STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, October 22, 2013

Hivi ndivyo wakzzi Dar walivyojitokeza kumuaga Uncle J

 Msafara wa Magari ambao moja wapo (la mbele) likiwa limebeba jeneza lenye mwili wa marehemu Julius Nyaisanga ukiingia kwenye viwanja vya leaders muda huu kwaajili ya wakazi wa jiji la Dar kuweza kutoa heshima zao za mwisho kwa Mwili wa Marehemu Julius Nyaisanga kabla ya Kusafirisha Kwao Tarime Mkoani Mara

Baadhi ya Ndugu, Jamaa na marafiki wakibeba jeneza lenye Mwili wa Marehemu Julius Nyaisanga Kwaajili ya kupeleka sehemu husika tayari kwa kutoa heshima za mwisho kwa wakazi wa jiji la Dar waliofika katika viwanja vya leaders muda huu
Sehemu Jeneza lenye Mwili wa Marehemu Julius Nyaisanga litakapowekwa kwaajili ya wakazi wa jiji la dar kuweza kutoa heshima zao za mwisho kabla ya kusafirishwa kwenda Tarime Mkoani Mara
 Baadhi ya wakazi wa jiji la dar waliojitokeza katika viwanja vya leaders muda huu
Baadhi ya Wakazi wa Jiji la Dar wakisubiria Kutoa Heshima zao za Mwisho kwa Mwili wa Marehemu Julius Nyaisanga Kabla haujasafirishwa kupelekwa Kwao Tarime Mkoani Mara.Picha zote na Josephat Lukaza wa Lukaza blog

Wafuasi wa Sheikh Ponda kidedea


Sheikh Ponda Issa Ponda katika harakati zake

MAHAKAMA Kuu Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam imewaachia huru watu 52 wanaodaiwa kuwa wafuasi wa Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda, baada ya kuona kwamba sheria ilikosewa kwa kuwafunga kifungo cha mwaka mmoja.
Mahakama hiyo imesema kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ilipaswa kuwahukumu kifungo cha miezi mitatu tu.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Jaji Salvatory Bongole baada ya kusikiliza hoja za rufaa iliyokatwa na wafuasi hao kupitia wakili wa utetezi, Mohammed Tibanyendera.

“Mahakama hii imeona kwamba washtakiwa kukutwa na hatia ya kosa la kula njama adhabu yake siyo sahihi, nimeifutilia mbali, lakini nakubaliana na kosa la pili na la tatu wana hatia,” alisema na kuongeza:

“Adhabu ya mwaka mmoja mliyopewa naibatilisha, mtakwenda jela miezi mitatu kama sheria ya Jeshi la Polisi inavyosema au faini Shilingi  50,000.”

Jaji Bongole alisema washtakiwa hao walihukumiwa kwenda jela kutumikia kifungo cha mwaka mmoja Machi 21, 2013 mpaka sasa wametumikia zaidi ya miezi mitatu.
“Kwa kuwa wameshatumikia zaidi ya miezi mitatu, natamka kwamba nawaachia huru wote, kwa sababu adhabu yenu mmeitumikia na zaidi,” alisema Jaji Bongole.

Jaji Bongole alisema washtakiwa waliotiwa hatiani na kufungwa mwaka mmoja jela kwa makosa ya kula njama, kufanya mkusanyiko usio halali na kukaidi amri ya Polisi iliyokuwa ikiwazuia kufanya maandamano kuelekea katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) kushinikiza Sheikh Ponda kuachiwa kwa dhamana ni Salum Makame na wenzake 51.

“Warufani mlipewa adhabu mbili katika kosa moja, mtu anapokula njama na kuiba, akitiwa hatiani kwa kosa la kuiba, kosa la kula njama linakufa,” alisema Jaji Bongole na kuongeza:

“Adhabu mliyopewa kwa kosa la kula njama na kukaidi amri ya Polisi haikuwa sahihi, kosa la pili nilipopitia ushahidi limethibitishwa kwamba mliandamana kwa kukaidi amri ya RPC (Kamanda wa Polisi wa Mkoa) iliyowakataza  kufanyahivyo.

“Kosa la pili na tatu nakubaliana na uamuzi wa Mahakama ya Kisutu uliowatia hatiani, kifungu namba 46 cha sheria za Polisi kilichotakiwa kutumika kuwapa adhabu hakikutumika, kifungu hicho kinatamka adhabu kwa makosa hayo ni kwenda jela miezi mitatu au faini ya Sh. 50,000.

“Kutiwa hatiani kwa kosa la kula njama na adhabu yake siyo sahihi, nimeifutilia mbali, kosa la pili na tatu nakubaliana na kutiwa hatiani, adhabu ya mwaka mmoja mliyopewa naibatilisha, mtakwenda jela miezi mitatu kama sheria ya Polisi inavyosema au faini Sh. 50,000.”

Jaji alisema: “Mlifungwa Machi 21, 2013 na Hakimu Mkazi Sundi Fimbo, mpaka sasa ni zaidi ya miezi mitatu, natamka kwamba nawaachia huru wote, mtoke gerezani sababu adhabu yenu mmeitumikia zaidi.”

Wafuasi hao walidaiwa kufanya maandamano Februari 15, mwaka huu wakishinikiza Sheikh Ponda kuachiwa kwa dhamana katika kesi ya uchochezi iliyokuwa ikimkabili katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Victoria Nongwa.

Machi 21, mwaka huu, Mahakama hiyo iliwahukumu kwenda jela mwaka mmoja kwa makosa hayo matatu waliyokuwa wakikabiliwa likiwamo la kukaidi amri ya Polisi iliyokuwa ikiwazuia kufanya maandamano kuelekea kwa DPP ili kushinikiza kiongozi wao apewe dhamana.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Fimbo alisema kuwa katika shtaka la kula njama upande wa mashtaka ulithibitisha bila kuacha shaka kwamba washtakiwa walikutana, wakakubaliana kufanya maandamano hivyo mahakama inawatia hatiani kwa kosa hilo.

Katika shtaka la kukusanyika na kuandamana, alisema mahakama inawatia hatiani.

Kuhusu kosa la kukaidi amri halali ya polisi alisema mahakama inawatia hatiani kwa kuwa  washtakiwa walipeleka maombi ya kufanya maandamano ya amani na Polisi waliyazuia kwa sababu hawakuwa na askari wa kutosha, lakini maandamano hayo yalifanyika baada ya kutoka msikitini.

Katika kosa la kwanza aliwahukumu washitakiwa kwenda jela mwaka mmoja. Katika shtaka la pili pia aliwahukumu mwaka mmoja jela huku kosa la tatu wakihukumiwa tena kifungo cha mwaka mmoja jela.

Hakimu Fimbo alisema adhabu hizo zinatumikiwa kwa pamoja hivyo aliwahukumu washtakiwa kifungo cha mwaka mmoja jela kila mmoja.
 

CHANZO: NIPASHE

Mmoja afa, wawili wakijeruhiwa kwa risasi



MTU mmoja amefariki baada ya kupigwa risasi kifuani na mwingine kujeruhiwa mikono yote miwili baada ya watu wasiojulikana kuwavamia na kutaka kuwapora mali huko Manyoni, Singida.

Tukio hilo limetokea katika Kijiji cha Igwamadete Kata ya Iseke Tarafa ya Nkonko wilayani humo baada ya mtu aliyejulikana kwa jina la Alody Joshua, 29 kupigwa risasi na majambazi hao.
 
Kadhalika Daudi Azaliwa amejeruhiwa mikono yote miwili baada ya kupigwa risasi na majambazi hao wakati wakitoka kwenye mnada wa Mpapa kuelekea nyumbani ndipo majambazi hao walipoanza kuwapiga na kuwanyanganya fedha na kusababisha  kifo cha mtu huyo.

Jeshi la Polisi-Manyoni limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kufafanua kuwa watu watatu wanashilikiwa kwa tuhuma za kuhusika na tukio hilo na kwamba wanatarajiwa kufikishwa mahakamani baada ya upelelzi kukamilika.
 
Chanzo Blog ya Singida.

Gaucho, Vialli waitwa Znz Heroes, Cannavaro, Morris watemwa


 
KIKOSI cha wachezaji 30 cha timu ya taifa ya Zanzibar (Zanzibar Heroes) kimetangazwa na kocha mkuu wa timu hiyo Salum Bahusi bila ya jina la nahodha wa Yanga, Nadir Haroub 'Cannavaro' na Aggrey Morris wa Azam.

Kwa mujibu wa habari kutoka Zanzibar, kikosi hicho ambacho kinatarajiwa kushiriki Kombe la Chalenji kuanzia Novemba 27 mwaka huu jijini Nairobi Kenya, Kocha wa Zanzibar Heroes, Bausi amesema kikosi hicho kitaingia kambini Oktoba 27 mwaka huu na kesho Jumatano wachezaji wote walioitwa watafanyiwa vipimo.

Kikosi kamili kilichoitwa na Bausi ni; MAKIPA ni Mwadini Ali (Azam), Abdallah Rashidi (Ruvu Shooting), Ali Suleiman (KMKM).

MABEKI ni Mohamed Azan (Polisi), Waziri Salum (Azam), Shafi Hassan (Malindi), Mohamed Faki (Zimamoto), Salum Haji (Miembeni), Said Yussuf (Mtende), Mohamed Othman (Jamhuri), Mussa Said (Chwaka Stars), Nassor Masoud ‘Chollo’ kutoka Simba.

VIUNGO ni Abdulhalim Humud 'Gaucho' (Simba), Sabri Ali (JKT Oljoro), Adeyum Saleh (Simba), Isihaka Othman (JKU), Ali Kani (JKT Oljoro), Hamad Mshamata (Chuoni), Suleiman Hamad (Miembeni), Awadh Juma na Masoud Ali wote wa Mtibwa Sugar.

WASHAMBULIAJI ni Seif Karihe (Azam), Suleiman Kasim Selembe (Coastal Union), Khamis Mcha 'Vialli' (Azam), Amour Omary (Miembeni), Amir Hamad (JKT Oljoro), Jaku Joma (Mafunzo), Faki Nahoda (Kimbunga), Hassan Seif (Mtibwa Sugar), Juma Ali Yussuf wa New Generation.

Rais Kikwete alilia Uncle J, kuagwa leo

Rais Jakaya Kikwete
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia Salamu za Rambirambi Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Mheshimiwa Dkt. Fenella Mukangara kufuatia kifo cha Mtangazaji Mkongwe hapa nchini na aliyekuwa Mkurugenzi wa Abood Media inayomiliki Kituo cha Televisheni cha Abood, Bwana Julius Nyaisanga maarufu kwa jina la Uncle J. Nyaisanga.

Bwana Nyaisanga aliyewahi kufanya kazi Radio Tanzania Dar es Salaam (RTD) ambayo hivi sasa ni TBC Taifa, na katika
Kampuni ya IPP Media ambako alikuwa Mkurugenzi wa Radio One, alifariki dunia tarehe 20 Oktoba, 2013 katika Hospitali ya Mazimbu iliyoko katika Manispaa ya Morogoro alikopelekwa kupatiwa matibabu ya ugonjwa wa kisukari.

“Nimeshtushwa, nimesikitishwa na kuhuzunishwa kutokana na kifo cha Mtangazaji Maarufu na Mkongwe hapa nchini katika Tasnia ya Habari hususan upande wa Utangazaji, Bwana Julius Nyaisanga kwani kuondoka kwake kumeacha pengo kubwa katika Tasnia hiyo”, amesema Rais Kikwete katika Salamu zake.

Rais Kikwete amesema alimfahamu Marehemu Julius Nyaisanga enzi za uhai wake kama Mtangazaji aliyekuwa na bidii kubwa ya kazi na mwenye sauti iliyokuwa na mvuto mkubwa kwa wasikilizaji katika sehemu zote alizowahi kufanyia kazi.

“Kwa hakika mchango wa Marehemu Julius Nyaisanga kwa maendeleo ya Taifa letu kupitia Utangazaji, ni mkubwa na wa kupigiwa mfano ambao sote kama Taifa hatuna budi kujivunia”, ameongeza kusema Rais Kikwete katika Salamu zake.

“Kutokana na msiba huu mkubwa, ninakutumia wewe Waziri wa Habari,  Utamaduni na Michezo, Mheshimiwa Dkt. Fenella Mukangara Salamu zangu za Rambirambi kwa kumpoteza mmoja wa Watangazaji Maarufu na Wakongwe hapa nchini. Aidha kupitia kwako naomba unifikishie Salamu zangu za Rambirambi na pole nyingi kwa Familia ya Marehemu Julius Nyaisanga kwa kuondokewa na Mhimili na Kiongozi wa Familia”.

Rais Kikwete amewahakikishia Wanafamilia, ndugu na jamaa wa Marehemu kuwa yuko pamoja nao katika kuomboleza msiba huu mkubwa. Amewaomba wawe na moyo wa uvumilivu na subira wakati huu wanapopita katika kipindi kigumu cha kuomboleza kifo cha mpendwa wao. Namuomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aipokee na kuilaza mahala pema peponi Roho ya Marehemu Julius Nyaisanga.

Vilevile Rais Kikwete ametoa pole kwa Waandishi wa Habari  na Watangazaji kote nchini kwa kumpoteza Mwanataaluma mwenzao ambaye kwa hakika kuondoka kwake kumesababisha pengo kubwa katika Taaluma ya Uandishi wa Habari na Utangazaji hapa nchini.

“Kutokana na juhudi alizokuwa nazo Marehemu, Waandishi wa Habari na Watangazaji kote nchini hawana budi kuiga mfano wake na kuendeleza yote mazuri aliyoyafanya kwa maendeleo ya nchi yetu na Taifa letu kwa ujumla”, amemalizia Salamu zake za Rambirambi Rais Kikwete.

Imetolewa na:

Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu.
Dar es Salaam.
21 Oktoba, 2013

Visome vyuo 10 vilivyofutwa na serikali

Naibu Waziri wa Elimu, Phillip Mulugo

SERIKALI kupitia Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imekunjua makucha yake kwa kutangaza kuvifuta vyuo 10 ambavyo havikusajiliwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) .

Naibu Waziri wa wizara hiyo, Philip Mulugo, alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaama mbele ya Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii na kuongeza kuwa kufutwa kwa vyuo hivyo ni kutokana na kutokufuata utaratibu wa kusajiliwa.

Alivitaja vyuo hivyo ni Media and Research Center, Vision Hotel and Tourism College, East Africa College of Hospitality and Tourism, The Africa Institute of Business Management na Aspiration Training Center, vyote vya Dar es Salaam.

Vingine ni Dar es Salaam School of Hair Design, Media and Values Training Institute na Information Technology Training Center vya Dar es Salaam. Pia alikitaja Chuo cha Morogoro School of Medical Sciences cha Morogoro.

Katika hatua nyingine, Mulugo alikiri kuwa kuna upungufu katika kutoa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kupitia bodi ya mikopo.

Alisema kuna changamoto nyingi zinazoikabili bodi hiyo zikiwamo urejeshwaji wa mikopo kwa wanafunzi waliomaliza chuo, mfumo wa utoaji wa mikopo, ufinyu wa bajeti na makosa yanayotokana na wanafunzi kukosea kujaza fomu za mikopo.

Monday, October 21, 2013

Pambano la Twiga Stars lapangulia ratiba Ligi Kuu

KAMATI ya Ligi ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) imefanya marekebisho ya ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) ili kupisha mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia kati ya Tanzania na Msumbiji.
Mechi hiyo ya kwanza ya raundi ya kwanza kwa mashindano ya wanawake wenye umri chini ya miaka 20 itachezwa Jumamosi (Oktoba 26 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 jioni.
U20 tayari imehamishia kambi yake hosteli ya Msimbazi Center, Dar es Salaam kutoka JKT Ruvu mkoani Pwani tangu wiki iliyopita kujiandaa kwa mechi hiyo. Fainali za Kombe la Dunia kwa U20 wanawake zitafanyika mwakani nchini Canada.
Marekebisho ya ratiba ya VPL yamegusa raundi zote tatu zilizobaki kukamilisha mzunguko wa kwanza. Kutokana na marekebisho hayo mechi za raundi ya 11 zitakuwa ifuatavyo; Oktoba 28 mwaka huu ni Coastal Union vs Mtibwa Sugar, Oljoro JKT vs Ashanti United, Ruvu Shooting vs Kagera Sugar na Simba vs Azam. Oktoba 29 mwaka huu ni Tanzania Prisons vs Mbeya City, Yanga vs Mgambo Shooting na Rhino Rangers vs JKT Ruvu.
Raundi ya 12 ni kama ifuatavyo; Oktoba 31 mwaka huu ni Simba vs Kagera Sugar, Novemba 1 mwaka huu ni JKT Ruvu vs Yanga. Novemba 2 mwaka huu ni Mgambo Shooting vs Coastal Union, Tanzania Prisons vs Oljoro JKT, Azam vs Ruvu Shooting, Mtibwa Sugar vs Rhino Rangers na Mbeya City vs Ashanti United.
Raundi ya 13 ni kama ifuatavyo; Novemba 6 mwaka huu ni JKT Ruvu vs Coastal Union, Ashanti United vs Simba, Kagera Sugar vs Mgambo Shooting, Rhino Rangers vs Tanzania Prisons na Ruvu Shooting vs Mtibwa Sugar. Novemba 7 mwaka huu ni Azam vs Mbeya City.
Mechi za kufunga raundi ya 10 zitachezwa keshokutwa (Oktoba 23 mwaka huu) kama ratiba inayoonesha. Mechi hizo ni kati ya Coastal Union vs Simba, Tanzania Prisons vs Kagera Sugar na Yanga vs Rhino Rangers.

Winta: Kisura wa Jumba la Dhahabu aliyepona kufa kwa Risasi

Msanii Angel John Komba 'Winta' katika pozi
LICHA ya kipaji cha kuzaliwa alichoanza kukionyesha tangu akiwa kinda wakati akisoma Shule ya Msingi Mgulani, msanii Angel John Komba 'Winta' anakiri kuwapenda na kuvutiwa kupita kiasi na Genevieve Nnaji wa Nigeria na Yvonne Cherly 'Monalisa' kulichangia kuingia kwake katika fani ya uigizaji.
Winta, mmoja wa waigizaji wa kike mahiri nchini aliyetamba na kazi mbalimbali kama tamthilia na filamu anasema nyota hao walikuwa wakimkosha kila alipoziona kazi zao na kuapa kuwa ni lazima na yeye aje kuwa staa kama wao.
"Nnaji na Monalisa ndiyo walinipa mzuka wa kujibidiisha katika sanaa ya uigizaji kwani walinikosha na mpaka sasa navutiwa nao," anasema.
Anasema kabla ya kuvutiwa na umahiri wa wanadada hao alikuwa amejikita kwenye sanaa ya kupiga na kucheza ngoma enzi akiwa darasa la sita na kuendelea hata alipojiunga na Sakhafa Sekondari ambapo tayari alishaanza kuigiza.
Hata hivyo anasema kujitosa kwake rasmi katika uigizaji, ilikuwa mwaka 2001 alipokutana na Jumanne Kihangale 'Mr Chuz' anayemtaja kama mmoja wa watu asiyoweza kuwasahau kwa alivyomsaidia kufika mahali alipo sasa na kuwa miongoni mwa waasisi wa kundi maarufu ya uigizaji la Fukuto Arts Professional.
"Kiukweli nilitumbukia rasmi kwenye uigizaji mwaka 2001 nikiwa miongoni mwa waasisi wa kundi la Fukuto na kazi ya kwanza kuicheza ilikuwa ni igizo lililokimbiza nchini la Jumba la Dhahabu na mingine iliyokuja baadaye kabla ya kuhamia kwenye filamu kwa kucheza kazi mbalimbali zilizonipaisha ndani na nje ya nchi," anasema.
Mrembo huyo anayeishabiki Simba na mabingwa watetezi wa England klabu ya  Manchester United, anasema tangu ameingia kwenye fani hiyo anashukuru amepata mafanikio mengi ya kujivunia baadhi hapendi yaanikwe gazetini.
Winta anadai mbali na manufaa ya kiuchumi, sanaa imemfanya afahamiane na watu wengi na kupata rafiki na kutembea sehemu mbalimbali.
"Nashukuru sanaa imenisaidia kwa mambo mengi ya kujivunia, japo sijaridhika kwa vile ndoto zangu ni kuja kumiliki kampuni binafsi itakayozalisha na kusambaza kazi zangu na za wasanii wenzangu," anasema.

MKASA
Kisura huyo anayependa kula ugali kwa mlenda na dagaa mchele wa kukaangwa, anasema sanaa ya Tanzania imezidi kupiga hatua kubwa kulinganisha na siku za nyuma japo anadai wizi na unyonyaji unawafanya wasanii washindwe kunufaika.
Anasema, lazima serikali na mamlaka zinazosimamia fani hiyo kutoa makucha yake ili kuwabana wanyonyaji na wezi wa kazi za wasanii ili kuinua maisha ya wasanii tofauti na sasa wengi wao wakiishi maskini tofauti na jasho lao.
Msanii Winta katika pozi
Pia anataka watengeneze miundo mbinu itakayowasaidia chipukizi kuendeleza vipaji vyao ili kusaidia kuondoa tatizo la ajira sambamba na serikali kuvuna pato kupitia fani hiyo.
Juu ya tukio la furaha, Winta anasema ni siku alipojaliwa kujifungua mtoto wa kiume aliyenaye, huku akidai hawezi kuusahau mkasa uliowahi kumkuta hivi karibuni alipokuwa na rafikize 'wakila bata' na kubadilishana mawazo baa.
Anasema akiwa na wenzake hawana hili wala lile, ghafla Pub waliyokuwepo (jina limehifadhiwa) ilivamiwa na majambazi ambao waliwamrisha wateja wote kulala na yeye kwa ubishi alikurupuka ili kukimbia na kufyatuliwa risasi iliyomkosakosa sentimita chache na kwa kiwewe alijikuta akitumbukia kwenye mtaro wa maji machafu yaliyochanganyika na kinyesi.
Winta anasema kila anapolikumbuka tukio hilo la kusalimika kufa kwa risasi na jinsi alivyokoga uchafu huo hukosa raha.
"Siwezi kulisahau tukio hilo kwa jinsi nilivyonusurika kifo cha risasi na kutumbukia kwenye mtaro wa kinyesi, yaani ilikuwa balaa. Ila nashukuru  Mungu aliinusuru roho yangu," anasema.
Winta ambaye hajaolewa japo ana mtoto mmoja, anasema hakuna msanii wa kiume anayemkuna nchini kama mkongwe Amri Athuman maarufu kama Mzee Majuto.
"Huyu mzee noma, hana mpinzani na anajua kitu anachokifanya katika fani," anasema mwanadada huyo anayejikubali mwenyewe kwa uwezo alionao.

ALIPOTOKAAngel John Komba 'Winta' alizaliwa mwaka 1982 katika hospitali ya Temeke, Dar es Salaam kabla ya kuanza Shule ya Msingi Mgulani kabla ya kujiunga na Sakhafa Sekondari ambapo tayari alishaanza kujishughulisha na sanaa akicheza, kupiga ngoma na kuigiza.
Winta anayependa kunywa Fanta Passion na Castle Light, baada ya kumaliza shule alitumbukia rasmi kwenye sanaa hiyo akianzia kundi la Fukuto Arts Professional na kutamba nalo na tamthilia kadhaa kabla ya kuangukia kwenye filamu.
Baadhi ya filamu alizoigiza mwanadada huyo anayependa kutumia muda wa ziada kuangalia 'muvi' kuchati na kusoma vitabu na magazeti ni pamoja na 'Shock' aliyoigiza na marehemu Steven Kanumba, 'I Hate My Birthday', 'Pigo la Yatima', 'Kovu la Laana' na nyingine.
Winta akiwa na marehemu Kanumba walipokuwa wakiigiza filamu ya The Shock
Winta anayewataka wasanii wenzake kutegemea vipaji walivyonavyo na kuvitumikia kwa ufanisi badala ya kujihusisha na skendo au vitendo vya ushirikiana.
"Hakuna siri kwa sasa wasanii wanaendekeza sana mambo ya kishirikiana kwa kushinda kupishana kwa waganga ili kuroga na kutembelea nyota za wenzao, ila ukweli mtu anayejiamini na kutegemea kipaji hawezi kufanya upuuzi huo ambao hausaidii zaidi ya kujidhalilisha," anasema.
Mwanadada huyo anayemshukuru mno Mr Chuz na watu wengine waliomsaidia kwa namna moja au nyingine kufika alipo, anaiomba jamii iwachukulie wasanii kama watu wengine na pale wanapokosea wasiwahukumu wote au kuwaona watu wa ajabu kwa sababu hakuna binadamu aliyekamilika.
"Pia watuunge mkono kwa kununua kazi zetu sambamba na kutusaidia kupambana na maharamia kwa kuacha kununua kazi feki badala yake wazinunue kazi halisi ili tuweze kuendelea kuwapa burudani," anasema.

Simba, Yanga waingiza Mil. 500

Wachezaji wa Simba na Yanga walipokuwa wakiumana jana
Na Boniface Wambura
PAMBANO la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara jana baina ya watani wa jadi Simba na Yanga lililochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na kumalizika kwa sare ya mabao 3-3 limeingiza jumla ya Sh. Milioni 500.7.
Mashabiki 57,422 ndiyo waliokata tiketi kushuhudia pambano hilo namba 63 kwa viingilio vya sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 15,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.
Ni tiketi 131 tu ndizo hazikuuzwa ambazo ni 90 za VIP A, 40 za VIP B na moja ya VIP C. Tiketi zilizochapwa kwa ajili ya mechi hiyo ni 57,558 ambayo ndiyo idadi ya viti vilivyopo kwenye uwanja huo. Kila klabu imepata mgawo wa sh. 123,025,564.32 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 76,382,084.75.
Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 62,555,371.69, tiketi sh. 7,309,104, gharama za mechi sh. 37,533,223.01, Kamati ya Ligi sh. 37,533,223.01, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 18,766,611.51 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 14,596,253.39.

Abdallah Juma: Aliyerudisha heshima ya hat-trick kwa wazawa Bara

Abdallah Juma alipokuwa Simba
 HALI aliyokumbana nayo akiwa na timu ya Simba msimu uliopita, ilimfanya mshambuliaji Abdallah Juma, kukaribia kutundika daluga na kuachana na soka.
Anasema alishaamua kuachana na soka na kwenda kufanya kazi za ufundi magari kutokana na alivyokatishwa tamaa na Simba iliyomsajili kutokea Ruvu Shooting.
Hata hivyo, baada ya ushauri wa watu wake wa karibu na mzuka wa soka alionao tangu utotoni, ulimbadili mawazo yake na kuamua kujiunga na Mtibwa Sugar.
Kitendo cha kujiunga Mtibwa kimeweza kumrejeshea furaha na hasa baada ya wiki iliyopita kufunga mabao matatu (hat-trick) na kuweka rekodi ya kuwa mchezaji wa kwanza mzawa kufanya hivyo tangu Juma Semsue aliyekuwa Polisi Dodoma kupiga hat-trick.
Semsue aliweka rekodi hiyo ya kufunga hat-trick msimu wa 2010-2011 wakati Polisi ilipoishindilia Villa Squad mabao 5-3, baada ya hapo ligi hiyo ilishuhudiwa ikiisha kwa misimu miwili mfululizo bila hat-trick nyingine.
Mwezi uliopita Mrundi Amisi Tambwe wa Simba ndiye aliyekuja kuvunja mwiko huo kwa kufunga mabao manne wakati timu yake ikiizabua Mgambo JKT 6-0 na ndiyo Juma akaifikia rekodi yake wakati Mtibwa ikiifunga Oljoro JKT 5-2.
"Nimejisikia furaha, sikutegemea na hii ni hat-trick yangu ya kwanza, pia imekuja nikitoka katika kipindi cha kukata tamaa cha kucheza soka," anasema.
Juma ambaye hufananishwa na wengi na Abdallah Juma mwenye asili ya Unguja aliyewahi kutamba Mtibwa akiweka rekodi ya kufunga mabao 25 katika msimu mmoja, yote ndani ya Uwanja wa Manungu, anasema tukio hilo litabaki kuwa historia kwake.
Anasema kinachomfanya achekelee ni namna alivyoweka rekodi katika Ligi Kuu Bara akiwa mzawa wa kwanza 'kutupia' hat-trick baada ya misimu miwili, pia namna alivyoibuka akiwa keshakata tamaa ya soka kwa mambo aliyofanyiwa Simba.
"Kitendo cha kuchezeshwa mechi mbili tena kwa muda usiozidi robo saa kwa msimu mzima Simba, kutokana na kutoaminiwa na kocha, kinanitia simanzi na siwezi kusahau maishani," anasema.
Mkali huyo aliyeanza kujipatia umaarufu wa kufumania nyavu akizichezea FC Kambarage, Polisi-Shinyanga na Mwanza Utd kabla ya kutua katika Ligi Kuu kupitia AFC Arusha, Kagera Sugar na Ruvu Shooting, anawashukuru makocha wa Mtibwa Sugar kwa kumrejeshea furaha yake.
"Wananiamini na wamenisaidia kurejea katika kiwango changu, nimecheza mechi tatu tu, lakini tayari nimeweka rekodi naamini nitaendelea kufanya vema zaidi," anasema.
Anaeleza kuwa, wakati mwingine makocha huchangia 'kuua' vipaji vya wachezaji kwa kuwakatisha tamaa kwa kutokana na kutowaamini na kushindwa kuwasaidia pale wanapotokea kukosea kutekeleza maagizo yao uwanjani.
"Namshukuru Mungu. Huu ni mwanzo kwani naamini nitaendelea kufumania nyavu ili kufikia lengo la kuitwa Taifa Stars na pia kucheza soka la kulipwa nje ya nchi," anasema.

Bendera
Mkali huyo anayependa kula ugali kwa dagaa na mboga za majani huku akishushia na maji na soda, anasema mafanikio yake kisoka licha ya kuchangiwa na makocha tofauti, lakini hawezi kumsahau Madaraka Bendera aliyemnoa akiwa AFC.
Anasema Bendera alimtengeneza akawa Juma 'Magoli' ndiyo maana alimezewa mate na kuhama timu moja hadi nyingine mpaka Msimbazi ambapo hata hivyo, waliishia 'kumchomesha mahindi'.
Shabiki huyo wa Arsenal  anayemzimia mshambuliaji wa zamani wa klabu hiyo ya England, Robin van Persie aliyepo Manchester Utd kwa sasa, anasema soka limemsaidia kwa mambo mengi japo hapendi yaanikwe gazetini.
"Nitakosa fadhila kama sitamshukuru Mungu jinsi soka lilivyonisaidia," anasema.
Juma analitaja pambano la Ligi Kuu Bara kati ya AFC Arusha dhidi ya Yanga misimu minne iliyopita kuwa ndilo gumu na asilolisahau.
"Mbali na kuwa la kwanza dhidi ya timu kubwa kama Yanga, lakini kitendo cha kuingia uwanjani dakika nane kabla ya mechi kwisha na kuisawazishia AFC bao, itabaki kumbukumbu ya milele kwangu" anasema.
Anasema katika pambano hilo Yanga ilitangulia kufunga mapema na kudumu hadi dakika ya 82 alipoingizwa na kocha Bendera na kufanikiwa kufunga bao la kusawazisha na kufanya matokeo kuwa 1-1.
Abdallah Juma
Msukuma
Abdallah Salum Juma, alizaliwa 1989 mkoani Shinyanga akiwa ni mtoto wa mwisho kwa tumbo la mama yake akitanguliwa na kaka yake kwenye familia ya watoto nane wa mzee Salum Juma.
Anasema soka lake lilianzia mkoani Shinyanga wakati akisoma Shule ya Msingi Mangejese. Anafafanua kuwa alikuwa akimudu nafasi nyingi uwanjani kuanzia ya ulinzi, kiungo, hadi ushambuliaji na timu yake ya 'chandimu' ikiwa ni Mwenge Stars kabla ya kusajiliwa Segese Stars ya Kahama kwa michuano ya Ligi.
Juma anasema alivutiwa kipindi hicho na Mashaka Ayoub aliyewahi kutamba timu mbalimbali za Ligi Kuu Bara na alipotoka Segese alisajiliwa Kambarage kisha AFC Arusha iliyovutiwa naye.
Aliichezea AFC kwa misimu kadhaa kabla ya kusajiliwa Kagera Sugar kisha kurudi tena AFC na kuteuliwa timu ya Mount Meru Warriors kwa michuano ya Kombe la Taifa na kuivutia Ruvu Shooting iliyomsajili kabla ya kutua Simba.
Abdallah Juma (kulia) akiwajibika uwanjani
Anasema soka la Tanzania linazidi kupiga hatua kubwa kwa vijana kuonyesha uhai wa kurejesha heshima ya Tanzania kimataifa, japo aliiomba serikali na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuongeza nguvu katika soka la vijana ili kuwaandaa mashujaa wa kesho.
Anasema hakuna kitu anachokitamani maishani mwake kama kulitumikia taifa lake kupitia timu ya taifa ambayo hajawahi kuinusa hata kidogo, huku akiota pia kucheza soka la kulipwa Ulaya na kuwataka wachezaji wenzake kujibidiisha kwenye mazoezi na kuzingatia nidhamu na miiko ya uchezaji wa soka.
Juma anayekiri kama siyo soka huenda angekuwa fundi magari mzuri kutokana na fani hiyo kuipenda na kuisomea kwa muda, anasema ligi kuu ya msimu huu ni ngumu na inayotoa changamoto kubwa kwa klabu pamoja na wachezaji wa timu shiriki.
"Ligi ya msimu huu kiboko, haitabiriki kutokana na ugumu wake, kitu ambacho ni kizuri kwa wachezaji na hata klabu kujipanga zaidi ili kupata matokeo mazuri," anasema.
Mchezaji huyo anasema anadhani timu bora itafahamika mwishoni mwa msimu pale itakapotwaa ubingwa na kupata uwakilishi wa mechi za kimataifa kwa sababu kwa sasa ni vigumu kutabiri kwa vile timu zote 14 zina nafasi sawa ya kutwaa taji hilo kwa kadri watakavyojipanga vema.

KR Mullar: Mkali wa Mapanga Shaa anayefananishwa na Gervinho



KR Mulla akikamua jukwaani
MASHABIKI wa muziki wanamuita 'Jibaba' CD 700' kutokana na kuwa na 'mapafu' ya kuhimili jukwaa akiimba na kucheza kwa muda mrefu, huku wale wa soka wamembatiza jina la Gervinho kutokana uwezo wake kisoka na kule kushabihiana kwake na nyota wa Ivory Coast aliyewahi kutamba Arsenal, Gervais Lombe Yao Kouassi maarufu kama 'Gervinho'.
Hata hivyo majina yake halisi ni Rashid Ziada 'KR Mullah', mmoja wa wasanii wakongwe wa muziki wa kizazi kipya aliyeasisi makundi kadhaa ambaye kwa sasa ametuliza 'mtima' wake katika kundi la Wanaume Halisi akiungana tena na 'swahiba' wake, Juma Kassim 'Sir Juma Nature'.
KR Mullah, ambaye kitaaluma ni fundi magari fani aliyoisomea Chuo cha VETA na kuifanya kwa muda kabla ya kutumbukia kwenye muzuki, ni kati ya vijana wachache waliojaliwa vipaji lukuki akimudu kuimba, kutunga, kucheza na kupanga muziki, huku pia akiwa mahiri katika soka akimudu nafasi mbalimbali uwanjani kuanzia nafasi ya beki, kiungo, winga hadi ile ya ushambuliaji.
Akiwa amewahi kuzichezea timu mbalimbali za mitaani katika maeneo yao ya Temeke akishiriki pia Ligi Daraja la Tatu na Nne, KR Mullah kwa sasa ni mmoja wa wachezaji anayeunda kikosi cha timu ya Golden Bush Veterani akiungana na wakali wa zamani za klabu za Simba, Yanga na Mtibwa Sugar.
Kupenda kwake soka na muziki kulimsababisha akaamua kuachana na kuchezea spana na 'oil' ili kutumikia fani hizo na kukiri kwamba kwa kiasi fulani zimemsaidia kiuchumi na kimaisha, japo hajaridhika na mahali alipo.
"Soka nalicheza kwa vile nalipenda na limenisaidia kufahamiana na watu wengi pamoja na kunisaidia kuwa pumzi kubwa jukwaani, lakini muziki ndiyo zaidi kwa kunisaidia kiuchumi, naishi na familia yangu kwa sababu ya muziki, japo sijaridhika," anasema.
Anasema japo anafarijika kuona muziki wa kizazi kipya ukikubalika mbele ya jamii tofauti na siku za nyuma, furaha yake itafikia kilele siku atakapoitwa kwenda kutumbuiza 'duniani' kama mastaa wengine wanaoletwa nchini.
"Siku nitakapoalikwa na kwenda kufanya kazi katika nchi zilizoendelea kimuziki sambamba na wakali wanaong'ara duniani, ndipo nitakapoona kweli sasa nipo juu na ndoto zangu za kuutangaza muziki wetu kimataifa imefanikiwa," anasema.
KR Mullah, aliyepewa jina hilo la Mullah akifananishwa na kiongozi aliyewahi kuvuma wa kundi la Taleban, Mullah Omar Mohammed kutokana na uwezo wa kutawala jukwaa na kuwaongoza wenzake kuwaburudisha mashabiki wao.
KR Mulla akionyesha umahiri waka katika soka
CHUJI
KR Mullah anayependa kula ugali kwa samaki na mboga za majani na kunywa maji na siku moja moja 'maji ya mende' anasema hakuna tukio la furaha kwake kama kukubalika kwa ubunifu wake wa staili ya kucheza ya 'Mapanga Shaa' inayotumiwa na kundi la TMK Wanaume Family.
"Hili ndilo tukio la furaha kuona ubunifu wangu ukitumika kama nembo ya kundi letu popote tulio na ninalizwa na matukio ya wasanii wenzetu kutangulia mbele ya haki wangali wadogo, inauma na kunitoa machozi," anasema.
Mkali huyo ambaye anajiandaa kupakua albamu yake ya pili binafsi itakayokuwa na zaidi ya nyimbo 10 ni shabiki mkubwa wa Yanga akimzimia kiungo mshambuliaji, Athuman Idd 'Chuji' na kimataifa anaishabikia Manchester United, japo anadai alijikuta akiipenda Arsenal kutokana na Gervinho, pia akidai anapenda soka la Cristiano Ronaldo.
"Kwa kweli Chuji ananikosha kwa soka lake, ni moja ya wachezaji wenye vipaji vikubwa vya soka ambao Tanzania tunapaswa kuwaringia, pia nakunwa na Ronaldo jamaa anakila kitu. Anastahili kuwa mchezaji bora wa dunia,"anasema.
Msanii huyo aliyetumbukia kwenye fani ya muziki miaka ya 1990  akianzia kwenye kundi la GMW- Mazimwi anasema lau kama siyo muziki huenda angebobea kwenye soka  kutokana na kuupenda mno mchezo huo akianza kucheza tangu akisoma Shule ya Msingi.
Anasema baada ya kutamba shuleni alizichezea timu kadhaa wakati huyo akifahamika kwa jia la utani kama 'Zico' baadhi ya timu hizo ni Sumu ya Mamba, Inter Milan, Gaza Fc katika michuano ya ligi na ile ya mchangani kabla ya sasa kutulia Golden Bush Veterani.

MUZIKI
KR Mullah aliyezaliwa zaidi ya miaka 30 iliyopita, alianza kupenda muziki tangu akiwa kinda kwa kupenda kusikiliza nyimbo za wasanii nyota wa zamani kama akina MC Hammer, Kriss Kross kabla ya kujumuika na vijana wenzake kuunda kundi la GMW Mazimwi wakati huo akisoma chuo cha ufundi VETA.
Baadaye aliungana na Juma Nature na kuunda kundi la Wachuja Nafaka kabla ya mwaka 2003 kushirikiana pamoja kuasisi kundi la TMK Wanaume Family ambalo hata hivyo lilikuja kugawanyika na kuzaliwa makundi matatu tofauti, likianza la Wanaume Halisi, kisha Temeke Unity.
Katika mgawanyiko huo huo KR Mullah aliamua kusalia TMK Wanaume Family akiwa na akina Chegge, Mhe Temba, Stico na wengine kabla ya mwishoni mwa mwaka jana kuamua kumfuata Sir Juma Nature katika kundi la Wanaume Halisi na kutoa kazi moja iitwayo 'Umemponza Mdomo'.
Mkali huyo ameshiriki albamu kadhaa za karibu makundi yote aliyowahi kufanya kazi, lakini pia alishatoa albamu yake binafsi iliyofahamika kama 'Kamua kwa Uwezo' na sasa anajiandaa kupakua albamu yake ya pili ambayo imeshatambulishwa na nyimbo kama 'Choo cha Kike' na 'Kelele'.
Nyimbo mbili ambazo anatarajiwa kuzitoa hivi karibuni ni 'Wivu' na 'Masela na Machizi' ambazo zote zitakuwa kwenye albamu hiyo.
KR Mulla akiwa na Rais Jakaya Kikwete
KR Mullah, anasema wimbo huo wa Wivu ndiyo utakaokuwa wa kwanza kutoka amaurekodia katika studio ya kundi lao ya Halisi Records kabla ya baadaye kufuatiwa na Masela na Machizi.
Mkali huyo anayelia na wizi wanaofanyiwa wasanii na kuiomba serikali iwasaidie, anasema hakuna akichukiacho kama 'bifu' za kijinga zifanywazo na wasanii wenzake alizodai zinachangia kurudisha nyuma maendeleo ya muziki.
Anasema siyo vibaya ukawapo ushindani na changamoto za kukuza muziki na siyo bifu za kuwekeana uhasama na hata kufikia wasanii kupigana au kuwa maadui, kwani haisaidii ingawa alikiri jambo hilo lipo hata kwa nyota wa dunia.
Mkongwe huyo anaiasa jamii kupambana kwa vitendo na ugonjwa wa Ukimwi kwa madai mabango na juhudi za serikali na wahamasishaji yameshatosha, huku akiwataka wasanii wenzake kupunguza kutumia dawa za kulevya.
Anasema wasanii hawazuiwi kutumia vilevi kama pombe kiasi kujiburudisha, lakini siyo kuvuka mipaka na kubwia unga au kuvuta bangi kama wehu kwani huwafanya wakose umakini wa kazi yao na kujiingiza katika vitendo viovu.

Ushindi mfululizo waipa jeuri Mtibwa Sugar

Kocha wa Mtibwa Sugar, Mecky Mexime
USHINDI wa mechi tatu mfululizo ulioiwezesha kuingia kwenye Tano Bora, umeifanya klabu ya Mtibwa Sugar ya Morogoro kujipa matumaini ya ubingwa.
Mabingwa hao wa zamani wa Tanzania ambao wamekuwa wakitoa dozi nene kwa wapinzani wao kwa mechi zake za karibu, wamesema ligi ya msimu huu haina mwenyewe hivyo hata wao wanaamini wanaweza kutwaa taji mwishowe.
Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mecky Mexime, alisema ligi ya msimu huu ni ngumu na isiyotabirika na hivyo hawawezi kujiondoa kwenye ubingwa wakati wanazidi kufanya vyema katika mechi zao.
Mexime alisema anachoamini ni vijana wake wazidi kutekeleza maagizo yake na kupata ushindi katika mechi zao ili kurejea mafanikio iliyowahi kupata klabu hiyo kwa kutwaa ubingwa wa Tanzania mara mbili mfululizo.
"Tunashukuru tumepata matokeo mazuri katika mechi zetu za karibuni na hii ni baada ya kurekebisha makosa na sasa tuna matumaini zaidi ya kuwa miongoni mwa timu zinaweza kutwaa ubingwa," alisema.
Kocha huyo aliyewahi kuwa nahodha wa Mtibwa na Taifa Stars, alisema pamoja na ushindi mara tatu mfululizo kwa timu yake hauwafanyi wabweteke badala yake wanajipanga zaidi ili kupata matokeo mazuri zaidi kwa mechi zao zilizosalia.
Kikosi cha timu hiyo yenye maskani yake katika mashamba ya Manungu, Turiani Morogoro, kinatarajiwa kushuka dimbani Jumamosi kwa kuumana na Coastal Union ya Tanga mechi itakayochezwa uwanja wa Mkwakwani na Mexime alisema wanajipanga ili wafanye vizuri katika mechi hiyo.
Kwa sasa Mtibwa inakamata nafasi ya tano ikiwa na pointi 16 sawa na za Yanga ila inazidiwa uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa na mabingwa watetezi hao waliopo nyuma ya mtani wao Simba yenye piointi 19.
Kileleni mwa msimamo mwa ligi hiyo kuna Azam na Mbeya City ambazo zote zina pointi 20 kila moja zikitofautiana uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa.

Gaucho akiri 'gemu' kumkataa lakini akwepa mzigo wa lawama

Abdulhalim Humud 'Gaucho'
KIUNGO Mshambuliaji wa Simba, Abdulhalim Humud 'Gaucho' amekiri kwamba hakuwa katika kiwango kizuri katika pambano lao la juzi dhidi ya wapinzani wao wa jadi Yanga, akidai 'gemu' lilimkataa, lakini amesema hadhani kama anapaswa kubebeshwa mzigo wa lawama kwa namna timu ilipocheza katika kipindi cha kwanza.
Kocha Mkuu wa Simba, Abdallah KIbadeni 'King' alikaririwa akimtupia lawama kiungo huyo kwa matoikeo ya 3-0 iliyopatya timu yake katika kipindi cha kwanza kabla ya kumtoa na nafasi yake kuchukuliwa na Said Ndemla na Simba kurejesha mabao yote matatu na kulazimisha sare ya mabao 3-3.
Akizungumza na MICHARAZO asubuhi hii Gaucho, alisema anamheshimu kocha wake na anaheshima kauli yake kutokana na Simba kucheza ovyo kipindi cha kwanza, lakini alisema kwake anaamini 'gemu' lilimkataa japo linaloweza kumtopkea mchezaji yeyote duniani.
Gaucho alisema anaamini kocha alimpanga kwa uwezo alionao na alioonyesha katika mechi kadhaa za nyuma, ila bahati mbaya gemu lilimkataa na hivyo kutocheza vyema, japo alisema hapaswi kulaumiwa pekee yake kwani karibu timu nzima ilishindwa kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
"Sijamsikia kocha akiyasema unayoniambia ila kama amenitupia lawama, sidhani kama ni sawa kwa sababu timu nzima katika kipindi cha kwanza hatukucheza vyema na kutimiza wajibu wetu, ila namheshimu kauli yake, japo lazima nikiri kwamba nilijiandaa sana kwa mchezo huo ila 'gemu' lilinikataa," alisema Gaucho.
Mchezaji huyo alirejea Simba akitokea Azam msimu uliopita, alisema kama mchezaji anajisikia vibaya kunyooshewa vidole kwa sababu inaweza kutafisriwa vibaya na mashabiki ilihali amekuwa akijitolea kwa uwezo wake kuhakikisha Simba inafanya vyema.
Kibadeni alionyesha kukerwa na baadhi ya wachezaji akiwamo Gaucho kwa jinsi walivyocheza katika kipindi cha kwanza na Simba kulala mabao 3-0 kabla ya kufanya mabadiliko na kusaidia kurejea mabao yote matatu kupitia kwa Betram Mombeki, Joseph Owino na Kaze Gilbert na kuifanya timu hiyo ipumue katika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 19.
Timu hiyo inatarajiwa kushuka dimbani keshokutwa kuvaana na Coastal Union ya Tanga katika mfululizo wa ligi hiyo iliyopo raundi ya 10 kwa sasa. Mechi hiyo itachezwa kwenye uwanja wa Mkwakwani Tanga.

Sunday, October 20, 2013

Juve yafa 4-2 kwa Fiorentina, Tevez atupia moja

Fiorentina striker Giuseppe Rossi
'Muuaji' Giuseppe Rossi akishangilia moja ya mabao yake matatu yaliyoiangamiza Juventus

KIBIBI cha Turin, Juventus leo imekiona cha mtema kuni baada ya kusasambuliwa mabao 4-2 ugenini na Fiorentina, licha ya kutangulia kujipatia mabao katika pambano la Ligi Kuu ya Italia Seria A.
Bao la penati la Muargentina, Carlos Tevez katika dakika ya kabla ya Paul Pogba kuongeza jingine dakika tatu baadaye yaliipa uongozi Juventus hadi wakati wa mapumziko.
Hata hivyo wenyeji waliingia kipindi cha pili na moto mkali na kurudisha bao moja ya jingine na kuongeza mengine mawili ya ushindi na kuibuka na ushindi huo mnono.
Giuseppe Rossi alipiga hat trick katika pambano hilo akianza kwa bao la penati dakika  66 kabla ya kuongeza jingine dakika 10 baadaye na kumalizia kazi dakika ya 81, ambapo kabla ya hapo Joaquim aliifunga bao la tatu dakika ya 78 na kupeleka msiba kwa Kibibi kizee.
Katika mechi nyingine genoa ikiwa nyumbani imeikwanyua Chievo mabao 2-1, Hellas Verona ilitakata kwao kwa kuilaza Parma mabao 3-2, Sampdoria iliizamisha Livorno mabao 2-1 na Sassuolo ikaizamisha Bolgna kwa magoli 2-1. Pambano jingine linalotarajiwa kucheza baadaye ni kati ya Torino na Inter Milan.



























Tottenham yainyoa Aston Villa kwao EPL

Andros Townsend (right) sends in the cross from which he scored for Tottenham at Aston Villa
Andros Townsend akiifungia Spurs bao la kwanza katika mechi ya leo

MABAO mawili ya kila kipindi yaliiwezesha Tottenham Hotspurs kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 Aston Villa ikiwa nyumbani kwao katika Ligi Kuu ya England.
Andros Townsend aliianza kuifungia Spurs bao dakika ya 31 na kudumu hadi kipindi cha kwanza kilipoisha na Saldado aliiongezea vijana wa Andre Villas Boaz bao dakika ya 69 na kuifanya timu hiyo ichupe kutoka nafasi ya saba hadi nafasi ya tano ikifikisha pointi 16.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena kesho kwa pambano moja baina ya Crystal Palace itakayoialika Fulham.


Simba yafanya maajabu Taifa, Ngassa aokoa nyumba zake


Mrisho Ngassa akishangilia bao lake leo uwanja wa Taifa

MRISHO Ngassa ameziokoa nyumba zake zisichomwe moto, lakini Yanga wameshindwa kulinda ushindi wao wa mabao matatu kama walivyoahidi baada ya Simba kuchomoa mabao na kulazimisha sare ya mabao 3-3.
Wapinzani hao wa jadi waligawana utawala wa vipindi, Yanga ikitawala kipindi cha kwanza na kujipatia mabao yake matatu kupitia kwa Mrisho Ngassa na Hamis Kiiza 'Diego' kabla ya Simba kung'ara kipindi cha pili.
Mabao ya Betram Mombeki na mabeki wa kimataifa Joseph Owino na Gilbert Kazze yalizima ndoto za Yanga kuwanyuka watani zao kwa mara ya pili mfululizo.
Pambano hilo lililosisimua wengi lililochezwa kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam limeisaidia tu Yanga kupanda nafasi moja toka ya tano hadi ya nne ikiishusha Mtibwa Sugar, huku Simba ikishindwa kurejea kileleni.
Sare hiyo imeifanya Simba ifikishe pointi 19, moja dhidi ya vinara Azam na Mbeya City ambazo jana zilitakata kwa ushindi wa bao 1-0 kila mmoja dhidi ya timu za maafande wa JKT Ruvu na Oljoro JKT.
Kwa ujumla Yanga itawabidi wajilaumu kwa matokeo hayo kwani ilikuwa na kila dalili za kuweza kulipa kisasi cha mabao 5-0 iliyopewa na Simba Mei mwaka jana na hata kurudisha bao 6-0 iliyofungwa miaka 36 iliyopita.
Kipindi cha kwanza iliwashika Simba na kucheza watakavyo hasa baada ya kiungo cha Simba 'kufa', lakini walionyesha kuridhika huku Simba kutumia muda wa mapumziko kurekebishana makosa na kujirekebisha.
Kuingia dimbani kwa Said Ndemla na William Lucian 'Gallas' walifanya Simba ipate uhai na kutawala kipindi cha pili na kuwafunika Yanga ambao walionekana kuridhika na kudhani wameshashinda mchezo huo.
Baadhi ya mashabiki wa soka wameonyesha kushangazwa na matokeo ya leo Yanga wakilaumiana na wachezaji wao, huku Simba wakishangilia, japo makocha wote wametoa lawama kwa wachezaji kwa jinsi walivyocheza.
King Kibadeni ameweka wazi kwamba katika kikosi chao kuna tatizo kubwa japo hakupenda kuweka bayana, huku Ernie Brandts akidiriki 'kuwatusi' wachezaji wake kwa kuruhusu mabao matatu kurudi.

Lakini kubwa ni kitendo cha Ngassa kufunga bao na kutimiza ahadi yake aliyotoa kwamba kama asingefunga au kutoa pasi ya bao basi angechoma moto nyumba zake tano.

Al Ahly yaifuata Orlando Pirates fainali za mabingwa Afrika

Al Ahly-caf-cl-final-2013
Al Ahly
NATIONAL Al Ahly ya Misri imefanikiwa kupenya katika Fainali za Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kuing'oa Cotton Sports ya Cameroon kwa mikwaju ya penati 7-6 katika pambano la nusu fainali ya pili iliyosiha muda mfupi uliopita.
Al Ahly ikiwa nyumbani imelazimishwa sare ya bao 1-1 na kufanya matokeo kuwa 2-2 na kulazimisha kupigiana penati ambapo wenyeji walipata 7 dhidi ya 6 za Wacameroon ambao Mohammewd Abo Trika alikosa mkwaju wake wakati akifungua hatua hiyo ya kupigianja penati.
Wenyeji walianza kupata bao dakika ya tatu tu kupitia kwa Abdallah El Said kabla ya wageni kusawaxzisha kipindi cha pili.

Monaco washindwa kurejea kileleni Ligue 1 yabanwa na Sochaux



LICHA ya kutangulia kupata mabao mawili ya haraka na kuongoza kwa muda mrefu, Monaco imeshindwa kurejea kileleni mwa msimamo wa Ligi ya Ufaransa baada ya kulazimishwa sare ya mabao 2-2 na Sochaux muda mfupi uliopita.
Monaco walienguliwa kileleni na PSG, ilianza makeke kwa kutangulia kufunga mabao mawili ya haraka kupitia kwa Ferreira Carrasco aliyefunga katika dakika ya 5 na 10 na kudumu hadi mapumziko.
Hata hivyo wenyeji walicharuka na kurejesha mabao hayo katika kipindi cha pili kupitia Cedric Bakambu dakika ya 57 na Joseph Lopy dakika ya 69 na kufanya matokeo yaishe kwa sare ya 2-2 na kuifanya Monaco kusalia nafasi ya pili ikiwa na pointi 22, mbili nyuma ya PSG.
Michezo mingine inaendelea muda huu katika viwanja kadhaa katika ligi hiyo ya Ufaransa

Lazio yanyukwa 2-1 na Atalanta, Milan yajitutumua Seria A

 
WAKATI Lazio muda mfupi uliopita imekubali kipigo cha mabao 2-1 toka kwa Atalanta, AC Milan jana iliendelea kujikongoja baada ya kupata ushindi kiduchu wa bao 1-0 ikiwa nyumbani San Siro dhidi ya Udinese.
Bao pekee la Milan lilifungwa na Valter Birsa akimalizia kazi nzuri ya Mbrazil Robinho na kuifanya ifikishe poingti 11 na kuiengua Udinese katika nafasi ya nane na kuishika wenyewe na Udinese ikiporomoka hadi ya tisa.
Mchezo mwingine uliochezwa pia jana, Cagliari iliizima Catania kwa mabao 2-1 kwa mabao ya Ibarbo na Pinilla huku la kufutia machozi la Catania lilifungwa na Bergessio.
Hivi punde tu pambano kati ya Atalanta dhidi ya Lazio limemalizika kwa Lazio ikiwa ugenini kucherzea kichapo cha mabao 2-1.
Cigarini alitangulia kuifungia wenyeji bao katika kipindi cha kwanza bao lilidumu hadi mapumziko kabla ya Brayan Perea kuisawazishia Lazio dakika ya 53, lakini bao la kwenye dakika ya 84 lililofungwa na Dennis liliwapa ushindi wenyeji.
Jioni hii kuna mechi nyingine za ligi hiyo, Juventus ikialikwa na Fiorentina, Inter Milan kupepetana na Torino, huku Genoa kuonyeshana kazi na Chievo.
Mechi nyingine zitakuwa ni kati ya Hellas Verona itakayoialika Parma na Livorno ikiikaribisha Sampodoria.

Polisi Dar wanasa wamwagia tindikali

 
Kamanda Kova
JESHI la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kujihusisha na matukio ya kumwagia watu kemikali aina ya tindikali.
Watuhumiwa hao ambao hata hivyo hawakutajwa majina, walikamatwa Oktoba 10, mwaka huu saa 2:00 asubuhi katika maeneo ya Lumumba, Kariakoo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana ofisini kwake, Kamishna wa Polisi, Kamanda wa Kanda hiyo Suleiman Kova alisema, watuhumiwa hao walikiri kuhusika na tukio moja la kummwagia mfanyabiashara Ally Farhat (33) ambaye ni raia wa Lebanon, tukio ambalo liliripotiwa katika Kituo cha Polisi Msimbazi.
"Taarifa za kiintelejensia zinaonesha mbinu zilizotumika katika tukio hilo zinawiana na tukio la kumwagiwa sumu aina ya tindikali mfanyabiashara aitwaye Said Mohamed maarufu kama Saad (42) ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Home Shopping Center (HSC), tukio ambalo lilifanyika maeneo ya Msasani katika jengo la Msasani City Mall mwezi Julai, mwaka huu," alisema Kamanda Kova.
Hata hivyo Kamanda Kova hakutaka kuwataja majina yao kutokana na kile alichosema bado wanaendelea kuwahoji hivyo wanahofia kupoteza ushahidi endapo majina hayo yatawekwa wazi.
Aidha alisema pia wanaendelea kuwahoji ili kubaini ushiriki wao katika tukio hilo, pia wanashirikiana na mikoa ya Zanzibar na mikoa mingine ili kubaini kama walishiriki katika matukio ya aina hiyo.
Aidha katika tukio jingine Kamanda Kova alisema, wamefanikiwa kumkamata mtuhumiwa mmoja Raia wa Somali aitwaye Jamal Ibrahim (42) akiwa na nyaraka za Serikali zikiwemo stakabadhi za malipo ya vibali vya makazi.
Kamanda Kova alitaja vitu alivyokutwa navyo mtu huyo kuwa ni pamoja na fomu namba 130 za maombi ya makazi, stakabadhi 21 za malipo ya vibali vya makazi, nakala nane za hati za kusafiria zenye picha za waombaji ambao ni raia wa Somalia na bahasha moja yenye picha mbalimbali za waombaji ambao ni raia wa Somalia.

Orlando Pirates yatangulia fainali za Mabingwa Afrika

ORLANDO Pirates ya Afrika Kusini imetangulia Fainali za Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya jana kupata sare ya bao 1-1 ikiwa ugenini dhidi ya Esperance ya Tunisia.
Pirates imefuzu fainali hizo kwa faida ya bao la ugenini kwani katika mechi yao ya kwanza iliyochezwa Afrika Kusini timu hizo zilitoka suluhu ya bila kufungana na sare ya jana ina maanisha imefuzu kwa faida ya bao la ugenini linalohesabiwa kama mawili.
Wageni hawakuwa na kazi rahisi kwani walimaliza dakika 45 za kwanza wakiwa 0-0 na kuingia kipindi cha pili kwa kishindo kwa kuwashtua wenyeji baada ya kupata bao la kuongoza lililofungwa katika dakika ya 51 na Rooi Petros Muhamutsa.
Hata hivyo wenyeji walichomoa bao hilo dakika chache baadaye kupuitia kwa Mohammed Iheb Msakni na matokeo kusalia hivyo hadi dakika ya mwisho na kuifanya Pirates kusubiri mshindi wa pambano la leo kati ya wenyeji Al Ahly ya Misri dhidi ya Cotton Sports ya Cameroon, ambazo katika mechi ya awali Wamisiri walilazimisha sare ugenini ya bao 1-1, hivyo kuwa na kazi ya kulazimisha suluhu ili kuungana na Wasauzi.

Mtangazaji aliyepigwa risasi aanza kufunguka juu ya mkasa wake, inatisha



Ufoo Saro akiwa na Rais Kikwete
MWANDISHI  wa Kituo cha Televisheni cha ITV, Ufoo Saro ambaye hivi karibuni alikumbwa na madhila ya kupigwa risasi na kujeruhiwa vibaya na mzazi mwenzie, ameanza kufunguka kidogo kidogo na kueleza kwa kina jinsi tukio zima lilivyotokea.  Akizungumza kwa sauti ndogo na taratibu na gazeti hili kando ya kitanda alicholazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, mwanahabari huyo alieleza kushangazwa na ujasiri na nguvu za aina yake ambazo zilimwezesha kutambaa na kujiburuza hadi eneo la karibu ya barabara ili kuomba msaada wa kukimbizwa hospitali.

Ufoo ambaye alionyesha dhahiri kutofurahishwa na baadhi ya taarifa zinazozingira tukio lake, alisema tayari alikuwa amewahakikishia polisi waliofika kumjulia hali hospitalini hapo kwamba alikuwa akisubiri afya yake iimarike kabla hajaeleza kwa kina kila anachokijua kuhusiana na tukio hilo.

“Alifika hapa kunijulia hali na kuangalia maendeleo yangu afande Msangi na nikasema nitakuwa tayari kueleza kila ninachokijua baada ya afya yangu kuimarika. Nasikitika kuna watu wanasema mambo wakifikia hatua ya kutaka kuonekana wananifahamu vizuri kuliko hata ninavyojifahamu mwenyewe,” alisema akionyesha kutofurahishwa na baadhi ya taarifa zinazoripotiwa kuhusu sakata lake.


Ufoo ambaye alifikishwa hospitalini hapo Jumapili ya wiki iliyopita kutokana na kujeruhiwa kwa risasi na mwanaume aliyezaa naye mtoto mmoja alisema anamshukuru sana Mungu kwa uzima alionao sambamba na kuelezwa kupata faraja kubwa na kutiwa moyo na mwajiri wake, ndugu, jamaa na marafiki.


Ufoo Saro kushoto akiwajibika
Mwanahabari huyo ambaye bado yuko chini ya uangalizi wa karibu wa madaktari baada ya kufanyiwa upasuaji wa kuondoa risasi mwilini mwake siku chache zilizopita, amelazwa katika chumba cha peke yake ambacho ingawa kina seti ya televisheni alisema alikuwa haruhusiwi kuiangalia kwa ushauri na maelekezo ya madaktari.

Huku akionekana wa chini ya uangalizi mwingine wa karibu na wa kudumu wa muuguzi ambaye muda wote wa mazungumzo haya alionekana kuwapo katika chumba hicho, Ufoo alisema alikuwa ana mapenzi makubwa kwa mzazi mwenzake huyo ambaye alipoteza maisha katika tukio hilo.

“Nilimpenda sana Antheri. Alikuwa kijana mtaratibu na mpole sana. Najua kile kilichotokea ni shetani tu na binafsi nilishasamehe alfajiri ile ile baada ya tukio lile,” alieleza Ufoo ambaye pia alimpoteza mama yake mzazi katika mkasa huo.

TUKIO ZIMA LILIVYOTOKEA

Ufoo ambaye mara kadhaa katika mazungumzo na gazeti hili alionekana kukunja uso akiashiria kupata maumivu, alionyesha eneo la chini ya bega katika mkono wake wa kulia lililofungwa na bandeji ambalo alisema ndipo alipopigwa risasi ya kwanza wakati akigeuka na kujaribu kuepuka mauti muda mfupi baada ya Antheri kumfyatulia risasi zilizomkuta mama yake mzazi.

Ufoo Saro alipokuwa akitolewa kwenye chumba cha upasuaji Muhimbili
Akijaribu kuvuta kumbukumbu ya tukio lilivyoanza, Ufoo alisema mzazi mwenzake huyo alifika nyumbani kwake akitokea Sudan alikokuwa akifanya kazi usiku huo huo wa tukio na akamtaka kwenda kwa mama yake (Ufoo) eneo la Kibamba, nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.

Kabla ya kufika Kibamba na kwa sababu ambazo Ufoo hakuzieleza, alimkariri mzazi mwenzake huyo akisema alikuwa amefikia uamuzi wa kujiua yeye na mtoto wao.

“Hata sijui ni nini kilitokea. Wakati tukitoka nyumbani Antheri alianza kwa kuniambia kwamba alikuwa amepanga kujiua yeye na mtoto wetu,” alisema Ufoo kabla ya kukaa kimya kwa sekunde kadhaa na kuendelea na simulizi yake ya kusikitisha.

Akiwa na sura ya ujasiri, Ufoo anasema pamoja na kumwambia maneno hayo bado Mushi alimsisitiza kwamba waende kwa mama yake (Ufoo) baadae warudi kumchukua mtoto wao japo Ufoo hakusema walitaka kwenda wapi baada ya hapo.

Alisema walipofika nyumbani kwa mama yake walikwenda moja kwa moja sebuleni na wakiwa wamekaa kwenye makochi baada ya salamu za hapa na pale ghafla Mushi akasimama akamwambia mama yake Ufoo kwamba; “Mama nimeishafanya maamuzi”

Kwa mujibu wa maelezo ya Ufoo, baada ya Mushi kutamka maneno hayo ghafla akaingiza mkono nyuma ya suruali  alikokuwa ameweka bastola  yake na kisha akaichomoa.

Katika maelezo yake Ufoo alisema baada ya kuichomoa bastola hiyo mama yake naye alisimama na kwenda kujaribu kumpokonya, kitendo hicho kilimfanya amiminiwe risasi mfululizo.

Alisema kuona hivyo aliamua kukimbia kuelekea jikoni ambapo Mushi alimuona na kuanza kumiminia risasi ambayo moja ilimpata eneo la mkono wa kulia ambayo ilitokezea mbele na kuchana titi la kulia.

Kwa mujibu wa Ufoo jeraha hilo halikumfanya akate tamaa ya kunusuru maisha yake kwani alijaribu kukimbia ingawa Antheri alifyatua risasi nyingine kadhaa ambazo zilimpata juu kidogo ya mgongo na kutokea tumboni ambazo zilisababisha aanguke chini

Akiendelea kusimulia, anasema ingawa alikuwa akivuja damu nyingi, na huku akijiburuza ardhini, Ufoo alisema wakati akitambaa aligeuka nyuma na akamuona Antheri akijielekeza bastola eneo la kidevu na alipofyatua risasi alianguka chini.

“Nikiwa chini nilimuona Antheri akijipiga risasi kidevuni na akaanguka chini, sikujua kilichofuata baada ya hapo kwani niliendelea kujiburuza ili kuokoa maisha yangu,” alisema Ufoo

ALIVYOJIOKOA

“Nyumbani kwetu, pale Kibamba si mbali sana na barabarani, wakati nikikaribia kufika barabarani wakati huo nikitokwa na damu nyingi huku nikihisi tumbo langu limejaa sana nilikutana na dada mmoja ambaye nilimuomba khanga ili nijifunge kuzuia damu zisitoke kwa wingi”.

Anasema dada yule alimpa khanga akajifunga na aliposogea barabarani alikutana na gari lililokuwa likiendeshwa na mwanamke mmoja.

“Nilipoona kuna gari linapita nikainuka kuomba msaada. Liliposimama nilimuona mwanamke akiendesha nikamweleza kwamba nilikuwa nimepigwa risasi na nilikuwa nikiomba msaada wake anikimbize hadi katika hospitali ya Tumbi na kwamba akifika pale tu aniache mlangoni.

“Si rahisi kuamini, yule mama alikataa kunisaidia akisema alikuwa akiwahi sehemu kumchukua mzazi. Sina la kusema niliamua kumsamehe tu yule mama ingawa niliumia sana,” alisema Ufoo.

Alisema muda mfupi tu baadaye alitokea kijana aliyekuwa na pikipiki, maarufu kwa jina la bodaboda ambaye alimuomba msaada wa kumkimbiza hospitali ya Tumbi na akakubali.

“Yule kijana aliniuliza iwapo nilikuwa ninao uwezo wa kujishikilia vizuri na niliposema nitaweza akanisaidia kupanda katika bodaboda.

“Wakati huo nilikuwa naona kama tumbo linazidi kujaa. Nikiwa kwenye pikipiki kuna wakati nilikuwa nikihisi kwamba naweza nikaishiwa nguvu na kuanguka katika barabara na kisha kupitiwa na gari na kupoteza maisha. Lakini nilipata ujasiri na kujishikilia,” alieleza kwa sauti ya chini.


Alisema anakumbuka wakati walipofika eneo la Kibaha ilipo mizani ya kupima uzito wa magari makubwa walikuta barabara ikiwa imejaa magari na yeye alimuomba dereva huyo wa bodaboda kupita hata nje ya barabara eneo la nyasi ili kumwahisha hospitalini jambo ambalo kijana yule alilifanya.

“Nilipofika eneo la mapokezi pale Tumbi nilimueleza muuguzi niliyemkuta kwamba nilikuwa nimejeruhiwa kwa risasi na nikamuomba asaidie kuokoa maisha yangu. Yule nesi alisita akitaka kwanza kupata kibali cha polisi (PF3) lakini nikaumuomba apigiwe simu, Kaimu Mganga Mkuu wa Tumbi, Dk. Dattan ambaye tunafahamiana”

“Baada ya muda mfupi Dk. Dattan alifika na nikamweleza yaliyonipata na mara moja nikaanza kuhudumiwa kwa kuniwekea dripu, na nikamsikia akiwaeleza wauguzi kwamba isingekuwa busara kwa hali niliyonayo kama wangeanza kuchukua picha za X-ray kwani hatua hizo zingeweza kusababisha kupoteza maisha,” alieleza akikumbuka yaliyojiri hapo Tumbi.

Kwa mujibu wa Ufoo, akiwa bado ana fahamu alimsikia daktari aliyekuwa akimhudumia akiomba msaada wa gari la kubeba wagonjwa ili limchukue na kumkimbiza katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili wito ambao ulijibiwa kwa maelezo kwamba lilikuwa halina mafuta.

Majibu hayo kwa mujibu wa Ufoo, yalisababisha daktari huyo aombe kuletewa gari la wagonjwa la wagonjwa maarufu (VIP) ambalo lililitwa na muda mfupi baadaye akapakizwa tayari kwa safari ya kukimbizwa Muhimbili.

Alisema wakati akikimbizwa Muhimbili anakumbuka namna alivyokuwa akipatwa na maumivu makali wakati wote gari ile ya wagonjwa ilipokuwa ikipanda matuta ya barabarani na kuna nyakati alikuwa akihisi kupoteza pumzi na kuishiwa nguvu. 


RAI

PSG yaua Ufaransa, Ibrahimovic akipiga bao la mwaka

Zlatan Ibrahimovic
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Ufaransa, PSG jana ilitoa kipigo cha mbwa mwizi wakati walipoisulubu Bastia kwa mabao 4-0 na kuiengua Monaco kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo kwa muda.
Mabao mawili ya kipindi cha kwanza kutoka kwa mshambuliaji 'mtukutu' kutoka Sweden Zlatan Abrahimovic moja likiwa la aina yake akiunganisha mpira kwa tiktak ya kisigino na kumtungia kipa wa Bastia.
Magoili mengine yalifungwa katika kipindi cha pili na Edinson Cavani na kuifanya PSG ikwee kileleni ikiwa na pointi 24.
Cavani aliifungia PSG bao la nne kwa mkwaju wa penati na kuzima matumaini ya wageni Bastia ambayo imeporomoka hadi nafasi ya 13 katika msimamo wa ligi hiyo.

Hata hivyo huenda mabingwa hao wakaa kwa muda tu katika kiti hicho cha uongozi kabla ya kuwapisha Monaco ambayo muda mchache ujao itashuka dimba la ugenini kupepetana na Sochaux. Monaco ikishinda itarejea kileleni kwa tofauti na mabao ya kufunga na kufungwa.
Katika mechi nyingine za ligi hiyo maarufu kama Ligue 1, juzi Ijumaa Nice iliinyoa Olimpique Marseille kwa bao 1-0, Reims ikilala nyumbani kwa mabao 2-1 mbele ya Toulouse, huku jana Ajaccio ikiwa nyumbani ilikubali kipigo cha bao 1-0 toka kwa Nantes, Evian TG nayo ikilala 2-1 nyumbani dhidi ya Guingamp, nayo Lille ikiicharaza Montpellier bao 1-0 na Rennes na Valenciennes zikitoka sare ya mabao 2-2.
Leo mbali na Monaco kuvaana na Sochaux ugenini, Saint Etienne itaialika Lorient na Olimpicque Lyon itapepetana na wageni wao Bordeaux.

Juma Luizio amchimbwa mkwara Tambwe

Juma Luizio (kushoto) alipokuwa katika mazoezi ya Taifa Stars nchini Uganda hiviu karibuni
MSHAMBULIAJI chipukizi anayekuja juu nchini anayeichezea Mtibwa Sugar, Juma Luizio 'Ndanda' amemchimba mkwara mkali wa mabao wa Simba Amissi Tambwe akimwabia asahau kuhusu kiatu cha dhahabu cha ufungaji bora msimu huu kwani hicho ni mali yake.
Luizio amesema anataka kuwa mfungaji bora msimu huu na kumuapia Tambwe kuwa atakula naye sahani moja.
Akizungumza na MICHARAZO hivi punde, Luizio ambaye jana alifunga mabao mawili wakati Mtibwa Sugar ikizamisha Mgambo JKT kwa mabao 4-1 na kufikisha jumla ya mabao saba moja nyuma ya Tambwe mwenye mabao nane, alisema lengo lake ni kufunga jumla ya mabao 17.
Chipukizi huyo aliyeanza kuitumikia timu ya wakubwa ya Mtibwa Sugar mwaka jana baada ya kupandishwa kutoka kikosi cha vijana, alisema amekuwa akitupia mipira nyavuni kwa lengo la kuwa Mfungaji Bora na kunyakua kiatu cha dhahabu.
Luizio alisema kila Mtibwa inapokuwa dimbani akili zake uziweka katika kutikisa nyavu na ndiyo maana amekuwa akifunga karibu kila mechi na kudai lengo ni kuwa mfungaji bora na siyo kuwasindikiza wenzake.
"Nafunga kwa sababu nataka kuwa mfungaji bora, nimepanga msimu huu nitupie jumla ya mabao 17 ambayo naamini yatanibebesha kiatu hicho, yakizidi haitakuwa neno," alisema.
Kuhusu kinara wa mabao kwa sasa Mrundi Amissi Tambwe wa Simba, Luizio alisema hana hofu naye kwani atamkamata na kumpita kutokana na kasi yake kuongezeka siku hadi siku.
Mshambuliaji huyo aliyewahi kuzichezea timu za Docks na Polisi Morogoro kabla ya kutua Mtibwa baada ya kung'ara kwenye michuano ya Taifa Cup na kuwa Mfungaji Bora namba mbili wa Uhai Cup mwaka uliopita, alisema ligi ni ngumu lakini atapigana kutimiza lengo.
Luizio alifichua siri ya mafanikio yake ya kufumania nyavu ni kuaminiwa na makocha na kuiga kwake mbinu za Zlatan Ibrahimovic anayemzimia.

Msiba! Mtangazaji Julius Nyaisanga 'Uncle J' hatunaye


Julius Nyaisanga enzi za uhai wake
TAARIFA zilizotufikia kutokana Morogoro zinasema kuwa, Mtangazajai nguli aliyewahi kutamba na vituo mbalimbali vya Radio kuanzia RTD, Radio One/ITV, Julius Nyaisangah 'Uncle J' amefariki dunia kutokana na kuugua kwa muda mrefu akiwa hospitali ya Mazimbu mjini humo.
Marehemu Nyaisanga anayekumbukwa kwa umahiri wake wa kutangaza taarifa habari na kuendesha vipindi vya Misakato na Klabu Raha Leo Show wakati yupo RTD na kisha kutisha na Mambo Mseto na Watoto Show akifahamika kama Babu wa Kimazichana akiwa Radio One, mpaka mauti yanamkumba alikuwa Mhairir Mtendaji wa Abood Media inayomiliki vituo vya Radio Abood na Abood Televisheni za mjini Morogoro.
Haijafahamika chanzo halisi cha mauti ya mtangazaji huyo, japo inaelezwa alikuwa akiigua kwa muda mrefu kisukari na Shinikizo la damu.
MICHARAZO inatoa pole kwa ndugu, jamaa na familia ya marehemu pamoja na wadau wote wa tasnia ya habari na kuwatakia subira katika kipindi hiki kigumu cha msiba.
Mungu ailaze roho ya marehemu mahali pema  Ameen