STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, September 26, 2011

Golden Boy, kuzinyuka na Miyeyusho

BINGWA wa UBO-Mabara, Mbwana Matumla 'Golden Boy' anatarajia kupanda ulingoni mwezi ujao kuzipiga na bondia Francis Miyeyusho katika pambano la kutetea taji lake litakalofanyika jijini Dar es Salaam.
Pambano hilo la uzani wa Bantam litakalokuwa la raundi 10, litafanyika Oktoba 30 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, likisindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Kwa mujibu wa kocha msaidizi wa kambi ya Kinyogoli Foundation inayowanoa mabondia watakaosindikiza pambano hilo la Matumla na Miyeyusho, Rajab Mhamila ni kwamba maandalizi ya pigano yanaendelea vema.
Mhamila, alisema pamoja na kwamba pambano hilo ni la kuwania taji la UBO, lakini pia limewagawa mashabiki wa ngumi kulingana na mahali wanapotoka mabondia hao nyota, ambapo Matumla yeye anatokea Temeke na Miyeyusho akitokea Kinondoni.
"Pambano la Matumla na Miyeyusho ni kama la watu wa Temeke na Kinondoni, huku yale ya utangulizi yatahusisha mabondia wa pande hizo mbili, hali inayofanya pigano hilo lijalo kuwa na msisimko wa aina yake," alisema Mhamila.
Mhamila, alisema pambano hilo la UBO limeratibiwa na Mood Bawazir wa kampuni ya Dar World Links na litasindikizwa na michezo ipatayo mitano ya utangulizi kati ya hiyo ni pigano linalosubiriwa kwa hamu kati ya Ramadhani Shauri wa Kinondoni dhidi ya Issa Sewe kutoka Temeke.
Pigano hilo la Matumla, linakuja miezi minne tangu bondia huyo alipopanda ulingoni na kulitetea taji lake hilo kwa kumchakaza Mkenya, Gabriel Ochieng katika pambano lililofanyika Mei Mosi, kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam.
Mabondia wote wawili yaani Matumla na Miyeyusho kwa sasa wapo kambini wakijifua kwa ajili ya pambano hilo, kila mmoja akitamba kuibuka na ushindi siku ya pigano hilo.

Mwisho

Maugo kuzichapa na Mkenya



BONDIA machachari wa ngumi za kulipwa nchini, Mada Maugo anatarajiwa kupanda tena ulingoni jijini Mwanza kuzipiga na Mkenya, ikiwa anatokea kuuguza kipigo toka kwa Francis Cheka.
Aidha bondia huyo amesema hayupo tayari kupigana tena na Francis Cheka, labda kama mwamuzi na majaji watakuwa ni wa kutoka nje ya nchi kwa kile alichodia waamuzi na majaji wa nchini humbeba mpinzani wake kila mara.
kizungumza na MICHARAZO, Maugo, alisema pambano hilo la Mkenya Mosses Odhiambo litafanyika Novemba kwenye uwanja wa CCM Kirumba.
Maugo, alisema pambano hilo lisilokuwa la ubingwa la raundi 10 na la uzani wa kati, ni maalum kwa maandalizi ya kwenda kupigana nje ya nchi katika pambano la kimataifa dhidi ya Mjerumani.
"Natarajia kupanda ulingoni mwezi Novemba kupigana na Mkenya katika pambano la raundi 10 la uzito wa kilo 72, lisilo la ubingwa kwa nia ya kujiweka fiti kabla ya kwenda kupigana ngumi za kimataifa dhidi ya Mjerumani," alisema Maugo.
Kuhusu kurudiana na Cheka, Maugo alisema atakuwa radhi kufanya hivyo kama majaji na waamuzi watatoka nje ya nchi kwa madai wa ndani humbeba mpinzani wake kama ilivyotokea kwenye mechi zao mbili ambapo zote alipigwa kwa pointi.
"Sintakuwa tayari kupigana tena na Cheka, labda kama waandaaji watawaleta majaji na mwamuzi kutoka nje, mpinzani wangu wamekuwa akibebwa ndio maana rekodi yake nje ya nchi ni mbovu tofauti na anavyotamba akicheza nyumbani," alisema.
Alisema wiki iliyopita akifuatwa na mmoja wa mapromota akiwataka wapigane na Cheka katika pambano la kusaka mbabe kati yao, na kuweka msimamo wake huo, hali iliyofanya muaandaji huyo kuamua kuachana na wazo la kuwapiganisha tena.
Maugo alipigwa kwa pointi na Cheka katika mapambano yaliyofanyika Januari Mosi, jijini Dar es Salaam na Septemba Mosi, mjini Morogoro, ambapo kote bondia huyo alikuwa akilalamikia 'kuchakachuliwa' matokeo.

Anti Fifi: Jimama linalotesa Bongo Movie, sasa ageukia utunzi wa vitabu







WAKATI mastaa wenye majina na umaarufu mkubwa kama wake nchini hupenda kuishi maisha 'bandia' ya kuhofia kujishughulisha na kazi au kujichanganya na watu
wengine wa kawaida, kwa Tumaini Biligimana au 'Anti Fifi', hali ni tofauti.
Licha ya umaarufu alionao kupitia sanaa aliyoanza kuifanya zaidi ya miaka 20 akianzia kama promota wa urembo, disko na muziki wa kizazi kipya, Anti Fifi anauza 'genge' la chakula eneo la Mwananyamala, alipika na kuuza mwenyewe.
Pia, nyota huyo haoni aibu kula 'chips dume' (mihogo ya kukaanga) au kupanda daladala katika mizunguko yake jijini Dar, licha ya kumiliki gari zuri la kisasa.
"Siwezi kuhofia kuishi nilivyozoea kwa sababu ya jina kubwa, kuishi 'bandia' ndiko kunakoponza mastaa wengi kuishia kwenye machafu wakitafuta mkato ya maisha ili waonekane bab'kubwa," alisema.
Alisema, tangu alipoanza kupata umaarufu hajawahi kuona aibu kujichanganya na watu wengine, jambo alilodai limemrahisishia mambo yake mengiu kimaisha na kisanii.
Anti Fifi, aliyefanya kazi na madansa wa nyota wa zamani kama Black Mosses, Master
Flash na wengine, alisema kitendo cha kupika na kuuza chakula katika mgahawa wake kumemfanya apate wateja wengi, baadhi wakienda ili kujiridhisha kama kweli ni yeye au wanamfananisha na mtu wanayemuona kwenye filamu.
Msanii huyo alisema anavyofahamu yeye, ustaa wa mtu kujizuia na matendo machafu na ya aibu mbele ya jamii, ila sio kuogopa kujichanganya au kuishi vile mtu apendavyo au alivyozoea.
"Ustaa ni kujiheshimu, kujithamini na kujichanganya na watu ili kujifunza mengi toka kwao yanayoweza kumsaidia msanii katika kukuza sanaa yake, sio kuishi maisha bandia ya hadhi ya juu, ilihali uwezo huo mtu hana," alisema.
Muigizaji huyo ambaye pia, ni mtunzi, mtayarishaji na mwandishi wa vitabu, alisema mbali na kuuga mgahawa, pia anajiuza mayai ya jumla katika nchi jirani, sambamba na nguo na vipodozi vya wanawake na watoto.
Alisema anaamini wasanii wakiamua kuishi jinsi walivyo kabla ya kupata umaarufu wanaweza kujiepusha na skendo chafu ambazo zimekuwa ni mazoea kwao na kuitia doa sanaa yao kwa ujumla.
"Sijisifii, ila mie ni baadhi ya wasanii wanaojiheshimu kwa vile naishi jinsi nilivyo, hivyo sikumbwi na skendo kwa kusaka umaarufu, bali kazi zangu ndizo zinazonipa 'ujiko' mbele ya jamii, kama unavyojua majuzi tu filamu niliyotunga ya 'Senior Bachelor' ilitwaa tuzo ZIFF."
Anti Fifi anayependa kula ugali kwa samaki na dagaa na kunywa juisi ya karoti na passion, alisema tangu atumbukie kwenye sanaa amenufaika kwa mengi, ikiwemo umaarufu, kujenga nyumba, kumiliki gari na kiwanja alichoanza kukijenga nyumba nyingine eneo la Mbezi.
"Najivunia sanaa pia, imenisaidia kuweza kutunga na kuuza hadithi za filamu, huku kwa sasa nikiwa nimetumbukia kwenye utunzi wa vitabu, nikijiandaa kutoa kitabu kiitwacho 'Migogoro ya Ndoa na Suluhisho Lake'," alisema.
Anti Fifi, aliyewahi kuishi maisha ya ndoa ya kiislam kuanzia mwaka 1989-2001 alipoachika, alisema matarajio yake ni kutaka kujitofautisha na wasanii wengine nchini akitaka kuwa mtunzi mahiri wa vitabu na filamu kwa ujumla.
Anti Fifi, aliyeokoka kwa sasa, alisema kama angekutana na Rais angemuomba asaidie kuiinua sanaa nchini na kukomesha uharamia, ili inawanufaishe wasanii.
"Hata mimi ningekuwa Rais ningeyafanya hayo, pamoja na kuondoa kero ya umeme nchini, kwani ni aibu kwa Tanzania yenye vyanzo vingi vya kuzalisha nishati hiyo kuwa na tatizo la ukosefu wa umeme na kuliingiza taifa kwenye hasara kubwa,: alisema.
Tumaini Biligimana, aliyezaliwa Julai 17, 1965 mjini Kigoma, akiwa mtoto wa sita kati ya 13 wa Mzee Biligimana, alisema hakuna tukio la furaha kwake kama aliposhiriki filamu ya Dar es Salaam akiigiza kama Jimama la Kikongo, linaloendesha genge la mabinti wahalifu, kiasi cha kufuatiliwa na Polisi, waliodhani huenda ndivyo alivyo.
"Huwezi amini nilifuatiliwa na Polisi kwenye duka na saluni yangu wakinipeleleza kwa kile walichokiona kwenye filamu hiyo niliyoiigiza mara nilipotua Dar nikitokea Kigoma," alisema.
Kisanii, Anti Fifi mwenye watoto watatu, Mohamed, 24 anayesoma kidato cha tano nchini Uganda, Omari, 21 anayesomea ufundi VETA na Zamda, 17 aliyepo kidato cha pili Shule ya Sekondari Kunduchi Beach, alianza tangu shuleni akicheza ngoma, kuimba na kupiga filimbi.
Alisema pia alikuwa mahiri wa kuchora, kubinuka sarakasi wakati wakisoma Shule ya Msingi Muungano na baadae Ujiji Sec, kabla ya kuajiriwa serikalini kama Mhasibu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma.
Baada ya miaka tisa ya utumishi wa umma, aliacha kazi hiyo na kujikita katika biashara akiwa promota wa fani ya urembo na disko, hadi mwaka 2001 aliposhiriki uzinduzi wa filamu ya Girlfriend na kupata kiu ya kuwa muigizaji baada ya kukutana na George 'Tyson' Otieno.
Alianza fani hiyo kwa kutunga na kuigiza filamu ya kwanza iitwayo Haraka ya Maisha ya mwaka 2002 kabla ya kuja Dar miaka miwili baadae kujiunga na kundi la Fukuto Arts na kushiriki filamu ya Dar es Salaam iliyomfungulia neema ya mafanikio.
Kazi nyingine alizoshiriki ni pamoja na Copy, Sound of Death, Senior Bachelor, I Deserve It, Kaburi la Mapenzi, Kizungumkuti, Fake Smile, Daddy, na nyinginezo baadhi akizitunga.
Anti Fifi anayechizishwa na rangi ya zambarau na pinki, alisema anawazimia Jacob Stephen 'JB', Irene Uwoya na Aunty Ezekiel, aliwaasa wasanii wenzake wajitume na kujichanganya kusaka maisha nje ya sanaa zao, kwa lengo la kuepusha kutumiwa ovyo.

Watanzania hawana utamaduni wa kusoma-EZAA





CHAMA cha Waandishi wa Vitabu Kanda ya Mashariki, EZAA, kimesema asilimia kubwa ya watanzania hawana utamaduni wa kupenda kusoma vitabu, jambo linalochangia kuwepo kwa ugumu wa soko la vitabu nchini.
Katibu Mkuu wa chama hicho, Jackson Kalindimya, aliyasema hayo wakati wa semina ya siku tatu ya watunzi wa vitabu vya hadithi za watoto, iliyofanyika kwenye ukumbi wa Msukuma, mjini Mlandizi, Pwani.
Kalindimya alisema Tanzania ina tatizo la watu kupenda kusoma, kitu ambacho kwa kiasi kikubwa kimekuwa kikiathiri soko la vitabu na maandishi mengi.
Hata hivyo, aliwaasa waandishi na watunzi wa vitabu kutokata tamaa badala yake kuzidi kuandaa kazi zenye mvuto ambavyo zitachochea wananchi kubadilika na kuanza kupenda kusoma kama ilivyo kwa mataifa mengi.
Kalindimya alisema tofauti na wananchi wa mataifa mengine ambao wawapo safarini au mahali popote hubeba vitabu au majarida kwa ajili ya kujisomea, kwa wananchi wa Tanzania ni wachache wanaofanya hivyo, kitu alichotaka watanzania wabadilike.
"Wananchi wanapaswa kubadilika na kujenga tabia ya kupenda kusoma kwani itawasaidia kuelimika, sambamba na kusaidia soko la kazi za waandishi," alisema.
"Licha ya hali hiyo, watunzi na waandishi msikate tamaa, muikabili changamoto hiyo kwa kuandaa kazi zenye mzuri zenye mvuto ambazo zitawabadilisha wananchi, pia ikirahisisha soko la kazi zenu," alisema.
Baadhi ya washiriki wa semina hiyo, ambao ni chipukizi katika utunzi na uandishi wa vitabu, waliwapongeza waandaaji wake kwa namna walivyowasaidia kuelewa mambo ambayo kabla ya hapo walikuwa hawana ufahamu nayo katika fani hiyo.

CBP yataka mrithi wa Shaaban Robert apatikane




WATUNZI na waandishi wa kazi za Fasihi nchini, wamepewa changamoto ya kujibidiisha katika fani zao, ili kumpata 'Shaaban Robert' mpya miongoni mwao atakayeendeleza na kudumisha fasihi katika kiwango alichokuwa nayo gwiji huyo.
Aidha jamii imeaswa kujenga utamaduni wa kuwanunulia na kuwasomea vitabu vya hadithi watoto wao kama njia ya kuchochea uwezo wao kuelewa na akili ambao utawasaidia katika masomo ya kitaaluma.
Katibu Mtendaji wa Mradi wa Vitabu vya Watoto Tanzania, CBP, Pili Dumea, ndiye aliyetoa wito huo kwa waandishi wakati wa ufungwaji wa semina ya siku tatu ya Waandishi wa Vitabu Kanda ya Mashariki, EZAA, iliyofanyika Mlandizi, mkoani Pwani.
Dumea, alisema watunzi na waandishi chipukizi wa kazi za fasihi wanapaswa kufanya kazi zao kwa umahiri, ili waweze kuja kumrithi Shaaba Robert, ambaye licha ya kufariki kitambo kirefu, bado amekosa wa kufikia umahiri wake katika fani hiyo.
"Semina na mafunzo haya yawe chachu kwenu katika kujibidiisha na kujituma katika fani hii mkiwa na lengo la kutaka kuwa warithi wa Shaaba Robert, ambaye licha ya kutokuwepo kazi zake zimeendelea kudumu milele," alisema Dumea.
Katibu huyo alisema CBP, ipo kwa ajili ya kuwasaidia watunzi na waandishi wa vitabu kufikia lengo la kuendeleza fasihi hasa vitabu vya hadithi vitakavyochochea maendeleo ya nchi kuanzia kwa watoto hadi watu wazima.
Pia, alisema jamii ni lazima iwe na utamaduni wa kuwasomea na kuwanunulia watoto vitabu kuwazoesha kusoma na kuchochea ufahamu wao na uwezo wao wa kimasomo darasani, akidai kusoma ni njia ya kusaidia uelewa na akili za mtu.
Naye Katibu Mkuu wa EZAA, Jackson Kalindimya, aliwaasa waandishi hao watumie vema uwezo wao wa 'kimungu' walionao katika kuchochea maendeleo ya nchi pamoja na kuijenga jamii katika maadili mema.
Kalindimya, alisema watunzi wa vitabu ambao wana uwezo wa kuumba dunia yao na viumbe wengine wakiwapa pumzi, tabia na uhusika unaoweza kuibadilisha jamii kutoka mahali pamoja hadi kwingine kimaendeleo na hata kimaadili kupitia kazi zao.
"Lazima mjivunie uwezo wa kimungu mlionao, kwa kuisaidia jamii kubadilika mahali ilipo hadi kwenye maendeleo, cha muhimu ni kutoa kazi nzuri zenye mvuto ambazo zitawafanya watu wazinunue na kuzisoma, kisha kuwabadilisha," alisema.

Mwisho

Wednesday, September 21, 2011

Kaseba amwinda Oswald


BONDIA mchachari nchini, Japhet Kaseba yupo katika maandalizi makali kwa ajili ya pambano lake dhidi ya mzoefu, Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo', akitamba kuwa anafanya hivyo ili kumzima mpinzani wake.
Kaseba na Oswald wanatarajiwa kupanda ulingoni kuzipiga katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 la uzani wa kati, litakalofanyika kwenye ukumbi wa Travertine, jijini Dar es Salaam.
Kila bondia amekuwa kwenye maandalizi ya pambano hilo, ambapo Kaseba, bingwa wa zamani wa dunia wa kick boxing, alikutwa na Micharazo kambini kwake, Mwananyamala Komakoma akijifua, huku akiapa kumshinda mpinzani wake.
"Kaka kama unavyoniona, nia yangu ni kutaka kurejesha heshima yangu katika ngumi kwa kutaka kumchakaza Oswald, siku tukikutana kwenye pambano hilo ambalo litasimamiwa na PST," alisema Kaseba.
Kaseba, alisema anaamini mazoezi anayofanya yatamwezesha kumnyuka Oswald ambaye kambi yake ipo Keko, ambapo amekuwa akisisitiza anataka kumshikisha adabu, muhimu mwamuzi amchunge Kaseba asirushe mateke yake.
Bondia huyo, alisema pambano lao na Oswald limeratibiwa na Gervas Muganda, litasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi ambapo aliyataja baadhi kuwa ni kati ya
Kaseba, alisema kabla ya pambano lake na Oswald ambaye amenukuliwa akitamba kumpiga akitaka waamuzi kumchunga asirushe mateke kwa kudhani yupo kwenye kick boxing, watasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Michezo hiyo ni pamoja na pigano la bingwa wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini, Ernest Bujiku dhidi ya Mbukile Chuwa.
Mapambano mengine ambayo yote yameandaliwa na mratibu, Gervas Muganda wa kampuni ya Babyface ni, Chaurembo Palasa dhidi ya Sweet Kalulu, Venance Mponji atapanda ulingoni kuzipiga na Jafar Majiha 'Mr Nice' na michezo miwili ya kick boxing.
Moja ya pambano hilo la Kick Boxing ni kati ya Ramadhani Mshana atapigana na Hamed Said na Kaseba alisema maandalizi yote kwa ajili ya michezo hiyo inaendelea vema.

Mwisho

Tuesday, September 13, 2011

Fella akamilisha albamu ya 'Rusha Roho'




MENEJA wa kundi mahiri la muziki wa kizazi kipya nchini la TMK Wanaume Family, Said Fella 'Mkubwa Fella', amekamilisha albamu yake mpya na ya kwanza ya miondoko ya taarab akiipa jina la 'Kunguni' ikiwa na nyimbo sita.
Akizungumza na MIcharazo, Mkubwa Fella, alisema albamu hiyo ambayo nyimbo zake zimewashirikisha wasanii nyota wa muziki huo kama Khadija Kopa, Maua Tego na Isha Mashauzi itaachiwa rasmi mtaani mapema mwezi ujao.
Fella alisema katika kutaka kuitambulisha albamu hiyo ameshafyatua video ya wimbo wa Kusonona, atakayoiachia rasmi Ijumaa wiki hii.
"Nimekamilisha albamu yangu yenye nyimbo sita ambapo mmoja nimeufanyia video na ninatarajiwa kuanza kuusambaza kwenye vituo vya runinga Ijumaa ijayo," alisema.
Alivitaja vibao vya albamu hiyo ni 'Simuachi', 'Midomo Imewashuka', 'Mchakamchaka', 'Sijapopoa Dodo', 'Kimodern Modern' na 'Kusonona'.
Fella alisema ushirikiano aliofanya na wasanii wenye majina makubwa katika muziki huo utasaidia kuibeba albamu hiyo, iliyotangulishwa na kibao cha Midomo Imewashuka kinachoendelea kutamba kwenye vituo kadhaa vya redio nchini.

Mwisho

Extra Bongo 'kujinafasi' Kanda ya Ziwa



BENDI ya muziki wa dansi ya Extra Bongo 'Wazee wa Kujinafasi' inatarajia kuondoka jijini dar es salaam kuelekea mikoa ya Kanda ya Ziwa Victoria ya Mara na Mwanza ili kufanya maonyesho kadhaa ya burudani.
Meneja wa bendi hiyo, Mujibu Hamis alisema kuwa Extra Bongo itaondoka jijini Dar es Salaam kesho Alhamisi ambapo inatarajia kufanya onyesho la kwanza keshokutwa Ijumaa katika ukumbi wa Magereza, mjini Musoma mkoani Mara.
"Kama utakumbuka, ilikuwa tuanze ziara ya mikoa hiyo kabla ya kuanza kwa mfungo wa Ramadhan, lakini bahati mbaya kulitokea mambo ambayo yako juu ya uwezo wetu tukalazimika kuahirisha ziara yetu," alisema Mujibu.
Alisema kuwa kwa sasa kila kitu kiko sana na kwamba wanamuziki wake wako tayari kwenda kuwaburudisha wapenzi wa bendi hiyo wa miji ya Musoma na Mwanza ambako wamekuwa wakisubiriwa kwa hamu.
"Katika ziara hii tutamtambulisha mnenguaji wetu mpya, Aisha Madinda pamoja na nyimbo za albamu ya pili ambazo ni Neema, Mtenda Akitendewa, Watu na Falsafa, Bakutuka, Mama Shuu na Fisadi wa Mapenzi," alisema.
Alisema, kabla ya kuondoka kuelekea mkoani Mara, leo Jumatano watafanya vyao kwa ajili kuwaaga wapenzi wa bendi hiyo kwenye onyesho litakalofanyika katika ukumbi wa Masai uliopo Ilala Bungoni.
Extra Bongo ni bendi inayokuja kwa kasi kwenye angaza za muziki wa dansi ikiwa na albamu ya kwanza ya 'Mjini Mipango' ambayo nyimbo zake 'Wema','Maisha Taiti', 'Laptop', 'First Lady' na 'Safari ya Maisha'.

Hammer Q aibuka Eagle Modern taarab



MUIMBAJI nyota wa muziki wa taarab nchini, Husseni Mohammed 'Hammer Q' ameanzisha kundi jipya la miondoko hilo, liitwalo Eagle Modern Taarab 'Wana Kimanumanu' likiwa limeshaachia nyimbo mbili mpya za kulitambulisha.
Akizungumza na Micharazo, Hammer Q, alisema kundi hilo linaloundwa na wasanii 16, linajiandaa kukamilisha albamu yao ya kwanza itakayokuwa na nyimbo tano, mbili kati ya hizo zimerekodiwa video na zimeshasambazwa ili virushwe hewani.
Hammer Q aliyekuwa Five Star baada ya awali kulitema kundi la Dar Modern Taarab, alizitaja nyimbo zilizorekodiwa audio na video kwa ajili ya kulitambulisha kabla ya kuanza kufanya maonyesho yake ni Tatu Bila na Zangu Dua.
"Baada ya kimya kirefu, nimeibuka nikiwa na kundi jipya la taarab liitwalo 'Eagle Modern Taarab na tayari tumeshakamilisha nyimbo mbili kati ya tano tunazoandaa kwa ajili ya albamu yetu ya kwanza," alisema Hammer Q.
Nyota huyo aliyetamba na vibao kama Pembe la Ng'ombe na Kitu Mapenzi akiwa Dar Modern, alisema kundi lao lina wasanii 16 baadhi yao wakiwa ni wale aliokuwa nao kundi la Dar Modern kama Latifa Salum, Ramadhani Kisolo na Aisha Athuman.
Wengine wanaounda kundi hilo jipya lililokua wiki chache tangu kuanzishwa kwa kundi jingine la Tanzania Moto Taarab ni; Mwanaidi Ramadhani, Asma Ally, Mohammed Mzaka na wengineo waliopo kambini wakijiandaa na kujitambulisha rasmi kwa mashabiki wa miondoko hiyo.
Hammer Q, alisema tayari nyimbo tano za albamu yao zimekamilika na kuzitaja majina yake na waimbaji wake kuwa ni; 'Tatu Bila'-Hammer Q, 'Zangu Dua'-Latifa Salum, 'Kunyamaza Kwangu'- Mwanaidi Ramadhani, 'Siri ya Mungu'-Aisha Athuman na 'Mapenzi ya Dhati'-Asma.

Sunday, August 28, 2011

Timu ya Ngumi kuondoka leo mchana




TIMU ya taifa ya mchezo wa ngumi itakayoiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya Michezo ya Afrika (All African Games) inatarajiwa kuondoka mchana huu kuelekea nchini Msumbiji, ikiwa na mabondia wanne pamoja na viongozi wawili.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi Tanzania, BFT, Makore Mashaga, aliiambia MICHARAZO kuwa, timu hiyo imelazimika kuwahia mapema kwenda Maputo, kutokana na kuwepo kwa mabadiliko ya kuanza kwa michuano hiyo kutoka Septemba 3 hadi Septemba 1.
Mashaga, alisema kikosi hicho kilitarajiwa kuondoka jana kwa ndege kikiwa na mabondia wanne na makocha wao wawili tayari kwenda kuwahi zoezi la upimaji afya litakalofanyika kesho (Agosti 30).
"Hapa ninapozungumza nawe nipo katika harakati za kukamilisha kuiwahisha timu uwanja wa ndege ili kuondoka kwenda Msumbiji, ambapo timu yetu itawakilisha na mabondia wanne na makocha wao wawili," alisema Mashaga.
Katibu huyo aliwataja mabondia hao kuwa ni Emilian Patrick atakayepigana uzani wa Feather, Martin Joseph (Middle) na Seleman Kidunda na Macmillian Patrick ambao watapigana uzito wa juu (kilo 91).
"Hao ndio mabondia watakaiwakilisha Tanzania baada ya kufanyika mchujo chini ya makocha, Hurtado Pimenter na msaidizi wake, ambao nao wapo kwenye msafara huo wa kwenda Msumbiji," alisema.
Mashaga alisema BFT ina imani kubwa kwa timu hiyo kufanya vema kama mabondia na makocha wao walivyowaahidi Watanzania kwamba wanaenda kushindana na sio kushiriki au kuwa wasindikizaji.
Mara ya mwisho Tanzania kufanya vema kwenye mashindano hayo kwa upande wa ngumi ilikuwa michuano ya mwaka 2007, yaliyofanyika nchini Algeria ambapo bondia Emilian Patrick aliambulia medali ya fedha.
Wakati huohuo timu ya taifa ya michezo ya Walemavu (Paralimpiki) yenye wachezaji watano inatarajiwa kuondoka Jumatano kwa ajili ya kushiriki michuano hiyo ya All African Games.
Timu zingine zitakazowakilisha Tanzania katika michezo hiyo ya 10 ya Afrika itakayofanyikia kwenye dimba la Zimpeto, mjini Maputo ni zile za Riadha, Netiboli na Soka ambazo zitaondoka pia Jumatano.

Mwisho

Villa yaapa kufa na Simba, yadai ushamba umeshawatoka




KLABU ya soka ya Villa Squad umedai 'ushamba' waliokuwa nao katika Ligi Kuu Tanzania Bara umeshawatoka na kuionya Simba isitarajie mteremko kwenye pambano lao lijalo.
Simba waliopo nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi hiyo nyuma ya Toto Afrika, itaikaribisha Villa katika pambano litakalochezwa Septemba 8, uwanja wa Mkwakwani, mjini Tanga.
Licha ya uongozi huo wa Villa, kukiri kuwa Simba ni timu nzuri, bado wanaionya kwamba isitarajie wepesi kutokana na kikosi chao kujipanga kuwakabili ili kushinda mchezo huo.
Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ramadhani Uledi, alisema mapema leo asubuhi kuwa, kipigo cha mabao 3-0 walichopewa na Toto Afrika katika mechi yao ya awali iliwatoa ushamba na kwa sasa kikosi chao kimeanza kuizoea ligi hiyo na kuonyesha ushindani wa kweli.
Uledi, alisema kuthibitisha hilo waliweza kuibana Kagera Sugar nyumbani kwao na kutoka sare ya bao 1-1 , hali inayowafanya kujiamini wanaweza kuikabili timu yoyote ikiwemo Simba na Yanga.
"Aisee tunaendelea kujiandaa kwa ajili ya pambano letu na Simba, kifupi ni kwamba tumeshaanza kuizoea ligi na kwamba wapinzani wetu wasitarajie mteremko Mkwakwani, hiyo Septmba 8," alisema.
Aliongeza, benchi lao la ufundi linatumia mapumziko ya wiki moja ya ligi kuu kurekebisha matatizo yaliyotokea katika mechi za awali ili kuweza kuingia dimbani kuikabili Simba wakiwa fiti.
"Timu inaendelea kujifua na tuna imani mapumziko yaliyopo yatawapa nafasi makocha na wachezaji kuweka mambo sawa," alisema.
Uledi alisema wachezaji wao wawili waliokuwa majeruhi wameanza kupaata nafuu na kwamba hadi siku ya pambano hilo hali yao itakuwa imetengemaa na kurejea dimbani kuisaidia timu yao.
Klabu hiyo ya Villa Squad inayoshikilia mkia kwa sasa katika msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi moja, ni miongoni mwa timu nne zilizopanda ligi kuu msimu huu, nyimngine zikiwa ni Coastal Union, JKT Oljoro na Moro United.

Mwisho

Saturday, August 27, 2011

Mnanda wamtoa Ferouz wa Daz Nundaz


MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Feruzi Mrisho 'Ferouz' aliye mbioni kuachia kazi yake mpya iitwayo 'Ndege Mtini', amedai kibao hicho alichokiimba katika miondoko ya Mchiriku utamrejesha kwenye chati yake ya zamani.
Ferouz aliyekuwa kimya karibu miaka mitatu iliyopita, alisema aliamua kuimba kibao hicho kipya alichomshirikisha chipukizi wa THT, Shoz Dia, miondoko ya 'mnanda' ili kurudi upya.
"Nimeamua kutoa upya na mnanda kwa nia ya kurejesha makali yangu, pia kuonyesha utoauti wa Ferouz wa Das Nundaz au wa 'Starehe' na huyu wa sasa," alisema.
Mkali huyo aliyetamba na vibao kadhaa kikiwemo hicho cha Starehe alichoimba na Profesa Jay, alisema kibao hicho cha Niwqe Nawe anachojiandaa kukifyatulia video yake, ni utangulizi wa ujio wa albamu yake mpya itakayofahamika kwa jina la 'Reserve'.
Aliongeza ndani ya albamu hiyo atakayowashirikisha wasanii kadhaa nyota akiwemo mshindi wa Tuzo Tano za Kili Music Awards-2011, 20 Percent itakuwa na nyimbo nane.
Feropuz alizitaja nyimbo hizo kuwa ni pamoja na Ndege Mtini, Nimemfukuza, 'Reserve' na Tusifuatane.
Hiyo itakuwa ni albamu ya tatu kwa mkali huyo kwani baada ya kutoa albamu ya 'Safari' mwaka 2004 iliyokuwa na wimbo wa Starehe, alifyatua nyingine ya pili iitwayo Sauti Nyimbo na Vyombo iliyokuwa na wimbo wa 'Mr Policeman, kabla ya kutoweka hadi alipobuka juzi.

Mwisho.

Kaseba, Oswald kuzipiga Okt Mosi




BINGWA wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini, Ernest Bujiku na Chaurembo Palasa ni kati ya mabondia watakaopanda ulingoni kusindikiza pambano la mkongwe Maneno Oswald na Japhet Kaseba litakalofanyika Oktoba Mosi.
Pambano hilo la raundi 10 lisilo la ubingwa la uzani wa kilo 72 la Kaseba na Oswald maarufu kama Mtambo wa Gombo litafanyikia kwenye ukumbi wa hoteli ya Travertine Magomeni likisimamiwa na Shirikisho la Ngumi za Kulipwa nchini, PST, chini ya uratibu wa promota, Gervas Muganda wa kampuni ya Babyface ya jijini Dar.
Akizungumza na Micharazo jana, Kaseba, alisema kabla ya yeye kupigana na Oswald watasindikizwa na michezo kadhaa akiyataja baadhi likiwakutanisha Chaurembo Palasa dhidi ya Sweet Kalulu, Ernest Bujiku atakayepigana na Mbukile Chuwa.
Kaseba alisema pia siku hiyo Venance Mponji atapanda ulingoni kuzipiga na Jafar Majiha 'Mr Nice' na kutakuwa na michezo miwili ya kick boxing ambapo Ramadhani Mshana atapigana na Hamed Said na jingine la wapiganaji chipukizi.
Mkali huyo alisema amekuwa akiendelea kujifua vema ili kuweza kukkabili Oswald aliyekiri ni mmoja wa mabondia bora na wenye uwezo mkubwa katika mchezo huo.
"Naendelea kujifua kwa lengo la kutaka kumshinda Oswald ambaye namheshimu kwa umahiri wake katika mchezo wa ngumi, naamini nikizembea anaweza kunitoa nishai," alisema Kaseba.
Katika hatua nyingine, bondia Stan Kessy anatarajiwa kupanda ulingoni Septemba 25 kupigana katika pambano lisilo la ubingwa dhidi ya Seleman Habib, ambalo litasindikizwa na michezo mitano tofauti ya utangulizi.
Mratibu wa pambano hilo litakalofanyikia kwenye ukumbi wa Friend's Rangers jijini Dar es Salaam, Dk John Magambo, alisema Kessy na Habib watapigana kwenye uzani wa middle raundi 10 na kusindikizwa na mabondia wengine.
Dk Magambo aliwataja watakaowasindikiza wawili hao ni Salehe Mkalekwa atayaepigana na Jafari Majiha, Doto KIpacha dhidi ya Jones Godfrey, Yohana Thobias atayepigana na Huseni Mashaka na Omar Rajab dhidi ya Husseni Mandula.

Mwisho

UAE embassy used US$ 80,000 for Tanzania Moslems



The United Arab Emirate (UAE) embassy in the country through its charity organization Khalifa Bin Zaayid Al Nahyaan has set aside $80.000 to provide food and other necessities to Muslims in the country during this holly months of Ramadhan.
Disclosing this, Abdallah Ahmedna, who represented UAE ambassador to the country, Mallalla Mubarak Al –Ameri he said the money has been set aside to help people during this month of ramadhan, he said it’s the traditional of his embassy to help people especially this holly months.
He was speaking this at a futari provided by his embassy at Anwar mosque in Msasani.
“This is the fourth year for our embassy through Khalifa Bin Zaayid Al Nahyaan to provide food and money to people during this month of ramadhan” he said
Ahmedna also disclosed that from tomorrow his embassy will start giving out money to the elderly, the disabled and other less privileged people, he said the money will help them to buy food and other necessities at Eid El Fitry .
He disclosed that the exercise will begin at Al Rahman mosque in Kinondoni

Ubalozi watumia Dola 80,000 kufuturisha waislam Tz




UBALOZI wa Nchi ya Falme za Kiarabu, UAE nchini kupitia taasisi ya kutoa huduma za kijamii ya Khalifa Bin Zaayid Al Nahyaan, umekuwa ukitumia Dola za Kimarekani 80,000 kila mwaka kufutisha waumini wa kiislam waliopo jijini Dar na mikoa mingine.
Taarifa hiyo ilitolewa juzi na Mhasibu wa Ubalozi huo, Abdallah Ahmedna, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kwa niaba ya Balozi wa UAE, Sheikh Mallalla Mubarak Al Ameri wakati wa kuwaturusiha waumini wa msikiti wa Anwar, Msasani.
Ahmedna, alisema fedha hizo zimekuwa zikitolewa karibu mwaka wa nne sasa na ubalozi wao kwa ajili ya kuwafuturisha na kuwasaidia waumini wa misikiti 10 iliyopo mikoa ya Dar es Salaam, Morogoro, Lindi, Mwanza, Tanga, Pwani na Mtwara.
Alisema, msaada huo wa futari, daku na fedha kwa wasiojiweza hutolewa kwa muda wa mwezi mzima wa mfungo wa mwezi wa Ramadhani kila mwaka, ambapo kwa Dar mbali na msikiti wa Anwar mwingine unaonufaika ni Al Rahman, uliopo Kinondoni.
"Kama waislam tumekuwa tukithamini waumini wa Tanzania kwa kuwafuturisha pamoja na kuwapa misaada, ambapo ubalozi umekuwa ukifadhili misaada hiyo kwa kiasi cha Dola za Kimarekani 80,000 kwa kila mwaka," alisema.
Baadhi ya waumini waliofuturishwa msikiti hapo waliushukuru ubalozi huo na kuomba watu wengine wenye uwezo kuiga mfano huo wakidai mwezi huu ndio wa waumini wa kweli kuonyesha upendo, ukarimu na kuhurumiana katika kutekeleza nguzo ya nne kati ya tano za Imani za Kiislam.

Mwisho

Sekretarieti ya CCM yashtukiwa, ila Nape mmmh!



WASOMI wa Vyuo vya Elimu ya Juu wanaokiunga mkono chama tawala, CCM, wamemtaka Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye asitishwe na kauli za watu wachache katika kuendeleza moto aliouanza dhidi ya vigogo wanaoatakiwa kujivua gamba wakiapa kumuunga mkono kwa hali yoyote.
Kadhalika wanachama wa CCM hasa vijana wajipange na kujitokeza kwa wingi kuwania nafasi za uongozi ndani ya Jumuiya ya chama hicho, ili kuleta mabadiliko yatakairejeshea heshima chama hicho mbele ya wananchi.
Katibu wa Shirikisho la Wana-CCM Vyuo vya Elimu ya Juu mkoa wa Dar es salaam, Asenga Abubakar, alitoa kauli hizo juzi kupitia taarifa aliyoitoa kwa vyombo vya habari akizungumzia kufifia kwa moto ulioanzishwa na Sekratarieti ya chama chao.
Abubakar, alisema moto ulioanzishwa na sekretarieti ya chama hicho chini ya Katibu Mkuu, Wilson Mukama, ni kama imefifia na hasa zile kelele zilizokuwa zikitolewa na Nape Nnauye, wakidai huenda zimetokana na vitisho vinavyotolewa dhidi yao.
Hata hivyo shirikisho hilo lilimtaka Nnauye, kutohofia vitisho hivyo na badala yake aendeleze moto zaidi ili kuhakikisha chama cgao kinasimama imara dhidi ya wachache wanaoutolea macho nafasi ya Urais kwa Uchaguzi Mkuu ujao wa mwaka 2015.
"Tunamuomba asitishwe na wanaoutolea macho uraisi wa 2015 na wafuasi wao, sisi tunamuonga mkono na tupo pamoja nae dhidi ya wachache hao wenye njaa," taarifa hiyo ya Abubakar inasomeka hivyo.
Taarifa hiyo ya Abubakar, licha ya kuihimiza sekretarieti hiyo kusimama imara, pia imewaomba na kuwataka wanachama wa CCM waliopo vyuoni na vijana kwa ujumla kujitokeza kwa wingi kuwania nafsi katika uchaguzi mkuu wa chama hjicho utakaofanyika mwakani, ili kuleta mabadiliko mbele ya umma wa Watanzania.
Kadhalika shirikisho hilo limesisitiza kwa kuwataka vijana wasiamini kwamba ndani ya CCM kuna ufisadi, bali wafuasi wachache wa chama hicho ndio wenye vitendo hivyo na hivyo wakijitokeza kushiriki uchaguzi watasaidia kurahisisha dhana ya kujivua gamba na kukifanya CCM kiwe makini nchini.
Kwa muda mrefu ndani ya CCM kumekuwa na msigano wa shinikizo la kuwataka baadhi ya wanachama wao wanaotuhumiwa kwa vitendo vya ufisadi kujivua gamba, kitu kilichomlazimisha aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Igunga, Rostam Aziz kung'atuka.
Wengine wanaotuhumiwa kwa vitendo hivyo walipewa muda hadi mwezi ujao kuamua mwenyewe kufuata mkumbo wa Rostam au wang'olewe kwa nguvu.

Wasomi CCM, wamlilia Kikwete avunje ukimya kwa yanayoendelea nchini



RAIS wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzaania, Dk Jakaya Kikwete ametakiwa kutekeleza kwa vitendo dhana ya uwajibikaji kwa kuwatimua kazi mawaziri ambao wizara zao zimekumbwa na kashfa ikiwemo wa Nishari na Madini na ile ya Maliasili na Utalii.
Aidha serikali imeombwa kuchukua hatua ya haraka katika kutatua matatizo yaliyopo katika sekta ya elimu ikiwemo suala la kutimuliwa kwa wahadhiri na kusimamishwa kwa wanafunzi wa vyuo vikuu vya Dodoma, UDOM, taasisi ya IMTU na Chuo cha Ustawi wa Jamii.
Wito huo umetolewa na Shirikisho la Wana-CCM Vyuo vya Elimu ya Juu mkoa wa Dar es Salaam, katika mkutano wa viongozi wake na waandishi wa habari uliofanyika juzi jijini humo.
Mwenyekiti wa Shirikisho hilo, Lusekelo Mwandemange, alisema bila Rais Kikwete kufanya maamuzi magumu katika utekelezaji wa vitendo dhana ya uwajibikaji ni wazi serikali yake itaendelea kupoteza sifa mbele ya wananchi.
Mwandemange alisema kwa kuwa dhana ya uwajibikaji ipo ndani ya CCM tangu enzi za Hayati Baba wa Taifa, Mwl Nyerere, katika kulinda maadili ya viongozi ni vema Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM Taifa akatekeleza kwa kuwawajibisha baadhi ya watendaji wake.
Mwenyekiti huyo alisema kwa kashfa zilizoikumba wizara za Nishati na Madini na ya Maliasili na Utalii za kusimamishwa baadhi ya watendaji wake haipaswi kuachwa kwa wahusika tu bila mawaziri wanaoziongoza wizara hizo kuwajibishwa kwa yaliyotokea.
Mwandemange alisema ni vigumu wananchi kuielewa serikali kama watu waliovurunda mambo serikalini wakapewa likizo za malipo na kurejeshwa kinyemela kwa bashasha kama mashujaa, wakati wanafunzi wanaosimama kutetea haki zao wakitimuliwa vyuoni bila huruma yoyote.
"Tunamuomba Mwenyekiti wetu wa CCM ambaye ndiye Rais wa Jamhuri, afumbe macho na kuwapiga chini (kuwaondoa) viongozi wote dhaifu serikalini, bila kufanya hivyo hatutaweza kurudisha taswira nzuri ya serikali na chama mbela ya wananchi," alisema Mwandemange.
Aliongeza pia kwa kulipongeza Bunge la Jamhuri kwa uamuzi wa kuunda Tume ya

kuchunguza upya sakata la katibu wa wizara ya Nishati na Madini, akiiomba Tume hiyo isiishie kwa David Jairo, bali iimulike wizara nzima pamoja na wizara nyingine za serikali zilivurunda.
"Tume hiyo ichunguze kashfa ya wizara ya Maliasili na Utalii ambayo waziri wake, Ezekiel Maige aliwasimamisha watendaji wake akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Wanyama Pori nchini, Obed Mbangwa bila mwenyewe kuwajibika kwa hilo," alisema.
"Kwa hili tunashangaa waziri anaendelea kukalia kiti kwa kuwasimamisha kazi watendaji wake kwa staili ile ile ya Jairo, alikuwa wapi siku zote hadi wabunge walipofichua, lazima naye awajibike, ndio maaana tunamkata Rais avunje ukimya kwa kuwajibisha wahusika," aliongeza.
Shirikisho hilo liligusia matatizo ya sekta ya elimu yaliyopo katika baadhi ya vyuo vikuu nchini kwa kuitaka serikali ichukue hatua za haraka kuyatatua, licha ya kuipongeza kwa uamuzi wa kuongeza posho za wanavyuo kutoka Sh 5,000 hadi kuwa Sh 7,000.
Uongozi wa shirikisho hilo kupiotia taarifa yao iliyosainiwa na Katibu Mkuu wao, Asenga Abubakar, umesema hawakubaliani na maamuzi ya fedha za mikopo kupelekwa moja kwa moja vyuoni badala ya Bodi ya Mikopo kama zamani wakidai itazidisha matatizo.
Pia waliiomba serikali kuwarejesha wanafunzi na wahadhiri walitimuliwa na kusimamishwa vyuo vya Chuo cha Ustawi wa Jamii, taasisi ya IMTU na UDOM, wakidai kinachofanywa dhidi yao ni uonevu aliodai kama shirikisho hawaridhiki nayo.

Monday, August 8, 2011

RITA yaingilia kati mgogoro wa Answar Sunna

WAKALA wa Usajili, Ufilisi na Udhamini nchini, RITA, umewataka waumini wa Jumuiya ya Answar Sunna Tanzania wanaoshinikiza uongozi wa juu ya jumuiya hiyo ung'oke madarakani kutulia hadi watapotoa maamuzi yao mwishoni mwa mwezi huu.
Waumini hao wa Answar Sunna wanataka uongozi wao ung'oke kwa kukiuka katiba na kushindwa kuiendesha kwa mafanikio jumuiya yao inayotajwa ni taasisi kubwa ya pili nchini baada ya Baraza Kuu la Waislam Tanzania, BAKWATA.
Meneja wa Ufilisi na Udhamini wa RITA, Linna Msanga Katema, aliiambia MICHARAZO kuwa, ofisi yao inatambua kuwepo kwa mgogoro ndani ya jumuiya hiyo baina ya waumini na uongozi wao na wanaendelea kuufanyia kazi.
Linna, alisema hatua waliyofikia katika kuutatua mgogoro huo ni vema waumini kupitia kamati yao maalum wakavuta subira ili waweze kutoa maamuzi mwishoni mwa mwezi huu baada ya kukutana na kupitia vielelezo vya pande hizo mbili.
Meneja huyo, alisema tofauti na hapo awali walipokuwa wakikosa ushirikiano toka kwa viongozi wanaolalamikiwa wakiwemo Baraza la Wadhamini na Amiri wa Jumuiya hiyo, Sheikh Juma Poli, sasa mambo ni shwari na ndio maana wanataka waumini watulie.
"Tumeshawaandikia barua kuomba watupe muda wa mwezi mmoja toka Julai 26 hadi Agosti 26, ili RITA tutoe maamuzi juu ya kinachoendelea baina ya pande hizo mbili, hivyo tunaomba waumini watulie haki itatendeka," alisema Linna.
Nao waumini hao waliofanya mkutano wao Jumapili iliyopita walitoa maamuzi ya kuvuta subiri ili kuona RITA itaamua nini, lakini wakisisitiza wanataka haki itendeke kwa manufaa ya jumuiya yao waliyodai inazidi kudumaa kutokana na uongozi uliopo.
Wakizungumza kwenye mkutano huo waumini hao waliutaka uongozi wa kamati yao inayoongozwa na Mwenyekiti wake, Hamis Buguza na Katibu, Abdulhafidh Nahoda, kuendelea kufuatilia kujua RITA itaamua kitu gani na wao wameamua kuvumilia.
Mzozo wa waumini na uongozi wa jumuiya hiyo ulianza tangu mwaka juzi kutokana na madai ya ukiukwaji katiba ikiwemo kutoitishwa kwa mikutano kwa muda wa miaka 10, pamoja na kubinafsishwa mali za jumuiya hiyo bila waumini hao kushirikishwa.
Katibu wa Baraza la Wadhamini wa Jumuiya, Abdalla Lihumbi, alinukuliwa na gazeti hili wiki iliyopita akikiri uongozi wao kwenda kinyume akidai wanafanya mipango ya kupata suluhu kwa manufaa ya jumuiya yao iliyotambuliwa kitaifa mwaka 1992.

Mwisho

Simba Day ni leo Arusha, uhondo wapungua




KUHAMISHWA kwa tamasha la klabu ya Simba, 'Simba Day' kupelekwa jijini Arusha kumevuruga baadhi ya ratiba zilizokuwa zimepangwa, ingawa uongozi umesema kila kitu kipo sawa na kwamba leo watatambulisha rasmi kikosi chao kipya cha msimu huu jijini humo.
Tamasha hilo linalofanyika kwa mwaka wa tatu mfululizo, awali lilipangwa kufanyika jijini Dar es Salaam, lakini limekwama baada ya kukosekana muafaka wa malipo baina ya uongozi wa klabu hiyo na ule unaosimamia uwanja wa Taifa, na kulazimika kupelekwa Sheikh Amri Abeid.
Kutokana na kuhamishwa huko mkoani Arusha, baadhi ya mambo yaliyotarajiwa kufanyika leo kama pambano la timu za vijana za Simba na Azam U20 limefutwa na badala yake itachezwa mechi ya timu ya veterani ya Arusha dhidi ya viongozi wa Simba.
Kadhalika, bendi na vikundi vilivyokuwa vitumbuize katika tamasha hilo, pia vimeshindikana sawa na tukio la utoaji wa tuzo za wadau walioisaidia Simba kwa hali na mali, ambapo kesho watapewa wachache watakaobahatika kwenda jijini Arusha na wengine watatangazwa tu.
Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, aliiambia MICHARAZO, kuwa pamoja na hali iliyotokea iliyowatatiza kidogo, kila kitu kinatarajiwa kufanyika kwa ufanisi leo ambapo timu yao itakitambulisha rasmi kikosi chao kipya chenye wachezaji wapya wa kimataifa.
"Ni kweli kuhamishwa kwa tamasha hili toka Dar hadi Arusha kumevuruga baadhi ya mambo, lakini kila kitu kipo sawa na wakazi wa Arusha watarajie burudani ya kutosha kwani mambo yamerekebishwa, ili kufanikisha tamasha hilo," alisema Kamwaga.
Kamwaga, alisema kikosi chao tayari kipo jijini humo tangu Ijumaa kikijifua kabla ya leo kuvaana na Simba ya Uganda iliyotarajiwa kutua jana na kusafiri kwenda Arusha kwa ajili ya mechi hiyo ya kirafiki ya kimataifa.
Alisema kikosi chao kipo kamili ukiondoa Mwinyi Kazimoto anayeendelea kujiuguza majeraha yake aliyopata siku ya mechi ya fainali ya Kombe la Kagame kati ya Simba na Yanga, huku wachezaji wengine wawili, Ulimboka Mwakingwe na Amri Kiemba wakirejea toka majeruhi.
Kamwaga alisema watatumia tamasha hilo na hasa mechi yao na Simba ya Uganda kupima kikosi chao kabla ya kuvaana na Yanga wiki ijayo katika pambano la Ngao ya Jamii ikiwa ni uzinduzi wa msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Simba na Yanga zinatarajiwa kuvaana Agosti 17 katika pambano litakalofanyika kwenye uwanja wa Taifa, ikiwa ni wiki kadhaa tangu timu hizo kukutana kwenye fainali hizo za kombe la Kagame na Yanga kuibuka mshindi wa bao 1-0 lililofungwa na Mghana Kenneth Asamoah.

Mwisho

Villa Squad yahaha kusaka Mil 7.2 kuianza Ligi Kuu

UONGOZI wa klabu ya soka ya Villa Squad inahaha kusaka kiasi cha Sh. Milioni 7 kwa ajili ya kuiwezesha timu yao kwenda kuianda Ligi Kuu Tanzania Bara 2011-2012 ugenini Kanda ya Ziwa, huku aliyekuwa mlezi wao, Abdalla Bulembo akisisitiza kujiweka kando katika uongozi.
Villa iliyorejea kwenye ligi hiyo baada ya kushuka daraja mwaka 2008, imepangwa kuanza mechi zake kwa kucheza na Toto Afrika siku ya uzinduzi wa ligi hiyo Agosti 20 kabla ya kuivaa Kagera Sugar ndipo irejee Dar es Salaam kucheza mechi za nyumbani.
Habari za ndani za klabu hiyo zilizothibitishwa na uongozi wake zinasema kuwa, kwa bajeti ya haraka inayotakiwa kwa timu hiyo kwenda kucheza mechi hizo mbili za awali za Ligi Kuu inahitajika kiasi cha Sh. Milioni 7.2 ambazo klabu haijui itazipata wapi kwa sasa.
Katibu wa Villa, Masoud Yasin, alisema kinachowachanganya zaidi ni kuchelewa kutolewa kwa fedha toka kwa wadhamini ambazo kwa kawaida hupitia Shirikisho la Soka Tanzania, TFF na kutoa wito kwa wadau wa soka wa Dar es Salaam hasa wakazi wa Kinondoni kuwasaidia.
"Tunaomba wadau wa soka watusaidie ili Villa tuweze kuianza ligi kwa umakini kwani tuna hali mbaya ya kiuchumi, na hasa kuzisaka fedha hizo kwa ajili ya mechi hizo mbili za kanda ya Ziwa ambapo bajeti yake ni zaidi ya Sh. milioni saba," alisema katibu huyo.
Yasin, alisema hali yao kiuchumi ni mbaya na hawajui watafanyaje katika ushiriki wao hasa baada ya mlezi wao, Abdalla Bulembo kujiweka kando akikataa hata kuzishika nafasi ambazo zipo nje ya katiba yao kama pendekezo lililotolewa na Rais wa TFF, Leodger Tenga.
Tenga alitoa pendekezo hilo wakati akitatua sakata la kuenguliwa kwa Bulembo kuwania Uenyekiti wa Villa na kuibua mtafaruku kabla ya kutulizwa kwa uchaguzi huo kufanyika kwa kuachwa wazi nafasi zilizokosa wagombea wake ikiwemo hiyo ya Mwenyekiti.
Bulembo mwenyewe alipotafutwa na gazeti hili, alikiri ni kweli hana haja ya uongozi baada ya TFF kumwekea kauzibe, ingawa alisema anasikitika na hali inayoendelea na viongozi wa soka nchini kushindwa kuonyesha dhamira ya kweli ya kuinua mchezo huo kupitia klabu ndogo.
"Sitaki hata kusikia habari za kuongoza tena, maadam TFF iliamua kunikwamisha basi mie naendelea na shughuli zangu, ila sidhani kama viongozi wa soka nchini wanania ya kuinua mchezo huu," alisema Bulembo.
Villa ni miongoni mwa timu nne zilizopanda ligi kuu toka daraja la kwanza nyingine zikiwa ni JKT Oljoro Arusha, Coastal Union ya Tanga na Moro United ya Dar es Salaam na tayari TFF imeshatangaza ratiba ya kuanza kwa ligi hiyo Agosti 20 ikishirikisha jumla ya timu 14.

Mwisho

Ubalozi wa UAE wafuturisha waislam Dar

UBALOZI wa Nchi ya Falme za Kiarabu, UAE nchini kupitia taasisi ya kutoa huduma za kijamii ya Khalifa Bin Zaayid Al Nahyaan, umeamua kuwafuturisha waumini wa dini ya kiislam wa Msikiti wa Al Rahman wa Dar es Salaam kwa mwezi mzima wa mfungo wa Ramadhani.
Msaada huo wa futari unaoambatana na tende, ulianzwa kutolewa juzi jioni ambao mamia ya waumini wa msikiti huo walipata fursa ya kufuru chakula hicho kabla ya usiku kugawiwa tende zilizotolewa na ubalozi huo wa UAE.
Imamu wa Msikiti huo wa Al Rahman uliopo eneo la Kinondoni, Sheikh Abdullah Salim Bahssany, akiwahutubia waumini wake wakati wakigawiwa futari hiyo, alisema huo ni msaada toka ubalozi wa UAE na utakuwa ukitolewa hapo kila siku hadi mwezi mtukufu wa Ramadhani utakapomalizika mwishoni mwa mwezi huu.
Imamu huyo aliwaambia waumini hao kuwa wale waliokuwa na shaka na kupata futari katika funga zao, waondoe hofu kwani sasa watakuwa wakipata chakula hicho, huku akiushukuru ubalozi huo kwa ukarimu iliyouonyesha kwa waumini hao.
"Jamani futari mnayokula leo imetolewa na ubalozi wa nchi za Falme za Kiarabu na msaada huu utakuwa ukitolewa kwa mwezi mzima katika mfungo huu wa Ramadhani hivyo msiwe na hofu katika funga zenu,"alisema Sheikh Bahssany.
Baadhi ya waumini waliofuturishwa msikiti hapo waliushukuru ubalozi huo na kuomba watu wengine wenye uwezo kuiga mfano huo wakidai mwezi huu ndio wa waumini wa kweli kuonyesha upendo, ukarimu na kuhurumiana katika kutekeleza nguzo ya nne kati ya tano za Imani za Kiislam.

Mwisho

Kondoo mwenye maandishi ya kiarabu azaliwa Kilimanjaro


KONDOO MWENYE MAANDISHI WA KIARABU YANAYOTAFSIRIKA 'YASIN' AKIWA KANDO YA MAMA YAKE PICHA KWA HISANI WA BLOG YA BURUDAN

Sunday, July 31, 2011

Uongozi wakana kumpa Nyagawa umeneja Simba



UONGOZI wa klabu ya soka ya Simba umekanusha taarifa kwamba umempa cheo cha umeneja kiungo wake iliyomtema kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania, Nico Nyagawa.
Nyagawa, aliyekuwa nahodha wa klabu hiyo ametemwa kwenye usajili wa kikosi kipya kitakachoitumikia timu hiyo msimu ujao, huku kukiwepo na taarifa kwamba kiungo huyo amekula shavu la kuteuliwa kuwa meneja wa timu hiyo.
Klabu ya Simba kupitria Afisa Habari wake, Ezekiel Kamwaga, alikanusha madai hayo ya kumpa Nyagawa umeneja, akisema cheo hicho bado kipo kwa King Abdallah Kibadeni, licha ya kukiri ni kweli wamemuacha mchezaji huyo kwa msimu ujao.
"Nyagawa hajapewa umeneja, ingawa ni kweli ametemwa kwenye orodha mpya ya kikosi cha Simba kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara," alisema Kamwaga.
Alisema kwa sasa uongozi wao unaangalia namna ya kumpa kazi nahodha wao huyo, kwa vile bado anaye mkataba na klabu hiyo hadi mwakani.
Alipoulizwa madai kwamba mchezaji huyo amekuwa akitaka kulipwa haki zake ili atimke zake kimoja Msimbazi, Kamwaga alisema hizo ni taarifa za uzushi kwa vile Nyagawa mwenyewe hajawahi kuueleza chochote uongozi juu ya jambo hilo hadi alipoongea na Sema Usikike.
"Hizo ni taarifa za uzushi tu, tulishazungumza na Nyagawa na ndio maana tunasema tupo katika mipango ya kumpa majukumu ndani ya Simba, " alisema.
Nyagawa aliyesajiliwa na Simba msimu wa 2005-2006 akitokea Mtibwa Sugar anatajwa kama mmoja wa wachezaji wenye nidhamu ya hali ya juu wa soka nchini, ingawa amekuwa na bahati mbaya ya kutoitwa mara kwa mara katika kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars.


Mwisho

Yanga yawatoa hofu mashabiki *Ni juu ya kutoweka kwa 'Diego'




UONGOZI wa klabu ya soka ya Yanga umewatoa hofu wanachama na mashabiki wake juu ya taarifa kwamba mshambuliaji wao nyota kutoka Uganda, Hamis Kizza 'Diego' ametoweka.
Kiza aliyeng'ara kwenye michuano ya Kombe la Kagame na kuibebesha taji mabingwa hao wa Tanzania Bara, ndiye aliyekuwa hajaripoti katika kambi ya timu hiyo inayojiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara pamoja na mechi ya Ngao ya Hisani dhidi ya Simba.
Afisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu, alisema hakuna ukweli kuwa Kizza 'amepeperuka' Jangwani kama inavyovumishwa, ila nyota huyo alikuwa na matatizo ya kifamilia na kwamba angewasili mwishoni mwa wiki.
Sendeu, alisema kama mshambuliaji huyo asingekuwa mali yao jina lake lisingekuwa kwenyue orodha ya wachezaji wapya wa kikosi chao, pamoja na kuitumikia Yanga kwenye michuano ya Kombe la Kagame ambapo walifanikiwa kutwaa taji ikiwa ni mara yao ya nne tangu 1974.
"Ni kweli Kizza amechelewa kuja, lakini haina maana ndio kaingia mitini kama baadhi ya vyombo vya habari vinavyotaka kupotosha, tunadhani atawasili kabla ya Jumapili," alisema.
Aidha, Sendeu, alisema wameamua kukacha kucheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya timu za Coastal Union na Azam kutokana na walioziratibu kushindwa kufanya mawasiliano na uongozi wao kulingana na programu za benchi lao la ufundi.
"Hizo mechi tulikuwa tukizisikia tu redio na kwenye vyombo vingine vya habari, lakini uongozi haukuwa na taarifa nazo na ndio maana tumeamua kuachana nazo, kwani tunahisi kuna ujanja ujanja uliokuwa ukifanyika hasa mechi ya Coastal," alisema Sendeu.
Yanga wanaoendelea kujinoa jijini Dar chini ya makocha wake, Sam Timbe na Fred Felix 'Minziro' walitangaza kufuta mechi hizo zilizokuwa zichezwe mwishoni mwa wiki katika miji ya Tanga na Dar es Salaam.

Tamasha la Simba Day usipime!




BURUDANI mbalimbali za muziki na pambano la kirafiki la kimataifa litakaloihusisha wawakilishi wa Uganda kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika zinatarajiwa kupamba tamasha la soka la klabu ya Simba, 'Simba Day' litakalofanyika Agosti 8 jijini Dar es Salaam.
Wawakilishi hao wa Uganda, Simba Fc inayomilikiwa na Jeshi la nchi hiyo ndiyo watakaokuja kupamba tamasha hilo, ambalo pia litashuhudia timu ya Simba U23, ikikwaruzana na Azam katika kunogesha shamrashamra hizo.
Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, aliiambia MICHARAZO kuwa, tamasha lao litapambwa na burudani za muziki toka kwa bendi mbalimbali za muziki wa dansi na wasanii wa muziki wa kizazi kipya ambao hata hivyo hakuwataja.
Kamwaga alisema shamrashamra hizo za burudani ya muziki zitafuatiwa siku hiyo na utoaji wa tuzo za heshima kwa wadau wa Simba wakiwemo wachezaji, makocha na viongozi wa zamani walioisaidia klabu yao tangu ilipoanzishwa pamoja na wale wanaoisaidia sasa klabu hiyo.
"Karibu kila kitu kimekaa vema kwa sasa ikiwemo kuthibitishwa kwa Simba ya Uganda kuja nchini kucheza nasi katika tamasha hilo, ambalo kabla ya pambano hilo kutakuwa na burudani za muziki na pambano la timu za vijana za Simba na Azam," alisema Kamwaga.
"Mbali na burudani hizo pia tutatoa tuzo za heshima kwa wadau wetu katika namna ya kukumbuka na kushukuru mchango wao," alisema Kamwaga.
Kuhusu maandalizi yao ya mechi yao ya Ngao ya Hisani iliyoapngwa kucheza Agosti 17, Kamwaga alisema yanaendelea vema ikiwemo kikosi chao kuendelea kujifua kwa mazoezi pamoja na kucheza kadhaa za kirafiki visiwani Zanzibar.
Alisema wana imani kubwa ya kufanya vema kwenye pambano hilo dhidi ya Yanga pamoja na kwenye msimu mpya wa ligi kuu utakaoanza wiki moja baada ya pambano hilo la Ngao ya Hisani.
Simba ina deni la kulipa kisasi kwa Yanga iliyowafunga kwenye mechi kama hiyo msimu uliopita kwa mikwaju ya penati na kipigo ilichopata kwenye fainali za Kombe la Kagame lililochezwa hivi karibuni jijini Dar es Salaam ambapo Mghana Kenneth Asamoah waliwaliza.
"Hatuna shaka na mechi zetu zijazo kutokana na maandalizi tuliyofanya huko Zanzibar," alisema Kamwaga aliyechukua nafasi hiyo hivi karibuni akimrithi, Clifford Ndimbo.

Mwisho