STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, April 19, 2012

TIBAIGANA AICHINJA YANGA



Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) iliyokutana jana (Aprili 17 mwaka huu) imetupa rufani ya Yanga iliyowasilishwa mbele yake kupinga uamuzi wa kupokwa pointi tatu kwa kumchezesha mchezaji asiyestahili.
Aprili 2 mwaka huu Kamati ya Ligi ya TFF iliipa Coastal Union ushindi wa pointi tatu na mabao matatu baada ya Yanga kumchezesha beki Nadir Haroub ‘Cannavaro’ kwenye mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya timu hizo iliyofanyika Machi 31 mwaka huu wakati akiwa na adhabu ya kukosa mechi tatu.
Yanga katika rufani hiyo iliwasilisha sababu nane za kupinga kupokwa pointi hizo, kubwa zikiwa Cannavaro hakustahili kutumikia adhabu ya kukosa mechi tatu, si aliyempiga refa Israel Nkongo, ripoti za refa na kamishna wa mechi yao dhidi ya Azam zilionesha dalili ya njama (conspiracy) kwani zilifanana.
Pia Cannavaro alikuwa miongoni mwa wachezaji ambao adhabu zao zilisimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu, Kamishna mstaafu wa Polisi, Alfred Tibaigana.
Katika uamuzi wake, Kamati imesema adhabu ya Cannavaro ya kukosa mechi tatu kwa mujibu wa Kanuni ya 25(c) ya Ligi Kuu ya Vodacom ilitolewa na refa na si Kamati ya Ligi kama ambavyo inalalamikiwa na Yanga, na kanuni hiyo haikatiwi rufani.
Pia barua ambayo TFF iliiandikia Yanga kuhusu adhabu ya mchezaji huyo ilikuwa wazi kwani ilikariri kanuni ya 25(c), hivyo kitendo cha klabu hiyo kumtumia mchezaji huyo ulikuwa ni uzembe wa kutoheshimu kanuni. Kama Yanga haikufahamu vizuri kanuni hiyo ilikuwa na fursa ya kuiandikia TFF kwa mujibu wa Kanuni ya 25(f) ili kupata ufafanuzi kabla ya kuamua kumtumia mchezaji huyo.
Vilevile adhabu zilizokuwa zimesimamishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu ni zile ambazo zilikuwa zimetolewa na Kamati ya Ligi, na si zile zilizotolewa uwanjani na refa.
Kuhusu madai ya conspiracy kwa ripoti za kamishna wa mchezo huo na refa, Kamati imebaini kuwa hazifanani, na suala lililokuwa likibishaniwa (contentious issue) lilikuwa ni kunyang’anywa pointi tatu.
Pia Kamati ilikariri Ibara ya 50 ya Kanuni za Nidhamu za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kuwa mchezaji anayembughudhi refa kwa njia yoyote ile anastahili kufungiwa kwa angalau mechi sita.

Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

Saturday, April 7, 2012

MAMIA WAFURIKA MSIBA WA STEVEN KANUMBA





MEYA wa Manispaa ya Kinondoni na Ilala, Yusuf Mwenda na Jerry Slaa ni miongoni
mwa viongozi waliojitokeza kwenye msiba wa nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba aliyefariki juzi usiku nyumbani kwake baada ya kuanguka katika mzozo na mpenzi wake.
Aidha umati mkubwa ulijitokeza kwenye msiba wa msanii huu uliopo nyumbani kwake
Sinza Vatican, jana ulisababisha msongamano mkubwa kiasi cha kuziba barabara ya
Makanya na kuwalazimisha askari polisi kufanya kazi ya ziada kuweka mambo sawa.
MiCHARAZO lililokuwepo msibani hapo, liliwashuhudia mameya hao na viongozi wengine kama Katibu wa Kamati ya Uchumi na Fedha CCM-Taifa, Mwigulu Nchemba na Diwani wa Kata ya Sinza, Renatus Pamba wakiwa na nyuso za huzuni wakitoa pole zao.
Viongozi hao kila mmoja alikuwa akiwapa pole wasanii waliofanya kazi na Kanumba
pamoja na watu wengine kabla ya baadhi yao kuondoka na kuwaacha mamia ya watu
wakiwemo wasanii nyota wa filamu wakiendelea na msiba huo.
Kutokana na wingi wa watu waliojitokeza kwenye msiba huo, iliwalazimisha waratibu wa msiba huo, kuwahamishi waombelezaji hao kwenye ukumbi wa Vatican Hoteli, huku wakiwazuia wengine kuingia ndani na kuleta tafrani za hapa na pale.
Mratibu wa Bongo Movie, Steven Mengele 'Steve Nyerere' alisema waliamua kuhamishia watu hotelini hapo kutokana eneo la nyumba ya marehemu Kanumba kutotosha kwa wingi wa waombolezaji waliojitokeza waliosababisha msongamano mkubwa.
Msongamano huo wa waombelezaji ulisababisha hata magari yanayotumia barabara ya
Makanya kushindwa kupita vema na kuwapa kazi ya ziada askari polisi wa kawaida na
wale wa barabarani kuyaongoza magari hayo.
Wasanii mbalimbali walikielezea kifo cha Kanumba kama pengo litakalochukua muda
mrefu kuziba katika tasnia ya sanaa hasa uigizaji wa filamu ambayo marehemu aliifanya kwa muda mrefu wa maisha yake tangu akiwa shuleni.
Mayasa Mrisho anayefanya kazi nyingi na Kanumba, alisema mpaka sasa haamini kama
Kanumba kafariki kwa namna kifo chake kilivyokuwa cha ghafla.
'Siamini, kama ni kweli Kanumba kafa," alisema huku akilia. Aliongeza Kanumba
amefariki wakati wakitoka kumalizia kazi yao mpya iitwayo 'Mr Price', huku pia
wakijiandaa kuingiza sokoni filamu yao mpya iitwayo 'Ndoa Yangu'.
Wasanii wengine kama Patcho Mwamba, Rajabu Jumanne 'Chilli', Issa Kipemba, Fatuma Makongoro 'Bi Mwenda' walisema itawachukua muda mrefu kumsahau mwenzao ambaye alikuwa mtu wa watu, asiye na makuu licha ya umaarufu mkubwa aliokuwa nao.
Nalo Baraza la Sanaa la Taifa, kupitia Katibu Mkuu wake, Ghonce Materego, walitoa
salamu za rambirambi kutokana na kifo hicho cha Kanumba wakidai kimeshtua na
kuwaachia pengo kubwa katika fani ya sanaa nchini.
"BASATA inaungana na familia za wafiwa na wasanii wote nchini kwa maombolezo ya msiba huu mkubwa na wa kihistoria. Kufiwa na msanii huyu mahiri kwenye tasnia ya filamu ni pengo kubwa kwa familia, Sekta ya sanaa na Taifa kwa ujumla kutokana na
ukweli kuwa, aliweza kuutangaza utamaduni na sanaa yetu nje ya mipaka," sehemu ya
rambirambi hiyo ya Basata inasomeka hivyo.
Steven Charles Kanumba, aliyezaliwa Januari 8, 1984 huko Shinyanga, alifariki usiku wa kuamkia jana kwa kile kinachoelezwa alisukumwa na kuanguka sakafuni na aliyekuwa
mpenzi wake, Elizabeth Michael 'Lulu' ambaye kwa sasa anashikiliwa na jeshi la Polisi.
Msanii huyo, aliyesoma Shule ya Msingi Bugoyi na Shule za Sekondari Mwadui, Dar
Christian Seminary na Jitegemee kabla ya kuanza kutamba kwenye sanaa kupitia kundi la Sanaa alilojiunga nalo mwaka 2002 hadi 2006 alipojiengua na kucheza filamu mbalimbali.
Baadhi ya kazi zake ni 'She is My Sister', 'Dar to Lagos', 'Cross My Sin', 'The Director', 'Hero of the Church', Sikitiko Langu, Dangerous Desire, Dar to Lagos, Cross My Sin, Village Pastor, Family Tears, Unfortunutes Love, My Valentine, The Shock, Deception na kazi ya mwisho kuitoa sokoni ni 'Kijiji Chatambua Haki'.

mwisho

SIMBA YATAKATA AFRIKA, LICHA YA KIPIGO YAFUZU 16 BORA KOMBE LA SHIRIKISHO




ANGURUMAPO SIMBA MCHEZA NANI? HAKUNAGA! Ndivyo tunavyoweza kusema baada ya klabu ya soka ya Simba kupenya kwenye hatua ya 16 Bora ya KOmbe la Shirikisho Afrika, licha ya kipigo cha mabao 3-1 ilichopewa usiku wa kuamkia leo na Entente Sportive de Setif ya Algeria.
Ikicheza wachezaji 10, Simba iliweza kupigana hadi dakika za nyongeza kupata bao pekee la kufutia machozi lililokuwa na faida kubwa kwao, kuwavusha hatua hiyo wakiwaduwaza waarabu wasiamini kilichowakuta baada ya kuamini wamemng'oa mnyama.
Shujaa wa Simba katika pambano hilo lililochezeshwa na waamuzi kutoka Tunisia alikuwa ni Mganda, Emmanuel Okwi aliyefunga katrika dakika ya 92 na kuifanya timu yake isonge mbele kwa faida ya bao la ugenini kutokana na matokeo ya jumla kuwa mabao 3-3.
Simba katika pambano lao la awali lililochezwa kwenye uwanja wa Taifa, Machi 25, ilishinda mabao 2-0 na hivyo kwa sare hiyo wamevuka kwa matokeo ya kuwa mabao 4-3.
Beki wa kutumainiwa wa Simba Juma Said Nyosso alitolewa uwanjani mapema baada ya kulimwa kadi nyekundu kwa kuonyesha ubabe uwanjani dhidi ya mshambuliaji wa Setif.
Wenyeji walitumia mwanya wa kutolewa kwa Nyosso kupachika bao la kuongoza lililofungwa dakika ya 34 na Mohammed Aoudia na kurejea kipindi cha pili kwa kasi kwa kufunga bao jingine kupitia mshambuliaji huyo mkali.
Bao la tatu la Setif, iliyokuwa ikiyotawala vipindi vyote viwili, ingawa juhudi zao za kuvuna mabao mengi zilizimwa na kipa Juma Kaseka, lilifungwa katika dakika ya 52 kupitia kwa Mokhtar Benmoussa.
Baada ya kupata mabao hayo Setif ilirejea nyuma na kulinda bao wakiamini wameshamaliza kazi kabla ya Okwi kuwaduwaza baada ya kuwachambua mabeki wa timu hiyo kisha kufumua shuti kali la mbali lililomshinda nguvu kipa wa Setif na kutinga wavuni.
Kwa ushindi huo, Simba sasa itakutana na mshindi kati ya FerroviƔrio Maputo ya Msumbiji au Al Ahly Shendi ya Sudan ambazo zinatarajiwa kuumana kesho Jumapili, huku timu ya Sudan ikiwa na faida ya bao moja iliyopata katika mechi yao wiki mbili zilizopita ilipowafunga wenyeji wao bao 1-0.
Katika mchezo wa jana kikosi cha Simba kilichoaanza dhidi ya ES Setif kiliwakilishwa na Juma Kaseja, Shomari Kapombe, Amir Maftah/Said Nassoro 'Chollo' , Juma Nyoso, Kelvin Yondani, Patrick Mafisango, Salum Machaku, Mwinyi Kazimoto, Felix Sunzu, Haruna Moshi 'Boban' na Emmanuel Okwi.

PICHA ZA BAADHI YA KAZI YA NDOA YANGU, MOJA YA FILAMU ZA MWISHO ZA KANUMBA INAYOTARAJIWA KUINGIA SOKONI KARIBUNI





ZA LEO LEO

BREAKING NEWS: STEVEN KANUMBA 'THE GREAT' IS NO MORE




MUIGIZAJI nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba, 28, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo nyumbani kwake Sinza Vatican, jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa habari za kuaminika na kuthibitishwa na rafikie wa karibu, Patcho Mwamba, Kanumba alifariki nyumbani kwake baada ya kuanguka akitokea bafuni kutokana na kuteleza.
Chanzo hicho kinasema kwamba Kanumba alianguka baada ya kusukumwa na mpenzi wake (jina tunalo) aliyekuwa akizozana nae badaa ya kupishana kiswahili.
"Brother Kanumba kafariki usiku wa kuamkia leo na maiti yake kwa sasa ipo Mumhimbili, ikisubiri taratibu za mazishi, ni kama utani ila ndio hivyo. Alisukumwa na kuangukia kisogo na kufariki papo hapo," chanzo hicho kilisema.
Aliongeza kwa sasa walikuwa wakiwasiliana na mama yake ambaye inadaiwa yupo Bukoba pamoja na familia yake iliyopo Shinyanga kujua taratibu za mazishi yake.
Patcho Mwamba alipoulizwa juu ya kifo cha Kanumba, alithibitisha lakini hakuweza kuweka bayana chanzo zaidi ya kusisitiza kuwa alianguka sakafuni nyumbani kwake na kufariki akiwahishwa Muhimbili, ambako kwa sasa mwili wake umehifadhiwa.
Steven Charles Kanumba alizaliwa Januari 8, 1984 mkoani Shinyanga akiwa ni mmoja kati ya watoto wa nne wa mzee Charles Kanumba.
Alisoma Shule ya Msingi Bugoyi, huko huko Shinyanga kabla ya kuendelea na masomo ya Sekondari katika Shule ya Mwadui, kisha kuhamia Shule ya Dar Christian Seminary, alipohitimu kidato cha nne. Baadaer alijiunga na masomo ya juu ya Sekondari na kumaliza Kidato cha Sita katika Shule ya Jitegemee, ambapo tayari alishaanza kujishughulisha na sanaa kupitia kundi la Kaole Sanaa alilotamba nalo na michezo mbalimbali iliyokuwa ikionyesha kwenye kituo cha ITV.
Baadae aliamua kujiengua katika kundi hilo na kucheza filamu akishirikiana na wasanii wenzake, Blandina Chagula 'Johari' na Vincent Kigosi 'Ray'.
Hadi anafariki msanii huyo alikuwa ni Muigizaji, Mtunzi, Mtayarishaji na muongozaji, akimiliki kampuni ya Kanumba the Great Films ambayo ilikuwa ikizalisha filamu na kuibua wasanii wengi chipukizi.
Marehemu alikuwa hajaoa wala kuwa na mtoto. Mungu aiweke roho ya marehemu mahali pema.

Thursday, January 19, 2012

'Ajuza' afyatua kibao na Mhe Temba




UNAWEZA kudhani ni utani, ila ukweli ni kwamba msanii chipukizi lakini mwenye umri mkubwa wa zaidi ya miaka 50, Mwanahija Cheka 'Bi Cheka' amefyatua kibao kipya cha miondoko ya kizazi kipya akishirikiana na nyota wa miondoko hiyo nchini, Mheshimiwa Temba.
Meneja wa msanii huyo, Said Fella, alisema kibao cha Bi Cheka kiitwacho 'Ni Wewe', kimerekodiwa katika studio za Poteza Records, chini ya utayarishaji wa Suleiman Daud 'Sulesh' au 'Mr India'.
Fella, alisema tofauti na umri wake wa miaka 51, Bi Cheka 'amechana' mno katika kibao hicho, kiasi kwamba hata Mheshimiwa Temba alimvulia kofia wakati wakirekodi.
"Huwezi amini, hajawahi kuimba kokote zaidi ya kuimba kaswida alipokuwa chuo, akimtaja mkongwe wa muziki wa dansi nchini, Maalim Muhidin Gurumo ndiye aliyekuwa mwalimu wake, lakini kazi kubwa aliyofanya kwenye wimbo huo mpya inashangaza," alisema Fella.
Aliongeza, ndani ya kibao hicho Bi Cheka anamlilia Temba awe wake kimapenzi, huku Temba akijaribu kumtolea nje kitu kilichoufanya wimbo huo kuwa wa kusisimua ambapo wanatarajia kuusambaza katika vituo vya redio kwa ajili ya kurushwa hewani.
Fella alisema mbali na kujipanga kuusambaza wimbo huo, pia wameanza maandalizi ya kufyatua video yake, huku wakiendelea kumrekodiwa nyimbo nyimbo kwa ajili ya albamu yake ambayo alisema huenda ikawa na nyimbo nane au kumi.
"Video ya kibao hicho ambacho Bi Cheka ameimba hip hop na kuchana mistari kama Da Brat (msanii nyota wa miondoko hiyo wa nchi ya Marekani), tunatarajia kuanza kurekodi wakati wowote kuanzia sasa," alisema Fella.
Fella, alisema msanii huyo aliwasiliana nae kumuomba amsaidie kumtolea kazi baada ya kusikia ana kituo cha kukuza na kuendeleza vipaji, ingawa alisitiza awali kwa umri alionao, lakini alimsihi ampe nafasi na mwenyewe ameridhika nae kwa uwezo mkubwa wa kuimba na upangiliaji wa sauti alionao.

Dar Modern kuzindua tatu kwa mpigo



KUNDI linalokimbiza kwenye miondoko ya mwambao nchini, Dar Modern Taarab 'Wana wa Jiji' wanatarajia kuzindua kwa mpigo albamu zao tatu mpya katika onyesho litakalofanyika mwezi ujao jijini Dar es Salaam.
Albamu hizo tatu za kundi hilo ni 'Sikukuchagua kwa Mapesa', 'Ndugu wa Mume Mna Hila' na 'Toto la Kiafrika' ambazo kila moja ina nyimbo nne.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Mkurugenzi wa kundi hilo, Mridu Ally Mridu 'Tx', alisema uzinduzi huo utafanyika mwishoni mwa Februari, mara baada ya kuwasili kwa kanda za kaseti za albamu hizo ambazo zinatengezwa kwa sasa nchini Kenya.
Mridu, alisema uzinduzi wao wamepanga kuufanya katika ukumbi wa Hoteli ya Travertine-Magomeni ama Diamond Jubilee yote ya jijini Dar es Salaam.
"Tupo katika mipango ya kufanya uzinduzi wa albamu zetu tatu kwa mpigo utakaofanyika ama Travertine au Diamond. Kwa sasa tunasubiri kaseti za albamu hizo zinazotengenezwa Kenya, kuwasili nchini ili tupange tarehe rasmi ya kufanyika kwa uzinduzi huo, ila utafanyika mwishoni mwa Februari," alisema.
Mridu alisema katika onyesho hilo la uzinduzi watawatambulisha wasanii wao wapya waliowanyakua hivi karibuni katika kuliimarisha kundi lao ambalo liliondokewa na mastaa wao kadhaa akiwemo Hammer Q, Hashim Said 'Big Sound' na wengineo.
Pia alisema mbali na kuzindua albamu mpya kwa kupiga nyimbo 12 za albamu hizo, pia watakumbushia nyimbo za albamu zao za zamani kama 'Ni Vijimambo Tu', 'Sote Twasaka Riziki', 'Kitu Mapenzi' na 'Gharika ya Moyo' maarufu kama 'Pembe la Ng'ombe'.
"Yaani itakuwa full burudani kwa namna tukavyowapa mashabiki wetu vitu mchanganyiko, kuanzia vile vya awali hadi hivyo vipya pamoja na kuutambulisha mtindo wetu mpya wa kunengua," alisema Mridui.
Kundi hilo la Dar Modern lilianzishwa rasmi mwaka 2006 likiundwa na wasanii mchanganyiko waliotoka kundi la Babloom Modern Taarab na mengine ya jijini Dar es Salaam.

Asilimia 80 ya waandishi wa habari hawajaajiriwa

RAIS wa Umoja wa Vilabu vya Waandishi wa Habari (UTPC), Kenneth Simbaya, amesema zaidi ya asilimia 80 ya waandishi wa habari nchini hawajaajiriwa na hawana mikataba ya aina yoyote ya kazi na wamiliki wa vyombo vya habari, licha ya kwamba wanafanya kazi katika mazingira magumu .
Simbaya aliyasema hayo jana, baada ya kutembelea Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoani Kilimanjaro (MECKI) na kuzungumza na wajumbe wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo iliyopo mjini Moshi.
Alisema utafiti uliofanywa na UTPC, umebaini zaidi ya asilimia 80 ya waandishi wa habari hapa nchini wanajitegemea kutafuta habari katika maeneo ya mjini na vijijini na hata kwenye maeneo ya hatari bila kuajiriwa ama kuwa na mikataba na wamiliki wa vyombo wanavyovifanyia kazi.
Alisema mwandishi pia amekuwa akilipwa ujira mdogo wa Sh. 5,000 na 3,000 hadi Sh. 1,500 kwa habari moja inayotoka gazetini, licha ya gharama kubwa anazotumia kutafuta habari hizo na kuwafikishia wenye vyombo vya habari.
Alisema kutokana na tatizo hilo kuwa kubwa, UTPC inafanya jitihada za makusudi kuwasiliana na wamiliki wa vyombo vya habari ili kuangalia namna waandishi wa habari wanakuwa na mikataba ya ajira kazini na hata kuendelezwa kitaaluma pindi wanapokuwa kazini kwa muda mrefu.
Alisema UTPC pia inakusudia kuanzisha vyombo huru vya habari yakiwemo magazeti, redio na televisheni, vitakavyowawezesha waandishi wa habari kuwa na vyombo vyao vinavyotumia habari sahihi na zilizofanyiwa utafiti na uchunguzi wa kina bila upendeleo.
Alitoa wito kwa waandishi wa habari pamoja na kufanyakazi katika mazingira magumu nay a hatari, kuzingatia maadili ya kazi zao na kuepuka kutumiwa na baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari kwa malengo yao binfsi.
Hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, alisema waandishi wengi wa habari wamekuwa wakifanya kazi kubwa na hata kuhatarisha usalama wa maisha yao, lakini hawalipwi mishahara kulingana na kazi wanazozifanya na badala yake wamegeuka kuwa ombaomba .
Mkuu huyo wa mkoa alisema waandishi wengi wamekuwa wakiishi kwa njia za kiujanja ujanja ili kusukuma maisha yao.

NB:Imeandikwa na Jackson Kimambo, NIPASHE-Moshi

Wednesday, January 18, 2012

Madame V awakumbuka wajane, yatima




MSANII mahiri wa muziki wa Zouk, ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Viti Maalum (CCM) Geita, Vicky Kamata amejitosa kwenye huduma za kijamii akiunda asasi yake binafsi inayoshughulikia kuwasaidia wajane, yatima na wasiojiweza.
Akizungumza na MICHARAZO, Kamata maarufu kama 'Madam V' alisema asasi hiyo inafahamika kwa jina la Victoria Foundation ambayo tayari imeshaanza kuendesha shughuli zake tangu mwishoni mwa mwaka jana.
Kamata aliyetamba na nyimbo kama 'Wanawake na Maendeleo' na 'Mapenzi na Shule', alisema ameianzisha asasi hiyo kutokana na kuguswa na matatizo ya baadhi ya watu hususan yatima na wajane waliopo ndani ya wilaya ya Geita unaotarajiwa kuwa mkoa.
Alisema kama mwanaharakati kijana anaona ni wajibu wake kujitolea kwa hali na mali kusaidia jamii hiyo ili nao angalau wajione ni wenye kuthaminiwa na kuongeza kuwa kila mtu ambaye ana uwezo wa kuwapiga tafu wenye matatizo wasisubiri kusukumwa.
"Hii ni njia ya kurudisha fadhila kwa jamii kutokana na kukubalika kwa kazi zangu kisanii na kuchaguliwa kwangu kuwa kama Mbunge, hivyo na wengine wenye uwezo wa kuwasaidia wenye matatizo wasisubiri kusukumwa kwani ni jukumu letu," alisema.
Kamata alisema kwa sasa anajiandaa kugawa baiskeli 50 na misaada mingine kwa watu wa tarafa nyingine za Geita baada ya awali kufanya hivyo tarafa ya Bugando, ambapo aligawa baiskeli 30 na kugawa vyakula na magodoro kwa vituo vya kulelea yatima vya Lelea na Feed & Tent International.

Fella asita kutoa albamu ‘Kusonona’



ALBAMU mpya ya miondoko ya 'Rusha Roho' ya Meneja wa kundi la TMK Wanaume Family, Said Fella iitwayo 'Kusonona Kusonona' haijasambazwa hadi sasa kutokana na kile ambachom mwenyewe amedai kuwa ni kuangalia kwa umakini kama ni muafaka kuitoa sasa ama la.
Akizungumza na MICHARAZO, Fella, alisema albamu hiyo yenye nyimbo sita iliyokuwa isambazwe mwishoni mwa mwaka jana, mpaka sasa haijatoka kwa sabahu hiyo ya kupima 'upepo'.
Fella alisema wakati akijiandaa kuitoa kazi hiyo mtaani, kulikuwa na kazi nyingine lukuki na hivyo kukubali kwamba atulie kwanza ili kuangalia mwenendo wa albamu zilizotangulia na kwamba huenda akaitoa mwisho wa mwezi huu.
"Ile albamu yangu ya 'Kusonona Kusonona' ya miondoko ya taarab, bado sijaiachia hadi sasa kutokana na hali ilivyokuwa sokoni, lakini kwa sasa nipo mbioni kufanya hivyo" alisema Fella.
Aliongeza, licha ya kwamba albamu bado haijaingia sokoni, lakini baadhi ya nyimbo zake zimekuwa zikifanya vema kwenye vituo vya redio na runinga baada ya kusambaza kwa nia ya kuitambulisha albamu hiyo kikiwemo 'Midomo Imewashuka'.
Ndani ya albamu hiyo, Fella amewashirikisha nyota kadhaa wa taarab wakiwemo Khadija Kopa wa TOT, Isha Ramadhani wa Mashauzi Classic na Maua Tego wa kundi la Coast Modern.
Fella alizitaja nyimbo zilizopo ndani ya albamu hiyo kuwa ni 'Simuachi', 'Midomo Imewashuka', 'Mchakamchaka', 'Sijapopoa Dodo', 'Kimodern Modern' na 'Kusonona Kusonona' iliyobeba jina la albamu.

Steve Nyerere kupakua ‘Respect Nyerere’



WAKATI filamu yake ya 'Mr President' ikiendelea kutamba, mkali wa kuigiza sauti za watu, Steven Mengele 'Steve Nyerere', sasa yuko mbioni kufyatua filamu iitwayo 'Respect Nyerere'.
Filamu hiyo itakayotolewa na kampuni yake ya 'Nyerere the Power', itahusiana na mambo mbalimbali ya kisiasa pamoja na hotuba za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere.
Muigizaji huyo ambaye ni mmoja wa viongozi waandamizi wa Bongo Movie, alisema safari ya kwenda Butiama alipozaliwa Mwalimu Nyerere imeiva kwa ajili ya kufyatua kazi hiyo ambayo alidai kwamba itakuwa kali pengine kuliko ya 'Mr President'.
"Nipo katika maandalizi ya kufyatua kazi mpya ambayo itahusisha masuala ya siasa na baadhi ya hotuba za kusisimua za Mwalimu Nyerere, mmoja wa viongozi wa mfano duniani," alisema Steve Nyerere.
Muigizaji, huyo alisema kila kinachoendelea katika upakuaji wa kazi hiyo atawafahamisha mashabiki wake.

Banana, JB, Riyama waja na DNA




MWANAMUZIKI nyota nchini, Banana Zorro anatarajia kuibukia kwenye filamu kupitia kazi mpya iitwayo DNA aliyoigiza na nyota wa fani hiyo kama Riyama Ally, Jacob Stephen 'JB' na Sabrina Rupia maarufu kwa jina la 'Cathy'.
Kazi hiyo mpya inayohusiana na masuala ya kijamii na namna hila zinavyoweza kufanywa katika upimaji wa vinasaba na kuleta mtafaruku, inatarajiwa kuingia sokoni wakati wowote kuanzia sasa.
Kwa mujibu wa taarifa za wasambazaji, ni kwamba kama anavyotamba katika muziki, Banana ambaye ni mtoto wa gwiji wa muziki wa dansi nchini, Zahir Ally Zorro ameonyesha umahiri mkubwa pia katika filamu.
"Ndani ya DNA, Banana Zorro kathibitisha kuwa habahatishi. Ameshawahi kucheza filamu kadhaa nyuma ikiwemo ya 'Handsome', na humu pia amefanya vizuri sana," imeelezwa katika taarifa hiyo.
Katika hatua nyingine, filamu mpya ya 'I Hate My Birthday' ya Vincent Kigosi 'Ray' inatarajiwa kuanza kusambazwa keshokutwa ambapo ndani yake wameshiriki nyota kadhaa kama Irene Paul na Aunty Ezekiel.

Mdogo wa Nsajigwa 'atua' Bandari Kenya



BEKI wa kutumainiwa wa timu ya 94 KJ inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara ya 94 KJ, ambaye ni mdogo wa nahodha wa Yanga, Shadrack Nsajigwa, Simon Joel Nsajigwa, ametua klabu ya Bandari Fc ya Kenya kwa ajili ya kufanyiwa majaribio.
Mchezaji huyo aliyefanana sura na umbo kama kaka yake, alienda kufanyiwa majaribio katika timu hiyo iliyoshuka daraja msimu huu toka Ligi Kuu ya Kenya, wiki mbili zilizopita baada ya mawakala wa timu kuvutiwa na soka lake.
Kocha wa timu ya 94 KJ, Mwinyimadi Tambaza, alisema walimruhusu mchezaji huyo kwenda kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa na amekuwa akiwasiliana naye kila mara kujua kinachoendelea.
Tambaza alisema walipowasiliana naye juzi alimfahamisha kuwa majaribio yake yanaendelea vema na atarejea nchini wiki ijayo ili kusubiri kitakachofuata juu ya hatma yake ya kuichezea timu hiyo iliyodakiwa na kipa Ivo Mapunda kabla ya kuitema iliposhuka daraja na kwenda kujiunga na Gor Mahia.
"Ni kweli beki wetu ambaye ni mdogo wa Shadrack Nsajigwa, yupo Kenya akifanyiwa majaribio katika timu ya Bandari na anatazamiwa kurejea nchini wiki ijayo kuungana na wachezaji wenzake kwa ajili ya duru la pili la Ligi Daraja la Kwanza wakati akisubiri tararibu nyingine za kuichezea timu hiyo ya Kenya," alisema Tambaza.
Tambaza, alisema ana imani kubwa kwa Nsajigwa mdogo kusajiliwa Bandari kutokana na kuwa na uwezo mkubwa kwa nafasi yake ya ulinzi wa pembeni kama ilivyo kwa kaka yake ambaye ni maarufu nchini kama 'Fuso'.

Mwisho

Coastal Union yakuna kichwa kwa Simba

UONGOZI wa klabu ya soka ya Coastal Union ya Tanga, umedai pambano lao la awali la duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Simba litakalofanyika wiki ijayo linawapasua vichwa wakitafakari mbinu za kuweza kuwapa ushindi wa mchezo huo.
Coastal iliyorejea Ligi Kuu msimu huu, itakwaruzana na Simba katika pambano la marudiano litakalofanyika Jumatano ijayo kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Afisa Habari wa timu hiyo, Eddo Kumwembe, alisema kuwa kuanza duru la pili kwa kuumana na Simba ni mtihani mgumu ambao unawafanya wajipange vema ili kufanya vema kabla ya kufunga safari kuwafuata Mtibwa Sugar kwenye dimba lao la nyumbani.
Kumwembe, alisema uongozi wao upo makini na pambano hilo kwa vile wanataka washinde ili kujiweka katika mazingira mazuri ya kuondoka nafasi za mkiani mwa msimamo wa ligi hiyo.
"Kuanza na timu kubwa kama Simba ni mtihani unaortuchanganya akili kwa sasa, tukijipanga kwa umakini mkubwa kuona tunaibuka na ushindi kabla ya kwenda kuvaana na Mtibwa huko Manungu," alisema Kumwembe.
Alisema lengo la uongozi wao ni kuona Coastal Union, inatoka maeneo ya mkiani na kuwa miongoni mwa timu za nafasi za juu, hasa baada ya kuongeza nyota kadhaa katika kikosi chao wakati wa usajili wa dirisha dogo.
"Tunataka Coastal ifanye vema kwenye duru hili, ndio maana hata kocha wetu aliamua kufuta mechi yetu dhidi ya Gor Mahia ya Kenya kusudi arekebishe mambo kutokana na kuwa nyuma ya mipango yake," alisema Kumwembe.
Kumwembe aliongeza, kwa kikosi walichonacho sasa ni wazi timu yao itarejesha makali yake ya zamani yaliyoipa ubingwa wa nchi.
Nyota waliongezwa katika kikosi cha Coastal ni Mkenya Edwin Mukenya, Ally Shiboli, Wanigeria Felix Amechi na Samuel Temi na wakali wengine waliokuwa katika usajili w awali wakiwemo washambuliaji Ben Mwalala na Aziz Gilla.

Mwisho

Mkubwa na Wanae: Kituo cha kuendeleza vipaji







WAKATI kituo cha kuendeleza vipaji vya sanaa kwa vijana cha 'Mkubwa na Wanawe'
kinachomilikiwa na Meneja wa TMK Wanaume Family, Said Fella kilipoanzishwa mwaka jana kilikuwa na msanii mmoja tu, Abdallah Kihambwe 'Dula Yeyo'.
Hata hivyo kikielekea kutimiza muda wa mwaka mmoja mnamo Februari 13, mwaka huu, kituo hicho kina jumla ya wasanii 37, wasichana 10 na waliosalia ni wavulana ambao wote wanaimba na kudansi.
Fella, maarufu kama 'Mkubwa Fella' ambaye ndiye Mkurugenzi wa kituo hicho alisema
alipata wazo la kuanzisha kituo hicho kilichosajiliwa kama kampuni, kutokana na kuvutiwa na mafanikio inayopata kituo kingine cha kuendeleza vipaji cha THT.
Alisema, pia alikianzishwa kwa nia ya kusaidia vijana wadogo kujiepusha kuingia kwenye makundi maovu yatakayoweza kuwapotosha na kufunza stadi za maisha kwa faida yao ya baadae mbali na kuvitumia vipaji vyao vya sanaa kama ajira rasmi.
Fella, alisema tangu kuanzishwa kwa kituo hicho ambayo anashirikiana kukiendesha na
wakurugenzi wenzake, Hamis Tale 'Babu Tale' na Mheshimiwa Temba, kimeweza kuwatoa wasanii karibu saba ambao wameanza kutamba kwenye fani ya muziki nchini.
"Tunashukuru tangu kuanzishwa kwa kituo hiki, tumefanikiwa kuwatoa wasanii kadhaa ambao wameanza kupata mafanikio katika muziki, licha ya kwamba tunakabiliwa na matatizo makubwa katika kituo chtu kwa vile hakina wafadhili wala wadhamini," alisema.
Aliwataja wasanii wanaokitangaza kituo hicho kwa sasa ni Aslay Isihaka 'Dogo Aslay'
anayetamba na wimbo wa 'Nakusemea' maarufu kama 'Naenda Kusema kwa Mama', Dula Yeyo, Mugogo anayekimbiza na wimbo wa 'Chongochongo' na Hassani Kumbi anayetamba na kibao cha 'Vocha' kilichopo katika mahadhi ya Mduara.
"Wengine ambao tumeanza kuwarekodia kutokana na kuiva kimuziki ni, H. Namba, Bashlee na Asnat wanaotarajia kuibuka na kibao kiitwacho 'Nipe Kidogo', kwa vifupi ni kwamba matunda yameanza kuonekana katika kuwaibua wasanii wapya," alisema.
Fella alisema licha ya kuwafunza namna ya kuimba na kucheza, wasanii waliopo kituo
hapo wanafundishwa stadi za maisha juu ya mapenzi na athari zake, matumizi ya dawa za kulevya na magonjwa mbalimbali kama Ukimwi na mengine na jinsi ya kuepukana nayo.
"Kwa upande wa muziki mwalimu wanayewanoa vijana hao ni Mhe Temba na Dulla Yeyo, wakati Meneja wa kituo ni Yusuf Chambuso na Prodyuza wa kituo ni Suleiman Daud maarufu kama Sulesh au Mr India," alisema Fella.
Juu ya namna ya kukihudumia kituo, Fella alisema wanatumia fedha zao wenyewe wakati wakisubiri kupata ufadhili, ambapo alisema kwa mwezi mzima hutumia si chini ya Sh. Mil moja kwa ajili ya malazi ya chakula.
"Unajua nyumba hii inayowatunzia wasanii ni ya kukodisha, tunalipa pango kwa mwezi
Sh. 250,000, huku huduma ya chakula kwa siku si chini ya Sh 25,000, hiyo ni mbali na
gharama za usafiri na ada kwa wanafunzi tunawaosemesha wenyewe," alisema.
Alisema licha ya wengi wa wasanii wao kutokea majumbani kwao kuja kujifunza fani zao kituo hapo, wapo wasanii 12 wanaoishi katika nyumba hiyo iliyopo Temeke, jijini Dar es Salaam.
Fella alisema matarajio yao hadi kufikia mwisho wa mwa huu wasanii zaidi ya 20 wawe
wameshatoka kisanii, na kuwasaidia vijana zaidi ndani na nje ya mkoa wa Dar es Salaam.
Hata hivyo alisema mafanikio hayo yatafikiwa pale atakapopata wafadhili na kuungwa
mkono na serikali katika jitihada zake za kuendeleza sanaa na kuwasaidia vijana kupata ajira kupitia muziki, sambamba na kuwajenga kimaadili.
Fella alisema kituo kwao kitu cha kwanza wanachozingatia ni nidhamu na kuwanyoosha wale wanaoonekana kwenda kinyume, pia wanathamini kipaji cha mtu bila kujali umri wake na bahati nzuri matunda yao yanaonekana kupitia wasanii walioanza kutamba sasa.
Naye Meneja wa kituo hicho, Yusuf Chambuso, alisema kuna vikwazo kadhaa wamewahi kukutana navyo kama baadhi ya wazazi kushindwa kuwaelewa katika wanachokusudia kwa kudhani watoto wao wanafunzwa uhuni, lakini wanapoeleweshwa huwapa sapoti.
Aliongeza wapo baadhi ya vijana wanaoenda kwao huwa hawana uwezo wowote kimuziki, lakini kupitia walimu wao huwasaidia na kuwaweka juu, akimtolea Aslay aliyedai licha ya kugundua kipaji cha muziki, walimsaidia kumweka sawa ndio maana leo anatisha.

Mwisho

Maneno, Matumla kusindikizwa PTA

MABONDIA wakongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Rashid Matumla 'Snake Man' na Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo' wanatarajiwa kusindikizwa na mabondia 10 tofauti katika pambano lao litakalofanyika mwezi ujao kwenye ukumbi wa PTA, jijini.
Oswald na Matumla watapigana katika pambano lisilo la ubingwa la uzani wa Super Middle, litakalofanyika Februari 25 kwa nia ya kumaliza ubishi baina yao.
Wawili hao walipigana Desemba 25 mwaka uliopita, na kutoka droo ya pointi 99-99 ambapo kila mmoja alinukuliwa kutokubaliana na matokeo hato akisema alistahili kutangazwa mshindi katika mchezo huo uliochezwa katika ukumbi wa Heinken Pub.
Mratibu wa pambano hilo, Issa Malanga, amesema kabla ya mabondia hao wakongwe kupanda ulingoni kutakuwa na michezo kadhaa ya utangulizi ambayo itahusisha mabondia chipukizi na wale wazoefu.
Malanga, alisema baadhi ya mabondia watakaowasindikiza akina Matumla ni Shomari
Mirundi atakayepigana na Mikidadi Abdallah 'Tyson' na Idd Mkenye dhidi ya Shabaan Mtengela 'Zunga Boy'.
Michezo mingine ya utangulizi itawakutanisha, Abdallah Mohamedi dhidi ya Saleh Mkalekwa na Ramadhani Mashudu ataonyeshana kazi na Hassan Kiwale 'Moro Best'.
Malanga alisema anafanya mipango mapambano hayo yapambwe na burudani ya muziki wa kizazi kipya toka kundi la TMK Wanaume Family, ingawa alisema kwa sasa ni mapema mno kwa vile bado hajafanya mazungumzo na wasanii wa kundi hilo.
Matumla na Maneno tayari walishapigana mara nne, mara mbili Matumla akiibuka na ushindi na moja Maneno kutoka kidedea na la mwisho ndilo lililoisha kwa sare inayolalamikiwa na wote wawili.

Mwisho

Juma Mgunda ala shavu Coastal, wawili watimuliwa



WAKATI nyota wa zamani wa kimataifa nchini, Juma Mgunda akila 'shavu' kwa kuteuliwa kuwa Kaimu Kocha Mkuu wa timu ya Coastal Union ya Tanga, wachezaji wawili wa timu hiyo wamefukuzwa kwa makosa ya utovu wa nidhamu.
Wachezaji waliotimuliwa Coastal kutokana na kushindwa kuripoti kwenye kambi ya timu hiyo inayojiandaa na mechi za duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara ni Daniel Busungu na Soud Abdallah aliyewahi kuichezea pia Simba msimu kadhaa ya nyuma.
Afisa Habari wa Coastal, Eddo Kumwembe, aliiambia MICHARAZO jana kuwa, Soud na Busungu wamechukuliwa hatua hiyo kutokana na kuonyesha dharau kwa uongozi wao ambao umekuwa ukiwabembeleza kujiunga na kambi ya mazoezi.
Kumwembe alisema kwa mfano Busungu licha ya kutumiwa nauli kwa ajili ya kwenda kambini hadi sasa hajaripoti wala kutoa maelezo jambo linaloonyesha hana nia ya kuichezea timu yao na ndio maana wamemtimua.
"Kwa kuwa tuna nia ya kuona timu yetu inafanya vema tumewatimua wachezaji hao kwa utovu wa nidhamu, kwani wameonyesha hawana nia ya kuichezea Coastal kwa vile fedha za nauli tumewatimua na bado wanatudengulia," alisema Kumwembe.
Aliongeza katika kuhakikisha wanafanya vema kwenye duru lijalo la ligi kuu linaloanza Jumamosi, timu yao imempa ulaji, mshambuliaji nyota wa zamani wa timu hiyo na Taifa Stars, Juma Mgunda kuwa Kaimu Kocha Mkuu.
Kumwembe alisema Mgunda, amechukuliwa kushika nafasi ya Jamhuri Kihwelu 'Julio' ambaye yupo Oman kwa mambo yake binafsi na atakapokuja ataendelea na cheo chake huku Mgunda atakuwa msaidizi wake katika benchi lao la ufundi.
"Timu kwa sasa ipo chini ya Juma Mgunda akisaidiana na Ally Jangalu, ingawa bado Julio tunamtambua kama kocha wetu hadi atakaporudi baada ya kumaliza mambo yake huko Arabuni," alisema Kumwembe.
Kumwembe, alisema kikosi chao kwa ujumla kipo vema tayari kwa mikikimikiki ya duru la pili, ambapo wao wataanza kwa kuvaana na Simba Jumatano ijayo, jijini Dar.

Mwisho

Snake Boy Jr ataka mabondia wapimwe VVU



BONDIA machachari nchini wa ngumi za kulipwa, Mohammed Matumla 'Snake Boy Jr', ametaka iwe ni lazima kwa mabondia wapimwe VVU kabla ya kupanda ulingoni kwa nia ya kuepusha maambukizi kwa wapiganaji.
Mtoto huyo wa bingwa wa zamani wa dunia wa WBU, Rashid Matumla 'Snake Man' alisema kuna udanganyifu mkubwa unaofanywa katika upimaji afya kwa mabondia kabla ya kupigana hali inayohatarisha usalama wa afya zao ulingoni.
Matumla, alisema ni lazima mabondia wawe wanapimwa afya zao na hasa VVU( Virusi vya Ukimwi), ili kuwaweka salama mabondia wawapo ulingoni ambapo hutokea wakapeana majeraha mauongoni yanayoweza kusababisha maambukizi kati yao.
"Nadhani ipo haja ya kufanyika kwa lazima upimaji wa VVU kama tunataka kuwaweka salama mabondia wetu, mara nyingi tumekuwa tukipanda ulingoni bila kupimwa afya zaidi ya uzito au kupimwa mapigo ya moyo tu, hili ni jambo la hatari," alisema.
Alisema kupitia baba yake amewahi kusikia kwamba kwa mabondia wa nchi za Ulaya wamekuwa makini katika suala la upimaji afya za mabondia kabla ya kupigana kwa lengo la kuwaweka salama na kuwapusha matatizo tofauti na ilivyo nchini.
Bondia huyo 'asiyepigika' tanu aingie kwenye ngumi za kulipwa mwaka juzi, alisema vyama na mabondia wanapaswa kusimamia jambo hilo kwa umakini mkubwa kwa vile inaweza kuleta athari kubwa baadae bila watu kujua tatizo limeanzia wapi.
Aliongeza, hata taarifa kwamba mabondia fulani wamepimwa na kugundulika wapo fiti ni propaganda tu, ukweli huwa hakuna kinachofanyika, japo alikiri suala la upimaji afya ni jambo binafsi la mtu, ila kwa mabondia kama yeye iwe lazima kwa usalama wao.
Kauli ya bondia huyo chipukizi inakaribiana na ile iliyowahi kutolewa na aliyekuwa Bingwa wa Dunia wa WBF, Karama Nyilawila aliyewahi kuvitaka vyama kusimamia suala la upimaji VVU kwa mabondia kabla ya kupanda ulingoni kupigana.

Mwisho

Moro Utd yaipigia hesabu Yanga

KLABU ya soka ya Moro United imesema ipo kwenye mahesabu makali ili kuhakikisha inaibuka na ushindi katika pambano lao la fungua dimba la duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya mabingwa watetezi, Yanga watakaumana nao Jumamosi ijayo.
Yanga na Moro United zinatarajiwa kushuka dimba la Taifa, Dar es Salaam kuumana katika mechi ya kufungua pazia la duru la pili, ambapo pia siku hiyo kutakuwa na mechi nyingine tatu katika viwanja tofauti nchini.
Katibu Mkuu wa Moro United, Hamza Abdallah, alisema kuwa akili zao zipo kwenye pambano hilo kwa lengo la kupata ushindi katika mchezo huo wa kufungua dimba ili kuanza vema na pia kujiweka katika mazingira mazuri.
Abdallah, alisema wanatambua kuwa pambano hilo litakuwa gumu kutokana na jinsi timu hizo mbili zinapokutana uwanjani mechi yao huwa na upinzani, lakini kubwa kwao ni kuona wanashinda baada ya pambano lao la awali kuisha kwa sare ya 1-1.
"Tunajipanga kuhakikisha tunapata ushindi katika mechi hiyo ya ufunguzi wa duru la pili, tunaamini kikosi tulichonacho ambacho kimeongezewa nguvu na wachezaji wapya na walimu katika benchi la ufundi, kitaisimamisha Yanga Jumamosi," alisema.
Katibu huyo alisema licha ya kwamba imewapoteza wachezaji nyota watatu, Omega Seme na Salum Telela waliorejea Yanga na Gaudence Mwaikimba kuhamia Azam, bado kikosi chao kitafanya vema baada ya kuwanasa wakali wengine kadhaa.
Baadhi ya wachezaji inayojivunia MoroUtd katika kikosi chao cha sasa ni pamoja na Jamal Mnyate toka Azam, Fred Mbuna aliyetoka Yanga, Salum Kanoni na Meshack Abel wote kutoka Simba waliosajiliwa kwenye dirisha dogo lililofungwa hivi karibuni.
Timu hiyo kwa sasa imejichimbia kambini eneo la Tabata, jijini Dar es Salaam tayari kwa ajili ya pambano hilo dhidi ya Yanga.

Mwisho

Tuesday, January 10, 2012

Diamond ahukumiwa miezi sina anusurika kwa kulipa faini





MAMIA ya watu waliofurika kushuhudia hukumu ya msanii nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini Naseeb Abdul a.k.a Diamond, walipigwa na butwaa baada ya kuhukumiwa kifungo cha miezi sita jela au kulipa faini ya Sh.50.000 kwa kosa la kumshambulia na kuharibu mali za mwandishi wa habari mkoani Iringa Francis Godwin.
Hatua hiyo imekuja baada ya msanii Diamond na wacheza shoo wake wawili kukiri kosa mbele ya mahakama yeye na wenzake kwa kuharibu Camera mbili, Lap top aina ya Accer pamoja na kumshambulia mwanahabari Francis Godwin Desemba 31 mwaka jana katika uwanja wa Samora mjini Iringa.
Akitoa hukumu hiyo hakimu wa Mahakama ya Mwanzo Hakimu Masua alisema kulingana na watuhumiwa wote watatu kukiri kosa hilo anawahukumu kwenda jela miezi 6 au kulipa fidia ya shilingi elfu hamsini kila mmoja na huku wakilazimika kumlipa Godwin shilingi elfu 30 kila mmoja na kufanya kufikia kiasi cha shilingi 90000 Wakitoa utetezi wao watuhumiwa hao walisema mahakama iwapunguzia adhabu kwa kuwa hawakukusudia kufanya kosa hilo, na wao walikuja mkoani hapa kwa ajili ya kutoa burudani, na kuwa tukio hilo wamelifanya kwa ghadhabu.
Mheshimiwa Hakimu ninaomba unipunguzie adhabu licha ya kutenda kosa hilo, kwani nakili kuwa nilipatwa na hasira kama binadamu na kuamua kuchukua uamuzi wa kufanya hayo, mimi sikukusudia kuja Iringa kufanya vurugu bali hali hiyo ilikuja baada ya kupata ghadhabu kama walivyo binadamu wengine,” alisema Diamond.
Naye mwanasheria Evaristo Myovela alisema kesi hiyo hakimu ametimiza wajibu wake, huku akimshauri Francis kukata rufaa kama hajaridhika na maamuzi ili kuipeleka kesi hiyo katika Mahakama nyingine kwa kufuata utaratibu wa sheria katika kuchukua maamuzi hayo.
Wakati wanahabari wakijadili juu ya hukumu ya Diamond , mara Waziri wa sera na uratibu wa sheria za bunge Willium Lukuvi alikatiza katika mahakama hiyo ndipo wanahabari wakataka kupata mawazo na uelewa zaidi juu ya hukumu hiyo.
Hata hivyo Diamond alilipa fidia hiyo na kuachiwa huru licha ya Godwin kuamua kupeleka barua mahakamani ya kuomba nakala ya kesi na 13. ya 2012 kwa ajili ya kukata rufaa

VICKY KAMATA ALIVYOMWAGA MISAADA GEITA





Mbunge Vicky Kamata amwaga misaada kwa walemavu, yatima mkoani Geita







MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa Mpya wa Geita, Vicky Kamata, amemwaga msaada wa wenye thamani zaidi ya Sh Milioni 10, unaohusisha vyakula, mavazi, magodoro na viti vya walemavu (wheel chair) 30 kwa wakazi wa tarafa ya Bugando mkoani humo.
Misaada hiyo ambao ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi zake kwa wakazi wa Geita waliomsaidia kuchaguliwa kwake kuwa mbunge kupitia CCM, ulitolewa juzi katika tarafa hiyo na vituo vya kulelea na kutunzia yatima vya Lelea na Feed & Tend International.
Kwa mujibu wa Kamata, misaada hiyo imehusisha viti vya walemavu 30, magodoro 50, maziwa, vyakula na nguo vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya Sh. Milioni 10 na kudai ugawaji huo umefanyika kwa awamu ya kwanza na utaendela kwa awamu nyingine mbili.
"Hii ni awamu ya kwanza ya utekelezaji wa ahadi zangu kwa wakazi wa Geita katika kuwasaidia wenye matatizo, natarajia kuendelea na ugawaji kama huo utakaohusisha baiskeli nyingine 50, ambazo tayari zimeshawasili toka nje ya nchi," alisema Kamata.
Mbunge huyo kijana, alisema misaada hiyo na mingine ambayo amekuwa akitoa kwa watu wenye matatizo mkoani mwake inafanywa chini ya mfuko wake wa Victoria Foundation ambayo yeye ni Mwenyekiti wake ikishirikiana na wafadhili wa nje ya nchi.
Alisema ukiondoa utekelezaji wa ahadi zake, lakini misaada hiyo inalenga kuwasaidia watu wenye matatizo waliopo mkoani humo, wanaondokana na adha walizonazo na kufurahia maisha kama watu wengine.

Mwisho

Friday, January 6, 2012

Oswald, Njiku, Palasa kuwasindikiza akina Cheka

MABONDIA wanaotamba kwenye mchezo wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Oswald, Chaurembo Palasa na Deo Njiku wa Moogoro wanatarajiwa kupanda ulingoni kuzichapa kusindikiza pambano la Francis Cheka dhidi ya Karama Nyalawila.
Cheka na Nyalawila wanatarajiwa kupigana Januari 28 kwenye pambano lisilo la ubingwa litakalofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri, Morogoro ambapo mratibu wa pambano hilo, Philemon Kyando 'Don King' ametangaza michezo ya utangulizi.
Kyando, ambaye ni Mkurugenzi wa Don King Kyando Promotion, alisema kabla ya Cheka na Nyalawila kupanda ulingoni kupigana, mabondia 10 tofauti watawasindikiza ambapo Chaurembo Palasa anatarajiwa kuzichapa na Deo Njiku.
Mabondia wengine watakaopigana katika pambano hilo la akina Cheka litakalokuwa na raundi 10 uzani wa Super Middle ni mkongwe Maneno Oswald aliyeambulia sare hivi karibuni mbele ya mkongwe mwenzake, Rashid Matumla atakayepigana na Hamis Ally wa Morogoro.
"Mapambano mengine ya utangulizi yatawahusisha, JUma Idd wa Dar dhidi ya JUma Afande wa Morogoro, pia kutakuwa na pambano jingine litakalowakutanisha mabondia wa kike watakaoonyeshana kazi siku hiyo," alisema Kyando.
Promota huyo aliyekuwa kimya kwa muda mrefu, alisema michezo hiyo ya Januari 28 itakuwa maalum kwa uzinduzi wa kampuni yake sambamba na kumpongeza Mbunge wake wa Jimbo la Morogoro, Aziz Abood kwa kusaidia maendeleo ya jimbo hilo.
"Unajua mie natokea eneo la Kihonda na nimekuwa nikivutiwa na kasi anayofanya mbunge huyo katika kuleta maendeleo ndio maana nimeandaa pambano hili la Cheka na Nyalawila lifanyike Morogoro kama kuunga mkono juhudi zake," alisema Kyando.
Kyando, aliyetamba miaka ya 1980 na 2000 kabla ya kuzimika, alisema ujio wake mpya utaenda sambamba na kuwainua mabondia chipukizi waliopo kila kona ya nchi badala ya kufuata mkumbo wa mapromota wengine kung'ang'ania mabondia wa mijini tu.
Cheka anayefahamika kama SMG na Nyalawila maarufu kama 'Captain' watapigana likiwa pambano lao la pili kwani walishawahi kukutana na kushindwa kutambiana kwa kutoa sare, ingawa kila mmoja kwa sasa anashikilia mataji makubwa duniani.
Nyalawila ni bingwa wa dunia wa WBF, huku mpinzani wake akishikia mataji ya UBO, ICB na Kamisheni ya Ngumi ya WBC.

Mwisho

BFT yateua 25 kushiriki kozi ya kimataifa ya ukocha

SHIRIKISHO la Ngumi za Ridhaa Tanzania, BFT, limetangaza majina ya makocha 25 walioteuliwa kushiriki kozi ya kimataifa ya mchezoitakayofanyika kati ya Januari 16-24.
Awali kozi hiyo ilipangwa kufanyika Novemba mwaka jana ikishirikisha makocha 30, lakini ilikwama kutokana na mkufunzi wa kimataifa toka Algeria aliyekuwa aiendeshe kushindwa kuwasili na kufanya BFT kuwapunguza washiriki watano safari hii.
Taarifa ya BFT inasema imewapunguza makocha hao watano kutokana na agizo la TOC linalosimamia kozi hiyo kufuatia hasara iliyopata awali wakati wa maandalizi ya awali ambayo hata hivyo haikufanyika.
Katibu wa BFT, Makore Mashaga, alisema idadi hiyo ya makocha hata hivyo inaweza kupunguzwa kulingana na bajeti iliyopo ambayo itawagharamia washiriki mwanzo mwisho katika kozi hiyo.
Mashaga aliwataja washiriki hao kuwa ni Rajabu Mhamila 'Super D', Anord Ngumbi,
Moses Lema, Anthon Mwang'onda na Edward Emmanuel kutoka Dar es Salaam, Yahya Mvuvi (Tabora), Joseph Mayanga na Zakaria Mwaseba wote wa Morogoro.
Wengine ni Omari Saady na Mussa Bakari (Mwanza), Ally Ndee (JKT-Mbeya), Emilio Moyo na Gaudence Uyaga (Pwani) Juma Lisso (Magereza-Kigoma), Lyinda Kalinga (Dodoma) na Abdallah Bakar (Tanga).
Washiriki wengine ni Mohammed Hashim (Polisi Dar es Salaam), Haji Abdallah, Said Omar na David Yombayomba (JWTZ), Mazimbo Ally, Rogated Damian na Fatuma Milanzi (JKT), Musa Maisori na Hamisi Shaaban (Magereza Dar es Salaam).
Katibu huyo alisema kozi hiyo itakayofanyika kwenye majengo ya Shule ya Sekondari Filbert Bayi, Kibaha-Pwani itaendeshwa na mkufunzi wa kimataifa Josef Diouf kutoka Shirikisho la Dunia la mchezo huo, AIBA atakayeshirikiana na Makamu wa Rais wa BFT, Michael Changarawe.

Mwisho

Bella awang'onga wasanii Bongo



RAIS wa bendi ya Akudo Impact, Christian Bella, amewataka wasanii wa Kitanzania kujenga mazoea ya kuwashirikisha wasanii wenye majina makubwa wa kimataifa na wanaoimba miondoko tofauti na yao kwa lengo la kuteka soko la kimataifa.
Pia, amesema bila bendi za Tanzania kubadilika na kuachana na kuiga kazi za wasanii wa nje hasa wakongo, ni vigumu kuweza kutamba katika soko la kimataifa kwa vile watu wanaowaiga tayari wameshajiwekea mizizi ya kutosha karibu kila kona ya dunia.
Bella, alisema mtindo anaoutumia AY kuwashirikisha wasanii mbalimbali wa kigeni unapanua wigo wa kazi za msanii huyo kufahamika kimataifa na kumtangaza vema.
Alisema jambo hilo linapaswa kuigwa na wengine, ambao wamezoea kufanya kazi na wasanii wenzao wa nyumbani au wanaoimba miondoko inayofanana.
"Unaona nimemshirikisha Isha Mashauzi katika kazi yangu 'Kilio cha Maskini' kwa lengo la kuteka mashabiki wa taarab, ila kwa kujitangaza kimataifa, lazima tuwashirikishe wasanii wa kigeni wenye majina makubwa tujitangaze," alisema.
Alisema wasanii wa Bongo wajiulize inakuwaje, Fally Ipupa aimbe na nyota wa Nigeria na miondoko yao haifanani, kisha wamwangalia AY na jitihada zake kisha wafuate nyayo hizo kwani zitawatangaza kimataifa tofauti na sasa.
Aliongeza, bendi za muziki wa dansi nchini ziache tabia ya kuiga kazi za wasanii wa nje hasa wakongo badala yake wabuni kazi zao wenyewe ili waweze kuteka soko la kimataifa.
Bella alisema bendi za Kibongo haziwezi kutamba soko la kimataifa kwa kupiga kama Koffi au JB Mpiana wakati kazi za wasanii hao zinatambulika karibu kila kona ya dunia.

Mwisho