STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, April 15, 2011

Ligi ya Kick Boxing sasa Juni





MICHUANO ya Ligi ya Ubingwa kwa Mchezo wa Kick Boxing iliyokuwa ichezwe mwishoni mwa Machi, imesogezwa mbele hadi Juni mwaka huu.
Mratibu wa michuano hiyo, Japhet Kaseba, alisema ligi hiyo imekwama kufanyika kutokana na kutingwa na mazoezi ya maandalizi ya pambano lake la Ngumi za Kulipwa kati yake na bondia Mada Maugo.
Kaseba atapigana na Maugo, wiki ijayo kwenye ukumbi wa PTA, Dar es Salaam katika pambano lisilo na mkanda la uzito wa kilo 72 kuwania nafasi ya kupigana na bingwa wa dunia, Francis Cheka wa Morogoro.
Akizungumza na MICHARAZO, Kaseba, alisema kubanwa na mazoezi kumemfanya ashindwe kuratibu ligi hiyo na kusema, mara baada ya pambano lake atatangaza tarehe rasmi ya ligi hiyo ingawa alisema kuna uwezekano ikafanyika mwezi Juni.
"Nimeshindwa kuratibu ligi kama nilivyopanga ifanyike Machi na sasa natarajia ifanyike Juni, ingawa tarehe nitaitangaza baada ya kumaliza pambano langu dhidi ya Maugo ambalo ndilo lililonifanya niwe 'bize', nataka kumpiga nikapigane na Cheka," alisema.
Kuhusu maandalizi ya pambano hilo, Kaseba alisema anaendelea vema na ana matumaini makubwa ya kushinda pambano hilo, la raundi 10 lililoandaliwa na Double K Entertainment, litakalosimamiwa na TPBO inayoongoza na Rais wake, Yasin 'Ustaadh' Abdalla.
"Kwa kweli naendelea vema, najifua usiku na mchana kuhakikisha nakuwa fiti nimpige Maugo, ili nikavaane na Cheka kuthibitishia mashabiki wangu kuwa, sikupigwa kihalali na Cheka kwenye pambano letu la uwanja wa Uhuru," alisema Kaseba.


Mwisho

Matumla kuzichapa Dodoma




BINGWA wa zamani wa Dunia wa Ngumi za Kulipwa nchini, Rashid Matumla 'Snake Man' anatarajiwa kupanda ulingoni siku ya Pasaka kuzipiga na Mkenya, Joseph Odhiambo katika pambano litakalofanyika mjini Dodoma.
Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO, Yasin Abdallah 'Ustaadh', alisema pambano lisilo la ubingwa la uzani wa Middle, litakuwa la raundi 10.
Ustaadh, alisema lengo la pambano hilo ni kusaidia kuinua mchezo wa ngumi mkoani humo sambamba na kuwapelekea burudani wakazi wa mji huo ambao watakuwa wakisherehekea sikukuu ya Pasaka.
"Dodoma imekuwa ikipelekewa burudani za muziki, mpira na kadhalika, lakini mchezo wa ngumi kwa muda mrefu haujafanyika mjini humo na TPBO tumeamua kuwapelekea pambano hilo kubwa kama njia ya kuhamasisha mchezo huo na kuwaburudisha wakati wa sikukuu," alisema.
Alisema maandalizi ya pambano hilo litakalodhaminiwa na mfanyabiashara maarufu wa mjini humo, Moshi Semayu yamekamilika na watautangazia umma pambano hilo litafanyikia wapi, ingawa alikuwa na hamu lifanyike uwanja wa Jamhuri, mjini humo.
Aliongeza, baada ya pambano hilo la Dodoma, TPBO ilikuwa itafanya mipango ya kuandaa michezo mingine ya ngumi za kulipwa katika mikoa ya Mbeya, Iringa, Singida na kadhalika kwa lengo la kuuhamasisha mchezo huo katika mikoa hiyo.
Matumla, aliyewahi kuwa bingwa wa dunia wa WBU, alisema yupo fiti kumchapa Odhiambo, ili kudhihirisha kuwa yeye bado wamo katikia mchezo huo uliomjengea sifa ndani na nje ya nchi.

Wakazi wa Udzungwa kufunzwa namna ya kutunza Mbega

SHIRIKA lisilo la kiserikali la STR8 UP Vibes imeandaa warsha maalum kwa wakazi wanaoizunguka hifadhi ya Udzungwa juu ya kuwatunza wanyama aina ya Mbega wekundu wanaopatikana kwenye hifadhi hiyo.
Warsha hiyo imepangwa kufanyika hivi karibuni, mkoani Morogoro, ambapo mbali ya kuwatunza wanyama hao lakini pia itakuwa na lengo la kutoa elimu ya kuvitunza vyanzo vya maji.
Akizungumza na Mtandao huu, mratibu wa warsha hiyo, Salum Kondo alisema kuwa, wameamua kuandaa warsha hiyo ili kuwapa elimu ya kutosha watu wote wanaoishi kando kando ya hifadhi za taifa kujua jinsi ya kuwatunza wanyama na vyanzo vya maji.
Kondo, alieleza kuwa kwa kuanzia wamemua kuanza na mkoa wa Morogoro, ambapo baadaye wataaendelea kwenye mikoa mingine iliyo na hifadhi za Taifa.
"Dhumuni letu ni kuwapa elimu watu wote wanaishi karibu na hifadhi za Taifa, lakini kutokana na umuhimu wa hifadhi za Udzungwa, tumekubaliana tuanzie huko" alisema.
Aliongeza kuwa kumekuwa na ongezeko kubwa la kuwauwa Mbega Wekundu, hali ambayo inaweza kusababisha wanyama hao kutoweka kabisa Duniani.
Kondo aliongeza kuwa kwa kuwa wanyama hao hupatikana, Udzungwa pekee, wameona kuna haja ya kuwalinda kwa gharama yeyote.
"Kama wakazi wa wanaizunguka hiafdhi ya Udzungwa watapatiwa elimu ya kutosha juu ya kuwatunza wanyama hao na namna ya kuwatumia kuwaingizia kipato, bila shaka wataacha kuwaua," alisema.
Kondo alisema katika Kongamano hilo litakalofanyika mkoani Morogoro linatarajia kuwashirikisha wadau mbali ikiwa ni pamoja na wanavijiji, wataalam kutoka wizara ya Maliasili na Utalii, ambapo pia kutakuwa na burudani mbalimbali zitakazowakilisha mila na tamaduni za mkoa huo.

KITABU CHA ASSOSA CHATOKA HADHARANI




Na Badru Kimwaga
MWANAMUZIKI mkongwe wa muziki wa dansi, Tshimanga Kalala Assosa, amekamilisha kitabu chake cha tafsiri ya Lugha ya Kilingala na Kiswahili kiitwacho 'Jifunze Lingala', ambapo licha ya kufunza lugha hizo mbili pia ina nyimbo kadhaa za wanamuziki wa zamani wa DR Congo (Zaire).
Kitabu hicho kilichoanza kuandaliwa tangu mwishoni mwa mwaka jana, tayari kimeshachapishwa na mwanamuziki huyo anayemiliki bendi ya Bana Marquiz anafanya mipango ya kuanza kuvisambaza ili wadau wa muziki wa lingala na wengineo waanze kukipata.
Akizungumza na MICHARAZO, Assosa, aliyewahi kutamba na bendi mbalimbali kama 'Negro Succes', 'Le Kamalee', 'Lipualipua' na 'Fukafuka', alisema kitabu hicho ni mwanzo wa kujitosa kwenye kazi ya uandikaji vitabu wenye lengo la kufundisha lugha ya Kilingala, moja ya lugha maarufu ya Congo.
Assosa, alisema msukumo wa kuandika kitabu hicho alichochapisha nakala 50,000 za awali kama majaribio ni kutokana na simu na maombi ya mashabiki wa muziki wanaofuatilia fasiri zake katika kituo cha TBC! kinachohusu miziki ya Kavasha.
"Nilikuwa napokea simu nyingi za kuwatafsiria watu baadhi ya nyimbo za nyota wa zamani wa Zaire (sasa DR Congo) na kupata wazo la kuandaa kitabu kwa mfumo wa kamusi ambao pia una nyimbo za wakali hao na tafsiri mbalimbali za maneno ya lugha hiyo," alisema Assosa.
Mtunzi na muimbaji huyo aliyefanyia kazi bendi nyingine za 'Mambo Bado', 'Legho Stars', 'DDC Mlimani Park', 'Marquiz du Zaire' na ile ya Original, alisema mafanikio ya mauzo ya kitabu hicho kitamfanya aweze kutoa muendelezo wake siku za baadae.
Assosa, alisema shukrani pekee katika maandalizi ya kitabu hicho 'toleo la kwanza' ni kwa wanachama wa klabu ya Dar Family Kavasha na Mhariri, Joseph Kulangwa aliyekihariri hadi kuweza kuchapishwa na kuandaliwa kuachiwa mtaani wakati wowote kuanzia sasa.
Mwanamuziki huyo aliyetamba kwa utunzi wa nyimbo kama 'Minou', 'Salama', 'Huba', 'Promotion' 'Masua' na 'Abisina' alizoimba kwa kushirikiana na Nyboma Mwandido, alisema pamoja na kutaka kujitosa jumla kwenye utunzi wa vitabu, bado hajaachana na kazi ya muziki akiwa na bendi yake ya Bana Marquiz ambayo inaendeela kutumbuiza kuanzia Alhamis hadi Jumapili kila wiki.

Mwisho

KASEBA, MAUGO WAPIMA UZITO KUZIPIGA KESHO PTA






MABONDIA Japhet Kaseba na Mada Maugo pamoja na watakaowasindikiza kwenye pambano lao litakalofanyika Jumamosi, wanatarajiwa kupima uzito wao leo jijini Dar es Salaam.
Upimaji huo wa uzito utafanyika kwenye ukumbi wa Idara ya Habari-MAELEZO saa 5 asubuhi, ukihusisha pia upimaji wa afya kama moja ya kampeni ya kupambana na ukimwi michezoni.
Akizungumza na MICHARAZO asubuhi ya leo, Mratibu wa pambano hilo, Kaike Siraju, alisema mabondia wote watakaopigana Jumamosi watapimwa leo tayari kwa michezo hiyo itakayofanyika kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es salaam.
Siraju, alisema mbali na Kaseba na Maugo watakaopogana kwenye pambano la kusaka mkali kati yao ili kupata tiketi ya kwenda kupigana na Francis Cheka, mabondia wengine watakaopimwa ni wale watakaosindikiza pambano hilo.
"Mabondia wanaotarajiwa kucheza siku ya Jumamosi kwenye pambano la kusaka mkali kati ya Kaseba na Maugo, watapimwa uzito na afya yao siku ya Ijumaa majira ya saa 5 asubuhi kwenye ukumbi wa Idara ya Habari-Maelezo," alisema Siraju.
Siraju, alisema maandalizi ya michezo yote ikihusisha pambano hilo la Nani Mkali la uzani wa Middle raundi 10, yamekamilika na kinachosubiriwa ni mashabiki kwenda ukumbini kupata burudani.
Michezo itakayosindikiza pambano hilo la Kaseba na Maugo, ni lile la Bingwa wa Kick Boxing wa Afrika, Kanda Kabondo atakayezipiga na Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo', nahodha wa zamani wa ngumi za ridhaa, Joseph Martin dhidi ya George Dimoso.
Mapambano mengine ni la Yohana Robert dhidi ya Saidi Zungu, Deo Njiku atakayepigana na Issa Sewa, Fadhili Awadh atapigana na Bakari Dunda na Hassan Mandula atatwangana na Uwesu Said, Mohammed Matumla 'Snake Boy Junior' atakayeonyeshana kazi na Sadiki Momba.

Mwisho

Mafisango ambadili Humud Simba






KIUNGO aliyetua Msimbazi kwa mbwembwe na kuishia kushindwa kutamba katika timu ya Simba kutokana na majeruhi ya mara kwa mara, Abdulhalim Humoud, ametua Azam akipishana na beki Mnyarwanda Patrick Mafisango.
Humoud aliyesajiliwa na Simba msimu uliopita akitokea Mtibwa Sugar, ikiwa ni siku chache tangu ang'are kwenye pambano la kihistoria la kimataifa kati ya Tanzania na Brazil, ni miongoni mwa wachezaji wapya waliotua Azam kwa ajili ya msimu ujao.
Kwa mujibu wa taarifa za mtandao wa klabu hiyo, kiungo huyo anayependa kufananishwa na Ronaldinho Gaucho, ametua Azam akibadilishana na beki Mafisango aliyeenda Msimbazi kuimarisha kikosi chao kilichopoteza ubingwa kwa Yanga.
Wachezaji wengine wapya waliotuma Azam, ikiwa ni kati ya wachezaji 20 waliopendekezwa na kocha wao, Stewart Hall ni pamoja na aliyekuwa kipa wa Yanga,
Obren Cuckovic toka Serbia na Mwadini Ally aliyekuwa Mafunzo ya Zanzibar.
Pia wamo Waziri Salum toka Mafunzo, Ghulam Abdallah wa Chuoni Zanzibar, Zahor Pazi wa African Lyon na nyota wa Ocean View, Khamis Mcha 'Viali'.
Habari hizo zinasema kuwa hao ni sehemu ya wachezaji wapya wanaotua Azam kuungana na wachezaji wengine walioisaidia klabu hiyo kushika nafasi ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ambao wameshasainishwa mikataba mipya.
Wachezaji hao kwa mujibu wa mtandao huo ni Manahodha Ibrahim Shikanda na Aggrey Moris, Malika Ndeule, Lackson Kakolaki, Erasto Nyoni, Ibrahim Mwaipopo, Seleman Kasim Selembe, Kalimangonga Ongala, Jamal Mnyate, Mrisho Ngassa na John Bocco.
Wachezaji vijana waliokuwa wamepandishwa kwenye kikosi hicho toka timu ya vijana na kubakishwa ni Himid Mao, Salum Aboubakar na Jamal Mnyate, wakiongezewa nguvu na kipa Daudi Mwasongwe aliyepandishwa toka Azam Academy.
Makipa Vladmir Nhyonkulu na Jackson Chove pamoja na wachezaji wengine kama saba walioichezea timu hiyo wapo katika hatihati ya kuendelea kubaki katika kikosi hicho kinachosukwa kwa ajili ya kuongeza upinzani kwa msimu ujao wa ligi kuu nchini.

Mwisho

Tundaman ni Bora Tuachane tu



MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya toka kundi la Tip Top Connection, Khaleed Ramadhan 'Tundaman', ameachia kibao kipya kiitwacho 'Bora Tuachane', akiwa mbioni kufyatua wimbo mwingine akiwashirikisha Mapacha wa kundi la P Square la Nigeria.
Nyimbo hizo mbili ni maandalizi ya kufyatuliwa kwa albamu yake mpya itakayokuwa ya nne kwa msanii huyo aliyetumbukia kwenye sanaa ya muziki mwaka 2007 akitokea kwenye soka.
Akizungumza na MICHARAZO, Tundaman, alisema kibao hicho cha 'Bora Tuachane' ambacho kinatarajiwa kusambazwa hivi karibuni ni simulizi la kweli linalomhusu yeye.
"Wakati albamu yangu ya Hali Yangu Mbaya ikitamba sokoni, nimeanza maandalizi ya kufyatua albamu mpya ya nne, ambapo nimeachia ngoma inakwenda kwa jina la 'Bora Tuachane' ambao ni simulizi la kweli linalonihusu mimi mwenyewe," alisema Tundaman.
Msanii huyo, mwenye mtoto mmoja wa kike aitwae Khairat, alisema kama zilivyo nyimbo zake za nyuma, kibao hicho kipo katika mahadhi ya 'kulalamika' na kutamba kitabamba kutokana na ujumbe uliopo na midundo yake inayovutia.
Aliongeza mbali na kibao hicho, pia ana wimbo mwingine mpya ambao ataimba kwa kushirikiana na wasanii wawili mapacha wa Nigeria, P Square.
"Kibao kingine ninachokiandaa ni The All One, ambacho nimewatumia mistari P Square ili waweke sauti zao, kabla ya kuja kuchanganywa, mie nitaimba kiswahili na wao wataimba kwa lugha ya Kiingereza, lengo likiwa ni kusaka hadhi ya kimataifa," alisema.
Tundaman, aliyewahi kuzichezea timu za Friends Rangers na Yanga kabla ya kuhamia kwenye muziki, hadi sasa ana albamu tatu, ambazo ni Neila iliyomtambulisha rasmi kwenye ulimwengu wa muziki huo, Nipe Ripoti alioshirikiana na Spark na Hali Yangu Mbaya, aliyoachia hivi karibuni.

Coast Modern wapika albamu ya nne



BAADA ya kutamba na albamu yao ya 'Damu Nzito', kundi mahiri la muziki wa taarab la Coast Modern 'Watafiti wa Mipasho', limeanza maandalizi ya albamu yao mpya ya nne ikiwa imeshakamilisha nyimbo zipatazo tatu hadi sasa.
Mkurugenzi wa kundi hilo, Omar Tego 'Special One' aliiambia MICHARAZO kuwa, nyimbo tatu kati ya nne zinazolengwa kuwepo kwenye albamu hiyo ijayo zimeshakamilika kutungwa na kufanyiwa mazoezi tayari kupelekwa studio kurekodiwa.
Hata hivuo Tego alikataa kuzitaja nyimbo hizo kwa madai ni mapema mno na pia kuhofia asiibiwe 'idea' na wapinzani wake katika muziki huo wa taarab nchini.
"Tupo katika maandalizi ya kufyatua albamu yetu mpya itakayokuwa ya nne kwa Coast Modern, tayari tumekamilisha nyimbo tatu na tumesaliwa na mmoja, kuhitimisha nyimbo zitazotakiwa kabla ya kuzipeleka studio kurekodiwa," alisema Tego.
Tego alisema kwa jinsi walivyojipanga, huenda albamu hiyo ikakamilika na kuwa mitaani kabla ya Julai, kwani karibu kila kitu kimekamilisha wanachosubiri ni kuingia studio.
Alisema wataichelewesha kidogo albamu hiyo kutoka hadi Julai kwa nia ya kutoa nafasi ya albamu yao ya sasa ya 'Damu Nzito' kuendelea kutamba kwenye soko la muziki huo.
"Unajua tumeachia 'Damu Nzito' muda mfupi tu uliopita, hivyo ili kuipa nafasi ya kufanya vema sokoni, ndio maana tumepanga kuitoa albamu yetu ya nne kabla ya Julai," alisema Tego.
Kabla ya albamu hiyo ya 'Damu Nzito' kundi hilo la Coast Modern, liliachia albamu mbili zilizotikisa muziki wa mwambao nchini za 'I'm Crazy For You' na 'Kupendwa Isiwe Tabu' iliyokuwa na kibao kilichotamba cha 'Chongeni Fenicha Sio Maneno' ulioimbwa na Tego.
Aidha Tego, alisema kundi lao linaendelea kuzitambulisha nyimbo zao mpya na zile za albamu zao zilizopita katika maonyesho yao, ambapo kila Ijumaa huwa kwenye ukumbi wa Kiburugwa Inn, Mbagala na Jumamosi ufanya makamuzi yao Bashnet Hall, Mtoni Mtongani, jijini Dar es Salaam.

Mwisho

Katundu ana Nadhiri ya Mapenzi Msondo






MTUNZI na muimbaji mahiri wa bendi ya Msondo Ngoma 'Baba ya Muziki', Juma Katundu ameibuka na kibao kipya kiitwacho 'Nadhiri ya Mapenzi', ambacho kimekamilisha idadi ya nyimbo sita za albamu mpya ya bendi hiyo inayoandaliwa kwa sasa.
Akizungumza na MICHARAZO, Shaaban Dede 'Mzee wa Loliondo', alisema Msondo imeongeza nyimbo mbili mpya ambazo zinakamilisha idadi ya nyimbo za albamu yao ijayo, kikiwemo kibao chake kiitwacho 'Suluhu' na hicho cha Katundu ambacho kinaendelea kufanyiwa mazoezi.
Dede, alisema kibao chake kingine kinachokemea Dawa za Kulevya, nacho kipo tayari isipokuwa hana hakika kama kitakuwa kwenye albamu hiyo ijayo ya Msondo Ngoma, moja ya bendi kongwe ya muziki wa dansi nchini.
"Kwa kifupi ni kwamba Msondo imekamilisha nyimbo nyingine mbili mpya, moja ukiwa ni wangu uitwao 'Suluhu' na kingine kimetungwa na Juma Katundu, kinaitwa 'Nadhiri ya Mapenzi'," alisema.
Dede, aliyetua hivi karibuni katika bendi hiyo akitokea Mlimani Park 'Sikinde' alisema pamoja na kukamilika kwa nyimbo hizo sita za albamu yao ijayo, bado wanamuziki wa bendi hiyo wanaendelea kutunga vibao vingine vinavyoendelea kufanyiwa mazoezi ili vipigwe ukumbini.
"Wanamuziki tunaendelea kutunga nyimbo nyingine kwa ajili ya kudhihirisha kuwa Msondo ni Baba ya Muziki kutokana na kuundwa na wanamuziki wanaojua majukumu yao, vibao hivyo vitakuwa vikipigwa kwenye maonyesho yetu ya ndani na nje ya jijini la Dar," alisema Dede.
Msondo, iliyokuwa na desturi ya kufyatua albamu mpya kila mwaka, kwa mwaka uliopita ilishindwa kufanya hivyo kwa kile kilichoelezwa na meneja wake, Said Kibiriti, maelekezo ya wasambazaji wa kazi zao waliotaka watoe nafasi kwa albamu yao ya 'Huna Shukrani' ifanye vema sokoni.
Albamu zilizofuatana pamoja kwa miaka karibu 10 mfululizo ni 'Cheusi Mangala', 'Demokrasi ya Mapenzi', 'Ndoa Ndoana', 'Kilio cha Mtu Mzima', 'Piga Ua Talaka Utatoa', 'Kaza Moyo', 'Ajali', 'Kicheko kwa Jirani' na 'Huna Shukrani' inayoendelea kutamba iliyoachiwa mwaka juzi.

Mwalubadu: Kujituma kumenipa tuzo 2010







ANAFAHAMIKA zaidi kama 'Mwalubadu', ingawa jina lake halisi ni Athuman Mussa Masangula, mmoja wa wachekeshaji mahiri nchini ambaye kipaji chake kilianza kuonekana tangu akiwa darasa la nne katika Shule ya Msingi Mgulani, jijini Dar es Salaam.
Mwalubadu alisema alianza kushiriki maigizo shuleni kwa kuigiza sauti za walimu wake na baadhi ya viongozi maarufu, huku akishiriki pia katika uchezaji ngoma na michezo mbalimbali.
Alikiendeleza kipaji chake hata alipokuwa Shule ya Sekondari Mzalendo, iliyopo Moshi, Kilimanjaro ambapo alikuwa akikodishwa kwa ajili ya kunogesha sherehe mbalimbali za harusi na kipaimara na kuzidi kupata umaarufu zaidi hadi alipomaliza masomo yake na kurejea Dar.
Alijiendeleza kielimu kwa kusomea masomo ya IT ngazi ya cheti pale Chuo Kikuu Mlimani, kitengo cha Kompyuta, huku akijishughulisha na masuala ya sanaa kupitia kundi la Katavi lililowahi kutamba na michezo ya kuigiza kiup[itia kituo cha ITV.
Baadhi ya michezo aliyoshiriki akiwa na kundi hilo yaliyomtambulisha kwa mashabiki ni 'Jabali', 'Miale' na 'Tunduni' kabla ya kuangukia kwenye filamu akiigiza 'Copy' mwaka 2007 na kufuatiwa na nyingine zikiwemo za vichekesho zilizomjengea jina kubwa nchini.
Mwalubadu ambaye kwa sasa ni mtangazaji wa kituo cha Radio cha Ebony FM iliyopo, Iringa, alisema alijikuta akipenda sanaa ya uigizaji na hasa vichekesho kwa kuvutiwa na Steve Urkel, aliyetamba na 'Family Matters' na Brian Deacon, aliyeigiza filamu kadhaa ya Yesu.
Alisema kujibidiisha na kujifunza kwa waliomtangulia kwenye fani ndiko kulikomfanya anyakue tuzo ya Mchekeshaji Bora wa mwaka 2010, kupitia mtandao wa Filamu Central.
Mkali huyo anayependa kucheza soka, muziki na kuangalia filamu za vichekesho, alisema pamoja na mafanikio aliyoyapata kwenye fani hiyo, bado hajaridhika na anajibidiisha zaidi ili zweze kuwa msanii wa kimataifa, akimiliki kampuni yake mwenyewe sambamba na kujiendeleza kielimu.
Baadhi ya kazi za filamu alizoshiriki na kumjengea jina kubwa katika fani hiyo nchini ni pamoja na 'Sheria', 'Lango la Jiji', 'Inye' na 'Kaka Ben' za vichekesho, huku filamu za kawaida ni 'The Strangers', 'Swahiba', 'Solomba' na nyinginezo.
Mbali na kuchekesha, Mwalubadu pia ni mtunzi na mwandishi wa filamu hizo, moja ya kazi yake binafsi ni 'King Mwalubadu'.
Mkali huyo aliyezaliwa Januari 10, miaka kadhaa iliyopita akiwa mtoto wa tatu wa familia ya Mzee Mussa Masangula, alisema hakuna jambo la furaha kwake kama siku alipoanza kutangaza katika kituo cha Ebony Fm, huku tukio la huzuni ni kufiwa na baba yake mzazi, kitu alichodai akisahau.

Mwisho

Jahazi, Manchester Musica kuonyeshana kazi 'Usiku wa Naksh'

ONYESHO la 'Usiku wa Naksh Naksh wa Mwambao na Mastaa wa Muziki na Filamu', litakuwa ni pambano lisilo rasmi la kundi la Jahazi Modern Taarab na bendi ya Manchester Musica.
Kwa mujibu wa mraribu wa onyesho hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Hoteli ya Travertine, Abdallah Mensah, makundi hayo mawili yataonyeshana umwamba mbele ya mashabiki watakoenda kulishuhudia.
Mensah, alisema tayari makundi hayo yameshaanza kutoleana tambo juu ya kufunikana siku ya onyesho hilo, ambalo litahusisha mastaa wengine kibao wa muziki akiwemo Prince Mwinjuma Muumin, aliyepo Africana Stars 'Twanga Pepeta'.
"Japo ni onyesho la kutoa burudani kwa kushirikisha wasanii mbalimbali nyota wa muziki na filamu, lakini ni kama mpambano wa Jahazi Modern Taarab na Manchester Musica, moja ya bendi zinazokuja juu kwa sasa nchini kwenye muziki wa dansi," alisema Mensah.
Wengine watakaopamba onyesho hilo litakalofanyika Mei 8 ni pamoja na Malkia wa Mipasho nchini, Khadija Kopa, Mwanaidi Shaaban, Hassani Ally, Maua Tego, Thabit Abdul na kundi la Kanga Moja 'Ndembendembe.'
Pia wasanii wa kundi la TMK Wanaume Family, Said Fella, Said Chegge pamoja na wakali wa filamu ambao bado wameweka kapuni kwa sasa nao watajumuika pamoja kuwapa wakazi wa jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake burudani ya aina yake kwa wakati mmoja.
"Unaweza kuona mchanganyiko uliopo siku ya onyesho hilo, utakavyoweza kuwapa burudani zaidi ya moja kwa wakati mmoja, maana mbali ya taarab na dansi, pia wasanii mbalimbali wa filamu na muziki wa kizazi kipya watakuwepo kutoa burudani kabambe," alisema Mensah.
Mensah, alisema kwa sasa anahaha kusaka wadhamini wa onyesho hilo, ili kulizidishia manjonjo kabla ya kufanyika kwake.

Mwisho

Madee kudondosha nyingine



MSANII mahiri wa muziki wa kizazi kipya nchini, Hamad Ally 'Madee', anatarajia kuachia hewani ngoma nyingine mpya baada ya wiki mbili zilizopita 'kudondosha' audio na video ya kibao kipya cha 'Napeleka Benki'.
Ingawa Madee hakuweza kuweka bayana kibao kipi kitakachofuata baada ya 'Napeleka Benki', lakini alisema wiki ijayo ataachia kazi nyingine mpya wakati akiendelea na maandalizi ya kupakua albamu yake mpya na ya nne.
Kiongozi huyo wa kundi la Tip Top Connection, alisema moja kati ya nyimbo zake saba alizokamilisha itaachiwa kuzidi kuitambulisha albamu hiyo mpya itakayokuwa na nyimbo nane.
"Natarajia kuachia wimbo mwingine mpya baada ya 'Napeleka Benki', sijui itakuwa ipi kati ya 'Nisikilize', 'Siku ya Mwisho', 'Mtasubiri', 'Pendo', 'Hifla', 'Amka' au 'Siri Zote Ninazo Mimi'," alisema Madee.
Madee alisema nyimbo zote za albamu hiyo ya nne tangu alipoingia kwenye fani ya muziki zimerekodiwa katika studio mbili tofauti za MJ Production na Bongo Records chini ya watayarishaji Makochali, Master J na P Funk.
Ingawa bado hajaipa jina albamu yake ijayo iitwe vipi, lakini hiyo itakuwa ni albamu ya nne kwa Madee baada ya awali kutamba na 'Kazi ya Mola', 'Hip Hop Haiuzi' na 'Pesa'.Msanii huyo aliyesherehekea siku yake ya kuzaliwa mwanzoni mwa wiki hii, aliwahi kutangaza kutaka kustaafu muziki, ili apumzike na kujiendeleza kimasomo, lakini kwa ushauri wa watu wake wa karibu pamoja na mashabiki wa muziki aliamua kufuta wazo hilo lililokuwa alifanye mwaka juzi.

Ray kumbe ni 'Handsome wa Kijiji'

WAKATI filamu yake ya 'Second Wife' ikiendelea kutesa mitaani kwa sasa, msanii mkali wa filamu nchini, Vincent Kigosi 'Ray' amekamilisha kazi yake nyingine mpya iitwayo 'Handsome wa Kijiji', ambayo kwa mara ya kwanza ameigiza kama mtu dhalili aishie kijijini tofauti na alivyozoeleka.
Filamu hiyo iliyokamilika wiki iliyopita imerekodiwa maeneo ya Bagamoyo, mkoani Pwani, baada ya ushauri wa mashabiki wake waliodai wamechoshwa kila mara kumuoa akiigiza kama mtu tajiri anayeishia kifahari mjini, na hivyo kumlazimisha kutekeleza wazo hilo na kwenda 'bush'.
Kazi hiyo mpya ambayo imewashirikisha wakali kadhaa wa fani hiyo nchini kama Ben Blanco, Mzee Magali, Tash, Hashim Kambi, Irene Paul na wengine ipo kwenye uhariri tayari kupelekewa sokoni.
Katima ujumbe kwa mashabiki wake, Ray, amewataka amewataka wadau wa filamu kukaa mkao wa kula kushuhudia picha ya aina yake ambayo, ndani yake ameigiza kwa jina la Hamza.
"Wadau wa kiwanda cha filamu Tanzania napenda kuwafahamisha kuwa filamu yenu mpya ya kipekee na yenye manjonjo mengi sasa yakamilika," sehemu ya ujumbe wa Ray kupitia mtandao wake unasomeka hivyo.
Pia unaongeza; Nawashukuru sana kwa kuweza kufuatilia mchakato mzima wa sinema yenu ya Handsome wa Kijiji subirini sana wadau mzigo huu maana kampuni ya Rj Company imekuja tofauti kabisa na watu walivyozoea."
Filamu hiyo ni ya tatu kwa Ray ndani ya mwaka huu, baada ya awali kuachia 'Family Disaster' na kisha 'Second Wife' iliyopo sokoni kwa sasa ikiendelea kufanya vema kati ya kazi zilizotoka mwezi uliopita.

Cloud aibuka na Basilisa



MSANII nyota na mkongwe wa fani ya uigizaji nchini, Issa Mussa 'Cloud' ameibuka na kazi mpya iitwayo 'Basilisa', akitamba kuwa ni moja ya kazi itakayoziba midomo wote wanaoziponda filamu za Kitanzania.
Cloud, aliyeanza kufahamika kupitia michezo ya kuigiza iliyokuwa ikirushwa na kituo cha ITV alipokuwa na kundi la Splended, alisema filamu hiyo iliyowashirikisha wasanii kadhaa nyota nchini imeshakamilika na kwa sasa ipo foleni kabla ya kuanza kuwa mitaani.
Filamu hiyo ambayo Cloud kaigiza katika nafasi tatu tofauti imekuja wiki kadhaa tangu mkali huyo kutamba na kazi kama Ukiwa, Pigo na Suria.
Cloud alisema ndani ya filamu hiyo amefanya mambo makubwa akishirikiana na wakali wenzake kama Adam Kuambiana, Wema Sepetu, Single Mtambalike 'Richie', Ummy Weslaunce 'Dokii', Suleiman Said 'Barafu', Kajala Masanja na wengineo.
"Sitaki kujisifu, lakini naamini Basilisa ni moja ya kazi makini itakayoleta mapinduzi katika sanaa ya filamu nchini, hii inatokana na vichwa vilivyoshirikishwa ndani yake na jinsi kazi yenyewe ilivyo na ubora wake kuanzia hadithi, upigaji picha, mandhari na mengineyo," alisema Cloud.
Alisema kitu cha muhimu ni mashabiki wa filamu kukaa mkao wa kula kuishuhudia kazi hiyo mpya itakayosambazwa na kampuni ya Steps Entertainment ambayo ilivutiwa na filamu hiyo.
"Kazi yangu inatarajiwa kusambazwa na Steps na itakuwa mitaani kabla ya mwisho wa mwezi huu, hivyo wadau wa filamu wakae mkao wa kula kupata kitu roho inapenda," alisema Cloud.
Ndani ya filamu hiyo, Cloud, ameshiriki baadhi ya vipande akiwa kama kichaa, jitu la kutisha na muonekano wake wa kawaida, huku simulizi kuu la kazi hiyo mpya ni kuiasa jamii juu ya kutodharau viumbe wengine kwa jinsi ya muonekano wao.

Tshimanga Kalala Assosa: Mkongwe wa muziki asiyechuja *Ajitosa kwenye utuzi wa vitabu







SI kila wakati mipango yetu inaweza kutimia kama yalivo matarajio. Unaweza kupanga kufanya jambo fulani lakini lisitimie, na badala yake likaja lingine ambalo hukulipanga, lakini likawa na faida pengine kuliko hata lile la awali.
Hivi ndivyo ilivyotokea kwa msanii wa muziki Tshimanga Kalala Assosa, ambaye hakuwahi kufikiria katika maisha yake kama ingetokea siku akawa mwanamuziki.
Malezi kutoka kwa wazazi wake wakati akiwa mdogo, yalimpa mwanga wa siku moja kuja kuwa mtumishi wa kiroho-padri.
Lakini baba yake aliyemlea kwa kipindi chote akiwa mdogo, naye alikuwa na mtazamo tofauti juu nini atakachokuja kukifanya mwanae.
Yeye (mzazi) alipenda sana mtoto wake aje kuwa daktari wa binadamu, lakini kumbe yote hayo hakuna lililotimia. Assosa ametua kwenye sanaa ya muziki.
Assosa ni mmoja wa wakongwe wa muziki wa dansi aliyeng'ara barani Afrika kupitia bendi kadhaa za Kongo (zamani Zaire) kama Negro Succes, Lipualipua, Fukafuka na Marquis du Zaire.
"Nilipokuwa mdogo mjini Kamana, Jimbo la Katanga, nilifanya kazi kanisani na kutamani kuwa Padri, wakati baba mzazi yeye alitaka nisome zaidi ili niwe daktari," alisema.
Assosa, maarufu kama 'Mtoto Mzuri', alisema alivutwa kwenye muziki kwa nyimbo za wakali wa zamani wa Kongo kama Franco, Vicky Longomba na Kabasela Joseph.
Ladha na utamu wa muziki wao ulimfanya asitishe mipango ya kusomea zaidi taaluma na kujiingiza kwenye elimu ya muziki akiwa darasa la 5.
Alianza kuimba kanisani, shuleni na baadaye mitaani akipigia bendi ndogo ndogo za mjini Kamana, kabla ya kuhamia Kinshasa katikati ya 1960 alipokutana na Bavon Marie Marie aliyemchukua katika bendi yake ya Negro Succes.
"Nilipata taabu sana kupata mafanikio ndani ya Negro Success kwa vile sikujua vema lugha ya Lingala. Nashukuru Bavon aliyenisaidia mpaka alipofariki kwa ajali ya gari mwaka 1970, na mimi kuhamia Lipualipua nikiwa na Nyboma Mwandido," alisema.
Makundi mengine aliyopitia mkali huyo aliyejitosa kwenye Uandishi wa Vitabu kwa sasa, akiwa ameachia kitabu kiitwacho 'Jifunze Lingala', ni Le Kamalee, Fukafuka, Marquiz du Zaire kabla ya kuja nchini na kupigia bendi mbalimbali.
Baadhi ya bendi alizopigia nchini ni DDC Mlimani Park, Makassy Band, Mambo Bado, Marquiz Original, Legho Stars kabla ya kuanzisha bendi ya Bana Marquiz inayotamba hadi sasa jijini Dar es Salaam.
Assosa alisema japo anasikitika kushindwa kuwa Padri, bado anashukuru fani ya muziki imemsaidia kwa mengi, ikiwemo kumudu maisha, akisomesha watoto na kuitunza familia yake, mbali na kufahamika na kumiliki mali ambazo hakupendwa zitajwe.
"Sio siri muziki umenisaidia kwa mengi na siwezi kuacha mpaka mwisho wa maisha yangu. Nimejikita kwenye uandishi wa vitabu, lakini haina maana ndio mwisho wangu wa muziki."
Mkali huyo, alizaliwa miaka 60 iliyopita akiwa mtoto wa pili kati ya nane, ameoana na Evangeline Paul Kimiti na kupata naye watoto.
Mkali huyo, alisema ameingia kwenye uandishi wa vitabu baada ya kuona Watanzania wengi wanapenda kujifunza Kilingala kwa kuzipenda nyimbo za Kongo.
"Nimeanza na 'Jifunze Lingala' ili kukidhi maombi ya mashabiki wa nyimbo za Lingala waliotaka tafsiri ya mashairi yake, ila nipo mbioni kutoa vingine ili niwasaidie wale wanaotaka kujifunza lugha hiyo," aliongeza.
Assosa anayependa kula Ugali kwa Kisamvu na Uyoga, aliwahi kucheza soka kama kiungo alipokuwa St Luhanga Seminary.
Assosa ni shabiki wa Manchester United, na mpenzi mkubwa wa mavazi ya rangi nyeupe na nyeusi. Hatumii kilevi.
Assosa, aliyetikisa Afrika na vibao kama Masua, Abisina, alichokitunga na kuimba na Nyboma, kabla ya mwenzake kumuomba akimiliki, alisema tukio la furaha kwake ni siku alipoanza kuwa na familia, huku akihuzunishwa na vifo vya wanamuziki wenzake.
Mtunzi na muimbaji huyo, alisema licha ya kutunga vibao vingi, kibao cha Bomoa Tutajenga Kesho alichotunga akiwa Mambo Bado, ndicho anachokikumbuka zaidi kwa jinsi kilivyomtia misukosuko na serikali ya awamu ya kwanza miaka ya 1980.
Assosa alisema japo alitunga kibao hicho bila ya maana yoyote zaidi ya kutoa burudani mashabiki wao, ulitafsiriwa vibaya na serikali ya Julius Nyerere kiasi cha kufikia kupigwa marufuku kwa kuonekana unachochea 'ufisadi'.
Kibao hicho alichotunga mwaka 1983, kina mistari isemayo 'Bomoa ee Bomoa ee Bomoa aa mamaa tutajenga kesho ooh i maee Oo Beti mayaiee ooh maax2'
Assosa, alisema kama angekutana na Rais angemuomba awe mkali kwa wanaoichezea amani na kutaka kuleta vurugu nchini.
"Rais awe mkali kwa wanaoichezea amani na utulivu wa nchi, machafuko na vita ni mambo mabaya, wanaovishabikia hawajui madhara yake," alisema.
Assosa aliyeitungia DDC Mlimani Park kibao cha 'Gama Nihurumie', alisema muziki wa Tanzania hautambi kama zamani kwa sababu ya uvivu wa wasanii wa sasa na bendi zote kupiga muziki unaofanana wakiiga toka Kongo.
"Zamani ilikuwa rahisi kujua miondoko ya Msondo, Sikinde, Marquiz au OSS, kwa vile zilikuwa zikipiga mirindimo yao, kwa sasa bendi zote zinapiga muziki wa aina moja wakiiga nje, ndio maana muziki wetu hautambi kimataifa," alisema.
Alisema jambo hilo lipo hata Kongo, kwa JB Mpiana, Koffi Olomide, Werrason, Ferre Gora na Fally Ipupa kutojitofautisha kama ilivyokuwa kwa akina Tabu Ley au Franco na African Jazz waliowapagawisha wazungu.

Mwisho

BOB JUNIOR AMCHAMBUA DIAMOND



MWIMBAJI na mtayarishaji wa muziki wa Bongo Fleva kutoka kundi la ‘Masharobaro’, Bob Junior ‘Rais wa Masharobaro amesema kuwa sababu ya msanii, Nasib Abdul ‘Diamond’ kukosa tuzo mwaka huu inasababishwa na kujikweza kwake.
Alisema Dimond baada ya kupata tuzo tatu mwaka jana amekuwa anajisikia na kujiona huku akitafuta wanawake wenye sifa mbaya ili aweze kuandikwa.
Bob Junior ambaye ndiye alitayarisha albamu ya msanii huyo ya kwanza alisema kuwa sifa zinamfanya msanii huyo kushindwa kufanikiwa katika tuzo za mwaka huu.
“Msanii huyo amekuwa akinitafuta hata mimi na kufikia kunilalamikia kuwa namuongezea fedha za kutengenezea nyimbo, kitu ambacho ni maamuzi ya kiofisi.
Alisema kuwa ukiachilia suala la kuchukua jina lake la Rais wa wasafi akibadilisha jina lake la rais wa masharobaro ambalo lina maana hiyo kwa sasa amekusanya genge kwa nia ya kumfanyia kitu kibaya, hali iliyomfanya atoe taarifa kituo cha polisi
http://mamapipiro.blogspot.com/

Saturday, March 12, 2011

Kanumba atambia 'The Shock'



MUIGIZAJI Nyota wa Filamu Tanzania, Steven Kanumba, ametamba kuwa kazi yake mpya ya 'The Shock' ambayo ipo kwenye foleni kabla ya kuachiwa mitaani ni 'funika bovu' ya mwaka 2011.
Kanumba, mshindi wa tuzo ya Muigizaji Bora wa Kiume 2010, alisema filamu hiyo iliyoandaliwa na kampuni yake ya Kanumba The Great Films ni moja ya kazi itakayokimbiza kwenye soko la filamu kutokana na namna iliyoandaliwa pamoja na washiriki wake walivyofanya kweli.
Akizungumza na Micharazo, Kanumba, alisema sio kawaida yake kujisifu, ila kazi hiyo ni moja ya kazi nzuri iliyouanza mwaka 2011.
Alisema wakati kazi hiyo ambayo inamuibua muigizaji mpya wa kike nchini Shez Sadry, ikiwa kwenye foleni kabla ya kuingia mitaani, kampuni yake inaendelea na maandalizi ya kazi nyingine.
"Sio siri kama kuna kazi itakayokimbiza mwaka huu, basi ni The Shock, kutokana na jinsi nilivyoiandaa na namna washiriki walivyofanya kazi ya ziada kudhihirisha kuwa fani yetu inazidi kupaa nchini," alisema.
Washiriki wengine waliopo ndani ya filamu hiyo ni mwanamuziki mahiri wa bendi ya FM Academia, Patcho Mwamba na wengine wengi.
Katika hatua nyingine, kampuni ya kusambaza filamu ya Kapico, imeamua kuibeba filamu mpya ya kusisimua ya Bangkok Deal inayohusisha majoka makubwa kama ilivyokuwa 'Anaconda'.
Filamu hiyo iliyoandaliwa na kampuni ya Huba Production, imewashirikisha wasanii wakali kama Charles Magali, Bambucha na wengine, wakati wowote itakuwa hewani kupitia Kapico moja ya wasambazaji wakubwa wa filamua za Kibongo nchini.
Mwisho

Sikinde wavamia ngome ya Msondo

BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Sikinde' imevamia ngome ya wapinzani wao, Msondo Ngoma kwa kuanzisha bonanza linalofanyika kila Jumapili kwenye ukumbi wa TCC Club-Chang'ombe.
Msondo kwa muda mrefu imekuwa ikifanya bonanza kila Jumamosi kwenye klabu hiyo, hivyo kutua kwa Sikinde ni kama kuwachokoza ikiwa ni wiki kadhaa tangu pambano lao kuahirishwa.
Katibu wa bendi ya Sikinde, Hamis Milambo, alisema bendi yao imelianza bonanza hilo tangu wiki iliyopita kwa kutumbuiza kuanzia saa 8 mchana hadi saa 12 kabla ya kumalizia burudani zao kwenye ukumbi wa SUWATA.
Milambo, alisema hilo ni bonanza la pili kwa bendi yao, baada ya kufanya pia bonanza jingine linalifahamika kama Konyagi Bonanza kila Jumamosi kwenye ukumbi wa DDC Kariakoo.
"Tangu wiki iliyopita tumekuwa tukifanya bonanza jipya kwenye ukumbi wa TCC Chang'ombe majira ya saa 8-12 kisha kuendelea na ratiba yetu pale SUWATA kuanzia saa 1-5 usiku," alisema.
Aliongeza kwa leo bendi yao itakamua kwenye bonanza lao la Konyagi ikitambulisha nyimbo zao mpya na zile za zamani zilizoifanya bendi hiyo kuwa Mabingwa wa Muziki Tanzania.
Baadhi ya nyimbo mpya za bendi hiyo ni Tunu ya Huba, Wanawake Wakiwezeshwa, Urithi, sambamba na zile za albamu yao ya Supu Imetiwa Nazi.
Mwisho

Filamu ya ngumi hadharani leo



FILAMU mpya inayozungumzia maisha ya bondia wa zamani na kocha wa sasa wa klabu ya Ashanti, Rajabu Mhamila 'Super D' iitwayo 'Super D:Boxing Coach', inatarajiwa kutolewa rasmi leo.
Filamu hiyo ambayo inahusisha pia mapambano kadhaa ya mabondia nyota duniani, itatolewa rasmi leo katika sherehe maalum itakayofanyika kwenye klabu ya ngumi ya Ashanti inayoadhimisha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.
Akizungumza na micharazao, Super D, aliyewahi kuzichezea klabu za Simba, Reli na Amana na kupigana na mabondia kama Mbwana Ally na wengineo, alisema filamu hiyo ni maalum kwa ajili ya kuhamasisha mchezo wa ngumi ambao umeshuka kiwango kwa sasa.
"Pamoja na kusimulia na kuonyesha michezo yangu tangu wakati nikipigana mwaka 1984, pia kuna mapambano ya wakali wa dunia katika mchezo wa ngumi za kulipwa," alisema Super D.
Super D, alisema filamu hiyo itazinduliwa leo na kuachiwa hadharani ili mashabiki wa ngumi na filamu kwa ujumla kuipata na kwenda kuishuhudia uhondo wake.
Aliyataja mapambano yaliyopo ndani ya filamu hiyo kuwa ni, ya Muhammad Ally, Iron Mike Tyson, Manu Pacquiao, Michael Moore, Llyod Mayweather, Oscar de La Hoya na wengineo.
"Kazi yangu itakuwa mitaani kuanzia Machi 12, wakati tukiadhimisha mwaka mmoja tangu Ashanti Boxing ianzishwe mie nikiwa miongoni mwa makocha wake," alisema.
Hiyo itakuwa ni filamu ya pili inayozungumzia mabondia wa zamani na mafunzo ya ngumi, awali bingwa wa dunia, Francis Cheka 'SMG' akifanya hivyo mwaka juzi kwa kutoa filamu kama hiyo ikiwa na jina na Francis Cheka na Historia Yake.

Talent wasubiri kidogo videoni



BENDI ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea' imekamilisha kurekodi video ya nyimbo za albamu yao mpya ya 'Subiri Kidogo', huku ikiendelea kuandaa albamu ya pili.
Mkurugenzi wa bendi hiyo, Husseni Jumbe, alisema video ya albamu hiyo imekamilika mapema wiki hii na kwa sasa inafanyiwa uhariri kabla ya kusambazwa sokoni na kwenye vituo vya runinga.
Jumbe, alisema video ya albamu hiyo yenye nyimbo sita imetayarishwa na kampuni moja ya jijini na ina mandhari ya kuvutia ikirekodiwa kwa kiwango cha hali ya juu.
"Tumekamilisha kuiweka kwenye video albamu yetu mpya ya Subiri Kidogo, kwa sasa inahaririwa kabla ya kuanza kusambazwa ili mashabiki wetu wapate uhondo," alisema Jumbe.
Alizitaja nyimbo zilizorekodiwa kwenye video hiyo ni 'Subiri Kidogo', 'Dillema', 'Nyuma ya Pazia', 'Songombingo' na 'Nimeamua Kunyamaza'.
Jumbe alisema video hiyo ikikamilika, tayari bendi yake yenye wanamuziki 10, imeshaanza kuandaa albamu mpya ijayo.
Alisema nyimbo nne kati ya sita za albamu hiyo zimeshakamilika na kuanza kutambulishwa kwenye maonyesho yao ambazo ni pamoja na 'Shoka la Bucha', 'Jipu la Moyo' na 'Kilio cha Swahiba' ambao awali ulipangwa kuwepo kwenye albamu yao ya kwanza.
"Kibao cha Kilio cha Swahiba tuliamua kukiweka kwa ajili ya albamu hii ya pili, ambayo tayari ina nyimbo zingine tatu," alisema Jumbe.
Jumbe, alisema kabla ya Juni, albamu hiyo aliyopanga kuiitwa kwa jina la Shoka la Bucha huenda ikakamilika rasmi.

Riyama Ally: Kisura mkali anayewagusa wengi







AKIIGIZA mwenye majonzi utamuonea huruma kwa jinsi atakavyolia kwa kumwaga machozi kama yupo msibani, akicheza kama mwendawazimu utamsikitikia kwa jinsi atakavyokuwa akila jalalani na kufanya vituko vyote wafanyavyo watu wenye kuugua kichaa.
Wengi hudhani yale anayoyafanya kwenye filamu ni mambo ya kweli kutokana na kucheza uhalisia asilimia 100, kitu kinachomfanya Riyama Ally kuwa mvuto wa pekee katika filamu anazoziigiza.
Mwanadada huyo mmoja wa waigizaji wa kike wakali nchini,alianza kufahamika mwishoni mwa miaka ya 1990 alipokuwa na kundi la Taswira na hasa igizo la Jabari lililokuwa likionyeshwa kwenye kituo cha ITV mwaka 2000.Katika igizo hilo lililokuwa gumzo nchini miaka hiyo, Riyama aliigiza kama mtoto aliyegeuzwa kichaa na mama yake mzazi aliyekosea masharti ya dawa za mganga ili kumdhibiti mumewe, ndilo lilothibitisha kuwa kisura huyo ni mkali.
Miaka mitatu baadae, yaani mwaka 2003 Riyama aliachana na Taswira na kutua kundi la Tamba Art, lililowahi kutamba na filamu kama Nsyuka na kuzidi kuonyesha makali yake.
Akiwa na kundi hilo linalomilikiwa na mganga maarufu wa tiba asilia, Dk Maneno Tamba, Riyama, alishiriki filamu mbalimbali zilizozidi kumjengea jina kutokana na staili yake ya uigizaji kama anayefanya kweli.
Baadhi ya filamu alizofyatua akiwa na kundi hilo ni pamoja na 'Miwani ya Maisha', 'Mzee wa Busara', Fungu la Kukosa na nyinginezo kabla ya kupata bahati ya kushiriki kazi nyingine nje ya kundi hilo.
Filamu kama 'My Darling','Simu ya Kifo', 'Darkness Night', 'Mwana Pango', 'Kolelo','Segito', Fake Promise na nyinginezo ni baadhi ya kazi hizo za nje zilizompaisha mrembo huyo mwenye asili ya mkoa wa Tanga.
Akiwa mmoja wa waigizaji wa kike wanaojiheshimu akiwa hana kashfa yoyote kama mastaa wengine wa aina yake, Riyama mbali na uigizaji, pia ni mtunzi wa filamu na mtayarishaji moja ya kazi yake binafsi ikiwa ni Mwasu iliyofanya vema sokoni kwa kitambo kirefu.
Riyama, mshindi wa tuzo ya Uigizaji Bora ya Risasi 2005-2006, kwa sasa yupo mbioni kuibuka na filamu mpya ya Second Wife, aliyoigiza na Vincent Kigosi 'Ray', Aisha Bui, Colleta Raymond na wengine.
Filamu hiyo inatarajiwa kuachiwa hadharani keshokutwa, ambapo kama kawaida yake, Riyama 'chozi' linamtoka kutokana na kutendwa sivyo ndivyo na 'mumewe' ndani ya filamu hiyo.
Riyama anayependa kusafiri, kupika na kulala anapokuwa nje ya fani yake ya uigizaji, ni shabiki mkubwa wa muziki wa taarab, kundi la Mambo Jambo na pia kusoma vitabu mbalimbali.

Mwisho

Benita: Kimwana aliyekacha 'utawa' aigize







TAMTHILIA ya 'Beyond Our Dreams'iliyokuwa ikirushwa kupitia kituo cha runinga cha NTA miaka ya katikati ya 1996 ndiyo iliyomtangaza Benita Nzeribe, mmoja wa waigizaji nyota wa Nigeria.
Mwaka 1998 alijitumbukiza kwenye fani ya uchezaji filamu na kazi mbili za awali za 'Notorious Virgin' na 'Gold Diggers' zilizomtangaza vema kwenye ulingwengu wa fani hiyo.
Filamu hizo ilitoka mwaka 1999-2000 na tangu hapo ameshiriki kazi mbalimbali zilizomjengea jina katika ukanda wa Nollywood na kufahamika kimataifa.
Mzaliwa huyo wa Jimbo la Anambra aliyewahi kunusurika kufa kwenye ajali ya gari, alisema pamoja na kipaji cha sanaa kuwa cha kuzaliwa, lakini kuvutiwa kwake na waigizaji Liz Benson wa Nigeria, Angeline Jolie na Cameroon Diaz wa Marekani ndiko kulikomtumbukiza huko.
Alisema, hata alipojiunga na Chuo Kikuu cha Abia, lengo lake lilikuwa kusomea masomo ya sanaa, lakini chuo hicho hakikuwa na kozi hizo na hivyo kuchukua masomo ya Lugha ya Kiingereza aliyohitimu kabla ya kuanza kuuza sura kwenye runinga.
Aliongeza kuwa bahati nzuri ni kwamba alipoanza kuigiza wazazi wake hawakumuangusha, ingawa baadhi ya wahitimu wenzake walimshangaa kwa kuichagua kazi hiyo ya uigizaji.
Benita, mtoto wa tatu kati ya wanne wa mfanyabiashara maarufu Mr Nzeribe na mama muuguzi mstaafu, tangu alipoanza kushiriki uigizaji wa filamu amecheza zaidi ya kazi 100 kati ya hizo akishirikiana na wakali kama mkongwe Olu Jacobs, Ejike Asiegbu, Ken Okonkwo, Fred Amata, Juliet Ibe na wengineo.
Moja ya filamu anayojivunia ni ile ya Peace of Mind, aliyocheza kama mke anayenyanyaswa na kupigwa na mumewe, kitu alichodai kimewahi kumtokea katika maisha yake ya kimapenzi.
Mwanadada huyo, ambaye pia ni mwanamitindo na mpambaji, majina yake kamili ni Benita Nnenna Adaeze Nzeribe, aliyezaliwa Uzoakwa, Ihiala, Jimbo la Anambra, elimu yake ya msingi na sekondari aliisoma katika miji ya Aba na Umuahia.
Pia alipitia mafunzo ya kiroho akiwa na lengfo la kuja kuwa mtawa, kabla ya kufuta wazo hilo na kati ya vitu anavyokumbuka katika makuzi yake ni tukio la baba yake kumnunulia gari lake la kwanza akiwa na miaka 14 tu.
"Tukio hili la baba kuninunulia gari nikiwa na miaka 14 siwezi kulisahau maishani mwangu kwani lililonyesha alivyonijali na kunithamini," alinukuliwa.
Kuhusu uigizaji wake wa filamu za kimapenzi, alisema ni jambo la kawaida kulingana na nafasia anayopangiwa na muongozaji wake, ila ni mtu anayejiheshimu na kuithamini kazi yake.
Alipoulizwa kama yupo tayari kuchojoa ili aigize utupu, Benita alisema katu hawezi kufanya upuuzi huo hata kwa kisi gani cha fedha hasa kutokana na hadhi ya familia yake nchini kwao.
Baadhi ya kazi alizoshiriki kisura huyo, mbali na zile zilizomtambulisha Nollywood ni Cross My Heart, Cross & Tinapa,Endless Madness,Tears of a Saint, Treasure Hunt,Breath Again,Buried Emotion,Enemies in Love, Games Men Play, Girls Cot,King of the Town na Life Abroad.
Pia ameshiriki Peace Talk, The Final Days, Christian Girls, Fools in Love, Hold Me Down, Paradise to Hell, Secret Affairs, The Scorpion, Under Arrest, Beyond Reason, My Desire,Stand by Me, A Night to Remember, Arrows, Great Change, Lagos Babes, Mission to Africa, Saved by Grace, Street Life, The One I Trust, Agony of a Mother, Fire on the Mountain na kadhalika.

Tuesday, March 8, 2011

Msamba 'ajitoa' Villa Squad *Ni baada ya kuirejesha Ligi Kuu

KOCHA aliyeipandisha daraja klabu ya Villa Squad hadi Ligi Kuu Tanzania Bara, Abdallah Msamba, ametangaza 'kuitema' timu hiyo akiutaka uongozi usake kocha mwingine wa kuiongoza kwenye ligi hiyo msimu wa 2011-2012.
Akizungumza na Micharazo, Msamba, alisema baada ya kutimiza jukumu la kuirejesha Ligi Kuu, Villa Squad anaona ni vema kupisha kocha mwingine wa kuendelea kuinoa timu hiyo katika ligi hiyo msimu ujao.
Msamba, alisema kujiondoa kwake kuinoa timu hiyo haina maana kuwa kajitoa kabisa Villa Squad, ila alisema kwa hadhi ya ligi ilivyo inapaswa timu iwe na mtu mwingine kukabiliana na mshikemshike wake.
"Nimeashautaarifu uongozi utafute kocha mwingine wa kuiandaa timu kwa ligi kuu ijayo, mie naishia hapa baada ya kuipandisha daraja, ila nitakuwa kocha msaidizi au mshauri kwa lengo la kuona Villa inafanya vema," alisema.
Winga huyo wa zamani wa Sigara, Simba na Kajumulo World Soccer, alisema ili kuweza kufanya vema kwenye ligi hiyo, Villa inahitaji kufanya marekebisho kidogo katika kikosi chake, chini ya kocha mwenye hadhi stahiki.
Alisema ana imani kama marekebisho hayo yatafanyika mapema na timu kuandaliwa mapema ikipata michezo mingi ya kujipima nguvu inaweza kutisha katika ligi hiyo iliyowahi kuicheza kabla ya kushuka msimu wa 2008-2009.
Villa Squad ni miongoni mwa timu nne zilizopanda Ligi Kuu msimu ujao baada ya kufanya vema kwenye Ligi Daraja la Kwanza iliyochezwa mjini Tanga.
Timu zingine zilizoungana na klabu hiyo yenye maskani yake Magomeni Mapipa ni JKT Oljoro waliokuwa mabingwa wa ligi hiyo ya daraja la kwanza, Coasta Union na Moro United zinazorejea tena kwenye Ligi Kuu ya Tanzania.

Mwisho

Mtambo wa Gongo, kuzigonga na Cobra Machi 12

BONDIA mkongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo' anatarajiwa kuvaana na Robert Mrossy 'Cobra' katika pambano la Middleweight, litakalofanyika Machi 20 mwaka huu.
Osward mwenye miaka 41 atapigana na Cobra katika pambano lililoandaliwa na Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO, Yassin Abdalla 'Ustaadh' litafanyika kwenye ukumbi wa Amana Club, Ilala jijini Dar.
Ustaadh aliiambia Micharazo kuwa, pambano hilo lisilo la ubingwa la raundi 12 ni maalum kwa ajili ya kupima viwango vya mabondia husika, pia kutoa fursa kwa mabondia wa mikoani kujitangaza kwenye mchezo huo.
Rais huyo wa TPBO, alisema Cobra ni bondia kutoka Arusha na hivyo kupata fursa ya kupigana na mkongwe Osward, kutampa nafasi ya kujitangaza katiuka mchezo huo.
Ustaadh alisema awali pambano hilo lilipangwa kufanyika Jumapili ijayo, ila kutokana na kuahirishwa kwa lingine la ngumi hizo za kulipwa kati ya Ashraf Suleiman na Awadh Tamim kutoka Machi 5 hadi Machi 12 imewafanya walisogeze mbele hadi Machi 20.
"Tumeona isingekuwa vema pambano letu lifanyika kama tulivyopanga Machi 13, wakati siku moja kungekuwa na pigano jingine la Ashraf na Tamim ambalo awali lilipangwa kufanyika Machi 5, lakini likasogezwa hadi Machi 12," alisema Rais huyo wa TPBO.

Kaseba, Maugo kutambulishwa rasmi leo

MABONDIA Mada Maugo na Japhet Kaseba wanaotarajiwa kupigana Aprili 16, pamoja na watakaowasindikiza pambano hilo wanatarajiwa kutambulishwa rasmi leo mbele ya waandishi wa habari.
Mratibu wa pambano hilo, Kaike Siraju aliiambia Micharazo jana kuwa leo watafanya mkutano na vyombo vya habari kulitambulisha rasmi pambano hilo ambalo litafanyika kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam.
"Nitawatambulisha rasmi mabondia wote watakaopigana Aprili 16 katika mkutano na vyombo vya habari utakaofanyika kesho (leo) kwenye ukumbi wa Habari-Maelezo majira ya saa 5," alisema Siraju.
Alisema katika mkutano huo, Maugo na Kaseba kila mmoja atapata fursa ya kuongea machache kuhusiana na pambano lao hilo la raundi nane uzito wa kilo 72 litakalokuwa la kusaka mkali baina yao wa kuzipiga na Francis Cheka.
Ingawa Siraju amekuwa akificha majina ya mabondia watakaoshindikiza pambano hilo, lakini uchunguzi wa Micharazo umebaini kuwa nahodha wa zamani wa timu ya taifa ya ngumi ya ridhaa, Joseph Martin ni miongoni mwao.
Martin aliyeachana na ngumi za ridhaa na kuingia za kulipwa atapigana na Sweet Kalulu, pia Francis Miyeyusho na Afande Juma nao watakuwepo katika usindikizaji.
Kwa mujibu wa Siraju, mgeni rasmi wa pambano hilo anatarajiwa kuwa Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova ambaye atamualika IGP Said Mwema kuhudhuria kwenye ngumi hizo.