STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, March 4, 2011

Jokha Kassim akwama kushebeduka

MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab, Jokha Kassim, amesema bado anaendelea kuhangaikia uzinduzi wa albamu yake binafsi ya 'Wacha Nijishebedue' iliyokwamba kuzinduliwa mwaka jana.
Uzinduzi wa albamu hiyo ulikwama katikati ya mwaka jana kutokana na sababu mbalimbali kubwa kukosa wafadhili na wadhamini wa kumpiga tafu.
Jokha, alisema bado hajakata tamaa kwa vile anaendelea kuwasiliana na wafadhili ili kufanikisha uzinduzi huo ndani ya mwaka huu.
"Najipanga kufanikisha uzinduzi wangu ndani ya mwaka huu, naamini Mungu atanisaidia nipata wadhamini wa kunipiga tafu," alisema.
Mwimbaji huyo alizitaja nyimbo zinazounda albamu yake hiyo 'Yamekushinda', 'Meseji za Nini', 'Kinyang'anyiro Hukiwezi', 'Kelele za Mlango' na Wacha Nijishebedue' uliobeba jina la albamu.
"Niliporekodi na kushuti video ya nyimbo zangu nilipata mfadhili na sasa anatafuta wengine watakaonisaidia kwenye uzinduzi wa albamu yangu, hivyo mashabiki wangu wajue kuwa bado ninahangaikia fedha," alisema.
Alisema, baadhi ya nyimbo zake ukiwemo uliobeba jina la albamu zimekuwa zikisikika kwenye vitu mbalimbali vya redio na televisheni na kumpa matumaini kwamba huenda akapata soko atapozindua.

Mtenda Akitendewa videoni

WIMBO mpya wa bendi ya Extra Bongo unatarajiwa kutambulishwa rasmi leo kwa mashabiki sambamba na vibao vingine na wanamuziki wapya uitwao, Mtenda Akitendewa umefyatuliwa video yake.
Video ya kibao hicho ambacho awali lilipangwa kufahamika kama 'Under 18' kimefyatuliwa na wanamuziki wa bendi hiyo wakiwa kambini kupitia kampuni ya Sophia Records ya jijini Dar es Salaam na utaanza kuonekana hewani wakati wowote kuanzia sasa.
Mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki 'Kamarade' aliiambia micharazo kuwa, waliamua kurekodi video ya wimbo huo wakiwa kambini kama njia ya kuwapa burudani mashabiki wao kuwaonyesha hawakuwa bure kambini bali walikuwa wakiwaandalia mambo mapya.
"Pamoja na kuandaa kazi mpya, lakini pia tumefyatua video ya moja ya vibao hivyo kiitwacho Mtenda Akitendewa ambacho kitaanza kuonekana wakati wowote,tumeshasambaza, kibao hicho na vingine pamoja na wanamuziki wapya tutawatambulisha rasmi Ijumaa (leo)," alisema.
Choki alisema onyesho la utambulisho kwa bendi yao utafanyika kwenye ukumbi wa New Msasani Club, ambapo kesho litafuatiwa na onyesho jingine TCC-Chang'ombe na kabla ya Jumapili kutambulishwa Mango Garden na kwenda kuvunja kambi yao ili kujiandaa kwenda Zanzibar.
Mtunzi na muimbaji huyo alizitaja nyimbo nyingine zitakazotambulishwa sambana na wanamuziki sita waliowanyakua wakienda kambini kutoka Twanga Pepeta ni Neema, Nguvu na Akili na Fisadi wa Mapenzi vinavyoandaliwa kwa ajili ya albamu mpya na ya pili.
Wanamuziki watakaotambulishwa kwenye maonyesho hayo ya mwishoni mwa wiki ni mtunzi na muimbaji nyota nchini, Rogert Hegga 'Caterpillar', Rapa Saulo John 'Ferguson', mpiga besi, Hoseah Mgohachi na wanenguaji Hassani Mohammed 'Super Nyamwela', Isaac Burhan 'Super Danger' na Otilia Boniface waliotoka African Stars 'Twanga Pepeta'.

Thursday, March 3, 2011

Maugo atamba atatumia siku 16 kumchapa Kaseba




WAKATI Japhet Kaseba akiwa ameshaanza mazoezi kujiandaa na pambano lao itakalochezwa mwezi ujao, bondia Mada Maugo, amesema hana haraka ya kufanya hivyo badala yake ataanza rasmi April Mosi, akidai siku 16 zitamtosha kujiandaa kumchakaza mpinzani wake huyo.
Kaseba na Maugo watapigana kwenye pambano maalum la 'Nani Zaidi' litakalofanyika April 16, kwenye ukumbi wa PTA, Dar es Salaam kwa ajili ya kusaka mshindi atakayepigana na bingwa wa dunia, Francis Cheka.
Kaseba ameshatangaza ameshaanza maandalizi ili kujiweka sawa kumpiga Maugo, ambaye kama yeye ameshawahi kujeruhiwa na Cheka siku za nyuma, lakini Maugo akizungumza na Micharazo alisema yeye bado hajaanza.
Maugo alisema yeye bao yupo yupo kwa sasa na ataanza rasmi April Mosi na kutumia siku 16 kabla ya kuvaana na Kaseba kujiweka fiti na kutamba siku hizo zinatosha kumchakaza bingwa huko wa dunia wa Kick Boxing.
"Sijaanza na wala sitarajii kuanza kwa sasa kwa vile pambano lenyewe ni jepesi sana kwangu, nitatumia siku 16 kabla ya pambano hilo kuanza mazoezi na nina uhakika wa kumchakaza Kaseba bila tatizo," alisema Maugo.
Maugo alisema pamoja na kwamba mpinzani wake kuanza kujinadi kuwa atampiga, yeye hataki kupiga domo na badala yake kuwaomba mashabiki wa ngumi kujitokeza ukumbini siku ya April 16 kushuhudia ukweli huo.
"Sitaki kujibishana maneno na Kaseba, sio kawaida yangu, mie ni mtu wa vitendo zaidi na hivyo nawasihi mashabiki waje ukumbi kuona kama Kaseba atamaliza raundi nane la pambano hilo ni hayo tu," alisema Maugo.
Mabondia hao wenye majina makubwa nchini watapambana katika pambano la raundi nane la uzani wa Kilo 72 lililoandaliwa na mratibu Kaike Siraju kupitia kampuni ya Kaike Promotion chini ya usimamizi wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO.

Mwisho

Nyilawila awafunika Cheka, Maugo



BINGWA wa Dunia wa Ngumi za Kulipwa anayeshikilia taji la WBF, Karama Nyalawila, ndiye Mtanzania anayeongoza kwa ubora miongoni mwa mabondia wa uzani wa Middle akiwafunika wakali kama Francis Cheka na Mada Maugo.
Kwa mujibu wa takwimu za ubora wa mabondia wa uzani huo duniani, kupitia mtandao wa Box Rec, Nyalawila anashikilia nafasi ya 74, wakati Cheka, Bingwa wa Dunia wa UBO, ICB na WBC yupo nafasi ya 142.
Maugo yeye anashika nafasi ya 196 akimzidi wakongwe Rashid Matumla 'Snake Man' na Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo' wanashika nafasi ya 327 na 370.
Nyalawila aliyetwaa taji hilo Desemba 3 mwaka jana huko Jamhuri ya Czech, ni miongoni mwa mabondia wanne wa kiafrika waliopo kwenye orodha wa mabondia 100 Bora Duniani wa uzani huo wa Middle.
Wengine waliopo kwenye orodha hiyo ni Mganda, Kassim Ouma anayeshika nafasi ya 32 akiwa ndiye kinara kwa mabondia wa Kiafrika, Assie Duran na Osumanu Adama wa Ghana waliopo nafasi ya 34 na 35 na Mnigeria, Eromosele Albert aliyepo anayeshikilia nafasi ya 38.
Bondia anayeongoza kwenye orodha ya wapiganaji wa uzani huo ni Sergio Gabriel Martinez wa Argentina anayefuatiwa na Felix Sturm wa Ujerumani na anmayeshikilia nafasi ya tatu duniani ni Danile Geale wa Australia.
Mabondia wa Kitanzania wanatengeneza 10 Bora yao wakiwafuata Nyalawila na Cheka ni, Mada Maugo (196), Thomas Mashali (212), George Dimoso (289), Maisha Samson (302), Rashid Matumla (327), Bagaza Mwambene (342), Stan Kessy (350) na Maneno Oswald 'Mtando wa Gongo' akiishika nafasi ya 370.

Kanumba ana 'shock', Ray atamba





BAADA ya kuanza mwaka na filamu ya 'Deception', muigizaji nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba 'The Great' ameibuka na filamu mpya iitwayo 'The Shock'.
Filamu hiyo ambayo imekamilika hivi karibuni na sasa ipo katika maandalizi ya kuachiwa mitaani, ni ya pili kwa msanii huyo kwa mwaka huu wa 2011.
Akizungumza na Micharazo, Kanumba alisema kama ulivyo utaratibu wake wa kuibua wasanii wapya katika fani hiyo, ndani ya 'The Shock' amemtambulisha muigizaji mpya mwanadada mrembo Shez Sadry ambaye amedai amefanya mambo makubwa kama mzoefu.
Kanumba alisema mbali na mwanadada huyo ambaye ndiye mhusika mkuu, pia kuna kuna muimbaji wa FM Academia Patcho Mwamba, Ben Braco, yeye mwenyewe na wengineo.
"Baada ya Deception sasa The Shock inakuja ambayo na kifaa kipya lakini kikali katika muigizaji, Shaz Sadry," alisema Kanumba.
Alisema filamu hiyo inatarajiwa kuachiwa mitaani ndani ya mwezi huu na itasambazwa na kampuni ya Steps Entertainment.
Katika hatua nyingine, mpinzani mkubwa wa Kanumba, Vincent Kigosi 'Ray' amesema filamu yake mpya ya 'Second Wife' inatarajiwa kuingia mitaani wiki ijayo na kuwataka mashabiki wa fani hiyo kukaa mkao wa kula kupata uhondo.
Katika filamu hiyo mpya, Ray ameigiza na wakali kama Riyama Ally, Coleta Raymond, Aisha Bui, muigizaji mpya mwanadada Skyner Ally na mtoto Aisha.
Ray amesema filamu hiyo ni 'funika bovu' kutokana na jinsi alivyoigiza kwa kushirikiana na wenzake na kusisitiza kuwa, hizo ni salamu kwa wapinzani wao kuwa RJ Production imekuja kivingine ndani ya mwaka 2011.

Madee asikitika Dogo Janja kuzinguliwa shuleni

MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya, Hamad Ally 'Madee' amedai kusikitishwa na kitendo ambacho amekuwa akifanyiwa msanii chipukizi anayemfadhili, Abdul-Aziz Chende 'Dogo Janja' na mmoja wa walimu wa Shule ya Sekondari ya Makongo anayosoma kwa sasa.
Akizungumza na Micharazo, Madee alisema kuwa, amesikitishwa na taarifa kwamba mmoja wa walimu wa shule hiyo amekuwa akimpa wakati mgumu Dogo Janja, jambo analohofia linaweza kushuka kiwango chake cha elimu darasani.
Hata hivyo Madee alisema tayari suala la mwalimu huyo ambaye hakumtaja jina, limeshafikishwa kwa mkuu wa shule hiyo, na Dogo Janja anaendelea kusoma kwa vile hana mpango wa kuhama.
"Kwa walimu wa namna hii wanaharibu viwango vya wanafunzi darasani, ila nashukuru mambo yameshamalizwa kwa Dogo kwenda kwa Mkuu na kulalamika na ticha huyo kuonywa," alisema.
Aliongeza ni vema walimu wakatambua kuwa wao ni walezi kwa wanafunzi na hivyo waishi
kama watoto wao na wanapokosea wawaelekeze hata kama kwa bakora, lakini wakizingatia
miiko na taaluma zao za kazi.
Dogo Janja, alinukuliwa na kituo kimoja akisema kuwa alikung'utwa na mwalimu wake huyo baada ya kutofautiana nae kiswahili, huku akidai mara kwa mara amekuwa akimzingua akimuita 'Dogo Jinga' badala ya jina lake la Dogo Janja, kitu kilichokuwa kikimnyima raha shuleni.
Madee, aliamua kumsaidia Dogo Janja mwenyeji wa Arusha kutokanan na kuvutiwa na kipaji chake na tayari ameshamkamilishia albamu mpya iitwayo Ngarenaro, akiwa pia ndiye anayemlipia ada shuleni hapo akijiandaa kumfyatulia video ya albamu hiyo yenye nyimbo 10.

Mtenda Akitendewa ya Extra Bongo videoni



WIMBO mpya wa bendi ya Extra Bongo unaotarajiwa kutambulishwa rasmi leo kwa mashabiki sambamba na vibao vingine na wanamuziki wapya uitwao, Mtenda Akitendewa umefyatuliwa video yake.
Video ya kibao hicho ambacho awali lilipangwa kufahamika kama 'Under 18' kimefyatuliwa na wanamuziki wa bendi hiyo wakiwa kambini kupitia kampuni ya Sophia Records ya jijini Dar es Salaam na utaanza kuonekana hewani wakati wowote kuanzia sasa.
Mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki 'Kamarade' aliiambia Micharazo kuwa, waliamua
kurekodi video ya wimbo huo wakiwa kambini kama njia ya kuwapa burudani mashabiki wao kuwaonyesha hawakuwa bure kambini bali walikuwa wakiwaandalia mambo mapya.
"Pamoja na kuandaa kazi mpya, lakini pia tumefyatua video ya moja ya vibao hivyo kiitwacho Mtenda Akitendewa ambacho kitaanza kuonekana wakati wowote,tumeshasambaza, kibao hicho na vingine pamoja na wanamuziki wapya tutawatambulisha rasmi Ijumaa," alisema.
Choki alisema onyesho la utambulisho kwa bendi yao litafanyika leo kwenye ukumbi wa New Msasani Club kabla ya kufuatiwa na maonyesho mawili ya TTC Chang'ombe litakalofanyika Jumamosi kisha Jumapili pale Mango Garden kabla ya kujiandaa kwenda Zanzibar.
Mtunzi na muimbaji huyo alizitaja nyimbo nyingine zitakazotambulishwa sambana na
wanamuziki sita waliowanyakua wakienda kambini kutoka Twanga Pepeta ni Neema, Nguvu
na Akili na Fisadi wa Mapenzi vinavyoandaliwa kwa ajili ya albamu mpya na ya pili.
Alipoulizwa kama kibao hicho ni 'dongo' mahasimu wao, African Stars 'Twanga Pepeta', Choki alisema sio kweli kibao cha Mtenda Akitendewa ni kijembe, ila alisema kama kuna mtu atakayeguswa nao na kulalamika ujue ndiye mhusika.
"Staili yetu ni kama ile ya zamani ya kurusha jiwe kwenye kiza, atakasema mmh, hujue limempata, ila sio kweli kama nimetunga mahususi kwa ajili ya mtu yeyote," alisema Choki.
Mkurugenzi huyo aliwataja wanamuziki watakaotambulishwa kwenye maonyesho hayo ya mwishoni mwa wiki ni mtunzi na muimbaji nyota nchini, Rogert Hegga 'Caterpillar', Rapa Saulo John 'Ferguson', mpiga besi, Hoseah Mgohachi na wanenguaji Hassani Mohammed 'Super Nyamwela', Isaac Burhan 'Super Danger' na Otilia Boniface waliotoka African Stars 'Twanga Pepeta'.

Akudo Impact yanyakua wanenguaji wapya





BENDI ya Akudo Impact imeongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji wa jukwaa baada ya
kuwanasa wanenguaji watatu kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.
Kwa mujibu wa meneja wa bendi hiyo George Kyatika, wanenguaji hao ni Mariam Sangwa,
Francine Bozi na Mary Sheli ambao tayari wameshatambulishwa kwenye maonyesho mbalimbali ya Akudo.
Meneja huyo alisema ujio wa wanenguaji hao unaifanya Akudo kuwa na jumla ya madansa sita wengine wakiwa ni Fanny Bosawa, Raissa Sangwa na Nadine Issala.
"Tumeongeza wanenguaji wakati huu ambao tuko kwenye maandalizi ya uzinduzi wa albamu
yetu ya History no Change ambayo itazinduliwa mwezi wa ujao," alisema Kyatika.
Alisema kuwa awali safu yao ya ushambuliaji wa jukwaa ilikuwa inapwaya hasa baada kupunguza baadhi ya wanenguaji ambao makali yao ya kufanya kazi yalikuwa yamepungua lakini sasa wamepata wapya.
Kyatika alizitaja baadhi ya nyimbo za albamu hiyo wanayojiandaa kuzindua kuwa ni 'Ubinafsi', 'Umefulia', 'Pongezi kwa Wanandoa' na 'Umejificha Wapi'.
Aliongeza kusema kuwa sasa Akudo imejipanga upya kuanzia kwenye uongozi wa bendi na
hivyo ana uhakika itaendelea kufanya vizuri kwa kuwaburudisha mashabiki na wapenzi wake.
Akudo imekuwa ikitamba na albamu yake ya kwanza ya Impact ambayo ilichangia kuipandisha chati bendi hiyo inayojiita Vijana wa Masauri ikiwa chini ya rais wake Christian Bella.

Wednesday, March 2, 2011

PAMBANO LA WATANI J'MOSI Furaha kubwa inasubiriwa *Ni Msimbazi au Jangwani?

VIGOGO wa soka nchini Simba na Yanga zinakutana Jumamosi katika 'big match' ya pekee kwa aina yake msimu huu wa Ligi Kuu ya Vodacom, huku Wekundu wa Msimbazi wakipania kulipa kisasi cha kufungwa katika mechi ya kwanza, na Yanga wakitamba kuendeleza ubabe.
Pambano hili la marudiano baada ya lile kwanza mwishoni mwa mwaka jana kwenye uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza na Simba kuloa bao 1-0, linafanyika kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Vita ya mechi hii ambayo tayari imeteka hisia za mashabiki wengi wa soka inatokana na namna timu hizo zinavyopokezana kukalia kiti cha uongozi wa ligi hiyo pamoja na Azam FC.
Kigogo kitakachoshinda katika mechi hiyo, kitakuwa kimejiweka kwenye mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa wa soka ambao kwa sasa uko mikononi mwa Simba.
Yanga ndio inayoongoza ligi hiyo kufuatia ushindi wake wa bao 1-0 dhidi ya Ruvu Shooting na kuiengua Simba waliokuwa kileleni kwa masaa tangu walipoichabanga Mtibwa Sugar mabao 4-1.
Jerry Tegete ndiye aliyekuwa shujaa kwa kufunga bao zuri wakati Simba ikilala 1-0 kwenye mechi ya kwanza, na amepania kurejesha tena huzuni kwa Simba kwenye mechi ya kesho.
Hata hivyo Yanga pia watashuka uwanjani kesho wakiwa na machungu ya kipigo cha mabao 2-0 ilichopewa na watani zao hao katika pambano la fainali la Kombe la Mapinduzi mapema mwaka huu visiwani Zanzibar.
Kipigo hicho hakikuonekana kuwauma sana Yanga, kwani walijitetea kwa kusema wachezaji wake wengi walikuwa na timu ya taifa iliyokuwa ikishiriki michuano ya Mto Nile nchini Misri.
Simba itashuka dimbani ikitokea chimbo lake la kawaida mjini Zanzibar, na Yanga wakiingia kusaka pointi mbili wakitoka Bagamoyo.
Simba kupitia nyota wake kadhaa kama Juma Jabu, Rashid Gumbo na Mohammed Banka wamesema hawana hofu ya pambano hilo.
Wamesema wamejiandaa kushinda mechi hiyo, na hakuna shaka matarajio yao yatatimia ili iwe sehemu nzuri ya maandalizi dhidi ya pambano lao la Klabu bingwa dhidi ya Mazembe.
"Hatuna hofu na Yanga, tutawafunga ili tukienda Lubumbashi kuvaana na TP Mazembe tukiwa na ari ya ushindi kama tunavyowakabili Yanga kufuatia kuilaza Mtibwa mabao 4-1," alisema Banka.
Hata hivyo Yanga kupitia Afisa Habari wao, Louis Sendeu alisema wachezaji wake watacheza kufa na kupona na kuifunga Simba ili kujiweka kwenye mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa.
"Kama tulivyofanya Mwanza ndivyo tutakavyorejea tena Jumamosi, timu ipo katika hali nzuri na tuna uhakika wa kuilaza tena Simba," alisema Sendeu.
Kama Yanga itashinda itazidi kujikita kileleni, lakini kama itakubali kipigo kwa watani zao maana yake wataporomoka na kuwapisha Simba warejee kileleni.
Timu hizo zinakutana Yanga ikiwa na kocha mpya, Sam Timbe kutoka Uganda, huku ikiwa na wachezaji wawili wapya ambao kwenye fainali za Kombe la Mapinduzi hawakuonyesha makali yoyote nao ni Davies Mwape na Juma Seif 'Kijiko'.
Simba kwa upande wao, itashuka dimbani ikiwa na mshambuliaji mwenye uchu Mbwana Samatta na Ally Ahmed 'Shiboli' ambao katika mechi ya Mwanza hawakuwepo.
Nani atakayeibuka na ushindi katika pambano la kesho na kuzima ngebe za wenzake? Bila shaka ni suala la kusubiri dakika 90 za mchezo huo.

INAFRIKA WAREJEA NA MBELEKO TOKA ULAYA




BAADA ya ziara ya miezi miwili na nusu ya maonyesho ya burudani katika nchi mbalimbali za Ulaya, bendi ya InAfrika imerejea nchini, ikijinadi kuwa, ziara yao ilikuwa ya mafanikio makubwa.
Bendi hiyo iliwasili jana majira ya saa 4 asubuhi, kupitia mmoja wa viongozi
na wanamuziki wake, Bob Rudala imesema itatumia siku chache kupumzika
kabla ya kuanza kuitambulisha albamu yao mpya mikoani.
Akizungumza na Micharazo mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam, alisema albamu hiyo ya pili kwao baada ya ile ya 'Indege', inaitwa 'Mbeleko'.
Rudala aliyewahi kutamba na nyimbo binafsi kama 'Nimekuchagua Wewe', alisema albamu hiyo ina nyimbo 10 zilizopigwa katika miondoko mbalimbali ya ngoma asilia za Tanzania.
Rudala alisema utambulisho wa albamu hiyo utaanzia mkoa wa Arusha wiki ijayo, kabla ya uongozi wa bendi hiyo kupanga mahali pengine pa kufanya hivyo.
Kuhusu ziara hiyo, Rudala alisema ilikuwa ya mafanikio makubwa na kwamba watatumia utambulisho wa albamu hiyo kuudhibitishia umma wa Tanzania kuwa walienda kujifunza mambo mengi kuendeleza muziki nchini.
"Tunashukuru tumerejea salama, ila kwa kifupi tumefarijika na mafanikio makubwa tuliyopata katika ziara hiyo na tunapumzika kwa siku kadhaa kabla ya kabla ya kuanza kuitambulisha albamu yetu ya Mbeleko," alisema.
Alizitaja baadhi ya nyimbo zilizopo kwenye albamu hiyo kuwa ni Mbeleko, Hatushangai, Jamila, Kitchen Party, Mimi Muafrika, Amina, Jua Limetua na kadhalika.
Aliongeza kuwa ziara yao waliyoifanya kuanzia Desemba mwaka jana, ilihusisha nchi tano za Uholanzi, Ujerumani, Uswisi, Austria na Romania ambapo mbali na bendi, pia InAfrika iliambatana na kikundi chao cha wanenguaji na wacheza sarakasi.
InAfrika ilianzishwa mwaka 1992 ikiwa na albamu ya kwanza ya 'Indege' ambayo pia hufahamika kama 'Omunwa'ambayo ilisaidia kuipandisha chati kwa nyimbo zake mchanganyiko zikiwemo zenye miondoko ya asili.

Monday, February 28, 2011

Nyawela atuma salamu kwa wapinzani wa Extra



DANSA maarufu nchini ambaye kwa sasa ni kiongozi wa safau ya unenguaji wa bendi ya Extra Bongo, Hassan Mohammed 'Super Nyamwela', amewataka wapinzani wake kukaa chonjo na ujio wake mpya akiwa na bendi hiyo.
Nyamwela, aliyetokea African Stars 'Twanga Pepeta' amesema muda wa mwezi mmoja waliokuwa kambini amefanya mambo makubwa ambayo anaamini yatawasambaratisha wapinzani wao mara watakapotoka mafichoni.
Akizungumza mara baada ya bendi hiyo kutambulisha 'shoo' pamoja na moja ya vibao vyao vipya kwa waandishi wa habari jana, kwenye kambi yao iliyopo Mbezi-Louis jijini Dar es Salaam, Nyamwela alisema wapo kamili kwa vita.
Nyamwela alisema muda mmoja wa mwezi waliokaa kambini wameweza kuandaa shoo mpya ambazo hazijawahi kuonwa kokote.
"Kama ulivyoo, hiyo ni sehemu tu ya kazi ambazo tumekuwa tukizifanya tangu tuingie kambini na ambazo zitaanza kuonekana hadharani Ijumaa tutakapotoka mafichoni na kufanya shoo za mwishoni mwa wiki," alisema.
Alisema kikosi chao kinachoundwa na wanenguaji tisa akiwemo yeye Super Nyamwela, Super Danger, Master B na King Lion ambao ni wanaume, huku wa kike ni Angela Alloyce, Otilia Boniface, Husna Ramadhani, Lavia Edward na Jamila Nassor.
Naye rapa mpya wa bendi hiyo, Saulo John 'Ferguson' amewataka mashabiki wa muziki wa dansi kusubiri kupata vitu vipya toka kwake kuliko vile walivyokuwa wamezoea kuvipata alipokuwa Twanga Pepeta.
"Nina rapu kibao, lakini sitaki kumaliza uhondo, Ijumaa tunaanza kutoka kwa kufanya onyesho pale New Msasani Club, watu waje wamuone Ferguson mpya," alisema rapa huyo mmoja wa waimbaji wapya wa Extra Bongo.

Mwisho

EXTRA BONGO KUTOKA MAFICHONI




BENDI ya Extra Bongo iliyokuwa kambini kwa muda wa mwezi mmoja, inatarajiwa kutoka mafichoni Ijumaa wiki hii tayari kufanya maonyesho matatu ya kuzitambulisha nyimbo zao mpya pamoja na kuwaanika hadharani wanamuziki walya iliyowanyakua wakiingia kambini.
Hata hivyo kambi hiyo iliyokuwa eneo la Time Square Resort, Mbezi Louis, jijini Dar es Salaam, itavunjwa rasmi Jumatatu kabla ya kupata boti kwenda visiwani Zanzibar kutumbuiza.
Akizungumza kwenye utambulisho wa nyimbo na staili yao ya uchezaji kwa waandishi wa habari jana, Mkurugenzi wa bendi hiyo, Ally Choki 'Kamarade' aliiambia Micharazo kuwa, bendi yao iliyokuwa kambini kwa muda wa mwezi mmoja itatoka mafichoni Ijumaa kwa ajili ya kufanya maonyesho matatu mwishoni mwa wiki kabla ya kwenda Zanzibar Machi 12.
Choki, alisema siku watakayotoka mafichoni, Extra Bongo itafanya onyesho kwenye ukumbi wa New Msasani Club, na siku itakayofuata itakuwa TCC Changombe na kumalizia burudani zao za utambulisho wa nyimbo, wanamuziki na unenguaji wao mpya pale Mango Garden, Kinondoni.
"Tunatarajia kutoka hadharani Ijumaa, ambapo tutafanya maonyesho matatu siku ya Ijumaa, Jumamosi na Jumapili kwa kutambulisha nyimbo mpya na unenguaji tuliokuwa tunapika tukiwa kambini, ila kambi tutaivunja rasmi Jumatatu," alisema Choki.
Choki alisema baadhi ya nyimbo zilizokuwa zikipikwa wakiwa kambini ambazo zitatambulishwa rasmi kwa mashabiki ni Mtenda Akitendwa, Neema, Fisadi wa Mapenzi na nyinginezo.
"Hizo ni baadhi ya nyimbo tulizokuwa tukiziandaa, na tutazitoa sambamba na kuwatambulisha wanamuziki wetu wapya na aina ya uenguaji chini ya uongozi wa Super Nyamwela," alisema.
Choki alisema kuwepo kwao kambini kumeijenga vema bendi yao na watatoka hadharani kwa nia ya kuleta changamoto na mabadiliko katika muziki wa Tanzania.
"Tumekuja kuleta mabadiliko na wapenzi watarajie mambo makubwa toka kwetu kwani kikosi cha wanamuziki 23 tuliopo ni jeshi la maangamizi, kizuri ni kwamba tunatambulisha nyimbo mpya na video ya Mtenda Akitendwa,ambayo tumepiga tukiwa kambini," alisema Choki.
Naye mmoja wa marapa wa bendi hiyo, Ramadhani Mhoza 'Pentagone' alisema kambi imewaivisha na kwamba mashabiki wa muziki watarajie mambo makubwa toka kwao.
"Aisee asikuambie mtu tumeiva vya kutosha tukiwa tayari kwa kazi, ebu piga picha hapa Pentagon, kule Ferguson, Shikito, Bob Kissa, Hegga, Choki, Nyamwela na wengine unadhani atapona mtu kweli hapa?" alisema Pentagoni.
Kiongozi wa wanenguaji, Super Nyamwela, alisema kile walichokuwa wakikipika kimeshaiva na wapenzi wa muziki wajiandae kupata burudani kabambe toka kwao wakiwa ni tofauti na Super Nyamwela aliyekuwa Twanga Pepeta.
Kikosi kamili cha Extra Bongo kilichokuwa kambini na kinacghotarajiwa kuanza kuwasha moto jijini kabla ya kwenda Zenji, kisha wakati wa Pasaka kukimbiza Kanda ya Ziwa ni pamoja na Ally Choki 'Kamarade', Ramadhani Mhoza 'Pentagone', Saulo John 'Ferguson', Rogart Hegga 'Catapillar', Bob KIssa' na Athanas Montanabe 'Shikito' ambao ni waimbaji.
Wapiga gitaa ni Ephraem Joshua 'Kanyaga Twende' na Mfaume Zablon 'Baba Watoto' (solo), Sara Kindeki (Rhythms) na Hoseah Mgohachi (Bass), huku wapiga Kinanda wakiwa ni Pablo Mwendambali na Sebastian Lundandikija.
Anayekung'ita ngoma mbili maarufu kama Tumba au Conga ni Salum Issa 'Cha Kuku', wakati mkaanga chips (Drums) ni Victor Machine, wakati wanenguaji mbali na Super Nyamwela, pia kuna Danger Boy, Master B, King Lion, Otilia Boniface, Husna ramadhani, Angela Alloyce, Lavia Edward na Jamila Nassor 'Queen Jamila'.

Saturday, February 26, 2011

MCHANGANYIKO WA HABARI

Kipigo chamchanganya kocha Toto


KIPIGO cha mabao 2-1 ilichopewa Toto Afrika na timu ya Mtibwa Sugar, kimemchanganya kocha wa timu hiyo ya Mwanza, Choke Abeid, aliyedai hakutegemea kama wangelala ila ameapa kupigana kufa na kupona kushinda mechi yao ijayo ya ugenini dhidi ya Kagera Sugar.
Toto ambayo kabla ya mechi hiyo iliidindia Simba na kisha kuilaza AFC Arusha, ilikumbana na kipigo hicho na kuiacha timu yao kwenye nafasi ya saba ikiwa na pointi 20, huku Choke akisema mipira ya faulo ya Mtibwa ndio iliyowamaliza.
Choke, mchezaji wa zamani wa Yanga, alisema Mtibwa walikuwa wazuri kwa mipira hiyo na kuwakwamisha kusogea nafasi waliopo, ingawa amesema wanajipanga vema kwa mechi ijayo ya Kagera itakayochezwa Machi 9.
"Kipigo kimetuchanganya, kwa vile tulijiamini tungeshinda, ila lazima nikiri mipira iliyokufa (faulo) ndio iliyotuumiza, ingawa tumekubali matokeo na kujipanga kwa mechi ijayo," alisema.
Choke, alisema licha ya mechi hiyo ijayo ni ngumu kutokana na Kagera kucheza nyumbani kwao, ila bado wanaamini wataenda kushinda ili kulipiza kisasi cha mabao 2-0 ilichopewa na wapinzani wao hao kwenye pambano lililochezwa jijini Mwanza, Oktoba 21, mwaka jana.
Kocha huyo alisema kuwepo kwa muda mrefu kabla ya pambano hilo, kutawapa fursa nzuri ya kurekebisha makosa yaliyowagharimu katika mchezo wao na Mtibwa Sugar ambao kwa ushindi huo imeweza kufikisha pointi 30 na kung'ang'ania nafasi yake ya nne waliopo.

***
Prisons yazifunda zilizopanda


TIMU ya Prisons ya Mbeya, imezitaka timu zinazoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara kukomaa na kutokubali kushuka daraja kirahisi kwa sababu, huko chini ni kugumu mno.
Prisons imetahadharisha kuwa bora hata hiyo Ligi Kuu yenyewe kuliko ligi daraja la kwanza Tanzania Bara ambapo kila timu inakuwa inatafuta nafasi ya kupanda daraja.
Katibu wa timu hiyo Antony Hau amesema tangu timu yao ishuke daraja miaka miwili iliyopita imekuwa ikijitahidi kupanda bila mafanikio kutokana na ugumu uliokuwepo.
"Yaani naziambia timu zinazoshiriki Ligi Kuu zikomae zisishuke daraja huku ni hatari, kubaya, ni kugumu sana, huko juu unakutana na timu zilizogawanyika, zingine zinataka ubingwa, zingine kubaki daraja, huku kila mmoja anataka kupanda kwa hiyo ligi inakuwa ngumu sana, " alisema.
Pamoja na hayo, Hau amesema kuwa utaratibu wa kutafuta timu za kupanda Ligi Kuu wa kuweka kituo kimoja kama michuano fulani haufai.
"Maana ya ligi ni timu zizungukane, zicheze nyumbani na ugenini, sasa ligi ya kituo kimoja, si ligi kwa maana ya ligi ni michuano fulani tu au kombe," alisema.
Alishauri kuwa ligi daraja la kwanza iwe inachezwa nyumbani na ugenini kama Ligi Kuu ili timu ziwe na nafasi pana ya kucheza mechi nyingi na pia kuondoa uwezekano au hisia ya mwenyeji kubebwa na kupanda daraja.
Ligi daraja la kwanza Tanzania Bara imemalizika na tayari timu za Coastal Union, Villa Squad, JKT Oljoro, na Moro United zimefanikiwa kuingia Ligi Kuu.
***

Pondamali:Haya yataibeba Villa Ligi Kuu


BAADA ya kuirejesha Villa Squad katika Ligi Kuu Tanzania Bara, kocha wa timu hiyo, Juma Pondamali 'Mensah' ameupa uongozi wa klabu hiyo mambo manne ya kuyatekeleza iwapo wanataka Villa isishuke tena daraja.
Villa ambayo ilishuka daraja msimu wa 2008-2009, ilirejea tena kwenye ligi hiyo baada ya kushika nafasi ya tatu katika Ligi Daraja la Kwanza ikiungana na timu za JKT Oljoro, Coastal Union na Moro United.
Kutokana na kutambua ugumu wa Ligi Kuu ulivyo kocha, Pondamali alisema ni vema uongozi wa klabu ya Villa ukajipanga mapema kuhakikisha timu yao hairejei ilikotoka kwa kufanya mambo manne muhimu ambayo anaamini yakaibeba klabu hiyo.
Pondamali, kipa wa zamani wa kimataifa aliyewahi kung'ara na klabu za Pan Afrika, Yanga na AFc Leopard, alisema jambo la kwanza ambalo uongozi wa Villa unapaswa kutekeleza ni kuongeza wachezaji wapya 12 katika kikosi chao ili kukiimarisha.
"Kikosi kinahitaji wachezaji wapta 12 kwa ajili ya kukiimarisha, hivyo ni vema uongozi ukalitekeleza hilo, Ligi Kuu Tanzania Bara ni ngumu na ina ushindani hivyo inahitaji wachezaji mahiri na wenye uwezo wa kuibeba timu," alisema.
Aliongeza kuwa jingine ni viongozi kuzungukia na kuhudhuria kwenye michuano yote ya ya mchangani kwa nia ya kusaka wachezaji wapya, akidai mbinu hizo ndizo zilizoisaidia na kuipa sifa Ashanti United iliwahi kutamba kwenye ligi kuu msimu kadhaa iliyopita.
"Mambo hayo yakifanywa naamini Villa tutadumu kwenye ligi, vinginevyo hata mie sintoweza kuendelee kukaa na klabu hiyo, hilo naliweka wazi," alisema Pondamali ambaye pia ni kocha wa makipa wa timu ya taifa, Taifa Stars akisaidiana na Mdemark Jan Poulsen.
Pondamali alitoa mapendekezo hayo katika mahojiano na kituo cha Radio One, akizungumzia mafanikio ya timu yake kurejea ligi kuu na mikakati ya kuzuia isishuke tena kama awali.
***

Mao, ahofia ratiba ya Ligi Kuu


KIUNGO mahiri wa timu ya soka ya Azam, Himid Mao, amedai ratiba ya Ligi Kuu Tanzania Bara bado inaonyesha hali ya upendeleo kwa baadhi ya timu kitu ambacho amesema sio haki.
Mao, mtoto wa kwanza wa nyota za zamani wa kimataifa nchini, Mao Mkami aliyewahi kung'ara na timu za Pamba na Simba, alisema ni vema TFF ikaangalia upta ratiba ya ligi hiyo.
Kiungo huyo aliyeteuliwa katika kikosi cha timu ya taifa ya vijana U23 kinachojiandaa kwenye Cameroon, alisema kwa ratiba iliyopo ni wazi ni vigumu kwa timu yao ya Azam kuendelea kukaa kileleni na kutwaa ubingwa.
"Ratiba ya sasa haitendi haki kwa baadhi ya timu, angalia Simba na Yanga zimecheza mechi chache, lakini bado wanapewa mapumziko marefu, hali ambayo haifanyi ligi iwe tamu, leo Azam tupo kileleni, lakini nafasi yetu sio ya kudumu kwa kuwa wenzetu wana mechi chache," alisema.
Alisema ni kweli vigogo hivyo vilikuwa vikiiwakilisha nchi kimataifa, ila kwa vile zilisharejea zingepaswa kucheza viporo vyao ili uwiano wa mechi uwe sawa na kuifanya ligi ichangamke zaidi.
Mao, alisema sio kama ana hofu ya timu yao kutwaa ubingwa, ila anaona kuwepo kwa tofauti na mechi kunaweza kutumiwa vibaya na timu zingine kuwavurugia mipango yao.
"Unajua kila mchezaji Azam akili yake kwa sasa ni kuona tunakuwa mabingwa, hivyo tunataka tufukuzane na wenzetu kama inavyotakiwa na sio kuachana kwa mechi katika ratiba kwani ni mbaya kwa upangaji wa matokeo," alisema.
Mkali huyo anayechekelea kuifungia timu yake kwa mara ya kwanza kwenye mechi za Ligi Kuu walipocheza na African Lyon na kuwalaza mabao 3-0, alisema anaamini pamoja na dosari ya ratiba bao Azam wataweka rekodi Tanzania Bara msimu huu.
Azam ambayo iliyokuwa ikiongoza kwenye msimamo wa ligi hiyo kabla ya mechi ya jana kati ya Simba na Mtibwa Sugar, ndio inayoongoza kwa kufunga mabao mengi hadi sasa ikiwa na mabao 32, yenyewe ikiruhusu mabao 11 tu.
***

Bakule ajiuengua TOT-Plus

MWANAMUZIKI Badi Bakule 'Jogoo la Mjini', amejivua uongozi wa bendi ya TOT-Plus 'Achinengule' ili kutoa nafasi kwa wengine kuongoza jahazi hilo.
Bakule, alimeiongoza TOT tangu mwaka 2005 alipowapokea Mwinjuma Muumin na Ally Choki waliowahi kuiongoza bendi hiyo kwa nyakati tofauti.
Akizungumza na Micharazo, Bakule alisema amelazimika kuachia ngazi kwa sababu chini ya uongozi wake haoni maendeleo yanayopigwa na bendi.
"Kila mwaka tumekuwa na mipango ya maendeleo isiyotekelezeka, hivyo bora niachie ngazi ili nipishe wenzangu kuongoza bendi," alisema.
Alisema amemuandikia 'bosi' wake, Kapteni Mstaafu John Komba kumjulisha rasmi dhamira yake na kwamba hatarajii kiongozi huyo kupinga uamuzi wake.
Alisema katika kipindi chote cha miaka mitano aliyokuwa kiongozi, hakuwahi kuamini kwamba Muumin na Choki waliondoka kwa sababu uongozi hautekelezi ahadi zake kwa vitendo, sasa ameamini.
"Naomba nieleweke kuwa sijaondoka TOT, nilichofanya ni kuachia ngazi nafasi ya uongozi baada ya kuona kwa muda wote huo bendi haipigia hatua za maendeleo na badala yake inazidi kuanguka," alisema Badi.
Alipoulizwa kuwa hatua hiyo inawezekana ni moja kati ya kuondoka kundini, Badi alisema kila jambo linawezekana na kwamba wakati wa kuamua vinginevyo ukifika anaweka wazi.
Micharazo ilipowasiliana na Komba kwa simu haikupokelewa ingawa taarifa zilizotufikia wakati tunakwenda mitamboni zinasema baada ya barua hiyo kumfikia mkurugenzi, alilazimika kuitisha kikao cha dharura na wanamuziki makao makuu ya bendi.
***
Extra Bongo kutoka mafichoni

BENDI ya Extra Bongo, iliyokuwa kambini karibu wiki tatu sasa, inatarajia kuvunja kambi hiyo na kuanza maonyesho yake kama kawaida.
Extra ilijichimbia kambini eneo la Mbezi Louis, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya maandalizi ya albamu yao mpya ya pili siku moja baada ya kuibomoa Africana Stars 'Twanga Pepeta' kwa kuwanyakua wanamuziki wake sita.
Ikiwa kambini, bendi hiyo pia imefanikiwa kurekodi video mbili za nyimbo zao za Neema na Under 18.
Kwa mujibu wa mkurugenzi wa bendi hiyo, Ally Choki Extra Bongo inatarajia kuingia mitaani kuanzia Ijumaa wiki hii itakapofanya onyesho maalum la kuwatambulisha wanamuziki wapya iliowachukua toka Twanga Pepeta.
Choki alisema onyesho hilo litafanyika katika ukumbi wa New Msasani Club na kufuatiwa na lingine la Jumamosi litakalofanyika katika ukumbi wa TCC-Chang'ombe.
"Jumapili tutarudi rasmi katika ukumbi wetu wa nyumbani wa Mango Garden ili kuendelea kutoa burudani sambamba na kuwatambulisha wanamuziki wapya," alisema.
Wanamuziki hao wapya ni Super Nyamwela, Super Danger, Otilia Boniface (wanenguaji) Hoseah Mgohachi (besi), Saulo John 'Ferguson' na Rogert Hegga (waimbaji).
Aliongeza kuwa kwa sasa bendi hiyo imekuwa ikifanyia mazoezi nyimbo nyingine mpya za 'Fisadi wa Mapenzi' na Chuki ambazo ni miongoni mwa zile zitakazokuwa kwenye albamu hiyo ya pili, huku wakiwa wanatambia mtindo na rapu mpya kutoka kwa wakali hao wapya.

Simba, Mtibwa ni kisasi kitupu kesho





SIMBA na Mtibwa Sugar kesho zinakutana katika mechi yenye sura na mvuto wa pekee kwa aina yake ligi kuu bara, huku wekundu hao wa Msimbazi wakipania kuiporomosha kileleni mwa msimamo Azam FC na wapinzani wao wakipania kulipa kisasi cha kupoteza mechi ya kwanza.
Hata hivyo ushindi kwa Simba utawapeleka kileleni kwa muda tu, kwani watani wao wa jadi--Yanga wanaoshika nafasi ya pili wanaweza kuwashusha juu iwapo wataifunga Ruvu Shooting keshokutwa uwanja wa Uhuru.
Azam ina pointi 35 sawa na Yanga, lakini vijana wa Jangwani wako nyuma kwa tofauti ya mabao ya kufungwa na kufunga, na Simba inaweza kufikisha pointi 37 kama itashinda mchezo wa kesho.
Kwa upande wao Mtibwa wenye kumbukumbu nzuri ya kuwalaza Yanga, wamepania kuwazima vigogo Simba, na iwapo hilo litatimia watakuwa wamekaza mwendo wa kuelekea kileleni kwa kufikisha pointi 33.
Mtibwa imetangaza vita kwa Simba kutokana na kipigo cha bao 1-0 kwenye mechi ya kwanza iliyoghubikwa na mazingira ya tuhuma za rushwa kabla ya mechi kuchezwa.
Mtibwa itamkosa mlinda mlango wake namba moja, Shaaban Kato ambaye anatumikia adhabu ya kutocheza mechi kufuatia kuonyeshwa kadi nyekundu kwenye mechi dhidi ya Toto Afrika ya Mwanza.
Kocha msaidizi wa Mtibwa, Mecky Mexime na bosi wake Tom Olaba, kila mmoja kwa nyakati tofauti wamesema wamejiandaa kushinda mechi hiyo.
"Nia yetu si kulipa kisasi tu, tumepania kushinda mechi zote zilizosalia na kutwaa ubingwa," alisema Maxime.
Olaba alilalamikia kadi nyekundu ya Kado, lakini hata hivyo alisema kukosekana kwa mlinda mlango huyo si tatizo la kuwanyima ushindi.
"Kwetu sisi hakuna mechi rahisi, hivyo maandalizi tunayofanya ni kwa ajili ya mechi ngumu," alisema Mexime, nahodha wa zamani wa Mtibwa na Taifa Stars.
Simba wenyewe waliokutana jana kujadili mambo mbalimbali, wamesema wamepania ushindi kabla ya kwenda Zanzibar kuiwekea kambi Simba.
Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala, alisema wamejiandaa vizuri kwa mechi hiyo.
"Tukimaliza mechi, Jumatatu asubuhi tunakwenda Zanzibar kwa ajili ya kuweka kambi kabla ya mechi inayofuata," alisema Mtawala.
Mtawala alisema Simba itaenda Zenji na kikosi chake chote isipokuwa Uhuru Seleman ambaye bado anauguza goti, huku Emmanuel Okwi, Joseph Owino na Hillary Echessa wakirejea toka kwenye majeruhi.
Simba na Yanga zinatarajiwa kukutana kwenye mechi ya marudiano itakayochezwa Machi 5 kwenye dimba la Taifa, Simba ikiwa na deni la kipigo cha bao 1-0 iliyopewa na Yanga kwenye mechi ya awali iliyochezwa jijini Mwanza kwa bao tamu la Jerry Tegete.
Mwisho

Simba wazidi kuikamia Mazembe

BAADHI ya nyota wa klabu ya Simba, wametamba kuwa hawana hofu yoyote juu ya pambano lao dhidi ya TP Mazembe ya DR Congo kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Wachezaji hao wa Simba wamesema licha ya kutambua ugumu watakaopata kwa wapinzani wao ambao ni mabingwa watetezi, bado wana imani ya kurejea rekodi ya mwaka 2003 walipoing'oa waliokuwa mabingwa watetezi wa michuano hiyo, Zamalek ya Misri.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti na gazeti hili katikati ya wiki iliyopita, wachezaji wa Simba walisema kama wawakilishi wa Tanzania wataendelea kupigana kiume kuona wanasonga mbele hata kama TP Mazembe wanatisha kwa sasa katika soka la kimataifa.
Beki wa kushoto wa Simba, Juma Jabu, alisema kama mabingwa wa Tanzania wataenda Congo kupigana kiume kuipeperusha bendera ya nchi kwa kushinda, ingawa wapo watu wanaoikatia tamaa.
Jabu, alisema hata mwaka 2003 Simba ilipuuzwa ilipopangwa na Zamalek, lakini walipigana kiume na kuing'oa mabingwa hao watetezi jambo linalowezekana kutokea msimu huu.
"Hakuna ubishi Mazembe ni wazuri na wanatisha Afrika na Dunia kwa ujumla, lakini kama wawakilishi hatutishwi nao, tutapigana kiume ili kusonga mbele, muhimu Watanzania watupe sapoti badala ya kutukatisha tamaa," alisema Jabu maarufu kama JJ.
Mchezaji mwingine aliyejinadi kutokuwa na hofu na Mazembe ni Rashid Gumbo, aliyekiri ni kweli Mazembe wanatisha, lakini bado wanaweza kufungika kama timu zingine muhimu mipango mizuri na kujituma kwao uwanjani.
"Tukijipanga na kucheza jihad uwanjani tunaweza kuweka maajabu, TP Mazembe ni timu kama timu zingine licha ya kuwa tishio, tutapigana kuhakikisha tunashinda," alisema Gumbo.
Kauli ya wachezaji hao zimekuja wakati wadau wengi wa soka wakiwemo wanaojiita wachambuzi wakiikatisha tamaa Simba kwa madai haiwezi kutoka kwa mabingwa hao watetezi katika mechi zao za raundi ya kwanza .
Simba ilipata fursa hiyo kwa kuing'oa Elan de Mitsodje ya Comoro kwa jumla ya mabao 4-2, ambapo katika mechi ya awali ilitoka suluhu ugenini kabla ya kushinda mechi ya marudiano iliyochezwa uwanja wa Uhuru Dar es Salaam.

Mwisho

Friday, February 25, 2011

NYota wa Simba waikamia Mtibwa Sugar J'pili

BAADHI ya nyota wa timu ya Simba, wametamba kuwa wataisambaratisha Mtibwa Sugar watakaoumana nao siku ya Jumapili.
Mabingwa hao watetezi wataikaribisha Mtibwa kwenye uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam katika pambano la mfululizo wa michuano ya Ligi Kuu Tanzania Bara.
Katika mechi yao ya awali iliyochezwa mjini Morogoro na kughubikwa na kashfa ya rushwa, Simba iliisambaratisha Mtibwa kwa bao 1-0.
Pamoja na kutambua ugumu wa pambano hilo, ambalo Mtibwa wameshanadi kutaka kulipiza kisasi na kujiweka kwenye nafasi nzuri katika msimamo wa ligi hiyo, wachezaji wa Simba wamedai hawatishiki kwa kuamini watashinda.
Juma Jabu 'JJ' beki wa kushoto wa mabingwa hao watetezi, alisema anaamini mechi ya kesho itakuwa na matokeo mazuri kwao kutokana na kiu yao ya kutaka kutetea tena taji lao.
"Hatuna shaka Mtibwa tutawasambatarisha, ili tuweze kutimiza lengo letu la kutetea taji, hivyo wanasimba wasiwe na hofu," alisema Jabu.
Jabu, alisema wanataka kushinda mechi hiyo ili kujiweka vizuri kabla ya kuvaana na watani zao, Yanga Machi 5 kisha kwenda kuvaana na TP Mazembe kwenye mechi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Naye kiungo mshambuliaji, Rashid Gumbo alijinasibu hana hofu na mechi hiyo ya kesho wala ile ya watani zao, Yanga.
Gumbo, alisema hawawezi kurudia makosa waliyofanya kwenye pambano lao na Toto Afrika ambapo walilazimishwa sare ya 2-2 na hivyo kuitahadharisha Mtibwa ikae chonjo kwa kipigo.
"Wasitarajie mteremko, hatufanyi makosa kama ya Mwanza, tulipolazimishwa sare na Toto," alisema Gumbo mmoja wa wafungaji vinara wa klabu hiyo.
Kama Simba itaifunga Mtibwa ni wazi itarejea kileleni tena ikiiengua Azam, lakini itaombea pia watani zao watakaoshuka dimbani Jumatatu wafanye vibaya ili wasiporomoshwe kwenye msimamo kabla ya kukutana Machi 5.

Mwisho

Mwaisabula aungana na OLaba kumsikitia Kado

KOCHA wa zamani wa klabu ya Yanga, Kennedy Mwaisabula, ameungana na kocha wa Mtibwa Sugar, Tom Olaba kuilalamikia kadi nyekundu aliyopewa kipa Shaaban Kado, siku chache kabla ya kuvaana na timu ya Simba.
Kado, anayeichezea pia timu ya taifa, Taifa Stars, alionyeshwa kadi hiyo katika mechi baina ya timu yake na Toto Afrika na kumfanya alikose pambano la kesho dhidi yao na Simba litakalochezwa kwenye uwanja wa Uhuru, jijini Dar.
Mwaisabula maarufu kama 'Mzazi' alisema kitendo cha Kado kulikosa pambano la kesho limepunguza ladha kutokana na ukweli kipa huyo ndiye mhimili wa Mtibwa Sugar na hivyo kuipungizia nguvu timu yake.
Kocha huyo aliyewahi kuzinoa timu kadhaa ikiwemo Bandari-Mtwara, Cargo, Twiga Sports, Villa Squad na TMK United, alisema kwa jinsi mazingira ya kadi hiyo ilivyotolewa huko Mwanza anahisi kama kuna 'mchezo mchafu'.
Alisema japo hana hakika, lakini huenda kadi hiyo imetolewa kwa nia ya kuidhofisha Mtibwa katika mechi yao ya kesho, kitu alichodai mambo kama hayo yanachangia kuporomosha kiwango cha soka la Tanzania.
"Nadhani ifikie wakati mambo kama haya ya ujanja ujanja kwa nia ya kuzibeba timu kubwa zikaachwa ili soka lisonge mbele, nimesikitishwa na kadi ya Kado kwa vile imepunguza msisimko kwa pambano lao na Simba," alisema.
Kauli ya Mwaisabula imekuja siku chache, tangu kocha wa Mtibwa, Mkenya Tom Olaba kulalamikia kadi hiyo iliyotolewa na mwamuzi Judith Gamba, akidai imeinyong'onyesha timu yake kwa ajili ya pambano hilo dhidi ya Simba.
Kado alipewa kadi na mwamuzi huyo baada ya kuilalamikia penati iliyopewa wenyeji wao, Toto Afrika ambapo pambano lilishia kwa Mtibwa kushinda 2-1.

Mabondia kuzipiga kuwachangia wahanga wa mabomu


MABONDIA mbalimbali kutoka mikoa tofauti wanatarajiwa kupigana katika michuano maalum kwa nia ya kusaka fedha za kuwasaidia wahanga wa milipuko ya mabomu ya Gongo la Mboto, jijini Dar es Salaam.
Michuano hiyo itakayochezwa sehemu nne tofauti ndani ya mikoa ya Dar, Pwani na Morogoro, imeratibiwa na kampuni ya Funiko Inc, chini ya uratibu wa mkurugenzi wake, Rowland Raphael Chulu 'Chen Lee Master'.
Chulu alisema michezo ya kwanza itafanyika kwenye ukumbi wa Hugho Tower Pub, Kigogo-Mburahati Machi 6, ambapo yeye atapigana na K kutoka Tanga pamoja na kusindikizwa na mapambano mengine ya utangulizi.
Aliwataja mabondia wengine watakaopigana siku hiyo ni Deus Tengwa atakayepigana na Kitonge wa Arusha, Abbas dhidi ya Abuu, Rahim Cobra na Abdul, Masoud Fighter dhidi ya Mrisho Mwana, Husseni Magali na Idd Rashid na Said Omary atapigana na Jembe wa Majembe.
"Pambano la pili litafanyika Machi 13 eneo la Bunju kwenye ukumbi wa Proud Tanzania, ambapo nitarudiana na K, na wiki inayofuata tutakuwa Bagamoyo kwenye ukumbi wa Police Mass ambapo nitachapana na Juma wa huko huko," alisema.
Alisema onyesho la tatu litachezwa kwenye ukumbi wa Makuti-Pub, Ifakara mkoani Morogoro kwa kuumana na Charles wa huko wakisindikizwa na michezo mingine ya utangulizi.
Chulu, aliyewahi kung'ara kwenye Kick Boxing kabla ya kutumbukia kwenye utayarishaji wa filamu nchini, alisema fedha zote zitakazopatikana kwenye maonyesho ya michezo hiyo zitapelekwa kwa wahanga.
Tangu tukio la milipuko ya mabomu litokee wiki mbili zilizopita watu mbalimbali wamekuwa wakitolea kuwasaidia wahanga, ambapo kesho kwenye uwanja wa Uhuru wasanii wa Bongofleva na wale wa filamu wataumana kusaka fedha za kuwasaoidia wahanga hao wa Gongo la Mboto.

Mwisho

Thursday, February 24, 2011

20% kuzindua Malumbano J'pili





MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Abbas Hamis Kinzasa '20 Percent' anatarajia kuzindua na kuitambulisha rasmi albamu yake mpya iitwayo 'Ya Nini Malumbano' siku ya Jumapili.
Uzinduzi huo utakaosindikizwa na wasanii kadhaa nyota nchini unatarajiwa kufanyika kwenye ukumbi wa Club Masai, Oysterbay jijini Dar es Salaam chini ya utaribu wa kampuni ya King Kif Entertainment.
Akizungumza na Micharazo leo asubuhi, mkurugenzi wa kampuni hiyo, Sigfred Kimasa 'King Kiff', alisema maandalizi ya onyesho hilo yamekamilika ikiwemo wasanii nyota kibao kukubali kumsinidikiza mkali huyo ambaye anasifika kwa nyimbo zenye mafunzo na ujumbe mwanana.
"Msanii 20 Percent atazindua albamu yake ya Ya Nini Malumbano, akisindikizwa na wasanii kadhaa nyota, katika onyesho litakalofanyika Jumapili kwenye ukumbi wa Club Maisha," alisema.
Aliwataja wasanii watakaomsindikiza mkali huyo ambaye pia ni mahiri katika uigizaji filamu ni pamoja na 'swahiba' wake, Seleman Msindi 'Afande Sele'. Man Wter ambaye pia ni mtayarishaji wa albamu hiyo, Ney wa Mitego, Sajna, Linex na Uncle G.
Mbali na kibao cha Ya Nini Malumbano, albamu hiyo ya 20 Percent ina nyimbo nyingine kama Tamaa Mbaya ambao umekuwa ukitamba kwenye vituo kadhaa vya redio nchini, Neno la Mwisho na Nimerudi Salama.
Nyimbo nyingine ni Nyerere, Nia Yao, Mwema, Naficha, Kubadili Mwendo na Ya Nini Malumbano.
Hiyo ni albamu ya tatu ya msanii huyo ambaye anatamba pia na nyimbo za Money Money, Bangi na nyingine, awali alitoa albamu za Money Money na Mama Neema ambazo zinadaiwa kufanya vema sokoni licha ya nyimbo zake kumpa tuzo kadhaa za muziki nchini.

.

Tuesday, February 22, 2011

Dokii ana scandal na JB



MSANII nyota wa muziki na filamu, Ummy Wenceslaus 'Dokii' amefyatua kazi yake mpya iitwayo 'Scandal' iliyowashirikisha wakali kadhaa wa fani hiyo nchini.
Filamu hiyo inayozungumzia masuala ya mapenzi na hila za baadhi ya watumishi wa Mungu, inatarajiwa kuachiwa mitaani kuanzia mwezi ujao ikiwa imetungwa na Dokii mwenyewe na kuongozwa na Adam Kuambiana.
Akizungumza na micharazo, Dokii, aliyeng'ara na michezo ya kuigiza kupitia kituo cha ITV akiwa na kundi la Mambo Hayo, alisema ndani ya filamu hiyo aliyoitunga mwenyewe, kuna wasanii mahiri kama Jacob Stephen 'JB'.
"Baada ya kimya tangu nilipoachia filamu ya Money Transfer, nimekamilisha kazi mpya iitwayo Scandal' ambayo nimeigiza na wasanii kadhaa nyota akiwemo mkali, JB, Colleta Raymond, Tini White na wengine," alisema Dokii.
Dokii aliwataja wasanii wengine waliopo ndani ya filamu hiyo ni pamoja na Jacqueline Pentezel 'Jack wa Chuz', Ramadhani Ally 'Taff', Tini White, Kishoka na wengine.
"Ni filamu ya kusisimua kwa jinsi ilivyoigizwa na ujumbe uliopo ndani ya kazi hiyo mpya," alisema Dokii.
Dokii, ambaye pia ni muimbaji wa muziki wa Injili amewahi kutamba na filamu kama Yoland, Hard Love Moro, Bad Friend, My Nephew, Lonely Heart na nyinginezo.
Kwa muda mrefu msanii huyo alikuwa wakiwachanganya mashabiki wake wakidhani ni Mkenya kutokana na kupenda kwake kuigiza lafudhi ya taifa hilo, ingawa ukweli yeye ni mwenyeji wa mkoa wa Morogoro.

Mwisho

Msalaba Wangu upo kwa Teddy

MTUNZI anayekuja juu katika fani ya utunzi wa riwaya, Teddy Chacha, amejitosa kwenye filamu na kuibuka na kazi mpya iitwayo 'Msalaba Wangu'.
Filamu hiyo inayozungumzia masuala ya kijamii na hasa kuwepo kwa imani potofu juu ya watu wenye ulemavu, imeshirikisha 'vichwa' kadhaa nyota vya fani ya uigizaji nchini akiwemo Pembe, 'Bi Hindu' na Charles Magali 'Mzee Magali'.
Akizungumza na Micharazo, Teddy alisema filamu hiyo ni zao la moja ya hadithi zake zinazochapishwa kwenye magazeti mbalimbali likiwemo NIPASHE, ambapo inazungumzia familia moja inayomkataa mtoto wao aliyezaliwa mlemavu wa akili.
Teddy, alisema filamu hiyo ni kama simulizi la kweli kutokana na kisa alichowahi kusimuliwa na kusema ni moja ya kazi yenye kuelimisha na kuiasa jamii juu ya kuepukana na mila na desturi potofu.
"Ni moja ya kazi yenye mafunzo na hasa kutokana na wahusika kubeba uhusika wao kwa kiwango cha hali juu," alisema Teddy.
Aliongeza kuwa filamu hiyo aliyotunga na kuiongoza mwenyewe, imerekodiwa na kampuni ya Magambo Entertainment na kwa sasa inamalizwa kuhaririwa kabla ya kutafutiwa soko tayati kuwapa wadau wa filamu burudani yenye mafunzo kwao.
Teddy, aliwataja washiriki wa filamu hiyo ni pamoja na Pembe, Bi Hindu, Mzee Magali, mtoto Yasin Kamba ambaye ndiye mhusika mkuu, Mohammed Hamis, Josephine Joseph na wengine.

Aisha Bui: Kisura anayetamba Bongo Movie




HANA muda mrefu tangu atumbukie kwenye faini ya uigizaji, lakini makali yake kupitia baadhi ya kazi alizoshiriki, zimemfanya Aisha Fat'hi maarufu kama Aisha Bui, kuwa tishio kwa waigizaji wakongwe wa kike.
Mwenyewe anakiri aliingia rasmi kwenye fani hiyo mwaka juzi kutokana na kuvutiwa na Wema Sepetu, licha ya kudai alipenda uigizaji licha ya kutowahi kujaribu tangu alipokuwa mdogo.
"Wema ndiye aliyechangia kujiingiiza kwangu kwenye filamu kutokana na kuvutiwa nae, ila tangu utotoni nilikuwa naipenda fani hiyo sambamba na ile ya uchoraji," alisema.
Alisema alipenda sana kuchora utotoni, kipaji ambacho anaamini kama angekiendeleza angefika mbali kwa vile alikuwa mahiri kuliko maelezo.
Filamu yake ya kwanza kumtangaza mwanadada huyo ni My Book, kisha kushiriki zingine kama Saturday Morning, Better Days, Not Without My Son, Continous Love na sasa ameibuka na Second Wife.
Aisha anayependa kuogelea, kufanya mazoezi na kupika, alisema kati ya kazi zote alizoshiriki ile ya Saturday Morning ndio filamu bomba kwake kwa jinsi alivyoigiza kwa umahiri.
"Saturday Morning, ndiyo picha kali kwangu wala sio siri," alisema kisura huyo.
Akiwa na ndoto za kuja kuwa muigizaji wa kimataifa, Aisha anasema hakuna anachochukia maishani mwake kama dharau ya uongo.
"Uongo na kufanyiana dharau ni vitu nisivyopenda maishani mwangu,"
Aisha Fat'hi aliyezaliwa mwaka 1983, alisema fani ya filamu nchini inazidi kupiga hatua, ingawa alisema bado haijawa na tija ya kutosha kutokana na kuwepo kwa wizi wa wajanja wachache.
Kisura huyo ambaye waliwahi kuhusishwa na marehemu Meddy Mpakanjia, hajaolewa wala
hana mtoto na mipango yake ni kujikita zaidi katika fani hiyo ili afike mbali ikiwezekana aje kumiliki kampuni yake binafsi ya kuzalisha filamu.
"Hizi ndizo ndoto zangu, kutamba kimataifa na kuja kumiliki kampuni yangu binafsi," alisema.
Aisha, alisema kwa umri wake na kiu ya mafanikio aliyokuwa nayo naamini atafika huko
akutakapo, muhimu Mungu amjalie umri na afya njema.

Saturday, February 19, 2011

Nyalawila apigiwa debe, Cheka ajipanga





MAPROMOTA wa Ngumi za Kulipwa nchini, wameombwa kujitokeza kumuandalia pambano la utetezi Bingwa wa Dunia wa WBF, Karama Nyalawila, ili asipoteze taji hilo.
Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO, Yasin 'Ustaadh' Abdalla, alisema ili kumuepushia Nyalawila asipoteze taji lake alilotwaa mwishoni mwa mwaka jana nchini Ukraine ni vema mapromota wakajitokeza kumuandalia pambano la utetezi.
Ustaadh, alisema kwa kanuni zilizopo katika mchezo huo, bingwa yeyote akikaa muda mrefu bila kupigana, hupoteza sifa ya kushikilia taji na hivyo anahofia yasije yakamkuta Nyalawila.
"TPBO tunawaomba waratibu wa michezo ya ngumi za kulipwa nchini kumuandalia pambano Nyalawila ili kutetea taji na kuepuka kulipoteza taji hilo lenye hadhi kubwa katika mchezo huo duniani," alisema Usraadh.
Rais huyo alisema oganaizesheni yake ipo tayari kufanya kazi na promota yeyote atakayekuwa tayari kumuandalia bingwa huo wa WBF pambano hilo kwa lengo la kutaka Tanzania iendelee kung'ara kimataifa.
Alisema kwa kitambo kirefu mabondia wa Tanzania wameshindwa kung'ara kimataifa na hivyo ni vema Nyalawila, Francis Cheka na wengine wanaoshikilia mataji wakawa wanapewa kipaumbele kuandaliwa michezo.
Katika hatua nyingine, bingwa wa dunia wa WBC, UBO, ICB, Francis Cheka, anajifua kujiandaa na pambano lake la kuwania taji la IBF litakalofanyika April 2, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na Micharazo toka Morogoro, Cheka, alisema pambano lake litafanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee na atapigana na Mmarekani, Marcus Upshaw.
"Natarajia kupanda ulingoni April 2 kwa kuzichapa na Mmarekani ambaye jina lake limenitoka, katika kuwania mkanda wa IBF uzito wa kilo 72," alisema.
Hilo litakuwa pambano la kwanza kwa Cheka tangu alipomshindwa kwa pointi Bingwa wa Afrika Mashariki na Kati, Mada Maugo katika pambano lisilo la mkanda lililochezwa Januari Mosi, kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar.

Mwisho

Msama Promotion yawasaidia Wahanga wa Mabomu Gongo la Mboto






WAHANGA wa milipuko ya mabomu yaliyotoka eneo la Gongo la Mboto, wameendelea kupewa misaada, baada ya Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha la Pasaka nchini, Alex Msama kutoa misaada ya vyakula.
Misaada hiyo yenye thamani ya karibu Sh. Mil. 3, ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Msama kupitia kituo cha runinga cha Cloud's, kwa lengo la kufikishwa kwa waathirika na milipuko hiyo iliyotokea katikati ya wiki kwenye kambi ya Jeshi la Wananchi Tanzania, JWTZ, kikosi cha 521 KJ.
Msama alisema kama sehemu ya jamii walioguswa na tukio la milipuko hiyo ya mabomu wameamua kutoa misaada hiyo kuitikia wito wa serikali, huku akiwahimiza watu wengine wenye uwezo kufanya hivyo.
"Tusiiachie serikali pekee yake kufanya kazi hii, ndio maana sisi kama sehemu ya jamii tumeamua kutoa msaada huu japo mdogo, lakini uwasaidie wenzetu walioathirika na tukio hilo linalosikitisha," alisema Msama.
Msaada huo uliotolewa ni magunia manne ya Mchele, Unga wa Ngano gunia 10, gunia mbili za Maharage na Sukari pamoja na ndoo mbili za mafuta ya Gunia za maharage na ndoo mbili za mafuta ya kupikia.
Msama alisema, pamoja na msaada huo, kamati yao inafanya mipango zaidi ya kuongeza misaada yao kwa wahanga hao kwa nia ya kuisaidia serikali na asasi nyingine zilizojitolea kwa hali na mali kuwafariji waathirika wa mabomu hayo.
Tukio la ulipukaji wa mabomu la Gongo la Mboto ni la pili katika kipindi cha karibu miaka miwili, baada ya awali kulipuka April 29, mwaka juzi kambi nyingine ya jeshi eneo la Mbagala, pia jijini Dar es Salaam.
Katika tukio hilo la pili, karibu watu 20 wakiwemo watoto wameripotiwa kupotea uhai wao, huku wengine wanaokadiriwa kufikia 400 wakijeruhiwa, mbali na kusababisha uharibifu wa mali na miundo mbinu kadhaa.
Tayari serikali imetangaza kuwalipa fidia wote walioathirika na tukio hilo, ambalo lilitokea majira ya usiku, siku ya Jumatano na kuleta taharuki kwa wakazi wengi wa jijini na wale wa mikoani.

Mwisho

Tuesday, February 15, 2011

TAMAGSARAI na mikakati yao dhidi ya uboreshwaji masoko


KUTOKANA na kuona hawana sauti ya pamoja na mahali pa kusemea matatizo na kero zinazowakabili katika shughuli zao, wauzaji wa mazao ya nafaka katika soko maarufu la Tandale waliamua kuunda umoja wao kama njia ya kupigania na kutetea haki zao.
Umoja huo wa wauza nafaka hao unafahamika kwa kifupi kama TAMAGSARAI ambao ni kifupi cha Umoja wa Wauza Nafaka na Wawekezaji wa Soko la Tandale kwa lugha ya Kiingereza na ulianzishwa rasmi mwaka 2000 ingawa usajili wake ulipatikana mwaka 2003.
Malengo makubwa ya umoja huo ulioasisiwa na watu 45 chini ya Uenyekiti wa Abeid Hamad Lunda na katibu Abdul Kambaya, mbali na kuwa sauti ya pamoja katika utatuzi wa kero na matatizo yao, pia kutaka kubadilisha mazingira na hali ya soko hilo na mengine Tanzania.
Mwenyekiti wa sasa wa umoja huo, Juma Dikwe, alisema masoko mengi nchini likiwemo lao la Tandale yana mazingira duni, machafu na hayavutii, kiasi kwamba yamekuwa yakikimbiwa na baadhi ya watu wanaoenda kwenye masoko ya kisasa maarufu kama 'Super Market'.
Dikwe, alisema kitu cha kinachowauma ni kwamba pamoja na masoko kuwa katika mazingira duni na machafu, kosi na ushuru utozwa kila siku na hazijulikani wapi zinapoenda wakati zilihitajiwa kuboresha masoko husika.
"Tunalipishwa kodi na ushuru, tegemeo letu fedha hizo zingerudi tena kwetu kwa kuboresha maeneo yetu ya kazi, lakini cha ajabu masoko yanakuwa machafu na kuhatarisha maisha yetu," alisema Dikwe.
Mwenyekiti huyo, alisema hata hivyo wanashukuru miaka karibu 10 tangu umoja wao uanzishwe wameweza kuielewesha serikali na kusaidia kuboresha soko lao na wanapigana zaidi kuona masoko mengine nayo yanakuwa katika na mazingira mazuri ya kufanyia kazi.
Alisema karibu masoko yote nchini hufanana kimazingira na hivyo ni vema yakafanyiwa marekebisho kuendana na wakati, ili kusaidia biashara kufanyika vema na kusaidia kuinua kipato cha wafanyabiashara, wakulima na taifa kwa ujumla.
Tangu umoja huo ulipoanzishwa hadi sasa una wanachama 105 ikiwa ni ongezeko la wanachama zaidi ya 60 kwa kipindi cha miaka saba iliyopita, huku ukiwa umesaidia kuandaa semina na mafunzo mara tatu kwa lengo la kuwaelimisha wanachama wao.
Semina ya kwanza ilifanyika mwaka 2007 iliyohusumu Elimu ya Utawala Bora iliyowahusisha viongozi wa serikali za mitaa na wanachama wao kwa lengo la kusimamia utekelezaji wa shughuli za serikali kwa ufanisi ikiwemo sekta ya masoko.
Kisha mwaka 2009 waliandaa mafunzo mengine yaliyohusu ufuatiliaji wa fedha za umma zilizotengwa kwa ajili ya sekta ya Masoko na mwaka huu waliandaa nyingine iliyohusu Usimamiaji wa Miradi na Rasilimali za Masoko ikiwa ni mradi wa miaka mitatu mfululizo.
Dikwe, alisema mradi huo, semina na mafunzo ya awali yaliandaliwa na umoja wao kwa msaada na ufadhili wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii, The Foundations for Civil Society na imekuwa ikiwahusisha wanachama wao na wachuuzi wengine wa masoko ya jijini Dar es Salaam.
"Mradi huu Usimamiaji wa Rasilimali za Masoko, ni wa miaka mitatu na tunashirikisha wachuuzi wa masoko karibu yote ya wilaya tatu za mkoa wa Dar es Salaam kwa vile matatizo ya masoko yanafanana kwa kiasi kubwa," alisema.
Mbali na kuendesha miradi na semina hizo, TAMAGSARAI pia huwasaidia wanachama wao wanapopata matatizo kama ya kufiwa na mengineyo kupitia fedha zinazopatikana toka kwa wafadhili wao na zile za michango ya ada inayotozwa kwa kila mmoja wao.
Pia husimama kama wadhamini kwa wanachama wao katika hupatikanaji wa mikopo toka kwa asasi za kifedha, ili kurahisisha kuboresha shughuli zao na kuihimiza serikali kuboresha masoko kwa kujenga mabanda ambayo yanakithi haja ya matumizi ya binadamu.
"Mabanda mengi yaliyopo kwenye masoko yetu ni mafupi na hayana ubora na imekuwa chanzo cha vifo vya wanachama na wachuuzi wengine kutokana na magonjwa ya kuambukiza kama Kifua Kikuu, na Kipindupindu na Homa ya Matumbo nyakati za mvua," alisema.
Alisema kwa takwimu za haraka kwa kipindi cha miaka saba, wanachama na wachuuzi wenzao 15 kati ya 50 walioathirika kwa ugonjwa wa Kifua Kikuu walifariki, huku wengine wakinusurika vifo wakati wa msimu wa mvua kutokana na ugonjwa wa Kipindupindu.
"Kwa kweli soko la Tandale na mengineyo nchini ni machafu na yanatisha nyakati za mvua na ndio maana TAMAGSARAI tumekuwa tukipigania kuboreshwa kwake, ili kuwaokoa watumiaji wake yaani wauzaji na wateja ambao wengi wanayakambia na kutukosesha mapato," alisema.
Moja ya mikakati yao kwa sasa ni kutaka kuunganisha nguvu zaidi katika umoja wao na kupanua huduma zao kutoka soko la Tandale tu na kuwa la nchi nzima likiunganisha wachuuzi na wauzaji wote wa nafaka, kwa lengo la kuwa na sauti moja yenye nguvu.
Pia wanajaribu kusaka mbinu na kuwaelimisha wanachama wao na wachuuzi wengine kwa ujumla juu ya upakiaji na uuzaji wa bidhaa zao katika hali ya kisasa ili kuvutia wateja hata wale ambao wanayachukulia masoko mengi kama ya watu wanyonge na wasio na hadhi.
"Tuimeshaanza kuwapa mafunzo wanachama wetu ili kupakia bidhaa zao kisasa, badala ya kuendelea kutoa huduma kizamani ambayo inachangia watu kukimbilia Super Market wakiona ni usasa zaidi, ingawa bidhaa ni zile zile na pengine zetu ni bora zaidi, " alisema.
Msisitizo wa umoja huo wenye safu kamili ya uongozi uliochaguliwa baada ya kuongozwa kwa muda na viongozi waasisi ni kuitaka serikali kutumia kodi na ushuru wanaotoza kwenye masoko kuboresha mazingira na masoko hayo kusaidia ajira na vipato vya watumiaji wake.
"Pia tunataka fedha zinazotengwa na serikali kwa ajili ya kuboresha huduma za masoko zitumike kwa malengo yaliyowekwa badala ya kufanyiwa ubadhilifu na wachache wenmye jukumu la kusimamia masoko," alisema Dikwe.
Aliongeza, pia ni vema masoko yakamilikishwa kwa vyama au wafanyabiashara wenyewe badala ya kuachiwa mawakala ambao wapo kifedha zaidi bila kuangalia uboreshaji wa mazingira ya masoko hayo kulingana na kodi na ushuru wanaotoza kila siku sokoni hapo.
Safu nzima ya umoja huo ambao kwa sasa unasaka soko la bidhaa zao nje ya nchi ni Mwenyekiti wake ni Juma Dikwe, Makamu wake, Juma Janga, Abdul Kambaya ndiye ni Katibu, wakati Sadiki Kubiga niu Mhazini.

Mwisho