya kutokea kizazaa langoni mwa Prisons.
Hadi mapumziko, tayari timu hizo zilikuwa zimefungana bao 1-1, Prisons wakitangulia kupata bao dakika ya nne kupitia kwa John Matei na beki Tumba Sued akaisawazishia Ashanti dakika ya 21. Hilo lilikuwa bao la nne la Tumba ambalo linamfanya kuwa sambamba na akina Didier Kavumbagu, Kipre Tchetche na Peter Michael.
Ibrahim Isaka wa Prisons kulia akipambana na Iddi Silas wa Ashanti United leo Chamazi

Prisons inayofundishwa na kiungo wa zamani wa Simba SC, Jumanne Challe ilianza vyema mchezo huo dakika 10 za mwanzo, lakini baada ya hapo, upepo ukabadilika na Ashanti wakauteka mchezo.
Ashanti wangeweza kumaliza dakika 45 za kwanza wakiwa wanaongoza kama si kukosa mabao ya wazi.
Kipindi cha pili, Ashanti inayofundishwa na kiungo wa zamani wa Simba SC, Nico Kiondo iliongeza kasi ya mashambulizi langoni mwa Prisons na kukosa mabao zaidi ya matatu ya wazi.
Hussein Swedi aliyetokea benchi dakika ya 51 kuchukua nafasi ya Lusako Mwakyusa alikuwa mwiba mkali mbele ya mabeki wa Prisons, lakini alipoteza nafasi mbili za wazi na Paul Maona alipoteza nafasi moja.
Kwa ushindi huo, Ashanti inatimiza pointi nane baada ya kucheza mechi tisa na sasa inasogea hadi nafasi ya 10 kutoka ya 13.
Ashanti United; Daudi Mwasongwe, Hussein Mkongo/Anthony Matangalu dk46, Jaffar Gonga, Tumba Sued, Samir Ruhava, Iddi Silas, Mussa Nampaka, Fakhi Hakika/Mwinyi Allydk83, Paul Maona, Joseph Mahundi na Lusajo Mwakyusa/Hussein Swedi dk51.
Prisons; Beno David, Salum Mashaka, Laurian Mpalile, Lugano Mwangama, Nurdin Issa/Frank William dk82, Omega Seme, John Matei, Freddy Chudu, Peter Michael, Hassan Isaka/Jumanne Elfadhil dk71 na Julius Kwanga/Jeremiah Juma dk47.

Watu 44 wafa ajali ya ndege Laos

Uwanja wa Ndege wa Luang

ABIRIA  wote waliokuwa wameabiri ndege nchini Laos wamefariki baada ya ndege iliyokuwa imewabeba kuanguka Kusini mwa nchi.
Maafisa katika nchi jirani ya Thailand wamesema kuwa ndege hiyo ilianguka ndani ya mto Mekong.
Aidha inaarifiwa kuwa ndege hiyo ilianguka kutokana na hali mbaya ya hewa muda mfupi kabla ya kutua katika uwanja wa Pakse. Ndege hiyo ilikuwa inatoka katika mji mkuu wa Laos wa Vientiane ilipoanguka asubuhi ya leo.
Msemaji katika wizara ya mambo ya nje Sek Wannamethee alisema kuwa abiria 39 na wafanyakazi 4 walikuwa ndani ya ndege hiyo
Alisema rai watano wa Thailand walikuwa miongoni mwa waliofariki.

BBC

Israel Nkongo kuzihukumu Simba, Yanga kiingilio Buku 5 tu

Simba, Yanga kuhukumiwa Jumapili na Nkongo
Na Boniface Wambura
KIINGILIO cha chini kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Simba na Yanga itakayochezwa Jumapili (Oktoba 20 mwaka huu) kitakuwa sh. 5,000. Kiingilio hicho ni kwa viti vya rangi ya kijani ambavyo ni 19,648.
Kwa upande wa viti vya rangi ya bluu kiingilio ni sh. 7,000, viti vya rangi ya chungwa itakuwa sh. 10,000, VIP C kiingilio ni sh. 15,000, VIP B itakuwa sh. 20,000 wakati VIP A yenye viti 748 tu tiketi moja itapatikana kwa sh. 30,000.
Tiketi zitaanza kuuzwa siku moja kabla ya mchezo huo utakaoanza saa 10 kamili jioni katika vituo mbalimbali.
Vituo hivyo ni Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala, Uwanja wa Uhuru, na BMM Salon iliyoko Sinza Madukani.
Mechi hiyo namba 63 itachezeshwa na Israel Nkongo kutoka Dar es Salaam, ambapo atasaidiwa na Hamis Changwalu wa Dar es Salaam pia, na Ferdinand Chacha wa Bukoba. Mwamuzi wa akiba ni Oden Mbaga wa Dar es Salaam.
Kamishna wa mechi hiyo atakuwa John Kiteve kutoka Iringa wakati mtathmini wa waamuzi (referees assessor) ni Stanley Lugenge wa Njombe.
Wakti huo huo: Mechi tatu za Ligi Daraja la Kwanza (FDL) katika kundi A na C zimesogezwa mbele kutokana na viwanja vya Kambarage, Shinyanga na Nangwanda Sijaona, Mtwara kuwa na shughuli nyingine za kijamii.
Katika kundi A, mechi kati ya Ndanda na Transit Camp iliyokuwa ichezwe Oktoba 19 mwaka huu sasa itafanyika Oktoba 21 mwaka huu kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona.
Stand United na JKT Kanembwa zilizokuwa zicheze Oktoba 19 mwaka huu, sasa mechi hiyo ya kundi C itafanyika Novemba 2 mwaka huu Uwanja wa Kambarage mjini Shinyanga. Nayo mechi ya Mwadui na Polisi Dodoma iliyokuwa ichezwe kwenye uwanja huo Oktoba 26 mwaka huu imesogezwa hadi Novemba 3 mwaka huu.

Tuesday, October 15, 2013

Neymar aiongoza Brazil kuizima Zambia

Prediksi Skor Brasil vs Zambia 15 Oktober 2013
MABINGWA wa zamani wa Afrika, Zambia leo imekiona cha moto baada ya kutandikwa mabao 2-0 na wenyeji wa Fainali za Kombe la Dunia za mwakani Brazil katika pambano la kirafiki la kimataifa lililochezwa Beijing China.
Mabao ya kipindi cha pili kutoka kwa mtokea benchi Oscar katika dakika ya 59 akimalizia pasi murua ya Paulinho na Dede kuongeza jingine dakika ya 66 kwa pasi ya nyota mpya wa Barcelona, Neymar yaliizamisha Zambia ambayo imeondokewa na kocha wake  Herve Renard aliyeteuliwa kuinoa timu ya darajha la kwanza ya nyumbani Ufaransa.
Zambia ilicheza ikiwa na kocha wake mpya, Mfaransa mwingine Patrice Beaumelle.

Katika mechi nyingine; Korea ya kaskazini imeitungua Mali mabao 3-1, huku Japan ikilala 1-0 kwa Belarus, Ufilipino ikiitafuna Pakistan mabao 3-1.


Misri yatunguliwa bao la sita, Ghana yanusa fainali za Kombe la Dunia

Asamoah Gyan and  Wael Gomaa

MAFARAO wa Misri imeendelea kufa mjini Kumasi baada ya muda mchache uliopita wakitunguliwa bao la sita na Ghana katika pambano lao la awali la hatua ya mwisho ya mchujo wa Fainali za Kombe la Dunia kwa Bara la Afrika.
Pamoja na kufanya mabadiliko ya kuwaingiza akina Tshabalala, Misri wamepotea kabisa kwa wewnyeji ambao wanacheza watakvyo wakiwa na uhakika kwa asilimia kubwa kutinga fainali hizo za WC za 2014 zitakazofanyika Brazili.
Bao hilo la sita limetupiwa kimiani na Christian Atsu dakika ya 89 na kuonyesha dhahiri Ghana imeshaingiza mguu mmoja katika fainali hizo licha ya kwamba pambano lao la marudiano baina yao litafanyika Nov. 19.
Game ishaisha na Misri kuwa na kibarua cha kushinda nyumbani kwao mechi ya marudiano kwa mabao 5-0?! Tusubiri tuone!

Siri yafichuka viungo bandia vya binadamu vilivyonaswa Kenya

HATIMAYE mmiliki wa kasha la mizigo lililonaswa katika Bandari ya Mombasa likiwa na sanamu za vibwengo vya kutisha, amejulikana.
Kwa mujibu wa taarifa rasmi, kampuni ya 'Market Masters' wanaomiliki maduka ya Village Market jijini Nairobi wamekiri kuagiza shehena hiyo kwa sherehe zao za kila mwaka. 
Wakati huo huo, mwanasiasa Omingo Magara amekanusha kuagiza shehena hiyo na akaitaka halmashauri ya ushuru nchini KRA kumuomba msamaha mara moja.
Aidha katika habari nyingine zilizonaswa zinasema kuwa huenda pia sanamu hizo nyingine zingekuja nchini Tanzania.

 Xdeejayz

Jahazi la Misri lazidi kuzama, Gyan atupia bao jingine

Asamoah Gyan and  Wael Gomaa
Gyan akichuana na Wael Gomma

JAHAZI ya mafarao wa Misri linazidi kuzama baada ya muda mfupi uliopita Asamoah Gyan kutupia bao jingine la nne kwa Ghana wakati mchezo ukiingia dakika ya 60 hivi sasa.
Gyan katupia bao hilo la pili kwake katika mchezo huo unaochezwa mjini Kumasi katika dakika ya 54.
Hivi punde tena Ghana imepata bao la tano kupitia Sulley Muntari katika dakika ya 73kwa mkwaju wa penati, kuonyesha imepania kuidhiri Misri ambayo imekuwa ikiinyanyasa kila inapokutana nayo ambapo katika mechi 18 za awali za kukutana kwa timu hizo Ghana imeshinda mara nne na kufungwa 9 huku michezo mitano ikiisha kwa sare.

RAIS JAKAYA KIKWETE AKUTANA NA VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA WENYE WABUNGE LEO


Rais akiwa na viongozi wa vyama vya upinzani  leo ambaye alikutana nao

Rais Jakaya Kikwete akisalimiana na Tundu Lisu  nyuma yake mwenyekiti wa NCCR James Mbatia

Rais akiwa viongozi ikulu leo

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
MKUTANO kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete na viongozi wa vyama vya siasa vyenye uwakilishi Bungeni umemalizika Ikulu, Dar Es Salaam, muda mfupi uliopita leo, Jumanne, Oktoba 15, 2013 kwa pande hizo mbili kukubaliana kama ifuatavyo:

Moja , kwamba  vyama vyote vya siasa nchini vyenye mawazo, maoni na mapendekezo ya kuboresha Sheria ya Kurekebisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba viwasilishe mapendekezo yao haraka Serikalini ili itafute namna ya kuyashirikisha mapendekezo hayo katika marekebisho ya Sheria hiyo.

Pili, kwamba vyama vya siasa nchini, kama wadau muhimu katika mchakato wa Katiba Mpya, viangalie namna ya kukutana na kujenga mfumo wa mawasiliano na maridhiano wa jinsi kwa pamoja vitakavyosukuma mbele mchakato huo kwa maslahi mapana ya nchi yao na mustakabali wa taifa. Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) kimepewa jukumu la kuratibu jambo hilo ikiwa ni pamoja na kuandaa mkutano wa vyama hivyo na wadau wengine nchini.

Viongozi wa vyama vyama vya siasa waliokutana na Mheshimiwa Rais Kikwete ni Mheshimiwa Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa CUF; Mheshimiwa Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa CHADEMA na Mheshimiwa James Mbatia ambaye ni Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi.
Wengine ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Mheshimiwa Philip Mangula, Mheshimiwa Isaack Cheyo ambaye amemwakilisha Mwenyekiti wa Chama cha UDP Mheshimiwa John Cheyo na Mheshimiwa Nancy Mrikaria ambaye amemwakilisha Mwenyekiti wa TLP Mheshimiwa Augustine Mrema. Waheshimiwa John Cheyo na Mrema wako nje ya nchi.

Wengine ambao wameambatana na wenyeviti wao ni Mheshimiwa H. Mnyaa na Bwana Julius Mtatiro wa CUF, Waheshimiwa Tundu Lissu na John Mnyika wa CHADEMA na Bwana Martin Mng’ongo wa NCCR-Mageuzi.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

15 Oktoba, 2013

Mhandisi Bashir Mrindoko azidi 'kuula'



                             TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemteua Mhandisi (Eng.) Bashir J. Mrindoko kuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji kwa kumpandisha cheo kutoka nafasi ya Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo.

Aidha, Rais Kikwete amemhamisha Mhandisi Mbogo Paulo Futakamba, Naibu KatibuMkuu, Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kwenda Wizara ya Maji kujaza nafasi iliyoachwa na Mhandisi  Bashir Mrindoko.

Taarifa iliyotolewa Dar es Salaam leo, Jumanne, Oktoba 15, 2013, na Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue imesema kuwa vile vile Rais Kikwete amemteua Mhandisi Raphael Leyan Daluti kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika kuchukua nafasi ya Mhandisi Futakamba.

Kabla ya uteuzi  wake, Mhandisi Daluti alikuwa Mkurugenzi wa Idara ya Umwagiliaji na Huduma za Ufundi katika Wizara hiyo ya Kilimo, Chakula na Ushirika.

Balozi Sefue amesema katika taarifa yake kuwa uteuzi na uhamisho huo umeanza Oktoba 13, mwaka huu, 2013.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.

15 Oktoba, 2013

Ghana yaikoboa Misri 3-1 ni mapumziko kwa sasa

StarAfrica
Ghana-Black Stars

MABINGWA wa zamani wa Afrika Ghana, ikiwa nyumbani mpaka sasa wakati wa mapumziko inaoongoza kwa mabao 3-1 dhidi na Mafarao wa Misri katika pambano la awali la hatua ya mwisho ya mtoano kuwania Fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2014.
Mkali Asamoah Gyan alianza kuwashtua mabingwa wa kihistoria wa Afrika, Misri kwa bao la dakika nne kabla ya beki wa Misri Wael Gomma kujifunga bao katika harakati za kuokoa mpira uliopigwa na Michael Essien na kuipa Ghana uongozi wa mabao 2-0 kwenye dakika ya 22.
Hata hivyo mkongwe Mohammed Aboutrika aliipunguza machungu kwa kufunga bao la Misri kwa mkwaju wa penati dakika ya 41 kabla ya Abdulmajed Waris kufunga bao la tatu dakika moja kabla ya mapumziko.
Tutaendelea kuwaletea matokeo juu ya mpambano huo,. licha ya kufahamu wapo wengine wanaoufuatilia 'live' kupitia kwenye runinga.

Ashanti United kuendeleza maajabu kesho Chamazi?

* Inaikaribisha Prisons, TFF takabidhi kitanda cha Upasuaji

Kikosi cha Ashanti United
Na Boniface Wambura

LIGI Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Oktoba 16 mwaka huu) kwa mechi moja kati ya Ashanti United na Tanzania Prisons itakayochezwa Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam kuanzia saa 10 jioni. Nayo Ligi Daraja la Kwanza (FDL) nayo inaendelea kesho (Oktoba 16 mwaka huu) kwa mechi moja ya kundi A ambapo Polisi Dar es Salaam itakuwa mwenyeji wa Tessema kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam. Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limekabidhi kitanda cha upasuaji kwa Hospitali ya Rufani ya Manispaa ya Temeke, ikiwa ni sehemu ya mchango wake kwa jamii.
Makabidhiano hayo yamefanyika leo (Oktoba 15 mwaka huu) kwenye ukumbi wa mikutano wa TFF ambapo Hospitali ya Temeke iliwakilishwa na Mwenyekiti wa Bodi ya hospitali hiyo James Syaga, Mganga Mkuu Dk. Amaani Malima na Matroni wa hospitali hiyo Deodata Msoma. Akikabidhi kitanda hicho chenye thamani ya sh. milioni 6.8, Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah alisema amefurahi kuwa ahadi ya kukabidhi msaada huo wa Hospitali ya Temeke umetimia licha ya kuchukua muda mrefu kutokana na ukweli kuwa fedha za kununulia kitanda hicho zinatokana na mchezo wa Ngao ya Jamii wa mwaka jana kati ya Simba na Azam FC. Alisema uamuzi wa kuiteua Hospitali ya Temeke ulitokana na ukweli kuwa pamoja na kwamba ofisi za TFF ziko wilayani Ilala, shughuli nyingi kubwa za Shirikisho linafanyika kwenye Manispaa ya Temeke na hivyo hospitali hiyo hufanya kazi kubwa ya kuhudumia watu mbalimbali wanaopata matatizo wakati wa michezo ya mpira wa miguu. Naye Mganga Mkuu wa Hospitali, Dk. Malima aliishukuru TFF kwa kutimiza ahadi yao na kwamba msaada huo umekuja wakati muafaka kwa kuwa wana vyumba vitatu vya upasuaji, lakini ni viwili tu vilivyo na vitanda kwa hiyo kitanda hicho kitakamilisha chumba hicho kianze kufanya kazi. Alisema Hospitali yake sio tu inahudumia wagonjwa kutoka wilayani Temeke, bali kutoka hata Mkoa wa Mtwara na sehemu nyingine zinazozunguka wilaya hiyo. Mwenyekiti wa Bodi ya Hospitali, James Syaga, ambaye alisema anawakilisha watu wanaohudumiwa na Hospitali ya Temeke, alishukuru kwa msaada huo na kuiomba TFF kuendelea kuangalia uwezekano wa kusaidia hospitali hiyo.

Kamati ya Rufaa ya Maadili yakata mzizi wa fitina

* Yamtupa rupango mgombea miaka 20
* Shafii Dauda, Kidau wapeta
* Mchakato wa  kampeni sasa ruksa
Shafii Dauda aliyepeta, japo amelimwa saini ya Sh Mil. 1

Na Boniface Wambura
KAMATI ya Rufani ya Maadili ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imewaadhibu walalamikiwa watano kati ya saba baada ya kufanya mapitio (revision) kwa uamuzi wa Kamati ya Maadili kutokana na maombi ya Sekretarieti, huku Richard Julius Rukambura akifungiwa miaka 20 kujihusisha na mpira wa miguu.
Sekretarieti ya TFF iliwasilisha maombi ya mapitio kwa Kamati ya Rufani ya Maadili ili kupata mwongozo kwa vile kulikuwapo mkanganyiko kwenye uamuzi wa Kamati ya Maadili, hivyo kuiwia vigumu kwake kuutekeleza.
Uamuzi huo wa mapitio umesomwa leo jioni (Oktoba 15 mwaka huu) mbele ya waandishi wa habari na wajumbe wa Kamati hiyo wakiongozwa na Makamu Mwenyekiti Victoria Makani.
Rukambura amefungiwa miaka 20 baada ya kupeleka masuala ya mpira wa miguu katika mahakama za kawaida kinyume na Ibara ya 75 ya Katiba ya TFF na kifungu cha 73(3)(b) cha Kanuni za Maadili za TFF toleo la 2013. Adhabu yake itamalizika Oktoba 15, 2033.
Kabla ya kutoa adhabu hiyo, Kamati imejiridhisha kuwa Rukambura ni mwanafamilia wa TFF kwa vile aliwahi kuwa Mwenyekiti wa klabu ya Pamba ya Mwanza, na fomu zake za kuomba uongozi TFF ziliidhinishwa na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Shinyanga. Vilevile ni ‘Leadership Aspirant’ kwa mujibu wa kifungu cha 2(v) cha Kanuni za Utii za TFF toleo la 2013.
Pia imesema kwa Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo kusajili Katiba ya TFF inayokataza masuala ya mpira wa miguu kwenda katika mahakama za kawaida, na kutaja vyombo vya haki vitakavyoshughulikia masuala hayo (judicial organs), Kamati ya Maadili ilikosea kutomtia hatiani mlalamikiwa kwa kuegemea Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Naye Shaffih Dauda, Kamati imebaini kuwa mwanafamilia wa TFF kwani ni Mwenyekiti wa Bombom FC, fomu yake ya kuomba uongozi ilipitishwa na klabu ya Simba na pia ameshakuwa kiongozi katika ngazi mbalimbali ndani ya Chama cha Mpira wa Miguu Wilaya ya Kinondoni (KIFA), hivyo yeye ni ‘Leadership Aspirant’ kwa mujibu wa kifungu cha 2(v) cha Kanuni za Utii za TFF toleo la 2013.
Hivyo Dauda amepatikana na kosa la kimaadili kwa kutotekeleza maagizo rasmi ya TFF ya kutosambaza barua iliyotoka Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kwenda kwa Rais wa TFF, Leodegar Tenga.
Kamati ya Rufani ya Maadili imempa onyo kali na faini ya sh. milioni moja anayotakiwa kuilipa ndani ya siku tatu ambapo akishindwa kufanya hivyo atafungiwa mwaka mmoja. Adhabu hiyo imetolewa kwa mujibu wa kifungu cha 6(1)(a),(c) na (h) cha Kanuni za Maadili za TFF toleo la 2013.
Akilipa faini ataweza kuendelea na mchakato wa kugombea nafasi ya uongozi aliyoomba.
Nazarius Kilungeja amepatikana na kosa la kimaadili kwa mujibu wa kifungu cha 73(8)(a) cha Kanuni za Maadili za TFF toleo la 2013, kwani akijua kuwa ana adhabu ya kinidhamu ya kufungia miaka mitano na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Rukwa (RUREFA) iliyoanza 2009 alichukua fomu kuomba uongozi TFF.
Hivyo, amefungiwa miaka mitatu, adhabu ambayo itakwenda sambamba na ile ya RUREFA ambapo kifungo chake sasa kitamalizika Oktoba 15, 2016.
Sekretarieti ya TFF imepewa onyo kali kwa kupokea fomu yake ya kugombea na malipo wakati akiwa amefungiwa. Onyo hilo pia limetolewa kwa Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu Tanzania (TAFCA) Mkoa wa Rukwa kwa kuidhinisha fomu yake ya kugombea.
Naye Wilfred Kidao Mzigama ambaye ni mjumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF amepatikana na kosa la kimaadili kwa kuwa na nyaraka la Kamati ya Utendaji bila kibali na kukiuka taratibu za kuwasilisha malalamiko kwa mujibu wa Ibara ya 12(2) na Ibara ya 50(1) na (5) ya Katiba ya TFF.
Amepigwa faini ya sh. milioni moja anayotakiwa kuilipa ndani ya siku tatu ambapo akishindwa atafungiwa mwaka mmoja. Akitekeleza adhabu hiyo ataweza kuendelea na mchakato wa kugombea uongozi kwa nafasi aliyoomba.
Vilevile Kamati hiyo imetoa onyo kali kwa Sekretarieti ya TFF na wajumbe wa Kamati ya Utendaji kwa kushindwa kudhibiti nyaraka muhimu za vyombo vyao.
Pia Kamati ya Rufani ya Maadili imempata na kosa la kimaadili Kamwanga Tambwe kwa mujibu wa kifungu cha 73(8) cha Kanuni za Maadili za TFF toleo la 2013, kwa kuingia kwenye mchakato wa uchaguzi wakati ana adhabu ya kinidhamu inayomalizika 2014.
Hivyo, amepewa adhabu ya kufungiwa miaka mitatu ambayo itakwenda sambamba na ile ya kinidhamu na kumalizika Oktoba 15, 2016. Pia Sekretarieti ya TFF, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Ruvuma (FARU) na Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu Tanzania (FRAT) Mkoa wa Ruvuma wamepewa onyo kali kwa kupokea na kuidhinisha fomu zake za kugombea uongozi wakati akitumikia adhabu ya kufungiwa.
Kamati ya Rufani ya Maadili imewakuta kutokuwa na hatia ya makosa ya maadili kama ilivyobaini Kamati ya Maadili walalamikiwa Riziki Juma Majala na Omar Isack Abdulkadir, hivyo wana haki ya kugombea uongozi kwa kufuata Katiba na Kanuni za TFF.
Kwa mujibu wa kifungu cha 74(4) cha Kanuni za Maadili za TFF toleo la 2013, uamuzi wa Kamati ya Rufani ya Maadili hauna fursa ya rufani wala marekebisho kutoka chombo kingine chochote isipokuwa FIFA na Mahakama ya Usuluhishi wa Michezo (CAS).

Golden Bush yaifyatua Pugu Veterani 1-0

Golden Bush Veterani

ILE timu ya Veterans isiyofungika hapa Dar es Salaam na mikoa ya jirani ilitoa kipigo cha goli dhidi ya wanzetu Pugu Veterans. Goli liliwekwa wavuni Said Swedi baada ya kuna safi kabisa iliyopigwa na Shomari Pengo. Goli hili lilipatikana kipindi cha kwanza mara baada mashambulizi ya haraka haraka yakiongozwa na beki za kupanda na kushuka zikiongozwa na Shadrack Nsajigwa, Faraj huku kiungo kikikamatwa barabara na Ticotico akishirikiana na Said Sued 'Panucci'. Kama si uhodari wa kipa wa Pugu basi Golden Bush tungeibuka na goli zaidi ya 5. Hata hivyo matokeo tumeyafurahia kwasababu tumepata ushindi ambao ulikuwa na walazima.
Kesho Golden Bush tutakuwa Stakishari kwa mualiko wa Stakishari Veterans kucheza mechi ya kirafiki na kusherekea sikukuu pamoja na wenzetu. Baada ya sikukuu timu yetu itaelekea Zanzibar kwa mechi za kirafiki ili kufanya maadalizi ya mwisho kabisa ya gemu yetu ya kufunga mwaka dhidi ya Wahenga. Game hii uwa inakusanya wakazi wote wa Sinza na sehemu mbalimbali za jirani hivyo tunalazimika kufanya maandalizi ya nguvu sana.
Tuko kwenye mchakato wa kuomba udhamini wa game hiyo ya kufunga mwaka, tunashukuru mungu big Companies ambazo zitambua ushawishi mkubwa wa game hii zimeshaonyesha nia ya kutaka kutudhamini na kufunya matanagazo kwa kutumia wachezaji wengi maarufu wanaounda vikosi hivi viwili yaani Wahenga na Golden bush Veterans.

Asanteni
Onesmo Waziri 'Ticotico' Mchezaji Mwandamizi Golden Bush FC.

Ghana, Misri leo hapatoshi zinakutana kwa mara ya 19

Ghana Black Stars
MABINGWA wa zamani wa Afrika na waliowahi kuwa wawakilishi wa bara la Afrika katika Fainali za Kombe la Dunia, Ghana na Misri leo zinatarajiwa kupepetana katika pambano la awali la hatua ya mwisho wa mchujo wa kuwania fainali zijazo za Kombe la Dunia zitakazofanyika nchini Brazili mwakani.
Timu hiuzo zinaumana leo kukamilisha mechi tano za mkondo wa kwanza za mchujo wa mwisho kusaka timu tano za Bara la Afrika zitakaliwakilisha katika fainali hizo za dunia.
Mechi nne za awali zilichezwa mwishoni mwa wiki na kushuhudiwa matokeo ya kusisimua, Ivopry Coast ikiitambia Senegal mabao 3-1, Algeria ikizabuliwa mabao 3-2 na Burkina Faso ugenini, huku Nigeria ikiilaza Ethiopia iliyokuwa nyumbani kwao kwa mabao 2-1 na Cameroon ikivimbiwa na Tunisia na kutoka suluhu ya 0-0.
Pambano la Misri na Ghana zinakumbusha fainali za kombe la Afrika za mwaka 2010 ambapo Ghana walilala bao 1-0 kwa Mafarao. Timu hizo zinakutana leo ikiwa ni mara ya 19 katika michezo ya kimataifa ikijumuisha mechi za mshindano na ile ya kirafiki.
Katika mechi 18 za awali baina ya timu hizo Ghana imekuwa wanyonge ikibamizwa mechi 9 na kushinda michezo minne tu na kuambulia sare katika mechi tano.
Hata hivyo mechi hiyo inazikutanisha Ghana wakionekana wazuri zaidi, licha ya Misri nao kutishwa ikiundwa na wachezaji nyota vijana na kufanya iwe vigumu kutabirika atakayemtesa mwenzake kabla ya kurudiana tena mwezi ujao na kuamua hatma ya timu moja wapo katika uwakilishi wa fainali hizo za dunia.