STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, May 21, 2012

Nchunga 'angolewa' Yanga kwa mabavu

MWENYEKITI wa klabu ya Yanga, Llyod Nchunga 'ameondolewa' madarakani na kundi la wanachama zaidi ya 700 waliokutana jana kwenye mkutano wao wa dharura. Wanachama hao waliokutana kwenye makao makuu ya klabu hiyo mitaa ya Twiga na Jangwani, walikubaliana kumuondoa madarakani Nchunga, kwa madai ya kushindwa kuiongoza Yanga na pia kukiuka katiba kwa kutoitisha Mkutano Mkuu tangu alipochaguliwa mnamo mwaka juzi. Hata hivyo, maamuzi hayo ili yaweze kupata baraka kisheria yatapelewa katika ofisi za Msajili wa Klabu na Vyama vya Michezo wa Manispaa ya Ilala ambapo Yanga ndipo imesajiliwa. Akitangaza maamuzi ya wanachama hao baada ya kuwauliza na wao kuitikia kwa sauti ya juu kwamba ha
Picha za matukio za mkutano wa wanachama wa Yanga waliokutana jana klabuni kwao na kumuengua madarakani Nchunga. wamtaki Nchunga, Katibu wa Baraza la Wazee, Ibrahim Akilimali, alisema kuwa wamefikia maamuzi hayo kutokana na uongozi waliouchagua kushindwa kuiongoza Yanga na kuruhusu 'ufisadi' kufanyika ndani ya klabu yao. Akilimali alisema kuwa wamekosa imani na Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo na baada ya kuona wameshindwa uongozi waliowapa na waliwataka waondoke ili kuepusha aibu ambayo hivi sasa inawakabili hasa kufuatia kupoteza ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara na kufungwa magoli 5-0 na watani wao Simba. "Tulimshauri atupe timu ili tuweze kuiandaa vyema kumvaa mtani, alikubali, lakini baadaye akatuita sisi ni wahuni na majina mengi yasiyofaa, sasa kwa hili tunasema kuanzia sasa Nchunga na wenzake si viongozi tena wa Yanga," alisema Akilimali na kushangiliwa na wanachama ambao walikutana kwenye uwanja wao wa Kaunda huku kukiwa na amani. Alisema kuwa makundi yaliyoko ndani ya klabu hiyo ndiyo yamewafikisha walipo na wamekubaliana waungane na kumaliza tofauti zao ili Yanga iwe moja. Mkutano huo kwa kauli moja pia ulipitisha jina la Rais wao zamani, Abbas Tarimba, kuwa mshauri wa Kamati ya Usajili ambayo itaanza kazi leo na kuhakikisha wanasajili wachezaji wenye uwezo na hatimaye kutetea ubingwa wao wa Kombe la Kagame. Wanachama hao waliazimia kutowaruhusu viongozi waliobaki kwenye Kamati ya Utendaji kuingia kwenye jengo hilo kwa sababu hawana imani nao tena. Pia Akilimali alisema kuwa hivi sasa Yanga inapaswa kuitisha mkutano wa uchaguzi kufuatia wajumbe wa Kamati ya Utendaji kujiuzulu na kubakia watano. Yusuph Mzimba, alisimama kwenye mkutano huo na kuwataka wanachama wa Yanga wabadilike na kutorudia makosa waliyoyafanya kwenye uchaguzi uliopita kwa kumchagua kiongozi huyo. Mzimba alisema kwamba wasikubali tena kutumika na kuchaguliwa viongozi wasiojua maana ya utawala. "Yanga ibadilike, sio kama ilivyokuwa huko nyuma," alisema Mzimba na kupigiwa makofi. Alisema Nchunga ameshindwa kusoma alama za nyakati kwa kufahamu kwamba sasa wanachama hawamtaki na hivyo alitakiwa mapema kujiuzulu hatimaye kulinda heshima yake. Wanachama kuanzia 500 wanaweza kuomba mkutano mkuu na kutoa maamuzi lakini ikiwa chini ya mkutano ulioitishwa na uongozi. Hata hivyo, Nchunga alikaririwa jana akisema kwamba mkutano huo ni batili kwa sababu haukuwa mkutano wa wanachama kama wazee walivyoubadili 'kihuni', bali ulipaswa kuwa ni baina ya uongozi na wazee wa klabu. Hadi kufikia jana Kamati ya Utendaji ya Yanga imebakia na viongozi wanne huku nane wakiwa wameshajiuzulu hivyo waliobaki hawawezi kukutana na kutoa maamuzi yoyote. Wajumbe ambao kuanzia juzi waliwasilisha barua za kujiuzulu ni pamoja na Paschal Kihanga, Mzee Yusuph na Mohammed Bhinda, ambaye alipokelewa kwa shangwe kwenye mkutano huo wa wanachama na kuahidi leo ataweka wazi sababu zilizoepelekea yeye kufikia maamuzi hayo. Mzee Yusuph katika barua yake amesema kuwa amefikia maamuzi hayo baada ya kuona wameshindwa kusimamia na kuiendesha klabu hiyo katika misingi ya weledi, uwazi na uwajibikaji. Wajumbe wengine waliojiuzulu ni Ally Mayai, Sarah Ramadhani, Seif Ahmed 'Magari', Abdallah Binkleb na Davis Mosha, wakati Theonest Rutashoborwa alifariki na kuipunguzia nguvu kambi ya uongozi.

Sh50m awaits Epiq Bongo Star Search 2012

The winner of this year Epiq Bongo Star Search (EBSS) 2012 will pocket Shs 50 million, Zantel Vice President-Commercial, Ahmed Mokhles announced on Friday. Speaking during the launching ceremony held at the Serena Hotel, Mokhles said that they have decided to increase the winner prizes from Shs 40 million of last year aiming to make the search competitive and reward the winners. Mokhles said that they are proud to be associated with a successful Tanzanian talent competition focusing on discovering and promoting new musical talent among the youth. He said that through Epiq Nation related products aimed at the youth, they believe this year’s contest will be very energetic, full of color and pomp and many surprises. He explained that Zantel has incorporated a fashion aspect to this year’s competition whereas local and young designers will be given an opportunity to dress the contestants and will be assessed by professional fashion designers. “We all now BSS has changed lives of many young people and would like to see this continue under our firm stewardship and are creating additional segments to the show such as fashion to give opportunities to more youths and benefit from this one o a kind partnership,” added Mokhles. Benchmark Production Managing Director, Rita Paulsen elaborate her happiness during the launch “This is very unique day in Tanzania Music industry as we officially launch epiq bongo star search 2012 with avibrant new sponsor who has come up with a fresh look towards bongo star search.” Epiq Bongo Star search will continue with its usual format of having auditions from all major towns around the country an thisi year it will be extended to eight regional that are Zanzibar, Lindi, Mbeya, Mwanza, Arusha, Tanga, Dodoma and Dar es Salaam.

Saturday, May 19, 2012

Doyi Moke awataka Yanga watulie

KIPA nyota wa zamani wa klabu za Majimaji-Songea, Simba na Yanga, Doyi Moke, amewasihi wanachama wa timu ya Yanga kumaliza matatizo yao kwa kukaa mezani na kuzungumza. Aidha, kipa huyo raia wa JK Congo na aliyewahi kuzidakia pia timu za Rayon Sport ya Rwanda na Vital'O ya Burundi, alisema wanayanga wanapaswa kukumbuka kuwa mbele yao kuna kibarua cha kutetea taji la Kombe la Kagame la klabu bingwa za Afrika Mashariki na Kati hivyo watulizane mapema. Akizungumza kwenye mahojiano maalum, mkali huyo ambaye kwa sasa ni mfanya biashara madini alisema Yanga watajuta mbeleni wasipokaa mezani. "Nadhani hali inayoendelea Yanga haileti ishara njema, pande zinazotofautiana zikae chini na kuzungumza, kuendelea kulumbana bila kupata muafaka ni kuiweka pabaya timu yao wakati wanakabiliwa na michuano ya Kombe la Kagame linaloanza Juni," alisema. Alisema hadhani kama kuendelea kujadili kipigo cha mabao 5-0 walichopewa na watani zao Simba au kupokonywa taji la ligi kuu itaisaidia klabu hiyo wakati matokeo hayo hayawezi kubadilika. Baadhi ya wanachama wa Yanga wamekuwa wakishinikiza mwenyekiti Lloyd Nchunga ajiuzulu mara moja, na katika kuhakikisha hilo wameitisha mkutano mkuu kesho klabuni huku mwenyekiti akiwa ametaja Julai 15 kuwa siku ya mkutano mkuu rasmi wa mwaka.
Doye Moke enzi akicheza soka nchini Tanzania

Mashujaa, Mashauzi kung'arisha Miss Tabata

BENDI zinazotamba nchini kwa sasa Mashujaa na Mashauzi Classic zitatumbuiza kwenye kinyang'anyiro cha kumtafuta mrembo wa Tabata kitakachofanyika Juni Mosi katika ukumbi wa Da West Park, Tabata. Mratibu wa shindano hilo, Godfrey Kalinga alisema wameamua kuweka burudani yenye ladha tofauti ili kukidhi kiu ya watu mbalimbali watakaohudhuria shindano hilo. Kalinga alisema siku hiyo pia itatumika kusherehekea miaka 10 tangu kuasisiwa kwa shindano la Miss Tabata. "Shindano la mwaka huu litakuwa ni la aina yake kwa sababu utakuwa ni mwaka wetu wa 10 tangua kuanza kuandaa Miss Tabata... ndio maana tunaleta burudani nyingi," alisema mratibu huyo wa Bob Entertainment na Keen Arts. Alisema warembo waliyowahi kushinda mataji mbalimbali ya shindano hilo, pia wamealikwa kusherehekea miaka 10 ya Miss Tabata. Shindano hili limedhaminiwa na Dodoma Wine, Redds, Integrated Communications, Fredito Entertainment, Multichoice Tanzania, Screen Masters, Kitwe General Traders, Step In Electronics, Brake Point, Atriums Hotel na Lady Pepeta. Warembo 10 wa kwanza watafuzu kushiriki Miss Ilala na baadaye Miss Tanzania. Mrembo anayeshikilia taji la Tabata kwa sasa ni Faiza Ally. Warembo wa Tabata wamekuwa wakifanya vizuri katika mashindano ya Miss Tanzania ambapo 2010 Consolata Lukosi alishinda nafasi ya tatu kabla ya kutangazwa kuwa balozi wa kinywaji cha Redds.
Visura watakaochuana kinyang'anyiro cha Miss Tabata 2012

'Ticotico' wa Simba aanzisha klabu binafsi ya soka, kuteta leo

ALIYEWAHI kuwa Katibu wa Kamati ya Fedha ya klabu ya Simba, Onesmo Waziri 'Ticotico' ameanzisha klabu ya soka iitwayo 'Golden Bush Fc', ambayo imeshasajiliwa rasmi tayari kwa ajili ya ushiriki wa michuano mbalimbali. Akizungumza na MICHARAZO, Ticotico, mmoja wa 'membaz' wa zamani wa Friends of Simba, alisema klabu yake imesajiliwa ndani ya wilaya ya Kinondoni na itakuwa na makao makuu yake eneo la Mabibo, Dar es Salaam. Alisema mpaka sasa timu hiyo imeanza kukusanya wachezaji chini ya kocha wa muda, nyota wa zamani wa timu ya Yanga, Waziri Mahadh 'Mandieta'. Ticotico, alisema katika kuhakikisha klabu yake inajiendesha kisasa ikiwa na ufadhili wa kutosha wameitisha mkutano na wadau wa soka wilayani Kinondoni, ili kujadili na kutoa mawazo yao. Mkutano huo unatarajiwa kufanyika leo Jumamosi mchana, kwenye majengo ya ofisi ya TANLAP, Kinondoni Biafra. Ticotico aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa klabu ya Red Coast iliyotamba Ligi ya TFF-Kanda, alisema lengo la kuanzisha klabu hiyo ni kuendeleza soka nchini sambamba na kuwasaidia vijana wenye vipaji vya mchezo huo. "Katika kuendeleza soka nchini nimeamua kuanzisha klabu itakayoitwa Golden Bush, ambayo imeshasajiliwa na Jumamosi tunatarajia kufanya mkutano au tuseme kongamano la wadau wa soka kupata mawazo namna ya kuifanya iwe klabu ya kipekee Kinondoni," alisema. Mwisho

KWAHERI JEMBE MAFISANGO TUTAKUKUMBUKA DAIMA

MAISHA UPITA, LAKINI MEMA NA MAZURI YA MTU HAYASAHAULIKI. TUTAKUKUMBUKA DAIMA PATRICK MUTESA MAFISANGO KWA UHAMIRI WAKO DIMBANI. KAPUMZIKE KWA AMANI BABA!

Jezi ya Mafisango yataifishwa SIMBA, Wengi wamlilia!

KLABU ya soka ya Simba imeamua 'kuitaifisha' jezi namba 30, aliyokuwa akiitumia kiungo wao wa kimataifa kutoka Rwanda, mwenye asili ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Patrick Mutesa Mafisango kama njia ya kumuenzi. Uongozi wa Simba umesema kuanzia sasa hautaitumia tena jezi hiyo kama heshima ya mchezaji huyo aliyefariki usiku wa kuamkia juzi, jijini Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Simba, Mwenyekiti wa Simba SC, Alhaj Ismail Aden Rage aliyasema hayo jana wakati akiwahutubia waombolezaji waliofika kuuaga mwili wa marehemu Mafisango kwenye viwanja vya TCC-Chang’ombe, Dar es Salaam, kabla ya kupelekwa uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwl JK Nyerere, ili kusafirishwa leo kwenda kwao Kongo kwa ajili ya mazishi yanayofanyika kesho Jumapili. Heshima, aliyopewa Mafisango inafanana ya ile ya kiungo wa zamani wa kimataifa wa Cameroon, Marc Vivien Foe na klabu yake, Manchester City ya England alipofariki Juni, 2003, ambapo jezi yake namba 23 ilitunzwa moja kwa moja. Kiungo huyo aliyekuwa ameitwa saa chache kujiunga na timu yake ya taifa ya Rwanda 'Amavubi' kwa kipindi alichoichezea Simba alijijengea jina kwa umahiri aliokuwa nao dimbani, kiasi cha kusamehewa hata alipofanya utovu wa nidhamu hivi karibuni kambi ya timu hiyo. Rage alisema msiba huu ni mkubwa kwa Simba kwa kuwa mchezaji huyo alikuwa ni muhimili mkubwa kwa timu hiyo akiwashauri wachezaji na kuwa nao karibu ndani na nje ya uwanja. “Mafisango alikuwa na mchango mkubwa kwa Simba na mara ya mwisho klabu kukumbumbwa na msiba mzito namna hii ilikuwa ni mwaka 1978 ambapo Simba ilimpoteza mchezaji wake mahiri Hussein Tidwa na ukweli ni kwamba wachezaji hawa tutawaenzi miaka yote na ndio sababu ya kutotumia tena jezi namba 30 kwa kuvaliwa na mchezaji yoyote,” alisema Rage. Rage alisema licha ya umahiri wa Mafisango Dimbani pia alikuwa mchezaji ambaye alitoa mchango mkubwa na hasa wachezaji wawapo nje ya nchi kutokana na umahiri wake wa kujua lugha mbalimbali ambapo alikuwa akiwasaidia wachezaji wenzake. “Ni pengo kubwa kwa kuwa mchezaji huyo alikuwa akijua lugha nyingi ikiwemo Kiswahili, Kingereza na Kifaransa na kuwasaidia wachezaji walipokuwa nje ya nchi tutamkubuka sana Mafisango,” aliongeza. Kutokana na machungu ya msiba huo Rage alishindwa kumaliza kusoma risala fupi ya marehemu mara baada ya kuishiwa nguvu na kumwaga machozi na kupelekea Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo Godfrey Nyange ‘Kaburu’ kumsaidia kusoma risala hiyo. “Mfisango ni mchezaji ambaye alikuwa akijituma nje na ndani ya uwanja na kabla ya kutua Simba Marehemu aliwahi kucheza soka katika timu mbalimbali ikiwemo Tp Mazembe ya DRC, APR ya Rwanda , Azam na Simba za Tanzania na pia alikuwa Nahodha wa timu ya Taifa ya Rwanda ‘Amavubi’ alisema Kaburu. Wakati wa kutoa heshima za mwisho katika uwanja wa Sigara maelfu ya watu walijitokeza uwanjani hapo wakiongozwa na mchungaji Tito Kihame ambaye aliongoza ibada ya kuuga mwili wa marehemu, Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Fenella Mukangara na viongozi mbalimbali wa serikali na viongozi kutoka klabu mbalimbali za hapa nchini. Mukangara aliwataka wachezaji wa Tanzania kujituma na kuwa na moyo kama ambao alikuwa nao Marehemu Mafisango kwa kujituma na kuwa na jitihada za zaidi nje na ndani ya uwanja kama ambavyo marehemu alivyokuwa akifanya. “Kifo chake ni pigo kubwa kwa Simba na Watanzania kwa ujumla na tunamshukuru kwa kuvuka mipaka na kuona umuhimu wa kuja na kucheza Tanzania na pia wachezaji wa Simba wasikate tamaa cha muhimu waendeleze kile ambacho alikiacha marehemu,” alisema Mukangara. “Ukweli ni kwamba katika familia ya soka hapa nchini tumepoteza mtu muhimu sana na tunamuombea kwa Mwenyezi Mungu ampumzishe kwa amani,” alisema Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania TFF Angetile Osiah. “Sisi Simba ni watani zetu na tunakuwa pamoja katika shida na hivyo basi mimi kama kiongozi wa Yanga nimeiwakilisha klabu nzima na tutaendelea kuwa bega kwa bega na watani zetu katika kipindi hiki kigumu ila mchezaji Mafisango alikuwa ni mchezaji hodari uwanjani hivyo basi anastaili kuigwa na wachezaji wengine,” alisema Selestine Mwesigwa katibu Mkuu wa Yanga. Nao wachezaji mbalimbali kutoka timu ya Taifa Taifa Stars walijitokeza na kubeba jeneza la mchezaji mwenzao na kuliingiza katika viwanja vya Sigara wachezaji hao Juma Kaseja, Jonh Bocco, Mwinyi Kazimoto, Shabani Nditi, Amiry Maftah, Nurdin Bakari, Agrey Moris na Juma Nyoso. Profesa Philemon Sarungi akimsaidia Rage Mara baada ya nyota hao kuufikisha mwili wa marehemu katika sehemu husika ambayo ilipangwa Kazimoto na Kaseja iliwalazimu watu wa ziada kujitokeza na kuwapa sapoti mara baada ya kushindwa kutembea na kuwapeleka katika eneo husika ambalo walikuwa wamepangiwa kukaa. Naye Msemaji wa klabu hiyo, Ezekiel Kamwaga alisema msafara wa leo kwenda Kongo kuusafirisha mwili wa Mafisango, Haruna Moshi 'Boban' atawakilisha wachezaji wa klabu hiyo huku kwa uongozi atakuwa Mjumbe wao wa kamati ya utendaji Joseph 'Mzee Kinesi' Itang’are. Kamwaga alisema mwili huo ungeondoka asubuhi ya leo ukiambatana na mtoto wa marehemu Crespo Tabu Mutesa, mwenye umri wa miaka mitano na mchezaji wa Yanga Haruna Niyonzima ambaye pia ni mchezaji wa timu ya Taifa ya Rwanda.

Thursday, May 17, 2012

MASKINI PATRICK MUTESA MAFISANGO!

KIFO kina usiri mkubwa na hakuna ajuae ila Mwenyezi Mungu! Ndio kauli inayoweza kuanza nayo kutokana na ukweli ni saa chache tu, tangu kiungo mahiri wa Simba, Patrick Mafisango kuitwa kwa mara ya kwanza baada ya kitambo kirefu kuwa nje ya kikosi cha timu ya taifa ya Rwanda 'Amavubi'. Mafisango aliyefariki alfajiri ya leo kwa ajali ya gari, alikuwa miongoni mwa wachezaji 32 walioitwa na kocha wa timu ya taifa ya Rwanda, Milutin 'Micho' Sredojovic kwa ajili ya kujiandaa na michuano ya kuwania Fainali za Afrika za 2013 na Kombe la Dunia za 2014. Kitambo kirefu marehemu Mafisango alikuwa hajajumuishwa katika timu hiyo kutokana na tatizo la utovu wa nidhamu, lakini kwa kiwango alichokionyesha kwa siku za karibuni akiwa na klabu ya Simba, Micho alishawishika kumuita katika timu hiyo. Hata hivyo, wakati akiwa anajiandaa kwenda Rwanda kujiunga na kambi ya timu hiyo kwa ajili ya michezo yao miwili ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya timu za Libya na Tunisia ambazo zimepangwa kucheza Mei 25 na 26. Wengine walioitwa katika kikosi hicho ni nahodha wa zamani, Hamad Ndikumana, aliyekuwa ametemwa muda mrefu, Hamdan Bariyanga, Olivier Kwizera na Francois Hakizimana na Haruna Niyonzima anayeichezea Yanga. Kwa hakika ni pigo kwa Amavubi, Simba na familia nzima ya mchezaji huyo ambaye alikuwa miongoni mwa wafungaji walioisaidia Simba kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara na kufika hatua ya 16 Bora ya Kombe la Shirikisho. Marehemu Patrick Mutesa Mafisango alizaliwa Machi 09, 1980
Innalillah Wainailahi Rajiun!

Azam itafanya maajabu Afrika-Nahodha

NAHODHA wa klabu ya soka ya Azam, Aggrey Morris, amesema ana imani timu yao itafanya maajabu katika ushiriki wao wa michuano ya kimataifa. Morris, alisema japo Azam wataiwakilisha nchi kwa mara ya kwanza, bado anaamini kwa namna uongozi wao ulivyojizatiti na kujipanga tangu ilipopanda daraja, timu yao itafika kule iliposhindwa wawakilishi wengine Beki huyo wa kati anayezichezea pia timu za taifa za Zanzibar na Taifa Stars, alisema aina ya wachezaji waliopo Azam na benchi la ufundi chini ya kocha Stewart John Hall, linampa jeuri ya kuamini timu yake itatisha Afrika. "Awali ya yote tunashukuru kwa kuweza kupata nafasi hiyo ya kuiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya kimataifa mwakani, lakini pia nataka kuwatia moyo wadau wa soka kwamba Azam haitawaangusha Afrika," alisema. Alisema, japo wachezaji karibu wote wa Azam kwa sasa wapo mapumzikoni, lakini akili zao zipo katika michuano hiyo ya Afrika. Kwa kushika nafasi ya pili katika Ligi Kuu Tanzania Bara, Azam imepata fursa ya kuiwakilisha Tanznaia katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika, ikiwa ni mara yao ya kwanza tangu timu hiyo ianzishwe mwaka 2004.

Cheka ajipanga kumtoa nishai Mzambia

BINGWA mpya wa IBF Afrika, Francis Cheka 'SMG' ametamba kwamba hatawangusha Watanzania katika pambano lake la kutetea taji hilo dhidi ya Mzambia, Stephen Chungu atayepigana nae Julai mwaka huu. Cheka, alisema kwa kutambua umuhimu wa pambano hilo anatarajia kuingia kambini mapema zaidi ili kujiweka fiti kabla ya kuvaana na Chungu katika pambano la uzani wa Super Middle la raundi 12. Awali Cheka alikuwa apambane na Mohammed Akpong wa Ghana, lakini kutokana na masharti aliyoyatoa bondia huyo, imemfanya waratibu wa IBF kumbadilishia Mzambia huyo mwenye rekodi ya kucheza michezo 16. "SItaki kuwaangusha Watanzania na hivyo nitaanza mapema kambi yangu ili kumkabili nikiwa fiti na kuhakikisha napata ushindi hiyo Julai," alisema. Cheka anayeshikilia pia mataji ya Kamisheni ya Ngumi Dunia, WBC, ICB na UBO, alisema ushindi wake dhidi ya Mada Maugo uliomfanya atwae taji hilo la IBF Afrika imekuwa kama chachu ya kuzidi kusaka mafanikio kimataifa. "Akili yangu kwa sasa ni kusaka mafanikio zaidi duniani, ndio maana sitaki kufanya uzembe wa aina yoyote katika pambano langu lijalo na mengine ya kimataifa ambayo ndiyo yenye ulaji mkubwa," alisema. Cheka alitwaa taji hilo kwa kumshinda Mada Maugo aliyekacha ulingo wakati wakijiandaa kwa raundi ya saba kwa kile alichodai alikuwa akiona 'kiza' na kumfanya bingwa huo wa IBF kushinda pambano la 11 mfululizo tangu 2008. Mwisho

Messi wa Simba achekelewa kuitwa Taifa Stars

MSHAMBULIAJI nyota kinda la klabu ya Simba, Ramadhani Singano 'Messi' amesema hakuamini kirahisi alipolisikia jina lake likitajwa na kocha mkuu wa timu ya taifa, Taifa Stars, Kim Poulsen kujiunga na kikosi cha timu hiyo. Akizungumza na MICHARAZO nyumbani kwao, Keko Machungwa jijini Dar es Salaam, Messi, alisema mara alipojithibitisha kwamba ni kweli ni miongoni mwa wachezaji wa timu hiyo aliporomoka hadi chini kumsujudia Mola wake. Mchezaji huyo aliyetamba na timu za Ubatan na Bombom kabla ya kuonwa na Simba, alisema kifupi ni kwamba amefurahia uteuzi huo akiamini kocha Poulsen amekiona kipaji chake na wajibu wake kutomuangusha. "Kwa kweli sikuamini kama ni mimi niliyetajwa katika kikosi hicho, ila ndugu zangu waliponithibitishia cha kwanza nilichofanya ni kusujudu kumshukuru Mungu kwani nimefurahi kupata fursa hii na sitamuangusha kocha," alisema. Alisema mbali na kujitahidi kwa uwezo wake wote kuonyesha fadhila kwa kocha Kim, pia asingependa kuwaangusha Watanzania ambao wamekuwa na matumaini makubwa na timu yao licha ya kushindwa kuwapa raha. "Ninachoomba nipate nafasi ya kuonyesha uwezo wangu kwa kushirikiana na wachezaji wenzangu ili kuweza kuisaidia timu ifanye vema na kusuuza roho za watanzania wenye wazimu wa soka," alisema Messi. Messi, aliyepandishwa kikosi cha kwanza cha Simba kitokea timu B ya klabu hiyo hiyo ni mara yake ya kwanza kuitwa Stars, ingawa tangu mwaka 2009 amekuwa akizichezea timu za taifa za vijana U17 na U20. Mchezaji huyo ni kati ya wachezaji 25 walioteuliwa na kocha Poulsen kwa ajili ya kujiandaa na mechi za kuwania kufuzu fainali za Kombe la Dunia na zile za Afrika zitakazofanyika kati ya mwaka kesho na 2014.
KIPA nyota wa zamani wa timu za Simba na Yanga, Doyo Moke, amesema umefika wakati wa wadau wa soka nchini kuwapa nafasi wachezaji wa zamani kuziongoza klabu za soka badala ya kuwaachia 'wavamizi' wanaziyumbisha. Moke, aliyewahi kung'ara pia na timu za Majimaji-Songea, Rayon Sports ya Rwanda na Vital'O ya Burundi, alisema watu wasio na uchungu waliovamia mchezo huo ndio wanaolifanya soka la Tanzania kushindwa kusonga mbele. Alisema, dhana kwamba lazima kiongozi wa soka awe na elimu ya Chuo Kikuu, imechangia kudumaza soka la Bongo kwa vile wengi wa wasomi hao wamekuwa akizitumia klabu wa masilahi yao ikiwemo kupata umaarufu. "Lazima watanzania wabadilike kwa kutoa nafasi kwa wachezaji wa zamani kuweza kuongoza soka la Tanzania, mataifa mengine yamefanya hivyo na kufanikiwa, kwa kuwa wachezaji huwa na uchungu wa kweli na soka," alisema. "Wengi wanaojitokeza sasa kuongoza klabu ni wavamizi wasiokuwa na uchungu na mchezo huo zaidi ya kujitafutia umaarufu ili waende kugombea nafasi za uongozi wa kisiasa na kujinufaisha kimasilahi wenyewe," aliongeza. Alisema, ingawa elimu ni kitu cha muhimu katika uongozi, lakini basi nafasi hizo wapewe wachezaji wenye elimu za kutosha kuweza kuongoza gurudumu la soka kama ilivyotokea kwa akina Leodger Tenga, Mtemi Ramadhani na wengineo ambao wameonyesha uwezo mkubwa na ufanisi wa hali ya juu. Kuhusu kinachoendelea kwenye klabu yake ya zamani ya Yanga, Moke mwenye asili ya Jamhuri wa KIdemokrasia ya Kongo, alisema ni lazima pande zinazolumbana zikae chini na kumaliza tofauti zao ili kuinusuru klabu yao. "Kulumbana hakuwezi kukusaidia wakati wana kibarua kigumu katika utetezi wao wa Kombe la Kagame, wakizembea hata taji hilo litapotea hivihivi," alisema. Tangu wafungwe mabao 5-0 na watani zao Simba na kulipoteza taji la Ligi Kuu Tanzania Bara, hali ndani ya klabu ya Yanga imekuwa si shwari ambapo wanachama na wazee wakilumbana na uongozi wao chini ya Mwenyekiti Llyod Nchunga. Mwisho

Patrick Mutesa Mafisango afariki kwa ajali ya gari

KIUNGO mahiri wa klabu ya soka ya Simba, Patrick Mutesa Mafisango "petit' amefariki dunia alfajiri ya leo baada ya kupata ajali ya gari jijini Dar es Salaam. Kwa mujibu wa taarifa ambazo MICHARAZO imezipata na kuthibitishwa na Mwenyekiti wa klabu hiyo ya Simba, Ismail Aden Rage, Mafisango aliyekuwa mmoja wa wachezaji tegemeo wa klabu hiyo katika ushiriki wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya Kombe la Shirikisho alifariki majira ya saa 10 akitokea klabu kujirusha. Imeelezwa kwamba, mchezaji huyo kutokla Rwanda, ingawa asili yake ni Jamhuri ya KIdeomkrasia ya Watu wa Kongo, alifariki wakati akitoka kujirusha klabu usiku na alipatwa na ajali hiyo maeneo ya TAZARA wakati akijaribu kumkwepa mwendesha Bodaboda na kujikuta wakiporomokea mtaroni na gari lake ambalo lilikuwa na watu wengine wawili. Watu hao wametajwa kuwa ni rafiki ya kiungo huyo mshambuliaji na mdogo wake ambao hata hivyo majina yake hayakuweza kupatikana mara moja. Mwenyekiti wa Simba, Ismail Rage, alisema yeye alipata taarifa na wakati akizungumza na blog hii alikuwa akiendelea kufanya mchakato wa msiba wa mchezaji wake huyo ambaye walimchukua kutoka Azam Fc. Kabla ya kutua Azam na kuonyesha uwezo mkubwa, Mafisango aliyezaliwa Machi 09, 1980 alikuwa akikipiga katika klabu ya ya nchini kwake APR ya Rwanda. Mafisango anakumbukwa kwa mchango wake mkubwa katika klabu hiyo akiifungia jumla ya mabao 11 katika Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, ambapo Simba imetwaa taji ikiwapoka watani zao Yanga. Pia alikuwa mmoja wa wafungaji walioisaidia Simba kufika hatua ya 16 Bora ya Kombe la Shirikisho kabla ya kutolewa na Al Ahly Shandy ya Sudan,ambapo alikosa mkwaju wake wa penati uliosababisha Simba kung'olewa kwa jumla ya mabao 12-11. Mungu aipumzishe kwa amani roho ya marehemu Patrick Mutesa mafisango Amin!

Super Nywamwela sasa aibuka na Ndungwe

DANSA kiongozi wa bendi ya Extra Bongo, Hassani Mussa 'Super Nyamwela' amefyatua kibao kipya kiitwacho 'Ndungwe'akiwa katika maandalizi ya kukamilisha albamu yake ya tatu. Akizungumza na MICHARAZO, Nyamwela alisema kibao hicho kilichopo katika miondoko ya Bongofleva, amekifyatulia katika studio za AM Records chini ya prodyuza 'Maneke. Nyamwela alisema huo ni wimbo wa pili kuurekodi kwa mwaka huu baada ya awali kupakua Tumechete, alichowashirikisha 'bosi' wake, Ally Choki, Banza Stone na Athanas Montanabe. "Nimeachia wimbo mpya wa Ndungwe, nilioimba pekee yangu katika kuwaonmyesha mashabiki wangu kwamba naweza miondoko yote, kwani wimbi huu nimeutoa katika miondoko ya Bongofleva," alisema. Nyamwela alisema, kwa sasa anafanya mipango ya kurekodi video ya wimbo huo, ili mashabiki wake wapate burudani, huku akiendelea kumalizia nyimbo nyingine za kukamilisha albamu yake ya tatu binafsi. Albamu mbili za awali za bingwa huyo wa zamani wa Bolingo mkoa wa Dar es Salaam ni 'Master of the Tample' na 'Afrika Kilomondo'.
Super Nyamwela akionjesha manjonjo yake katika mazoezi ya bendi yake ya Extra Bongo

Friday, April 20, 2012

Shija Mkina achekelea kuitungua Yanga


MFUNGAJI wa bao pekee lililoizamisha na kuitemesha Yanga ubingwa wa Ligi Kuu
Tanzania Bara, Shija Mkina wa Kagera Sugar, amedai kufarijika mno kuitungua timu hiyo.
Mshambuliaji huyo za zamani wa Bandari Mtwara na Simba, alisema ingawa ni kawaida
yake kufumania nyavu, lakini kuifunga Yanga ni faraja kubwa kwake kwa vile imeisaidia timu yake kujihakikishia nafasi ya kusalia kwenye ligi kuu msimu ujao.
Mkina, aliyejiondoa Simba kwa lazima baada ya kushindwa kupewa nafasi na aliyekuwa
kocha wa timu hiyo, Mganda Moses Basena ambaye hayupo kwa sasa katika klabu hiyo,
alisema bao hilo dhidi ya Yanga lilikuwa muhimu kwa timu yake ya Kagera.
"Nashukuru kwa kuweza kufungia timu yao bao muhimu lililotuhakikishia pointi tatu
zinazotufanya tusiwe na hofu ya kushuka daraja," alisema.
Mchezaji huyo, aliyewahi kuwa mfungaji bora alipokuwa na Bandari Mtwara, alisema ligi ya msimu huu ilikuwa ngumu kuliko misimu ya nyuma na ndio maana hadi sasa ni vigumu kujua timu inayoshuka daraja au itakayonyakua ubingwa licha ya Simba kupewa nafasi.
"Naamini ligi zote zingekuwa hivi, basi soka letu lingekuwa lipo juu na klabu zetu kufanya vema kwenye michuano ya kimataifa," alisema Mkina.
Kwa ushindi iliyopata ya Yanga, imeifanya Kagera Sugar kufikisha jumla 26 na ikisaliwa na mechi tatu dhidi ya Toto Afrika inayotarajiwa kucheza kesho mjini Bukoba, Coastal Union watakaoumana nao Aprili 30 mjini Tanga kisha kufunga msimu kwa kuvaana na Azam.

Mwisho

Polisi Moro yaifuata Mgambo Ligi Kuu, vita yabakia kwa Prisons Mbeya, Polisi Dar

WAKATI timu za soka za Mgambo ya Tanga na Polisi Moro zikiwa zimeshajihakikishia
kucheza Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao, vita vya kuwania nafasi hiyo imesalia kwa
timu za Polisi Dar na Prisons ya Mbeya ambazo zitafunga dimba Jumatatu.
Polisi Moro jana ilijihakikishia nafasi ya kupanda daraja baada ya kuilaza Mbeya City mabao 2-0 na kufikisha pointi 17 na kuongoza msimamo wa fainali za Ligi Daraja la Kwanza zinazochezwa kwenye uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro.
Mgambo ilikuwa timu ya pili kupata nafasi hiyo katikati ya wiki baada ya kuilaza Transit Camp mabao 3-0 na kufikisha pointi 15 zinazowaweka nafasi ya pili ya msimamo wa ligi hiyo.
Nafasi ya tatu ya kupanda daraja imesaliwa kwa timu za Polisi Dar ambayo jana ilipata ushindi wa mabao 3-0 mbele ya JKt Mlale ya Songea na kufikisha pointi 10 ikishika nafasi ya nne nyuma ya Prisons ambayo yenye ina pointi 11.
Hata hivyo Prisons Mbeya ambayo ilitarajiwa kushuka dimbani leo jioni ndiyo yenye
nafasi kubwa ya kuchukua nafasi hiyo kutokana na pointi ilizonazo pia kuwa na kiporo
cha mechi moja ya ziada itakayochezwa Jumatatu dhidi ya Polisi Dar.
Iwapo timu hiyo itateleza kwa Rhino au kutoka sare itamaanisha kwamba mechi yao ya Jumatatu dhidi ya 'Vijana wa Kova' itakuwa ni kama fainali katika kuwania
nafasi hiyo moja ya kucheza ligi kuu msimu ujao.
Uongozi wa Polisi Dar kupitia kocha wake, Ngello Nyanjaba, alisema hawajakata tamaa
kupanda ligi kuu, licha ya kuwa na nafasi finyu nyuma ya Prisons ya Mbeya.
"Tunasubiri kuona inakuwaje hadi dakika za mwisho," alisema Nyanjaba.

Msimamo wa Fainali za 9 Bora kabla ya mechi za leo:

TIMU P W D L F A Pts
1. Mgambo Shooting 7 4 3 - 12 3 15
2. Polisi-Moro 7 5 2 - 14 4 17
3. Prisons-Mbeya 6 3 2 1 8 5 11
4. Polisi Dar 7 2 4 1 9 4 10
5. Mbeya City 7 2 2 3 7 8 8
6. Rhino Rangers 7 2 2 3 4 6 8
7. Mlale JKT 7 1 2 4 5 13 5
8. Polisi-Tabora 6 1 2 3 5 11 5
9. Transit Camp 6 - 1 5 2 12 1

Mwisho

Kocha Julio kuweka historia ya aina yake nchini


KOCHA maarufu nchini, Jamhuri Kihwelu 'Julio' anatarajiwa kuweka rekodi ya aina yake
nchini leo atakapokalia benchi za timu mbili tofauti katika pambano moja kati ya Coastal Union ya Tanga anayoifundisha na CDA-Dodoma anayojiunga nayo.
Mchezo huo maalum wa kirafiki kwa timu hizo utachezwa kwenye uwanja wa Jamhuri
mjini Dodoma, ambapo Coastal watautumia kumuaga na CDA kumkarisha kocha huyo
kwa ajili ya kuinoa kwa michuano ya Ligi ya TFF-Taifa inayotarajiwa kuanza hivi karibuni.
Julio aliyeisaidia Coastal kusalia Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya awali kuchechemea, ameodai ameombwa na uongozi wa CDA, timu aliyowahi kuichezea miaka ya nyuma, jambo alilodai ameliafiki kwa moyo mmoja.
Akizungumza kutoka mjini Dodoma, Julio alisema amekubali kuachana na Coastal Union
ili aifundishe CDA klabu iliyomuibua katika maisha yake ya soka na katika mechi ya leo atakaa kwenye benchi za timu zote kwa dakika 45 za kila kipindi.
Kocha huyo mwenye maneno mengi, alisema dakika 45 za awali atakalia benchi la timu
yake ya sasa ya Coastal Union na katika kipindi cha pili atahamia katika benchi la CDA.
"Najiandaa kuachana na Coastal Union na kutua CDA baada ya kufuatwa na viongozi na
Jumamosi timu hizo mbili zitacheza mechi maalum ya kirafiki Coastal ikiniaga na CDA
kunikaribisha na kitakaa kwenye mabechi ya timu zote mbili kwa kila kipindi," alisema.
Julio alisema japokuwa imekuwa ngumu kwa makocha wenye majina kama yeye kukubali
kuzinoa timu za madaraja ya chini, lakini yeye anataka kuisaidia timu hiyo hadi ipande Ligi Kuu Tanzania Bara kuwahamasisha wengine kujitolea kusaidia timu za chini.
Kitendo cha kocha huyo kukaa katika benchi za timu mbili tofauti katika mchezo huo
itamfanya Julio aweke historia ya aina yake nchini, ingawa marehemu Syllersaid Mziray aliwahi kuzifundisha Simba na Yanga kwa wakati tofauti katika michuano ya Kombe la AICC mwishoni mwa miaka ya 1980, iliyokuwa ikifanyika mjini Arusha.

Mwisho

Thursday, April 19, 2012

Rage awatuliza wana Simba kuhusu Ngassa

WAKATI klabu ya soka ya Azam ikikanusha taarifa kwamba winga wao nyota, Mrisho Ngassa kuwa na mipango ya kutua Simba, Mwenyekiti wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage, amewatoa hofu wanachama wa klabu hiyo kwa kuwaeleza 'SUBIRINI TUONE'. Rage, alisema kama Ngassa atatua Msimbazi au la, litafahamika baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu Tanzania Bara, ila kwa sasa ni mapema mno kulizungumzia hilo. "Kama wao wamekanusha kwamba huyo mchezaji atakuja Simba, basi subirini, ila kwa sasa ni vigumu kuanza kulisemea hilo wakati hatujui mkataba wa Ngassa na klabu yake ukoje," alisema Rage. Mwenyekiti huyo mwenye 'kismati' na klabu hiyo ya Simba, alisema kuanza kumzungumzia Ngassa kabla hawajawasiliana na uongozi wa Azam ni kwenda kinyume na sheria za FIFA, ila amesisitiza watu wasubiri kujua ukweli wa mambo. Juzi chombo kimoja cha habari kiliripoti taarifa kwamba Simba inakaribia kumnyakua Ngassa kwa ajili ya kuichezea timu hiyo kwenye michuano ya kimataifa, hiyo itafanyika iwapo Simba itafuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho-Afrika. Hata hivyo Azam kupitia msemaji wake, Jaffer Idd Maganga, alisema hakuna kitu kama hicho na wanashangaa uzushi huo. "Hakuna kitu kama hicho, Simba haijawahi kutufuata kutueleza jambo hilo, wala Ngassa, pia mchezaji huyu bado ana mkataba na klabu hiyo ni ajabu kusikia kwamba anataka kwenda Simba, kivipi?" alihoji msemaji huyo. Hata hivyo suala la Ngassa kutua Simba lilitajwa tangu mchezaji huyo alipoihama Yanga na kutua Azam, ambapo ilielezwa ilikuwa janja ya kumvuta mchezaji huyo kutua Msimbazi na hasa alipokuwa akitafutiwa nafasi ya kucheza soka la kulipwa.
Mrisho Ngassa (kushoto) akiwajibika uwanjani na timu yake ya Azam. Hapa alikuwa akichuana na aliyekuwa mshambuliaji wa Simba, Mussa Hassani Mgosi ambaye kwa sasa anacheza soka la kulipwa DR Congo.

Villa Squad mambo bado magumu

LICHA ya kufurahia ushindi wa mabao 4-2 iliyopata timu yao dhidi ya Coastal Union ya Tanga, iliyofufua matumaini ya kusalia Ligi Kuu Tanzania msimu ujao, uongozi wa klabu ya Villa Squad umedai mambo bado magumu kwao na kuomba msaada zaidi. Katibu Mkuu wa Villa, Frank Mchaki, alisema bado wanahitaji msaada wa hali na mali ili kuisaidia timu yao katika maandalizi ya mechi zake zilizosalia ili kuweza kujihakikishia nafasi ya kusalia ligi kuu msimu ujao. Mchaki, alisema japo ushindi wao wa mwishoni mwa wiki umewaongezea tumaini jipya la kujinusuru kushuka daraja, lakini ni vigumu kujihakikishia jambo hilo kulingana na ukaribu wa pointi uliopo baina ya timu zilizopo chini katika msimamo wa ligi hiyo. "Tunashukuru kupata ushindi ambao umefufua matumaini yetu ya kusalia ligi kuu, ila bado tuna kazi ngumu na tunahitaji wadau wa soka watusaidie kwani kiuchumi tuna hali mbaya huku tukikabiliwa na mechi ngumu za kumalizia msimu," alisema Mchaki. Mchaki alisema anaamini timu yao ikisaidiwa kwa hali na mali itajiandaa vema kwa mechi tatu zilizosalia ambazo kama wakizishinda zote zitawafanya wasalie kwenye ligi hiyo. Villa, iliyorejea ligi kuu msimu huu ikitokea Ligi Daraja la Kwanza kwa ushindi iliyopata dhidi ya Coastal imewafanya wafikishe pointi 22 ikiwa nafasi ya 12 huku ikisaliwa mechi dhidi ya timu za African Lyon itakayocheza nao keshokutwa jijini Dar, kishaa kuvaana na JKT Oljoro kisha Ruvu Shooting watakaofunga nao dimba la msimu huu.

Kinyogoli aandaa tamasha la ngumi

NYOTA wa kimataifa wa zamani wa ngumi nchini, Habib Kinyogoli kupitia taasisi yake ya Kinyogoli Foundation, inatarajiwa kuendesha michuano maalum ya ngumi iitwayo 'Top Ten Boxing Festival-2012' litakaloanza rasmi Mei 4, jijini Dar es Salaam. Michuano hiyo itakayoshirikisha mabondia wa ngumi za aina zote yaani za ridhaa na kulipwa itafanyika kwenye ukumbi wa Panandi Panandi kwa ajili ya kuibua na kuendeleza vipaji vya mchezo huo kwa kusaka wakali 10 wa kila uzito katika ngumi hizo. Akizungumza na MICHARAZO, Msaidizi wa Kinyogoli, Rajabu Mhamila 'Super D' alisema mabondia na klabu zinazotaka kushiriki michuano hiyo wanatakiwa kujiandikisha mapema kabla ya kuanza kwake akidai itakuwa ikichezwa hadi kupatikana wakali hao. Super D, alisema ameamua kubuni 'ligi' hiyo kwa lengo la kuleta mabadiliko katika mchezo wa ngumi kwa kuibua vijana watakaoisaidia taifa kwa michuano ya kimataifa. Naye Kinyogoli maarufu kama Master, alisema ameamua kuanzisha michuano hiyo katika kuendeleza juhudi zake za kukuza ngumi ambazo zilikwama miaka ya nyuma. "Japo michuano hii itaonekana kama mipya, lakini ni kama wazo nililolibuni miaka 30 iliyopita niliposaidia kuibua vipaji vilivyokuja kutanza nchini kama akina Matumla na wengine," alisema Kinyogoli. Alisema, anaamini michuano hiyo itakapokamilika itasaidia kuibua nyota wapya na kuvihimiza vyama na wadau wa ngumi kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya kushuhudia mchuano sambamba na kuwapiga tafu wale watakaofanya vema kwa faida ya taifa.
Kocha wa ngumi, Rajabu Mhamila 'Super D' msaidizi wa nyota wa zamani wa ngumi nchini, Habib Kinyogoli 'Master' wanaoandaa ligi maalum ya mchezo huo itakayoanza Mei 4.

Mashale awataka Maugo, Cheka

BAADA ya kutwaa ubingwa wa taifa wa TPBO, bondia Thomas Mashale amesema sasa yupo tayari kupigana ama Mada Maugo au Francis Cheka kwa nia ya kuanza kusaka mataji yanayotambuliwa kimataifa. Akizungumza na MICHARAZO, Mashale alisema kwa kuwa mabondia hao wawili ndio walio kwenye viwango vya hali ya juu kwa sasa katika uzani wa kati ni vema akapata fursa ya kupigana ili kuanza mbio zake za kusaka ubingwa wa Dunia. "Kwa sasa natamani kupigana na bondia yeyote kati ya Cheka au Maugo ambao wanatarajiwa kupigana hivi karibuni, lengo ni kutaka kuanza mchakato wa kusaka mataji ya kimataifa," alisema. Alisema kati ya mabondia hao haoni wa kumtisha hasa baada ya kupata uzoefu wa kutosha katika michezo yake mbalimbali aliyocheza tangu aingie kwenye mchezo huo. Mashale, alisema cha muhimu anachoombea kwa sasa ni kupatikana promota wa kumuandalia pambano kati ya mmoja wa mabondia hao ambao wanacheza wote kwenye uzani mmoja wa Middle. Kuhusu ushindi wake alioupata wiki iliyopita dhidi ya Seleman Said 'Galile' Mashale, alisema ulitokana na kufanya vema katika raundi saba za awali na kukiri kwamba mpinzani wake ni mzuri na alimpa usumbufu mkubwa. Alipoulizwa kama yupo tayari kurudiana na Galile, Mashale alisem yu radhi iwapo mpinzani wake huyo atakuwa hajaridhika na matokeo ya ushindi wake uliokuwa wa pointi baada ya kuonyeshana umwamba katika pambano la raundi 10.
Bondia Thomas Mashale 'Simba wa Teranga', akiwa na taji lake la TPBO, mara baada ya kumpiga kwa pointi Seleman Said Galile. Kwa sasa bondia huyo anamtaka kati ya Mada Maugo au Francis Cheka ili apigane nao.

Barcelona yaleteza darajani, yadungwa 1-0

Didier Drogba akishangilia bao lake la pekee lililoisaidia Chelsea kuizima Barcelona kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya mechi iliyochezwa usiku wa kuamkia leo.
BAO lililoifungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Ivory Coast, Didier Drogba dakika za lala salama kabla ya mapumziko ilitosha kuisaidia Chelsea kuizima Barcelona ya Hispania katika pambano la kwanza la nusu fainali baina yao lililochezwa Uingereza.
Drogba alifunga bao hilo pekee dakika ya pili ya dakika za majeruhi baada ya kutimu dakika 45 za kipindi cha kwanza kwenye Uwanja wa Stamford Bridge, London, England Licha ya Barcelona ambao ndio mabingwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa sasa kucharuka katika kipindi cha pili, ilijikuta ikishindwa kurejesha bao hilo hadi pambano lilipomalizika.
Kwa ushindi huo, Chelsea sasa inahitaji sare yoyote kwenye mechi ya marudiano ugenini, Uwanja wa Camop Nou ili kutinga fainali, ambako itacheza na mshindi kati ya Bayern Munich ya Ujerumani na Real Madrid ya Hispania.
Mechi ya kwanza ya kwanza baina ya timu hizo mbili wenyeji Bayern Munich waliitungua Real Madrid mabao 2-1, hivyo Real inahitaji ushindi wa bao 1-0 kama inataka kutinga fainali.

Mgambo Shooting yatinga Ligi Kuu Tanzania Bara, Prisons, Polisi Moro zanusa

TIMU ya soka ya maafande wa Mgambo Shooting ya Tanga imekuwa timu ya kwanza kutinga Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya jana kuisasambua Transit Campo ya Dar kwa mabao 3-0.
Mgambo inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa, ilipata ushindi huo uliowaingiza Ligi Kuu ikiifuata Coastal Union kwenye pambano lililochezwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Mjini Morogoro kunakofanyika fainali za 9 Bora ya Ligi Daraja la Kwanza.
Katika mchezo huo Mgambo ilipata mabao yake kupitia kwa washambuliaji wake, Juma Mwinyimvua aliyefunga mabao mawili katika dakika za 16 na 37 na Nassoro Gumbo aliyefunga kwenye muda wa nyongeza za mchezo huo.
Kwa ushindi huo Mgambo imefikisha jumla ya pointi 15 ambazo haziwezi kufikiwa na timu nyingine ukiondoa Polisi Moro ambao nao wanainyemelea nafasi ya kucheza ligi hiyo msimu ujao.
Katika pambano jingine lililochezwa jioni kwenye uwanja huo, mabingwa wa zamani wa Tanzania, Prisons-Mbeya ilinusa kufuzu ligi kuu msimu ujao baada ya kuicharaza Polisi-Tabora mabao 3-0
Mabao ya Prisons waliofikisha pointi 11 kwa ushindi huo wa jana, yalifungwa na John Mtai aliyefunga mawili na jingine kutumbukizwa kimiani na Peter Michael katika dakika ya nne ya mchezo huo uliochezeshwa vizuri na Shabaan Shata wa Kigoma.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena mchana wa leo kwa mechi kati ya Polisi Moro dhidi ya Mbeya City kabla ya JKT Mlale ya Songea kuumana na Polisi Dar.

Msimamo kamili wa Ligi hiyo ya 9 Bora hadi sasa ni kama ifuatavyo;


MSIMAMO WA 9 BORA LIGI DARAJA LA KWANZA

P W D L F A Pts
1. Mgambo Shooting 7 4 3 - 12 3 15
2. Polisi-Moro 6 4 2 - 12 4 14
3. Prisons-Mbeya 6 3 2 1 8 5 11
4. Mbeya City 6 2 2 2 7 6 8
5. Rhino Rangers 7 2 2 3 4 6 8
6. Polisi Dar 6 1 4 1 6 4 7
7. Mlale JKT 6 1 2 3 5 10 5
8. Polisi-Tabora 6 1 2 3 5 11 5
9. Transit Camp 6 - 1 5 2 12 1

Mwisho

Yanga yatemeshwa taji, Simba kidogo kulibeba jumla




KIPIGO cha bao 1-0 ilichopewa na Kagera Sugar jana kwenye uwanja wa Kaitaba, umeifanya Yanga kulitema taji la ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Yanga iliyokuwa watetezi wa taji hilo ilikumbana na kipigo hicho ikiwa ni cha pili ndani ya siku tatu, baada ya awali kufungwa mabao 3-2 na Toto Afrika jijini Mwanza na kuwafanya wasalie na pointi 43 na michezo mitatu ambayo hata ikishinda yote haiwezi kuzifikia pointi za watani zao, Simba wanaojiandaa kulitwaa taji hilo.
Bao lililoizamisha Yanga lilitumbukizwa wavuni na Shija Mkina na kukatisha ndoto za Yanga ambao walikuwa wakisubiri pointi zao walizopokwa na Kamati ya Mashindano ya TFF kutokana na rufaa waliyokata ambayo imetupiliwa mbali na Kamti ya Nidhamu na Usuluhishi ya Alfred Tibaigana.
Wakati Yanga ikitota Kagera na kuweka rekodi na kupoteza pointi sita katika Kanda ya Ziwa kwa mara ya kwanza, watani zao Simba jana walitakata uwanja wa Taifa baada ya kuinyoa JKT Ruvu mabao 3-0.
Ushindi uliifanya Simba ifuzu kucheza michuano ya CAF msimu ujao baada ya kujihakikishia kumaliza katika moja ya nafasi mbili za juu kutokana na kufikisha pointi 56 ambazo haziwezi kufikiwa na Yanga.
Azam yenye pointi 50 huku ikiwa na mechi moja mkononi, itaikaribisha Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Chamazi Jumamosi.
Simba ilianza kuhesabu goli la kwanza katika dakika ya kwanza ya mchezo kupitia kwa kiungo Uhuru Selemani aliyefunga kwa kichwa akiunganisha krosi ya Mganda Emmanuel Okwi na kiungo kipenzi cha mashabiki wa Simba, Haruna Moshi 'Boban' akafunga moja ya mabao bora ya msimu wakati alipokimbia na mpira kutokea katikati ya uwanja na kupiga shuti lililomshinda kipa Amani Simba wa JKT katika dakika ya 17.
Kiungo wa timu ya taifa, Taifa Stars, Mwinyi Kazimoto alifunga goli la 'kideoni' katika dakika ya 64 na kuisogeza Simba jirani zaidi na ubingwa.
Matokeo mengine ya ligi hiyo kwa jana, Ruvu Shootingi ilishinda 1-0 dhidi ya Moro United, bao lililotumbukizwa wavuni na Saleh Kitala dakika ya 90, huku Toto wakiendeleza wimbi la ushindi kwa kuicharaza African Lyon mabao 2-0.
Nao watoto wa Julio, Coastal Union, ilizinduka baada ya kichapo cha aibu cha mabao 4-2 toka kwa Villa Squad kwa kuitandika Polisi Dodoma mabao 3-l.
Kipigo hicho kimezidi kuiweka pabaya Polisi Dodoma kwani sasa ni kudra za Mungu tu ndizo zinazoweza kuinusuru isishuke daraja kurejea Ligi Daraja la Kwanza.

TIBAIGANA AICHINJA YANGA



Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Aprili 17 mwaka huu) imetupa rufani ya Yanga iliyowasilishwa mbele yake kupinga uamuzi wa kupokwa pointi tatu kwa kumchezesha mchezaji asiyestahili.
Aprili 2 mwaka huu Kamati ya Ligi ya TFF iliipa Coastal Union ushindi wa pointi tatu na mabao matatu baada ya Yanga kumchezesha beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya timu hizo iliyofanyika Machi 31 mwaka huu wakati akiwa na adhabu ya kukosa mechi tatu.
Yanga katika rufani hiyo iliwasilisha sababu nane za kupinga kupokwa pointi hizo, kubwa zikiwa Cannavaro hakustahili kutumikia adhabu ya kukosa mechi tatu, si aliyempiga refa Israel Nkongo, ripoti za refa na kamishna wa mechi yao dhidi ya Azam zilionesha dalili ya njama (conspiracy) kwani zilifanana.
Pia Cannavaro alikuwa miongoni mwa wachezaji ambao adhabu zao zilisimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu, Kamishna mstaafu wa Polisi, Alfred Tibaigana.
Katika uamuzi wake, Kamati imesema adhabu ya Cannavaro ya kukosa mechi tatu kwa mujibu wa Kanuni ya 25(c) ya Ligi Kuu ya Vodacom ilitolewa na refa na si Kamati ya Ligi kama ambavyo inalalamikiwa na Yanga, na kanuni hiyo haikatiwi rufani.
Pia barua ambayo TFF iliiandikia Yanga kuhusu adhabu ya mchezaji huyo ilikuwa wazi kwani ilikariri kanuni ya 25(c), hivyo kitendo cha klabu hiyo kumtumia mchezaji huyo ulikuwa ni uzembe wa kutoheshimu kanuni. Kama Yanga haikufahamu vizuri kanuni hiyo ilikuwa na fursa ya kuiandikia TFF kwa mujibu wa Kanuni ya 25(f) ili kupata ufafanuzi kabla ya kuamua kumtumia mchezaji huyo.
Vilevile adhabu zilizokuwa zimesimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu ni zile ambazo zilikuwa zimetolewa na Kamati ya Ligi, na si zile zilizotolewa uwanjani na refa.
Kuhusu madai ya conspiracy kwa ripoti za kamishna wa mchezo huo na refa, Kamati imebaini kuwa hazifanani, na suala lililokuwa likibishaniwa (contentious issue) lilikuwa ni kunyang’anywa pointi tatu.
Pia Kamati ilikariri Ibara ya 50 ya Kanuni za Nidhamu za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kuwa mchezaji anayembughudhi refa kwa njia yoyote ile anastahili kufungiwa kwa angalau mechi sita.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)