STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, April 20, 2012

Shija Mkina achekelea kuitungua Yanga


MFUNGAJI wa bao pekee lililoizamisha na kuitemesha Yanga ubingwa wa Ligi Kuu
Tanzania Bara, Shija Mkina wa Kagera Sugar, amedai kufarijika mno kuitungua timu hiyo.
Mshambuliaji huyo za zamani wa Bandari Mtwara na Simba, alisema ingawa ni kawaida
yake kufumania nyavu, lakini kuifunga Yanga ni faraja kubwa kwake kwa vile imeisaidia timu yake kujihakikishia nafasi ya kusalia kwenye ligi kuu msimu ujao.
Mkina, aliyejiondoa Simba kwa lazima baada ya kushindwa kupewa nafasi na aliyekuwa
kocha wa timu hiyo, Mganda Moses Basena ambaye hayupo kwa sasa katika klabu hiyo,
alisema bao hilo dhidi ya Yanga lilikuwa muhimu kwa timu yake ya Kagera.
"Nashukuru kwa kuweza kufungia timu yao bao muhimu lililotuhakikishia pointi tatu
zinazotufanya tusiwe na hofu ya kushuka daraja," alisema.
Mchezaji huyo, aliyewahi kuwa mfungaji bora alipokuwa na Bandari Mtwara, alisema ligi ya msimu huu ilikuwa ngumu kuliko misimu ya nyuma na ndio maana hadi sasa ni vigumu kujua timu inayoshuka daraja au itakayonyakua ubingwa licha ya Simba kupewa nafasi.
"Naamini ligi zote zingekuwa hivi, basi soka letu lingekuwa lipo juu na klabu zetu kufanya vema kwenye michuano ya kimataifa," alisema Mkina.
Kwa ushindi iliyopata ya Yanga, imeifanya Kagera Sugar kufikisha jumla 26 na ikisaliwa na mechi tatu dhidi ya Toto Afrika inayotarajiwa kucheza kesho mjini Bukoba, Coastal Union watakaoumana nao Aprili 30 mjini Tanga kisha kufunga msimu kwa kuvaana na Azam.

Mwisho

Polisi Moro yaifuata Mgambo Ligi Kuu, vita yabakia kwa Prisons Mbeya, Polisi Dar

WAKATI timu za soka za Mgambo ya Tanga na Polisi Moro zikiwa zimeshajihakikishia
kucheza Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao, vita vya kuwania nafasi hiyo imesalia kwa
timu za Polisi Dar na Prisons ya Mbeya ambazo zitafunga dimba Jumatatu.
Polisi Moro jana ilijihakikishia nafasi ya kupanda daraja baada ya kuilaza Mbeya City mabao 2-0 na kufikisha pointi 17 na kuongoza msimamo wa fainali za Ligi Daraja la Kwanza zinazochezwa kwenye uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro.
Mgambo ilikuwa timu ya pili kupata nafasi hiyo katikati ya wiki baada ya kuilaza Transit Camp mabao 3-0 na kufikisha pointi 15 zinazowaweka nafasi ya pili ya msimamo wa ligi hiyo.
Nafasi ya tatu ya kupanda daraja imesaliwa kwa timu za Polisi Dar ambayo jana ilipata ushindi wa mabao 3-0 mbele ya JKt Mlale ya Songea na kufikisha pointi 10 ikishika nafasi ya nne nyuma ya Prisons ambayo yenye ina pointi 11.
Hata hivyo Prisons Mbeya ambayo ilitarajiwa kushuka dimbani leo jioni ndiyo yenye
nafasi kubwa ya kuchukua nafasi hiyo kutokana na pointi ilizonazo pia kuwa na kiporo
cha mechi moja ya ziada itakayochezwa Jumatatu dhidi ya Polisi Dar.
Iwapo timu hiyo itateleza kwa Rhino au kutoka sare itamaanisha kwamba mechi yao ya Jumatatu dhidi ya 'Vijana wa Kova' itakuwa ni kama fainali katika kuwania
nafasi hiyo moja ya kucheza ligi kuu msimu ujao.
Uongozi wa Polisi Dar kupitia kocha wake, Ngello Nyanjaba, alisema hawajakata tamaa
kupanda ligi kuu, licha ya kuwa na nafasi finyu nyuma ya Prisons ya Mbeya.
"Tunasubiri kuona inakuwaje hadi dakika za mwisho," alisema Nyanjaba.

Msimamo wa Fainali za 9 Bora kabla ya mechi za leo:

TIMU P W D L F A Pts
1. Mgambo Shooting 7 4 3 - 12 3 15
2. Polisi-Moro 7 5 2 - 14 4 17
3. Prisons-Mbeya 6 3 2 1 8 5 11
4. Polisi Dar 7 2 4 1 9 4 10
5. Mbeya City 7 2 2 3 7 8 8
6. Rhino Rangers 7 2 2 3 4 6 8
7. Mlale JKT 7 1 2 4 5 13 5
8. Polisi-Tabora 6 1 2 3 5 11 5
9. Transit Camp 6 - 1 5 2 12 1

Mwisho

Kocha Julio kuweka historia ya aina yake nchini


KOCHA maarufu nchini, Jamhuri Kihwelu 'Julio' anatarajiwa kuweka rekodi ya aina yake
nchini leo atakapokalia benchi za timu mbili tofauti katika pambano moja kati ya Coastal Union ya Tanga anayoifundisha na CDA-Dodoma anayojiunga nayo.
Mchezo huo maalum wa kirafiki kwa timu hizo utachezwa kwenye uwanja wa Jamhuri
mjini Dodoma, ambapo Coastal watautumia kumuaga na CDA kumkarisha kocha huyo
kwa ajili ya kuinoa kwa michuano ya Ligi ya TFF-Taifa inayotarajiwa kuanza hivi karibuni.
Julio aliyeisaidia Coastal kusalia Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya awali kuchechemea, ameodai ameombwa na uongozi wa CDA, timu aliyowahi kuichezea miaka ya nyuma, jambo alilodai ameliafiki kwa moyo mmoja.
Akizungumza kutoka mjini Dodoma, Julio alisema amekubali kuachana na Coastal Union
ili aifundishe CDA klabu iliyomuibua katika maisha yake ya soka na katika mechi ya leo atakaa kwenye benchi za timu zote kwa dakika 45 za kila kipindi.
Kocha huyo mwenye maneno mengi, alisema dakika 45 za awali atakalia benchi la timu
yake ya sasa ya Coastal Union na katika kipindi cha pili atahamia katika benchi la CDA.
"Najiandaa kuachana na Coastal Union na kutua CDA baada ya kufuatwa na viongozi na
Jumamosi timu hizo mbili zitacheza mechi maalum ya kirafiki Coastal ikiniaga na CDA
kunikaribisha na kitakaa kwenye mabechi ya timu zote mbili kwa kila kipindi," alisema.
Julio alisema japokuwa imekuwa ngumu kwa makocha wenye majina kama yeye kukubali
kuzinoa timu za madaraja ya chini, lakini yeye anataka kuisaidia timu hiyo hadi ipande Ligi Kuu Tanzania Bara kuwahamasisha wengine kujitolea kusaidia timu za chini.
Kitendo cha kocha huyo kukaa katika benchi za timu mbili tofauti katika mchezo huo
itamfanya Julio aweke historia ya aina yake nchini, ingawa marehemu Syllersaid Mziray aliwahi kuzifundisha Simba na Yanga kwa wakati tofauti katika michuano ya Kombe la AICC mwishoni mwa miaka ya 1980, iliyokuwa ikifanyika mjini Arusha.

Mwisho

Thursday, April 19, 2012

Rage awatuliza wana Simba kuhusu Ngassa

WAKATI klabu ya soka ya Azam ikikanusha taarifa kwamba winga wao nyota, Mrisho Ngassa kuwa na mipango ya kutua Simba, Mwenyekiti wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage, amewatoa hofu wanachama wa klabu hiyo kwa kuwaeleza 'SUBIRINI TUONE'. Rage, alisema kama Ngassa atatua Msimbazi au la, litafahamika baada ya kumalizika kwa Ligi Kuu Tanzania Bara, ila kwa sasa ni mapema mno kulizungumzia hilo. "Kama wao wamekanusha kwamba huyo mchezaji atakuja Simba, basi subirini, ila kwa sasa ni vigumu kuanza kulisemea hilo wakati hatujui mkataba wa Ngassa na klabu yake ukoje," alisema Rage. Mwenyekiti huyo mwenye 'kismati' na klabu hiyo ya Simba, alisema kuanza kumzungumzia Ngassa kabla hawajawasiliana na uongozi wa Azam ni kwenda kinyume na sheria za FIFA, ila amesisitiza watu wasubiri kujua ukweli wa mambo. Juzi chombo kimoja cha habari kiliripoti taarifa kwamba Simba inakaribia kumnyakua Ngassa kwa ajili ya kuichezea timu hiyo kwenye michuano ya kimataifa, hiyo itafanyika iwapo Simba itafuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho-Afrika. Hata hivyo Azam kupitia msemaji wake, Jaffer Idd Maganga, alisema hakuna kitu kama hicho na wanashangaa uzushi huo. "Hakuna kitu kama hicho, Simba haijawahi kutufuata kutueleza jambo hilo, wala Ngassa, pia mchezaji huyu bado ana mkataba na klabu hiyo ni ajabu kusikia kwamba anataka kwenda Simba, kivipi?" alihoji msemaji huyo. Hata hivyo suala la Ngassa kutua Simba lilitajwa tangu mchezaji huyo alipoihama Yanga na kutua Azam, ambapo ilielezwa ilikuwa janja ya kumvuta mchezaji huyo kutua Msimbazi na hasa alipokuwa akitafutiwa nafasi ya kucheza soka la kulipwa.
Mrisho Ngassa (kushoto) akiwajibika uwanjani na timu yake ya Azam. Hapa alikuwa akichuana na aliyekuwa mshambuliaji wa Simba, Mussa Hassani Mgosi ambaye kwa sasa anacheza soka la kulipwa DR Congo.

Villa Squad mambo bado magumu

LICHA ya kufurahia ushindi wa mabao 4-2 iliyopata timu yao dhidi ya Coastal Union ya Tanga, iliyofufua matumaini ya kusalia Ligi Kuu Tanzania msimu ujao, uongozi wa klabu ya Villa Squad umedai mambo bado magumu kwao na kuomba msaada zaidi. Katibu Mkuu wa Villa, Frank Mchaki, alisema bado wanahitaji msaada wa hali na mali ili kuisaidia timu yao katika maandalizi ya mechi zake zilizosalia ili kuweza kujihakikishia nafasi ya kusalia ligi kuu msimu ujao. Mchaki, alisema japo ushindi wao wa mwishoni mwa wiki umewaongezea tumaini jipya la kujinusuru kushuka daraja, lakini ni vigumu kujihakikishia jambo hilo kulingana na ukaribu wa pointi uliopo baina ya timu zilizopo chini katika msimamo wa ligi hiyo. "Tunashukuru kupata ushindi ambao umefufua matumaini yetu ya kusalia ligi kuu, ila bado tuna kazi ngumu na tunahitaji wadau wa soka watusaidie kwani kiuchumi tuna hali mbaya huku tukikabiliwa na mechi ngumu za kumalizia msimu," alisema Mchaki. Mchaki alisema anaamini timu yao ikisaidiwa kwa hali na mali itajiandaa vema kwa mechi tatu zilizosalia ambazo kama wakizishinda zote zitawafanya wasalie kwenye ligi hiyo. Villa, iliyorejea ligi kuu msimu huu ikitokea Ligi Daraja la Kwanza kwa ushindi iliyopata dhidi ya Coastal imewafanya wafikishe pointi 22 ikiwa nafasi ya 12 huku ikisaliwa mechi dhidi ya timu za African Lyon itakayocheza nao keshokutwa jijini Dar, kishaa kuvaana na JKT Oljoro kisha Ruvu Shooting watakaofunga nao dimba la msimu huu.

Kinyogoli aandaa tamasha la ngumi

NYOTA wa kimataifa wa zamani wa ngumi nchini, Habib Kinyogoli kupitia taasisi yake ya Kinyogoli Foundation, inatarajiwa kuendesha michuano maalum ya ngumi iitwayo 'Top Ten Boxing Festival-2012' litakaloanza rasmi Mei 4, jijini Dar es Salaam. Michuano hiyo itakayoshirikisha mabondia wa ngumi za aina zote yaani za ridhaa na kulipwa itafanyika kwenye ukumbi wa Panandi Panandi kwa ajili ya kuibua na kuendeleza vipaji vya mchezo huo kwa kusaka wakali 10 wa kila uzito katika ngumi hizo. Akizungumza na MICHARAZO, Msaidizi wa Kinyogoli, Rajabu Mhamila 'Super D' alisema mabondia na klabu zinazotaka kushiriki michuano hiyo wanatakiwa kujiandikisha mapema kabla ya kuanza kwake akidai itakuwa ikichezwa hadi kupatikana wakali hao. Super D, alisema ameamua kubuni 'ligi' hiyo kwa lengo la kuleta mabadiliko katika mchezo wa ngumi kwa kuibua vijana watakaoisaidia taifa kwa michuano ya kimataifa. Naye Kinyogoli maarufu kama Master, alisema ameamua kuanzisha michuano hiyo katika kuendeleza juhudi zake za kukuza ngumi ambazo zilikwama miaka ya nyuma. "Japo michuano hii itaonekana kama mipya, lakini ni kama wazo nililolibuni miaka 30 iliyopita niliposaidia kuibua vipaji vilivyokuja kutanza nchini kama akina Matumla na wengine," alisema Kinyogoli. Alisema, anaamini michuano hiyo itakapokamilika itasaidia kuibua nyota wapya na kuvihimiza vyama na wadau wa ngumi kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya kushuhudia mchuano sambamba na kuwapiga tafu wale watakaofanya vema kwa faida ya taifa.
Kocha wa ngumi, Rajabu Mhamila 'Super D' msaidizi wa nyota wa zamani wa ngumi nchini, Habib Kinyogoli 'Master' wanaoandaa ligi maalum ya mchezo huo itakayoanza Mei 4.

Mashale awataka Maugo, Cheka

BAADA ya kutwaa ubingwa wa taifa wa TPBO, bondia Thomas Mashale amesema sasa yupo tayari kupigana ama Mada Maugo au Francis Cheka kwa nia ya kuanza kusaka mataji yanayotambuliwa kimataifa. Akizungumza na MICHARAZO, Mashale alisema kwa kuwa mabondia hao wawili ndio walio kwenye viwango vya hali ya juu kwa sasa katika uzani wa kati ni vema akapata fursa ya kupigana ili kuanza mbio zake za kusaka ubingwa wa Dunia. "Kwa sasa natamani kupigana na bondia yeyote kati ya Cheka au Maugo ambao wanatarajiwa kupigana hivi karibuni, lengo ni kutaka kuanza mchakato wa kusaka mataji ya kimataifa," alisema. Alisema kati ya mabondia hao haoni wa kumtisha hasa baada ya kupata uzoefu wa kutosha katika michezo yake mbalimbali aliyocheza tangu aingie kwenye mchezo huo. Mashale, alisema cha muhimu anachoombea kwa sasa ni kupatikana promota wa kumuandalia pambano kati ya mmoja wa mabondia hao ambao wanacheza wote kwenye uzani mmoja wa Middle. Kuhusu ushindi wake alioupata wiki iliyopita dhidi ya Seleman Said 'Galile' Mashale, alisema ulitokana na kufanya vema katika raundi saba za awali na kukiri kwamba mpinzani wake ni mzuri na alimpa usumbufu mkubwa. Alipoulizwa kama yupo tayari kurudiana na Galile, Mashale alisem yu radhi iwapo mpinzani wake huyo atakuwa hajaridhika na matokeo ya ushindi wake uliokuwa wa pointi baada ya kuonyeshana umwamba katika pambano la raundi 10.
Bondia Thomas Mashale 'Simba wa Teranga', akiwa na taji lake la TPBO, mara baada ya kumpiga kwa pointi Seleman Said Galile. Kwa sasa bondia huyo anamtaka kati ya Mada Maugo au Francis Cheka ili apigane nao.

Barcelona yaleteza darajani, yadungwa 1-0

Didier Drogba akishangilia bao lake la pekee lililoisaidia Chelsea kuizima Barcelona kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya mechi iliyochezwa usiku wa kuamkia leo.
BAO lililoifungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Ivory Coast, Didier Drogba dakika za lala salama kabla ya mapumziko ilitosha kuisaidia Chelsea kuizima Barcelona ya Hispania katika pambano la kwanza la nusu fainali baina yao lililochezwa Uingereza.
Drogba alifunga bao hilo pekee dakika ya pili ya dakika za majeruhi baada ya kutimu dakika 45 za kipindi cha kwanza kwenye Uwanja wa Stamford Bridge, London, England Licha ya Barcelona ambao ndio mabingwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa sasa kucharuka katika kipindi cha pili, ilijikuta ikishindwa kurejesha bao hilo hadi pambano lilipomalizika.
Kwa ushindi huo, Chelsea sasa inahitaji sare yoyote kwenye mechi ya marudiano ugenini, Uwanja wa Camop Nou ili kutinga fainali, ambako itacheza na mshindi kati ya Bayern Munich ya Ujerumani na Real Madrid ya Hispania.
Mechi ya kwanza ya kwanza baina ya timu hizo mbili wenyeji Bayern Munich waliitungua Real Madrid mabao 2-1, hivyo Real inahitaji ushindi wa bao 1-0 kama inataka kutinga fainali.

Mgambo Shooting yatinga Ligi Kuu Tanzania Bara, Prisons, Polisi Moro zanusa

TIMU ya soka ya maafande wa Mgambo Shooting ya Tanga imekuwa timu ya kwanza kutinga Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya jana kuisasambua Transit Campo ya Dar kwa mabao 3-0.
Mgambo inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa, ilipata ushindi huo uliowaingiza Ligi Kuu ikiifuata Coastal Union kwenye pambano lililochezwa kwenye uwanja wa Jamhuri, Mjini Morogoro kunakofanyika fainali za 9 Bora ya Ligi Daraja la Kwanza.
Katika mchezo huo Mgambo ilipata mabao yake kupitia kwa washambuliaji wake, Juma Mwinyimvua aliyefunga mabao mawili katika dakika za 16 na 37 na Nassoro Gumbo aliyefunga kwenye muda wa nyongeza za mchezo huo.
Kwa ushindi huo Mgambo imefikisha jumla ya pointi 15 ambazo haziwezi kufikiwa na timu nyingine ukiondoa Polisi Moro ambao nao wanainyemelea nafasi ya kucheza ligi hiyo msimu ujao.
Katika pambano jingine lililochezwa jioni kwenye uwanja huo, mabingwa wa zamani wa Tanzania, Prisons-Mbeya ilinusa kufuzu ligi kuu msimu ujao baada ya kuicharaza Polisi-Tabora mabao 3-0
Mabao ya Prisons waliofikisha pointi 11 kwa ushindi huo wa jana, yalifungwa na John Mtai aliyefunga mawili na jingine kutumbukizwa kimiani na Peter Michael katika dakika ya nne ya mchezo huo uliochezeshwa vizuri na Shabaan Shata wa Kigoma.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena mchana wa leo kwa mechi kati ya Polisi Moro dhidi ya Mbeya City kabla ya JKT Mlale ya Songea kuumana na Polisi Dar.

Msimamo kamili wa Ligi hiyo ya 9 Bora hadi sasa ni kama ifuatavyo;


MSIMAMO WA 9 BORA LIGI DARAJA LA KWANZA

P W D L F A Pts
1. Mgambo Shooting 7 4 3 - 12 3 15
2. Polisi-Moro 6 4 2 - 12 4 14
3. Prisons-Mbeya 6 3 2 1 8 5 11
4. Mbeya City 6 2 2 2 7 6 8
5. Rhino Rangers 7 2 2 3 4 6 8
6. Polisi Dar 6 1 4 1 6 4 7
7. Mlale JKT 6 1 2 3 5 10 5
8. Polisi-Tabora 6 1 2 3 5 11 5
9. Transit Camp 6 - 1 5 2 12 1

Mwisho

Yanga yatemeshwa taji, Simba kidogo kulibeba jumla




KIPIGO cha bao 1-0 ilichopewa na Kagera Sugar jana kwenye uwanja wa Kaitaba, umeifanya Yanga kulitema taji la ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Yanga iliyokuwa watetezi wa taji hilo ilikumbana na kipigo hicho ikiwa ni cha pili ndani ya siku tatu, baada ya awali kufungwa mabao 3-2 na Toto Afrika jijini Mwanza na kuwafanya wasalie na pointi 43 na michezo mitatu ambayo hata ikishinda yote haiwezi kuzifikia pointi za watani zao, Simba wanaojiandaa kulitwaa taji hilo.
Bao lililoizamisha Yanga lilitumbukizwa wavuni na Shija Mkina na kukatisha ndoto za Yanga ambao walikuwa wakisubiri pointi zao walizopokwa na Kamati ya Mashindano ya TFF kutokana na rufaa waliyokata ambayo imetupiliwa mbali na Kamti ya Nidhamu na Usuluhishi ya Alfred Tibaigana.
Wakati Yanga ikitota Kagera na kuweka rekodi na kupoteza pointi sita katika Kanda ya Ziwa kwa mara ya kwanza, watani zao Simba jana walitakata uwanja wa Taifa baada ya kuinyoa JKT Ruvu mabao 3-0.
Ushindi uliifanya Simba ifuzu kucheza michuano ya CAF msimu ujao baada ya kujihakikishia kumaliza katika moja ya nafasi mbili za juu kutokana na kufikisha pointi 56 ambazo haziwezi kufikiwa na Yanga.
Azam yenye pointi 50 huku ikiwa na mechi moja mkononi, itaikaribisha Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Chamazi Jumamosi.
Simba ilianza kuhesabu goli la kwanza katika dakika ya kwanza ya mchezo kupitia kwa kiungo Uhuru Selemani aliyefunga kwa kichwa akiunganisha krosi ya Mganda Emmanuel Okwi na kiungo kipenzi cha mashabiki wa Simba, Haruna Moshi 'Boban' akafunga moja ya mabao bora ya msimu wakati alipokimbia na mpira kutokea katikati ya uwanja na kupiga shuti lililomshinda kipa Amani Simba wa JKT katika dakika ya 17.
Kiungo wa timu ya taifa, Taifa Stars, Mwinyi Kazimoto alifunga goli la 'kideoni' katika dakika ya 64 na kuisogeza Simba jirani zaidi na ubingwa.
Matokeo mengine ya ligi hiyo kwa jana, Ruvu Shootingi ilishinda 1-0 dhidi ya Moro United, bao lililotumbukizwa wavuni na Saleh Kitala dakika ya 90, huku Toto wakiendeleza wimbi la ushindi kwa kuicharaza African Lyon mabao 2-0.
Nao watoto wa Julio, Coastal Union, ilizinduka baada ya kichapo cha aibu cha mabao 4-2 toka kwa Villa Squad kwa kuitandika Polisi Dodoma mabao 3-l.
Kipigo hicho kimezidi kuiweka pabaya Polisi Dodoma kwani sasa ni kudra za Mungu tu ndizo zinazoweza kuinusuru isishuke daraja kurejea Ligi Daraja la Kwanza.

TIBAIGANA AICHINJA YANGA



Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Aprili 17 mwaka huu) imetupa rufani ya Yanga iliyowasilishwa mbele yake kupinga uamuzi wa kupokwa pointi tatu kwa kumchezesha mchezaji asiyestahili.
Aprili 2 mwaka huu Kamati ya Ligi ya TFF iliipa Coastal Union ushindi wa pointi tatu na mabao matatu baada ya Yanga kumchezesha beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya timu hizo iliyofanyika Machi 31 mwaka huu wakati akiwa na adhabu ya kukosa mechi tatu.
Yanga katika rufani hiyo iliwasilisha sababu nane za kupinga kupokwa pointi hizo, kubwa zikiwa Cannavaro hakustahili kutumikia adhabu ya kukosa mechi tatu, si aliyempiga refa Israel Nkongo, ripoti za refa na kamishna wa mechi yao dhidi ya Azam zilionesha dalili ya njama (conspiracy) kwani zilifanana.
Pia Cannavaro alikuwa miongoni mwa wachezaji ambao adhabu zao zilisimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu, Kamishna mstaafu wa Polisi, Alfred Tibaigana.
Katika uamuzi wake, Kamati imesema adhabu ya Cannavaro ya kukosa mechi tatu kwa mujibu wa Kanuni ya 25(c) ya Ligi Kuu ya Vodacom ilitolewa na refa na si Kamati ya Ligi kama ambavyo inalalamikiwa na Yanga, na kanuni hiyo haikatiwi rufani.
Pia barua ambayo TFF iliiandikia Yanga kuhusu adhabu ya mchezaji huyo ilikuwa wazi kwani ilikariri kanuni ya 25(c), hivyo kitendo cha klabu hiyo kumtumia mchezaji huyo ulikuwa ni uzembe wa kutoheshimu kanuni. Kama Yanga haikufahamu vizuri kanuni hiyo ilikuwa na fursa ya kuiandikia TFF kwa mujibu wa Kanuni ya 25(f) ili kupata ufafanuzi kabla ya kuamua kumtumia mchezaji huyo.
Vilevile adhabu zilizokuwa zimesimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu ni zile ambazo zilikuwa zimetolewa na Kamati ya Ligi, na si zile zilizotolewa uwanjani na refa.
Kuhusu madai ya conspiracy kwa ripoti za kamishna wa mchezo huo na refa, Kamati imebaini kuwa hazifanani, na suala lililokuwa likibishaniwa (contentious issue) lilikuwa ni kunyang’anywa pointi tatu.
Pia Kamati ilikariri Ibara ya 50 ya Kanuni za Nidhamu za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kuwa mchezaji anayembughudhi refa kwa njia yoyote ile anastahili kufungiwa kwa angalau mechi sita.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Saturday, April 7, 2012

MAMIA WAFURIKA MSIBA WA STEVEN KANUMBA





MEYA wa Manispaa ya Kinondoni na Ilala, Yusuf Mwenda na Jerry Slaa ni miongoni
mwa viongozi waliojitokeza kwenye msiba wa nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba aliyefariki juzi usiku nyumbani kwake baada ya kuanguka katika mzozo na mpenzi wake.
Aidha umati mkubwa ulijitokeza kwenye msiba wa msanii huu uliopo nyumbani kwake
Sinza Vatican, jana ulisababisha msongamano mkubwa kiasi cha kuziba barabara ya
Makanya na kuwalazimisha askari polisi kufanya kazi ya ziada kuweka mambo sawa.
MiCHARAZO lililokuwepo msibani hapo, liliwashuhudia mameya hao na viongozi wengine kama Katibu wa Kamati ya Uchumi na Fedha CCM-Taifa, Mwigulu Nchemba na Diwani wa Kata ya Sinza, Renatus Pamba wakiwa na nyuso za huzuni wakitoa pole zao.
Viongozi hao kila mmoja alikuwa akiwapa pole wasanii waliofanya kazi na Kanumba
pamoja na watu wengine kabla ya baadhi yao kuondoka na kuwaacha mamia ya watu
wakiwemo wasanii nyota wa filamu wakiendelea na msiba huo.
Kutokana na wingi wa watu waliojitokeza kwenye msiba huo, iliwalazimisha waratibu wa msiba huo, kuwahamishi waombelezaji hao kwenye ukumbi wa Vatican Hoteli, huku wakiwazuia wengine kuingia ndani na kuleta tafrani za hapa na pale.
Mratibu wa Bongo Movie, Steven Mengele 'Steve Nyerere' alisema waliamua kuhamishia watu hotelini hapo kutokana eneo la nyumba ya marehemu Kanumba kutotosha kwa wingi wa waombolezaji waliojitokeza waliosababisha msongamano mkubwa.
Msongamano huo wa waombelezaji ulisababisha hata magari yanayotumia barabara ya
Makanya kushindwa kupita vema na kuwapa kazi ya ziada askari polisi wa kawaida na
wale wa barabarani kuyaongoza magari hayo.
Wasanii mbalimbali walikielezea kifo cha Kanumba kama pengo litakalochukua muda
mrefu kuziba katika tasnia ya sanaa hasa uigizaji wa filamu ambayo marehemu aliifanya kwa muda mrefu wa maisha yake tangu akiwa shuleni.
Mayasa Mrisho anayefanya kazi nyingi na Kanumba, alisema mpaka sasa haamini kama
Kanumba kafariki kwa namna kifo chake kilivyokuwa cha ghafla.
'Siamini, kama ni kweli Kanumba kafa," alisema huku akilia. Aliongeza Kanumba
amefariki wakati wakitoka kumalizia kazi yao mpya iitwayo 'Mr Price', huku pia
wakijiandaa kuingiza sokoni filamu yao mpya iitwayo 'Ndoa Yangu'.
Wasanii wengine kama Patcho Mwamba, Rajabu Jumanne 'Chilli', Issa Kipemba, Fatuma Makongoro 'Bi Mwenda' walisema itawachukua muda mrefu kumsahau mwenzao ambaye alikuwa mtu wa watu, asiye na makuu licha ya umaarufu mkubwa aliokuwa nao.
Nalo Baraza la Sanaa la Taifa, kupitia Katibu Mkuu wake, Ghonce Materego, walitoa
salamu za rambirambi kutokana na kifo hicho cha Kanumba wakidai kimeshtua na
kuwaachia pengo kubwa katika fani ya sanaa nchini.
"BASATA inaungana na familia za wafiwa na wasanii wote nchini kwa maombolezo ya msiba huu mkubwa na wa kihistoria. Kufiwa na msanii huyu mahiri kwenye tasnia ya filamu ni pengo kubwa kwa familia, Sekta ya sanaa na Taifa kwa ujumla kutokana na
ukweli kuwa, aliweza kuutangaza utamaduni na sanaa yetu nje ya mipaka," sehemu ya
rambirambi hiyo ya Basata inasomeka hivyo.
Steven Charles Kanumba, aliyezaliwa Januari 8, 1984 huko Shinyanga, alifariki usiku wa kuamkia jana kwa kile kinachoelezwa alisukumwa na kuanguka sakafuni na aliyekuwa
mpenzi wake, Elizabeth Michael 'Lulu' ambaye kwa sasa anashikiliwa na jeshi la Polisi.
Msanii huyo, aliyesoma Shule ya Msingi Bugoyi na Shule za Sekondari Mwadui, Dar
Christian Seminary na Jitegemee kabla ya kuanza kutamba kwenye sanaa kupitia kundi la Sanaa alilojiunga nalo mwaka 2002 hadi 2006 alipojiengua na kucheza filamu mbalimbali.
Baadhi ya kazi zake ni 'She is My Sister', 'Dar to Lagos', 'Cross My Sin', 'The Director', 'Hero of the Church', Sikitiko Langu, Dangerous Desire, Dar to Lagos, Cross My Sin, Village Pastor, Family Tears, Unfortunutes Love, My Valentine, The Shock, Deception na kazi ya mwisho kuitoa sokoni ni 'Kijiji Chatambua Haki'.

mwisho

SIMBA YATAKATA AFRIKA, LICHA YA KIPIGO YAFUZU 16 BORA KOMBE LA SHIRIKISHO




ANGURUMAPO SIMBA MCHEZA NANI? HAKUNAGA! Ndivyo tunavyoweza kusema baada ya klabu ya soka ya Simba kupenya kwenye hatua ya 16 Bora ya KOmbe la Shirikisho Afrika, licha ya kipigo cha mabao 3-1 ilichopewa usiku wa kuamkia leo na Entente Sportive de Setif ya Algeria.
Ikicheza wachezaji 10, Simba iliweza kupigana hadi dakika za nyongeza kupata bao pekee la kufutia machozi lililokuwa na faida kubwa kwao, kuwavusha hatua hiyo wakiwaduwaza waarabu wasiamini kilichowakuta baada ya kuamini wamemng'oa mnyama.
Shujaa wa Simba katika pambano hilo lililochezeshwa na waamuzi kutoka Tunisia alikuwa ni Mganda, Emmanuel Okwi aliyefunga katrika dakika ya 92 na kuifanya timu yake isonge mbele kwa faida ya bao la ugenini kutokana na matokeo ya jumla kuwa mabao 3-3.
Simba katika pambano lao la awali lililochezwa kwenye uwanja wa Taifa, Machi 25, ilishinda mabao 2-0 na hivyo kwa sare hiyo wamevuka kwa matokeo ya kuwa mabao 4-3.
Beki wa kutumainiwa wa Simba Juma Said Nyosso alitolewa uwanjani mapema baada ya kulimwa kadi nyekundu kwa kuonyesha ubabe uwanjani dhidi ya mshambuliaji wa Setif.
Wenyeji walitumia mwanya wa kutolewa kwa Nyosso kupachika bao la kuongoza lililofungwa dakika ya 34 na Mohammed Aoudia na kurejea kipindi cha pili kwa kasi kwa kufunga bao jingine kupitia mshambuliaji huyo mkali.
Bao la tatu la Setif, iliyokuwa ikiyotawala vipindi vyote viwili, ingawa juhudi zao za kuvuna mabao mengi zilizimwa na kipa Juma Kaseka, lilifungwa katika dakika ya 52 kupitia kwa Mokhtar Benmoussa.
Baada ya kupata mabao hayo Setif ilirejea nyuma na kulinda bao wakiamini wameshamaliza kazi kabla ya Okwi kuwaduwaza baada ya kuwachambua mabeki wa timu hiyo kisha kufumua shuti kali la mbali lililomshinda nguvu kipa wa Setif na kutinga wavuni.
Kwa ushindi huo, Simba sasa itakutana na mshindi kati ya Ferroviário Maputo ya Msumbiji au Al Ahly Shendi ya Sudan ambazo zinatarajiwa kuumana kesho Jumapili, huku timu ya Sudan ikiwa na faida ya bao moja iliyopata katika mechi yao wiki mbili zilizopita ilipowafunga wenyeji wao bao 1-0.
Katika mchezo wa jana kikosi cha Simba kilichoaanza dhidi ya ES Setif kiliwakilishwa na Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Amir Maftah/Said Nassoro 'Chollo' , Juma Nyoso, Kelvin Yondani, Patrick Mafisango, Salum Machaku, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi 'Boban' na Emmanuel Okwi.

PICHA ZA BAADHI YA KAZI YA NDOA YANGU, MOJA YA FILAMU ZA MWISHO ZA KANUMBA INAYOTARAJIWA KUINGIA SOKONI KARIBUNI





ZA LEO LEO

BREAKING NEWS: STEVEN KANUMBA 'THE GREAT' IS NO MORE




MUIGIZAJI nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba, 28, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo nyumbani kwake Sinza Vatican, jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa habari za kuaminika na kuthibitishwa na rafikie wa karibu, Patcho Mwamba, Kanumba alifariki nyumbani kwake baada ya kuanguka akitokea bafuni kutokana na kuteleza.
Chanzo hicho kinasema kwamba Kanumba alianguka baada ya kusukumwa na mpenzi wake (jina tunalo) aliyekuwa akizozana nae badaa ya kupishana kiswahili.
"Brother Kanumba kafariki usiku wa kuamkia leo na maiti yake kwa sasa ipo Mumhimbili, ikisubiri taratibu za mazishi, ni kama utani ila ndio hivyo. Alisukumwa na kuangukia kisogo na kufariki papo hapo," chanzo hicho kilisema.
Aliongeza kwa sasa walikuwa wakiwasiliana na mama yake ambaye inadaiwa yupo Bukoba pamoja na familia yake iliyopo Shinyanga kujua taratibu za mazishi yake.
Patcho Mwamba alipoulizwa juu ya kifo cha Kanumba, alithibitisha lakini hakuweza kuweka bayana chanzo zaidi ya kusisitiza kuwa alianguka sakafuni nyumbani kwake na kufariki akiwahishwa Muhimbili, ambako kwa sasa mwili wake umehifadhiwa.
Steven Charles Kanumba alizaliwa Januari 8, 1984 mkoani Shinyanga akiwa ni mmoja kati ya watoto wa nne wa mzee Charles Kanumba.
Alisoma Shule ya Msingi Bugoyi, huko huko Shinyanga kabla ya kuendelea na masomo ya Sekondari katika Shule ya Mwadui, kisha kuhamia Shule ya Dar Christian Seminary, alipohitimu kidato cha nne. Baadaer alijiunga na masomo ya juu ya Sekondari na kumaliza Kidato cha Sita katika Shule ya Jitegemee, ambapo tayari alishaanza kujishughulisha na sanaa kupitia kundi la Kaole Sanaa alilotamba nalo na michezo mbalimbali iliyokuwa ikionyesha kwenye kituo cha ITV.
Baadae aliamua kujiengua katika kundi hilo na kucheza filamu akishirikiana na wasanii wenzake, Blandina Chagula 'Johari' na Vincent Kigosi 'Ray'.
Hadi anafariki msanii huyo alikuwa ni Muigizaji, Mtunzi, Mtayarishaji na muongozaji, akimiliki kampuni ya Kanumba the Great Films ambayo ilikuwa ikizalisha filamu na kuibua wasanii wengi chipukizi.
Marehemu alikuwa hajaoa wala kuwa na mtoto. Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema.

Thursday, January 19, 2012

'Ajuza' afyatua kibao na Mhe Temba




UNAWEZA kudhani ni utani, ila ukweli ni kwamba msanii chipukizi lakini mwenye umri mkubwa wa zaidi ya miaka 50, Mwanahija Cheka 'Bi Cheka' amefyatua kibao kipya cha miondoko ya kizazi kipya akishirikiana na nyota wa miondoko hiyo nchini, Mheshimiwa Temba.
Meneja wa msanii huyo, Said Fella, alisema kibao cha Bi Cheka kiitwacho 'Ni Wewe', kimerekodiwa katika studio za Poteza Records, chini ya utayarishaji wa Suleiman Daud 'Sulesh' au 'Mr India'.
Fella, alisema tofauti na umri wake wa miaka 51, Bi Cheka 'amechana' mno katika kibao hicho, kiasi kwamba hata Mheshimiwa Temba alimvulia kofia wakati wakirekodi.
"Huwezi amini, hajawahi kuimba kokote zaidi ya kuimba kaswida alipokuwa chuo, akimtaja mkongwe wa muziki wa dansi nchini, Maalim Muhidin Gurumo ndiye aliyekuwa mwalimu wake, lakini kazi kubwa aliyofanya kwenye wimbo huo mpya inashangaza," alisema Fella.
Aliongeza, ndani ya kibao hicho Bi Cheka anamlilia Temba awe wake kimapenzi, huku Temba akijaribu kumtolea nje kitu kilichoufanya wimbo huo kuwa wa kusisimua ambapo wanatarajia kuusambaza katika vituo vya redio kwa ajili ya kurushwa hewani.
Fella alisema mbali na kujipanga kuusambaza wimbo huo, pia wameanza maandalizi ya kufyatua video yake, huku wakiendelea kumrekodiwa nyimbo nyimbo kwa ajili ya albamu yake ambayo alisema huenda ikawa na nyimbo nane au kumi.
"Video ya kibao hicho ambacho Bi Cheka ameimba hip hop na kuchana mistari kama Da Brat (msanii nyota wa miondoko hiyo wa nchi ya Marekani), tunatarajia kuanza kurekodi wakati wowote kuanzia sasa," alisema Fella.
Fella, alisema msanii huyo aliwasiliana nae kumuomba amsaidie kumtolea kazi baada ya kusikia ana kituo cha kukuza na kuendeleza vipaji, ingawa alisitiza awali kwa umri alionao, lakini alimsihi ampe nafasi na mwenyewe ameridhika nae kwa uwezo mkubwa wa kuimba na upangiliaji wa sauti alionao.

Dar Modern kuzindua tatu kwa mpigo



KUNDI linalokimbiza kwenye miondoko ya mwambao nchini, Dar Modern Taarab 'Wana wa Jiji' wanatarajia kuzindua kwa mpigo albamu zao tatu mpya katika onyesho litakalofanyika mwezi ujao jijini Dar es Salaam.
Albamu hizo tatu za kundi hilo ni 'Sikukuchagua kwa Mapesa', 'Ndugu wa Mume Mna Hila' na 'Toto la Kiafrika' ambazo kila moja ina nyimbo nne.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Mkurugenzi wa kundi hilo, Mridu Ally Mridu 'Tx', alisema uzinduzi huo utafanyika mwishoni mwa Februari, mara baada ya kuwasili kwa kanda za kaseti za albamu hizo ambazo zinatengezwa kwa sasa nchini Kenya.
Mridu, alisema uzinduzi wao wamepanga kuufanya katika ukumbi wa Hoteli ya Travertine-Magomeni ama Diamond Jubilee yote ya jijini Dar es Salaam.
"Tupo katika mipango ya kufanya uzinduzi wa albamu zetu tatu kwa mpigo utakaofanyika ama Travertine au Diamond. Kwa sasa tunasubiri kaseti za albamu hizo zinazotengenezwa Kenya, kuwasili nchini ili tupange tarehe rasmi ya kufanyika kwa uzinduzi huo, ila utafanyika mwishoni mwa Februari," alisema.
Mridu alisema katika onyesho hilo la uzinduzi watawatambulisha wasanii wao wapya waliowanyakua hivi karibuni katika kuliimarisha kundi lao ambalo liliondokewa na mastaa wao kadhaa akiwemo Hammer Q, Hashim Said 'Big Sound' na wengineo.
Pia alisema mbali na kuzindua albamu mpya kwa kupiga nyimbo 12 za albamu hizo, pia watakumbushia nyimbo za albamu zao za zamani kama 'Ni Vijimambo Tu', 'Sote Twasaka Riziki', 'Kitu Mapenzi' na 'Gharika ya Moyo' maarufu kama 'Pembe la Ng'ombe'.
"Yaani itakuwa full burudani kwa namna tukavyowapa mashabiki wetu vitu mchanganyiko, kuanzia vile vya awali hadi hivyo vipya pamoja na kuutambulisha mtindo wetu mpya wa kunengua," alisema Mridui.
Kundi hilo la Dar Modern lilianzishwa rasmi mwaka 2006 likiundwa na wasanii mchanganyiko waliotoka kundi la Babloom Modern Taarab na mengine ya jijini Dar es Salaam.

Asilimia 80 ya waandishi wa habari hawajaajiriwa

RAIS wa Umoja wa Vilabu vya Waandishi wa Habari (UTPC), Kenneth Simbaya, amesema zaidi ya asilimia 80 ya waandishi wa habari nchini hawajaajiriwa na hawana mikataba ya aina yoyote ya kazi na wamiliki wa vyombo vya habari, licha ya kwamba wanafanya kazi katika mazingira magumu .
Simbaya aliyasema hayo jana, baada ya kutembelea Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoani Kilimanjaro (MECKI) na kuzungumza na wajumbe wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo iliyopo mjini Moshi.
Alisema utafiti uliofanywa na UTPC, umebaini zaidi ya asilimia 80 ya waandishi wa habari hapa nchini wanajitegemea kutafuta habari katika maeneo ya mjini na vijijini na hata kwenye maeneo ya hatari bila kuajiriwa ama kuwa na mikataba na wamiliki wa vyombo wanavyovifanyia kazi.
Alisema mwandishi pia amekuwa akilipwa ujira mdogo wa Sh. 5,000 na 3,000 hadi Sh. 1,500 kwa habari moja inayotoka gazetini, licha ya gharama kubwa anazotumia kutafuta habari hizo na kuwafikishia wenye vyombo vya habari.
Alisema kutokana na tatizo hilo kuwa kubwa, UTPC inafanya jitihada za makusudi kuwasiliana na wamiliki wa vyombo vya habari ili kuangalia namna waandishi wa habari wanakuwa na mikataba ya ajira kazini na hata kuendelezwa kitaaluma pindi wanapokuwa kazini kwa muda mrefu.
Alisema UTPC pia inakusudia kuanzisha vyombo huru vya habari yakiwemo magazeti, redio na televisheni, vitakavyowawezesha waandishi wa habari kuwa na vyombo vyao vinavyotumia habari sahihi na zilizofanyiwa utafiti na uchunguzi wa kina bila upendeleo.
Alitoa wito kwa waandishi wa habari pamoja na kufanyakazi katika mazingira magumu nay a hatari, kuzingatia maadili ya kazi zao na kuepuka kutumiwa na baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari kwa malengo yao binfsi.
Hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, alisema waandishi wengi wa habari wamekuwa wakifanya kazi kubwa na hata kuhatarisha usalama wa maisha yao, lakini hawalipwi mishahara kulingana na kazi wanazozifanya na badala yake wamegeuka kuwa ombaomba .
Mkuu huyo wa mkoa alisema waandishi wengi wamekuwa wakiishi kwa njia za kiujanja ujanja ili kusukuma maisha yao.

NB:Imeandikwa na Jackson Kimambo, NIPASHE-Moshi

Wednesday, January 18, 2012

Madame V awakumbuka wajane, yatima




MSANII mahiri wa muziki wa Zouk, ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Geita, Vicky Kamata amejitosa kwenye huduma za kijamii akiunda asasi yake binafsi inayoshughulikia kuwasaidia wajane, yatima na wasiojiweza.
Akizungumza na MICHARAZO, Kamata maarufu kama 'Madam V' alisema asasi hiyo inafahamika kwa jina la Victoria Foundation ambayo tayari imeshaanza kuendesha shughuli zake tangu mwishoni mwa mwaka jana.
Kamata aliyetamba na nyimbo kama 'Wanawake na Maendeleo' na 'Mapenzi na Shule', alisema ameianzisha asasi hiyo kutokana na kuguswa na matatizo ya baadhi ya watu hususan yatima na wajane waliopo ndani ya wilaya ya Geita unaotarajiwa kuwa mkoa.
Alisema kama mwanaharakati kijana anaona ni wajibu wake kujitolea kwa hali na mali kusaidia jamii hiyo ili nao angalau wajione ni wenye kuthaminiwa na kuongeza kuwa kila mtu ambaye ana uwezo wa kuwapiga tafu wenye matatizo wasisubiri kusukumwa.
"Hii ni njia ya kurudisha fadhila kwa jamii kutokana na kukubalika kwa kazi zangu kisanii na kuchaguliwa kwangu kuwa kama Mbunge, hivyo na wengine wenye uwezo wa kuwasaidia wenye matatizo wasisubiri kusukumwa kwani ni jukumu letu," alisema.
Kamata alisema kwa sasa anajiandaa kugawa baiskeli 50 na misaada mingine kwa watu wa tarafa nyingine za Geita baada ya awali kufanya hivyo tarafa ya Bugando, ambapo aligawa baiskeli 30 na kugawa vyakula na magodoro kwa vituo vya kulelea yatima vya Lelea na Feed & Tent International.

Fella asita kutoa albamu ‘Kusonona’



ALBAMU mpya ya miondoko ya 'Rusha Roho' ya Meneja wa kundi la TMK Wanaume Family, Said Fella iitwayo 'Kusonona Kusonona' haijasambazwa hadi sasa kutokana na kile ambachom mwenyewe amedai kuwa ni kuangalia kwa umakini kama ni muafaka kuitoa sasa ama la.
Akizungumza na MICHARAZO, Fella, alisema albamu hiyo yenye nyimbo sita iliyokuwa isambazwe mwishoni mwa mwaka jana, mpaka sasa haijatoka kwa sabahu hiyo ya kupima 'upepo'.
Fella alisema wakati akijiandaa kuitoa kazi hiyo mtaani, kulikuwa na kazi nyingine lukuki na hivyo kukubali kwamba atulie kwanza ili kuangalia mwenendo wa albamu zilizotangulia na kwamba huenda akaitoa mwisho wa mwezi huu.
"Ile albamu yangu ya 'Kusonona Kusonona' ya miondoko ya taarab, bado sijaiachia hadi sasa kutokana na hali ilivyokuwa sokoni, lakini kwa sasa nipo mbioni kufanya hivyo" alisema Fella.
Aliongeza, licha ya kwamba albamu bado haijaingia sokoni, lakini baadhi ya nyimbo zake zimekuwa zikifanya vema kwenye vituo vya redio na runinga baada ya kusambaza kwa nia ya kuitambulisha albamu hiyo kikiwemo 'Midomo Imewashuka'.
Ndani ya albamu hiyo, Fella amewashirikisha nyota kadhaa wa taarab wakiwemo Khadija Kopa wa TOT, Isha Ramadhani wa Mashauzi Classic na Maua Tego wa kundi la Coast Modern.
Fella alizitaja nyimbo zilizopo ndani ya albamu hiyo kuwa ni 'Simuachi', 'Midomo Imewashuka', 'Mchakamchaka', 'Sijapopoa Dodo', 'Kimodern Modern' na 'Kusonona Kusonona' iliyobeba jina la albamu.

Steve Nyerere kupakua ‘Respect Nyerere’



WAKATI filamu yake ya 'Mr President' ikiendelea kutamba, mkali wa kuigiza sauti za watu, Steven Mengele 'Steve Nyerere', sasa yuko mbioni kufyatua filamu iitwayo 'Respect Nyerere'.
Filamu hiyo itakayotolewa na kampuni yake ya 'Nyerere the Power', itahusiana na mambo mbalimbali ya kisiasa pamoja na hotuba za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Muigizaji huyo ambaye ni mmoja wa viongozi waandamizi wa Bongo Movie, alisema safari ya kwenda Butiama alipozaliwa Mwalimu Nyerere imeiva kwa ajili ya kufyatua kazi hiyo ambayo alidai kwamba itakuwa kali pengine kuliko ya 'Mr President'.
"Nipo katika maandalizi ya kufyatua kazi mpya ambayo itahusisha masuala ya siasa na baadhi ya hotuba za kusisimua za Mwalimu Nyerere, mmoja wa viongozi wa mfano duniani," alisema Steve Nyerere.
Muigizaji, huyo alisema kila kinachoendelea katika upakuaji wa kazi hiyo atawafahamisha mashabiki wake.

Banana, JB, Riyama waja na DNA




MWANAMUZIKI nyota nchini, Banana Zorro anatarajia kuibukia kwenye filamu kupitia kazi mpya iitwayo DNA aliyoigiza na nyota wa fani hiyo kama Riyama Ally, Jacob Stephen 'JB' na Sabrina Rupia maarufu kwa jina la 'Cathy'.
Kazi hiyo mpya inayohusiana na masuala ya kijamii na namna hila zinavyoweza kufanywa katika upimaji wa vinasaba na kuleta mtafaruku, inatarajiwa kuingia sokoni wakati wowote kuanzia sasa.
Kwa mujibu wa taarifa za wasambazaji, ni kwamba kama anavyotamba katika muziki, Banana ambaye ni mtoto wa gwiji wa muziki wa dansi nchini, Zahir Ally Zorro ameonyesha umahiri mkubwa pia katika filamu.
"Ndani ya DNA, Banana Zorro kathibitisha kuwa habahatishi. Ameshawahi kucheza filamu kadhaa nyuma ikiwemo ya 'Handsome', na humu pia amefanya vizuri sana," imeelezwa katika taarifa hiyo.
Katika hatua nyingine, filamu mpya ya 'I Hate My Birthday' ya Vincent Kigosi 'Ray' inatarajiwa kuanza kusambazwa keshokutwa ambapo ndani yake wameshiriki nyota kadhaa kama Irene Paul na Aunty Ezekiel.

Mdogo wa Nsajigwa 'atua' Bandari Kenya



BEKI wa kutumainiwa wa timu ya 94 KJ inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara ya 94 KJ, ambaye ni mdogo wa nahodha wa Yanga, Shadrack Nsajigwa, Simon Joel Nsajigwa, ametua klabu ya Bandari Fc ya Kenya kwa ajili ya kufanyiwa majaribio.
Mchezaji huyo aliyefanana sura na umbo kama kaka yake, alienda kufanyiwa majaribio katika timu hiyo iliyoshuka daraja msimu huu toka Ligi Kuu ya Kenya, wiki mbili zilizopita baada ya mawakala wa timu kuvutiwa na soka lake.
Kocha wa timu ya 94 KJ, Mwinyimadi Tambaza, alisema walimruhusu mchezaji huyo kwenda kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa na amekuwa akiwasiliana naye kila mara kujua kinachoendelea.
Tambaza alisema walipowasiliana naye juzi alimfahamisha kuwa majaribio yake yanaendelea vema na atarejea nchini wiki ijayo ili kusubiri kitakachofuata juu ya hatma yake ya kuichezea timu hiyo iliyodakiwa na kipa Ivo Mapunda kabla ya kuitema iliposhuka daraja na kwenda kujiunga na Gor Mahia.
"Ni kweli beki wetu ambaye ni mdogo wa Shadrack Nsajigwa, yupo Kenya akifanyiwa majaribio katika timu ya Bandari na anatazamiwa kurejea nchini wiki ijayo kuungana na wachezaji wenzake kwa ajili ya duru la pili la Ligi Daraja la Kwanza wakati akisubiri tararibu nyingine za kuichezea timu hiyo ya Kenya," alisema Tambaza.
Tambaza, alisema ana imani kubwa kwa Nsajigwa mdogo kusajiliwa Bandari kutokana na kuwa na uwezo mkubwa kwa nafasi yake ya ulinzi wa pembeni kama ilivyo kwa kaka yake ambaye ni maarufu nchini kama 'Fuso'.

Mwisho

Coastal Union yakuna kichwa kwa Simba

UONGOZI wa klabu ya soka ya Coastal Union ya Tanga, umedai pambano lao la awali la duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Simba litakalofanyika wiki ijayo linawapasua vichwa wakitafakari mbinu za kuweza kuwapa ushindi wa mchezo huo.
Coastal iliyorejea Ligi Kuu msimu huu, itakwaruzana na Simba katika pambano la marudiano litakalofanyika Jumatano ijayo kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Afisa Habari wa timu hiyo, Eddo Kumwembe, alisema kuwa kuanza duru la pili kwa kuumana na Simba ni mtihani mgumu ambao unawafanya wajipange vema ili kufanya vema kabla ya kufunga safari kuwafuata Mtibwa Sugar kwenye dimba lao la nyumbani.
Kumwembe, alisema uongozi wao upo makini na pambano hilo kwa vile wanataka washinde ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kuondoka nafasi za mkiani mwa msimamo wa ligi hiyo.
"Kuanza na timu kubwa kama Simba ni mtihani unaortuchanganya akili kwa sasa, tukijipanga kwa umakini mkubwa kuona tunaibuka na ushindi kabla ya kwenda kuvaana na Mtibwa huko Manungu," alisema Kumwembe.
Alisema lengo la uongozi wao ni kuona Coastal Union, inatoka maeneo ya mkiani na kuwa miongoni mwa timu za nafasi za juu, hasa baada ya kuongeza nyota kadhaa katika kikosi chao wakati wa usajili wa dirisha dogo.
"Tunataka Coastal ifanye vema kwenye duru hili, ndio maana hata kocha wetu aliamua kufuta mechi yetu dhidi ya Gor Mahia ya Kenya kusudi arekebishe mambo kutokana na kuwa nyuma ya mipango yake," alisema Kumwembe.
Kumwembe aliongeza, kwa kikosi walichonacho sasa ni wazi timu yao itarejesha makali yake ya zamani yaliyoipa ubingwa wa nchi.
Nyota waliongezwa katika kikosi cha Coastal ni Mkenya Edwin Mukenya, Ally Shiboli, Wanigeria Felix Amechi na Samuel Temi na wakali wengine waliokuwa katika usajili w awali wakiwemo washambuliaji Ben Mwalala na Aziz Gilla.

Mwisho

Mkubwa na Wanae: Kituo cha kuendeleza vipaji







WAKATI kituo cha kuendeleza vipaji vya sanaa kwa vijana cha 'Mkubwa na Wanawe'
kinachomilikiwa na Meneja wa TMK Wanaume Family, Said Fella kilipoanzishwa mwaka jana kilikuwa na msanii mmoja tu, Abdallah Kihambwe 'Dula Yeyo'.
Hata hivyo kikielekea kutimiza muda wa mwaka mmoja mnamo Februari 13, mwaka huu, kituo hicho kina jumla ya wasanii 37, wasichana 10 na waliosalia ni wavulana ambao wote wanaimba na kudansi.
Fella, maarufu kama 'Mkubwa Fella' ambaye ndiye Mkurugenzi wa kituo hicho alisema
alipata wazo la kuanzisha kituo hicho kilichosajiliwa kama kampuni, kutokana na kuvutiwa na mafanikio inayopata kituo kingine cha kuendeleza vipaji cha THT.
Alisema, pia alikianzishwa kwa nia ya kusaidia vijana wadogo kujiepusha kuingia kwenye makundi maovu yatakayoweza kuwapotosha na kufunza stadi za maisha kwa faida yao ya baadae mbali na kuvitumia vipaji vyao vya sanaa kama ajira rasmi.
Fella, alisema tangu kuanzishwa kwa kituo hicho ambayo anashirikiana kukiendesha na
wakurugenzi wenzake, Hamis Tale 'Babu Tale' na Mheshimiwa Temba, kimeweza kuwatoa wasanii karibu saba ambao wameanza kutamba kwenye fani ya muziki nchini.
"Tunashukuru tangu kuanzishwa kwa kituo hiki, tumefanikiwa kuwatoa wasanii kadhaa ambao wameanza kupata mafanikio katika muziki, licha ya kwamba tunakabiliwa na matatizo makubwa katika kituo chtu kwa vile hakina wafadhili wala wadhamini," alisema.
Aliwataja wasanii wanaokitangaza kituo hicho kwa sasa ni Aslay Isihaka 'Dogo Aslay'
anayetamba na wimbo wa 'Nakusemea' maarufu kama 'Naenda Kusema kwa Mama', Dula Yeyo, Mugogo anayekimbiza na wimbo wa 'Chongochongo' na Hassani Kumbi anayetamba na kibao cha 'Vocha' kilichopo katika mahadhi ya Mduara.
"Wengine ambao tumeanza kuwarekodia kutokana na kuiva kimuziki ni, H. Namba, Bashlee na Asnat wanaotarajia kuibuka na kibao kiitwacho 'Nipe Kidogo', kwa vifupi ni kwamba matunda yameanza kuonekana katika kuwaibua wasanii wapya," alisema.
Fella alisema licha ya kuwafunza namna ya kuimba na kucheza, wasanii waliopo kituo
hapo wanafundishwa stadi za maisha juu ya mapenzi na athari zake, matumizi ya dawa za kulevya na magonjwa mbalimbali kama Ukimwi na mengine na jinsi ya kuepukana nayo.
"Kwa upande wa muziki mwalimu wanayewanoa vijana hao ni Mhe Temba na Dulla Yeyo, wakati Meneja wa kituo ni Yusuf Chambuso na Prodyuza wa kituo ni Suleiman Daud maarufu kama Sulesh au Mr India," alisema Fella.
Juu ya namna ya kukihudumia kituo, Fella alisema wanatumia fedha zao wenyewe wakati wakisubiri kupata ufadhili, ambapo alisema kwa mwezi mzima hutumia si chini ya Sh. Mil moja kwa ajili ya malazi ya chakula.
"Unajua nyumba hii inayowatunzia wasanii ni ya kukodisha, tunalipa pango kwa mwezi
Sh. 250,000, huku huduma ya chakula kwa siku si chini ya Sh 25,000, hiyo ni mbali na
gharama za usafiri na ada kwa wanafunzi tunawaosemesha wenyewe," alisema.
Alisema licha ya wengi wa wasanii wao kutokea majumbani kwao kuja kujifunza fani zao kituo hapo, wapo wasanii 12 wanaoishi katika nyumba hiyo iliyopo Temeke, jijini Dar es Salaam.
Fella alisema matarajio yao hadi kufikia mwisho wa mwa huu wasanii zaidi ya 20 wawe
wameshatoka kisanii, na kuwasaidia vijana zaidi ndani na nje ya mkoa wa Dar es Salaam.
Hata hivyo alisema mafanikio hayo yatafikiwa pale atakapopata wafadhili na kuungwa
mkono na serikali katika jitihada zake za kuendeleza sanaa na kuwasaidia vijana kupata ajira kupitia muziki, sambamba na kuwajenga kimaadili.
Fella alisema kituo kwao kitu cha kwanza wanachozingatia ni nidhamu na kuwanyoosha wale wanaoonekana kwenda kinyume, pia wanathamini kipaji cha mtu bila kujali umri wake na bahati nzuri matunda yao yanaonekana kupitia wasanii walioanza kutamba sasa.
Naye Meneja wa kituo hicho, Yusuf Chambuso, alisema kuna vikwazo kadhaa wamewahi kukutana navyo kama baadhi ya wazazi kushindwa kuwaelewa katika wanachokusudia kwa kudhani watoto wao wanafunzwa uhuni, lakini wanapoeleweshwa huwapa sapoti.
Aliongeza wapo baadhi ya vijana wanaoenda kwao huwa hawana uwezo wowote kimuziki, lakini kupitia walimu wao huwasaidia na kuwaweka juu, akimtolea Aslay aliyedai licha ya kugundua kipaji cha muziki, walimsaidia kumweka sawa ndio maana leo anatisha.

Mwisho