STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, September 11, 2012

Omari Matuta: Wanchope wa Mtibwa aliyeamua kutundika daluga kwa muda

Omar Matuta 'Wanchope'



Omar Matuta 'Wanchope' (kati) akishangilia bao lililoipa Mtibwa Ubingwa wa Kombe la Tusker lililofungwa na Rashid Gumbo (kulia), Kushoto yao ni Uhuru Seleman alipokuwa wakiichezea Mtibwa Sugar

UMAHIRI wake wa kuwasumbua mabeki na kuwatungua makipa hodari uwanjani, ilimfanya Omar Matuta abatizwe jina la 'Wanchope' akifananishwa na nyota wa zamani wa Costa Rica aliyetamba timu za West Ham na Manchester City, Paulo Wanchope.
Kwa wanaomkumbuka Wanchope aliyezichezea pia Derby County na Malaga alikuwa na kipaji kikubwa cha ufungaji kilichomfanya ashikilie nafasi ya pili ya wafungaji bora wa timu yake ya taifa akiifungia mabao 45 katika mechi 73 alizoichezea.
Kama ilivyokuwa kwa Wanchope, ndivyo ilivyokuwa kwa Matuta, ambaye katika timu zote alizozichezea kuanzia zile za Ligi daraja la nne mpaka za Ligi Kuu Tanzania  amekuwa akifungia mabao muhimu na kuwa tegemeo.
Nyota huyo aliyewahi kutamba na timu za Ndanda Republic, Vijana Ilala, AFC Arusha kabla ya kudakwa na Mtibwa Sugar tangu mwaka 2004 anakumbukwa na mashabiki nchini kwa mabao yake mawili yaliyoipa nafasi timu ya vijana 'Serengeti Boys' tiketi ya kucheza Fainali za Vijana Afrika za mwaka 2005.
Matuta alifunga katika ushindi wa 3-1 dhidi ya vijana wa Zimbabwe yaliyoifanya ifuzu kwa jumla ya mabao 4-1 baada ya kwenda kushinda 1-0 Harare kwa bao la Nizar Khalfan, hata hivyo waliondolewa fainali na kufungiwa na CAF kwa udanganyifu.
Bao lake la pili katika mechi hiyo, Matuta analitaja kama bao bora kwake kwa namna alivyolifunga, ingawa mechi isiyofutika kichwani mwake ilikuwa ni dhidi ya Ethiopia mwaka 2005 kwa namna walivyofanyiwa vimbwanga na kufungwa kwa hila.
Matuta, ameamua kupumzika soka msimu huu baada ya kumalizika kwa mkataba wake na Mtibwa klabu anayoitaja kuwa bora kwake na anayeishabikia.
"Nimeamua kupumzika ili nifanye mambo yangu binafsi, ila  nikiwahi kumaliza huenda  nikarejea tena dimbani kwenye duru la pili la ligi kuu, ingawa sijui itakuwa timu ipi."
Mkali huyo anayefurahia soka kumpa mafanikio kimaisha ikiwamo kujenga nyumba Kigamboni na kumiliki miradi kadhaa ya biashara, anasema hajawahi kuona klabu iliyo makini na inayojali wachezaji wake kama Mtibwa Sugar.
Anasema kama mfumo wa klabu hiyo wa kujali na kuwathamini wachezaji wake ndio unaomfanya aiheshimu Mtibwa iliyomuuguza goti lake kwa miaka miwili kitu alichodai kwa klabu nyingine nchini ni vigumu kufanya jambo hilo hata kama umeisaidia vipi.

OWINO
Matuta asiyekumbuka idadi ya mabao aliyoyafunga kwa kutoweka kumbukumbu,  anasema licha ya umahiri wake dimbani, kwa beki wa kimataifa wa Azam, Mganda Joseph Owino ndiye ananayemnyima raha kwa uwezo wake mkubwa kisoka.
"Ni bonge la beki, anacheza kwa akili na ndiye anayenisumbua dimbani tangu nianze kukutana nae katika mechi za kimataifa na zile za Ligi Kuu Tanzania Bara."
Matuta anayependa kula ugali kwa samaki au nyama choma na kunywa vinywaji laini, anasema uwezo wake uwanjani na mwili na nguvu alizojaliwa huwa hapati shida kwa  mabeki wenye papara na wanaotumia nguvu, tofauti akutanapo na Owino.
Matuta, ambaye hajaoa ila ana mtoto mmoja aitwae Zuma, anayesoma darasa la tatu katika Shule ya msingi Bunge, anasema soka la Tanzania licha ya kusifiwa kukua ukweli  limedumaa kwa muda mrefu kutokana na sababu kadhaa.
Anadai moja ya sababu hizo ni u-Simba na u-Yanga uliowaathiri karibu wadau wote wa soka, kufutwa kwa mfumo wa ligi ya madaraja kama ilivyokuwa zamani na kupewa kisogo kwa michezo ya Yosso.
"Usimba na uyanga na kubadilishwa kwa mfumo wa ligi ya madaraja kama ilivyokuwa zamani ni sababu ya kukwama kwetu sawa na kupuuzwa kwa soka la vijana wenzetu wamekuwa wakilitegemea kupatia mafanikio yao," anasema.
Anasema ni muda wa wadau wa soka kubadilika japo anakiri huenda ikawa ngumu kwa namna ushabiki huo ulivyowathiri watu, pia akiwaomba viongozi wa FA na klabu kuwekeza nguvu kwa vijana sawia na kuwaruhusu kucheza soka nje ya nchi.

MIKWAJU
Matuta, mwenye ndoto za kufika mbali kisoka na kuwa mfanyabiashara mkubwa hapo baadae, anasema wakati akiibukia kwenye soka alipata wakati mgumu kwa baba yake ambaye ni marehemu kwa sasa aliyekuwa hapendi acheze soka badala yake asome.
Anadai baba'ke alilazimika wakati mwingine kumcharaza bakora ili kumzuia kucheza soka na kukazinia masomo, lakini haikusaidia kitu kwani alijikuta akikacha hata masomo ya sekondari ili ajikite kwenye soka.
"Nilikacha masomo ya sekondari pale JItegemee kwa ajili ya soka, wakati mwingine huwa najuta, lakini nafarijika kwa mafanikio niliyonayo," anasema.
Matuta aliyemudu pia nafasi za kiungo, anawashukuru makocha Mussa Stopper, Mzee Panju na Abdallah Kibadeni waliogundua na kukikiendeleza kipaji chake, pia akiwataja wazazi wake na uongozi mzima wa Mtibwa kumsaidia kufika hapo alipo.
Mkali huyo, aliyezaliwa mwaka 1988, akiwa mtoto wa nne kati ya watano wa Mzee Othman Matuta, anadai alivutiwa kisoka na nyota wa zamani wa RTC Kagera, Msabah Salum, licha ya kukiri kukunwa na soka la Ronaldo de Lima na Romario wa Brazil.
Matuta alianza safari yake kisoka tangu akisoma Shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko, akiichezea timu ya yosso ya Vijana Ilala na baadae kupandishwa timu B na baadae kutua Ndanda kuichezea Ligi Daraja la Nne wilayani Ilala kabla ya kurudishwa Vijana Ilala alioisaidia kuipandisha Ligi Kuu Tanzania Bara mwaka 2002.
Bao pekee aliloifungia Vijana dhidi ya Pallsons ya Arusha ndilo lililoipandisha daraja timu hiyo jambo ambalo anadai anajivunia mpaka sasa kabla ya kuichezea AFC Arusha katika michuano ya Nane Bora ya Ligi Kuu na mwaka 2004 kutua Mtibwa aliyoichezea mpaka msimu uliopita akiisaidia kuiwezesha kushika nafasi ya nne katika Ligi Kuu.
Akiwa Mtibwa, Matuta anayechizishwa na rangi zote isipokuwa zenye mng'ao mkali,

alitwaa nao ubingwa wa Kombe la Tusker- 2008, akiwa mmoja wa walioifungia mabao akishirikiana na Uhuru Seleman, Monja Liseki na Rashid Gumbo.
Kuhusu timu ya taifa aliyoichezea kuanzia timu za vijana tangu mwaka 2004, anasema inaweza kufuzu fainali za kimataifa iwapo TFF na wadau wote wataipa maandalizi ya kutosha.
Anasema chini ya kocha Kim Poulsen anamatumaini makubwa licha ya kutaka wadau kumpa nafasi kocha huyo na kuepukwa kubadilishwa kila mara kwa kikosi cha timu hiyo ili kuwafanya wachezaji wazoeane.
Pia anataka timu za taifa za vijana zipewe kipaumbele zikitafutiwa wadhamini wake ili kuwa na maandalizi mazuri, huku akiitaka TFF irejeshe mfumo wa ligi ya madaraja na kuwa wakali kwa wavunjaji wa kanuni za sheria za soka.

Omar Matuta 'Wanchope' akiwa ameshikilia kombe la Tusker la mwaka 2008 alilotwaa na Mtibwa Sugar

Vazi la taifa miaka 51 ya Uhuru wa Tanganyika

Waziri wa Habari Utamaduni Vijana na Michezo Dk Fenella Mukangara

VAZI rasmi la Taifa linatarajia kuanza kuvaliwa siku ya kilele cha sherehe za miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania zitakazofanyika Desemba 9, mwaka huu imeelezwa.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Waziri wa Habari, Utamaduni, Vijana na Michezo, Dk. Fenella Mukangara, alisema vazi hilo litavaliwa baada ya mchakato mzima wa kulipata vazi hilo utakapokamilika ambapo umepitia hatua mbalimbali.
Waziri Fenella alisema wizara yake inatarajia kuchukua michoro minne kati ya tisa iliyopitishwa na Kamati ya Vazi la Taifa iliyoundwa ambapo pia mchakato huo unahusisha kupata aina ya kitambaa kitakachotumika kutengenezea vazi hilo.
Waziri huyo alisema kuwa michoro hiyo minne (miwili ya vazi la kitenge na mingine ya khanga) itachukuliwa na kuwasilisha kwa sekretariati ya Baraza la Mawaziri ambalo litatakiwa kufanya maamuzi kabla ya Oktoba 31 mwaka huu.
"Baada ya kupata vazi hilo,kila mtu atakuwa na uhuru wa kuvaa mtandio, kushona gauni, shati au kuvaa kitambaa cha kichwani ambacho kitakuwa kinaonyesha vazi la taifa," alisema Fenella.
Katibu wa Kamati ya Vazi la Taifa, Angella Ngowi alisema kuwa kamati yake ilipokea maoni kutoka katika sehemu mbalimbali nchini na kuongeza kwamba mchakato wa kupata vazi hilo ulianza mwaka 2003.
Alisema kuwa michoro yote iliyopo katika mchakato huo ina rangi za bendera ya taifa na alama mbalimbali kama picha ya mlima Kilimanjaro, mwenge wa Uhuru, ala za muziki na picha za wanyama (Twiga na Pundamilia).


Hosea Mgohachi: Mpiga besi wa Extra afurahie muziki kumwezesha kimaisha

Hosea Mgohachi akiwa kwenye pozi kwenye ukumbi wa White House, Kimara

Moja ya nyumba za mwanamuziki Hosea Mgohachi
Hosea Mgohachi akicharaza gitaa kwenye mazoezi ya bendi yake ya Extra Bongo
Hosea akionyesha manjonjo yake kwenye moja ya maonyesho ya Extra Bongo nchini Finland hivi karibuni ilipoenda kwa ziara maalum nchi za Scandinavia
WAKATI wasanii na wanamuziki wengine wakilia kwamba fani zao zimekuwa zikishindwa kuwanufaisha kimaisha kwa sababu hizi na zile, kwa mkung'uta gitaa la besi wa Extra Bongo, Hosea Mgohachi 'Fukuafuku' kwake ni tofauti. Mgohachi, anasema anashukuru Mungu muziki aliouanza tangu akiwa kinda akiimba na kupiga ala shuleni na kanisa la Anglican-Kurasini, umemsaidia kwa mengi kiasi hajutii kujitosa kwke kuifanya fani hiyo. "Sio siri muziki umenisaidia mengi kiasi najivunia fani hii kwani, imeniwesha kumiliki nyumba mbili zilizopo Mbagala Kilungule na Mbagala Kuu, pia nina mradi wa 'Bodaboda' wenye pikipiki kadhaa," anasema. Mbali na hayo, Mgohachi anasema muziki umemwezesha pia kutembea nchi kadhaa duniani, kupata rafiki na kuitunza familia yake kwa pato la fani hiyo. Mgohachi, mwenye ndoto za kuja kuwa mfanyabiashara mkubwa, anasema siri ya mafanikio yake imetokana na nidhamu yake katika matumizi ya fedha na kiu kubwa aliyonayo ya kuwa mfanyabiashara atakapostaafu muziki. "Mtu hupata mafanikiokwa kujituma kwa bidii, ila kubwa ni suala la nidhamu hasa kwa matumizi ya fedha, kitu ambacho nimekuwa nikizingatia kwa muda mrefu hadi kufika hapa nilipo," anasema. Anasema hata kwa wasanii na wanamuziki wenzake ni vema wakazingatia hilo iwapo wanataka kufika mbali licha ya ukweli pato litokanalo na sanaa kukiri kuwa dogo kulinganisha na ukubwa wa kazi. MDUDU Mpiga gitaa huyo aliyesoma darasa moja na nyota wa muziki wa kizazi kipya anayetamba kundi la Wanaume Halisi, Sir Juma Nature, anasema wakati akichipukia kwenye muziki alivutiwa na kwaya za St James na Kristo Mfalme. Ila kwa sasa anadai anakunwa na wapiga gitaa Minicha na Kapaya waliopo pamoja na nyota wa DR Congo, Werrason Ngiama Makanda na mpiga solo nyota wa Extra Bongo, aliyewahi kutamba na bendi kadhaa nchini Ephrem Joshua 'Kanyaga Twende'. "Hawa jamaa nawazimia sana kwa ucharazaji wao wa magitaa, hasa Joshua, yaani tukiwa kundi moja utashangaa vitu tunavyotoa," anasema. Mkali huyo, anayeitaja Extra Bongo kama bendi bomba kwake kwa namna inavyomtunza na kumlipa dau kubwa kuliko bendi zote alizowahi kuifanyia kazi, anasema hakuna chakula anachopenda kula nyama ya nguruwe maarufu kama 'Kitimoto' au 'Mdudu'. "Aisee katika vyakula ninavyopenda kula hakuna kama 'mdudu' yaani ukitaka kunifurahisha we nipe nyama hii kwa ndizi za kuchoma ," anasema. Mgohachi, ambaye hajaoa kwa sasa ingawa yu mbioni kufanya hivyo kwa mwanamke anayeishi naye, anasema pia anapenda kunywa soda na siku moja moja kusuuza roho yake kwa kugida bia. OKWI Akiwa na watoto watatu, Wilson, 7 anayesoma darasa la pili Shule ya Msingi Mwananyamala, Mery, 7, anayesoma darasa la pili Shule ya Msingi Mtoni na Junior, 3, Mgohachi anasema japo soka halicheza sana utotoni mwake, lakini ni shabiki mkubwa wa mchezo huo. Anasema yeye ni shabiki mkubwa wa Simba na Manchester United akimtaja Emmanuel Okwi anayichezea Simba kama anayemkuna kwa umahiri wake wa kufumania nyavu uwanjani. "Kati ya nyota wanaonipa raha katika soka Emmanuel Okwi ndiye kinara wao, huyu jamaa ana akili ya kufunga, mjanja na ana kipaji cha kipekee hata Yanga wanamjua," anasema kwa utani huku akicheka. Mgohachi anayepiga magitaa yote na kupapasa kinanda, anasema hakuna tukio la furaha maishani mwake kama alipomaliza kujenga nyumba yake ya Mbagala Kuu na kusitikishwa na kifo cha dada yake kilichotokea mwaka 1999. Juu ya muziki wa Tanzania, Mgohachi anayeiomba serikali iitupie macho fani ya sanaa ili kuwainua wasanii, anasema umepiga hatua kubwa tofauti na miaka ya nyuma, ingawa anataka wanamuziki kubadilika na kuwa wabunifu zaidi./ Anasema ubunifu utaweza kuutangaza muziki huo kimataifa kama ilivyokuwa ikifanywa na makundi kama Tatu Nane, InAfrica Band na wengine. "Lazima tuwe wabunifu tuweze kutamba kimataifa, tuachane na kasumba na kupenda kuwaiga wakongo tunawatangaza zaidi wao badala ya muziki wetu," anasema. ALIPOTOKA Hosea Simon Mgohachi, alizaliwa Aprili 14, 1978 jijini Dar es Salaam akiwa mtoto wa nne kati ya watano wa familia yao, alisoma Shule ya Msingi Kurasini alipoanza kuonyesha kipaji chake cha sanaa akiimba kwaya na kupiga ala. Mbali na shuleni, Mgohachi pia alikuwa akiimbia kwaya ya kanisa lao la Anglican chini ya walimu Charles na Yaredi Disanura kabla ya kupitia makundi ya Chikoike Sound na Mwenge Jazz. Bendi yake ya kwanza kuifanyia kazi kama mwanamuziki kamili ni African Beat mnamo mwaka 1998 kabla ya kutua Mchinga Sound 'Wana Kipepeo' akiwa na rafikie Ibrahim Kandaya 'Profesa' aliyepo Msondo Band kwa sasa. Bendi nyingine alizofanyia kazi mwanamuziki huyo anayewaasa wasanii wenzake na watanzania kwa ujumla kujiepusha na Ukimwi kwa kujenga utamaduni wa kuwa waaminifu na kupima afya zao sawia na kutumia kondomu inaposhikana ni Double M Sound, Double Extra, Chipolopolo na African Vibration. Pia amewahi kufanya kazi za muziki Umangani kwa zaidi ya mara mbili wakati akiipigia bendi ya African Stars 'Twanga Pepeta' kabla ya mwaka jana kuhamia Extra Bongo alionao mpaka sasa akiwa amerejea nao kutokea nchi za Skandinavia. Mgohachi anayependa kutumia muda wake kuangalia vipindi vya runinga na kusikiliza muziki wa Bongofleva akimzimia Sir Juma Nature anasema atakuwa mchoyo wa fadhila kama hatawashukuru wazazi wake, Mama Shuu, Mudhihir Mudhihir na Ally Choki kwa namna walivyomfikisha hapo alipo.

Hosea Mgohachi akiwa katika pozi
Hosea Mgohachi akiwa na mwanae Junior

Wednesday, September 5, 2012

Eddo Boy: Kinda la Simba achekeleaye kuitungua Mtibwa Sugar

LICHA ya kuibuka mfungaji bora wa michuano ya Super8, mshambuliaji kinda wa Simba, Edward Christopher Shija 'Eddo Boy' a.k.a Teko Modise, amedai hajafurahishwa kama alivyoibebesha timu yake ubingwa wa michuano hiyo. Eddo, alisema tuzo ya ufungaji bora kwake isingekuwa na maana kama Simba isingekuwa mabingwa kwa jinsi walivyojituma na kuipigania timu yao. "Ingawa mechi ya fainali dhidi ya Mtibwa Sugar kwangu ni mechi ngumu kuwahi kuicheza kwa jinsi ilivyokuwa na funga nikufunge, ila sijivunii tuzo ya ufungaji bora wala kung'ara kwangu zaidi ya kuipa Simba ubingwa," alisema. Alisema, mara pambano lilipoisha akiifungia bao la ushindi katika matokeo ya mabao 4-3, alijisikia faraja kwa kutwaa taji jingine akiwa na Simba. "Mechi na Mtibwa sintoisahau kwa walivyocheza na kurejesha mabao yetu kila tulipofunga kabla ya kuwazidi ujanja kwa bao la nne lililotupa ubingwa, hakika najisikia fahari kwa kuilaza Mtibwa na kuipa Simba taji jingine," alisema. Kabla ya taji hilo, Eddo alishatwaa na Simba mataji ya Rolling Stone 2011, Kinesi 2011, Uhai 2011 na Ujirani Mwema lililochezwa mwaka huu. Pamoja na mafanikio yote, Eddo anayeichezea pia timu ya taifa, akipandishwa mwaka huu na kocha Kim Poulsen toka timu ya U20, alisema habweteki wala kulewa sifa. "Siwezi kulewa sifa kwa mafanikio niliyonayo kwa kipindi kifupi, ndoto zangu nije kucheza soka la kulipwa Ulaya na kutamba kimataifa," alisema. LUNYAMILA Eddo, alizaliwa Septemba 10, 1992 mjini Tabora akiwa mtoto wa pili kati ya watatu kwa familia iliyolelewa na mama pekee. Elimu ya Msingi aliisoma Shule za Choma Chankola,Tabora na Mwele ya Morogoro, kabla ya kujiunga na Sekondari za St Francis na baadae Makongo. Kisoka alianza kutamba tangu akiwa darasa la tatu akiwa Morogoro, timu yake ya chandimu ikiwa ni Jamhuri Ball Boys na baadae Moro Kids iliyowakusanya baadhi ya nyota wanaotamba kwa sasa nchini. Alisema wakati akichipukia alivutiwa na baadhi ya nyota wa zamani wa Simba na Yanga kama Edibily Lunyamila, Salvatory Edward, Mark Sirengo na Nteze John wa Simba, huku akimtaja kocha Yahya Belini kama mtu aliyekigundua na kukiendeleza kipaji chake. Eddo alisema safari yake kisoka ilipata vikwazo vingi toka kwa mama yake aliyekuwa hapendi kabisa acheze, kiasi cha kumchapa, kumnyima chakula na hata kumfungia na kulala nje pale alipomkaidi na kujihusisha na soka. "Mama yangu aliyekwishafariki hakupenda nicheze soka, ila nilikuwa nunda na kuishia kulambwa bakora, kunyimwa chakula na hata kufungiwa mlango na kulala nje, ingawa sikukata tamaa," alisema. Alisema jambo zuri ni kwamba kabla mama yake hajafariki mwaka 2005 alishaanza kusikia sifa zake kisoka toka kwa shoga zake na kumuacha acheze hasa alipohamia Makongo jijini Dar es Salaam. Eddo, aliyedai hajaonana na baba yake mzazi tangu mwaka 1998 baada ya kutengana na marehemu mama yao, alisema roho inamuuma kuona mamaye akifa bila kula jasho lake kisoka. YANGA B Eddo, anayependa kula vyakula vyote na kunywa vinywaji laini, alisema safari yake kisoka alipohamia Dar aliwahi kuichezea Yanga B aliyokuja kuachana nayo baada ya kuona hawana muelekeo wowote wa kimaendeleo.maendeleo. Alisema alienda Yanga baada ya kuisaidia Kinondoni kutwaa ubingwa wa Copa Coca Cola mwaka 2007 na kisha kuifikisha timu ya Kinondoni katika fainali za Taifa na kulazwa na Ilala mabao 5-0. Alisema alipoachana na Yanga alirejea darasani katika Shule ya Lord Baden Powell kabla ya kutimkia Moro United B aliyoichezea kabla ya kutua Miundo Mbinu ya Lindi aliyoipandisha daraja la kwanza na kuichezea timu ya mkoa wa Lindi katika michuano ya Kombe la Taifa 2009. Alisema mara baada ya fainali hizo na Lindi kufungwa na Singida, ndipo aliponyakuliwa na Simba kung'ara nao akinyakua mataji na tuzo mbalimbali hadi kupandishwa katika kikosi cha kwanza cha timu hiyo msimu uliopita. Eddo anayezishabikia Arsenal, Barcelona, Orlando Pirates na Brazil akiwazimia Neymar, Samuel Etoo na Ronaldo de Lima, alisema soka limempa mafanikio mengi kisoka na maisha ingawa hakupenda mambo yake yaanikwe. "Soka limenisaidia mengi, ila sipendi kila mtu ajue, najivunia na kiu yangu ni kung'ara zaidi nicheze soka la kulipwa Ulaya, safari yangu bado kabisa Simba sio mwisho wangu," alisema. Eddo ambaye hajaoa wala kuwa na mtoto, ingawa angependa kuwa na watoto watatu atakapooa, alitoa wito kwa wachezaji wenzake kujituma, kujiamini na kuwa na nidhamu waweze kufika mbali. Pia aliwakumbusha viongozi wa soka nchini kubadilika na kuachana na tabia ya kutumia nguvu na fedha nyingi kuwapapatikia 'mapro' wa kigeni na badala yake kuwekeza katika soka la vijana ili kulisaidia taifa hapo baadae. "Mafanikio ya kikosi cha Simba B ni funzo kwa viongozi na wadau wa soka nchini wawekeze katika soka la vijana badala ya kupigana kumbo kugombea mapro wa nje, fedha wazitumiapo kwao zisaidie soka la vijana," alisema. Eddo anayetamani kuwa mfanyabiashara mkubwa atakapostaafu soka na anayependa muziki wa reggae akimzimia J Booge, Biggy Signal na P Square, aliwashukuru mama yake, makocha wote waliomnoa na rafiki na wachezaji wenzake kwa kufika hapo alipo. Nyota huyo asiyeamini mambo ya uchawi katika soka akiamini mazoezi ndio kila kitu, alisema angekutana na Rais au waziri wa michezo angewaomba zijengwe na kuanzishwa shule maalum za michezo. pia kutaka soka la vijana lipewe kipaumbele zaidi. Mwisho

KIMOBITEL ALIVYOREJEA 'NYUMBANI' EXTRA BONGO

PICHA ZA MATUKIO WAKATI WA UTAMBULISHO WA KHADIJA MNOGA KIMOBITEL ALIPOREA BENDI YA EXTRA BONGO JANA JIJINI DAR ES SALAAM.

Mzee Yusuf aanzisha kampuni kusambaza kazi ili kudhibiti wezi

NYOTA wa muziki wa taarab nchini, Mzee Yusuf 'Mfalme' amefungua kampuni yake binafsi ya usambazaji wa kazi zake na wasanii wengine iitwayo MY Collection. Akizungumza na MICHARAZO, mkurugenzi huyo wa kundi la Jahazi Modern Taaran alisema ameamua kufungua kampuni hiyo ili kusaidia kuthibiti uchakachuaji na wizi wa kazi zake ambao umekuwa ukimkomesha mapato mengi. Alisema kampuni hiyo ambayo imeshafungua duka la kuuzia cd na dvd katika mitaa ya Likoma na Mhonda itakuwa ikihusika na usambazaji na uuzaji wa kazi za Jahazi Modern na zile za wasanii wengine iwapo watapenda kufanya hivyo kwake. "Katika kukabiliana na vitendo vya wizi wa kazi zangu, nimeamua kufungua kampuni ya usambazaji na uuzaji wa cd na dvd ambayo itahusika na kazi zote za Jahazi Modern, ila kama kutakuwa na watakaotaka kuwasaidia kusambaza kazi zao sitakuwa na noma," alisema. Naye Meneja Masoko wa kampuni hiyo, Mussa Msuba duka walillofungua litakuwa likihusika na kuuza kazi za taarab kwa jumla na rejereja ili kuwarahisishia mashabiki wa muziki huo eneo la kupata burudani hiyo. "Hili ni duka la awali tu, pnago ni kufungua karibu kila kona ya nchi kuwarahisishia mashabiki mahali pa kupata burudani za taarab kwa matumizi yao ya majumbani na ya kibiashara kwa ujumla na hasa kazi za Jahazi ambao wanatarajia kutoa albamu mpya ya tisa," alisema Msuba. Uamuzi wa Mzee Yusuf kufungua kampuni na duka hilo, imekuja mwezi mmoja baada ya kunasa baadhi ya albamu zake zilizochakachuliwa walipoendesha msako wakishirikiana na wadau wengine wa sanaa wakiwemo Shirikisho la Filamu Tanzania, TAFF na Bongo Movie.

Erick Mawalla: Kinda anayeililia ligi ya vijana, kombe la Taifa

KUTOKUWEPO kwa ligi ya muda mrefu na ya kudumu kwa timu za vijana na kutopewa kipaumbele kwa michuano ya Kombe la Taifa, kunamfanya beki kinda anayepanda chati nchini, Erick Mawalla 'Sekana' aamini ni sababu ya kudidimia kwa soka la Tanzania. Beki huyo aliyetua African Lyon akitokea timu iliyoshuka daraja ya Moro United anasema michuano ya timu za vijana na Kombe la Taifa kwa mtazamo wake ndio ukombozi wa soka la Tanzania na kurejesha makali yake katika anga la kimataifa. "Hatuwezi kufanya vema kwenye michuano ya kimataifa iwapo hatuna ligi ya vijana, lazima iwepo mipango ya kuanzisha ligi hiyo na kuipa kipaumbele michuano ya Kombe la Taifa, ambayo siku za nyuma ilitumika kuibua nyota waliotamba nchini," anasema. Anasema hata klabu na mataifa yanayofanya vema katika soka la kimataifa, zilipoteza fedha zao kuwekeza kwa vijana na mavuno yao yanavutia kila mtu, kitu ambacho ametaka Tanzania nayo kufuata nyayo hizo ili ifanikiwe. "Bila kuwepo kwa ligi ya kudumu ya vijana, au shule maalum za kukuzia vipaji tangu utotoni na kutopewa kipaumbele kwa michuano muhimu kama Kombe la Taifa ni vigumu kuwa na timu imara kuanzia ngazi za klabu mpaka timu za taifa," anasema. Erick aliyeanza kucheza soka tangu shuleni kama winga kabla ya kubadilishwa na kuwa beki, anasema kuanzia serikali, wafadhili, viongozi na mashabiki watambue hakuna njia ya mkato ya mafanikio katika michezo bila watu kuwekeza fedha zao katika sekta hiyo. NYOTA NJEMA Kinda hilo, linalopenda kula chakula cha aina yoyote mradi akimdhuru na kunywa Juisi, anasema anashukuru soka kumsaidia kwa mengi ikiwamo kutwaa mataji na tuzo kadhaa tangu akiwa kinda ukiacha mafanikio binafsi ya kimaisha. "Siwezi kusema nimefanikiwa sana, ila nashukuru kwa muda mfupi niliopo katika soka nafarajika nimeweza kupata mafanikio ya kujivunia ikiwamo kutwaa vikombe, tuzo na kupata fedha zinazosaidia kuendesha maisha yangu," anasema. Erick, 'swahiba' mkubwa wa Mfungaji Bora wa michuano ya Super 8 anayeichezea Simba, Edward Christopher 'Eddo Boy', anasema moja ya mataji ambayo hawezi kusahau maishani mwake ni Kombe la Copa Coca Cola 2007 akiwa na timu ya vijana ya Kinondoni. "Hili ndilo lilikuwa taji langu la kwanza kubwa katika maisha ya soka, kwa hakika nilifurahi mno kuipa Kinondoni taji hilo, ingawa nimeshatwaa pia ubingwa wa Kombe la Taifa nikiwa na Ilala na mwaka jana tulishika nafasi ya tatu katika michuano kama hiyo," anasema. Erick, aliyeingia kwenye soka kwa kuvutiwa na 'mapacha' wa zamani wa klabu anayoishabikia ya Manchester United, Dwight Yorke na Andy Cole, anasema kabla ya kuibukia kwenye Coca Cola, kipaji chake kilianza kuonekana Kijitonyama Stars aliyoichezea tangu akiwa darasa la sita. "Baadae nilitua Yanga B nikiwa na swahiba wangu Eddo Boy na wengine, lakini kutokana na klabu hiyo kuonekana haikuwa na mipango endelevu ya soka la vijana, nilihamia Moro Utd B na kuichezea kwa misimu kadhaa akishuka na kupanda nayo Ligi Kuu," anasema. Chipukizi huyo anasema alikuwa katika kikosi cha Moro kilichoshuka daraja msimu wa 2009-2010 na kuirejesha tena Ligi Kuu msimu uliopita kabla ya kuzama tena na yeye kukimbilia African Lyon. Matarajio ya Erick anayeishabikia pia Real Madrid na aliyewataja makocha Juma Matokeo na Seleman Kiiza kama watu waliosaidia kukuza kipaji chake, ni kucheza soka la kulipwa nje ya nchi akidai tayari ameanza kipango ya jambo hilo. "Kiu yangu kubwa ni kucheza soka la kulipwa hasa Ulaya, naamini ni kipaji na uwezo wa kufanya hivyo, ingawa napenda kabla ya hapo nipate fursa ya kulitumikia taifa langu," anasema. Mchezaji huyo anasema licha ya kuitwa mara kadhaa katika vikosi vya timu za vijana U17 na U20, kiu yake kubwa ni kuichezea Taifa Stars. NSAJIGWA Erick anayehuzunishwa na kifo cha baba yake kilichotokea mwaka 2006, anasema licha ya kucheza mechi nyingi, pambano gumu kwake ni lile la Moro United dhidi ya Yanga lililochezwa msimu uliopita na lililoisha kwa sare ya mabao 2-2. Anasema anaikumbuka mechi hiyo hasa kwa tukio lililofanywa na aliyekuwa nahodha wa Taifa Stars, Shadrack Nsajigwa cha kumpiga 'kiwiko' winga wao Benedict Ngassa na kutolewa nje kwa kadi nyekundu na jinsi Yanga iliyosawazisha bao la pili. "Ni mechi hiyo na ile ya nusu fainali dhidi ya Mwanza katika michuano ya Kombe la Taifa 2011 tuliyopoteza ndizo ninazozikumbuka kwa ugumu na namna zilivyojaa upinzani," anasema. Erick Lawrance Mawalla alizaliwa Julai 5, 1993 jijini Dar es Salaam akiwa mtoto wa kwanza kati ya wanne wa familia yao, alisoma Shule ya Msingi Bunge kabla ya kutua Makongo Sekondari kutokana na kipaji chake cha soka. Akiwa Makongo ndiko alikoitwa timu ya vijana ya Kinondoni na baadae timu ya taifa ya U17 kabla ya kupandishwa ile ya U20 chini ya kocha Kim Poulsen. Anasema kama kuna watu anaowashukuru kumsaidia kufanikiwa kisoka na maisha basi si wengine zaidi ya wazazi, makocha wake na wachezaji wenzake bila kuusahau uongozi wa Moro United. Erick anayependa kusikiliza muziki na kuangalia filamu, anasema kama angekutana na Rais wau Waziri wa Michezo kilio chake kingekuwa juu ya kujengwa shule maalum za michezo.

Kimobiteli arejea Extra Bongo, atua na moja mpya

BENDI ya muziki wa dansi ya Extra Bongo imemrejesha kundini aliyekuwa muimbaji wao Khadija Mnoga 'Kimobitel' aliyekuwa ametimkia African Stars 'Twanga Pepeta'. Uongozi wa Extra Bongo ulisema umemrejesha kundini mwanamuziki huyo baada ya mwenyewe kuridhia kurudi huku bendi yao ikiwa ina upungufu mkubwa katika safu ya uimbaji kwa sauti ya kike. Mkurugenzi wa Extra, Ally Choki, alisema wakati wa kumtambulisha muimbaji huyo mbele ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana kuwa kurejea kwa Kimobitel kutasaidia kuimarisha safu yao ya uimbaji. Choki alisema Kimobitel aliyeikacha Extra Bongo miezi kadhaa iliyopita amerejea kundini akiwa na 'zawadi' kwa mashabiki kwa kuja na wimbo mpya uitwao 'Mgeni'. Mkurugenzi huyo alisema Extra Bongo inatarajiwa kumtambulisha rasmi Kimobiteli kwa mashabiki wiki ijayo baada ya kufanya mazoezi ya kutosha na wenzake. Kimobitel alisema amerejea Extra Bongo bila kulazimishwa na mtu huku akidai bendi aliyotoka hakuwa na mkataba wowote na hivyo anawaomba mashabiki wa bendi hiyo wampokee na watarajie mambo mazuri kutoka kwao. "Nimeamua mwenyewe kurejea Extra Bongo, na yale yaliyopita yamepita tuangalie mapya ninachoomba mashabiki wetu wasubiri vitu adimu toka kwangu," alisema. Mwanadada huyo aliyewahi kutamba na bendi mbalimbali ikiwemo African Revolution na Double M Sound, alisema anaamini aliwakwaza watu alipoondoka Extra Bongo, lakini ni suala la kusameheana kwani ametambua alipotoka na amerejea nyumbani akihitaji kupokelewa vema. Naye kiongozi wa bendi hiyo, Rogart Hegga 'Katapila' alisema wana Extra Bongo wamefurahishwa na ujio wa Kimobitel akidai bendi yao sasa imekamilika vya kutosha hasa baada ya kushindwa kuziba pengo la mwanamuziki huyo tangu alipoondoka. Alisema licha ya kwamba mwanamuziki huyo atatambulishwa rasmi wiki ijayo, lakini bendi yao itaendelea na maonyesho yao kama kawaida wiki hii kwa siku za Ijumaa na Jumapili kufanya vitu vyao White House-Kimara na Jumamosi Meeda Club, Sinza. Mara baada ya utambulisho wa mwanamuziki huyo kwa waandishi, alitambulishwa pia kwa wanamuziki wote wa Extra Bongo ambapo kwa kauli moja wanamuziki hao walimpokea na kumkaribisha nyumbani wakimuahidi ushirikiano ili bendi yao izidi kupaa.

Monday, August 13, 2012

Simba, Azam, Mtibwa zafuzu semi fainali Super8

TIMU za soka za Simba na Azam zinatarajiwa kukumbushia mechi yao ya robo fainali za Kombe la Kagame 2012 zitakapokutana katika nusu fainali ya Super 8 baada ya zote kufuzu hatua hiyo ya michuano hiyo maalum inayodhaminiwa na BancABC. Simba imetinga hatua hiyo baada ya kuifunga Zimamoto ya Zanzibar mabao 2-0 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba mjini Mwanza. Simba walioingiza kikosi chao cha pili kwenye michuano hiyo, kinachonolewa na Kocha Suleiman Abdallah Matola, ilipata mabao yote yote kupitia kwa kiungo chipukizi anayeinukia vema katika soka ya Tanzania, Christopher Edward kipindi cha pili. Christopher ambaye hukomazwa pia kwenye kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars na kikosi cha kwanza cha Simba, alifunga bao la kwanza penalti dakika ya 50, baada ya beki Miraj Adam kuangushwa kwenye eneo la hatari. Edward ambaye ni kipenzi cha kocha Mserbia wa Simba, Profesa Milovan Cirkovick, alifunga bao la pili dakika ya 55 baada ya kuwapiga chenga mabeki watatu wa Zimamoto kabla ya kumchambua kipa wa timu hiyo ya Zanzibar. Pamoja na Simba SC kuwania ubingwa wa michuano hiyo, lakini sasa Christopher ameingia kwenye mbio za kiatu cha dhahabu cha michuano hiyo, kwa kufikisha mabao manne, akiwa anaongoza. Katika michezo mingine ya kuhitimisha hatua ya makundi ya michuano hiyo, Uwanja wa Chamazi, Jamhuri FC iliichapa 4-0 Mtende, zote za Zanzibar mabao ya washindi yakifungwa na Sadik Rajab dakika ya 20, 44, Issa Achimwene aliyejifunga dakika ya 82 na Suleiman Khatib dakika ya 88. Kwenye Uwanja wa Ushirika mjini Moshi, Azam FC ilitoka nyuma kwa bao 1-0 na kuifunga Polisi Moro FC mabao 2-1, mabao yake yakitiwa kimiani na beki Said Mourad dakika ya 20 na Abdi Kassim ‘Babbi’ dakika ya 70, wakati la Maafande wa Morogoro lilitiwa kimiani na Mokili Rambo dakika ya kwanza. Polisi ilimpoteza mchezaji wake, Abdallah Rajab dakika ya 88 aliyetolewa nje kwa kadi nyekundu. Uwanja wa Amaan, Zanzibar, Kocha Mecky Mexime ataiongoza Mtibwa Sugar katika mchezo wa mwisho wa makundi dhidi ya wenyeji Super Falcon FC. Katika Kundi A, Simba SC inaongoza kwa pointi zake nne, baada ya kutoa sare moja na kushinda moja, ikifuatiwa na Zimamoto na Mtende zinazofungana kwa pointi tatu kila moja, wakati Jamhuri inashika mkia kwa pointi yake moja. Kundi B, Mtibwa inaongoza kwa pointi zake sita ikifuatiwa na Azam FC na Polisi Moro, zenye pointi tatu kila moja, wakati Falcon inashika mkia, ikiwa haina pointi hata moja. Kwa kufuzu hatua hiyo, Simba inatarajiwa kuvaana na Azam, ambao katika mechi yao ya Kagame waliishindilia 'Mnyama' mabao 3-1 yote yakiwekwa kimiani na John Bocco aliyepo Afrika kwa sasa kifanya majaribio katika klabu ya Super Sports. Mechi nyingine itakayochezwa mapema saa 8 siku hiyo ya Jumamosi itazikutanisha Mtibwa Sugar dhidi ya jamhuri ya Pemba. Mechi zote za Nusu fainali na fainali zote zitachezwa Dar es Salaam. Mdhamini wa michuano hiyo, Banc ABC anagharamia usafiri wa ndege kwa timu zote kutoka kituo kimoja hadi kingine, malazi na jezi. Kanuni za mashindano haya ni kushirikisha timu zilizoshika nafasi tatu za juu katika Ligi Kuu za Bara na visiwani na mbili zilioongoza katika kupanda Ligi Kuu zote mbili, lakini kwa Bara, Yanga waliokuwa washindi wa tatu msimu uliopita, walijitokea na nafasi yao ikachukuliwa na Mtibwa Sugar ambayo ilishika nafasi ya nne kwenye Ligi Kuu. Bingwa wa michuano hiyo mipya itakayokuwa ikifanyika kila mwaka, ataondoka na Sh. Milioni 40, mshindi wa pili Sh. Milioni 20, wa tatu Sh. Milioni 15 sawa na wa nne, wakati washiriki wengine wataondoka na Sh. Milioni 5 kila moja. NUSU FAINALI Agosti 15, 2012 Mtibwa Sugar Vs Jamhuri (Saa 8:00 mchana) Simba SC Vs Azam FC (Saa 10:00 jioni) (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam)

Sunday, August 12, 2012

Chelsea, Man City kufungua pazia la msimu mpya EPL leo

PAZIA la msimu mpya wa Ligi Kuu ya England (EPL)kwa mwaka 2012/13 linatarajiwa kufunguliwa rasmi leo Jumapili kwa mechi ya kuwania Ngao ya Jamii kati ya Mabingwa wa Ligi Kuu England, Manchester City, na Mabingwa wa FA Cup, Chelsea, ambao pia ni Mabingwa wa Ulaya. Pambano la timu hizo mbili zitakazoshuka dimbani leo zikiwa na mabadiliko yanayotofautiana katika vikosi vyao unatarajiwa kuchezwa kwenye uwanja wa Villa Park, kuanzia saa 9 Alasiri kwa saa za Afrika Mashariki na Kati. Wakati Chelsea ikiwa na nyota wapya walionunuliwa hivi karibuni kwa ajili ya msimu mpya, Man City wao hawana mabadiliko yoyote. Chelsea itashuka dimbani leo ikiwa haina kinara aliyewapa mataji hayo mawili inayoyashikilia kwa sasa Didier Drogba, kutoka Ivory Coast aliyehamia katika klabu ya Shanghai Shenhua ya China akiungana na Nicolas Anelka. Vifaa vipya vilivyosajiliwa na ambavyo vimeanza kuonyesha makeke katika mechi za kujipima nguvu kujiandaa na msimu mpya utakaoanza mwishoni mwa wiki ijayo ni Eden Hazard, Marko Marin na Oscar lakini ni Hazard na Marin ambao wanaweza kucheza Mechi hii na Man City kwa vile Oscar atakuwa bado yuko na nchi yake Brazil kwenye Olimpiki. Msimu uliopita, Timu hizi ziligawana ushindi kwa Chelsea kuifunga Man City 2-1 Mwezi Desemba na Man City kuifunga Chelsea 2-1 Mwezi Machi. Katika Mechi zao za hivi karibuni, Mechi za kujipasha kwa ajili ya Msimu mpya, Chelsea imekuwa na matokeo yasiyoridhisha kwa kushinda Mechi moja tu kati ya 4 walizocheza na kufungwa zilizobaki wakati Man City wamecheza Mechi 5 na kushinda 3 na kufungwa mbili. Chelsea hawana majeruhi yeyote lakini Man City watamkosa Nahodha wao Vincent Kompany na Micah Richards ambao wameumia. Vikosi vinatarajiwa kupangwa kwa siku ya leo ni kama ifuatavyo: Chelsea [Mfumo 4-3-3]: Cech, Ivanovic, Terry, Cahill, Cole, Mikel, Meireles, Lampard, Ramires, Torres, Hazard Man City [Mfumo 4-4-2]: Hart, Zabaleta, Savic, Lescott, Clichy, Yaya Toure, De Jong, Nasri, Johnson, Tevez, Aguero

Rage adanganya Simba, alia akijitoa TFF Na Waandishi Wetu, Dodoma na Dar es Salaam

SIKU sita tangu awadanganye wanachama wa Simba kuwa mchezaji Emmanuel Okwi amefanya majaribio na kufuzu Ulaya, mwenyekiti wa klabu hiyo Isamil Aden Rage amelia hadharani akitangaza kujitoa uongozi wa moja ya kamati za TFF -- shirikisho la soka. Rage jana alitangaza kujivua nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Katiba, Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya TFF, akituhumu baadhi ya viongozi wa shirikisho hilo kutoitendea haki timu yake. Mwenyekiti huyo wa Simba ambaye pia ni Mbunge wa Tabora Mjini (CCM) aliwaambia wanachama wa Simba katika mkutano Jumapili iliyopita kuwa Okwi alifanya majaribio na kufuzu katika klabu ya Red Bull Salzburg ya Austria. Lakini akizungumza na Nipashe mapema wiki hii, Okwi alisema hakufanya majaribio yoyote Ulaya kutokana na kusumbuliwa na Malaria tangu awasili barani humo mpaka kurejea Uganda na kisha Simba. Alipoulizwa kama haoni kuwa aliwadanganya wanachama wa Simba alipowaeleza jambo ambalo linakanushwa na mchezaji husika jana, Rage ambaye alidai pia kuwa mchezaji huyo atakuwa akilipwa euro 300,000 kwa mwezi na Redbull alisema: "Okwi hakwenda kutalii kule... mimi ninasema kitu kilicho sahihi. "Alifanya majaribio na kufuzu. Haya maneno mengine ni ya magazeti tu... sasa kama hajafanya majaribio alienda kufanya nini kule kwa kipindi cha wiki nzima." Kwa mujibu wa taarifa za mtandao rasmi wa kompyuta wa Red Bull Salzburg, imesajili wachezaji wawili tu kati ya tarehe za Okwi kwenda Ulaya mpaka kurudi -- Valon Berisha kutoka Viking Stavanger na Havard Nielsen kutoka Valerenga Oslo. Zote za Norway. Akizungumza na waandishi wa habari Bungeni mjini Dodoma jana, Rage alisema amejitoa katika kamati hiyo baada ya kuchukizwa na kitendo cha Yanga kumsajili beki wa APR ya Rwanda, Mbuyi Twite ambaye Simba ilishaingia naye mkataba, na kwa baraka za TFF. Alisema TFF ina wajumbe wengi ambao ni wanazi wa Yanga na hivyo kushindwa kuitendea Simba haki. “Kama serikali na mamlaka za kusimamia soka zitaonekana zinapendelea timu moja, basi wapenzi na wanachama wa Simba wanaweza kuamua kuangalia kwingineko ambako wanadhani watapata haki zao za msingi,” alisema Rage na kulazimika kukatisha kwa muda mkutano wake baada ya kumwaga machozi. Rage hakufafanua Serikali inaingiaje katika suala la kuonewa kwa Simba huko anakodai, wala kama amepewa ridhaa na wanachama wa Msimbazi kuishutumu serikali yao kwa niaba yao. Wakati huo huo, Katibu Mkuu wa Yanga, Celestine Mwesigwe, amesema kuwa wanasubiri muda ufike wamtangaze rasmi Mbuyi Twite atakayechezea timu hiyo msimu ujao wa ligi kuu ya Bara. "Hiko kitu kipo (usajili wa Mbuyi), lakini siwezi kuzungumzia suala hilo kwa sasa," alisema. "Ngoja tusubiri wakati wake ufike na mchezaji ataonekana hapa kwa sababu hili sasa hivi limekuwa na mvutano kidogo." Chanzo:NIPASHE JUMAPILI

Pambano la watani wa jadi Msondo wajichimbia Dodoma, Sikinde wajificha

HOMA ya pambano la wapinzani wa jadi kwenye muziki wa dansi nchini kati ya Msondo Ngoma 'Baba ya Muziki' na Mlimani Park 'Sikinde' linalotarajiwa kufanyika Idd Mosi kwenye viwanja vya Leaders Club limechukua sura mpya baada ya bendi mmoja kukimbia mji na nyingine kwenda kusikojulikana. Bendi ya Msondo imelikimbia jiji la Dar es Salaam na kwenda kujichimbia mkoani Dodoma kujiandaa kikamilifu na pambano hilo la aina yake dhidi ya mahasimu wao. Meneja wa bendi hiyo Said Kibiriti amesema kuwa bendi iko Dodoma ikifanya mazoezi ya 'kufa mtu' ili kuwatoa nishai Sikinde na wasiwe na hamu tena ya kuomba pambano siku nyingine. "Tunataka tutoe dozi siku hiyo, tutawasambaratisha na waogope tena kupambana na sisi, mashabiki wetu wasiwe na wasiwasi bendi yetu iko sawa na sasa inajifua na siku ya Idd El Fitri wajitokeze kwa wingi kuja kuishangilia Msondo," alisema Kibiriti. Kwa upande wa Sikinde, kiongozi wa bendi hiyo Habib Jeff amesema kuwa bendi yao ipo jijini Dar es Salaam, lakini akagoma kabisa kutaja sehemu ilipojichimbia. "Ndugu yangu sisi tupo hapa hapa Dar, ila siwezi kukwambia tupo wapi, tunaogopa hujuma, si unajua tena linapokuja suala la Msondo na Sikinde ni kama Simba na Yanga kwa hiyo mashabiki watatuona tu siku siku hiyo, wala hatusemi kwa sasa yuko wapi ila hapa hapa Dar," alisema. Kiongozi huyo amewataka mashabiki wake kujazana kwa wingi siku ya Idd Mosi kwenye viwanja vya Leaders Club kuipa sapoti bendi yao ili iibwage Msondo. Pambano hilo limeandaliwa na kampuni ya Keen Arts na kudhaminiwa na Konyagi. Bendi hizo zilipambana kwenye sikukuu ya Krisimasi mwaka jana kwenye ukumbi wa TCC. Mwisho

Ruvu Shooting yatangaza kikosi chake kipya, yasajili 26

KLABU ya soka ya Ruvu Shooting Stars inayojiandaa na Ligi Kuu Tanzania Bara imetangaza usajili wa wachezaji wao 26 kwa ajili ya msimu mpya wa ligi hiyo utakaoanza mwezi ujao. Miongoni mwa waliosajiliwa na kikosi hicho kinachonolewa na kocha Charles Boniface Mkwasa ni pamoja na waliokuwa washambuliaji nyota wa Kagera Sugar, Hussein Swedi na Said Dilunga. Msemaji wa klabu hiyo, Masau Bwire aliiambia MICHARAZO leo asubuhi kuwa, usajili huo ambao unatarajiwa kuwasilishwa kesho kwenye ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, umezingatia umri, kipaji na uwezo wa mchezaji kutokana na mapendekezo ya kocha wao. Bwire, alisema kati ya wachezaji hao 26 waliosajiliwa na klabu yao, sita ni wachezaji wapya na waliosalia ni wale walioichezea timu hiyo msimu uliopita. Aliwataja wachezaji wapya walionyakuliwa na timu yao kuwa ni Said Dilunga, Husseni Swedi, Mau Bofu aliyekuwa akiichezea Azam, Gideon Sepo, Kulwa Mobi aliyeichezea Polisi Dodoma msimu uliopita na Philemon Mwandesile aliyekuwa timu ya Toto Afrika. Wachezaji wa zamani waliobakishwa kikosi ni pamoja na kipa Benjamin Haule, Michael Norbert, Gido Chawala, Godhard Msweku, Liberatus Manyasi, George Assey, Mangasin Mbonosi, Paul Ndauka, Jumanne Juma, Shaaban Suzan, Said Madega na Nyambiso Athuman. Wengine ni Raphael Keyala, Frank Msese, Michael Aidan, Gharib Mussa, Ayuob Kitala, Ernest Jackson na Baraka Nyakamande. Bwire alisema wachezaji waliotemwa na kikosi hicho kutokana na sababu mbalimbali ni pamoja na Mohammed Kijuso, Emmanuel Mwagamwaga, Yusuph Mgwao na Kassim Kilungo.

Timu za Maafande wa JKT waandaliwa michuano maalum wazialika Coastal, Lyon

TIMU za soka za Coastal Union ya Tanga na African Lyon ya Dar es Salaam zinatarajiwa kushiriki michuano maalum ya 6 Bora zinazozihusisha timu za maafande wa JKT, kwa ajili ya kuziandaa vema na ushiriki wao wa Ligi Kuu. Michuano hiyo itakayokuwa ikifanyika kila mwaka kulingana na uwepo wa timu hizo za maafande inatarajiwa kuanza siku ya Jumatano na itakuwa ikichezwa kwenye uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani. Msemaji wa michuano hiyo itakayochezwa kama ligi hadi kupata mshindi wake, Masau Bwire aliiambia MICHARAZO mapema leo kuwa timu nne za maafande wa JKT ndizo walengwa wakuu wa michuano hiyo ila katika kuipa msisimko zaidi wamezialika Coastal Union na African Lyon. Bwire alisema wamezialika timu hizo kwa imani itazipa changamoto timu zao ili kuanza kuhimili mikikimikiki kabla ya kuanza kwa ligi kuu. "Katika kuziandaa timu zetu za JKT na kuhakikisha zinafanya vema kwenye Ligi Kuu msimu huu, tumeziandalia michuano maalum ya Sita Bora ambayo itaanza Agosti 15 na tumezialika Coastal Union na African Lyon, kutokana na kuonekana zina viwango bora," alisema Bwire. Alizitaja timu za JKT zilizolengwa kwa michuano hiyo ni wenyeji JKT Ruvu, Ruvu Shooting Stars, JKT Oljoro ya Arusha na JKT Mgambo Shooting ya Tanga iliyopanda daraja msimu huu. Bwire alisema ratiba michuano hiyo itaanza kwa kuzikutanisha timu za JKT Ruvu na Ruvu Shooting siku ya Jumatano, siku inayofuata itakuwa zamu za JKT Oljoro dhidi ya Mgambo Shooting na Agosti 17 Coastal Union itavaana na Lyon. "Hizo ni mechi za awali na ratiba kamili inatarajiwa kutolewa kuanzia Jumanne ili kuwapa fursa mashabiki wa soka kuifuatilia na hatimaye kujua nani atakayeibuka mshindi wa michuano hiyo maalum," alisema. Mwisho

Saturday, August 11, 2012

Kivumbi cha awali cha BancABC Super8 kesho

KIVUMBI cha hatua ya makundi ya michuano ya BancABC Super8 inatarajiwa kuhitimishwa kesho kwa viwanja vinne kuwaka moto katika miji tofauti ya Tanzania Bara na Zanzibar. Kwa mujibu wa ratiba ya makundi ya michuano hiyo inayoshirikisha timu nane, nne toka kila upande wa Tanzania Bara na Zanzibar ni kwamba Simba ambao walizinduka toka kwenye kipigo cha mabao 3-1 toka kwa Wakenya City Stars kwenye Simba Day kwa kuinyuka Mtende, itakuwa kwenye dimba la CCm Kirumba, Mwanza kuumana na Zimamoto ya Zanzibar. Mechi nyingine ya kundi hilo itazikutanisha timu za Jamhuri na Mtende zote za visiwani Zanzibae kwenye uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam. Kwa mechi za kundi B ratiba inaoonyesha Mtibwa Sugar iliyoigaragaza Azam nyumbani kwao 'Chamazi' kwa mabao 2-0 itashuka dimba la Amaan Zanzibar kuumana na mabingwa wa Ze nji, Falcon iliyolala kwa Polisi Moro katika mechi yao iliyopita. Nao Polisi Moro iliyorejea Ligi Kuu msimu huu, itakuwa kwenye uwanja wa Ushirika Moshi kuumana na Azam Fc. Timu nne, mbili toka kila kundi zitakazoshika nafasi mbili za juu zitacheza hatua ya nusu fainali ambazo zitachezwa kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Wanamasumbwi chipukizi Bongo kuvuna nini Idd Pili?

MASHABIKI wa ngumi za kulipwa nchini wanatarajia kupata burudani ya aina yake siku ya Idd Pili, wakati mabondia wawili chipukizi Ramadhani Shauri na Nassib Ramadhani watakapoanda ulingoni kuzipiga. Mabondia hao walio chini ya kocha Christopher Mzazi watazipiga na mabondia kutoka Kenya na Uganda katika michez itakayofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam kuwania mataji ya IBF. Shauri yeye atapanda ulingoni kuzichapa katika pambano la kuwania ubingwa wa IBF-Afrika uzani wa vinyoya (Featherweight) la raundi 10 dhidi ya Mganda, Sunday Kizito. Bondia Nassib anayeshikilia taji la chama cha World Boxing Forum (WBF), atatangulia kuzipiga na Twalib Mubiru kutoka Kenya katika pambano la uzani wa Bantam kuwania ubingwa wa IBF-Afrika Mashariki na Kati. Michezo hiyo yote inaratibiwa na promota Lucas Rutainurwa ambaye ni Mkurugenzi wa kampuni ya Kitwe General Traders na kusimamiwa na Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa nchini, TPBC. Kwa mujibu wa Rais wa TPBC ambaye pia ni Rais wa IBF Afrika/USBA, Onesmo Ngowi, pambano la Shauri na Kizito ndilo pigano kuu (main bout) na limepewa jina la 'The Rumble in the City of Heaven's Peace'. Ngowi, amemtaja Shauri kama 'mfalme' mpya aliyeanza kutishia hadhi za mabondia wengine nchini kutokana na kipaji kikubwa alichonacho katika mchezo huo wa ngumi za kulipwa. Rais huyo alisema rekodi aliyonayo na namna ya uchezaji wake akiwa ulingoni imemfanya awe anamfananisa na nyota wa zamani wa ngumi za kulipwa kutoka Marekani Sugar Ray Leonard. Katika umri alionao usiozidi miaka 25, Shauri tayari amekuwa na kivutio cha aina yake kutokana na haiba yake ya uchezaji na rekodi aliyonao tangu aanze kucheza mchezo huo chini ya kocha Mzazi wa gym iliyopo Mabibo jijini Dar es Salaam. Bondia huyo amecheza mapambano 15, akishinda michezo 12, kupoteza miwili na kuambulia sare moja, huku akishikilia nafasi ya pili kati ya 40 katika orodha wa mabondia wa uzito wake akitangliwa na Roger Mtagwa. Kwa upande wa mpinzani wake yeye ana rekodi ya kucheza mapambano 22 akishinda 12, kupoteza tisa na kupata sare moja. Ngowi anaamini pambano hilo litasisimua mashabiki wengi wa ngumi ambao kwa mua mrefu hawajapata kushuhudia mabondia vijana wakiwania mataji ya kimataifa. 'Ni zamu ya kuwapa nafasi mabondia chipukizi kuonyesha vipaji vyao na kuwania mataji ya kimataifa kuitangaza Tanzania," alisema Ngowi. Kuhusu pambano la Nassib Ramadhani, Ngowi alisema nalo linatarajiwa kuwa gumzo kutoka na rekodi alizonazo bondia huyo aliyecheza mapambano 11 na kushinda tisa akipoteza mawili. Nassib pia ndiye anayeongoza orodha wa mabondia 21 wa Tanzania wa uzani wake huku katika orodha ya dunia akishika nafasi ya 88 kati ya mabondia 636. Mpinzani anayecheza nae rekodi yake inaonyesha amecheza michezo 20 akishinda 11 na kupoteza saba huku akitoka sare miwili, hali inayofanya pambano lao litakuwa na msisimko na mvuto wa aina yake. Mbali na michezo hiyo siku hiyo kwa mujibu wa Ngowi kutakuwa na michezo mingine kadhaa ya utangulizi ambayo itatoa burudani kwa mashabiki wa ngumi wa mkoa wa Dar es Salaam na mikoa ya jirani. Ngowi alisema lengo la Kamisheni la Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBC ni kuhakikisha kila miezi miwili kunakuwa na mapambano ya kimataifa kwa mabondia wa Tanzania baada ya kushuhudiwa 'ukame' wa mataji kwa muda mrefu. "Pia lengo letu ni kutoa nafasi kwa mabondia chipukizi kuonyesha vipaji vyao sambamba na kuendeleza mpango maalum ulianzishwa na IBF-Afrika/USBA kutangaza utalii kupitia mchezo huo wa ngumi," alisema. Tayari mabondia hao watakaoonyeshana kazi siku hiyo ya Idd Pili, wamejichimbia kambini wakijiandaa na mapambano hayo, huku mratibu Lucas Rutainurwa, akisisitiza kila kitu kinaendelea vema akiwataka mashabiki wa ngumi kujitokeza siku ya siku. Kama alivyonukuliwa Rais wa TPBO ambaye pia ni msemaji wa TPBC, Yassin 'Ustaadh' Abdallah, huenda hiyo ikawa ni nafasi nzuri kwa mabondia hao chipukizi wa Tanzania kuanza safari ndefu ya kufikia mafanikio yaliyowahi kufikiwa na wakongwe kama Rashid Matumla aliyewahi kunyakua ubingwa wa dunia wa WBU. Tusubiri tuone kipi kitakachovunwa na mabondia hao katika michezo
yao hiyo, ambayo itafanyika wiki chache kabla ya kumshuhudia Mtanzania mwingine, Thomas Mashale hajapanda ulingoni nchini Ujerumani kuwania taji la UBO Vijana uzani wa Kati kwa kupigana na mwenyeji wake Arthur Hermann. Awali pambano hilo linaloratibiwa na Becker BoxPromotion lilipangwa kufanyika wiki iliyopita nchini humo, lakini limeahirishwa hadi Septemba 5 mjini Berlin, Ujerumani.

African Lyon yamnasa kocha mpya toka Argentina

KLABU ya soka ya African Lyon jana imemtambulisha kocha wao mpya kutoka Argentina, Pablo Ignacio Velez, waliyeingia naye mkataba wa mwaka mmoja, huku mwenyewe akiahidi kufanya mabadiliko zaidi ya soka kwenye timu hiyo. Pablo raia wa Argentina aliyasema hayo jana baada ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja kuitumikia timu hiyo na kusisitiza lengo lake kubwa ni kuhakikisha vijana wanapewa nafasi ya kuonyesha vipaji vyao na ndivyo itakavyokuwa Afrika Lyon. “Sikuja Tanzania kutafuta pesa, ndoto yangu kubwa ilikuwa kufundisha soka barani Afrika hivyo wakati ni sasa,” alisisitiza kocha anayezungumza lugha ya ‘kiispanyola’. Pablo alisema “kazi ya aina yoyote lazima ipewe muda na mchezaji lazima atengenezwe hivyo watanzania wawe na subira kwa ajili ya kupata matunda mazuri ya vijana hapo baadae kutoka African Lyon. Kocha huyo aliyewahi kuzichezea timu za taifa za vijana chini ya miaka 17 na 20 za Argentina hakusita kusisitiza suala la nidhamu kwa wachezaji wa timu hiyo ya ndani na nje ya uwanja. “Nidhamu ni muhimu kwa wachezaji wangu cha msingi tushirikiane katika kufanikisha hili kwa vijana kwani mchezaji anatakiwa kati ya miaka 18 na 19 awe ametengeneza jina kupitia soka ,” alisema Pablo. Naye Mmiliki wa African Lyon, Rahmu Kangezi alisema lengo la kumleta kocha huyo ni kuhakikisha timu hiyo inajongea mbele zaidi. Kangezi alisema licha ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja lakini wanaweza kumtumia Pablo kwa kipindi kirefu kulingana na mfumo wa kuhakikisha wanaendeleza vijana katika timu yao. “Pablo ni zaidi ya kocha, ana uwezo pia amecheza mpira pia ni kocha wa kwanza kutoka Argentina kuja Tanzania hivyo tunaimani timu yetu ya African Lyon itafika mbali zaidi kisoka,” alisitiza Kangezi. Pablo mwenye miaka 38 aliyechukua mikoba iliyoachwa na Jumanne Chale amewai kuifundisha klabu ya Atletico Colo Colo De Chile (1998). Klabu nyingine alizowai kufundisha ni Atletico Calchin (2000), Atletico Belgrano De Cordoba (1997), Atletico River Plate (1993-1995). Klabu nyingine ni Banco De Cordoba (1991 na 1997), Deportivo Lasallano (1992) Atletico Argentino Penarol kwa miaka minne na klabu nyingine nyingi za Hispania na Argentina.

Yanga kutafuta kocha mwingine iwapo...!

UONGOZI wa mabingwa wa soka Afrika mashariki na Kati, Yanga, umesema utatafuta kocha mwingine kama mwalimu wao Tom Saintfiet atapata kazi ya kufundisha timu ya taifa ya Kenya. Hata hivyo, Yanga imesema mpaka sasa haina taarifa rasmi juu ya kocha wake huyo kutakiwa na Shirikisho la soka Kenya kwa ajili ya kuifundisha timu yake ya taifa hivyo inasubiri barua kutoka KFF. Akizungumza na Nipashe jana, Afisa habari wa Yanga, Luis Sendeu, alisema endapo KFF itaonyesha dhamira ya kumtaka Saintfiet hawatomzuia. "Hatutaweza kumzuia," alisema Sendeu. "Tutakaa naye na kujua nini cha kufanya, lakini napenda kuwaambia kuwa sisi kama Yanga hatuna taarifa za kocha wetu kutakiwa Kenya. "Ila kama tutapata taarifa rasmi uongozi utajua nini cha kufanya," alisema Sendeu. Itabidi klabu itafute kocha mwingine endapo itaridhia kusitisha mkataba wa miaka miwili wa mwalimu huyo Mbelgiji aliyeanza kuifundisha mwezi uliopita. Sendeu alisema kuwa kwa sasa kocha huyo anaendelea na programu zake za kuiandaa timu kwa ajili ya msimu ujao wa ligi kuu ya Bara ambao utaanza mwezi ujao. "Kocha Tom yupo na kikosi akikiandaa kwa ajili ya ligi kuu ya Bara... na yeye ana programu zake ambazo anazifanyia kazi kuhakikisha timu inakuwa katika kiwango cha juu zaidi ya sasa pindi ligi kuu itakapoanza," alisema. Alisema viongozi wa Yanga wanaamini uwezo ambao timu hiyo ilionyesha kwenye mashindano ya Kagame ndiyo ambao utahamishiwa kwenye ligi na kufuta makosa waliyoyafanya msimu uliopita ambapo ilivuliwa ubingwa na mahasimu wao Simba. Yanga ilionyesha soka la hali juu kwenye michuano hiyo licha ya kuanza kwa kipigo, ikishinda michezo yake sita iliyofuatia hadi kutetea Kombe la Kagame. CHANZO:NIPASHE JUMAMOSI

Mkali wa mikono aimwagia sifa Azam Fc

NYOTA wa klabu ya mpira wa mikono ya Ngome, Ally Khamis 'Muba' ameimwagia sifa klabu ya Azam Fc kwa mafanikio makubwa iliyopata kwa kipindi kifupi tangu iingie kwenye Ligi Kuu Tanzania na kudai imeleta mapinduzi yanayopaswa kuwa changamoto kwa Simba na Yanga. Muba, aliyewahi kuwa mlinda mlango enzi akisoma kabla ya kujitosa kwenye mpira wa mikono, alisema kinachofanywa na Azam, kinapaswa kuigwa na klabu nyingine katika kuendeleza mchezo huo sambamba na kurejesha heshima ya timu za Tanzania katika anga la kimataifa. Alisema, anaamini kungekuwa na klabu zenye malengo na mipango inayotekelezeka kama Azam ni wazi soka la Tanzania lingepiga hatua kubwa. "Lazima niseme ukweli mie nakunwa na mafanikio ya Azam, yanatia moyo na kuonyesha wenye timu hiyo walivyo na malengo na nadhani klabu nyingine zinapaswa kujifunza kutoka kwao iwapo zinataka kufika mbali," alisema. Muba, alisema pamoja na kuipongeza klabu hiyo, bado haipaswi kubweteka kwani safari iliyopo mbele yao ni kubwa na inayohitaji moyo wa ustahamilivu hususani katika ushiriki wao wa michuano ya kimataifa ambapo mwakani itaiwakilisha Tanzania katika Kombe la Shirikisho Afrika.

Kocha wa Juventus atupwa 'jela', kisa...Rushwa!

ROME, Italia MAHAKAMA ya Michezo ya Italia imemtupa 'jela' kocha wa mabingwa wa nchini humo, Juventus, Antonio Conte kwa muda wa miezi 10 jana kwa kosa la kushindwa kuripoti tukio la upangaji matokeo ya mechi katika kashfa ya kamari ya upangaji matokeo ambayo imetikisa soka ya Italia, shirikisho la soka limesema. Kocha huyo aliyeiongoza Juventus kutwaa ubingwa wa Serie A msimu uliopita, ameadhibiwa kwa mechi mbili za Siena za Mei 2011, wakati akiwa kocha wa timu hiyo ya daraja la kwanza, Serie B. Mahakama hiyo ilimuachia beki wa klabu hiyo Leonardo Bonucci na winga wa kulia Simone Pepe kwa kuwaona hawakuhusika na kashfa hiyo. Waendesha mashitaka walisema kundi la wacheza kamari maharamia wa kimataifa lilikuwa likilipa wachezaji ili wafungishe timu zao katika kashfa ya upangaji matokeo michezoni ambayo inafanana na ile iliyochafua sifa ya soka ya Italia katika miaka ya 1980. Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, mpo!
Chanzo: Reuters

Mabeki wa pembeni waipa presha Simba

BAADHI ya wanachama na mashabiki wa klabu ya soka ya Simba, wameanza kuwa na wasiwasi na uwezo wa timu yao, wakiushauri uongozi kushirikiana na benchi la ufundi kuhakikisha wanaimarisha safu ya ulinzi hususani mabeki wa pembeni. Wanachama na mashabiki hao wamedai kuingiwa na wasiwasi kutokana na matokeo ya hivi karibuni iliyopata timu yao ikionekana kupwaya karibu kila idara jambo linalowatia shaka kama wataweza kutetea taji lao la Ligi Kuu Tanzania Bara. Mmoja wa wanachama hao, aliyeomba kuhifadhiwa jina lake, alisema beki za pembeni wa Simba zimepwaya na kukosekana watu wa kuifanya timu yao itishe kama ilivyozoeleka na kudai ukuta huo umeathiriwa kutokana na kuumia mara kwa mara kwa ajina Nassor Cholo na Amir Maftah. "Kwa miaka mingi Simba imekuwa ikisifika kuwa na 'ma-fullback' visiki na viungo imara, lakini kwa mechi kadhaa zilizopita tumebaini safu hizo zimepwaya na ajabu uongozi umeimarisha kiungo na kusahau beki hizo za pembeni," alisema mwanachama huyo. Naye mnazi mkubwa wa klabu hiyo Leila Mwambungu, alisema kuna haja viongozi na benchi la ufundi kuhakikisha wanasaka wachezaji wa pembeni mapema ili kuimarisha kikosi kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa ligi kuu Septemba Mosi na michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika mwakani. "Safu ya ulinzi ya Simba ina tatizo hasa mabeki wa pembeni, hivyo viongozi na benchi la ufundi lifanyie kazi dosari hiyo mapema kabla ya kuanza kwa ligi ili tusije tukaumbuka," alisema Leila. Simba iliyong'olewa kwenye hatua ya Robo Fainali ya michuano ya Kombe la Kagame kwa kipigo cha mabao 3-1 toka kwa Azam, ilirejea kupokea kipigo kama hicho Jumatano iliyopita dhidi ya City Stars ya Kenya wakati wa sherehe za Simba Day zilizofanyika jijini Dar. Kabla ya kipigo hicho cha Wakenya, Simba ililazimishwa sare ya baoa 1-1 na Jamhuri ya Kenya katika michuano ya Super 8 baada ya kuongoza bao 1-0 katika pambano lililochezwa kwenye uwanja wa Chamazi, nje kidogo ya jijini Dar.

Sikia hii, eti :Kazimoto ni kama Xavi, Iniesta

MCHEZAJI nyota wa timu ya mpira wa kikapu ya ABC, Gilbert Batunga 'B10' amesema kwa sasa nchini hakuna kiungo mwenye kiwango cha kipekee kama alichonacho Mwinyi Kazimoto wa klabu ya Simba. Batunga, alisema kwa kiwango alichonacho Kazimoto kiuchezaji anaweza kumlinganisha na viungo nyota wa klabu ya Barcelona na timu ya taifa ya Hispania, Xavi na Andre Iniesta. Mkali huyo, alisema Kazimoto ana sifa zote za mchezaji wa nafasi yake na kudai iwapo kama atapewa nafasi zaidi huenda akafika mbali kwa sababu kokote anaweza kucheza. "Kwa kweli licha ya Tanzania kuwa na vijana wenye vipaji katika soka, binafsi sijaona kama Mwinyi Kazimoto. Huyu jamaa ana ujua na kuuchezea mpira, nadhani akipewa nafasi huenda akafika mbali na kuitangaza nchi kimataifa," alisema. Alisema, anaamini umahiri wake ndio ulioifanya Simba kuamua kumvua 'gwanda' toka JKT Ruvu ili wapate huduma zake, ingawa alisema hali ya majeruhi imekuwa ikimuangusha mkali huyo. Mwinyi Kazimoto, anayeichezea pia timu ya taifa, Taifa Stars alitua Simba msimu uliopita akitokea JKT Ruvu, amekuwa akitajwa kama mmoja wa viungo mahiri nchini kwa sasa akiwekwa kundi moja na wakali kama Salum Abubakar 'Sure Boy', Shaaban Nditi na wengineo.

Baada ya Chaguo, Richie ana Tamaa kwa Rado

BAADA ya kukamua vilivyo katika filamu ya 'Chaguo Langu', muigizaji mahiri nchini Single Mtambalike 'Richie', ameibuka katika kazi nyingine ambayo imekuwa ikifanya vema sokoni iitwayo 'Tamaa Yangu' ya msanii, Simon Mwapagata 'Rado'. Akizungumza na MICHARAZO, Rado alisema filamu hiyo miongoni mwa kazi zake tatu ambazo zimeingizwa sokoni hivi karibuni, ambapo mbali na 'Tamaa Yangu', nyingine ni 'Hatia' na 'XXL'. Rado alisema katika filamu ya 'Tamaa Yangu', mbali na Richie, pia ameigiza na wakali kama Deo Shija na mwanadada Regina Mroni, aliyewahi kutamba na filamu ya 'Aisha'. "Nimeachia kazi tatu kwa mpigo, XXL, 'Hatia' na 'Tamaa Yangu' ambayo nimeigiza na mkongwe Single Mtambalike, Deo Shija na Regina Mroni," alisema Rado. Kutoka kwa kazi hiyo ya 'Tamaa Yangu' kunamfanya Richie, aendelea kukimbiza sokoni miongoni mwa wakongwe wa fani hiyo kwani ni wiki kadhaa ameachia kazi yake mpya ya 'Chaguo Langu aliyoigiza na wakali kama Jacklyn Wolper na Adam Kuambiana. Kabla ya 'Chaguo Langu', Richie alitamba kwa muda mrefu na filamu ya 'Diana', aliyoigiza na Halima Yahya 'Davina' na Sabrina Rupia 'Cath'. Mkongwe huyo aliyewahi kutamba akiwa na makundi ya Mambo Hayo na Kamanda Assemble yaliyokuwa wakionyesha michezo yake kwenye vituo vya ITV na CTN, kwa sasa inaelezwa yupo 'location' kwa ajili ya kufyatua kazi nyingine mpya.

TAFF, Bongo Movie, wasambazaji waungana kudhibiti wezi

MAKAMPUNI ya usambazaji wa kazi za wasanii kwa kushirikiana na Shirikisho la Filamu Tanzania, TAFF na Mamlaka ya Mapato Tanzania, TRA, wameungana pamoja na kutangaza 'vita' dhidi ya maharamia na wezi wa kazi za wasanii kwa lengo la kukomesha vitendo hivyo. Wasambazaji hao, Steps Entertainment, PAPAZI, Msama Promotions na wengine wameamua kushirikiana na TRA, Bongo Movie na TAFF kwa nia ya kukomesha vitendo hivyo sawia na kulinda masilahi ya wasanii ambao wamenyonywa kwa muda mrefu. Wakizungumza katika mkutano uliofanyika jana jijini Dar es Salaam
viongozi wa 'umoja' huo walisema umefika wakati wa kukomesha tatizo hilo la muda mrefu ambalo limekuwa likiwakatisha tamaa wadau wa sanaa nchini. Rais wa TAFF, Simon Mwakifwamba, alisema wameona hakuna njia ya kukomesha hilo kama sio kufanya kazi kwa pamoja katika kulishughulikia akidai anashangazwa na kukithiri kwa hali hiyo ilihali kuna sheria juu ya udhibiti wa jambo hilo. Alisema, mbali na muunganiko wao, pia wanaiomba serikali kutekeleza ahadi yake ya kuwasaidia wasanii kupambana na maharamia, aliodai wapo kila pembe ya nchi hii wakifanya uhalifu wao kwa kujiamini kana kwamba wapo juu ya sheria. Mwakifwamba aliongeza kwa kusema lau kazi za wasanii zitasimamiwa vizuri, zitaliongezea taifa pato kubwa kw avile soko la sanaa kwa sasa limekuwa na mafanikio makubwa ingawa bado inawanufaisha wachache. Naye Mwenyekiti wa Bongo Movie, Jacob Steven 'JB' alisema sanaa inaweza kuwa na nafasi ya tatu kwa kuchangia pato la taifa ukiacha pato linalotokana na sekta za madini, maliasili na utalii. Kwa upande wa TRA, Meneja Usimamizi, Msafiri Ndimbo alisema Mamlaka hiyo imejipanga kudhibiti wizi wa kazi hizo kuanzia Januari mwakani baada ya serikali kupitia Bunge lake kukubalina kuweka mikakati ya kupamba na suala hilo.

Wednesday, August 8, 2012

Azam yazidi kung'ang'ania Redondo yaionya Simba

WAKATI kiungo Ramadhani Chombo 'Redondo' akisisitiza kuwa, hana mkataba na klabu ya Azam na ndio maana ameamua kusaini kuichezea Simba, uongozi wa klabu ya Azam umeendelea kushikilia msimamo kwamba kiungo huyo ni mali yao na Simba 'imeliwa'. Katibu Mkuu wa Azam, Idrissa Nassor alisema wao sio wehu wakurupuke kung'ang'ania kwamba Redondo ni mali yao iwapo hawana mkataba nae na kudai Simba wanajisumbua na kuweza kuwakuta kama lililowakuta kwa mchezaji Ibrahim Juma 'Jebba' waliokuwa wakimng'ang'ania kutaka kumsajili. Nassor ambaye ni maarufu kwa jina la 'Father' alisema, Redondo ni mali yao kwa vile wana mkataba utakaomalizika mwakani mwezi Juni, na hivyo Simba kama wanamhitaji kiungo huyo ni wajibu wa kuzungumza nao ili wawape kwa utaratibu unaotakiwa. "Sio sio wajinga kumng'ang'ania Redondo, pia hatuwezi kumzuia iwapo anataka kwenda Simba, ila taratibu zinatakiwa kufuatwa kwa vile tunaye mkataba nae unaomalizika Juni mwaka 2013," alisema Nassor. Alisema kinachoendelea kwa Simba na Redondo hakutofautiani na sakata la Jebba ambaye Simba ilidai kumsajili na kwenda nae kwenye michuano ya Ujirani Mwema kabla ya kubaini kwamba walikuwa wakijisumbua kutokana na ukweli mchezaji huyo alikuwa na mkataba na Azam. Hata hivyo Redondo akizungumza na vyombo vya habari jana, alisema yeye hana mkataba na Azam kwa vile mkataka wake wa awali ulishaisha tangu Juni mwaka huu, pia akisema kilichomfanya aondoke ni kutoitwa na viongozi kupewa mkataba mpya. Pia alisema 'kifungo' cha miezi minne alichopewa na uongozi wa Azam kwa tuhuma za utovu wa nidhamu ni sababu nyingine iliyomfanya 'aipe' kisogo timu hiyo na kutua Simba ambayo aliichezea kabla ya kutua Azam misimu miwili iliyopita.