STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, April 27, 2014

Papa Francis aweke rekodi, ateua mapapa wawili kuwa watakatifu

Papa Francis, kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani
UMATI mkubwa wa watu wamekusanyika mjini Vatican kushuhudia tukio la kihistoria ambapo viongozi wawili wa zamani wa Kanisa Katoliki, Papa John Paul II na Papa John XXIII wametangazwa watakatifu.
Ibada iliyoendeshwa kwa pamoja kati ya Papa Francis na mtangulizi wake Papa Benedict XVI imeangaliwa na karibu mahujaji milioni moja na wengine mamilioni ya watu kupitia matangazo ya televisheni na redio.
Karibu ujumbe wa wageni 100 wamehudhuria sherehe hiyo, wakiwemo kutoka koo za kifalme na wakuu wa nchi na serikali.
Hii ni mara ya kwanza kwa papa wawili kutangazwa kwa wakati mmoja kuwa watakatifu.
Waandishi wa habari wanasema hatua hii inachukuliwa kama njia ya kuziunganisha kambi mbili za wapenda mageuzi na wasiotaka mabadiliko ya sheria katika Kanisa Katoliki.
Chanzo BBC Swahili

Kocha mpya Stars aita wapya tisa yumo Javu, Maguli

Hussen Javu aliyeitwa Stars ya kuivaa Malawi
Elias 'Magoli' Maguli naye kaongezwa na kocha mpya wa Stars
kochaaaa
Kocha mpya wa Stars
 KOCHA Mkuu mpya wa Taifa Stars, Mart Nooij amewaongeza wachezaji tisa katika kikosi cha timu hiyo kinachojiandaa kwa mechi ya kirafiki na timu ya Malawi(The Flames) ambayo itakachezwa Mei 4 mwaka huu katika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.
Stars iliyonyolewa mabao 3-0 jana na Burundi huku kocha huyo akishuhudia uwanjani, ambapo Rais wa TFF, Jamal Malinzi alimtambulisha na kueleza wamemsainisha mkataba wa miaka miwili kuinoa timu hiyo.
Wachezaji walioongezwa na kocha huyo ni Edward Manyama (JKT Ruvu), Elias Maguli (Ruvu Shooting), Hassan Dilunga (Yanga), Hussein Javu (Yanga), John Bocco (Azam), Kelvin Friday (Azam), Oscar Joshua (Yanga), Nadir Haroub (Yanga) na Shomari Kapombe (AC Cannes, Ufaransa).
Walioondolewa ni pamoja na beki Kelvin Yondani wa Yanga ambaye aliitwa awali na sababu za kuondolewa ni kushindwa kuripoti kambini.
Kikosi hicho cha Taifa Stars inategemewa kuingia kambini kesho Aprili 28 jijini Mbeya kujiandaa kwa mechi dhidi ya Malawi.
Wakati huo huo, Tanzania (Taifa Stars) imepangiwa kucheza na Zimbabwe katika raundi ya pili ya mechi za mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika (AFCON) zitakazofanyika mwakani nchini Morocco.
Kwa timu ya Taifa Stars itaanzia nyumbani ambapo mechi ya kwanza itachezwa kati ya Mei 16 na 18 wakati ile ya marudiano itachezwa Harare kati ya Mei 30 na Juni 1 mwaka huu.

Chelsea yaizima Liverpool Anfield

Demba Ba akiiandikia Chelsea bao dakika ya 45 ya mchezo wao wa leo
Mimi ndiyo Only Special bwana!! Mourhino akijipiga kifua kuonyesha umahiri wake kwa kuzima Liverpool kwao kwa maba 2-0
Liverpool wakiwa hawamini kama wamelala nyumbani
 CHELSEA chini ya kocha wake, Jose Mourinho ikiwa ugenini kwenye uwanja wa Anfield imefanikiwa kuisimamisha Liverpool baada ya kuizamisha Liverpool kwa mabao 2-0 katika Ligi Kuu ya England.
Liverpool ambayo ilikuwa ikitarajiwa kujiandikishia rekodi ya kuelekea kunyakua taji la kwanza la Ligi Kuu baada ya miaka 24, ilishindwa kuamini kama imelala nyumbani kwao kwa vijana wa Mourinho.
Mabao ya 'jioni' katika kila kipindi kupitia kwa Demba Ba na Willian yalitosha kuipa ushindi huo Chelsea na kuwasogelea wapinzani wao kwenye mbio za kuelekea kwenye ubingwa wa ligi hiyo.
Demba Ba alifunga bao la uongozi dakika chache kabla ya timu kwenda mapumziko kabla ya Torres kuvunja mtego wa kuotea na kumpa pasi murua Willian aliyezamisha bao sekundu chache kabla ya mchezo huo kumalizika.
Chelsea iliyotumia muda mrefu 'kupaki basi' na kuinyima fursa Liverpool kuipenya ngome ya vijana hao wa The Blues ambap hawakutarajiwa kupata ushindi huo katika mechi yao leo.
Hii ni kwa sababu Mourinho alishatangaza mapema angekichezesha kikosi cha pili ili kuweka nguvu kwa mechi ya marudiano ya Ligi ya Mabingwa hatua ya nusu fainali dhidi ya Atletico Madrid watakaowafuiata Stanford Bridge siku ya Jumanne.
Kwa ushindi huo, Chelsea imeweza kupunguza pengo la pointi na kufikisha mbili nyuma ya wapinzani wao wanaoongoza msimamo wa ligi hiyo wakiwa na pointi 80 wakati ligi imesaliwa na raundi mbili kabla ligi haijamalizika mwezi ujao.
Dakika chache zijazo Manchester City waliopo nafasi ya pili watakuwa ugenini kuvaana na Crystal Palace katika mfululizo wa ligi hiyo wakiwa na pointi 74 kutokana na mechi 34.

Mwina Kaduguda afunguka Simba kuelekea Uchaguzi Mkuu

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiZr9zB8jynEIPYNspsH_GwAc4jaqA8REf2Q-oJCyB6nAKNQ2kgA75m-MIsYRtg2OI10zit1RxQuwsAYGdpBLXRovzv0G3Hjj-YfxjRNokWlOMH28psVc5VT2CReAAJu_QmISgPokUHzlw/s1600/DSC_6361.JPG
Mwina Kaduguda (kushoto) akiwa na aliyekuwa mwenyekiti wake, Hassan Dalali walipokuwa wakiukabidhi uongozi wa sasa wa Simba, chini ya mwenyekiti wake Ismail Rage
KATIBU Mkuu wa zamani wa Simba, Mwina Kaduguda ameyataka makundi yanayosigana ndani ya klabu hiyo kukaa pamoja na kumaliza tofauti zao kabla ya  kuelekea kwenye Uchaguzi Mkuu unaoatarajiwa kufanyika hivi karibuni.Kaduguda alisema lengo la makundi hayo kukaa meza moja ni kujenga umoja na mshikamano kwa lengo la kupata viongozi bora wanaokubalika.
Aidha amewakumbusha wanachama wa klabu hiyo kuhakikisha wanachagua viongozi ambao wataiwezesha Simba kuwa moja na itakayokuwa na uwezo wa kunyakua ubingwa wa Afrika.
Akizungumza kwenye kituo cha radio Clouds Fm leo mchana, Kaduguda alisema uzoefu alionayo katika kuongoza soka ndani ya klabu hiyo na kwingine umemfanya kuitambua kinachokwaza soka la Tanzania kusonga mbele mojawapo ikiwa ni mifarakano ya kuendekeza makundi.
Kaduguda aliyewahi kuwa Katibu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kipindi ikiitwa FAT, alisema ndani ya Simba kuna makundi ambayo yamekuwa yakiwagawa wanachama kila upande ukitaka kundi lao litoe kiongozi kitu alichodhani kinapaswa kudhibitiwa mapema.
Alisema ni vyema makundi yaliyopo kukaa meza moja kwa nia ya kuijenga Simba kuelekea kwenye uchaguzi kwa kuiwezesha klabu hiyo kupata viongozi bora watakaoivusha mahali ilipo na kuja kutamba Afrika, la sivyo inaweza kukutwa na yaliyozikuta Gor Mahia au AFC Leopard za nchini Kenya, zilizopotea kwenye umaarufu wao wa soka kabla ya kuibuka tena.
"Hakuna siri ndani ya Simba kuna makundi kama ya Simba Taleban, Friend's of Simba na Banyamulenge ambalo hata hivyo limelegalega, nashauri wanayounga mkono makundi hayo yakae pamoja na kumaliza tofauti na kujadiliana kiongozi gani anayewafaa kuwaongoza."
Kaduguda alisema na kuongeza, pia makundi hayo yanapaswa kutowapuuza au kuwabeba watu kwa sababu ya haiba yao au uwezo wa kiuchumi, akieleza hata wasio na uwezo wa kifedha wana haki na nafasi kubwa ndani ya klabu hiyo.
Pia aliwakumbusha wanachama wa klabu hiyo kuwa makini katika uchaguzi huo ili kuipa Simba viongozi makini na bora watakaoiwezesha klabu yao kutamba kimataifa badala ya kuwabeba watu ambao watakuja kuwanyima raha kwa miaka minne ijayo.
Klabu ya Simba inaelekea kufanya uchaguzi mkuu baada ya uongozi wa sasa chini ya Mwenyekiti wao, Ismail Aden Rage kumaliza muda wao mwezi ujao.
Hata hivyo uchaguzi huo bado haujatangazwa rasmi na Kamati ya Uchaguzi ya klabu hiyo kwa sababu ya kusubiri kupitishwa kwanza kwa Katiba yao mpya na ofisi ya Msajili ili kuweka hadharani mchakato kamili ya kinyang'anyiro hicho.

PSG yakwama kutangaza ubingwa Ufaransa

http://static.goal.com/334600/334648hp2.jpg
KLABU ya PSG  inalazimika kusubiri hadi wiki ijayo kuona kama itatetea na kunyakua taji la Ligi Kuu ya Ufaransa mapema baada ya mpango huo kukwama mbele ya timu iliyopo mkiani Sochaux na kulazimishwa sare ya bao 1-1 katika ligi hiyo.
Bao la kujifunga la Mbrazil Thiago Silva liliinyima PSG fursa ya kutawazwa mabingwa wapya na kuwafanya wababe hao kufikisha pointi 83.
PSG ilionekana kama wangesherehekea ubingwa ikiwa ugenini baada ya Edinson Cavani kufunga bao dakika ya 24 na lililodumu hadi wakati wa mapumziko.
Cavani alifunga bao hilo kiufundi baada ya kupokea krosi pasi ya Thiago Motta kwa kifua kabla ya kujikunjua na kuiandikia PSG bao.
PSG itabidi wasubiri pambano lao lijalo dhidi ya Rennes kukamilisha kiu yao ya kunyakua taji kwa ya pili mfululizo mbelebya Monaco waliopo nafasi ya pili wakiwa na pointi 75 huku timu zote zikisaliwa na michezo mitatu kila moja.
Hata hivyo p

Hatma ya waliosimamia Ruvu kujulikana kesho

http://api.ning.com/files/RbGVjb*ZO54uy37SpnuBHdFW7xexpiQ8bPS114bo6aA*6lpw39ydLeFhzsy4HxtWhz99xUAiwN2Yp679VDZwThtXKHkwDf9M/kiijiko.JPG
Kijiko
HATMA ya wachezaji watatu wa timu ya Ruvu Shooting waliosimamishwa kwa muda usiojulikana siku moja kabla ya kuvaana na Azam katika mechi za mwishoni mwa msimu uliopita wa Ligi Kuu Tanzania Bara, inatarajiwa kujulikana kesho Jumatatu wakati Kamati ya Utendaji ya timu hiyo itakapokutana kuipitia na kuijadili ripoti ya kocha wao, Mkenya Tom Oloba aliyeiwasilisha kwao juzi Ijumaa.
Wachezaji hao beki Ibrahim Susan 'Chogo' kiungo Juma Seid 'Kijiko' na mshambuliaji Cosmas Lewis walisimamishwa na viongozi kwa tuhuma za utovu wa nidhamu baada ya kutoweka kambini bila taarifa zozote wakielekea kwenye mechi hiyo na Azam iliisha kwa mabingwa wapya wa msimu huu, Azam kuibuka na ushindi mnono wa mabao 3-0 na kuvunja mwiko wa Ruvu kufungwa Mabatini.
Afisa Habari wa Ruvu, Masau Bwire alisema licha ya awali uongozi kupanga kuwaita wachezaji hao ili wajieleze, suala hilo lilishindikana kutokana na kubanwa na ratiba ya mechi za kufungia msimu, hivyo watakutana Jumatatu kuamua hatma yao.
Bwire alisema wataamua hatma ya wachezaji hao kutegemeana na ripoti ya benchi la ufundi la timu hiyo iliyowasilishwa kwao na kocha wao Tom Olaba ambayo ina mapendekezo kwa ajili ya msimu ujao.
"Hatma ya wachezaji watatu na wengine ambao wataachwa au kubakishwa kwenye kikosi cha Ruvu kwa ajili ya msimu ujao itafahamika Jumatatu (kesho) wakati viongozi watakapokutana ili kuipitia na kuijadili kwa kina ripoti ya kocha iliyowasilishwa kwetu siku ya Ijumaa," alisema.
Aliongeza, uongozi huo pia utafanya tathimini ya msimu mzima wa ligi kwao kama wamefanikiwa katika malengo yao na kujipanga kwa msimu ujao ili kuhakikisha yale yaliyowaangusha msimu huu yasijirudie na Ruvu Shooting iendelee kuwa timu ya upinzani na siyo shiriki katika ligi hiyo ambayo iliyoshuhudia ushindani ya hali ya juu.
Ruvu Shooting imekuwa na msimu mzuri mwaka huu baada ya kufanikiwa kumaliza nafasi ya sita ikiwa na pointi 38 ikilingana na klabu ya Simba na Kagera Sugar waliotofautiana nao mabao ya kufunga na kufungwa.

Souchaux yachomoa bao la PSG

http://www.getfootballnewsfrance.com/assets/Silva.jpg
Brazil Thiago Silva kajifunga bao
BAO la kujifunga la Thiago Silva la dakika 56, limeisaidia wenyeji Sochaux kusawazisha bao katika mechi inayoendelea ya Ligi Kuu ya Ufaransa ambayo inaweza kutoa bingwa wa ligi hiyo.
Pambano linaingia dakika ya 70 na matokeo yakiwa 1-1, wakati PSG inahitaji ushindi wowote leo kuweza kutangazwa mabingwa kwa mara ya pili nchini humo kwani itafikisha pointi 85 na michezo mitatau mkononi ambazo hazitaweza kufikiwa na timu yoyote ikiwamo wapinzani wao wa karibu Monaco.

Bao moja lamliza Amissi Tambwe

Tambwe akiwa na Mombeki
MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Simba na Mfungaji Bora wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu, Amissi Tambwe amesema pamoja na kunyakua kiatu cha dhahabu, lakini hajafurahishwa na kushindwa kutimiza lengo lake la kufunga jumla ya mabao 20.
Tambwe aliyesajiliwa na Simba kwa mkataba wa miaka miwili akitokea Vital'O ya Burundi, aliwaahidi mashabiki kwamba angefunga jumla ya mabao 20 kama lengo lake la kuendeleza rekodi yake ya kufumania nyavu iliyompa kiatu cha dhahabu pia katika michuano ya Kombe la Kagame ya mwaka jana iliyofanyika nchini Sudan.
Mrundi huyo alisema kitendo cha kushindwa kupata bao moja la kukamilisha idadi ya mabao aliyopania msimu huu, inamuuma ingawa hakuwa na jinsi kwa jinsi alivyokuwa akikamiwa uwanjani na wakati mwingine kuumizwa na kushindwa kucheza mechi zilizofuata.
"Nasikitika kushindwa kukamilisha idadi ya mabao niliyokuwa nimepania msimu wangu wa kwanza ndani ya Simba, nilipanga nifunge 20, lakini moja nimeshindwa kulipata mpaka ligi ilipomalizika," alisema Tambwe.
Hata hivyo mchezaji huyo ambaye amekuwa gumzo na aliyeweka rekodi ya kufunga hat trick mara mbili baada ya ukame wa muda mrefu wa kufungwa idadi hiyo ya mabao katika ligi ya Tanzania tangu alipokuwa amefanya hivyo Juma Semsue wa Polisi Dodoma mwaka 2010, alisema anajipanga kwa msimu ujao panapo majaliwa.
Tambwe alisema anaamini tayari amepata uzoefu wa kutosha wa ligi ya Tanzania hivyo atajua namna ya kujipanga kuendelea kuwaliza makipa na timu pinzani kama alivyofanya katika msimu huu akifikia rekodi ya ufungaji wa mabao mengi iliyowahi kuwekwa na John Bocco misimu miwili iliyopita.
Katika msimu uliopita Mfungaji Bora alikuwa Kipre Tchetche wa Azam aliyefunga mabao 17 ambaye msimu huu aliungana na wachezaji Elias Maguli wa Ruvu Shooting na Mrisho Ngassa kufunga mabao 13 kila mmoja na kushika nafasi ya pili nyuma ya Tambwe.
Tambwe jana aliiongoza timu yake ya taifa ya Intamba Murugamba kuitoa nishai timu ya taifa, Taifa Stars kwa kuwacharaza mabao 3-0 katika mchezo maalum wa sherehe za Muungano, akisaidiana na mkali mwingine anaycheza Yanga, Didier Kavumbagu kila mmoja akifunga bao moja.
Kwa kunyakua kiatu hicho cha dhahabu, Tambwe amejihakikishia kuzoa kitita cha Sh. Mil 5.2 toka kwa wadhamini wa Ligi Kuu kampuni ya Vodacom.

Sunderland 'yaua' England yatoka mkiani

Sunderland striker Connor Wickham (left) watches as his header puts his side in front against Cardiff
Sunderland ilipokuwa ikijitetea EPL muda mfupi uliopita
VIBONDE wa Ligi Kuu ya England, Sunderland ikiwa uwanja wao wa nyumbani wa Stadium of Light imefanya mauaji ya kutisha baada ya kuigagadua Cardiff City kwa mabao 4-0. huku wageni hao walicheza pungufu kwa nusu nzima ya mchezo huo kwa kuonyeshwa kadi nyekundu..
Sunderland iliyokuwa mkiani ilichupa hadi nafasi ya 17 kwa kufikisha pointi 32 ilipata ushindi huo wa pili mfululizzo baada ya wiki iliyopita kuinyuka Chelsea na kuiacha Cardiff wakiwapokea kwenye nafasi hiyo katika hatari ya kushuka daraja.
Ushindi huo wa Sunderland uliopatikana muda mfupi uliopita kupitia mabao ya Conor Wickham aliyefunga mabao mawili katika dakika ya 26 na 86, huku jingine lililokuwa la pili likifungwa na Fabio Borini kwa mkwaju wa penati dakika za nyongeza kabla ya timu kwenda mapumziko.
Bao jingine lililoisaidia timu hiyo kufikisha jumla ya pointi 32 wakati mechi ligi ikielekea ukingoniu lilifungwa na Muitaliano Emanuele Giaccherini dakika ya 76.

PSG yabaki kidogo kutetea taji la Ligi Ufaransa

http://images.football365.com/13/09/800x600/PSG-v-Toulouse-Edinson-Cavani-celeb_3011490.jpg
Cavani aliyeitanguliza PSG kwenye taji la Ligue 1 nchini Ufaransa
KLABU ya PSG ya Ufaransa inaelekea kunyakua ubingwa wa ligi ya nchi hiyo kwa mara ya pili wakati huu ikiwa uwanjani ikiongoza bao 1-0 ugenini dhidi ya Sochaux.
Mechi ikiwa inaelekea mapumziko, PSG imebakiza hatua chache kabla ya kunyanyua juu ubingwa wa nchini baada ya Edinson Cavani kutupia bao dakika ya 25.
Kabla ya mechi hiyo PSG ipo kileleni ikiwa na pointi 82, ikiwaacha wapinzani wao wa karibu Monaco ambayo jana ilipata ushindi wakiwa na pointi 75 na kusaliwa na mechi tatu ambazo kama itashinda itakusanya jumla ya pointi 84 tu ambazo kama PSG itashinda leo itakuwa imezivuka na hakuna wa kuweza kuzifikia pointi zake 85.
MICHARAZO itawaletea taarifa zaidi kujua kama matajiri hao wa Paris wameweka kibindoni taji hilo wakiwa bado na mechi tatu mkononi.

Pambano la Mashali, Nyilawila lipo halipo

Thomas Mashali
http://www.ibn-tv.com/wp-content/uploads/2012/02/Nyilawila.jpg
Karama Nyilawila
PROMOTA wa pambano la ngumi za kulipwa kuwania ubingwa wa UBO, kati ya Thomas Mashali na Karama Nyilawila, Ally Mwazoa amesisitiza kuwa mchezo huo upo kama ulivyopangwa siku ya Mei Mosi.
Mwazoa ametoa ufafanuzi huo baada ya kuwepo kwa taarifa kwamba pambano hilo la kimataifa halitakuwepo kama ilivyopangwa na kwamba mashabiki wasisumbuke kwenda PTA  kulishuhudia.
Akizungumza na MICHARAZO kwa njia ya simu toka jijini Tanga, Mwazoa alisema hafahamu wanaoeneza taarifa kwamba mchezo huo haupo ilihali alishalitangaza mapema na mabondia wanaendelea kujiandaa.
Hata hivyo alisema kwa namna hali ilivyo analazimika kukutana na mabondia hao wawili kuweza kuwekana sawa kabla ya kupanda ulingoni.
"Nilishatangaza mapema kwamba mabondia hao watapigana Mei Mosi, sasa taarifa kwamba pambano hilo halipo kwa kweli sijui uvumi unatokea wapi, hata hivyo nimewaita mabondia wote mjini hapa niweze kuzungumza nao," alisema Mwazoa.
Mwazoa alisema huenda wapinzani wake wanamfanyia hila pengine kwa kuona amekuwa kivutio kikubwa kwa mabondia kutokana na uhakika katika makubaliano na hata michezo anayoiandaa.
Mashali aliyemtwanga Japhet Kaseba hivi karibuni na kunyakua ubingwa wa UBO Afrika, atapambana na Nyilawila baada ya muda mrefu wa kila mmoja kumponda mwenzake kuwa hana ubavu wa kukabiliana naye kwenye ulingo.
Bondia huyo kwa sasa anauguza majeraha aliyoyapara kupoitia ajali aliyopata eneo la Kimara Suka wakati akiwa njiani kuelekea Tanga kuonana na promota huyo
Nyilawila aliwahi kuwa bingwa wa dunia wa uziato wa kati anayetambuliwa na WBF kabla ya kushindwa kwenyda kutetea taji lake hilo ili kuzipiga na Francis Cheka katika paambano la kirafiki mjini Morogoro na kudundwa.

Al Ahly yatinga ligi ya makundi Kombe la Shirikisho

Al Ahly ya  Misri
WALIOKUWA mabingwa wa Afrika, Al Ahly ya Misri imefuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho licha ya kunyukwa mabao 2-1 na Difaâ El Jadida  ya Morocco ikiungana na Sewe Sport ya Ivory Coast iliyoing'oa Bayelsa United ya Nigeria.
Bao la ugenini walilopata Al Ahly dhidi ya wenyeji wao liliisaidia kuivusha hatua hiyo baada ya matokeo ya jumla kuwa mabao 2-2, baada ya mchezo wao wa kwanza kupata ushindi wa bao 1-0.
Al Ahly waliyoiondosha Yanga kwenye raundi ya pili ya Ligi ya Mabingwa ya Afrika kabla ya kutolewa na Al Ahly Bengazhi na kutupwa kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.
Katika mechi nyingine Sewe Sport ya Ivory Coast iliifunga Bayelsa United ya Nigeria kwa bao 1-0 na kufuzu hatua ya makundi kwa jumla ya mabao 3-0 baada ya wiki iliyopita kushinda mabao 2-0.
Kinyang'anyiro cha michuano hiyo kinaendelea tena leo kwa michezo itakayozikutanisha Nkana Red Devils ya Zambia itakayokuwa ugenini dhidi ya Bizertin ya Tunisia, ambapo mechi yao ya awali iliisha kwa suluhu ya kutofungana.
Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini ambayo ilikung'utwa mabao 2-1 nyumbani na ASEC Memosa itakuwa Ivory Coast kujaribu kubadilisha matokeo dhidi ya wapinzani wao hao, nayo Coton Sport ikiwa na hazina ya ushindi wa mabao 2-1 iliyopata nyumbani dhidi ya Petro de Luanda itakuwa nchini Angola kuangalia wanatokaje ugenini.
Nazo timu za Léopards de Dolisié ya Jamhuri ya Kongo na Medeama ya Ghana zitapepetana Accra Ghana, huku wenyeji wakiwa nyuma kwa mabao 2-0, huku Etoile du Sahel ya Tunisia itakuwa nyumbani kuikaribisha Horoya ya Guinea walioshindwa kutambiana wiki iliyopita.
Mechi nyingine ya mwisho itazikutanisha timu za Real Bamako na 'ndugu' zao, Djoliba katika pambano lililozikutanisha timu za nchi moja ya Mali.
Katika mechi ya kwanza Real ilipata ushindi wa mabao 2-1 nyumbani na hivyo leo ikiwa ugenini itakuwa na kazi ya kulinda nafasi yake na kutinga hatua ya makundi ambayo kwa kawaida ina mamilioni ya fedha kutoka Shirikisho la Soka Afrika (CAF).

Ronaldo atuma salamu kwa Bayern Munich

Cristiano Ronaldo scores to put Real Madrid ahead against Osasuna
Ronadl alivyokuwa akiitesa Osasuna usiku wa jana
CRISTIANO Ronaldo ametuma salamu kwa mabingwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, Bayern Munich baada ya usiku wa jana kutupia kambani mabao mawili wakati Real Madrid ilipoizamisha timu ya Osasuna kwa mabao 4-0 katika Ligi Kuu ya Hispania.
Ronaldo ambaye amerejea tena dimbani toka kwenye majeraha, aliiongoza Madrid kupata ushindi huo mnono uliowasogeza karibu na mahasimu wao wa jiji la Madrid Atletico Madrid wanaongoza msimamo wa ligi hito katika uwanja wa Santiago Bernabeu.
Real Madrid keshokutwa itakuwa ugenini nchini Ujerumani kuumana na Bayern Munich katika pambano la marudiano la nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa baada ya wiki hii kupata ushindi wa bao 1-0 nyumbani, huku Ronaldo na Gareth Bale wakiwa hawapo fiti kama mechi yao ya jana dhidi ya Osasuna.
Mkali huyo alifunga bao la kwanza dakika ya sita kwa kazi nzuri ya Angel di Maria, bao lililodumu hadi kipindi cha kwanza kumalizika kabla ya kuongeza la pili katika dakika ya 52 akimalizia kazi ya Isco.
Bao la tatu lilifungwa na Sergio Ramos katika dakika ya 60 kwa kazi murua ya di Maria na Daniel Carvajal alimalizia udhia dakika saba kabla ya kumalizika kwa mchezo huo kwa kazi muru ya Isco na kuifanya Madrid kufikisha pointi 82, tatu nyuma ya Atletico inayocheza leo.
Katika mechi nyingine za ligi hiyo Elche ikiwa nyumbani ililazimishwa sare ya 1-1 na Levante siku ya Ijumaa wakati jana Granada ilipokea kipigo cha mabao 3-0 toka kwa wageni wao Rayo Vallecano, wakati Getafe ilishinda nyumbani bao 1 - 0 dhidi ya  Málaga.
Nayo timu ya Real Betis ikiwa uwanja wao wa nyumbani ilitandikwa bao 1-0 na Real Sociedad wakati leo ligi hiyo imeendelea leo kwa Espanyol ikiwa nyumbani kulazwa mabao 2-1 na Almería na baadaye   Valencia itaumana na vinara, Atletico Madrid, Athletic Club itaumana na Sevilla na Villarreal itaialika Barcelona kabla ya kesho Celta Vigo kupepetana na Real Valladolid.

Thursday, April 24, 2014

Yohan Cabaye ajiandaa kutwaa taji la pili la Ligi Ufaransa

http://i.dailymail.co.uk/i/pix/2014/01/31/article-2549777-1B1CA23300000578-208_634x471.jpgKIUNGO Yohan Cabaye nyota wa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Ufaransa PSG, Yohan Cabaye anajiandaa kunyakua taji lake la pili la ligi hiyo iwapo timu yake hiyo itapata ushindi katika pambano lao dhidi ya Sochaux litakalochezwa Jumapili.
PSG imebakisha pointi tatu tu kutetea taji hilo baada ya jana kupata ushindi mwembamba dhidi ya Evian TG na kuzidi kuikimbia Monaco, wapinzani wao wa karibu waliopo nafasi ya pili na waliowaacha kwa pointi 10 huku ligi ikisaliwa na mechi nne kabla msimu haujafungwa.
Cabaye aliyesajiliwa kwenye usajili wa majira ya baridi akitokea Newcastle United ya Uingereza anasema atakuwa mwenye furaha iwapo PSG itatwaa taji hilo ambalo kwake itakuwa ni mara ya pili baada ya kunyakua mara ya kwanza mwaka 2011 akiwa na Lille.
Mkali huyo anayeichezea pia timu ya taifa ya Ufaransa, anasema angependa kuongeza medali nyingine ya dhahabu katika chumba chake kupitia PSG.
"Tuna hamu kubwa ya kupata mafanikio ya kunyakua taji hilo na kitu hicho ni muhimu sana kwangu," alisema Cabaye, 28 na kuongeza; "Itakuwa vyema kama nitanyakua ubingwa huo nikiwa na PSG."
Mwishoni mwa wiki Cabaye alifanikiwa kunyakua Kombe la Ligi wakati PSG ilipoicharaza Olympique Lyon mabao 2-1 kwa mabao la Edinson Cavani na kudai ingawa hajawahi kunyakua Kombe la Ligi au Kombe la Mfalme mara mbili, lakini katika ligi anaamini itafanikiwa na anajiandaa kushangilia furaha ya ushindi huo anaousubiri kwa hamu.

Sturridge arejea,, Chelsea ikipanga kupumzisha nyota wake

http://www3.pictures.zimbio.com/gi/Daniel+Sturridge+Liverpool+v+Fulham+Premier+HI6EojIbLKll.jpg
Daniel Sturridge
http://i.dailymail.co.uk/i/pix/2013/03/06/article-2288964-09591184000005DC-339_306x423.jpg
Kocha wa Chelsea Jose Mourinho
 WAKATI kocha Jose Mourinho akidaiwa kutaka kuwapumzisha wachezaji wake nyota wake katika pambano lao la Ligi Kuu dhidi ya Chelsea ili kuitafutia kasi Atletico Madrid katika mechi ya nusu fainali ya marudiano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, wapinzani wao Liverpool wanachekelea kurejea kwa Daniel Sturridge.
Sturridge anategemewa kurejea kutoka katika majeruhi katika mchezo huo wa Jumapili ambao watakwaana na Chelsea.
Nyota huyo wa kimataifa wa Uingereza mwenye miaka 24 alikuwa akilalamika maumivu ya msuli katika ushindi wa mabao 3-2 waliopata dhidi ya Manchester City Aprili 13 hivyo kupelekea kutolewa nje. 
Toka apate majeruhi hayo alikosa mechi moja lakini sasa anategemewa kurejea tena uwanjani kuisaidia Liverpool katika mchezo huo muhimu ambao kama wakishinda utawafanya kuendelea kujikita kileleni hivyo kuweka hai matumaini yao ya ubingwa wa Ligi Kuu. 
Sturridge amesema kwa sasa anajisikia vyema na ni mategemeo yake atakuwepo katika mchezo huo wa Jumapili lakini itategemea kama kocha Brendan Rodgers atamchagua.
Katika hatua nyingine, Kocha wa Chelsea, Jose Mourinho amesema anataka kuwapumzisha nyota wake kwa ajili ya safari kwenda Anfield kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Liverpool Jumapili ijayo. 
Chelsea bado wako katika kinyang’anyiro cha taji la ligi wakiwa wamebakiwa na michezo mitatu lakini Mourinho anataka kuhamishia nguvu zake katika mchezo wa marudiano wa nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Atletico Madrid. 
Katika mechi yao ya kwanza iliyochezwa juzi, Chelsea iling'ang'aniwa na wenyeji wao Atletico kwa kutoka suluhu.
Hata hivyo, kocha huyo amesema uamuzi huyo wa kuwapumzisha baadhi ya nyota wake unaweza usiwe wa kwake kuufanya kwa sababu anataka kusikiliza na mawazo ya wengine. 
Kipigo cha mabao 2-1 walichopata Chelsea kutoka kwa Sunderland mwishoni mwa wiki iliyopita kinamaanisha hata kama wakishinda mchezo wa Anfield inaweza isitoshe kuizuia Liverpool kushinda taji la ligi baada ya kupita miaka 24.
Liverpool inaoongoza msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi 80, huku wapinzani wao waliopo nafasi ya pili wana pointi 75 moja zaidi ya ilizonazo Manchester City iliyo na mchezo mmoja zaidi ya timu hizo mbili za juu zilizocheza mechi 35.

Bomu jingine lalipuka Kenya

MATUKIO  ya kigaidi yamekua yakichukua vichwa vya habari mara nyingi nchini Kenya hasa baada ya nchi hiyo kupeleka wanajeshi wake nchini Somalia kupambana na wanamgambo wa kikundi cha kigaidi cha Al Shabaab.
Saa tatu na nusu usiku wa April 23 2014  bomu jingine limelipuka ndani ya gari karibu na kituo cha Polisi Nairobi.
Waziri wa mambo ya ndani amethibitisha kwa kusema Polisi wawili wamepoteza maisha kati ya watu wanne ambao wameuwawa huku hao wengine wawili wakihofiwa kuwa ni Mahabusu waliokuwemo kwenye gari hilo na Polisi.

Mhe Temba, Chegge Waueni sasa!

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEj0xQoDnodEV9YYagUy0z9ZP5UpB52s4xbJjVzKwckA9t_5NJAr8AiEwl5VLg4SNI0Eai2GGsmoYGrWg7xq_-dy-LFWWRWtAzTTh_YVzi9J0tS628PHayncwU1-X7JWpIpqp6zF5OQ5/s1600/Temba+and+Chege.jpgNYOTA wa muziki wa kizazi kipya wanaotoka kundi la TMK Wanaume Family, Chegge na Mhe Temba wanatarajia kuachia hewani wimbo wao mpya uitwao 'Waue' waliowashirikisha 'membaz' wa Mkubwa wa Wanawe.
Wasanii walioshirikishwa na wakali hao ni Maromboso na YP ambao nao wanatokea 'ukoo' wa TMK Wanaume Family na Mkubwa na Wanae.
Mkurugenzi wa Mkubwa na Wanawe na Meneja wa wasanii hao, Said Fella 'Mkubwa' aliiambia MICHARAZO kuwa, wimbo huo utaachiwa 'audio' na video wiki mbili zijazo baada ya kukamilisha baadhi ya mambo.
Mkubwa, alisema wimbo huo umerekodiwa katika studio zao za Mkubwa na Wanae chini na mtayarishaji, Shirko na video imefanywa na Adam Juma kupitia kampuni yake ya Visual Lab.
"Wasanii Temba na Chegge wamekamilisha kurekodi 'audio' na video ya wimbo wao uitwao 'Waue' wallioimba na Maromboso na YP, na tunapanga kuachia kazi hizo kwa pamoja wiki ijayo," alisema.
Chegge na Mhe Temba wamekuwa wakitoa kazi za pamoja mbali na zile za binafsi za kila mmoja nje ya nyimbo za kundi lao la TMK Wanaume Family.

Mashauzi, Sikinde kuwasindikiza Talent Band

http://4.bp.blogspot.com/-O6fGijIG-Xg/TpazwGlqCXI/AAAAAAAAAIQ/RB1Z12Ke5k8/s320/Hussin+Jumbe
Hussein Jumbe 'Mtumishi'

http://api.ning.com/files/QB639EYNFoD4efIjz*tu6A-tokrUhXrM*zilTmqFjwPaPBf8MRFVKag*kDP98VUlJn2dEoatnVAzlwDEnsygi3UIFRYdWmh1/MITIKISIKOYAPWANIDARLIVE16.JPG?width=650
Ishi Mashauzi atakayemsindikiza Hussein Jumbe na Talent Band
KUNDI maarufu la muziki asilia la Ngoma Afrika na kundi la muziki wa taarab la Mashauzi Classic, yanatarajiwa kupamba uzinduzi wa albamu mpya ya Talent Band utakaofanyika wiki ijayo jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na MICHARAZO, Mkurugenzi wa Talent Band, Hussein Jumbe alisema kuwa uzinduzi huo utafanyika Aprili 30 kwenye ukumbi maarufu Kisuma Night Park lililopo eneo la Temeke Mwembeyanga na watasindikizwa na makundi hayo mawili.
Jumbe alisema pia bendi yake ya zamani ya Mlimani Park 'Wana Sikinde' watakuwepo ukumbini kumpiga tafu kwenye uzinduzi huo wa aina yake.
"Natarajia kufanya uzinduzi wa albamu ya bendi yetu ya Talent iitwayo 'Kiapo Mara Tatu' na makundi ya Mlimani Park, Mashauzi Classic na Ngoma Afrika watanisindikiza siku hiyo pale Mwembeyanga," alisema.
Jumbe alisema kuwa, maandalizi ya uzinduzi huo unaendelea vyema na kuwataka mashabiki wa muziki wa dansi kujitokeza kupata burudani ambayo wameikosa kwa muda mrefu jijini Dar es Salaam.

Arsenal yaingia mbio za kumwinda van Gaal

http://www.101greatgoals.com/wp-content/uploads/2014/04/Louis-Van-Gaal-Bayern-Mun-001.jpg
Kocha van Gaal
 KLABU ya Arsenal imedaiwa kufanya mawasiliano na kocha Louis van Gaal, anayetajwa kuchukua mikoba ya David Moyes aliyetimuliwa na klabu ya Manchester United juzi.
Duru za kispoti zinasema kuwa, Arsenal imelazimika kuwasiliana na Mholanzi huyo kutokana na kutokuwa na uhakika na mustakabaliwa wa kocha wake Arsene Wenger. 
Hata hivyo Arsenal bado ina matumaini kuwa Wenger atasaini mkataba mpya wa miaka miwili waliokubaliana Octoba mwaka jana, lakini inajulikana anaweza kujiuzulu kama akishindwa kufikia malengo aliyojiwekea baada ya kumalizika kwa msimu. 
Imebainika kuwa Mfaransa huyo aliwaambia marafiki zake kuwa anafikiria kuacha kuinoa Arsenal kama awatashinda Kombe la FA na kumaliza katika nafasi nne za juu kwenye msimamo wa Ligi Kuu. 
Kutokana na hali hiyo kumekuwa na mipango ya muda mfupi inayofanywa na Arsenal, mojawapo ni kujaribu kufanya mazungumzo na Van Gaal ambaye mkataba wake na timu ya taifa ya Uholanzi unamalizika baada ya Kombe la Dunia.
Mbali na kuwindwa na Arsenal, kocha huyo pia amekuwa akitajwa kunyemelewa na klabu za Manchester United na Tottenham Hotspurs ambao nao wanataka achukue nafasi ya Tim Sherwood mwishoni mwa msimu huu.
Kocha huyo mwente rekodi za kuvutia amekuwa akiwania kutokana na uwezo wake wa kuwaongoza na kuwadhibiti wachezaji hata wale wakorofi. 

Januzaj aichagua Ubelgiji

http://i.huffpost.com/gen/1235023/thumbs/o-ADNAN-JANUZAJ-570.jpg?6
Januzaj
WINGA chipukizi wa klabu ya Manchester United, Adnan Januzaj ameamua kuiwakilisha Ubelgiji katika michuano ya soka ya kimataifa. 
Kocha wa timu ya taifa ya Ubelgiji, Marc Wilmots ametangaza katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa twitter amefurahishwa na uamuzi uliochukuliwa na mchezaji huyo. 
Januzaj amezaliwa jijini Brussels akiwa na wazazi wenye asili ya Kosovo na Albania na kujiunga na United mwaka 2011. 
Chipukizi huyo mwenye umri wa miaka 19 alikuwa na nafasi ya kuzichezea nchi za Kosovo, Albania, Turkey, Serbia na hata Uingereza lakini sasa anaweza kuwemo katika kikosi cha Ubelgiji kitakachoshiriki Kombe la Dunia. 
Kikosi kamili cha wachezaji 30 wa Ubelgiji kinatarajiwa kutajwa Mei 13 mwaka huu.

Kocha mpya Stars kutua nchini Jumamosi

http://www.clubofmozambique.com/pt/sectionnews/data/entretenimento/mart_nooij.jpg
Huyu ndiye kocha mpya wa Taifa Stars

 KOCHA Mkuu mpya wa Taifa Stars, Martinus Ignatius Maria maarufu kama Mart Nooij anatarajiwa kuwasili nchini Jumamosi alfajiri (Aprili 26 mwaka huu) tayari kwa ajili ya kuanza kazi ya kuinoa timu hiyo.
Nooij (59) atawasili saa 7.20 usiku kwa ndege ya Ethiopia Airlines ambapo anatarajia kukutana na waandishi wa habari Jumamosi mchana, saa chache kabla ya kuanza mechi ya kirafiki kati ya Taifa Stars na Burundi itakayochezwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mkenya kuzihukumu Stars na Intamba Murugamba

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjbouke40Ajpgip-WYtuNcSkslDTj7_vx1cW1lSk8TTr-VrfSpd48or2vfOoU95GSaeEPAw2h5x4McRiOOgSk6nbUS6SUXQKo3lzFQl3LThJA16UJsJRVH5TDtfBRQTKxdCPu8d59WboTi_/s400/waamuzi.jpg
Mwamuzi Ogwayo atakayezichezesha Stars na Intamba Murugamba
MWAMUZI Anthony Ogwayo mwenye beji ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kutoka Kenya ndiye atakayechezesha mechi kati ya Tanzania (Taifa Stars) na Burundi (Intamba Mu Rugamba) itakayochezwa keshokutwa (Aprili 26 mwaka huu)  Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Ogwayo katika mechi hiyo ya maadhimisho ya miaka 50 ya muungano wa Tanganyika na Zanzibar, atasaidiwa na Gilbert Cheruiyot na Oliver Odhiambo wote pia kutoka Kenya. Mwamuzi wa mezani atakuwa Israel Mujuni wa Tanzania.
Burundi inatarajia kuwasili nchini leo (Aprili 24 mwaka huu) saa 12 jioni kwa ndege ya Kenya Airways na itafanya mazoezi kesho (Aprili 25 mwaka huu) saa 10 jioni kwenye Uwanja wa Taifa.
Nayo Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ipo kambini jijini Dar es Salaam kujiandaa kwa mechi hiyo ambayo itakuwa ya kwanza tangu kuanza kwa mpango wa maboresho wa timu hiyo.
Makocha wa timu zote mbili pamoja na manahodha wao kesho (Aprili 25 mwaka huu) saa 5 asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) watakuwa na mkutano na waandishi wa habari kuzungumzia mechi hiyo.
Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani. Kwa VIP A kiingilio kitakuwa sh. 20,000 wakati VIP B na C ni sh. 10,000.

Zawadi za washindi Ligi Kuu Tanzania Bara zatangazwa

* Amissi Tambwe kuzoa Mil 5.2
* Azam kama bingwa kunyakua Mil 75
Mabingwa wapya wa Ligi Kuu Azam watakaozoa Mil 75
Tambwe wa Simba kajihakikishia Sh Mil 5.2
MSHAMBULIAJI Amisi Tambwe wa Simba atalamba Sh. milioni 5.2 za zawadi ya mfungaji bora zitakazotpolewa na wadhamini wakuu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, kampuni ya huduma ya simu ya Vodacom Tanzania baada ya kuibuka mfungaji bora wa msimu wa 2013/14 wa ligi hiyo.

Aidha, timu yenye nidhamu italamba Sh. milioni 16 ikiwa ni ongezekon la Sh. milioni moja ikilinganishwa na ilivyokuwa msimu uliopita.

Hayo yamebainishwa na Ofisa Uhusiano wa Nje wa Vodacom Tanzania, Salum Mwalim katika mkutano na waandishi wa habari muda mfupi uliopita kwenye ofisi za Makao Makuu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) zilizopo katikati ya Jiji la Dar es Salaam.

ZAWADI ZA WASHINDI LIGI KUU BARA 2013/2014
Bingwa: Sh. Milioni 75
Mfungaji Bora: Sh. Milioni 5.2
Timu yenye Nidhamu; Sh. Milioni 16
Kipa Bora: Sh. Milioni 5.2
Refa Bora; Sh. milioni 5.2
  Mwalim amesema mabingwa Azam FC watazawadiwa Sh. milioni 75 ikiwa ni ongezeko la Sh. milioni 5 ikilinganishwa na ilivyokuwa msimu uliopita.   Kipa bora, mwamuzi bora watapata Sh. milioni 5.2 kila mmoja ikikwa ni ongezeko la Sh. 200,000.Timu yenye nidhamu italamba Sh. milioni 16, ikiongezeka kutoka Sh. 15 ya msimu uliopita zilizochukuliwa na Yanga.   Silas Mwakibinga, Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu (TPLB), aliyekuwa amefuatana na Mwalim kwenye mkutano huo na waandishi wa habari, alisema tarehe ya kutolewa kwa tuzo hizo itatangazwa baada ya wiki moja.

Kivumbi Europa League kutimka leo Juve yaifuata Benfica

Juve itavuna nini leo Ureno
KIVUMBI cha Nusu Fainali  ya Ligi Ndogo ya Ulaya (UEFA Europa League) kinatarajiwa kutimka usiku wa leo wakati timu nne zilizotinga hatua hiyozitakapopepetana kwenye viwaja viwili tofauti.
Klabu za Sevilla na Valencia zote kutokea Hispania zilizopangwa kucheza pamoja zitakutana kwa mara ya kwanza katika hatua hiyo, wakati mabingwa wa Italia Juventus watakwaruzana na Benfica ya Ureno katika mechi zinazotarajia kuwa na msisimko wa aina yake.
Valencia na Sevilla ambazo zilipindua matokeo yao ya awali walipolazwa ugenini na kushinda nyumbani kwa idadi kubwa ya mabao dhidi ya Porto na Basel zinakutana kwa mara ya kwanza kwenye michuano ya Ulaya.Mechi za mkondo wa kwanza baina ya timu hizo mbili itaanziua nyumbani kwa Sevilla kabla ya wiki ijayo kuwafuata wapinzani wao hao.
Timu zote mbili zimewahi kunyakua taji hilo kwa vipindi tofauti, Sevilla mara mbili mfululizo mwaka 2006 na 2007 na wenzao walitangulia mwaka 2004.
Juventus itakayokuwa ugenini ilishawahi kunyakua taji hilo mara tatu mwaka 1977, 1990 na 1993 na ingependa kufanya kweli katia michuano ya mwaka huu baada ya ndoto zao na kutamba Ligi ya Mabingwa Ulaya kukwama na kutolewa kwenye hatua ya 16 Bora.
Waitalia hao wanaoelekea kutetea taji lao la Seria watakutana na Benfica ambao hawajawahi kunyakua taji hilo la Europa, ingawa mkononi tayari wana taji la ligi kuu ya nchi yao ya Ureno.
Ikitamba na nyota wake kama Carlos Tevez, Andre Pirlo, Paul Pogba na wengine Juventus itahitaji ushindi ugenini ili mchi yao ya marudiano wilki ijayo iwe nyepesi ingawa watarajie kupata upinzani mkali kwa mabingwa hao wa Ureno inayotambia wakali wake kama Lima kutoka Brazil., Rodrigo, Cordozo, na Andre Gomes

Real Madrid yaizima Bayern Munich, ila kazi wanayo ugenini

Benzema (9) akishangiulia bao lake pekee lililoizamisha Bayern Munich
MABINGWA watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, Bayern Munich imekubali kichapo cha bao 1-0 toka kwa wenyeji wao Real Madrid katika mechi ya mkondo wa kwanza ya Nusu fainali ya pili ya michuano hiyo iliyochezwa usiku wa kuamkia leo mjini Madrid -Hispania.
Baoa pekee la dakika ya 19 ya mchezo lililotumbukizwa kimiani na Karim Benzema lililitosha kuwapa wenyeji ushindi huo mwembamba kwenye uwanja wa Santiago Bernabeu.
Katika mchezo huo ilishuhudiwa wachezaji ghali wa klabu ya Real Madrid wanaodaiwa kuwa wagonjwa kupishana katika kipindi cha pili na kuwapa faraja vijana wa Carlo Ancelotte kupumua kabla ya wiki ijayo kurudiana na Wajerumani hao waliopoteza bafasi kadhaa za kufunga katika mechi hiyo.
Real Madfrid itakabiliwa na kazi nzito katika mchezo wa marudiano ili kulinda ushindi huo na kuvuta unyonge wa kutolewa mara katika hatua hiyo na wapinzani wao hao.