STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, March 7, 2015

Wawili waumia Twiga Stars ikijianda kuvaana na Zambia

WACHEZAJI wawili wa timu ya Taifa ya wanawake, Twiga Stars, wameshindwa kufanya mazoezi kutokana na kuwa majeruhi kwenye Uwanja wa Karume, Ilala jijini Dar es Salaam

Wachezaji ambao ni majeruhi ni Fatuma Khatib anayecheza beki ya kulia na Ziada Ramadhani beki wa kushoto na waliumia kwenye mchezo wa kirafiki wa timu hiyo dhidi ya timu ya makipa ikiwa ni maandalizi ya mchezo wa kufuzu Kombe la Mataifa Afrika dhidi ya Zambia Machi 22, mwaka huu.

Akizungumzia hali zao kocha wa Twiga Stars, Rogasian Kaijage alisema kuwa wachezaji hao wanaendelea na matibabu na anatarajia wiki ijayo watakuwa wamepona.

“Leo hawakufanya mazoezi kwa sababu wana maumivu, lakini natarajia mapema wiki ijayo watakuwa wamepona kwani wanaendelea vizuri na matibabu”, alisema Kaijage

Kaijage alisema kutokana na program ya mazoezi aliyoendesha tangu timu hiyo ianze kambi mwishoni mwa mwezi uliopita anatarajiwa kuwa na mchezo mmoja wa kujipima nguvu katikati ya mwezi huu.

Twiga Stars ambayo imeweka kambi katika Hosteli za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) zilizopo ndani ya Uwanja wa Karume, Ilala, Dar es Salaam imeingia moja kwa moja katika hatua ya pili kucheza na Zambia kufuatia kuwa na matokeo mazuri katika msimamo wa viwango vya soka la wanawake barani Afrika.

Wachezaji waliopo kwenye kikosi cha Twiga ni Asha Rashid, Esther Chaburuma, Fatuma Bushiri, Fatuma Hassan, Fatuma Mustapha, Fatuma Omari, Eto Mlenzi, Mwajuma Abdallah, Sofia Mwasikili, Zena Khamis, Mwanahamisi Omar, Fadhila Hamad, Anastazia Anthony na Shelder Boniface.

Wengine ni Thereza Yonna, Happines Hezron, Amina Ally, Donizia Daniel, Fatuma Issa, Vumilia Maarifa, Maimuna Hamisi, Najiati Abbas, Stumai Abdallah, Zuwena Aziz, Irene Joseph, Dawa Haji Vuai, Belina Julius na Amina Ramadhani.

Spurs yailipua QPR kwao yaipumulia Liverpool

.
Muunganiko wa picha zilizochapishwa na Daily Mail zikionyesha mpambano wa Spurs na QPR ulivyokuwa leo
MSHAMBULIAJI Harry Kane amefunga mabao mawili jioni ya leo na kuiwezesha timu yake ya Tottenham Hotspur kupata ushindi muhimu ugenini dhidi ya QPR katika mechi ya kiporo cha Ligi Kuu ya England.
Kane ambaye amekuwa moto wa kuotea mbali alifunga mabao hayo katika kila kipindi na kuifanya Spurs kufikisha pointi 50 na kupaa hadi nafasi ya sita nyuma ya Liverpool iliwatanguliwa kwa pointi 51.
Mshambuliaji huyo kinda alifunga bao la kwanza dakika ya 34 kabla ya kuongeza la pili dakika ya 68 na wenyeji wanaopambana kuepuka kushuka daraja ilip[ata bao la kufutia machozi kupitia Sandro katika dakika ya 75.

Jonny Evance, Papiss Cisse wafungiwa England

http://i.dailymail.co.uk/i/pix/2015/03/06/2652640E00000578-2983103-Evans_left_and_Cisse_clash_near_the_half_way_line_at_St_James_Pa-a-1_1425663667950.jpgBEKI wa Manchester United, Jonny Evance na Mshambuliaji wa Newcastle United, Papiss Cisse, wamefungiwa kwa kitendo chao cha kutemeana mate katika pambano lililochezwa majuzi.
FA iliwafungulia mashtaka wachezaji hao baada ya awali mwamuzi wa pambano hilo kutoliona tukio halisi ya wachezaji hao kujigeuza 'nyota'kwa kutemeana mate.
Evance aliyekanusha shtaka lake amefungiwa mechi sita wakati mwenzake amefungiwa mechi saba ikiwamo sita ya kosa hilo na moja kwa kosa alililowahi kulifanya hivi karibuni la kumpiga mtu kiwiko.
Awali Cisse alikubali  mashitaka yaliyotolewa na Chama cha Soka cha Uingereza-FA kwa kumtemea mate beki wa Manchester United Jonny Evans.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 29, aliomba radhi kutokana na tukio hilo lakini amekanusha kama alifanya kwa makusudi.

Kiingilio Simba, Yanga Buku 7 tiketi zaanza kuuzwa

Yanga
Simba
TIKETI za pambano la kesho kati ya Simba SC na Young African litakaofanyika kwenye dimba la Uwanja wa Taifa kuanzia majira ya saa 10 kamili za jioni zimeanza kuuzwa kama ilivyotangazwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Mchezo huo wa kesho utachezeshwa na mwamuzi Martin Saanya kutoka Morogoro, akisaidiwa na Soud Lila (DSM) mshika kibendera wa kwanza, Florentina Zabron (Dodoma) mshika kibendera wa pili, Mwamuzi wa akiba Israel Mjuni (DSM), na kamisaa wa mchezo ni Ame Santimeya (DSM).
Viingilio vya mchezo huo, VIP A sh. 40,000, VIP B sh. 30,000, VIP C sh. 20,000, Rangi ya Machungwa (Orange) sh. 10,000, huku Rangi ya Bluu na Kijani ikiwa ni sh. 7,000.
Tiketi zimeanza kuuzwa leo Jumamosi saa 2 kamili asubuhi katika vituo vya, Karume (Ofisi za TFF), Mgahawa wa Steers (Posta Mpya), Oilcom (Buguruni), BigBon (Kariakoo), Olicom (Ubungo), Dar Live (Mbagala), Uwanja wa Uhuru, Kivukoni (Ferry) na Makumbusho (kituo cha mabasi).
Magari yenye vibali maalum ndiyo yatakayoruhusiwa kuingia ndani ya uwanja kesho Jumapili kwa kupitia barabara ya Mandela na Uwanja wa Uhuru, barabara ya Chang'ombe itafungwa kuanzia saa 12 kamili asubuhi.
TFF inawaomba, wapenzi, washabiki na wadau wa mchezo kununua tiketi katika vituo vilivyotajwa ili kuepuka kuuziwa tiketi bandia, ili kuimarisha ulinzi na usalama wa mchezo, mashabiki wenye mabegi, silaha, vilevi na chupa za maji hawataruhusiwa kuingia navyo uwanjani.
Aidha katika mchezo huo TFF itatoa ujumbe maalum kupitia kwa wachezaji kuhamasisha juhudi za Taifa za kuzuia mauaji dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi (Albino)

Azam yalipa kisasi JKT , Coastal yabanwa Tanga

Mfungaji wa bao pekee la Azam

BAO pekee kutoka kwa Mrundi, Didier Kavumbagu limeiwezesha mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara kulipa kisasi kwa JKT Ruvu.
Azam walipata ushindi huo kwenye uwanja wa Chamazi na kuifanya timu hiyo kuzidi kuwapumulia Yanga waliopo kileleni ambao kesho watashuka dimbani kuvaana na Simba.
Kavumbagu alifunga bao hilo lililokuwa la tisa kwake msimu huu katika ligi hiyo katika dakika ya 17 akiunganisha mpira wa krosi ya beki Shomari Kapombe na yeye kuufungwa kwa kichwa.
Azam imefikisha pointi 30, moja pungufu na ilizonazo Yanga yenye 31 ambao kesho watakuwa vitani dhidi ya Simba kwenye uwanja wa Taifa/ Kati mechi ya mkondo wa kwanza JKT Ruvu ndiyo iliyokuwa timu ya kwanzsa iliyovunja rekodi ya Azam ya kushinda mechi mfululizo 38 baada ya kuichapa bao 1-0.
Katika mchezo mwingine uliochezwa leo mabingwa wa zamani wa soka nchini, Coastal Union kwenye uwanja wao wa nyumbani wa Mkwakwani Tanga walilazimishwa sare ya mabao 2-2 na Kagera Sugar.
Mabao ya Coastal yalifungwa na Seleman Kibuta na Rama Salim wakati wageni walipata mabao yake kupitia kwa Atupele Green na Enock Kyaruzi.
Pambano jingine kati ya Polisi Moro dhidi ya Ruvu Shooting limeshindwa kufanyika mpaka siku ya Jumanne kutokana nna uwanja wa Jamhuri Morogoro kutumika na shughuli za sherehe za Siku ya Wanawake inayofikia kilele kesho Jumapili.

Friday, March 6, 2015

Berry Black ajiunga Mkubwa na Wanae atoa 'Byebye'

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEihS4zZARw-TfuBJsdn2gLhVxk0_0S7PM1Osw6yjrHX153vcpTeVQpNfb9Hz2xO_CNqAUi5ySCsVlj4JsJXCsSLvM_lmIEDHoKdGDnYfPP5svuamSbQ7jWLS6IPpjXBIVrJEAx2JcY__i8/s1600/photo+%252818%2529.JPG
Berry Black
MSANII nyota wa zamani wa kundi la 2 Berry, Berry Black amejiunga na 'lebo' ya Mkubwa na Wanae na tayari ametengeneza ngoma mpya iitwayo 'Byebye' alioimba akiwashirikisha wasanii wa Yamoto Band, Maromboso na Aslay.
Akizungumza na MICHARAZO, Mkurugenzi wa Kituo cha Mkubwa na Wanae, Said Fella alisema kuwa, msanii huyo ameingia mkataba wa kufanya kazi chini ya lebo yao na wamesharekodi wimbo mmoja uliotokana sambamba na video yake.
Fella alisema wimbo huo wa 'Byebye' umetengenezwa katika studio za Vibe Records chini ya mtayarishaji wake, Shirko na video imetengenezwa kupitia kampuni ya Kwetu Studio chini ya Msafiri Shaaban.
"Tumeamua kumrejesha hewani Berry Black kwa kumchukua Mkubwa na Wanae na tumeshatengeneza kazi moja ya 'Byebye' aliyoimba na madogo wa Yamoto na tutaiachia hadharani Ijumaa (leo) audio na video yake," alisema Fella.
Fella alidokeza kuwa baada ya kufanya utambulisho wa kazi hiyo ya Berry Black visiwani Zenji wakisindikiza onyesho la Yamoto Band, wataanza mipango ya kumtoa hadharani Ferooz nyota wa zamani na muasisi wa Daz Nundaz ambaye naye yupo Mkubwa na Wanae ambaye amesharekodi nyimbo mbili ambazo hakutaja majina yake

Yamoto Band kupeleka za uzunguni Zenji

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhdD6fCyy7ZBqhFtxtqvW5KpIIwHWzTVxWC8ihmF-NkUM-D0pXao8M7JfLrwK7djE5X5N3mWgOIuauilu7bH-Do-ghMxGXiA0Y5a4DH8oSeGyOGLbxMeun64ypd3T4AmQDqVXwRxUQepsy9/s1600/IMG_20150107_010322.jpgBAADA ya kurejea kutoka Uingereza walipoenda kutumbuiza mjini London kundi la Yamoto Band linatarajiwa kwenda kuonuyesha makali ya ugahibuni visiwani Zanzibar Jumapili hii.
Mkurugenzi wa kundi hilo, Said Fella aliliambia MICHARAZO kuwa, Yamoto wataenda kutambulisha nyimbo zao mpya na ubunifu waliotoka nao kwa Malkia katika onyesho litakalofanyika Ngome Kongwe, visiwani humo.
Fella alisema onyesho hilo litasindikizwa na wasanii mbalimbali kutoka TMK na wale wa visiwani humo.
"Tumerejea juzi kutoka Uingereza na Jumapili tunatarajiwa kuvuka maji kwenda Zanzibar kwa ajili ya uitambulisho wa mambo mapya ya Yamoto Band, onyesho litafanyika Ngome Kongwe na kusindikizwa na wasanii mbalimbali.
Katika hatua nyingi msanii Nikki Mbishi aliyetangaza hivi karibuni kuachana na fani ya muziki amevunja ukimya kwa kuibuka na wimbo uitwao 'Sihusiki nao' akimshirikisha mshindi wa BSS 2013, Walter Chilambo.
Nikki alitangaza kuachana na muziki na kuibua mjadala mkubwa ambao ulisababisha kushambuliwa na baadhi ya marapa wenzake wakidai 'amechemsha'.

Ronaldo amfunika Messi kwa utajiri duniani

Ronaldo
Messi
LONDON, England
MSHAMBULIAJI nyota wa Real Madrid, Cristiano  Ronaldo  ndiye mwanasoka tajiri zaidi duniani akiwa na utajiri wa kiasi cha Pauni Mil. 152 ikiwa ni Pauni 7 zaidi ya mpinzani wake Lionel Messi.
Baada ya kufanya vizuri mwaka 2014 na kushuhudia Ronaldo akiiwezesha Real Madrid kupata mafanikio katika Ligi ya Mabingwa wa Ulaya na kushinda tuzo ya Ballon d'Or, aliongeza tofauti ya nafasi ya utajiri wake na nyota huyo wa Barcelona na Argentina.
Kwa mujibu wa orodha ya matajiri iliyotolewa na Goal.com Alhamisi, Ronaldo na Messi ndio wanaotamba kwa utajiri zaidi kuliko wanasoka wengine kwa sasa katika soka la kulipwa.
Jumla ya utajiri wao, ambao unatokana na matangazo pamoja na mishahara na bonasi, ni zaidi ya ule alionao Neymar, anayeshika nafasi ya tatu akiwa na utajiri wa thamani ya pauni Milioni 97.9.
Zlatan Ibrahimovic wa Paris Saint-Germain na Sweden anautajiri wa Pauni Milioni 76.1, wakati Wayne Rooney wa Manchester United ndiye anayeongoza kwa utajiri kwa wachezaji Waingereza akishika nafasi ya tano kwa dola Milioni 74.6.
Kaka wa Brazil yeye kwa sasa anashikilia nafasi ya sita akiwa na pauni Milioni 69.6, akifuatia na Samuel Eto'o (pauni Milioni 63.1), Raul (pauni Milioni 61.6) na Ronaldinho (Milioni 60.2).
Kiungo wazamani wa England Frank Lampard, kwa sasa anaichezea Manchester City kabla yakwenda New York City katika Ligi Kuu ya Marekani, anakamilisha orodha ya 10 bora kwa kuwa nba utajiri wenye thamani ya pauni milioni 58.
Wachezaji wengine Waingereza waliopo katika 20 bora ni Rio Ferdinand (nafasi ya 12, pauni Milioni 52.2), Steven Gerrard (nafasi ya 14, pauni Milioni 46.4) na John Terry (nafasi ya 20, pauni Milioni 40.6).
Kuna wachezaji wengine wawili zaidi wa Man City katika orodha hiyo, pamoja na Yaya Toure katika nafasi ya 15 akiwa na utajiri wa pauni Milioni 44.9 na Sergio Aguero katika nafasi ya 19 na utajiri wa pauni Milioni 42.
Mwaka jana orodha ya matajiri wa Goal iliyotolewa ilibainisha kuwa Ronaldo alikuwa na utajiri wenye thamani ya pauni Milioni 122, huku Messi akimkimfuatia kwa nyuma kwa utajiri wa pauni Milioni 120.5.

Wachezaji wa Kano Pillars ya Nigeria wapigwa risasi


Kikosi cha Kano-Pillars ya Nigeria.
ABUJA, Nigeria
WACHEZAJI watano wa timu ya Kano Pillars wamejeruhiwa kwa risasi na watu wenye silaha katika shambulio lililofanywa na kundi la watu wakati wakisarifi kwenda Owerri kwa ajili ya kuanza kwa msimu mpya wa Ligi Kuu ya Nigeria.
"Wachezaji watano waliojeruhiwa kutokana risasi hizo ni pamoja na Gambo, Ogbonaya, Eneji Otekpa, Murtala Adamu, na Moses Ekpai," klabu hiyo iliandika katika mtandao wa Twitter. 
"Watu hao wenye silaha pia walichukua simu za mkononi na vitu vingine vya thamani kutoka kwa wachezaji ".
Kutokana na tukio hilo la uvamizi, mchezo wa Jumamosi dhidi ya Heartland ameahirishwa kwa muda usiojulikana.
Timu ya Kano ilikuwa ikisafiri kwa basi ikiwa na watu 25, wakiwemo wachezaji 18, wakati tukio hilo likitokea saa 7:15 mchana kwa saa za hapa.
Wachezaji watano waliojeruhiwa walipata matibabu katika hospitali ya rufaa ya Centre huko Lokoja.
Kano walikuwa wakijianda kutetea taji la Nigeria, ambapo walianza msimu kwa ushindi dhidi ya Al Malakia katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa wa Afrika raundi ya awali wikiendi iliyopita.
Hatahivyo, bado haijajulikana kama ratiba ya mabingwa Kano dhidi ya Moghreb Athletic Tetouane Machi 13 itaendelea kama ilivyopangwa.

VUMBI LA LIGI KUU BARA WIKIENDI HII LIPO HIVI:

Yanga
Azam
Mtibwa Sugar
Ndanda
Simba
VUMBI la Ligi Kuu Tanzania Bara linatarajiwa kuendelea tena kesho kwa mechi tatu kabla ya Jumapili jiji la Dar kusimama wakati wapinzani wa jadi nchini, Simba na Yanga kumaliza ubishi kwenye uwanja wa Taifa.
MICHARAZO imekuwekea ratiba ya ligi hiyo kwa siku ya kesho na Jumapili kama ifuattavyo na msimamo wa ligi ulivyo kwa sasa na wanaoongoza kwa ufungaji mabao.
Ratiba:
Kesho Jumamosi
Polisi Moro vs Ruvu Shooting
Coastal Union vs Kagera Sugar
JKT Ruvu vs Azam FCr

Jumapili
Mgambo JKT vs Ndanda FC
Mtibwa Suga vs Mbeya City
Simba vs Yanga

MSIMAMO LIGI KUU TANZANIA BARA:
                            P   W    D    L   F    A   GD Pts
01.  Yanga           15  09  04   02  21 08  13  31
02.  Azam            15  07  06  02  22  12  10  27
03.  Simba           16  05  08  03  20  12  08  23
04. Coastal Union16  05  07   04  12  10  02  22
05. Mtibwa Sugar 15  05  07  03  17  15  02  22
06. Kagera Sugar 16  05  06  05  12  13  -1   21
07. Stand Utd      17  05  06   06 16  18  -2   21
08. Ruvu Shooting17 05  06   06 12  14  -2   21
09. JKT Ruvu        16  05  05  06 14  15   -1  20
10. Polisi Moro      16  04  07  05 13  15   -2  19
11. Ndanda Fc      16  05  04  07 15  19   -4  19
12. Mbeya City     16  04  06  06  11  15   -4  18
13. Mgambo JKT  14  04  02  08  07  20  -13 14
14. Prisons          17  01  10   06  10  20  -10 13
Wafungaji:
8- Didier Kavumbagu(Azam)
7- Rashid Mandawa, Absalim Chiidebere (Kagera Sugar)
6- Samuel Kamuntu (JKT Ruvu), Ame Ali (Mtibwa), Simon Msuva (Yanga)
5- Danny Mrwanda (Yanga), Kipre Tchetche (Azam),Emmanuel Okwi (Simba)
4- Rama Salim (Coastal), Ibrahim Hajibu (Simba), Nassor Kapama (Ndanda), Heri Mohammed,(Stand Utd), Yahya Tumbo (Ruvu Shooting)
3- Ally Shomari (Mtibwa),  Jacob Massawe (Ndanda), Frank Domayo (Azam), Malimi Busungu (Mgambo), Atupele Green (Kagera), Amissi Tambwe, Mrisho Ngassa (Yanga)
2- Shaaban Kisiga, Dan Sserunkuma, Elias Maguli (Simba), Salum Kanoni, (Kagera Sugar), Aggrey Morris (Azam),  Najim Magulu, Jabir Aziz (JKT Ruvu), Jerry Tegete, Coutinho (Yanga), Ibrahim Kihaka (Prisons), Mussa Mgosi (Mtibwa), Mussa Said (Stand Utd), Ally Nassor (Mgambo), Nicolaus Kabipe (Polisi), Peter Mapunda (Mbeya City) Lutimba Yayo (Coastal Union)

Dokii afichua kilichomkimbiza Yanga kwenda Azam

Dokii
MUIGIZAJI nyota aliye pia muimbaji wa muziki, Ummy Wenceslaus 'Dokii' ambaye alikuwa mmoja wa mashabiki wakubwa wa Yanga amefichua siri ya kutangaza kuitema timu hiyo na kujiunga kuishangilia Azam FC.
Akizungumza na MICHARAZO katika mahojiano maalum kwa njia ya simu, Dokii alisema ameamua kuitosa Yanga ambayo keshokutwa itashuka dimbani kuvaana na Simba kutokana na kuvutiwa na uwezo wa wachezaji pamoja na viongozi wa klabu hiyo ya Azam.
"Kilichonifanya kuitosa Yanga na kuhamia Azam ni ubora wa wachezaji na uongozi wa jumla," alisema.
Alipoulizwa ataendelea kuishabikia Azam hata kama imeng'oka michuano ya kimataifa alipoibukia kwa mara ya kwanza wakati timu hiyo ikiumana na El Merreikh na kushinda 2-0, Dokii alisema Azam milele kwake kwani ni moja ya timu yenye muono wa mbali wa kimaendeleo.
"Vyovyote iwavyo mimi na Azam, nitaishangilia na kuipa sapoti kokote ilipo hata kama hatuendelei michuano ya kimataifa," alisema Dokii.
Dokii aliyekuwa miongoni mwa wasanii wanaoizimikia Yanga alionekana 'bize' uwanja wa Azam akishangilia timu hiyo akijipamba 'ki-Azam' tofauti na alivyozoeleka na hata kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi alikuwa akiishangilia timu yake ya Yanga iliyotoka robo fainali.

Nyota wa Filamu anusurika kifo ajali ya ndege

http://img2.timeinc.net/people/i/2004/04/30anniversary/sexiestman/hford.jpg 
NYOTA wa filamu wa Hollywood, Harrison Ford, anapatiwa matibabu katika Hospitali moja mjini Los Angels baada ya ndege yake kuukuu kuanguka katika uwanja wa Gofu.
Mcheza filamu huyo mwenye umri wa miaka 72 alikuwa akiendesha ndege hiyo mwenyewe.
Ndege hiyo ndogo ilinasa kwenye mti wakati ilipokuwa ikitua kwa dharura.
Mashuhuda wa ajali hiyo wamesema Harrison Ford alikuwa amejeruhiwa, akionekana kuwa na damu iliyotapakaa usoni.
Matabibu wamesema Ford anaendelea vizuri na kuwa hali yake itatengemaa kabisa.
Muigizaji huyo aliyeanza kuigiza tangu mwaka 1966, amewahi kujeruhiwa wakati wa kuigiza filamu zake ikiwamo mgongo mwaka 1983 na baadaye kifundo cha mguu Juni mwaka jana akiitengeneza  picha iitwayo 'Star Wars: The Force Awakens'.
Ntyota huyo anasifika kwa uigizaji wake makini wa filamu zilizompa ujiko miongoni wa filamu hizo ni American Graffiti, Star Wars, Apocalypse Now, The Frisco Kid, The Empire Strikes Back, Raiders of the Lost Ark, Blade Runner, Return of the Jedi, Indiana Jones and the Temple of Doom na Witness.
Nyingine ni; The Mosquito Coast, Working Girl, Indiana Jones and the Last Crusade, Regarding Henry, Patriot Games, The Fugitive, Clear and Present Danger, Sabrina, Air Force One, Six Days Seven Nights, What Lies Beneath, K-19: The Widowmaker, Indiana Jones and the Kingdom of the Crystal Skull, Extraordinary Measures, Cowboys & Aliens, 42, Ender's Game na Paranoia.

SIKILIZA NGOMA MPYA YA SNURA ft NAY WAMITEGO- HAWASHI

Thursday, March 5, 2015

MATAJIRI WA ARSENAL 'FUNIKA BOVU' EPL

MMOJA wa wamiliki wa klabu ya Arsenal, Alisher Usmanov ndiye anaongoza orodha ya mabilionea duniani ambao wanamiliki klabu za Ligi Kuu nchini Uingereza.
Usmanov ambaye anamiliki hisa asilimia 15 za klabu hiyo, anashilikilia nafasi ya 71 katika orodha za matajiri duniani ambazo zimetolewa na gazeti la Forbes mwaka huu.
Anayefuata ni bilionea wa klabu ya Queens Park Rangers-QPR Lakshmi Mittal anayeshika nafasi ya 82 kwa kuwa na utajiri unaokadiriwa kufikia paundi bilioni 8.8.
Mmiliki wa klabu ya Chelsea Roman Abramovic yuko katika nafasi ya 137 kwa akiwa na urajiri unaokadiriwa kufikia paundi bilioni 5.9 akifuatiwa na mmiliki mwingine wa Arsenal Stan Kroenke anayeshika nafasi ya 225 akiwa na urajiri unaofikia paundi bilioni 4.1.
Wengine ni mmiliki wa Tottenham Hotspurs Joe Lewis anayeshika nafasi ya 277 kwa utajiri wa paundi bilioni 3.5, Mike Ashley wa Newcastle nafasi ya 318 kwa utajiri wa paundi bilioni 3.2 na mmiliki wa Leicester City Vichai Srivaddhanaprabha anayeshika nafasi ya 714 akiwa na utajiri wa paundi bilioni 1.8.
Mmiliki wa Stoke City Denise Coates yuko katika nafasi ya 737 akimiliki utajiri wa paundi bilioni 1.6 akifuatiwa na mwanahisa wa Arsenal Farhad Moshiri anayeshika nafasi ya 894 huku tajiri wa Liverpool John Henry akifunga orodha ya 10 bora kwa kushinka nafasi ya 1190 katika orodha ya matajiri duniani.
Orodha kamili ipo hivi hapo chini:
Na.       JinaKlabuUtajiri
71Alisher UsmanovArsenal (15%)£9.4bn
82Lakshmi MittalQPR (33%)£8.8bn
137Roman AbramovichChelsea£5.9bn
225Stan KroenkeArsenal£4.1bn
277Joe LewisTottenham£3.5bn

318Mike AshleyNewcastle£3.2bn
714Vichai SrivaddhamaprabhaLeicester City£1.8bn
737Denise CoatesStoke City£1.6bn
894Farhad MoshiriArsnenal (15%)£1.4bn
1190John HenryLiverpool£1bn

HUYU NDIYE KIJANA TAJIRI KULIKO WOTE AFRIKA

* NI MTANZANIA, MBUNGE MOHAMMED DEWJI
http://www.bongo5.com/wp-content/uploads/2013/07/Mohammed-Dewji.jpg
Mohammed Dewji kafunika Afrika
MFANYABIASHARA maarufu nchini Tanzania ambaye pia ni  Mbunge wa Singida Mjini (CCM), Mohammed Dewji kwa mara ya kwanza ameingia kwenye orodha ya mabilionea 29, akiwa tajiri kijana kuliko wote barani Afrika.
Jarida la Forbes la Marekani limemtaja Dewji (39), katika nafasi ya 24 ya matajiri wa Afrika akiwa na utajiri wa Dola 1.3 bilioni za Marekani (Sh2.34 trilioni) unaotokana na biashara mbalimbali anazozifanya kupitia kampuni yake ya Mohammed Enterprises (Metl Group).“Dewji alibadilisha biashara aliyoanzisha baba yake kutoka uuzaji bidhaa na kuwa na viwanda vya Metl,” inasema sehemu ya habari inayomuhusu bilionea huyo Mtanzania .
“Alinunua viwanda vya nguo na mafuta vilivyokuwa vinamilikiwa na Serikali kwa bei ndogo na kuvifanya viwe na faida zaidi kwa kutumia mtindo wa kisasa wa menejimenti,” inaongeza ripoti hiyo.
Metl ina viwanda vya kutengeneza nguo na bidhaa nyingine za matumizi ya binadamu vikiwamo vyakula, sabuni na vinywaji. Pia ina mapato yanayozidi Dola 1.4 milioni za Marekani (Sh2.5 trilioni) kwa mwaka.
Katika kampuni hiyo, ambayo imekuwa na ushindani dhidi ya kampuni kubwa nyingine kama Said Salim Bakhresa, Dewji anamiliki asilimia 75 ya hisa zote.
Kwa mujibu wa tovuti yake, Metl inaendesha shughuli za uagizaji na usafirishaji bidhaa kutoka na kwenda nje, uzalishaji unaohusisha nguo, vinywaji na vyakula, usagaji nafaka, nishati na petroli na utengenezaji baiskeli.
Pia inahusika na huduma za simu, fedha, kilimo na pia ina kitengo cha kontena kwenye Bandari ya Dar es Salaam.
Dewji anashika nafasi mbili juu zaidi ya kada maarufu wa CCM na aliyekuwa mbunge wa Jimbo la Igunga, Aziz Rostam (50) aliyewekwa nafasi ya mwisho.
Rostam amefungana nafasi ya 26 na mabilionea wa Nigeria, Abdulsamad Rabiu na Femi Otedola wenye utajiri wa Sh1.8 trilioni kila mmoja.
Orodha hiyo ya 29 bora inaoongozwa na bilionea wa Nigeria, Aliko Dangote akiwa na utajiri wa Dola 15.7 bilioni za Marekani (Sh28.2 trilioni), kiwango ambacho ni mara moja na nusu ya bajeti ya Serikali ya Tanzania ya mwaka 2014/15.
Forbes linamtaja Rostam kuwa na utajiri wenye thamani ya Dola 1 bilioni za Marekani (Sh1.8 trilioni), kiwango ambacho kimebaki pasi na mabadiliko kutoka orodha ya mwaka jana. Rostam anamiliki asilimia 35 ya hisa katika kampuni ya huduma za simu za mkononi ya Vodacom.

NABII HUYU KIBOKO! AWATUNDIKA MIMBA MADEMU ZAIDI YA 20


Wanawake na mabinti waliopewa mimba na nabii/mchungaji huyo.

HABARI kutoka Nigeria zinaripoti kuwa wanawake zaidi ya 20 wakiwemo wake za watu na mabinti wamepachikwa mimba na mtu anayejifanya 'Nabii' ambaye aliwadanganya kuwa aliambiwa na Roho Mtakatifu kufanya nao mapenzi.
 
 Nabii huyo alifahamika kwa jina la Timothy Ngwu ambaye ni mchungaji kiongozi wa kanisa la Vineyard Ministry of the Holy Trinity huko Enugu tayari anashikiliwa na jeshi la polisi la jimbo hilo kwa kosa la kuwalazimisha kufanya nao mapenzi na wanawake hao.

Mchungaji huyo amedai anatii wito wake wa kinabii na kiroho alioitiwa na kufanya sawa na mapenzi ya Mungu kwa kuwapa mimba yeyote yule aliyechaguliwa na kuwekwa wazi na Roho mtakatifu bila kujali kama mwanamke huyo ameolewa ama la alisema msemaji wa jeshi la polisi Enegu kamanda Ebere Amaraizu akitoa taarifa kwa vyombo vya habari na kudai kwamba mwanamke akijifungua mtoto hubakia kwenye huduma hiyo na mzazi wake.

Taarifa kutoka kwa familia za mchungaji huyo zinasema mkewe aitwaye Veronica Ngwu ambaye alichoshwa na tabia ya mumewe hasa alipompa ujauzito mdogo wake na kuamua kumripoti Polisi. 
 
Kwa upande wa kaka wa mtuhumiwa ambaye hakutaka jina lake lifahamike ameiambia Vanguard report kwamba amekuwa akimuonya kaka yake juu ya tabia yake kwa muda mrefu lakini hakutaka kusikiliza, amesema gadhabu ya Mungu imeshuka juu ya kaka yake.


"Ngoja niwaambie hasira ya Mungu imemshukia kaka yangu tumekuwa tukimuonya kila siku kuacha alichokuwa akifanya amejaza boma letu kwa kuzaa watoto bila uangalifu na kutuambia tunamuonea wivu kwasababu anafanya maagizo ya Mungu" alisema kaka mtu.
 
Aliongeza "kwamba angalia majengo yote ya kanisa ameyageuza kuwa ya kwake kwa jina la huduma yake, alimfukuza mkewe wa ndoa waliyezaa naye watoto watatu na kuanza kuwajaza mimba wake za watu na mabinti wadogo, we angalia boma lote limejaa watoto wa jinsia zote alilalamika kaka huyo"

Aidha kaka huyo amesema waumini wote wa kanisa la kaka yake ni wapumbavu kwa sababu mwanamke hawezi kumuacha mumewe na kwenda na mwanaume mwingine kwa kisingizio cha kwenda kumuabudu Mungu na kufanya zinaa, na kudai hawezi kujiingiza katika tatizo hilo, "Vero amefungua msaada kwa wamama hao ngoja wayamalize na polisi ila nataka huduma hii ifungwe kabisa" alisema

Ngwu ameiambia NaiJ kwamba kaka yake ana wake wapatao watano na watoto 13 pamoja na wake za watu kwa madai ya kufuata mapenzi ya Mungu. 
 
Amedai hajawahi kufanya mapenzi na wake za watu ila amefanya hivyo endapo waume zao wamekubaliana na ombi la Roho mtakatifu. Calista Omeje na Assumpta Odo ni wanawake ambao waliawaacha waume zao ili kuishi na nabii huyo kwakuwa ilikuwa ni upako wa kinabii wa mchungaji huyo.

Calista ambaye ana watoto 10 na mumewe alipewa mimba na mchungaji huyo ila mtoto alikufa, amesema mwanamke huyo alimkabidhi mchungaji huyo binti yake huku Odo naye amesema mchungaji huyo amempa mimba yeye na binti yake.
Chanzo  Wilfredasuqu

Fainali Kombe la Mfalme Hispania ni Barcelona vs Atletico Bilbao

Barcelona celebrate
Neymar akipongezwa na Messi baada ya kufunga huku Suarez akiwajongelea kwa furaha
Lionel Messi
Messi akiwajibika
KLABU za Barcelona na Athletic Bilbao zinatarajiwa kuvaana kwenye pambano la Fainali za Kombe la Mfalme (Copa del Rey) litakalochezwa Mei 30.
Timu hizo zimefuzu hatua hiyo baada ya kufanikiwa kushinda mechi zao za marudiano ya Nusu fainali ya michuano hiyo, Barcelona wakiichapa wenyeji wao Villarreal kwa mabao 3-1. Mabao hayo yaliwekwa kimiani na Neymar aliyefunga mawili na jingine la Luis Suarez.
Ushindi huo umeifanya vijana hao wa Luis Enrique kupenya kwa jumla ya mabao 6-2, kwani katika pambano lililochezwa Febaru 11 walishinda idadi kama hiyo.
Wapinzani wao Athletic Bilbao ikaisasambua Espanyol mabao 2-0 na kusonga mbel kwa jumla ya mabao 3-1 kwani katika pambano lao la awali walishindwa kutambiana kwa kutoka sare ya 1-1.

GHARIKA! MVUA ZAUA WATU 42, WENGINE 96 WAJERUHIWA

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEh14yp-wBksDb2aWv2jU5eXK_DLVeBzzxVVj9B4xyYWtfoly_eXgTWQ8ELZGAP48SidmeqnRD_Biaxg2Bjy9ypcZYYhQuJmjZ2I1xFmTVTu0appX1mnT0Y_bsxNlvKnnRquRUnSSfGXvmA/s1600/kahama+1.jpg
Moja ya nyumba iliyoporomoshwa na mvua zinazoendelea kunyesha
Na Mwandishi Wetu, Kahama
ZAIDI ya watu 40 wameripotiwa kufariki mjini Kahama, Shinyanga kutokana na mvua kubwa huku wengine wapatao 96 wameripotiwa kujeruhiwa na kupoteza makazi.
Aidha mikoa ya Kilimanjaro, Morogoro, Pwani na Tabora mvua kama hizo zenye kuambatana na upepo mkali zimeleta uharibifu mkubwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) imeonya huenda mvua hizo za mawe zikaendelea kunyesha mfululizo na watu wawe na tahadhari.
Awali iliripotiwa kuwa 39 wamefariki dunia na wengine zaidi ya 69 wamejeruhiwa baada ya nyumba zao kuwaangukia na kuwafunika usiku wa kuamkia leo kufuatia mvua kubwa iliyonyesha wilayani Kahama, mkoani Shinyanga. 
Taarifa hizo zilizothibitishwa na Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya amesema mvua hiyo kubwa iliambatana na upepo mkali, hivyo nyumba nyingi zilianguka na nyingine kuezuliwa na kuharibiwa kabisa.
 Bw. Mpesya amesema hadi majira ya asubuhi walikuwa wamefanikiwa kupata miili ya watu 39 waliopoteza maisha baada ya kufukua nyumba nyingi, na majeruhi wamekimbizwa hospitali ya wilaya kwa matibabu zaidi. 
Mkuu huyo wa Wilaya amesema nyumba nyingi zimeanguka na zoezi la kutafuta watu waliojeruhiwa au kupoteza maisha bado linaendelea kwa kasi.
Hata hivyo idadi ya waliopoteza maisha na waliojeruhiwa ilizidi kuongezeka kadri shughuli za uokozi ilipokuwa inaendelea na kuleta simanzi kubwa kwa taifa.

Aibu! Watanzania 443 wanaswa na dawa za kulevya ughaibuni

http://api.ning.com/files/NWvFMlVPFcx5SxCYa4RDXr0NMMnq6gRcpSfjyInB*mxa*WWMz0x1MendQbi7EkT588mJKfgz3DjGsbaCvcR6Q0AgTJ03rTXA/Pipi.jpg
Baadhi ya dawa zilizowahi kunaswa nchini
http://api.ning.com/files/NGHxxVgVd17fuWKh*v1l7*4NyFc2GYTkLp2o69tup7nXuo4nQgBPU2OuQ-it1jCnSiXwKCGVj6KQ*c8ylkYzAyOgRGizDiJb/IMG_0532.jpgBIASHARA ya Dawa za Kulevya bado ni kizungumkuti kwa taifa la Tanzania, kwa raia wake wapatao 443 kunaswa katika mataifa mbalimbali duniani.
Hata hivyio ni angalau udhibiti juu ya biashara hiyo nchini imeanza kuonekana kwa kunaswa kwa 'unga' upatao tani 2.3 (kilo 2300).
Imeelezwa kuwa Tanzania imefanikiwa kudhibiti zaidi ya tani 2.3 za dawa za kulevya zilizokamatwa na vikosi vya wanamaji huku za zaidi ya watanzania 443 wamekamatwa katika nchi mbalimbali duniani wakihusishwa na usafirishaji na utumiaji wa dawa za kulevya. 
Akizungumza jijini Dar es Salaam katika uzinduzi wa ripoti ya dawa za kulevya ya Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na Kudhibiti Dawa za Kulevya na Makosa ya Jinai (UNODC) Mwakilishi kutoka Tume ya Kudhibiti Dawa za Kulevya nchini Tanzania Bw. January Ngisi amesema tatizo la dawa za kulevya katika ukanda wa Afrika Mashariki bado ni kubwa na kueleza kwa kushirikiana na vyombo vya dola wameridhia mikataba ya kupunguza upatikanaji wa dawa za kulevya.
Kwa upande wake Afisa Uhusiano wa Umoja wa Mataifa nchini Tanzania Bi. Stela Vuzo amesema ripoti hiyo imeitaka serikali kuwasaidia watoto wasijingize katika matumzi ya dawa za kulevya ambazo zimekuwa na madhara makubwa ikiwemo athari za kiafya na iwekwe mikakati itakayotokomeza uingizwaji na utumiaji wa dawa za kulevya nchini.

Arsenal, Chelsea, Man U zatamba ugenini, Liverpool moto chini!

Adrian dives in vain as Hazard's header sails past the Spanish shot stopper and into the back of West Ham's net
Hazard akiifungia Chelsea bao pekee dhidi ya West Ham
Sanchez celebrates doubling Arsenal's lead mid way through the second half at Loftus Road
Sanchez wa Arsenal akishangilia bao la pili alilolifunga yeye wakati wakiizamisha QPR
David Silva shoots the ball past Leicester goalkeeper Mark Schwarzer to give Manchester City the lead just before half-time
Silva akiwatungua Leichester City
Ashley Young fires home the winner for Manchester United to earn his side a valuable three points at Newcastle 
Ashley Young akifunga bao la 'jioni' kuipa ushindi murua Manchester City ugenini dhidi ya Newcastle Utd
MABAO mawili kupitia kwa Olivier Giroud na Alexis Sanchez yameiwezesha Arsenal kuikomalia nafasi ya tatu, huku Chelsea wakijiimarisha kileleni mwa msimamo wa Ligi Kuu ya England baada ya zote kupata ushindi katika mechi zao zilizochezwa usiku wa jana.
Arsenal ikiwa uwanja wa ugenini nyumbani kwa QPR ilipata mabao hayo katika kipindi cha pili na kuizamisha wenyeji wao kwa mabao 2-1, huku Chelsea nao wakipata ushindi ugenini mwa West Ham United kwa bao 1-0 bao lililofungwa Eden Hazard akimalizia kazi ya Ramires.
Katika pambano la Arsenal na QPR, Giroud alianza kuifungia timu yake bao dakika ya 64 kabla ya dakika nne baadaye Sanchez kuongeza la pili na wenyeji kuja kupata la kufutia machozi dakika ya 82 kupitia kwa Charlie Austin.
Kwa ushindi iliyopata Chelsea imeifanya mabingwa hao wa Kombe la Ligi kufikisha pointi 63, huku wapinzani wao wakisaliwa na pointi 39 na kukamata nafasi ya 10 huku Arsenal wakiwafukuzia mabingwa watetezi Manchester City waliopo nafasi ya pili kwa kufikisha pointi 54.
City wenyewe alipata ushindi wa mabao 2-0 nyumbani dhidi ya Leicester City na kuwqafanya wafikishe pointi 58 baada ya kushuka dimbani mara 28. Mabao ya washindi yaliwekwa kimiani na David Silva na James Milner.
Katika mechi nyingine za ligi hiyo, Liverpool ikiwa nyumbani ilipata ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Burnley, Manchester United ikiwa ugenini ilipata ushindi muhimu wa bao 1-0 mbele ya Newcastle United, huku Stoke City ikiitambia Everton kwa kuilaza mabao 2-0 na Tottenham Hotspur ilipata ushindi mujarabu kwenye uwanja wake wa nyumbani wa White Hart Lane kwa kuilaza Swansea City kwa mabao 3-2.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena keshokutwa kwa pambano moja tu kati ya QPR dhidi ya Spurs na timu nyingine zitakuwa kwenye majukumu ya Kombe la FA kabla ya ligi hiyo kuendelea wikiendi ijayo ya Machi 14 na 15.

Wednesday, March 4, 2015

TFF yaijibu Yanga kuhusu kinda la Simba

http://i1.wp.com/millardayo.com/wp-content/uploads/2015/01/Jerry-Muro.jpg
Jerry Muro
BAADA ya uongozi wa Yanga kudai kuhujumiwa na Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), bodi hiyo imewajibu wanajangwa kwamba 'Mkuki kwa Nguruwe, kwa binadamu mchungu'. Mapema leo, uongozi wa Yanga umetishia kutoingiza timu uwanjani katika mechi yao ya Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya JKT Ruvu Stars iliyopangwa kuchezwa Uwanja wa Taifa Machi 11, kutokana na kile ulichodai kutoshirikishwa katika uamuzi wa mabadiliko ya ratiba.
Jerry Muro, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Yanga, amesema jijini hapa leo kuwa uongozi wa Yanga ulikuwa unatambua kwamba kikosi chake kingecheza dhidi ya JKT Ruvu leo kabla ya kuivaa Simba SC Jumapili, lakini kimeshangaa baada ya kusoma kwenye mitandao kwamba mechi yao dhidi ya JKT Ruvu Stars haipo.
Hata hivyo, Fatma Shibo, Kaimu Ofisa Mtendaji wa TPLB, amesema mabadiliko ya ratiba ya Ligi Kuu Tanzania Bara hayajafanywa kwa siri na yametokea kutokana na ushiriki wa timu nne za ligi hiyo, Azam FC, Mtibwa Sugar FC, Simba SC na Yanga katika michuano ya Kombe la Mapinduzi mapema mwaka huu. Fatma amekanusha madai ya Yanga kwamba mechi yao dhidi ya JKT Ruvu Stars wanayodai ilipangwa kuchezwa leo kwamba yamefanywa kwa siri, kwa vile uongozi wa wanajangwani ulitaarifiwa tangu Febuari 16 juu ya mabadiliko ya ratiba ya ligi.
"Mabadiliko ya ratiba ya ligi kuu yametokea kutokana na ushiriki wa timu nne za Tanzania Bara katika michuano ya Kombe la Mapinduzi visiwani Zanzibar Januari mwaka huu," Fatma amesema.
"Hili la pili la Yanga kudai hatukuwashirikisha katika kupangua mechi yao dhidi ya JKT Ruvu si kweli kwa sababu tuliwasiliana na uongozi wa Yanga tangu Februari 16. Labda wawe na tatizo la kutofungua email, lakini Katibu Mkuu wao (Jonas Tiboroha) alisema aliona email yetu kuhusu suala hilo," amesema zaidi Fatma.
Ofisa huyo amesema bodi haina njama zozote za kuihujumu Yanga katika mechi zake kwani waliibeba pia katika kuilazimisha Tanzania Prisons irejeec Mbeya kutoka Dar es Salaam kucheza dhidi yao mechi waliyoshinda 3-0 jijini Mbeya juzi.
"Kama ni watu wa kulalamika, walipaswa kulalamika Prisons kwa sababu walikuwa hapa Dar es Salaam, lakini tukawaambia warejee kwao Mbeya kucheza dhidi ya Yanga baada ya uongozi wa Yanga kutuomba wacheze mechi zao zote zsa Mbeya kabla ya kwenda Botswana. "Mpaka sasa bodi inadaiwa pesa ya gharama za usaffiri na timu ya Prisons kwa sababu tuliwafanya wasafiri mara mbili kutoka Dar es Salaam kwenda Mbeya na kurudi tena hapa Dar es Salaam," amesema zaidi Fatma.
Katika hoja zake, Muro amedai TPLB ni janga la kitaifa na kwamba kusogezwa mbele kwa mechi hiyo dhidi ya kikosi cha Felix Minziro cha JKT Ruvu, ni hujuma dhidi ya Yanga  kwa kuwa timu hiyo ya Jangwani jijini hapa itakuwa na siku mbili tu za kupumzika baada ya kucheza dhidi ya maafande hao kabla ya kuivaa Platinum ya Zimbabwe katika mechi yao ya kwanza ya raundi ya kwanza ya michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika Jumamosi.
Huku akihoji kiwango cha elimu cha Kaimu Ofisa Mtendaji wa TPLB, Fatma na watendaji wengine wa bodi hiyo, Muro amesema tayari uongozi wa Yanga umewasilisha barua TFF tangu jana kusaka ufafanuzi wa mabadiliko ya ratiba hiyo.
“Kwa sasa mpinzani wetu ni Azam FC na siyo Simba, mechi dhidi ya Simba kwetu ni kwa sasa kama bonanza, siyo kipaumbele chetu, sisi tunawasubiri siku hiyo ifike tucheze nao, lakini hawana jipya kwa tunawazidi pointi nyingi,”ametamba Muro.
"Azam kesho na keshokutwa tunamwacha mbali maana mpaka sasa tuko mbele yake kwa pointi nne katika msimamo wa ligi, sisi wapinzani wetu na klabu ambazo unaweza kuzilinganisha na sisi ni Kaizer Chief ya Afrika Kusini au TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo ambazo zinacheza michuano ya kimataifa," amesema zaidi Muro

Pep Guardiola hana mpango wa kuhama Bayern

http://www.predapublishing.com/the-sportist/wp-content/uploads/2014/10/pg-68-garside-pa.jpgKOCHA wa klabu ya Bayern Munich, Pep Guardiola amesema hana mpango wowote wa kuikacha timu hiyo mwishoni mwa msimu kufuatia kuzuka tetesi kuwa anataka kuhamia Manchester City.
Mkataba wa Guardiola na mabingwa hao wa Bundesliga unatarajiwa kumalizika majira ya kiangazi mwaka 2016 lakini mazungumzo ya mkataba mpya yamesimamishwa hatua iliyozua minong’ono ya kuondoka.
Hata hivyo, Guardiola ameweka wazi kuwa bado anataka kuendelea kuinoa Bayern na hajafanya mazungumzo na klabu nyingine yeyote.
Akihojiwa Guardiola amesema hajapokea ofa yeyote kutoka kwa City kwa klabu nyingine kwani matumaini yake ni kubakia Bayern kwa kipindi kirefu.
Guardiola aliendelea kudai kuwa kwa sasa bado ana mkataba na Bayern na anapenda kuheshimu hilo mpaka hapo watakapokaa tena na kuzungumza juu ya mkataba mpya.

Air Jordan nouma! awafuka wanamichezo wote duniani

https://usatftw.files.wordpress.com/2014/09/ap_britain_ryder_cup_golf_67543664.jpg?w=1000&h=736MCHEZAJI mkongwe wa mpira wa kikapu nchini Marekani, Michael Jordan 'Air Jordan' ameendelea kuweka rekodi katika vitabu hata baada ya kustaafu mchezo huo baada ya kutajwa kama mwanamichezo pekee aliyechomoza katika orodha ya mabilionea ulimwenguni.
Wakati akicheza kikapu katika ligi maarufu nchini Marekani NBA, Jordan aliweka rekodi mbalimbali kutokana na umahiri pindi anapokuwa uwanjani lakini hali hiyo imebadilika kwani hivi sasa ameonyesha kuwa mahiri kibiashara pia.
Jordan mwenye umri wa miaka 52 ametajwa kushika nafasi ya 1,741 katika orodha ya watu matajiri duniani ambayo hutolewa na jarida la Forbes kila mwaka akiwa mwanamichezo pekee kuchomoza katika orodha hiyo.
Nguli amepata utajiri mkubwa kutokana na kuingia mkataba na kampuni ya vifaa vya michezo ya Nike ambao ulimuingizia zaidi ya dola bilioni 2.25 mwaka 2013 pamoja na kumiliki hisa asilimia 89 zenye thamani ya dola milioni 700 katika timu ya Charlotte Hornets.

Prisons yamfurusha Mwamaja, Makatta amrithi

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjaJrEavPqz6tdbaPJoZmvtYQffdUBf8ZB4pv78v6DDUEKBlffZJyhLOcc-KGwJFL0hn5CO0P6O5Fj_T_zQU8jrYulHMFe7oQSEzt6e49kVAVtP6uu4macHTa9l2xDasmWECDTPulRIcOs/s1600/mwamaja.JPG
Kocha David Mwamaja aliyesitishiwa mkataba wake na Prisons-Mbeya
KLABU ya Prisons Mbeya imemtimua aliyekuwa Kocha wao mkuu, David Mwamaja na nafasi yake imechukuliwa na Mbwana Makatta aliyewahi kuinoa timu hiyo siku za nyuma.
Mkurugenzi wa Ufundi wa Prisons, Hassain Yusuph alithibitisha kusitishiwa mkataba kwa kocha Mwamaja na kunyakuliwa kwa Makatta aliyekuwa akiinoa timu ya Ligi Daraja la Kwanza, Oljoro JKT.
Timu hiyo ndiyo inayoburuza mkia katika msimamo wa ligi hiyo wakikusanya pointi 14 tu baada ya jioni ya leo kulazimisha sare ya 0-0 na JKT Ruvu kwenye mchezo uliochez a kwenye uwanja wa Chamazi.
Hassain alisema kuwa mabadiliko hayo yamefanywa kutokana na kocha Mwamaja kushindwa kuiweka pazuri timu hiyo na kocha mpya atainoa timu hiyo kwa kipindi chote kilichofuata cha kumalizia ligi.

Mtibwa Sugar yazinduka, Ndanda yaiua Ruvu

Mtibwa Sugar waliozinduka
Polisi Moro waliokubali kichapo mbele ya Mtibwa leo
TIMU ya Mtibwa Sugar wametakata kwenye uwanja wa nyumbani baada ya kuicharaza Polisi Moro kwa mabao 2-1 katika pambano lililochezwa uwanja wa Manungu Complex
Mtibwa ambao kwa muda mrefu walikuwa hawajashinda walipata mabao yake kupitia kwa Ally Shomari na Said Mkopi baada ya awali wageni wao kuitangulia kufunga bao kwa mkwaju wa penati kupitia Said Bahanuzi.
Kwa ushindi huo Mtibwa wamepanda hadi katika nafasi ya tano wakifikisha pointi 22.
Katika mechi nyingine za ligi hiyo Ndanda Fc ya Mtwara iliitambia nyumbani Ruvu Shooting kwa kuilaza mabao 2-1 katika pambano kali lililochezwa uwanja wa Mabatini, Mlandizi Pwani.
Ndanda walianza kuandika bao la kuongoza katika kipindi cha kwanza kabla ya kuongeza jingine kupitia kwa Omega Seme na wenyeji Ruvu walijipatia bao la kufutia machozi dakika za lala salama.
Bao hilo lilifungwa na Yahya Tumbo na kuifanya Ndanda kufikisha pointi 19 wakati Ruvu wakiswaliwa na pointi 21.
Ligi hiyo itaendelea tena siku ya Jumamosi na Jumapili kutakapochezwa pambano la watani wa jadi Simba na Yanga.