STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, August 27, 2013

Mpinzani wa Cheka kutua leo, Mashali bado 'amgomea' Maugo

http://www.minnesotaboxing.com/Interviews/phil_codrington.jpg
Bondia Phil 'The Drill'  Williams
Phil "The Drill" Williams/ SnapLocally.com
Phil 'The Drill' Williams
WAKATI bondia Phil 'The Drill' Williams kutoka Marekani pamoja na kocha na daktari wake wanatarajia kutua nchini usiku wa leo ili kumkabili Francis Cheka, Thomas Mashali ameendelea kusisitiza kuwa hatapigana na Mada Maugo siku ya Ijumaa.
Cheka na Williams wanatarajiwa kupigana kuwania ubingwa wa kimataifa wa WBF katika pambano la uzani wa Super Middle raundi 12 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, jijini Dar es Salaam siku ya Agosti 30.
Rais wa TPBO-Limired wanaosimamia pambano hilo na mingine itakayochezwa siku hiyo, Yasin Abdallah 'Ustaadh' alisema usiku wa jana wametuma tiketi ya bondia huyo na wasaidizi wake na watatua nchini leo saa nne kasorobo usiku.
Ustaadh alisema Mmarekani kutua kwa bondia huyo ni kuonyesha maandalizi ya pambano hilo yamepamba moto huku akiwaonya mashabiki na mabondia wasio na nidhamu kujihadhari mapema siku ya pambano kwa ulinzi utakaokuwepo.
"Bondia wa Marekani Phil Williams atatua nchini Saa 3:50 usiku wa kesho (leo) akiwa na kocha wake, Filbert Songola na Dk aitwaye Charles na TPBO-Limited tunawaonya mashabiki kujiepusha na uhuni siku ya pambano," alisema.
Alisema onyo hilo wanalitoa mapema kutokana na ukweli mapambano hayo yanatarajiwa kuhudhuriwa na mabalozi, mawaziri na viongozi wenye heshima zao na kwamba ulinzi utakuwa mkali hiyo asingependa wachache kuwavurugia.
Katika hatua nyingine bondia Thomas Mashali ameendelea kusisitiza kuwa hatapanda ulingoni Ijumaa kuzipiga na Mada Maugo akisema halitambui pambano hilo.
"Msimamo wangu ni ule ule kwa sasa akili yangu ipo kwenye pambano la kimataifa dhidi ya Mmalawi Chiotcha Chimwemwe nitakayepigana naye mjini Blantire nchini Malawi," alisema Mashali maarufu kama Simba  Asiyefugika.
Mashali alisema wameingia mkataba wa kupigana na Chimwemwe katika pambano la uzito wa kati litakalochezwa Oktoba 29 na kudai kwa kutambua ukali wa mpinzani wake ameanza mapema kujifua ili aweze kufanya vyema.

Kanali Msechu mgeni rasmi tamasha la Home Gym, Victoria kuwasha moto

Baadhi ya wanamuziki wa Victoria Sound, Mwinjuma Muumin na Waziri Sonyo wakiwajibika
WAKATI wadhamini wakianza kujitokeza kudhamini Tamasha maalum la kuadhimisha miaka 15 ya kituo cha mazoezi cha Home Gym, waratibu wamemtaja mgeni rasmi wa tamasha hilo kuw ani Kanali H.A Msechu wa 501.
Tamasha hilo linatarajiwa kufanyika Jumamosi hii kwenye uwanja wa Mwenge, jijini Dar es Salaam ukishirikisha michezo na wanamichezo mbalimbali wa soka, kutunisha misuli, kunyanyua vitu vizito na burudani ya muziki.
Mkurugenzi wa Home Gym, Andrew Mwangomango aliiambia MICHARAZO kuwa tayarui wadhamini wameanza kujitokeza kuwapiga tafu na kwamba tayari wamepata uthibitisho kuwa Kanali Msechu ndiye atakayekuwa mgeni rasmi.
"Kanali Msechu wa Kikosi cha 501 ndiye atakayekuwa mgeni rasmi wa tamasha letu ambalo linaendelea kuandikisha wanamichezo wanaopenda kushinda siku hiyo katika michezo wa kunyanyua vitu vizito na kutunisha misuli," alisema.
Mwangomango, aliongeza kuwa baadhi ya wadhamini wameanza kujitokeza  kuwapiga tafu na kuwaomba wengine wajitokeze wakati siku zikikaribia kwa ajili ya tamasha hilo litakalopambwa na bendi ya Victoria Sound.
"Bado tunahitaji wadhamini hivyo wenye kupenda kutusaidia wajitokeze kwani ni tamasha la aina yake likiwa na michezo ya kukikimbiza na kukamata kuku, kanga na sungura na soka litakalohusisha klabu za matevetani zaidi ya 20," alisema.
Kituo hicho cha Home Gym kilichopo Mwenge-Kijijini, kilianzishwa mwaka 1998 kikitoa mafunzo wa mazoezi ya viungo na michezo ya kunyanyua vitu vizito na utunishaji wa misuli.

Timu za Ruvu zachekelea kuanza vyema, yapania wapinzani wao wa Mbeya

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhaF1tsqvUmrtMICozA4dHcA_DetF8axYj97O_uDj0kkxxGOF6_BpM4UZbrAuxFzz8p04g6_20F6Y4D6lFqVkIPGh9tQ3Ad3NlFKR5UQCPex36z5AyqjybyV9U-_8S_GqOtYG6DPFj3-2QH/s640/JKT+RUVU+KIKOSI.jpg
JKT Ruvu
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEhXtdUgJUQpoqJDsDusQZKcGKBjAz5VsgkU1d7LoYMp8k9R4EJMliB6GKtLSqbJpXRRbSWfurfjs0QQYhasY-3DPyM87v27C4nM5jOY7vrLhH7s7iM01OrbSAtJ0p-IIcVEFh_2tSEaTI4E/s640/RUVU+SHOOTING.jpg
Ruvu Shooting
UONGOZI wa timu za Ruvu Shooting na JKT Ruvu za Pwani umefurahishwa na kuwapongeza makocha na wachezaji wao kwa kuanza vyema msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara kwa kupata ushindi wakidai huo ni mwanzo tu.
Ruvu Shooting ilianza kwa kishindo ligi hiyo kwa kuinyuka Prisons ya Mbeya kwa mabao 3-0,  wakati maafande wenzake wa JKT walipata ushindi wa 2-0 jijini Tanga walipoumana na Mgambo JKT.
Ushindi huo umeziweka timu hizo kileleni sambamba na Yanga walioishindilia Ashanti United kwa mabao 5-1 katika mechi za ufunguzi wa ligi hiyo mwishoni mwa wiki na kuufanya uongozi wa klabu hizo kuwapongeza kwa kazi nzuri.
Afisa Habari wa timu hizo za JKT, Masau Bwire alisema uongozi unawapongeza makocha Charles Boniface na Mbwana Makatta na wasaidizi wao pamoja na wachezaji wa kuanza vyema pazia la ligi kuu kwa kupata ushindi.
"Tumefurahishwa na mwanzo nzuri uliofanywa na timu zetu na tunawapongeza makocha na wachezaji kwa kazi nzuri waliyofanya tukiamini wataendelea kugawa dozi hata katika mechi zijazo. Hii ni tahadhari kwa wapinzani wetu msimu huu," alisema Bwire.
Bwire alisema kwa sasa timu zao zinaelekeza nguvu kwa mechi zao za kesho ambapo Ruvu Shooting itakuwa ugenini mjini Mbeya kuumana na Mbeya City, wakati 'ndugu' zao JKT Ruvu watakuwa Mabatini, Mlandizi kuvaana na Prisons.

Tchico Tchikaya: Mkali aliyewakimbiza akina Kanda Bongoman

* Kibao cha Soukous Machine kilimtambulisha dunia nzima
* Kwa sasa yupo Australia na bendi mpya ya Warako Musica



http://img.youtube.com/vi/U6ojiWpk6tk/0.jpg
UNAPOLITAJA jina la Tchico Tchicaya kwa wapenzi na mashabiki wa muziki wa Soukous, akili zao zitaenda hadi miaka zaidi ya 20 iliyopita wakikumbukia kibao cha  Soukous Machine kilichomtambulisha mno mwanamuziki huyo.
Kibao hicho kilichofyatuliwa mwaka 1987, kilimtambulisha vema Tchico kama mmoja wanamuziki wabunifu na aliyekuwa akipenda na kuuenzi utamaduni wa nchi yake ya Jamhuri ya Congo (Congo-Brazzaville).
Wakati kibao hicho kinatamba wanamuziki wakali wa Congo-Kishansa kama akina Pepe Kalle, Nyboma Mwandido, Kanda Bongoman na wengine ndio kwanza walikuwa wameanza kuiteka dunia kwa muziki wao na kumfanya Tchico kuenda nao sambamba na nguli hao ambao baadhi wameshafariki.
Nguli huyo ambaye kwa sasa ameweka maskani yake nchini Australia akiwa na bendi mpya iitwayo Warako Musica akishirikiana na Passi Jo, katika kibao hicho aliweka madoido ya ngoma asilia na milio ya ndege iliyovutia.
Katika kibao hicho mwanamuziki huyo, alikuwa akiisifia Afrika na kutaja majina ya baadhi ya miji ya nchi za bara hilo, huku akiufagilia muziki huo wa Soukous, ambao unaendelea kubamba mpaka leo katika medani ya muziki.
Tchico aliyeanza muziki zaidi ya miaka 30 iliyopita, majina yake kamili ni  Pambou-Tchicaya Tchico, lakini majina yake ya mwisho ndiyo yakifahamika zaidi kwa wapenzi wa muziki wa Soukous aliokuwa akiupiga.
Ukali wa Tchico ulianza kuonekana mwaka 1970 alipoanza muziki kama muimbaji katika bendi iliyofahamika kwa jina la Monta Lokoka iliyokuwa na maskani yake katika mji mkuu wa Congo, Brazzaville.
Akiwa na bendi hiyo alifanikiwa kupakua na kutamba na albamu kali mbili zilizofahamika kwa majina ya Rina ya mwaka 1970 na Loemarthe iliyotoka mwaka 1971.
Miaka miwili baada ya kujiona kaiva vema, mkali huyo alijitosa katika bendi ya Les Bantous de la Capitale akiwa mmoja wa waimbaji nyota wa bendi hiyo iliyokuwa maarufu mwa makundi yaliyotamba enzi hizo jijini Brazzaville.
Ndani ya Les Bantous de la Capitale, Tchico alitoka na albamu za Isabelle ya 1972, Celia-Shantina (1973) na Santana ya mwaka 1974, ambapo baadaye alifyatua albamu nyingine za Shanta Maguy (1974), Sambela Sambela (1975) na Ah Ponton la Belle mwaka 1976 akiwa na kundi la African Kings.
Mwaka 1977 na 1979 Tchico alipeleka 'maujuzi' yake nchini Nigeria alipoishi na kufanikiwa kupakua albamu nne tofauti ambazo zilimpa mafanikio makubwa kiasi cha kubatizwa jina la utani la  Voix d'or.
Katika kipindi hicho cha mafanikio ndipo alipokuwa akiimba na mkali Lolo Lolita ambapo walifyatua albamu iliyotamba ya Jeannot.
Mwaka 1983, Tchico aliamua kwenda Paris Ufaransa, kabla ya kufuatwa baadaye na utiriri mkubwa wa wanamuziki wa Kicongo kwenda nchini humo.
Akiwa katika jiji hilo la maraha, Tchico, aliweza kurekodi nyimbo mbalimbali katika studio tofauti tofauti, kulikoenda sambamba na kubadilika kwa jina la bendi yake toka Afro Festival hadi Les Evades de Ponton la Belle na kisha baadaye Les Officiers de la Musique Africaine.
Nyota yake ilizidi kung'ara zaidi katikati ya mwaka 1980 na mwanzoni mwa 1990 baada ya kubadili jina la kundi lake toka Orchestre Kilimandjaro hadi kuwa La Voix d' Or au Soukous Machine akitumia moja ya vibao vilivyompaisha kama jina la kundi, ambapo alifyatua vibao mbalimbali vikali vilivyotambulisha karibu bara zima la  Afrika na dunia kwa ujumla.
Baadhi ya nyimbo alizotoa kipindi hicho ni pamoja na Lucie Matanga, Paris-Tropical, Les larmes de Les Iles, Kembo Na Nzambi, Guyguy wa Mapendo, Adios Luluna, Jambo Afrika, Deliverance na A'Argent Ange ou Demon.
Kutokana na kutambulika huko dunia nzima, mwanzoni mwa karne mpya yaani miaka ya 2000, aliamua kuhamia na kuweka makazi yake nchini Australia akiendelea na kazi yake ya muziki akiwa na Passi Joo katika bendi yake mpya iitwayo Warako Musica aliyotoa nao albamu ya 'Ya Banganga'.
Baadhi ya wanamuziki walioshiriki kutoa kibao cha Soukous Machine cha mwaka 1987 na ambacho pengine ndicho maarufu kwa Watanzania ni pamoja na yeye Tchico Tchicaya aliyeongoza katika uimbaji, Jacqueline Brouta na Samba Kadhy Bell waliokuwa waimbaji waitikiaji.
Katika gitaa la solo alikuwa Denis la Cloche, huku Casanova de Ketchel akicharaza gitaa la rhythms na katika gitaa zito la besi alisimama Remy Salomon, na 'mkaanga chips' (mpiga dramu) alikuwa ni Denis Hekimian.
Lolitta Babind alikuwa akipiga nyanga, wakati mpapasa kinanda alisimama mkali wa zamani aliyeitwa Tony na Jean Marie Kabongo na wajina wake, Jean Claude Leandre walikuwa wakipuliza ala za upepo Kabono akipuliza 'Domo la Bata' na mwenzie akipiga tarumbeta.
Mbali na kibao ca Soukous Machine, Tchico pia alitamba na vibao vingine kama Africa Dance Machine, Sonima, African Carnaval, Cocktail Tropical,
L'ambiance à Paris, Dynamic Afro-Soukous, L'argent domine le monde, Full Steam Ahead, Nostalgie d'Afrique, Amour maternel, Mon enfant na Giselle.
Nyingine ni pamoja na Amie Clara, Tania, Rosalie, Jeannot, Lucia, dans Tam Tam d'Afrique, Méditation, L'heure a sonné, Operation Soukous, Mamy Rosa, Josintha,  From Congo to Nigeria, Ah Ponton la Belle na nyinginezo.
Ingawa ni miaka mingi imepita bila ya nyimbo za mkali huyo kusikika hapa nchini, lakini bila shaka Tchico hatasahulika kirahisi kwa vile namna ya uvaaji wake na hata upigaji wake wa muziki katika bendi alizozifanyia kazi, umemfanya kuwa vichwani kwa wapenzi wa muziki hususani wa Soukous.

Monday, August 26, 2013

Mfanyabiashara mwingine wa madini auwawa kwa risasi Arusha

MFANYABIASHARA wa madini ya Tanzanite, Bw. Steven Alex, amepigwa risasi jana jioni na watu wanaodhaniwa kuwa majambazi eneo la Pangani, jijini Arusha na kuporwa zaidi ya sh. milioni 60.
Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, walisema mfanyabiashara huyo alikuwa ndani ya gari lake akiwa amepaki eneo la Pangani ili aweze kulipa madeni kwa watu waliokuwa wamemuuzia madini.
Walisema ndani ya gari hilo ambalo lilifungwa vioo, alikuwa na wenzake wawili ambapo ghafla walitokea vijana watatu waliokuwa na pikipiki aina ya Toyo ambazo namba zake hazikufahamika wakiwa wameifunika na mifuko ya nailoni.
“Walimgongea dirishani wakitaka afungue mlango, huyu mfanyabiashara hakufungua ndipo vijana hao walichomoa bastola na kuanza kugonga tena kwenye dirisha la gari. 
 
Emmanuel Shilatu

CCM yamaliza vikao vyake Dodoma, UVCCM yamtosa Shigella

Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiongoza kikao
cha NEC, mjini Dodoma leo mchana. Kushoto ni Katibu Mkuu
wa CCM Abdulrahman Kinana.
BASHIR NKOROMO, Dodoma

HALMASHAURI Kuu ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) leo imemamliza kikao chake cha siku tatu chini ya Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete ikiwa imeridhia mapendekezo kadhaa ya Kamati Kuu ya CCM, ikiwemo kumfuta uongozi Mbunge wa jimbo la Mjini Magharibi, Zanzibar,  Mansor Yusuf Himid.

Kikao hicho pia kimeridhia, uteuzi wa Makatibu wateule wapya wa Jumuia za CCM, za Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM), Jumuia ya Wazazi na Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT).

Katika uteuzi huo mapendekezo hayo yaliyofanywa na Kamati Kuu ya CCM, na kuridhiwa na NEC, kwa upande wa Umoja wa Vijana wa CCM ameteuliwa aliyekuwa Kaimu Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro, Sixtus Mapunda na kwa upande wa Jumuia ya Wazazi ni Mjumbe wa NEC kutoka Pemba, Seif Shabani Mohamed, huku kwa upande wa UWT akiachwa Katibu Mkuu wa sasa, Amina Makilagi.

Mapunda atachukua nafasi iliyokuwa imneshikiwa na Martine Shigela ambaye ameongoza UVCCM kwa miaka mitano sasa, na Seif Shabani Mohammed kutoka Pemba akichukua nafasi iliyokuwa ikishikiliwa na Hamis Suleiman Dadi ambaye pia amekuwa katika wadhifa kwa miaka mitano sasa.

Pia, NEC imeridhia mapendekezo  ya Kamati Kuu kwa ajili ya kuziba nafasi Makatibu wa CCM wa mikoa mitatu ya Morogoro,  Kaskazini Pemba na Geita ambayo kwa mujibu wa maelezo yaliyotolewa imekuwa wazi kwa muda mrefu sasa kutrokana na sababu mbalimbali ikiwemo kifo.

Kufuatia mapendekezo hayo ya Kamati Kuu, ambayo yameridhiwa na NEC, walioteuliwa na mikoa yao ikiwa kwenye mabano ni Msaidizi Kitengo cha  Uchaguzi, CCM Ofdisi Ndogo ya Makao Makuu ya CCM, Romuli Rojas John (Morogoro), aliyekuwa Katibu Katibu wa wilaya ya Mkinga, Kassim Mabrouk Mbarak (Kaskazini Pemba) na aliyekuwa Katibu wa CCM Igunga, Mary Maziku (Geita).

Kuhusu sakata la madiwani wa Bukoba mjini, CCM imesema suala hilo, linaendelea kushughulikiwa ambapo baada ya kikao hicho cha NEC, Kamati kuu iliendelea kukutana na viongozi wa wilaya ya Bukoba, Mwenyekiti wa CCM na Katibu wa wilaya hiyo.

Mapema kabla ya kikao cha NEC, Kamati Kuu ilikutana na Mbunge wa Bukoba mjini Khamis Kagasheki na Meya wa Manispaa ya Bukoba mjini na kuwahoji, wakati jana Kamati Kuu ilikutana na  Mwenyekiti na Katibu wa CCM mkoa wa Kagera.
 Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiongoza kikao cha NEC, leo Agosti 26, 2013 mjini Dodoma. Kulia ni Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana
 Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana akitoa utangulizi kabla ya Mwenyekiti wa CCm Rais Jakaya Kikwete (kushoto) kufungua kikao cha NEC, Agosti 26, 2013
 Baadhi ya wajumbe wa NEC, ukumbini. Kulia mstari wa mbele ni Mjumbe wa Kamati ya Ushauri ya Viongozi wastaafu wa CCM, John Malecela ambaye ni mwalikwa kwenye kikao hicho.
 Mjumbe wa NEC, Mama Salma Kikwete akiteta jambo na Katibu wa NEC, Uchumi na Fedha, Zakiah Meghji kabla ya kikao cha NEC kuanza, Makao Makuu ya CCM mjini Dodoma.
 Mjumbe wa NEC, Dk. Fenela Mkangala na Katibu wa NEC, Siasa na Uhusiano wa Kimataifa, Dk. Asha-Rose Migiro wakijadili jambo kabla ya kikao cha NEC kuanza leo Agosti 26, 2013, Makamo Makuu ya CCM mjini Dodoma.
Wajumbe wa NEC kutoka Pemba wakiwa nje ya ukumbi kabla ya kikao kuanza. Kutoka Kushoto ni Hamadi Bakari Ali, Mwinyi Fakih Hassan, Ali Issa Ali,  Masoud Mohammed Abdallah, Seif Shaaban Mohammed na Mussa Fumu Mussa.

Jaji Francis Mutungi aapishwa kuongoza ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa

 Rais Jakaya Mrisho Kikwete akimkabidhi vitendea kazi Msajili mpya wa Vyama vya Siasa Jaji Francis Mutungi Ikulu jijini Dar es salaam leo.
 Jaji Mutungi akila kiapo
 Picha ya pamoja.

Mabao 19 yafungwa pazia la Ligi, Tegete, Mkude, Kondo nouma, wawili wajifunga wenyewewaan


Jerry Tegete (kulia) akiwa na baba yake
JUMLA ya magoli 19 yamepachikwa katika siku ya ufunguzi wa pazia la Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2013-2014, huku wachezaji watatu, Jerry Tegete wa Yanga, Jonas Mkude wa Simba na  Bakar Kondo wa JKT Ruvu wakiongoza msimamo wa wafungaji kwa sasa.
Tegete aliyafunga mabao hayo wakati Yanga wakiiua Ashanti Uniteda kwa mabao 5-1, wakati Mkude aliwatungua Rhino Rangers na Kondo alifanya hivyo wakati JKT wakiizamisha Mgambo JKT kwao jijini Tanga.
Mechi sita kati ya saba zilizochezwa kwenye ufunguzi wa ligi hiyo zilikuwa na mabao, wakati pambano la jijini Mbeya kati ya wenyeji Mbeya City na Kagera Sugar ndilo pekee lililoisha bila kutikiswa nyavu.
Kadhalika mechi mbili kati ya hizo saba zilishuhudiwa wachezaji wakijifunga magoli, ambapo Laurian Mpalile alijifungwa na kuisaidia Ruvu Shooting kupata ushindi mnono wa mabao 3-0 dhidi ya Prisons anayoichezea hali iliyomkuta pia beki wa Oljoro JKT, Yusuf Machonge akliyeunganisha wavuni mwake mpira uliopigwa na Mkenya Crispian Odulla wa Coastal Union wakati Wagosi wa Kaya wakishinda mabao 2-0 jijini Arusha.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena Jumatano wiki hii kwa timu zote 14 kushuka dimbani viwanja saba tofauti ambapo jijini Dar vinara na watetezi wa ligi hiyo, Yanga itawalika Coastal Union, huku Simba itakuwa jijini Arusha kuvaana na Oljoro, wakati JKT Ruvu itarudi nyumbani Pwani kuumana nna Prisons Mbeya.
Mechi nyingine itazikutanisha Kagera Sugar itakayokuwa dhidi ya ndugu zao wa Mtibwa kwenye uwanja wa Manungu,Turiani
Ratiba ya mechi hizo zijazo za Jumatano ni kama ifuatavyo;
Mtibwa Sugar vs Kagera Sugar
Rhino Rangers vs Azam
JKT Ruvu  vs Prisons
Mbeya City vs Ruvu Shooting
Mgambo  vs Ashanti United
JKT Oljoro vs Simba
Young  vs Coastal Union

Msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2013-2014                                    P  W  D  L  F  A  GD  PTS
Yanga                     1   1   0   0   5  1    4    3
Ruvu Shooting        1   1   0   0   3   0   3    3
Coastal Union         1   1   0   0   2   0   2    3
JKT Ruvu               1   1   0   0   2   0   2    3
Rhino Rangers        1    0   1   0   2   2   0    1
Simba                     1   0   1   0   2   2   0    1
Azam                     1    0   1   0   1   1   0    1
Mtibwa Sugar         1   0   1   0   1    1   0   1
Kagera Sugar         1    0   1   0   0   0   0   1
Mbeya City            1    0   1   0   0   0   0   1
Mgambo                1   0   0   1   0   2   -2   0
Oljoro                    1   0   0   1   0   2   -2   0
Prisons                   1   0   0   1   0   3   -3   0
Ashanti                   1   0   0   1   1   5   -4   0

Wafungaji:
2- Jerry Tegete (Yanga), Jonas Mkude (Simba), Bakar Kondo (JKT Ruvu)
1- Abdul Banda (Coastal), Haruna Niyonzima, Nizar Khalfan, Simon Msuva (Yanga), Saad Kipanga, Iman Joel (Rhino Rangers), Aggrey Morris (Azam), Laurian Mpalile (Prisons-OG), Elias Maguli, Jerome Lembeli (Ruvu Shooting),  Yusuph machonge (Oljoro-OG), Juma Liziu (Mtibwa Sugar), Shaaban Juma (Ashanti Utd)

Jina la Rais Kikwete lahusishwa kutaka kupora ardhi ya wanakijiji Bagamoyo

Katibu wa wamiliki wa mashamba na makazi wa kijiji cha Buma, Gumbo Majibwa akisoma taarifa kwa wananakijiji wenzake, huku pembeni yake Mwenyekiti Hassani Tenela akimsikiliza kwa makini katika mkutano wao wa kupinga kutaka kuchukuliwa kwa maeneo yao ili kumpish mradi wa hospitali ya kimataifa inayodaiwa itamilikiwa JWTZ
Mmoja wa wamiliki wa mashamba na makazi wa kijiji cha Buma akiandikisha jina katika karatasi ya mahudhurio

Sehemu ya wahudhuriaji wakisikiliza kwa makini taarifa juu ya sakata la kutaka kuporwa kwa maeneo yao


Wamikili wa mashamba na makazi kijiji cha Buma, wilaya ya Bagamoyo wakiwa kwenye mkutano wao uliofanyika juzi Jumamiosi
Mpaka kieleweke hapa....Ardhi yetu anaitaka Rais au Jeshi? wanaulizana wamamiliki wa ardhi ya kijiji cha Buma

Najiorodhesha ili wasiseme sikuwepo!
Khadija Omary mmoja wa wanaomiliki ardhi katika kijiji cha Buma akitoa hoja na kuuliza maswali katika mkutano wao wa Jumamosi.

Viongozi wa Kamati waliosimama kando ya gari wakisoma taarifa kwa wamiliki wenzao kuhusu sakata la kutaka kuporwa kwa ardhi yao,.

Na sisi tumo mpaka kieleweke!

Hata iwe vipi ardhi yetu haiwezi kuchukuliwa kienyeji


Husna Mohammed naye hakuwa nyuma kutoa maoni yake. Mwanamama huyo ni mmoja wa watu sita walioteuliwa katika kamati maalum ya kwenda kumuona Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Dk Shukuru Kawambwa ili kujua ardhi yao inachukuliwa na mwekezaji aliyetafutwa na Rais au ni JWTZ

"Tujiadharini isije kuna matapeli wanalitumia jeshi na jina la Rais kutaka kupora eneo leo. Hospitali gani inayojengwa katika eneo la ekari 1500? Dk Ally Ponza alihoji katika makutano huo
Tupo nanyi mwanzo mwisho mpaka kieleweke, hatukubali kirahisi kuachia ardhi yetu.

Frank Lyimo naye alitaka upatikane uthibitisho juu ya nani anayetaka kuchukua ardhi yao ili wasije wakambebesha lawama Rais Kikwete bure wakati kumbe hajui chochote kinachoendelea katika kijiji cha Buma.

Tupo pamoja

Katibu Gumbo Majubwa akitoa ufafanuzi baada ya kuulizwa na wanakijiji wenzake

Umoja ni nguvu! Hapa mwanzio mwisho mpaka tujue ukweli

Mwenyekiti wa kamati Hassan Tenela akifafanua jambo kwa wamiliki wenzake kuhusu ufuatuiliaji wao juu ya sakata la kutaka kuporwa ardhi yao.

"Jamani, tumeelezwa jeshi limetumwa tu kusaka ardhi, lakini mwekezaji ametafutwa na Rais alipokuwa nje ya nchi, lakini cha ajabu Mbunge wetu hajui na wala bajeti ya kulipwa fidia kwa kuporwa ardhi haipo kwenye Bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ya 2013-2014' Mwenyekiti Hassan Tenela akiwafafanulia wenzake mahali alipofikia.
JINA la Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dk Jakaya Kikwete linadaiwa kutumika kuwatisha wamiliki wa mashamba na makazi wa Kijiji cha Buma, kilichopo Kata ya Kiromo wilaya ya Bagamoyo-Pwani ili waachie maeneo yao yanayodaiwa kutaka kuporwa kwa kisingizio cha kupisha mradi wa hospitali kubwa ya kimataifa inayodaiwa itamilikiwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).
Wamiliki hao walitoa tuhuma hizo katika mkutano wa pamoja na  viongozi wa kamati yao, uliofanyika siku ya jumamosi kijiji hapo, ambapo uongozi wa kamati yao ulisema kuwa baada ya awali kuelezwa kwamba mradi huo ni wa JWTZ sasa wanaambiwa unahusu Rais Kikwete.
Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Hassani Tenela alisema katika kufuatilia kinachoendelea juu ya mgogoro wa kuporwa maeneo yao, alielezwa na Mwenyekiti wa Kitongoji cha Chambezi, Abdallah Mchayungu kuwa, mradi huo siyo wa jeshi bali ni mradi uliopelekwa kwao na Rais Kikwete baada ya kupata mwekezaji nje ya nchi, hivyo ni lazima waachie eneo lao.
Hata hivyo alisema taarifa hiyo imewapa shaka na kuhisi kama jina la Rais linatumika ili kuwatisha kwa sababu awali walijulishwa ni jeshi linalotaka eneo lao ambapo bila kupata ridhaa yao waliweka alama (beacons) wakitaka eneo kwao na katika kijiji cha jirani cha Mataya.
"Kama mradi huo una mikono ya Rais, vipi mwenyewe kutowahi kuzungumzia kokote na kama ni jeshi mbona katika bajeti ya wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ya 2013-2014 hakuna fungu la fidia kwa vijiji vya Buma na Mataya? Katibu wa wamiliki hao, Gumbo Majubwa alihoji.
Majubwa alisema pia suala kwamba fidia ya kila ekari kutofautiana kati ya vijiji hivyo viwili inawapa shaka na kusema wanaendelea kushikilia msimamo wao wa kugoma kutoa maeneo yao hadi wahakikishwe mwekezaji halali anayetaka eneo hilo na wakae wakubaliane naye.
Katibu huyo alisema taarifa walizonazo ni kwamba kwa wenzao wa Mataya waliolazimishwa na kuridhia kuachia maeneo yao watalipwa kila ekari Sh Mil. 3, wao wa Buma wakidaiwa watalipwa  Sh Mil 7-10 kwa kila ekari kitu kinachomshangaza kwa vile ardhi inayochukuliwa ni moja.
Mara baada ya uongozi wa wamiliki hao kutoa taarifa hiyo, baadhi ya wamiliki walisema licha ya kwamba tangu awali walikuwa na shaka na mradi ulioelezwa utafanyika katika vijiji hivyo vya Buma na Mataya ukihusisha eneo la ekari 1500, kutajwa kwa Rais Kikwete linawatia shaka zaidi.
"Tunaomba uongozi wa kamati ufuatilie ukweli kama mradi huu unamhusisha Rais au jina lake linatumika kama njia ya kututisha, kwani pia zipo taarifa kwamba hata Mbunge wetu Dk Shukuru Kawambwa hajui lolote kuhusu mradi huu," alisema Dk Ally Ponza.
Dk Ponza, pia alisema kwa ufahamu wake ekari 1500 kwa mradi wa hospitali tu ni kubwa mno na kuhoji isije  ikawa ni matapeli wanaotaka kulitumia jeshi au jina la rais kuwapora ardhi yao ambayo wanamiliki kwa miaka mingi iliyopita.
Wamiliki wengine pamoja na uongozi wa kamati yao ulimtuhumu diwani wao, Hassan Usinga, wakidai wanahisi anawazunguka na kushiriki katika kutaka kuporwa kwa ardhi yao hasa kutokana na usaliti wanaodai amekuwa akiuonyesha tangu saka hilo lilipoanza.
"Katika mkutano tuliofanya Agosti 17 alitamka mwenyewe akidai yu tayari kumpa mwanakijiji wa Mataya viwanja vitatu vilivyopimwa na vyenye hati vilivyo barabarani ili atoe eneo lake kupisha mradi huu, tujiulize iweje awe tayari kutoa eneo lake kwa mradi usiomhusu?" Alihoji Samuel Lema.
Naye Husna Mohammed, alisema wanahisi viongozi wa kitongoji na kijiji chao pamoja na diwani lao moja na wanafanya mipango kuporwa ardhi yao kwa kuwalazimisha kama wenzao wa Mataya na kutaka kuugomea mkutano waliouitisha viongozi utakaofanyika Septemba 7.
Baada ya majadiliano marefu hatimaye wamiliki hao na uongozi wao uliazimia mambo matatu kuunda kamati ya watu sita kufuatilia ukweli wa mtu anayetaka kuchukua eneo lao kama ni Mwekezaji wa Rais Kikwete au jeshi, kuonana na Mbunge wao Dk Kawambwa ili awape ufafanuzi juu ya kuwepo kwa mradi huo au la.
Pia kuuzuia mahakamani mkutano ulioitishwa na uongozi wa kijiji utakaohudhuriwa na wanaodaiwa wawakilishi wa jeshi wanaoitaka ardhi yao, mpaka kwanza wapate uthibitisho wa kuwepo kwa mradi huo wa hospitali.
Katika kutaka kupata ufafanuzi wa sakata hilo na tuhuma zilizoelekezwa kwake, MICHARAZO lilimsaka Diwani Hassan 'Wembe' Usinga' kwa njia ya simu ambapo kwanza alikanusha suala la kuwasaliti wapiga kura wake akidai mradi huo ulipitishwa na wanakijiji wenyewe mwaka 2010.
Hata hivyo alikiri juu ya ahadi yake ya kumpa mwanakijiji wa Mataya aliyemtaja kwa jina la Mzee Nyanza viwanja vitatu ili atoe ardhi yao kama njia ya kumsaidia kutoka porini na kukaa barabarani na kudai  siyo kama kuna mkono wake katika mradi huo.
"Wamiliki hao wanashindwa kunielewa tu, mimi nipo hapa kusimamia haki zao ndiyo maana umeitishwa mkutano Septemba 7 ili wazungumze na wanaotaka ardhi yao, kudai mimi nawasaliti ni kutaka kunionea kwani mradi ulitambulishwa tangu 2010, wakati sijawa diwani," alisema diwani huyo.
Aliongeza kilichotokea ni kweli haya yeye hakuwa anaujua mradi huu na kuufuatilia na kugundua waliokuwepo wakati mradi ukipitishwa waliouza maeneo yao kwa watu wengine ambao ndiyo wanaoibua hoja za kuugomea, huku akikana mradi huo kumhusu Rais Kikwete na kusisitiza ni mradi wa Jeshi, ingawa alishindwa kufafanua iweje lichukuliwe eneo kubwa la ekari 1500 huku bajeti la kulipia fidia haikutajwa katika bajeti ya 2013-2014 ya wizara yao.
"Aaah wanataka eneo hilo, lakini walisema wataanza kulipa eneo la eka 250 au 300 kwa vile bajeti waliyonayo kwa sasa inahusu eneo hilo, japo mpaka sasa bado utathimini wa kiwango cha malipo hakijaanza na siyo kweli kama fidia zinatofautiana katika vijiji hivyo," alisema diwani huyo.
Alifafanua kuwa ni kweli wanajeshi hao waliweka alama bila kuwashirikisha wamiliki halali wa maeneo hayo, akidai walifanya hivyo kuweka alama ya eneo wanalolihitaji kwanza na sasa ndiyo wameanza tararibu za kutaka kulimiki kihalali eneo hilo na kutaka wanakijiji kuelewa.
"Huu mradi utakuwa mkubwa kwa mujibu wa wawakilishi wa Jeshi waliokuja kujitambulisha kwa uongozi wa kijiji cha Buma Agosti 20, hivyo wananchi waupokee kwa moyo mmoja kwani una manufaa kwao, ingawa wana hiari ya kutoa eneo lao baada ya kujiridhisha," alisema.
Hata hivyo Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo, Dk Shukuru Kawambwa ambaye ni Waziri wa Elimu na Ufundi, alipoulizwa mradi huo, alisema ofisi yake haina taarifa rasmi ya kina na kudai ataanza kuufuatilia ili ajue ukweli wa mradi huo kisha atatoa taarifa kwa vyombo vya habari.
"Ofisi yangu ina taarifa za juu juu tu, tumeanza kufuatilia kujua ukweli ila nitahadharishe wananchi wawe makini na miradi inayoibuliwa hivi sasa ili wasiingwe mkenge," alisema Dk Kawambwa.
Naye Mkuu wa Wilaya hiyo, Ahmed Kipozi alipotafutwa na MICHARAZO alisema asingekuwa tayari kuzungumza suala hilo kwa vile suala hilo lipo chini ya Afisa Ardhi, ingawa alisema wilaya yake suala la migogoro ya ardhi imekuwa kama fasheni na kuikuta tangu aingie madarakani.
"Kwa kweli siwezi kufafanua lolote kuhusu suala la kijiji hicho cha Buma au kwingineko kwa sababu wanaohusika kutoa majibu kamili ni afya ardhi, ila ukweli migogoro ya ardhi hapa Bagamoyo ni ya kawaida, ni vyema kama ukija kupata ufafanuzi zaidi," alisema DC huyo.

Dillish wa Namibia ndiye mshindi wa BBA The Chase 2013







MSHIRIKI kutoka nchini Namibia, Dillish; ndiye aliyeibuka mshindi wa Shindano la Big Brother Africa-The Chase 2013 na kuondoka na kitita cha Dola za Kimarekani 300,000 katika fainali zilizofanyika usiku huu (Agosti 25)
Dillish mwenye miaka 24, hajawahi kuwa head of the house hata siku moja katika siku zote 91 alizokuwa ndani ya jumba, alishawahi kuwa nominated mara 5 na mara zote alibaki kwa kura za Africa, na hajawahi kuwa na mahusiano na mshiriki yoyote.


Dillish amekuwa ni mwanamke wa pili kushinda BBA tangu ilivyoanzishwa, baada ya Cherise kutoka Zambia kushinda kwenye BBA season  7 zilizopita


Katika top 5 waliobaki, alianza kutoka Beverly (Nigeria), akafuatia Melvin (Nigeria) na watatu kutoka ni Elikem (Ghana) wa nne ni Cleo (Zambia) na hatimaye Dillish kuwa mshindi wa BBA The Chase 2013.
Katika shindano hilo Tanzania iliwakilishwa na Nando na Feza ambao walitolewa mapema, Nando kwa utovu wa nidhamu na mwenzake kwa kup[ata kura chache wiki mbili zilizopita.

Barca bila Messi, Neymar akianzia benchi yashinda 1-0

Messi na Neymar

IKICHEZA bila ya nyota wake Lionel Messi na ikimuanzisha benchi Mbrazil Neymar, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Hispania, Barcelona wameibuka na ushindi kiduchu wa bao 1-0 ugenini dhidi ya Malaga.
Messi alishindwa kuwekwa kikosini kutokana na kuwa majeruhi, lakini hiyo haikuifanya Barca washindwe kufurukuta baada ya kujipatia bao la dakika za lala salama kabla ya kwenda mapumziko lililofungwa na beki Adriano Correia na kujipatia pointi tatu muhimu.
Huo ni ushindi wa pili mfululizo kwa mabingwa hao katika ligi hiyo baada ya wiki iliyopita kuanza kwa kishindo kwa kuicharaza Levante kwa mabao 7-0 walipoumana nao uwanja wa Nou Camp.
Katika mechi nyingine ziliuzochezwa leo, Atletico Madrid walipata ushindi mnono wa mabao 5-0 wakiwa nyumbani dhidi ya Rayo Vallecano, nazo timu za Levante na Sevilla zikitoshana nguvu kwa kutoka sare ya bila kufungana. 
Pambano linaloendelea kwa sasa ni kati ya Real Betis dhidi ya Celta Vigo ambapo mpaka sasa matokeo ni 0-0 ikiwa ni dakika ya 13.

Sunday, August 25, 2013

Man City yachinjwa Cardiff, Saldado akiendelea kuibeba Spurs

Hero: Fraizer Campbell's goals could prove vital all season for the newly-promoted side
Campbell (10) akishangilia moja ya mabao yake na wachezaji wenzake wa Cardiff
WAKATI Roberto Saldado akiendelea kuibeba Tottenham Hotspur kwa kuipa ushindi wa pili mfululizo katika Ligi Kuu ya England vijana wa Manuel Pellergrini, Manchester City jioni hii wameonja kipigo toka kwa Cardiff.
Man City wamejikuta wakizodolewa kwa kulazwa mabao 3-2 na waliopanda daraja Cardiff katika pambano lililojaa upinzani mkubwa.
Mabao mawili  ya lala salama yaliyofungwa kwa kichwa na Fraizer Campbell yalitosha kuwazima Man City waliokuwa ugenini na kuwapa wenyeji ushindi wa kwanza Cardiff.
City walikuwa wa kwanza kupata bao kupitia kwa Edin Dzeko muda mchache baada ya kuanza kwa kipindi cha pili baada ya dakika 45 za awali timu hizo kushindwa kutambiana.
Hata hivyo bao hilo lilirudishwa na Cardiff dakika ya 60 na Aaron Gunnarsson kabla ya Campbell kufunga mabao yake dakika za 79 na 87 na City kuambulia bao jingine dakika ya 90 lililofungwa na Alvaro Negredo.
Katika mechi nyingine ya ligi hiyo iliyotangulia kuchezwa, Tottenham ilipata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya wageni wao Swansea City kwa bao la penati iliyofungwa na Saldado ambaye ni bao lake la pili baada ya wiki iliyopita kuifungia pia Spurs bao la penati iliposhinda ugenini.

Rage nouma! Asaka ITC za Warundi na kuzipata watashuka dimbani Jumatano kuikabili Oljoro

Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage

Kifaa kipya cha Simba Gilbert Kazze ambaye ITC yake imeshatua na ataanza kibarua Jumatano jijini Arusha

Tambwe Amissi nyota wa mabao anayetarajiwa kuanza kazi na JKT Oljoro
  TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
 
MWENYEKITI wa Simba, Mhe; Ismail Aden Rage, leo mchana amefanikisha upatikanaji wa Hati za Uhamisho wa Kimataifa (ITC), kwa wachezaji wawili wa klabu hiyo kutoka nchini Burundi -Amissi Tambwe na Gilbert Kaze. 
Wachezaji hao wawili ambao pia ni tegemeo la timu ya soka ya taifa ya Burundi (Intamba Murugamba), hawakucheza katika mechi ya Ligi Kuu ya Tanzania iliyochezwa jana kutokana na kutokamlika kwa uhamisho huo, jambo lililoleta usumbufu mkubwa kwa benchi la ufundi, wachezaji wenyewe, uongozi na wapenzi na washabiki wa  klabu. 
Rage aliondoka jijini Dar es Salaam jana usiku na imechukua chini ya saa 24 kuweka kufanikisha suala hilo. Katika taarifa yake kwa wana Simba, Mbunge huyo wa Tabora Mjini alisema amelazimika kuingilia kati suala hilo kwa sababu lilihusu baadhi ya taratibu muhimu za Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) na ukweli kwamba viongozi wa Vitalo, klabu waliyotoka wachezaji hao hawakuwa mjni na hivyo kuchelewa kwao kungeigharimu Simba. 
"Kila walipokuwa wakipigiwa simu kwa takribani siku tatu mfululizo walikuwa wakisema kwamba wako milimani. Sasa hawa watu wa Burundi wakikwambia wako miliman wanamaanisha wameenda kijijini kwao. Kuongea kwa simu pekee kusingetosha na ndiyo Kamati ya Utendaji ya Simba iliomba niende mwenyewe Burundi ili suala hili liishe," alisema. 
Hii ni mara ya pili kwa Rage, ambaye ana uzoefu wa kuongoza soka kwa zaidi ya miongo mitatu, kuingilia kati suala la uhamisho wa wachezaji wa kimataifa. Miaka miwili iliyopita, Mwenyekiti huyo alilazimika pia kusafiri kwenda nchi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati kushughulikia uhamisho wa mchezaji Gervais Kago ambao nao ulikuwa na matatizo. 
Kutokana na kupatikana kwa ITC hizo, Kaze na Tambwe sasa wataruhusiwa kucheza katika mechi ya Ligi Kuu dhidi ya JKT OIljoro ya Arusha iliyopangwa kufanyika Jumatano ijayo mjini Arusha. Klabu ya Simba tayari imewakatia wachezaji hao vibali vya kufanya kazi hapa nchini. 
Wachezaji wengine wa kigeni wa Simba, Joeph Owino na Abel Dhaira, walicheza katika mechi ya jana kutokana na kukamilisha taratibu zote za uhamisho na kuwa na vibali vya kufanya kazi hapa nchini.
 
Imetolea na
 
Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
SimbaSC

CHAMIJATA chatembeza bakuli kusaka Mil 40

Mwenyekiti wa CHAMIJATA, Mohammed Kazingumbe
CHAMA Cha Michezo ya Jadi Tanzania (CHAMIJATA) kimewaomba wadau wa michezo kujitokeza kukisaidia chama hicho shilingi milioni 40 ili kufanikisha mashindano ya Taifa ambayo yanatarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Septemba 20 hadi 24 mwaka huu.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa CHAMIJATA Mohamed Kazingumbe wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii jijini Dar es Salaam.
Alisema mashindano hayo ambayo yatashirikisha mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani ni moja ya utaratibu wa chama hicho kufanya michezo ya jadi kila mwaka kwa lengo la kukuza tamaduni za nchi.
Kazingumbe alisema katika mashindano hayo wanatarajia kuwa kutakuwa na michezo mbalimbali kama bao, kurusha mshale, mdako, mirela, kukuna nazi na mingine mingi ambayo itakuwa ikitambulisha michezo ya jadi nchini.
“Tunatarajia kufanya mashindo ya michezo ya jadi ya Taifa kuanzia Septemba 20 hadi 24 ila mpaka sasa changamoto kubwa ambayo inatukabili ni fedha hivyo tunaomba wadau wenye kupenda michezo hii wajitokeze kusaidia,” alisema.
Alisema hadi sasa ni mikoa michache imethibitisha kushiriki ambayo ni Pwani, Simiyu, Lindi, Morogoro, Dar es Salaam pamoja na baadhi ya taasisi za Serikali ila bado mikoa mingine inaendelea kuonyesha nia ya kushiriki.
Mwenyekiti huyo alisema mikoa ambayo bado haijathibitisha kushiriki inatakiwa kufanya hivyo hadi ifikapo Agosti 30 mwaka huu ambapo maandalizi mengine yatakuwa yanendelea.
Kazingumbe alisisitiza kwa vyama vya mikoa na wilaya kuhakikisha kuwa vinafanya mandalizi ya kutosha ili kuhakikisha kuwa ushindani unakuwa mkubwa na kuleta tija.
Aidha alivitaja vyama vya michezo ya jadi na mikoa kuhakikisha kuwa wanashirikiana ili kufanikisha mashindano hayo.

Yanga, Ashanti wavuna Milioni 102

Na Boniface Wambura
MECHI ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Yanga na Ashanti United iliyochezwa jana (Agosti 24 mwaka huu) katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 102,856,000.

Watazamaji 17,744 walikata tiketi kushuhudia mecchi hiyo namba moja ya VPL msimu wa 2013/2014 iliyomalizika kwa mabingwa watetezi Yanga kuibuka na ushindi mnono wa mabao 5-1.

Viingilio katika mechi hiyo vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 24,400,102.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 15,689,898.31.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 12,406,831.75, tiketi sh. 4,453,890, gharama za mechi sh. 7,444,099.05, Kamati ya Ligi sh. 7,444,099.05, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 3,722,049.53 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 2,894,927.41.

Msondo Ngoma yatumbuiza kwa mara ya kwanza bila Gurumo

Baadhi ya wanamuziki wa Msondo Ngoma wakitumbuiza kwa mara ya kwanza baada ya mwanamziki mkongwe wa bendi hiyo Muhidini Gurumo kustaafu. Kutoka kushoto ni Shabani Lendi, Hamisi Mnyupe, Saidi Mabera, Juma Katundu na Shabani Dede.
Wanamuziki wa Msondo Ngoma kushoto ni Shabani Lendi,Hamisi Mnyupe,Saidi Mabera,Juma Katundu na Mustafa Pishuu wakitumbuiza bila gwiji, Muhidin Gurumo aliyetangaza kustaafu muziki.
Wanamuziki wa Msondo, Abdul Ridhiwani, Eddo Sanga, Athuman Kambi na Juma Katundu wakionyesha manjonjo yao katika onyesho lao la jana.
Wanamuziki Abdul Ridhiwani, Eddo Sanga, Athuman Kambi, Juma Katundu na Mustafa Pishuu wakitumbuiza.
Wasanii Hamisi Mnyupe kushoto na Romani Mng'ande wakiwajibika jukwaani