STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, July 27, 2011

Banka aishtaki Simba kwa TFF




KIUNGO Mohammed Banka ameishtaki klabu yake ya Simba kwa Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, juu ya sakata lake la kutaka kupelekwa kucheza kwa mkopo katika timu ya Villa Squad bila ridhaa yake.
Banka, aliyeichezea Simba kwa mafanikio tangu ilipomsajili baada ya kutemwa na Yanga, msimu wa 2008-2009, alisema ameamua kuchukua maamuzi huo kutokana na kuona viongozi wa Simba wanamzungusha kuhusu suala la uhamisho wake.
Mwanasheria aliyepewa kazi ya kumpigania Banka, John Mallya, aliiambia MICHARAZO jana kuwa, wameandika barua Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, ili kuingilia kazi suala la mteja wao kabla ya hatua zingine za kisheria kufuata.
Mallya, alisema wameamua kuandika barua hiyo, TFF kutokana na kuona viongozi wa Simba wanakwepa kukutana kulimaliza suala la Banka, kutokana na wenyewe kukiuka mkabata baina yao na mchezaji huyo kama sheria zinavyoelekeza.
Alisema walikuwa katika mazungumzo mazuri na viongozi wa klabu hiyo, lakini juzi walipopanga kukutana ili kulimaliza suala hilo, wenzao walishindwa kutokea na kuona ni vema waombe msaada TFF, kabla ya kuangalia cha kufanya kumsaidia mteja wao.
Afisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alikiri kupokewa kwa barua hiyo ya ombi la Banka kutaka shirikisho lao kuingilia kati na kudai itapelekwa kunakohusika kufanyiwa kazi.
"Ni kweli barua hiyo imefika kwetu, Banka akiomba TFF iingilie kati sakata lake la Simba," alisema Wambura.
Naye Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alikiri kuwepo kwa mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea baina ya pande hizo mbili, ingawa alisema alikuwa hajaipata nakala ya barua hiyo ya malalamiko ya Banka iliyopelekwa TFF.
"Hilo la kushtakiwa TFF, silijui kwani sijapata barua, pia siwezi kuliongelea kwa undani kwa vile lilikuwa linashughulikiwa na viongozi wa juu, ambao kwa bahati karibu wote wameenda Uturuki kushughulikia suala la ujenzi wa uwanja," alisema.
Banka, amekuwa akisisitiza kuwa kama Simba haimhitaji ni bora mlipe chake aangalie ustaarabu wake kuliko kumlazimisha kwenda Villa Sqaud iliyorejea ligi kuu msimu huu.

Mwisho

Bingwa wa Kick Boxing Kenya atua Bongo kuzipiga




BINGWA wa Kick Boxing kutoka Kenya, Rukia Kaselete ametua nchini tayari kwa ajili ya pambano lake dhidi ya Mtanzania Jamhuri Said, watakaosindikiza pambano la nani mkali kati ya Amour Zungu wa Zanzibar na Mchumia Tumbo wa Tanzania Bara.
Michezo hiyo iliyoandaliwa na Bingwa wa Dunia wa Kick Boxing anayeshikilia mikanda ya WKL na WKC, Japhet Kaseba inatarajiwa kucheza siku ya Jumamosi kwenye ukumbi wa DDC Keko, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Kaseba, alisema maandalizi ya michezo hiyo kwa wastani inaendelea vema ikiwemo mabondia wote kuwasili jijini akiwemo mkenya huyo atakayepigana na Jamhuri kusindikiza pambano la Zungu na mwenzake.
Kaseba alisema mabondia wote watakaoshiriki michezo hiyo ya Kick Boxing na Ngumi za Kulipwa wanatarajiwa kupimwa afya zao siku ya Ijumaa kwenye gym yake, iliyopo eneo la Mwananyamala jijini Dar es Salaam.
"Kwa kweli kila kitu kinaenda vema ikiwemo mabondia wote kuwasili Dar tayari kwa ajili ya michezo hiyo ya Jumamosi, ambapo Amour Zungu atazipiga na Mchumia Tumbo katika pambano la kusaka mkali kati yao," alisema Kaseba.
Kaseba alisema mbali na pamoja ya pambano la Kaseleta na Jamhuri, siku hiyo pia kutakuwa na michezo mingine ya utangulizi ambapo wanadada Asha Abubakar wa Kisarawe na Fadhila Adam wa Dar wataonyeshana kazi kwenye kick boxing.
"Wengine watakaopigana siku hiyo ni kati ya Dragon Kaizum dhisi ya Faza Boy, Idd na Dragon Boy na Lion Heart ataonyeshana kazi na Begeje," alisema.
Aliongeza pambano la ngumi za kulipwa zitawakutanisha wakongwe wa mchezo huo, Ernest Bujiku dhidi ya Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo'.

Mwisho

Viongozi Simba waenda kumalizana na Waturuki



VIONGOZI wa klabu ya soka ya Simba wameondoka nchini juzi kuelekea Uturuki kwa ajili ya kwenda kumalizia taratibu za ujenzi wa uwanja wao mpya wa kisasa utakaojengwa eneo la Bunju, nje kidogo ya jijini la Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Afisa Habari wa klabu hiyo, Ezekiel Kamwaga, viongozi walioondoka ni Mwenyekiti Ismail Aden Rage na Katibu wake, Evodius Mtawala.
Kamwaga alisema Rage na Mtawala waliondoka juzi kuelekea nchini humo kufanya mazungumzo ya mwisho na uongozi wa kampuni ya Petroland, ambayo ndiyo itakayoujenga uwanja huo utakaoingiza watazamaji wasiopungua 60,000.
"Viongozi wetu wawili wa juu wameondoka nchini jana, kwenda Uturuki kwa ajili ya kumalizana na watakaotujengea uwanja wetu wa kisasa utakaokuwa eneo la Bunju," alisema Kamwaga.
Afisa Habari huyo, alisema viongozi wao wameenda kuweka mambo sawa kabla ya wakandarasi hao kuja kuanza kazi yao na kuifanya Simba kufuata nyayo za klabu kubwa barani Afrika kama ASEC Memosa au Kaizer Chief zenye viwanja vikubwa vya kisasa.
Uwanja huo utakaokuwa wa kisasa na mkubwa kama ule wa Taifa, utaigharimu Simba kiasi cha Shilingi Bilioni 75 hadi utakapomalizika ukihusisha uwanja wa kuchezea, maduka, kumbi za mikutano na burudani, mbali na hoteli na kituo cha michezo.
Kwa hapa nchini ukiondoa Yanga yenye kuumiliki uwanja wa Kaunda, klabu nyingine yenye uwanja wake mwenyewe ni Azam iliyoujenga eneo la Chamanzi, Mbande nje kidogo ya jijini la Dar es Salaam ambao utaanza kutumika msimu mpya wa Ligi Kuu.

Mwisho

Simba yawaita DCMP Da kumjadili Mgosi




UONGOZI wa klabu ya soka ya Simba, umeutaka uongozi wa timu ya DC Motema Pembe ya DR Congo, kuja jijini Dar es Salaam kuzungumza nao ili waachiwe kiungo mshambuliaji, Mussa Hassani Mgosi vinginevyo imsahau kumpata.
Motema Pembe imeonyesha nia ya kumsajili Mgosi, isipokuwa inamtaka kama mchezaji huru, kitu kinachopingwa na uongozi wa Simba wenye mkataba bao ikidai kama ina ya dhati ya kumnasa mchezaji huyo wake wazungumze mezani waafikiane.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alisema klabu yao ipo tayari kumuacha Mgosi aende DCMP, ila kama uongozi wa klabu hiyo utakuja kuzungumza nao ili kumhamisha kwani ni mchezaji wao halali.
Kamwaga alisema Simba haina nia ya kumbania Mgosi, ila kwa hali ilivyo ni vigumu kwao kumtoa winga huyo bure wakati wana mkataba naye.
Kamwaga, alisema Simba itaona raha iwapo mchezaji huyo atajiunga na DCMP kama ilivyokuwa kwa akina Mbwana Samatta na Patrick Ochan walisajiliwa TP Mazembe, ila wenzake wanamtaka bure kitu kinachowafanya wamzuie hadi kieleweke.
"Kama kweli wana nia na Mgosi waje wazungumze nasi, Mgosi ana mkataba Simba na hivyo hatuwezi kumuachia bure," alisema.
Kamwaga, alisema tayari wameshaifahamisha TFF juu ya msimamo wao na wanasubiri kuona uongozi wa DCMP utafanya nini kuamua hatma ya Mgosi, ambaye jina lake lipo kwenye orodha ya usajili wa klabu ya Simba kwa msimu ujao wa ligi kuu Tanzania Bara.
Alisema kama mipango yake ya kwenda Congo itakwama, Mgosi ataendelea kuichezea timu yao kwa msimu ujao hadi atakapomaliza mkataba utakaoisha mwakani.
Katika hatua nyingine, Kamwaga alisema klabu yao inatarajiwa kuianika timu watakaocheza nao kwenye Tamasha la Siku ya Simba 'Simba Day' litakalofanyika Agosti 8 mwaka huu.
Kamwaga alisema klabu yao ilipeleka maombi kwa klabu tatu za nje ya nchi na leo wanatarajia kutangaza timu watakayocheza nao katika tamasha hilo
"Timu itakayotusindikiza kwenye Simba Day tutaitangaza kesho (leo) pia tutaanika kila kitu juu ya maandalizi ya tamasha hilo," alisema Kamwaga.

Mwisho

Talent Band kutambulisha mpya Sinza

BENDI ya muziki wa dansi ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea' inatarajiwa kuvamia kitongoji cha Sinza ili kuitambulisha albamu yao mpya ya 'Shoka la Bucha'.
Mkurugenzi wa bendi hiyo, Husseni Jumbe, aliambia MICHARAZO jana kuwa, onyesho hilo litafanyika kesho kwenye ukumbi wa Nouvel Social Centre (zamani Rufita) ambapo watatambulisha nyimbo zote zilizopo kwenye albamu hiyo mpya.
Jumbe, alisema onyesho hilo limeratibiwa na Mkurugenzi wa ukumbi huyo aliyemtaja kwa jina la Mamaa Joyce.
"Baada ya kuikamilisha albamu yetu mpya ya Shoka la Bucha, Talent Band, inatarajiwa kuitambulisha albamu hiyo katika onyesho maalum litakaloofanyika siku ya Alhamis kwenye ukumbi wa Nouvel Social Centre," alisema Jumbe.
Jumbe alizitaja nyimbo zitakazotambulishwa kwenye onyesho hilo kuwa ni Shoka la Bucha, Kiapo Mara Tatu, Kilio cha Swahiba na zile za albamu yao ya kwanza ya Subiri Kidogo.
Naye mratibu wa onyesho hilo, Joyce alisema kila kitu kipo sawa na wanachosubiri ni kupata burudani toka kwa Talent.

Mwisho

Tamasha kubwa la sanaa kufanyika Moro

WASANII zaidi ya 100 wa mkoani Morogoro wanatarajia kufanya tamasha kubwa litakaloshirikisha sanaa za aina mbalimbali.
Mratibu wa tamasha hilo lililopewa jina la 'Wakali Concert', Athuman Mswagala 'Mahita' aliiambia Micharazokwa njia ya simu kutoka Morogoro kuwa tamasha hilo litafanyika Julai 30 katika ukumbi wa Vijana Social ulioko mjini hapa.
Mswagala, alisema lengo la tamasha hilo litakalowahusisha wasanii wa mkoa huo wa fani mbalimbali ni kufahamiana na kuibua vipaji vipya.
Alisema maandalizi kwa ajili ya tamasha hilo yanakwenda vizuri na kwamba kinachosubiriwa ni kufanyika kwa tamasha hilo.
Alisema katika tamasha hilo litakalokuwa likifanyika kila mwaka, wasanii watakaofanya vizuri watazawadiwa zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na fedha taslimu.
"Kimsingi, maandaalizi yanakwenda vizuri na wasanii wengi wamethibitisha kushiriki hali ambayo naamini itakuwa burudani tosha kwa wakazi wa Morogoro" alisema.
Naye, mkurugenzi wa kampuni ya Katundu, wanaodhamini tamasha hilo, Mohamed Katundu, alisema kampuni yake imeamua kudhamini tamasha hilo kwa lengo la kusapoti wasanii wa Morogoro.
Katundu alisema hiyo ni moja ya mipango ya kampuni yake kuhakikisha wasanii mkoani hapa wanapata mafanikio makubwa kupitia sanaa mbalimbali.

Saturday, July 16, 2011

Sunzu asaini mkataba wa miaka miwili



MSHAMBULIAJI wa Kimataifa kutoka Zambia, Felix Mumba Sunzu amesaini mkataba wa miaka miwili ya kuichezea klabu ya soka ya Simba kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa.
Makamu Mwenyekiti wa Simba, Godfrey Nyange Kaburu, aliuambia mtandao wa MICHARAZO jana usiku kwamba wameshamalizana na Sunzu na kwamba mchezaji huyo atarejea kwao wakati wakifanya taratibu za uhamisho wake wa kimataifa toka Al Hilal.
"Kila kitu kipo ok, baada ya mkutano mrefu baina yenu amekubali kusaini mkataba wa miaka miwili kuwepo Simba," alisema Kaburu.
Kaburu hakupenda kueleza kwa undani mambo mengine waliyokubaliana na mchezaji huyo.
Kadhalika, Kaburu alikanusha taarifa kwamba wamemnyakua mshambuliaji wa Yanga, Jerry Tegete akidai wanaheshimu mkataba uliopo baina ya Yanga na mchezaji huyo.
"Hizo ni taarifa za mtaani, ila si kweli, mtu ambaye tumemalizana nae ni Sunzu, huyo Tegete wala hatuna mpango nae," alisema.
Pia alisema sio kweli kama beki wao king'ang'anizi, Kelvin Yondan, amewakacha na kwenda Yanga kwa maelezo bado wana mkataba naye, pia kisheria Yanga wanapaswa waonane nao kama ni kweli walimtaka mchezaji huyo.
"taratibu zipo wazi, pia Yondan ana mkataba wa kuichezea Simba sasa ataendaje Yanga, hizi ni nyepesi nyepesi tu ila mchezaji huyo bado yupo Simba, alisema Kaburu.
Katiak hatua nyingine ni kwamba wachezaji wawili, Mohammed Banka na Athuman Idd 'Chuji' huenda wakaichezea Villa Squad kwa mkopo baada ya kuridhiana na Simba juu ya wachezaji hao wanaomudu nafasi ya kiungo.
Viongozi wa Villa waliuambia mtandao huu walikuwa wakimalizana na Simba, lakini hawakuweka kila kitu bayana wakidai watazungumza leo.

Friday, July 15, 2011

Twiga Stars kuanza na Ghana All African Games

SHIRIKISHO la Soka Afrika, CAF, imetangaza ratiba ya michuano ya soka kwa timu za wanawake zinazoshiriki michuano ya Afrika (All African Games) ambapo timu ya taifa ya Tanzania, Twiga Stars itaanza kibarua chake kwa kuumana na Ghana.
Michuano hiyo ya Afrika inatarajiwa kuanza kufanyika Septemba 3-18 kwenye mji wa Maputo, Msuimbiji, ambapo kwa mujibu wa ratiba hiyo ya CAF ni kwamba Twiga iliyopo kundi B itafungua dimba kwa kuumana na Ghana siku ya Septemba 5.
Timu zingine zilizopo katika kundi hilo ni Afrika Kusini na mabingwa wapya wa Kombe la COSAFA, Zimbabwe.
Ratiba hiyo ya CAF inaonyesha kuwa Twiga itashuka dimbani tena Septemba 8 kucheza na Afrika Kusini kabla ya kumaliza mechi zake, Septemba 11 kwa kucheza na Zimbabwe.
Twiga imejikuta kundi moja na timu hizo mbili ambazo ziliichachafya katika michuano ya Kombe la COSAFA, ambapo Afrika Kusini waliokuwa nao kundi moja waliwalaza bao 1-0 kabla ya Zimbabwe kuifunga kwenye mechi ya nusu fainali kwa mikwaju ya penati 4-2.
Timu zingine zitakazoshiriki michuano hiyo na zilizopangwa kundi A ni wenyeji Msumbiji, Cameroon, Algeria na Guinea, ambapo washindi wawili wa kwanza wa kila kundi ndizo zitakazosonga mbele kwa hatua ya nusu fainali.
Nigeria ndiyo waliokuwa mabingwa wa mwaka 2007, lakini hawakufanikiwa kufuzu
kwa michuano hiyo mwaka huu ambayo hufanyika kila baada ya miaka minne.
Wakati huo huo mikoa mitatu ya Dodoma, Mwanza na Ruvuma imeteuliwa kuwa vituo vya kuendeshea semina na mitihani ya utimamu wa mwili (physical fitness test) kwa waamuzi wa daraja la pili na tatu inayotarajiwa kufanyika mapema mwezi ujao.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kupitia Afisa Habari wake, Boniface Wambura, ni kwamba semina na mitihani hiyo itafanyika kwa muda wa siku tatu kuanzia Agosti 2-5 katika vituo hivyo.
Taarifa hiyo inasema washiriki wa semina na mitihani hiyo watajitegemea kila kitu kuanzia gharama za usafiri, chakula na malazi, huku vyama vya soka vya mikoa ya Tanzania Bara vikihimizwa kuwakumbusha washiriki kuhudhuria semina na mafunzo hayo kwa faida yao.
Iliongeza kuwa semina na mitihani hiyo itatumika kuwapandisha daraja washiriki hao.
Hiyo ni semina ya pili kuandaliwa na TFF ndani ya kipindi kifupi ikiwa ni maandalizi na msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara, kwani karibu wiki moja sasa ilikuwa ikiendesha semina kama hiyo inayowahusisha waamuzi wa daraja la IA na IB iliyokuwa ikifanyika katika miji ya Mwanza na Dar es Salaam.
Semina na mitihani hiyo ilianza Julai 13 na inatarajiwa kufungwa leo Julai 16.

Stars kukipiga ughaibuni na Palestina, Jordan

KATIKA kujiweka fiti kabla ya kumaliza viporo vya michezo yake miwili iliyosalia ya kuwania kufuzu Fainali za Afrika za mwaka 2012, timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars inatarajiwa kwenda Mashariki na Kati kucheza mechi mbili za kirafiki za kimataifa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kuopitia Afisa Habari wake, Boniface Wambura inasema, Stars itaumana na timu za mataifa ya Palestina na Jordan mapema mwezi ujao.
Wambura alisema mechi ya kwanza ya timu hiyo inayoshikilia nafasi ya tatu katika kundi D lenye timu za Morocco, Afrika ya Kati na Algeria, itachezwa siku ya Agosti 10 katika mji wa Ramallah dhidi ya wenyeji wao Palestina.
Mechi ya Tanzania na Palestina itakuwa ni kama marudiano, kwani mapema mwaka huu timu hizo zilipepetana hapa nchini katika pambano jingine la kirafiki la kimataifa.
Katika mechi hiyo ilichezwa Februari 9 kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, Stars iliitambia Palestina kwa kuilaza bao 1-0, bado lililofungwa na winga mahiri, Mrisho Ngassa ambaye kwa sasa yupo Marekani kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Seattle Sounders inayoshiriki ligi ya Marekani, MLS.
Wambura aliongeza Stars itashuka tena dimbani Agosti 13 kupepetana na Jordan katika pambano litakalochezwa kwenye mji mkuu wa nchi hiyo ya Jordan, Amani.
Wambura alisema Stars itaondoka nchini Agosti 7 na kikosi cha timu hiyo kinatarajiwa kutajwa mara baada ya kocha mkuu wa timu hiyo, Jan Poulsen kurejea kutoka mapumziko nchini Denmark, mapema mwezi ujao.
Stars inahitaji ushindi katika mechi zake zilizosalia dhidi ya Algeria itakayochezwa nyumbani na ile ya mwisho dhidi ya Morocco, iwapo inataka kufuzu fainali hizo za Afrika zitakazofanyika mwakani katika nchi za Guinea ya Ikweta na Gabon.

Hatimaye Sunzu atua Bongo


MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa timu ya Al Hilal ya Sudan, Felex Sunzu ametua nchini mapema leo tayari kufanya mazungumzo na klabu ya Simba ili kuichezea tyimu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2011-2012.
Sunzu alitua leo asubuhi akiambatana na mkewe na hadi wakati huu alikuwa akiendelea kufanya mazungumzo na uongozi wa Simba ili kuweza kumwaga wino wa kuichezea klabu hiyo.
Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange Kaburu aliyempokea mshambuliaji huyo aliyeng'ara kwenye mihuano ya Kombe la Chalenji iliyofanyika mwishoni mwa mwaka jana akiichezea Zambia, iliyoalikwa amesema wakati wowote wataweka taarifa juu ya kumnasa rasmi mkali huyo.
Kwenye uwanja wa ndege, Sunzu ambaye alikuwa akitokea mapumzikoni nchini Nigeria, alisema amekuja nchini na kama atapata fursa ya kumalizana na Simba basi mashabiki wa timu hiyo watarajie makubwa kutoka kwake muhimu apewe ushirikiano.
Nyota huyo ambaye ameshindwa kuitumikia Al Hilal kwa kiwango stahiki kiasi cha klabu yake kutaka kumtoa kwa mkopo, alisema anazifahamu Simba na Yanga na anaimani atang'ara nchini kama ilivyo kwa mzambia mwenzake Davis Mwape aliyepo Yanga.
Simba inahaha kusaka mshambuliaji wa kuziba nafasi ya Mbwana Samatta aliyenunuliwa na TP Mazembe, ambayo Sunzu anaonekana kama 'muarubaini'wa tatizo la safu butu ya ushambuliaji ya timu hiyo iliyoshindwa kutwaa taji la Kagame kwa kulazwa na Yanga bao 1-0 katika mechi ya fainali baina yao iliyochezwa Jumapili iliyopita.

Rostam Aziz alipobwaga manyanga Igunga



UTANGULIZI

WAZEE wangu, kwanza kabisa kabla ya kueleza kile ambacho kimenisukuma kuzungumza nanyi leo, napenda kuanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kufikia siku hii ambayo inatukutanisha waja wake.

Wazee wangu wa Igunga, baada ya kufanya hivyo napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru ninyi nyote mmoja mmoja na katika umoja wenu kwa kuitikia wito wangu, kijana wenu, niliyewaomba nije nizungumze nanyi siku hii ya leo.

Nafanya hivyo nikitambua vyema kwamba, kama si nyinyi wazee wangu na wengine wengi ambao hatuko nao hapa leo kwa sababu mbalimbali, ambao mmekuwa na imani kubwa nami nisingeweza kufikia hapa nilipofika sasa.

Wazee wangu, waasisi wa taifa letu walitufundisha kutambua na kuheshimu ukweli kwamba; ‘Uongozi ni Dhamana’ dhana ambayo kila ninapokaa na kutafakari huwa inanirejesha nyuma na kukumbuka jinsi nyinyi mlivyokaa katika umoja wenu na kuniteua mimi, miongoni mwa vijana wenu wengi, kuwa mwakilishi wa Jimbo la Igunga tangu mwaka 1994.

Katika kipindi hicho chote cha utumishi wangu, nyinyi wazee wangu mmekuwa mhimili muhimu ambao umeniwezesha kutimiza wajibu wangu kwa bidii kubwa, maarifa na nidhamu ya hali ya juu nikitambua namna ambavyo mmekuwa na imani kubwa juu yangu.

Ari na moyo wa imani, ushirikiano na mshikamano ambao wazee wangu mmekuwa nao kwangu ndiyo ambao kwa kiwango kikubwa umetuwezesha kufanya kazi kwa pamoja, tukishinda changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikilikabili jimbo letu katika kipindi chote ambacho mmeendelea kuniamini kuwa mbunge wenu kwa miaka 18 sasa.

Wakati nikitambua na kuheshimu ukweli kwamba katika kipindi chote cha ubunge wangu mmekuwa na imani kubwa nami na kuniunga mkono kwa dhati, naamini kwamba kwa upande wangu pia nimejitahidi kwa kadiri nilivyoweza, kutimiza matarajio ya wananchi wa Igunga.

Miongoni mwa mafanikio makubwa tuliyoyafikia kupitia ushirikiano wetu na uongozi wa pamoja ni kwamba, mwaka 1994 Igunga ilikuwa ni wilaya ya mwisho kwa maendeleo mkoani Tabora lakini leo ndiyo ya kwanza, taa za barabarani, bima ya afya kwa kila kaya, zahanati kila kijiji na shule nyingi kuliko idadi ya kata zilizomo kwenye wilaya.

Wazee wangu, nayasema haya nikitambua kwamba, kama ilivyo katika maeneo mbalimbali hapa nchini, mafanikio makubwa tuliyoyapata katika nyanja za elimu, afya, makaazi bora na kilimo katika kipindi chote ambacho mmendelea kuniamini kuwa mbunge wenu kwa miaka 18 sasa.

Wakati nikitambua na kuheshimu ukweli kwamba katika kipindi chote cha ubunge wangu mmekuwa na imani kubwa nami na kuniunga mkono kwa dhati, naamini kwamba kwa upande wangu pia nimejitahidi kwa kadiri nilivyoweza, kutimiza matarajio ya wananchi wa Igunga.

Wazee wangu, nayasema haya nikitambua kwamba, kama ilivyo katika maeneo mbalimbali hapa nchini, mafanikio makubwa tuliyoyapata katika nyanja za elimu, afya, makaazi bora na kilimo katika kipindi hicho chote hayajaweza kumaliza changamoto zote za maendeleo ambazo zinatukabili.

Wazee wangu, ingawa nimekuwa na kawaida ya kukutana na kuzungumza nanyi mara kwa mara, mmoja mmoja na wakati mwingine katika umoja wenu, wito wangu wa leo una makusudi ambayo kwa kiwango kikubwa ni tofauti na yale ambayo tumeyazoea.

Japokuwa ujumbe ninaotaka kuzungumza nanyi wazee wangu, si mgeni sana masikioni mwenu, tofauti ya leo na mikutano yetu mingine iliyopita ni uamuzi ambao nimekusudia kuufanya na ambao nitayatangaza muda mfupi ujao.

YATOKANAYO

Wazee wangu, naamini mmekuwa mkifuatilia kwa karibu hali ya siasa nchini na hususani afya ya kisiasa na matukio mengine ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho mimi ni mwanachama wake na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) nikiuwakilisha Mkoa wetu wa Tabora.

Naamini kwamba katika kufuatilia kwenu mtakuwa mmebaini kuwapo kwa matukio ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakitokea huku yakiligusa jina langu na wakati fulani nafasi yangu kama kiongozi wa chama hicho.

Wazee wangu, nayasema hayo kwa sababu mara kwa mara ninapokutana nanyi nikiwa katika ziara zangu jimboni na wakati mwingine mnapowasiliana nami kwa njia mbalimbali mmekuwa mkionesha kuguswa kushitushwa na kutaka kujua kulikoni kuhusu mambo hayo yanayotokea.

Mimi, kama mnavyonijua nyote, ni mtu muwazi na mkweli. Siku zote nimekuwa mwepesi sana wa kuwaeleza kuhusu kila kinachotokea ili kuwaondoa hofu na wakati huo huo kuwahakikishia kwamba masuala yasiyo na msingi hususani yale yanayogusa siasa za kitaifa hayawezi kutuondoa katika mstari sahihi wa kuwahudumia wananchi wa Igunga, mkiwamo nyinyi wazee wangu ambao mmeniamini na kunituma kuwawakilisha.

Nyinyi wenyewe ni mashahidi wazuri kwamba tangu matukio yanayogusa jina langu yaanze kutokea miezi michache tu baada ya Serikali ya Awamu ya Nne inayoongozwa na Rais Jakaya Kikweti kuingia madarakani kwa mara ya kwanza mwaka 2005, tumekuwa tukiyapuuza na tukaendelea kufanya kazi pamoja kwa bidii.

Bado naamini na nitaendelea kuamini kwamba tulifanya uamuzi sahihi wa kuyapuuza matukio hayo kwani mbali ya kuendelea kutimiza malengo mbalimbali yaliyokuwamo katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya CCM, pia mliendelea kuniamini kwa nafasi yangu ya kuwa mwakilishi wenu bungeni na hata mkaniruhusu nibebe jukumu jingine kubwa la kuwa Mjumbe wa NEC ninayewakilisha mkoa wetu wa kihistoria wa Tabora.

Wazee wangu, nyinyi ndiyo watu mnaolifahamu vyema jimbo letu la Igunga na hakika nyinyi ni sehemu muhimu ya watu wanaojua historia ya kisiasa ya Mkoa wa Tabora kwa miaka mingi hata kabla ya kuja kwa mfumo wa vyama vingi hapa nchini.

Hakuna shaka hata kidogo kwamba, Tabora ni kitovu hasa cha uasisi wa siasa za vyama vingi hapa nchini. Ni wazi kwamba huwezi ukazungumzia chimbuko la vyama vya upinzani tunavyoviona hapa nchini leo pasipo kugusa mkoa huu ambao umekuwa chimbuko la wanasiasa wenye mizizi hapa na nchini kwa ujumla.

Majina ya wanasiasa wa aina ya wazee wetu, hayati Chifu Said Abdallah Fundikira na Christopher Kassanga Tumbo, Kasela Bantu (Mungu awalaze mahala pema peponi), James Mapalala, Profesa Ibrahim Lipumba na mengi mengine yana mizizi yao katika Mkoa wetu wa Tabora.

Kutokana na ukweli huo basi ni wazi kwamba, nikiwa Mbunge wa Igunga kwa vipindi vinne mfululizo na wakati huo huo nikiwa Mjumbe wa NEC kwa vipindi vitatu mfululizo, moja ya kazi ambazo nimezifanya kwa uaminifu na kwa bidii kubwa huku nikiungwa mkono na kushirikiana nanyi ni ile ya kuhakikisha kwamba mkoa huu pamoja na kuwa kitovu cha upinzani unaendelea kubakia kuwa ngome muhimu ya kisiasa ya CCM.

Si vibaya tukakumbushana kwamba, wakati nachaguliwa kuwa mjumbe wa NEC wa Mkoa mwaka 1997, jimbo moja katika mkoa wetu lilikuwa likishikiliwa na upinzani. Leo hii Tabora ni mkoa pekee miongoni mwa mikoa iliyotuzunguka ambao haukupoteza jimbo hata moja kwenda upinzani katika Uchaguzi Mkuu wa 2010. Mafanikio haya tuliyafikia kwa pamoja kutokana na ushirikiano wenu wazee wangu.

Wazee wangu, Waswahili wanasema usione vyaelea, vimeundwa. Kazi ya kuijenga CCM katika mazingira yenye mizizi hasa ya upinzani nikiwa mbunge na hususani M-NEC kutoka Mkoa wa Tabora haijapata kuwa rahisi na itaendelea kuwa ngumu na ambayo mapambano yake ni makali sana.

Wazee wangu, kwa namna ya pekee kabisa napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru nyinyi wazee wangu wa Igunga na wananchi wenzangu wote wa Mkoa wa Tabora kwa kushikamana na kuifanya kazi hiyo kwa bidii, uaminifu na mafanikio makubwa.

Matunda ya kazi hiyo kubwa yanaonekana. Pamoja na kuwa kitovu cha kihistoria cha siasa za upinzani, Tabora ndiyo mkoa pekee katika eneo hili ambao unaongozwa na wabunge wote kutoka CCM baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana na hata kabla ya hapo.Kwa sababu hiyo basi, wazee wangu, sote katika umoja wetu ukiacha mafanikio makubwa tuliyopata katika jimbo na Wilaya yetu ya Igunga, tunayo mambo mengine ya msingi ya kujivunia. Kwa moyo wa dhati na kwa unyenyekevu mkubwa napenda kuwapongeza kwa namna mlivyojitoa kukipigania na kukitetea chama chetu kwa ari na nguvu ya kipekee.KUJIVUA GAMBAWazee wangu, chama chetu chini ya uongozi wa Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete kimeamua kwa kauli na nia moja kujitathmini na kufanya mabadiliko makubwa ya kimfumo yenye lengo la kukiwezesha kiendelee kubakia chama kinachoaminiwa na kuungwa mkono na Watanzania walio wengi.Dhamira ya mwelekeo huo wa kufanya mabadiliko ya ndani ya chama chetu ilitangazwa rasmi na Mwenyekiti wetu Rais Kikwete wakati wa kilele cha maadhimisho ya miaka 34 ya kuzaliwa kwa CCM, mjini Dodoma.Katika hotuba yake hiyo, Rais Kikwete aliyafananisha mabadiliko hayo na tabia ya kawaida na ya asili ya nyoka na wanyama wengine kadhaa ya ‘Kujivua Gamba’.Wazee wangu hatua ya kwanza ya utekelezaji wa azimio hilo na mwelekeo huo sahihi ilifanyika mjini Dodoma wakati wa kikao cha Kamati Kuu ya Taifa ya CCM ambacho mimi nilikuwa mjumbe wake.Wakati wa kikao hicho, wajumbe wote wa Kamati Kuu na wale wa Sekretarieti ya chama chetu wa wakati huo kwa kauli moja tulikubaliana kujiuzulu, lengo likiwa ni kumpa Mwenyekiti wetu fursa nzuri ya kufanya mabadiliko ya uongozi yatakayotoa nafasi ya kupata mwelekeo mpya wa Chama.Wazee wangu, tulifanya hivyo tukionesha kuunga mkono kwa asilimia 100 kile ambacho bado naendelea kuamini kuwa ni mawazo sahihi na yenye mwelekeo thabiti ya Mwenyekiti wetu ambayo kwa kiwango kikubwa yalikuwa yakiakisi matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa urais, ubunge na udiwani wa Oktoba mwaka jana.Niliseme kwa maneno machache tu hili. Ingawa ni kweli kwamba Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana umekirudisha madarakani chama chetu kwa kukipa ushindi mkubwa katika uchaguzi wa urais, ubunge na udiwani kwa Tanzania Bara na Zanzibar, kiwango cha ushindi tulichopata kimeonyesha waziwazi dalili za wananchi kupunguza imani yao kwetu kuilinganisha na ilivyokuwa mwaka 2005.Tungekuwa ni chama cha siasa cha ovyo iwapo tungepuuza kupungua kwa kura za rais kutoka zaidi ya asilimia 80 tulizopata mwaka 2005 hadi kufikia aislimia 61 mwaka jana kiwango ambacho ni pungufu kwa asilimia 20 ya kura katika kipindi cha miaka mitano tu, hasa ikizingatia ukweli kwamba mgombea urais ni mtu yule yule.Tungekuwa ni chama cha siasa kilichokosa umakini iwapo tungekaa pasipo kuchukua hatua zozote za kujiimarisha baada ya matokeo ya Uchaguzi Mkuu kuonesha wazi kukua kwa upinzani ambao umeongeza idadi ya wabunge na madiwani katika pande zote mbili za muungano.Matokeo hayo ya uchaguzi ambayo hapana shaka yamekitikisa chama chetu yalitukumbusha wasia ambao tuliachiwa na Baba wa Taifa aliyesema; ‘Bila ya CCM Madhubuti Nchi Yetu Itayumba’.Wazee wangu, kwa sababu ya kutambua ukweli kwamba hakuna haki isiyo na wajibu kama nilivyosema awali, mimi na wenzangu tuliokuwa katika Kamati Kuu tuliona ulazima, haja na umuhimu wa kukubali kwa kauli moja wito wa kututaka tujiuzulu ikiwa ni hatua moja ya kujipanga na kukijenga upya chama chetu.KUJIVUA GAMBA KWAPOTOSHWAWazee wangu, kilichotokea baada ya kujiuzulu kwetu kila aliye ndani na nje ya chama chetu amekisikia na anakifahamu. Chama kilipata safu mpya ya uongozi iliyotokana na kuundwa kwa Sekretarieti inayoongozwa na Katibu Mkuu wetu mpya, Mhe. Wilson Mukama, na Kamati Kuu iliyokuwa na sura tofauti na ile ya awali.Wakati tukitafakari na kuangalia mustakabali mpya wa kisiasa ndani ya chama chetu, ghafla yalianza kutokea mambo ambayo chokochoko zake zilianza kusikika tangu tukiwa ndani ya Kamati Kuu ambayo ilijiuzulu baadaye.Mara tu baada ya kumalizika kwa kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa ambacho kilichagua wajumbe wapya wa Kamati Kuu na kuidhinisha uundwaji wa Sekretarieti mpya, dhana ya kujivua gamba ambayo naamini Mwenyekiti wetu aliianzisha kwa nia njema ilianza kuenezwa ikichukua tafsiri na mwelekeo tofauti na ule wa awali.Wajumbe wawili wa Sekretarieti, Naibu Katibu Mkuu (Tanzania Bara), Mhe. John Chiligati, na Katibu wa Idara ya Itikadi na Uenezi, Mhe. Nape Nnauye, walisikika wakitangaza kwamba Halmashauri Kuu ya Taifa ilikuwa imefikia uamuzi wa kuwapa siku tisini wale walioitwa watuhumiwa wanaokabiliwa na tuhuma za ufisadi ndani ya chama kujitoa katika nafasi zao za uongozi vinginevyo watafukuzwa na chama.Wazee wangu, baada ya kushinikizwa sana na vyombo vya habari wawataje kwa majina wanasiasa waliokuwa wakituhumiwa kwa ufisadi ambao ni wajumbe wa NEC na ambao wanapaswa kujiuzulu nyadhifa zao, wajumbe hao wa Sekretarieti walikwenda mbele zaidi.Baada ya awali kuwaeleza waandishi wa habari kwamba majina ya watuhumiwa hao yalikuwa yakifahamika kutokana na kuhusishwa katika kashfa tofauti kama zile za Richmond, EPA na ununuzi wa rada, mwishoni viongozi hao walikaririwa wakiyataja majina ya wanasiasa watatu kuwa ndiyo ambao walikuwa wakilengwa na maamuzi hayo.

Wazee wangu, nilishangazwa na kushitushwa na namna porojo na fitina za kisiasa zilivyofinyangwa kwa mara nyingine tena baada ya kusikia jina la mbunge wenu ambaye ni mimi, likitajwa kuwa miongoni mwa yale matatu ya viongozi waliokuwa wakitakiwa eti kupima wenyewe na kisha kuchukua uamuzi wa kujiuzulu nafasi zao za uongozi ndani ya NEC katika kipindi cha siku tisini.Niliseme hili mapema. Mshangao na mshituko wangu haukusababishwa na kutajwa kwa jina langu, la hasha, bali namna uamuzi halisi wa NEC na hususani dhana nzima ya ‘kujivua gamba’ ilivyoweza kupindishwa na wajanja wachache na kisha kuendeshwa kwa maslahi binafsi ya kikundi fulani cha watu.Pili, nilishangazwa na kushitushwa na hatua ya viongozi wa chama changu ambacho nimekitumikia kwa bidii na uaminifu mkubwa kufanya juhudi kubwa hata kukivisha kikao kitukufu cha NEC uamuzi ambao msingi wa hoja zake ni vita vya kimakundi ya kisiasa yaliyo ndani ya CCM kwa upande mmoja na propaganda za vyama vya siasa vya upinzani na vyombo vya habari kwa upande mwingine.Tatu, nilishangazwa na kushitushwa na ujasiri ambao umekuwa ukioneshwa na baadhi ya viongozi wetu wapya wa Sekretarieti wanaolitaja jina langu na kulihusisha na kile wanachokiita ufisadi ambao hata ukweli wa kimazingira na kihistoria ukiachilia mbali ushahidi wa wazi umeshathibitisha kwamba ni porojo za kisiasa zilizotokana na makovu na matarajio ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 na ule ujao wa 2015.Wazee wangu, nyinyi ni mashahidi kwamba, mbali ya mimi mwenyewe kujitokeza kupitia vyombo vya habari na kueleza wazi kwamba sijapata kujihusisha katika vitendo vyovyote vya ukiukwaji wa maadili ya uongozi au vya rushwa, hakuna ushahidi wowote uliotolewa unaonihusisha na kashfa yoyote miongoni mwa zile zilizotajwa.Wazee wangu, ni wazi kwamba kama chama chenye siasa chenye dhamana ya kuwaoongoza Watanzania kutoka katika lindi la ufukara, maradhi, matatizo ya makaazi na mengineyo siku zote tunapaswa kuwa makini katika kuhakikisha kwamba changamoto za kuwaongoza na kuwakomboa wananchi waliotupa dhamana hazitikiswi na mawimbi ya matakwa ya nyakati ama ya vyombo vya habari au wapinzani wetu wa kisiasa walio nje ya CCM.Ni kwa sababu ya kulitambua hilo na hasa kuyatambua madhara yanayoweza kukipata chama chetu na nchi yetu iwapo tutaendekeza siasa za kupakana matope pasipo na sababu za msingi, kuchafuana kusikokoma na kulipizana kisasi ndiyo maana nimeona nitumie fursa hii kuzungumza nanyi wazee wangu ili kuweka kumbukumbu sahihi.MAAMUZI YANGUWazee wangu, nimetafakari sana na kimsingi nimefikia hatua ya kupima yale ambayo yamekuwa yakisemwa na kuandikwa juu yangu na ambayo kwa mtazamo wangu unaoungwa mkono na wanafamilia yangu, marafiki zangu na washirika wangu wa kibiashara walio ndani na nje ya nchi, naona umefika wakati muafaka wa kuchukua hatua.Kwa sababu ya kutambua uzito wa hatua ninazokusudia kuzichukua, niliona halitakuwa jambo la hekima hata kidogo iwapo ningefanya hivyo pahala pengine popote bali hapa Igunga mbele ya nyie wazee wangu.Baada ya kukaa na wanafamilia yangu, marafiki na washirika wangu wa kibiashara niliona halitakuwa jambo la busara hata kidogo kuendelea kuvutana na viongozi wa chama changu na wanachama wenzangu wa CCM katika mambo ambayo yanaweza kumalizwa kwa njia muafaka.Wazee wangu, sina budi niwaeleze kwamba, mbali ya athari za kisiasa na kifamilia, vita vya ovyo vya kisiasa kama hivi tunavyoviendesha na kuviendeleza ndani ya CCM na ndani ya nchi yetu huwa vina athari kubwa katika ulimwengu wa kibiashara. Athari kama hizo za kibiashara huingia ndani zaidi kuliko vichwa vya habari vya magazeti vinavyolenga kuchafuana, na athari hizo huwa kubwa zaidi kwa mtu kama mimi kwa sababu tofauti na wengine wengi hapa nchini, mimi ni mfanyabiashara wa kimataifa.

Katika ulimwengu wa kibiashara wa leo, vita hivi ambavyo vinaweza kuonekana kuwa ni vidogo tu vyenye malengo ya kuchafuana kisiasa, vinakuwa na athari kubwa katika uhusiano wa kibiashara kuliko hata wale wasioelewa wanavyoweza kukadiria. Ndiyo maana nimeona ni afadhali sasa niwape nafasi wale wanaoendesha siasa hizi uchwara na zisizo na tija waendelee na siasa zao hizo ambazo kwa bahati mbaya kwao, mimi sina muda nazo na siwezi kuwa sehemu yake. Na mimi kwa upande wangu niendelee na maisha yangu.Kutokana na ukweli huo na sababu zote hizo basi, kwa moyo wa dhati na kwa nia thabiti, hatua ya kwanza niliyoiona kuwa ninapaswa kuichukua ilikuwa ni hii ya kuitikia wito unaotokana na msukumo wa ndani ya nafsi yangu wa kuamua kukomesha kabisa malumbano na mivutano isiyo na manufaa kwangu binafsi, kwa viongozi wa chama changu na chama chenyewe.Msukumo huo si mwingine bali ni ule wa kuamua kuachia nafasi zangu zote za uongozi ndani ya chama, nikianzia na ile ya ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa nikiuwakilisha Mkoa wa Tabora na hii ya ubunge wa Igunga ambazo kama si kwa baraka za chama changu nisingelikuwa nazo.Napenda kuliweka hili sawa sawa. Uamuzi wangu wa kuachia nafasi zangu zote za uongozi nilizopata kwa tiketi ya CCM haukutokana na wala haumaanishi kukubaliana na shinikizo lililopotoshwa kuhusu azma ya utekelezaji wa dhana ya kujivua gamba, la hasha, bali dhamira ya dhati ya kuachana na siasa hizi uchwara (gutter politics) na kutumia muda wangu kushughulika na biashara zangu.Aidha, nimefikia uamuzi huo lengo likiwa ni kuwajengea heshima na imani machoni mwa wanachama na wananchi wengine, viongozi wangu ambao naamini baada ya mimi kujitoa watapata fursa ya kutafakari upya changamoto nyingine mbadala zinazowakabili ambazo msingi wake ni dhamana kubwa walizo nazo za kukiongoza chama chetu na nchi yetu kupitia Serikali yake.Wakati nachukua uamuzi huu, natambua vyema kwamba, watatokea watu ndani ya chama chetu na nje ambao watafanya kila juhudi kupotosha au kupindisha ukweli kuhusu hatima yangu ya kisiasa baada ya kujiweka kando na kujipa mimi mwenyewe na chama changu fursa ya kutafakari kwa kina majaaliwa yangu na ya nchi yangu katika siku zijazo.Nafanya hivyo nikiwa na imani thabiti kwamba, uamuzi wangu huu, hususani ule wa kuachia nafasi yangu ya ubunge, yatakipa fursa nyingine CCM ya kuendelea kuliongoza jimbo letu la Igunga katika kipindi cha miaka minne ijayo kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Kwa upande mwingine, uamuzi wangu huu naona ni fursa kwa viongozi wa Chama changu cha CCM kutafakari na kuamua njia wanayoiona wao ni sahihi kuichukua kwa hatima na mustakabali wa chama chetu na ambayo wanaamini itakipa nguvu mpya ya kisiasa dhidi ya vyama vya upinzani.Sambamba na hilo, ninayo imani thabiti kwamba, uamuzi wangu wa kubakia kuwa mwanachama wa kawaida na mtiifu wa CCM utakuwa chachu kwa chama changu na kwa Serikali yake kuwatumikia wananchi kwa Ari Zaidi, Kasi Zaidi na Nguvu Zaidi.Mwisho kabisa, nikimalizia naomba nitumie fursa hii kutoa heshima za pekee kwa Rais Jakaya Kikwete kwa kazi kubwa aliyoifanyia na anayoendelea kuifanyia nchi yetu. Amefanya mengi na makubwa kuiendeleza nchi yetu na watu wake kuliko inavyothaminiwa na kufahamika. Kazi yake kubwa inashindwa kuthaminiwa na kufahamika kutokana na siasa chafu tunazoziendesha Tanzania. Wasia wangu kwa wanasiasa wenzangu, waandishi wa habari na Watanzania wenzangu kwa ujumla ni kuwa tunahitaji kuisaidia nchi yetu kwa kufanya siasa zenye mwelekeo wa kujenga ambazo ndiyo hasa zinapaswa kuwa siasa kwa maana halisi ya neno hilo.

Wazee wangu, baada ya maelezo hayo, nawashukuru sana kwa kunisikiliza na kunielewa.Ahsanteni sana.
Mwisho…

Ndolo, Fabriges wagonganisha vichwa Yanga


PANGA pangua ya nani abaki na yupo atoke kati ya Tonny Ndolo na Haruna Niyonzima 'Iniesta' ndani ya usajili mpya wa mabingwa wapya wa Kombe la Kagame, Yanga, imeibua mzozo ndani ya klabu hiyo.
Ndolo, Mganda aliyesajiliwa toka Kagara Sugar na Iniesta aliyetoka APR ya Rwanda, mmoja kati yao anapaswa kuachwa kwenye usajili ili kutekelezwa kwa kanuni ya idadi ya wachezaji wa kigeni wanaopaswa kusajiliwa na klabu za soka nchini.
Yanga tayari imetimiza idadi ya wachezaji sita wa kigeni, mmoja zaidi ya idadi inayotakiwa na TFF na kwa maana hiyo kuilazimisha klabu hiyo kupunguza jina moja na mzozo unakuja juu ya nani aachwe kati ya wachezaji hao wawili kutokana umuhimu wao katika kikosi hicho.
Awali ilikuwa ikitajwa kwamba mshambuliaji Hamis Kiza 'Diego' ndiye aliyekuwa katika hatihati ya kubakishwa Yanga, lakini kwa kiwango alichokionyesha kwenye michuano ya Kagame akiifungia mabao muhimu akishirikiana na 'mapro' wengine wawili, Davis Mwape wa Zambia na Kenneth Asamoah aliyewapa ubingwa mbele ya Simba, hali imekuwa kizungumkuti.
Mchezaji mwingine wa kigeni aliyepo Yanga ni kipa Yew Berko kutoka Ghana ambaye msimu uliopita wa Ligi Kuu Tanzania Bara alichaguliwa kuwa Kipa Bora akimfunika Juma Kaseja.
Habari za ndani za klabu hiyo zinasema mapendekezo ya kocha Sam Timbe tangu awali ni kuachana na Iniesta, lakini kamati ya usajili imekuwa ikimkumbatia kiungo huyo, ikitaka wa kuachwa awe Ndolo, kitu ambacho kocha hataki kusikia kutokana na kumhitaji nyota huyo.
Hali hiyo imefanya hata Msemaji wa klabu hiyo, Louis Sendeu kushindwa kujua ukweli yupi kati ya wachezaji hao wawili ndiye atakayeachwa wakati dirisha la uhamisho wa wachezaji likifungwa Alhamisi iliyopita.
"Kwa kweli mie sijui nani ataachwa, ila hatma yao itafahamika wakati wowote kwa vile tunajua tunatakiwa kupunguza jina la mchezaji mmoja kutokana na kuzidisha idadi ya wachezaji wa kigeni inayotakiwa na kanuni za usajili nchini," alisema Sendeu.

Msiwaite wafanyakazi wenu wa ndani majina mabaya


WAAJIRI wa wafanyakazi wa majumbani nchini, wameombwa kuachwa kuwaita majina
mabaya watumishi wao, kwa madai kufanya hivyo ni kushusha hadhi na utu wa wafanyakazi hao ambao ni watu muhimu kwao na familia zao kwa ujumla.
Kadhalika wametahadhariwa kuepuka tabia ya kuwaajiri wafanyakazi wenye umri chini ya
miaka 17 kutokana na ukweli umri huo ni mdogo kwa ajira na pia ni kosa kulingana na sheria za kimataifa kuhusu ajira za watoto.
Hayo yalisemwa na wawezeshaji wa semina ya siku moja ya 'Waajiri Makini' iliyoandaliwa na Shirika la kuhudumia Afya na Maendeleo ya Wanawake na Watoto ya Kiota, (KIWOHEDE), walipokuwa wakitoa mafunzo ya kujenga mauhusiano bora kati ya waajiri na wafanyakazi wa majumbani, iliyofanyika katikati ya wiki iliyopita.
Edda Kawala na Stella Mwambenja wote kutoka KIWOHEDE, walisema tabia ya waajiri
kuwaita majina mabaya watumishi wao na kuwanyanyasa au kuwabagua ni jambo baya kwani
linashusha hadhi na utu wa wafanyakazi hao kinyume na sheria na mikataba wa kazi kimataifa.
Wawezeshaji hao walisema ni wajibu waajiri kuishi kwa wema na watumishi wao kwa
kuwafanya kama sehemu ya familia zao badala ya kuwabagua na kunyanyapaa, kitu ambacho sio ubinadamu na kinachochangia uhasama usio na maana baina ya wawili hao.
Pia waliwataka waajiri kuchungua kuajiri wafanyakazi wenye umri mdogo ili wasiweze kunasa kwenye mikono ya sheria inayokataza ajira kwa watoto.
"Mbali na kuchunga umri, pia msiwe mnawabagua wafanyakazi wenu wakati wamekuwa
msaada mkubwa katika majumba yenu kwa kazi wanazowafanyia, muwalipe vema na kwa
wakati kwa vile nao ni wanastahili mahitaji kama watu wengine," alisema Stella.

Wafanyakazi wa Majumbani sasa wapata 'Rungu'

KUPITISHWA kwa Mkataba wa Kimataifa wa 189 wa Shirika la Kazi Duniani, ILO,
kumeelezwa kuwa kama ni 'rungu' kwa wafanyakazi wa majumbani kuwashughulikia waajiri
wao watakaokiuka sheria na mikataba ya kazi kama ilivyo kwa wafanyakazi wengine nchini.
Mkataba huo wa kuwatambua wafanyakazi hao wa majumbani ulipitishwa Juni 16 mwaka huu
katika mkutano wa 100 wa ILO uliofanyika nchini Uswisi, ambapo siku moja kabla ya
kupitishwa kwake, Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete alihutubia mkutano huo kuuridhia,
Akizungumza na MICHARAZO, Mratibu wa Shirika la Wafanyakazi wa Majumbani Kanda ya
Afrika, IUF, Bi Vick Kanyoka, alisema kuridhiwa kwa mkataba huo kumetoa fursa na nafuu kwa watumishi hao wa majumbani ambao kwa miaka mingi walikuwa hawathaminiwi nchini.
Bi Kanyoka, alisema kulingana na mkataba huo ni kwamba wafanyakazi wa majumbani kwa
sasa wanatambuliwa kama wafanyakazi wengine wakihitajiwa kulindwa na kupewa haki zao
ikiwemo kusainishwa mikataba na makubaliano kabla ya kuanza kazi kwa muajiriwa.
Mratibu huyo alisema kitu cha muhimu baada ya kupitishwa kwa mkataba huo ni serikali ya Tanzania na wananchi wake kuutekeleza kwa vitendo mkataba huo ili kuhakikisha wafanyakazi wanajivunia kazi yao tofauti na siku za nyuma walipokuwa wakijificha.
"Kwa hakika kupitishwa kwa mkataba huo wa 189 ni kama rungu kwa wafanyakazi wa
majumbani kuweza kuwabana waajiri wao, ambao kwa miaka mingi walikuwa wakiwabagua,
kuwanyanyasa na kuwadharau wakiwachukulia kama 'vijakazi'," alisema.
Aliongeza kwa kuwataka watumishi hao kuwa mstari wa mbele katika utekelezaji wa mkataba huo kwa kutokubali kuajiriwa kabla ya kuingia mkataba na kuridhia haki zake stahiki katika ajira yake, ili inapotokea tatizo mbele ya safari iwe rahisi kusaidiwa.
Bi Kanyoka, aliwasihi pia waajiri kuridhia na kuutekeleza mkataba huo kwa kuamini watumishi hao ni kama sehemu za familia zao na hivyo kuwapa huduma na stahiki zote ikiwemo kuwalipa fedha kulingana na kima wanachokubaliana na kwa muda muafaka.
"Pia wawajali na kuwathamini kwa sababu wao ni watu tegemeo kwao na familia zao, hivyo kukaa nao kwa ubaya ni kusababisha matatizo ambayo tumekuwa tukishuhudia katika jamii yetu," alisema.
Mratibu huyo alisema mkataba huo ulipitishwa kwa kupigiwa kura 396 za ndio huku kura 16 zikiukataa miongoni mwa nchi zilizougomea ikiwa ni taifa la Uingereza, huku mataifa ya Afrika ikiwemo Tanzania na yale ya Amerika Kusini na Kaskazini yakiongoza kwa kuupitisha.

Thursday, July 14, 2011

Banka yu tayari wa lolote Simba



KIUNGO nyota wa timu ya Simba na timu ya taifa, Taifa Stars, Mohammed Banka, amesema ingawa hajapata taarifa rasmi ya kutemwa ndani ya kikosi hicho, lakini yupo tayari kwa lolote mradi alipwe chake kwa kuvunjwa mkataba alionao na klabu hiyo.
Aidha amedai kusikitishwa na lawama anazotupiwa kwa kushindwa kung'ara kwenye pambano la fainali za Kombe la Kagame dhidi yao na Yanga, wakati ilifahamika kuwa ametoka majeruhi kitu ambacho hata kocha Moses Basena alikuwa akifahamu.
Akizungumza na MICHARAZO mapema leo, Banka alisema hana taarifa za kuachwa na Simba kama baadhi ya vyombo vya habari vilivyoripoti jana, lakini kama jambo hilo ni kweli hana jinsi zaidi ya kukubaliana na mapendekezo ya viongozi wake.
Banka alisema kitu cha msingi ni klabu ya Simba imlipe chake kwa kuvunja mkataba wao, ili akatafute maisha pengine, ingawa alisema amesikitishwa na kushutumiwa kwa kuwa miongoni mwa walioikosesha Simba taji la saba la michuano ya Kagame.
"Kwa kweli sijapewa taarifa yoyote rasmi zaidi ya kusoma kwenye vyomvo vya habari, lakini kama uongozi umeazimia hivyo, sitakuwa na jinsi zaidi ya kusubiri kulipwa changu kwa kuvunjwa mkataba nitafute mahali pa kwenda," alisema.
Aliongeza, kucheza kwake chini ya kiwango katika mechi ya Simba na Yanga katika fainali za Kagame ilitokana na kutoka kuwa majeruhi, kitu ambacho hata mwenyewe alishtuka alipoagizwa na kocha Basena kuingia dimbani.
"Kocha aliniambia kabla ya mechi atanichezesha kipindi cha pili ili kuangalia maendeleo yangu ya kupona majeraha, hivyo alivyoniambia niingie nilishangaa, lakini kama mchezaji ninayezingatia nidhamu sikuweza kumbishia, ila Simba wasinielewe vibaya," alisema Banka.
Kiungo huyo alisema anaamini mchango wake ndani ya Simba ni mkubwa kuliko lawama anazopewa sasa, lakini kwa kuwa soka ndivyo lilivyo anajiandaa kutafuta maisha mahali pengine kwa kuamini 'riziki' yake imeisha ndani ya klabu hiyo.
Banka, pamoja na Mussa Hassani Mgosi na Athumani Idd 'Chuji' walitajwa kuwa miongoni mwa waliopendekezwa kutemwa ndani ya Simba kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa kutokana na kuonyesha kiwango duni kwenye Kombe la Kagame, ambapo Simba ilifungwa na Yanga bao 1-0.

Mwisho

Bujibu kuchapana na Mtambo wa Gongo


WAKATI michuano ya Ligi ya Kick Boxing iliyotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu ikiahirishwa hadi Desemba, mabondia wakongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Osward na Ernest Bujiku wanatarajiwa kupamba ulingoni kupigana.
Maneno Osward maarufu kama Mtambo wa Gongo atapigana na Bujiku katika moja ya mapambano ya ngumi yatakayoshindikiza pambano la Kick Boxing kati ya Amour Zungu wa Zanzibar dhidi ya Mchumia Tumbo litakalofanyika Julai 30 kwenye ukumbi wa DDC Keko, Dar es Salaam.
Kaseba alisema, mbalio na pambano la Osward na Bujiku siku hiyo pia mabondia wa kike, Jamhuri Said wa Tanzania atapimana ubavu na Rukia Kaselete wa Kenya katika pambano jingine la Kick Boxing.
Alisema michezo mingine itakayosindikiza mipambano hiyo ni kati ya Fadhila dhidi Demu wa Kisarawe, Dragon Kaizum atakayepigana na Faza Boy, Idd dhidi ya Dragon Boy, Lion Heart dhidi ya Begeje na michezo mingine ya ngumi za kulipwa.
Kaseba alisema michezo hiyo inafanyika ili kuwapa burudani wakazi wa Dar es Salaam ambao walikuwa wakijiandaa kushuhudia ligi ya Kick Boxing ambayo imeahirishwa hadi Desemba kwa ajili ya kufanya maandalizi ya kutosha.
"Tumeamua kuahirisha ligi ya Kick Boxing hadi Desemba kutoa muda kwa mabondia kujiandaa na kufanya katika kiwango cha kimataifa, hivyo ili kutowanyima raha wadau wa mchezo huo tumeandaa michezo kadhaa ya Kick Boxing na ngumi za kulipwa siku ya Julai 30 itakayofanyika kwenye ukumbi wa DDC Keko," alisema Kaseba.
Alisema Bujiku na Osward kila mmoja kwa sasa yupo katika maandalizi makali ya kuonyeshana umwamba wakikumbushia enzi zao wakitamba kwenye mchezo huo.

Mwisho

Waajiri wapigwa msasa kuishi na wafanyakazi wa majumbani



WAAJIRI wa wafanyakazi wa ndani watakiwa kutowabagua na kuwanyanyasa watumishi wao wa ndani na badala yake kuishi nao kwa wema kutokana na ukweli wao ni watu wa karibu na wasiri wakubwa wa familia zao.
Wito huo umetolewa kwenye semina ya siku moja iliyoandaliwa na Asasi ya kiraia ya KIWOHEDE kwa lengo la kujenga mauhusiano mema baina ya waajiri na watumishi wa kazi za ndani ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakichukuliwa kama vijakazi.
Mgeni rasmi wa semina hiyo, Sheikh Shughuli Sheikh, ambaye ni Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Malapa Kata ya Buguruni na Mwezeshaji wa semina hiyo Edda Kawala, walisema kuna umuhimu wa waajiri kuwaona wafanyakazi wa majumbani kama sehemu ya familia zao.
Sheikh, alisema kutokana na mchango na umuhimu wa wafanyakazi wa ndani ambao ni tegemeo la waajiri katika kusaidiwa kazi za nyumbani ni vema watumishi hao wakapewa heshima na kuthaminiwa kama wanafamilia.
"Wao ndio wanaowapikieni, kuwafulieni na kazi nyingine za ndani, hivyo ni wasiri na watu muhimu katika familia zenu hivyo ni vema kukaa nao kwa wema mkiwajali na kuwathamini tofauti na baadhi yenu mnavyowafanyia," alisema Sheikh.
Naye Mwezeshaji alisema lengo la semina hiyo ni kuona waajiri na wafanyakazi hao wa ndani wanakuwa na mauhisiano mema, pamoja na kila mmoja kuhakikisha wanakuwa na mikataba au makubaliano yanayolinda haki na hadhi ya kila mmoja.
Alisema KIWOHEDE, imebaini zipo baadhi ya nyumba au waajiri wamekuwa wakiwabagua watumishi wao na kuwanyima haki zao stahiki na kuchangia kuwepo kwa uhasama na kuifanya kazi hiyo kudharaulika mbele ya jamii.
Washiriki wa semina hiyo wengi wao wakiwa ni akinamama, walisema kuna mambo mengine hawakuwa wanayajua juu ya haki za msingi za watumishi hao na semina hiyo imewafungua macho na kuahidi kuwa 'mabalozi' mema warejeapo makwao.
Semina hiyo ilielekeza umri stahiki wa wafanyakazi wanaopaswa kuajiriwa kwa kazi za majumbani, haki za msingi stahiki za watumishi hao na namna ya uwajibikaji wa kila mmoja kati ya waajiri na wafanyakazi hao.

Mwisho

Tanzania yapongezwa kuridhia mkataba wa ILO


SERIKALI ya Tanzania imepongezwa kwa kuwa miongoni mwa nchi zilizopitisha Mkataba wa Kimataifa wa Kutambuliwa kwa Wafanyakazi wa Majumbani, iliuyopitishwa kwenye Mkutano wa 100 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO).
Kadhalika Rais Jakaya Kikwete amepongezwa kwa hutuba aliyoisoma kwenye mkutano huo juu ya serikali ya Tanzania kuwatambua wafanyakazi hao kama watumishi halali wanaoostahiki hakio zote wa waajiriwa, akiombwa kuhakikisha utekezaji unafanyika.
Mratibu wa Shirika la Wafanyakazi wa Majumbani Kanda ya Afrika (IUF), Vick Kanyoka, akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam alieleza maazimio ya mkutano wa ILO uliofanyika mwezi uliopita mjini Geneva, Uswisi.
Kanyoka, alisema kitendo cha Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zilizopigia kura ya kupitisha mkataba huo wa 189 wa kuwatambua wafanyakazi wa majumbani ni ushindi kwa wafanyakazi wote ambao kabla ya hapo walikuwa wakichukuliwa kama watumwa.
Aliongeza IUF, inaipongeza Tanzania na Rais Jakaya Kikwete aliyehutubia kwenye mkutano huo Juni 15 mwaka huu na kuiomba serikali hiyo itekeleze kwa vitendo mkataba huo ili wafanyakazi wa majumbani kupata haki na kuthaminiwa kama wafanyakazi wengine.
Alisema ingawa sheria ya kuwalinda na kuwatetea wafanyakazi majumbani ipo, lakin i utekelezaji wake umekuwa ni tatizo na ndio maana IUF inaiomba Tanzania kuhakikisha jambo hilo linapata ufanisi ili kuleta usawa miongoni mwa watumishi hao.
"IUF tunaipongeza Tanzania na Rais wake kwa kuridhika kupitishwa kwa mkataba wa 189 wa kutambulika kwa wafanyakazi wa majumbani, uliopitioshwa Juni 16 mwaka huu ambapo ulipitishwa kwa kura 396, huku 16 zikiukataa miongoni mwa mataifa yaliyoukataa likiwa ni Uingereza," alisema Kanyoka.
Mratibu huyo alisema ni kutekelezwa kwa vitendo kwa mkataba huo kutatoa fursa ya waajiri kuwathamini na kuwajali watumishi hao kwa kuingia nao mkataba na kuwalipa haki zao stahiki kma ilivyo kwa watumishi wengine.
Alisisitiza ni muhimu wafanyakazi hao kusaidia kufanikisha uitekelezaji huo kwa kuwa wa kwanza kuhakikisha wanaingia mikataba na makubalino na waajiri wao kabla ya kuanza kazi ili watakapofanyiwa kinyume iwe rahisi kutetewa na kupata haki zao.

Mwisho

Saturday, July 9, 2011

Ligi ya Kick Boxing yaiva

MICHUANO ya Ligi ya Kick Boxing inatarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu jijini Dar es Salaam kwa mabondia wa kike na wa kiume kuumana kuwania ushiriki wa fainali za taifa zitakazofanyika baadaye mwaka huu.
Kwa mujibu wa mratibu wa michuano hiyo, Japhet Kaseba, alisema michuano hiyo itafanyika Julai 31 kwenye ukumbi wa DDC Mlimani, Mwenge jijini Dar es Salaam.
Kaseba, alisema kabla ya kufanyika kwa michuano hiyo anatarajiwa kukutana na mabondia washiriki kwa lengo la kuwapa darasa dhidi ya mchezo huo ambao safari hii utashirikisha wakongwe na chipukizi ikiwa ni mikakati ya kuendeleza mchezo huo.
"Michuano yetu ya ligi ya Kick Boxing itafanyika mwishoni mwa mwezi huu kwenye ukumbi wa DDC Mlimani, ambapo mabondia mbalimbali wake wa waume chipukizi na wakongwe wataonyesha kazi safari hii," alisema.
Kaseba alisema kwa sasa anaendelea na mipango ya kusaka wadhamini kwa ajili yua kulipiga tafu shindano lao ambalo limekuwa kikifanyika kwa mwaka wa tatu sasa katika njia ya kurejesha msisimko wa michuano hiyo iliyompa mataji ya Afrika na Dunia.
Katika hatua nyingine bingwa wa Kick Boxing wa Uganda, Moses Golola, alifanikiwa kumchakaza bondia toka Sudan, Abdul Quadir Rahim mwishoni mwa wiki jijini Kampala, akisisitiza ana hasira ya kutaka kupigana na Kanda Kabongo wa Tanzania.
Golola aliyepigwa na Kabongo katika pambano la kuwania ubingwa wa Afrika, alisema ushindi wake wa KO ya raundi ya pili dhidi ya Msudan ni salamu kwa Kabongo kuwa ajiandae kwa ajili ya kisasi siku wakikutana ambapo huenda ikawa ndani ya mwaka huu.

Klabu za ngumi kupepetana Ilala

KLABU za ngumi za ridhaa za Amana na Matimbwa ni miongoni mwa klabu zaidi ya tano zinazotarajiwa kuonyeshana kazi katika mfululizo wa michuano maalum ya mchezo huo inayoendelea wilayani Ilala jijini Dar es Salaam.
Klabu zingine zitakazopambana katika michezo itakayofanyika mwishoni mwa wiki hii ikiratibiwa na taasisi ya Kinyogoli Foundation ni Ashanti, Big Right na zingine ambazo hazikuweza kufahamika mapema.
Mratibu wa michuano hiyo, Rajab Mhamila 'Super D' alisema michezo hio itafanyika Jumamosi kwenye ukumbi wa Panandipanandi, Ilala Bungoni.
Super D, alisema maandalizi ya michezo hiyo yamekamilika ikiwemo vikosi vya timu zote kuendelea kujifua.
Aliwataja baadhi ya mabondia watakaoziwakilisha klabu zao kuwa ni Ibrahim Class, Khalfan Othman, Kassim Sambo na Saidi Ally kwa upande wa Amana, wakati Matimbwa itawakilishwa na Mohamed Matimbwa, Mohamed Muhani, Edson Joviki na Mohamed Kumbilambali.
Kwa upande wa Ashanti, Super D alisema itawakilishwa na mabondia kama Uwesu Manyota, Ramadhani Kimangale, Mark Edson na wengine na mipambano yao itachezwa kwa raundi nne nne kila mmoja.
Aliongeza kwa kutoa wito kwa wadau wa ngumi kujitokeza kuzisaidia klabu shiriki na mabondia vifaa vya michezo na mahitaji yao mengine ili kuwatia moyo wa kuupenda mchezo huo.

Wednesday, June 29, 2011

Hapa na pale za Micharazo



Villa Squad yaangukia wadau

UONGOZI mpya wa klabu ya soka ya Villa Squad, umekiri una kazi ngumu katika kuiongoza klabu hiyo kutokana na hali mbaya kiuchumi iliyonayo na kuwaangukia wadau wa soka wa wilaya ya Kinondoni kujitokeza kuisaidia kwa hali na mali.
Villa iliyorejea Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kushuka daraja mwaka 2008, ilipata viongozi wake mwishoni mwa wiki katika uchaguzi mkuu uliohusisha nafasi za makamu mwenyekiti na wajumbe wa kamati ya utendaji tu.
Makamu Mwenyekiti, Ramadhani Uledi, alisema kwa jinsi hali ilivyo mbaya kiuchumi katika klabu hiyo wanalazimika kuwaomba viongozi, wanasiasa na wakazi wa wilaya yao kuisaidia kwa hali na mali klabu yao ili kuhimili vishindo vya ligi hiyo wasirudie makosa ya mwaka 2008.
Uledi, alisema Villa kwa sasa ni kama 'jicho' kwa wakazi wa Kinondoni kutokana na kuwa timu pekee kushiriki Ligi Kuu baada ya awali kuteremka daraja na hivyo ipewe sapoti ikisaidiwa ili irudi 'mchangani'.
"Pamoja na kuwashukuru wanachama kutuchagua kuiongoza Villa, tulikuwa tunaomba tupewe sapoti ya kutosha kwa wadau wa soka na wakazi wa Kinondoni kuiunga mkono kwa kuisaidia kwa hali na mali ili imudu mikikimikiki ya ligi kuu na tusirejee makosa ya 2008 tuliposhuka daraja," alisema Uledi.
Aliongeza uongozi wao ulitarajiwa kupanga siku ya kukutana kwa ajili ya kujadili mambo mbalimbali pamoja na kuteua kamati za kuusaidia uongozi wao katika maandalizi ya ushiriki wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao inayotarajiwa kuanza Agosti 20 mwaka huu.
***

Yanga waituliza Ruvu Shooting


BAADA ya Ruvu Shooting kuitemea cheche Yanga kwa kumchukua beki wao Oscar Joshua bila kufuata taratibu, uongozi wa Yanga umewatuliza ukisema watamalizana nao tu.
Yanga imeipoza Ruvu kwa kusema isubiri mapesa ya mchezaji huyo kwani hata wao wanajua kuwa ametokea kwao.
Msemaji wa Yanga Louis Sendeu amesema, uongozi wao unafahamu kuwa Joshua hajaokotwa jalalani ila kuna timu ametoka, hivyo haiwezi kumsajili bila kufuata taratibu.
"Hili ni suala la muda tu, sisi tutakutana na viongozi wa Ruvu Shooting na tutamalizana tu, hala hakuna tatizo," alisema Sendeu.
Yanga imeamua kupoza makali hayo, baada ya Ruvu kuwa mbogo na kusema kuwa itapinga sehemu yoyote yule mchezaji wao huyo kwenda Yanga kwa sababu hawakumchukua kihalali.
Viongozi wa Ruvu waliripotiwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari, walisema kuwa mchezaji huyo ana mkataba na timu yao.
Kabla hata Yanga haijamalizana na Ruvu, tayari mchezaji huyo ameanza kuitumikia timu hiyo kwenye michuano ya Kagame.
Mchezaji huyo mwenye uwezo wa kucheza beki na kiungo amejiunga na Yanga akitokea Ruvu Shooting ambako nako alichukuliwa kutoka Toto African ya Mwanza.
***

Mcuba kuwasaka 10 Bora ngumi taifa


MABONDIA wa timu ya taifa ya ngumi waliopo kambi ya mazoezi jijini Dar es Salaam wanatarajiwa kuchuana wenyewe kwa wenyewe ili kuchujwa na kupatikana mabondia 10 watakaoiwakilisha nchi kwenye michuano ya 'All African Games'.
Michuano hiyo ya Afrika inatarajiwa kufanyika kati ya Septemba 3-18 mjini Maputo Msumbiji.
Mchujo wa mabondia wa Tanzania unatarajiwa kufanywa na Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mcuba Pimintel Hutardo ambaye anatarajia kuwashindanisha wachezaji wake kusaka wakali 10.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi za Ridhaa Tanzania, BFT, Makore Mashaga, alisema kocha Hutardo atawachuja mabondia hao katika michezo itakayofanyika kwenye kumbi mbalimbali za jijini Dar es Salaam ukihusisha mapambano 20.
Mashanga alisema baada ya mchujo huo mabondia 10 watakaosalia wataendelea kujifua pamoja na kwenda kucheza mechi za majaribio katika nchi kadhaa ambazo Tanzania imapata mialiko na kuzitaja ku ni pamoja na England, India, Scotland na Mauritius.
Katibu huyo alisema sababu ya kocha kuendesha zoezi hilo la mchujo kwa kushindanisha mabondia hao wenyewe ni kupata wachezaji wenye uwezo wa kuisaidia Tanzania kwenye michuano hiyo ya Afrika ambayo inatarajiwa kushirikisha karibu nchi 55.
***

Kinondoni yaapa Pool Taifa


MABINGWA watetezi wa michuano ya taifa ya Pool ya 'Safari Lager National Pool Championship 2011' yaliyoanza kutimua vumbi Juni 30, wametamba kutetea vema ubingwa huo waliouchukuwa mwaka jana mkoani Arusha.
Katibu mkuu wa chama cha pool cha Kinondoni (KIPA), Zaharo Ligalu aliwaambia makatibu wakuu juzi wa klabu 10 zitakazoshiriki mashindano hayo kuwa wamejipanga vema kuhakikisha hawapotezi ubingwa huo.
Ligalu aliyasema hayo wakati wa upangaji wa ratiba ya mashindano hayo kwenye ukumbi wa Meeda Club uliopo Sinza Jijini Dar es salaam.
Alisema kuwa licha ya ushindani mkubwa ambao wanategemea kuupata kutoka kwa mikoa mingine lakini hakuna sababu ya kuchukuwa tena ubingwa huo kutokana na Kinondoni kusheheni vipaji vya wachezaji wa mchezo huo.
"Makatibu wenzangu wa klabu naomba niwambie kuwa tumejipanga kuhakikisha ubingwa unarudi tena Kinondoni, hivyo endeleeni kuwaandaa wachezaji wenu vizuri ambao nina imani ndiyo watakaosaidia Kinondoni kutetea vema ubingwa wetu,"alisema Ligalu.
Alisema kuwa kikubwa ambacho kitafanikisha kutetea ubingwa huo ni ushirikiano wa pamoja wa wadau wote wa mchezo huo wa Kinondoni.
Klabu zinazoshiriki mashindano hayo ngazi ya mikoa kwa upande wa Kinondoni ni Shoko, Topland, Meeda, 4 wayz, Madrid, Mkwajuni, Ubungo Terminal, Jaba, Bahama mama na Mlalakuwa.
Fainali za taifa ambazo Kinondoni itatetea taji lake zitafanyikia kwenye ukumbi wa Kilimani mkoani Dodoma.

===========
Akudo, Mapacha Wa3 uso kwa uso


BENDI za muziki wa dansi za Akudo Impact na Mapacha Watatu, zinatarajia kufanya onyesho la pamoja linalolenga kudumisha urafiki baina ya wanamuziki wa bendi hizo mbili.
Mratibu wa onyesho hilo, Mkurugenzi wa kampuni ya Biggy One Entertainment, Abubakar Mwanamboka, alisema bendi hizo zitaonyeshana kazi kesho kwenye ukumbi wa Vatican, Dar.
"Lengo letu ni kutaka kuonyesha kwamba bendi za muziki wa dansi zinaweza kushirikiana na kuondoa mawazo yaliyojengeka miongoni mwa baadhi ya watu kuwa wanamuziki wa bendi mbili hawawezi kushirikiana," alisema.
Alisema, majigambo kati ya bendi moja na nyingine siyo ugomvi bali ni njia ya kuvuta mashabiki na kwamba kampuni yake imeandaa onyesho hilo ili kudhihirisha kuwa wanamuziki wanaweza kushirikiana katika kazi yao.
Mratibu huyo alisema, mbali na bendi hizo mbili kutoa burudani kwenye onyesho hilo, piaatakuwepo msanii wa muziki wa kizazi kipya H. Baba ambaye naye atafanya vitu vyake.
Aliongeza onyesho hilo la Akudo na Mapacha ni la kwanza kuratibiwa na kampuni yake.
Akudo Impact imekuwa ikitamba na albamu ya kwanza ya 'Impact' wakati Mapacha Watatu nayo ikitamba na albamu ya kwanza ya 'Jasho la Mtu' na sasa bendi hizo kila moja iko kwenye maandalizi ya albamu ya pili.


Mwisho

Sunday, June 26, 2011

MCHANYATO WA MICHARAZO

Tisa wamwagwa Mtibwa Sugar

KLABU ya soka ya Mtibwa Sugar, imetangaza kuwatema wachezaji wake 9 akiwemo mkongwe Faustine Lukoo na kipa Soud Slim waliomaliza mkataba wa kuichezea klabu hiyo.
Kwa mujibu wa Msemaji wa klabu hiyo, Thobias Kifaru, baadhi ya wachezaji wengine waliopewa mkono wa kwaheri katika mashamba ya Manungu, Morogoro ni winga Julius Mrope aliyeenda Yanga na Obadia Mungusa aliyesajiliwa na Simba.
Kifaru, aliwataja wachezaji wengine ni Yusuph Mgwao, Yona Ndabila anayeenda kucheza soka la kulipwa nje ya nchi, Mganda Boban Zilintusa waliyeshindwa kumtumia kwa kukosa ITC, ambaye walimsajili na kushindwa kumtumia kwa kukosa ITC, na Lameck Dayton.
"Tumeacha jumla ya wachezaji tisa, akiwemo mkongwe Faustine Lukoo baada ya kumaliza mikataba ya kuitumikia klabu yetu na wengine kuhamia klabu zingine za Ligi Kuu, ila Ndabila aliyekuwa na mkataba aliomba kusitisha kwa vile anataka kwenda kucheza soka nje," alisema.
Hata hivyo Kifaru hakuweka bayana juu ya wachezaji Salum Machaku na kipa Shaaban Kado ambao wametajwa kutua kwa watani wa jadi wa soka la Tanzania, Simba na Yanga kwa msimu ujao wa ligi kuu.
Machaku anayeichezea pia timu ya taifa, Taifa Stars imedaiwa amesajiliwa Simba na Kado anayechezea timu za vijana U20 na ile ya wakubwa tayari imethibitishwa amenyakuliwa na Yanga kwa ajili ya msimu ujao utakaoanza Agosti 20 mwaka huu.
***

Fainali Pool Taifa zaiva


FAINALI za taifa za mchezo wa pool za 'Safari Lager National Pool Champioship 2011' zinatarajia kuanza mwezi ujao.
Kwa mujibu wa Meneja wa bia ya Safari Lager, Oscar Shelukindo, fainali hizo zitafanyika kati ya Julai 27-30 kwenye ukumbi wa Kilimani mkoani Dodoma.
Shelukindo alisema, fainali hizo zitatanguliwa na mashindano ya ngazi za mikoa yatakayoanza Juni 30 hadi Julai 17, ikishirikisha mikoa 14 ya Tanzania Bara.
Alisema mara baada ya mashindano hayo kukamilika katika ngazi za mikoa kila mkoa utaunda kombaini ya wachezaji kwa ajili ya kuwakilisha kila mkoa katika ngazi ya fainali hizo za taifa.
Shelukindo alisema bingwa wa fainali hizo atanyakulia Sh.mil. 5, mshindi wa pili ataondoka na mil. 3, mshindi wa tatu Mil. 2 na mshindi wa nne Mil 1.
Aliongeza fainali hizo ambazo zitahusisha na wachezaji mmoja mmoja wanaume na wanawake, bingwa kwa upande wa wanaume atazawadiwa Sh.Sh.500,000, mshindi wa pili Sh.250,000, mshindi wa tatu Sh.200,000 na mshindi wa nne Sh.100,000
Kwa upande wa wanawake bingwa atapewa Sh.350,000, mshindi wa pili Sh.200,000, mshindi wa tatu Sh.150,000 na mshindi wa nne Sh.50,000.
Aliongeza kwa kuzitaja zawadi kwa upande wa ngazi ya mikoa kuwa bingwa atajinyakulia Sh. 700,000, mshindi wa pili ataondoka na Sh.350,000, mshindi wa tatu atazawadiwa Sh.200,000 na mshindi wa nne Sh150,000.
Kwa upande wa mchezaji mmoja mmoja ngazi ya mikoa (wanaume) bingwa atajinyakulia Sh.350,000, mshindi wa pili Sh.200,000, mshindi wa tatu Sh.150,000 na mshindi wa nne Sh.100,000,
Kwa upande wa wanawake bingwa atapewa Sh.250,000, mshindi wa pili Sh.150,000, mshindi wa tatu Sh.100,000 na mshindi wa nne Sh.50,000.
Mikoa itakayoshiriki ni mabingwa watetezi Kinondoni, Ilala na Temeke, Shinyanga, Mwanza, Kagera Mbeya, Tanga, Arusha, Kilimanjaro, Dodoma, Iringa, Manyara na Morogoro.
***

Toto Afrika yazionya Kagera, Mtibwa Sugar


KLABU ya soka ya Toto Afrika ya Mwanza imezitaka klabu zinazotaka kuwasajili nyota wao kutotumia mlango wa nyuma na badala yake zionane nao na kufanya mazungumzo.
Uongozi wa Toto, umesema umelazimika kutoa tahadhari hiyo kutokana na kuwepo kwa taarifa zinazoripotiwa na vyombo vya habari juu ya timu za Kagera Sugar na Mtibwa Sugar kuwanyakua wachezaji wao wawili nyota bila ya wenyewe kujua lolote.
Wachezaji walioufanya uongozi huo kucharuka mapema ni mshambuliaji, Husseni Sued anayedaiwa kutua Kagera Sugar na kiungo Mohammed Soud aliyevumishwa kunyakuliwa na klabu ya Mtibwa ya Morogoro.
Katibu wa klabu hiyo, Salum Kaguna, alinukuliwa hivi karibuni akisema kuwa, hawana taarifa zozote za wachezaji hao kunyakuliwa na timu hizo kwa vile hakuna mazungumzo yoyote yaliyofanywa hadi ssa baina yao na klabu hizo.
Kaguna, alisema ni vema klabu zinazowataka wachezaji ziende mezani kuzungumza kwa sababu nyota hao wana mikataba na hivyo hawatakuwa radhi waondoke kienyeji.
"Hatuzuii wachezaji wetu kuondoka kama wamepata timu, muhimu ni taratibu zifuatwe, mfano Soud anayetajwa kutua Mtibwa, yeye ana mkataba wa miaka mitatu ya Toto akiwa ametumikia miaka miwili na kubakisha mmoja utakaoisha mwakani," alisema Kaguna.
Viongozi wa Mtibwa na Kagera hawakupatikana kuweka bayana kinachoendelea juu ya harakari zao za kuwanyakua wachezaji hao na onyo hilo la uongozi wa Toto Afrika ambayo imekuwa ikijinadi imepania kufanya kweli msimu ujao katika Ligi Kuu Tanzania Bara.
***

TAVA yapongezwa, yashauriwa


CHAMA cha Mpira wa Wavu nchini, TAVA, umepewa 'kifyagio' kwa kujitahidi kurejesha hadhi ya mchezo huo, lakini kikashauriwa kuwekeza nguvu zao ngazi za chini hususani katika mashule ili kuzalisha nyota wa baadaye watakaoisaidia Tanzania kimataifa.
Kifyagio na ushauri huo umetolewa na mchezaji nyota wa zamani wa klabu ya Jeshi Stars, Ibrahim Christopher 'Michael Power' alipozungumza na MICHARAZO na kusema uongozi wa TAVA umekuwa ukijitahidi katika hali ya mazingira magumu kuinua tena mchezo huo nchini.
Christopher, alisema kukosekana kwa wadhamini ni tatizo lililochangia kuufanya mchezo wa wavu kudodora, lakini jitihada za viongozi wa chama chao umesaidia kuendesha michuano ya kitaifa na kimataifa jambo la kupongezwa.
Alisema hata hivyo bado TAVA inapaswa kuelekeza nguvu zao katika ngazi za chini kusaka nyota wa baadae ikiwezekana kuendesha michuano katika shule za msingi na sekondari ili kuwapa morali vijana kujitosa kwenye mchezo huo.
"Kwa kweli TAVA inafanya kazi katika mazingira magumu kwa kutokuwa na wafadhili wala wadhamini, lakini bado naiomba waelekeza nguvu zao kwa vijana toka ngazi za chini ili waje kuchukua nafasi zetu kuendelea mchezo huu," alisema.
Nyota huyo aliyeisadia Mzinga ya Morogoro kutwaa taji la Ligi ya Muungano lililofanyika mjinio Tanga, alisema kadhalika wachezaji na viongozi wa zamani wa mchezo huo wanapaswa kujitokeza kuusaidia uongozi wa sasa katika kuhakikisha wavu inarejesha makali yake.
"Viongozi na wachezaji wa zamani wamejiweka kando, wanapaswa kutoka mafichoni kusaidiana na TAVA kurejesha makali ya mchezo huo," alisema.
***


'Wazee wa Kizigo' wapata meneja


BENDI ya Extra Bongo 'Wazee wa Kizigo', imepata meneja ambaye atabeba jukumu la kusimamia shughuli zote za bendi hiyo ili isonge mbele kufikia malengo ya kuwa matawi ya juu.
Kiongozi wa bendi hiyo Rogert Hegga, alimtaja meneja huyo mpya kuwa ni Mujibu Hamis aliyewahi kuifanya kazi katika bendi za FM Acdeamia na Mashujaa Musica.
Hegga alisema, kwa vile Mujibu ni mzoefu wa kazi hiyo kwa muda mrefu, ana uhakika mchango wake utakuwa mkubwa ndani ya Extra Bongo ambayo inazidi kupanda chati kila kukicha.
"Fitina za muziki anazijua sana na sisi tunaamini kwamba tukiwa naye kwenye bendi yetu ya Extra Bongo tutaendelea kupiga hatua zaidi ili kufikia malengo ambayo tumejiwekea," alisema Hegga.
Alisema, Extra Bongo haikuwa na meneja hali ambayo ilikuwa inachangia baadhi ya shughuli za bendi kukwama na kwamba sasa amempata Mujibu ambaye atatumia uzoefu wake kusimamisha maendeleo ya Extra Bongo.
Katika hatua nyingine kiongozi huyo alisema, Extra Bongo imeanzisha ushirikiano wa maonyesho ya pamoja na vikundi mbalimbali vya burudani ili kujenga urafiki kati ya wanamuziki wake na wasanii wa vikundi hivyo.
Alisema ushirikiano huo ulianza wiki iliyopita kwa kufanya onyesho la pamoja na vikundi vya Baikoko, Kiti Tigo, Werawera na Khanga Moja ambavyo vina umaarufu miongoni mwa mashabiki wa burudani.

Sikinde yabakisha mbili albamu mpya





BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Sikinde' imebakisha nyimbo mbili kabla ya kukamilisha albamu mpya itakayokuwa na nyimbo sita.
Katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo, alisema hadi sasa bendi yao imekamilisha nyimbo nne ambazo zilitarajiwa kutambulishwa jana kwa mashabiki wao katika onyesho maalum la uzinduzi wa vyombo vyao.
Milambo alizitaja nyimbo hizo nne zilizokamilika kuwa ni 'Jinamizi la Talaka', 'Mihangaiko ya Kazi', 'Kinyonga' na 'Deni Nitalipa'.
"Tumekamilisha nyimbo nne ambazo tutazitambulisha kwa mashabiki wetu na mbili za mwisho tayari zimeshaandikwa mashairi ingawa hazijapewa majina yake," alisema Milambo.
Alisema nyimbo hizo za awali zimetungwa na waimbaji wao mahiri akiwemo mkongwe, Hassani Rehani Bitchuka na wengineo.
Tangu ilipopakua albamu ya 'Supu Imetiwa Nazi', Sikinde haijapakua albamu nyingine tena mpya na hivi karibuni iliondokewa na mtunzi na muimbaji wake nguli, Shaaban Dede aliyetua kwa mahasimu wao, Msondo Ngoma ambapo ameshaibuka na nyimbo mbili mpya.
Nyimbo hizo ni 'Suluhu' uliowekwa kwenye albamu mpya ya Msondo na kingine cha 'Vita Dhidi ya Dawa za Kulevya' uliowekwa kiporo kwa albamu ijayo ya bendi hiyo.

Jumbe ahidi Talent kufanya makubwa Kilwa Masoko

MWANAMUZIKI nyota wa bendi ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea', Husseni Jumbe, amejigamba kuwa atafanya makamuzi ya haja kwenye onyesho la bendi yake litakalofanyika Jumatano ijayo mji wa Kilwa Masoko, mkoani Lindi.
Jumbe na bendi yake wanatarajia kwenda kutambulisha albamu yao mpya na ya pili iliyokamilika hivi karibuni katika onyesho litakalofanyika Jumatano ijayo (Juni 29) kwenye ukumbi wa Kilwa PM Resort.
Akizungumza na MICHARAZO, Jumbe, alisema wamepania kwenda kuwapa burudani wakazi wa mji huo kutokana na kwamba hiyo itakuwa ni mara yao ya kwanza kwenda mjini Kilwa.
Alisema katika onyesho hilo Talent itatambulisha albamu yao ya awali ya 'Subiri Kidogo' na ile moya iitwayo 'Shoka la Bucha' ambayo imekamilika hivi karibuni ikiandaliwa kupakuliwa video zake.
"Tumejiandaa vya kutosha kuwapa burudani wakazi wa Kilwa katika onyesho letu la Juni 29, tunaamini tutakidhi kiu ya muda mrefu ya mashabiki wa muziki wa eneo hilo," alisema Jumbe.
Jumbe, alizitaja nyimbo watakazozitambulisha katika onyesho hilo lililoratibiwa na mmiliki wa ukumbi huo, Yohana Miwa, kuwa ni 'Shoka la Bucha', 'Usiku Haulaliki', 'Kiapo Mara Tatu', 'Kilio cha Swahiba' na zile za albamu yao iliyopita ya 'Subiri Kidogo' iliyozinduliwa Novemba, 2010.
Mkongwe wa dansi alisema pia katika onyesho hilo watawapigia mashabiki watakaohudhuria nyimbo za albamu zake binafsi za 'Mapenzi ya Siri' na 'Kwetu ni Wapi', pamoja na vibao alivyowahi kung'ara navyo akiwa na bendi za DDC Mlimani Park na Msondo Ngoma.