STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, November 12, 2011

Bundi wa Sikinde kupelekwa Studio

BENDI kongwe za muziki wa dansi nchini, Mlimani Park 'Sikinde' ipo mbioni kuingiza studio kibao kipya cha 'Bundi', ikiwa katika harakati za kufyatua albamu mpya itakayokuwa na nyimbo sita.
Kibao hicho kipya kimetungwa na Abdalla Hemba, mmoja wa waimbaji mahiri wa bendi hiyo ambayo kwa sasa inatamba na wimbo wa 'Jinamizi la Talaka', kinachodaiwa ni 'dongo' kwa mahasimu wao, Msondo Ngoma wanaotamba na kibao cha 'Suluhu'.
Mmoja wa viongozi wa Sikinde, Hamis Milambo, alisema kibao cha 'Bundi', kitarekodiwa wakati wowote kuanzia sasa sambamba na vingine vitakavyokuwa katika albamu yao mpya.
Milambo alisema mbali na Jinamizi la Talaka na Bundi, nyimbo nyingine za albamu hiyo zilizokamilika ni 'Asali na Shubiri' uliotungwa na Shukuru Majaliwa, 'Nitalipa Deni', uliotungwa na bendi mzima ya Sikinde, 'Kilio cha Kazi'-Hassani Bitchuka na 'Nisamehe'-Hemba.
Wakati Sikinde wakijiandaa kuhitimisha albamu yao hivyo, kwa upande wa mahasimu wao, Msondo Ngoma wameibuka na kibao kingine kipya kiitwacho 'La Kuvunda' utunzi wa mkali Shaaban Dede 'Mzee wa Loliondo' ambaye anatamba pia na kibao kiitwacho 'Suluhu'.
Msondo ambao wameanza kurekodi nyimbo zao mpya kwa ajili ya albamu yao mpya, imeachia kibao hicho kipya ikiwa ni maandalizi ya albamu ya mwaka ujao.
Albamu yao ya sasa wanaotarajia kuiingiza sokoni mara itakapokamilika kurekodiwa inatarajiwa kufahamika kwa jina la 'Nadhiri ya Mapenzi' ambayo ni jina la kibao kilichotungwa na Juma Katundu.
Nyimbo nyingine za albamu hiyo na watunzi wake kwenye mabao ni 'Kwa Mjomba Hakuna Urithi (Huruka Uvuruge), Dawa ya Deni (Is'haka Katima 'Papa Upanga), LIpi Jema na Baba Kibene za Edmund Sanga 'Eddo Sanga' na 'Suluhu' (Shaaban Dede).

Mwaikimba aahidi ubingwa Azam






SIKU moja tangu amwage wino wa kuichezea Azam kwa mechi za duru la pili la Ligi Kuu
Tanzania Bara, Mshambuliaji Gaudence Mwaikimba 'Andy Carroll' ameahidi kuipigania klabu hiyo ili iwe bingwa mpya wa soka nchini.
Mwaikimba aliyekuwa akiichezea Moro United, aliyotua mapema msimu huu akitokea Kagera Sugar, alisema anaamini ana deni kubwa la kulipa fadhila ya kuaminiwa na klabu ya Azam kiasi cha kumsajili, ila atakachofanya yeye ni kushirikiana na wenzake kuipa ubingwa msimu huu.
"Kwangu ni furaha kubwa kutua Azam, moja ya klabu zenye malengo na muono wa mbali
katika soka la Tanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla. Wajibu wangu kama mchezaji ni kuhakikisha naipigania ifanye vema ikiwemo kuwa mabingwa wapya nchini," alisema.
Mshambuliaji huyo anayeshikilia nafasi ya pili katika orodha ya wafungaji mabao msimu huu, alisema kwa vile karibu wachezaji anayeenda kukutana nao Azam amewahi kucheza nao katika klabu mbalimbali na timu ya taifa, Taifa Stars hana hofu ya kuelewana nao mapema.
"Kwa mfumo wa soka letu toka klabu moja hadi nyingine kufanana, naamini itanichukua
muda mfupi kuzoeana na wenzangu na kubwa nalopenda kuwaahidi mashabiki wa Azam
kwamba watarajie mambo makubwa katika duru lijalo," alisema.
Kuhusu suala la uhakika wa namba kwa nafasi anayocheza ambayo tayari ndani ya Azam
inayo wachezaji nyota kama John Bocco, Mwaikimba alisema hana tatizo lolote kwa vile
anajiamini yeye ni mchezaji mzuri na mwenye uwezo mkubwa ndio maana amesajiliwa Azam.
Nyota huyo aliyewahi kuwika na klabu za Tukuyu Stars, Yanga, Ashanti United na Prisons Mbeya ni mmoja wa wachezaji wapya waliotua Azam ambayo imewatema wachezaji wao wawili wa kimataifa kutoka Ghana, Wahabu Yahya na Nafiu Awudu.
Mwingine aliyesajiliwa Azam katika dirisha hilo dogo ni beki wa zamani wa kimataifa wa Simba, Joseph Owino na huku mshambuliaji Jerry Tegete wa Yanga ni miongoni mwa
wanaowindwa na klabu hiyo.

Thursday, October 20, 2011

Filamu ya CPU kuzinduliwa rasmi Novemba 24




FILAMU mpya ya kisasa ya CPU, iliyowashirikisha wasanii nyota nchini kama Sauda Kilumanga, Dotnata Posh, Masinde, Dude na wengineo inatarajiwa kuzinduliwa rasmi Novemba 24 kwenye ukumbi wa New World Cinema, Mwenge.
Mratibu wa filamu hiyo, Evance Bukuku, alisema CPU ambayo ni kifupi cha maneno Children Protection Unity (Kitendo cha Kuwalinda Watoto), imetengenezwa na kampuni ya Haak Neel Production ikishirikisha wasanii zaidi ya 150.
Bukuku, alisema filamu hiyo iliyorekodiwa kwa teknolojia ya kisasa kwa kutumia helkopta baada ya kuzinduliwa Novemba 24, itaanza kuonyesha eneo la Mlimani City kwa muda wa wiki moja kwa kiingilio kitakachotangazwa baadae.
"Filamu yetu ya CPU ambayo imewashirikisha wahusika wakuu wanne na wasaidizi 30, itazinduliwa Novemba 24 mwaka huu kabla ya kuanza kuonyesha kwenye juumba la sinema la Mlimani City kwa wiki moja kuanzia Novemba 25- Desemba 2," alisema.
Aliongeza baada ya maonyesho hayo, kampuni yao inafanya mipango ya kwenda kuionyesha bure filamu hiyo inayozungumzia masuala mbalimbali yanayopingana na unyanyasaji na ukatili wa watoto pamoja na matendo mengine ya kihalifu.
Bukuku aliitaja mikoa itakayoenda kuonyesha filamu hiyo bure ni Mwanza, Arusha, Dodoma, Dar, Mbeya na Zanzibar.
Baadhi ya washiriki wa filamu hiyo, Steven Singh Sandhu na Sauda Kilumanga waliiambia MICHARAZO kuwa, kile ambacho watanzania walikuwa wakikisubiri kwa muda mrefu katika tasnia ya filamu sasa wamekipata kupitia filamu hiyo ya CPU.
"Ni filamu bab kubwa, ikiwa imetengenezwa kwa kiwango cha hali ya juu na ni moja ya filamu yenye uhalisi na ujumbe maridhawa kwa jamii, kitu ambacho kabla ya hapo haikuwahi kutokea," alisema Sandhu maarufu kama Salvador au .The Pride'.
Naye Sauda alisema kama mhusika mkuu katika filamu hiyo ameonyesha namna gani jamii ikishirikiana inaweza kutatua matatizo yanayowakabili watoto vikiwemo vitendo vya kikatili na uhalifu mwingine.

Belle 9, Godzilla kupamba Miss Utalii Dodoma

WASANII nyota wa muziki wa kizazi kipya nchini, Belle 9 na Godzilla wanatarajiwa kupamba shindano la kumsaka mrembo wa utalii wa Dodoma, Miss Utalii Dodoma litakalofanyika wiki ijayo mjini Dodoma.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamati ya Miss Utalii Tanzania kupitia Rais wake, Gideon Chipungahelo, shindano hilo litafanyika kwenye ukumbi wa Club La Aziz siku ya Oktoba 29.
Taarifa hiyo inasema, shindano hilo ambalo ni muendelezo wa kusaka wawakilishi wa mikoa kwa ajili ya fainali za taifa za kumsaka Miss Utalii Tanzania 2011-2012 litakalofanyika mapema mwakani.
Chipungahelo, alisema shindano hilo litapambwa na burudani mbalimbali ikiwemo
la wasanii wa kizazi kipya wanaotamba katika miondoko ya R&B na hip hop, Belle 9, Godzilla, na vikundi vya ngoma asilia kikiwemo Yangeyange Arts cha Dodoma.
"Shindano la Miss Utalii Dodoma, linatarajiwa kusindikizwa na burudani za wasanii Belle 9, Godzilla na vikundi vya ngoma asilia. Maandalizi kwa ujumla yapo vema kwa nia ya kulinogesha shindano hilo," Chipungahelo alisema katika taarifa hiyo.
Tayari wadhamini mbalimbali wamejitokeza kwa nia ya kulidhamini shindano hilo ambalo mbali na kusaka kisura wa mkoa, pia itatoa wawakilishi wa kushiriki shindano la taifa litakalofanyika mwakani ambalo litrahusisha washiriki toka mikoa na kanda tofauti.

Mwisho

Sare zatawala daraja la Kwanza, Polisi Dar, Mbeya City moto

MECHI za raundi ya pili ya Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara, zimetawaliwa na 'mdudu' wa sare baada ya michezo minne kati ya sita iliyochezwa jana kutoa matokeo hayo katika mikoa tofauti.
Katika mechi hizo nne, Rhino Rangers ya Tabora ililazimishwa sare ya 1-1 na AFC Arusha, huku Manyoni Fc na Polisi Morogoro zilishindwa kutambiana kwa kutofunga katika mechi za kundi C.
Katika mechi za kundi A, TMK United na Transit Camp zilitoshana nguvu kwa kutofungana katika pambano lililochezwa Mkwakwani Tanga, , sawa na ilivyokuwa kwa mchezo wa kundi hilo kati ya Morani- Manyara dhidi ya wageni wao JKT Mgambo ya Tanga.
Mechi pekee ya kundi hilo la A lililotoa ushindi ni ile ya Polisi Dar es Salaam iliyoifunga Burkina Faso mabao 5-3 kwenye uwanja wa Mabatini-Mlandizi, na kuwafanya 'maafande' hao maarufu kama 'Vijana wa Kova' kujikita kileleni mwa kundi hilo.
Timu hiyo ya Polisi Dar inaongoza kundi hilo ikiwa na pointi sita, mabao sita ya kufunga na kufungwa mabao matatu, ikifuatiwa na Polisi Morogoro yenye pointi nne.
Katika pambano jingine lililotoa ushindi kwa mechi hizo za juzi ni kati ya timu ya Jiji la Mbeya, Mbeya City iliyoilaza JKT Mlale ya Ruvuma mabao 3-1 na kujikita kileleni mwa kundi hilo ikiwa na pointi sita na mabao manne ya kufunga.
Mechi nyingine za kundi hilo la B zinatarajiwa kuchezwa leo ambapo timu ya Small Kids itaikaribisha mjini Morogoro, Prisons ya Mbeya, huku Majimaji Songea itaumana na Polisi Iringa mjini Songea, na timu za 94 KJ na Polisi Tabora zitaumana katika kundi C kwenye pambano litakalochezwa uwanja wa Mabatini-Mlandizi.
Ligi hiyo inashirikisha jumla ya timu 18 ambazo zinawania nafasi tisa za kucheza hatua ya pili ya fainali za ligi hiyo ili kusaka timu nne za kupanda Ligi Kuu msimu ujao.

Pambano la Maugo, Odhiambo laiva Mwanza



BONDIA mchachari wa ngumi za kulipwa nchini, Mada Maugo, amesema maandalizi ya pambano lake dhidi ya Mkenya, Joseph Odhiambo litakalofanyika keshokutwa, yamekamilika ikiwemo kutarajia kumpokea mpinzani wake kesho jijini Mwanza.
Maugo na Odhiambo wanatyarajia kuonyesha katima katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 uzani wa middle, litakalosindikizwa na mabondia wakongwe nchini Joseph Marwa na Rashidi Matumla, ambalo litafanyika Jumapili uwanja wa CCM -Kirumba.
Akizungumza na MICHARAZO kwa njia ya simu toka kwenye kambi yake mjini humo, Maugo, alisema mpinzani wake anatarajia kutua jijini Mwanza kesho tayari kwa ajili ya kupima uzito siku ya Jumamosi kabla ya kupanda ulingoni Oktoba 23.
Maugo, alisema pia ameshamalizana na wasanii watakaosindikiza pambano hilo ambalo lengo lake ni kuhamasisha na kuendeleza mchezo wa ngumi katika mikoa ya Kanda ya Ziwa.
"Maandalizi ya pambano langu dhidi ya Mkenya Joseph Odhiambo yanaendelea vizuri na nawaomba mashabiki wajitokeze kwa wingi siku ya Jumapili kuweza kushuhudia mpambano huo na yale yatakayotusindikiza," alisema Maugo.
Maugo alisema miongoni mwa mapambano yatakayowasindikiza ni lile la Rashid Matumla dhidi ya Emma Kichere wa jijini Mara na Joseph Marwa atakayepigana na Chuku Dusso., huku Marwa atapigana na Chuku Duso.
"Emma Kichere ni bondia chipukizi wa mkoa wa Mara atazipiga na Matumla na Marwa atapigana na Chuku Duso anayetoka mkoa wa Mwanza, ndipo mimi na Odhiambo tutapanda ulingoni kuhitimisha michezo ya siku hiyo,' alisema Maugo.
Maugo alisema wasanii watakaosindikiza pambano lao ni H-Baba, Dudu Baya na wengine chipukizi ambao wanatokea mikoa hiyo ya Kanda ya Ziwa.
Pambano hilo la Jumapili kwa Maugo ni maalum kwa ajili ya kujiandaa na mchezo wa kimataifa dhidi ya Mjerumani, atayechuana nae kuwania mkanda wa IBF.

Mwisho

Kamanda Kova kushuhudia Mbwana, Miyeyusho wakipigana Diamond Jubilee

WAKATI Mbwana Matumla 'Golden Boy' na Francis Miyeyusho 'Chichi Mawe' wakianza kutupiana 'madongo' juu ya pambano lao la kuwania mkanda wa Mabara wa UBO, Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika pambano hilo.
Mratibu wa pambano hilo la kuwania ubingwa wa Mabara wa UBO, litakalochezwa Oktoba 30, Mohammed Bawazir wa Dar World Link, alisema Kova ndiye atakayemvisha taji mshindi wa mchezo huo.
Bawazir, alisema kamanda Kova ambaye ni Mlezi wa mchezo wa ngumi nchini, amekubali mualiko wa pambano hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
"Maandalizi ya pambano la Mbwana Matumla atakayetetea taji lake la UBO -Inter Continental dhidi ya Francis Miyeyusho yanaendelea vema ikiwemo Kamanda Kova kukubali kuwa mgeni rasmi wa mchezo huo," alisema.
Mratibu huyo alisema kala ya wababe hao kupanda ulingoni yatafanyika mapambano mengine matano ya utangulizi likiwemo litakalowakuanisha mabondia wakike, Asha Ngedere na Salma Kiobwa.
Pambano jingine ni la kuwania ubingwa wa taifa wa PST kati ya Juma Fundi na Fadhil Majiha.
Wakati maandalizi yakiwa hivyo Mbwana na Miyeyusho kila mmoja kwa wakati wake jana amejitapa kuibuka na ushindi katika pambano hilo litakalokuwa la raundi 12 la uzani wa Bantam.
Miyeyusho alisema amejiandaa kumvua taji Matumla, licha ya kutambua ni bondia mzuri asiyetabirika.
"Niko fiti kwa ajili ya kushinda pambano hilo, sina wasiwasi, ila naomba mashabiki wake kushuhudia ninavyompiga Mbwana kwa KO," alisema.
Mbwana mwenyewe, alisema hana maneno mengi kwani anaamini yeye ndiye bingwa na haitakuwa rahisi kwake kukubali kupokwa taji lake na Miyeyusho.
"Mie sina maneno, nimezoea kutekeleza mabmbo kwa vitendo hivyo mashabiki wangu waje ukumbini kuona nitafanya nini, ila siwezi kukubali taji langu ya UBO liniondoke," alisema.
Mabondia hao watakutana katika pambano la tatu baina yao, ambapo mara mbili za mwanzo walipokutana Februari 21, 2004 na Januari 17, 2009, Mbwana aliibuka na ushindi kitu ambacho Miyeyusho amedai hakubali kupigwa tena katika mchezo huo wa Oktoba 30.

Mwisho

Ferguson awatoa hofu mashabiki Extra Bongo


RAPA nyota wa bendi ya Extra Bongo, Saulo John 'Ferguson' amewatoa hofu mashabiki wa bendi hiyo, juu ya taarifa kwamba yupo mbioni kuiacha na kurejea alipotoka.
Ferguson, ambaye ni mtunzi na muimbaji aliyetua Extra Bongo mapema mwaka huu akitokea African Stars 'Twanga Pepeta', alisema taarifa zilizosambazwa kwamba yupo mbioni kuondoka katika bendi hiyo ni uzushi wenye nia ya kumharibia.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, rapa huyo aliyewahi kuzifanyia kazi Double Extra, Majahazi ya Zanzibar, Mchinga G8 'Timbatimba' na Extra Bongo 3x3, alisema wadau wa bendi yake wasiwe na hofu, kwani hana mpango wa kuondoka.
"Sina mpango wa kuondoka na wala sijawahi kuwaza kufanya hivyo kwa sababu ni vigumu niache embe bivu nililonalo na kulifuata bichi kwingine," alisema bila kufafanua.
Alisema, uzushi wa yeye kutaka kuondoka zilitolewa wakati akiwa ziarani mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na bendi yake na kumfanya alazimike kuitisha mkutano huo ili kutoa ufafanuzi, kuwaondoa shaka wadau wa bendi hiyo wanaoweza kumfikiria vibaya.
"Nimepata usumbufu mkubwa kwa mashabiki na familia yangu wakiniona sina utulivu, ndio maana nimewaita ili kuweka bayana kwamba taarifa za mtaani uzushi unaoenezwa na watu wasionitakia mema," alisema.
Aliongeza kuwa, kuthibitiha kuwa 'yupo sana' Extra Bongo, amewaandalia mashabiki hao rapu mpya iitwayo Mdudu ambayo itawashindanisha mashabiki hao katika maonyesho yao ambapo mshindi atajinyakulia runinga ya inchi 24.
"Nimekuja na rapu mpya iitwayo mdudu, ili kuonyesha nipo sana Extra Bongo na kuzima uzushi huo kwamba natarajia kurejea nilipotoka," alisisitiza.
Wakati huo huo, Kiongozi wa Extra Bongo, Rogart Hegga 'Catapillar' ameeleza ziara yao mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, ilikuwa ya mafanikio na kuonyesha namna gani bendi yao inavyokubalika, huku wakiwapongeza wakazi wa mikoa hiyo kwa mapokezi waliyowapoa.
Hegga, alisema bendi yao iliyorejea jijini Dar juzi, imewafanya waamini malengo waliyojiwekea ya kuteka soko la muziki wa Tanzania, linaelekea kufanikio na kuwaomba mashabiki wao kuzidi kuwaunga mkono.

Mwisho

Friday, September 30, 2011

Msondo yaingia studio kurekodi albamu mpya



BENDI kongwe ya Msondo Ngoma, mapema leo asubuhi imeingia studio kurekodi kibao kipya kiitwacho 'Suluhu', ikiwa ni maandalizi ya upakuaji wa albamu yao mpya.
Mmoja wa viongozi wa bendi hiyo, Shaaban Dede, aliiambia MICHARAZO kuwa, nyimbo zao mpya zitarekodiwa katika studio za Fabreas Records na kwa kuanza leo anarekodi kibao cha 'Suluhu', ambacho amekitunga yeye.
Dede, alisema mara baada ya kibao hicho kurekodiwa kitasambazwa kwenye vituo vya redio kwa nia ya kukitambulisha huku, bendi yao ikiendelea kumalizia nyimbo nyingine tano zilizosalia.
"Tumeingia leo studio kwa Fabreas kwa lengo la kufyatua kibao cha Suluhu na vingine kwa ajili ya albamu yetu mpya ijayo," alisema Dede.
Alisema nyimbo nyingine za albamu hiyo ambazo zimeshakamilika ni 'Dawa ya Deni', 'Lipi Jema', 'Kwa Mjomba Hakuna Urithi', 'Baba Kibene' na 'Nadhiri ya Mapenzi'.
"Nadhani muda si mrefu mashabiki wetu na wale wa muziki kwa ujumla wataipata albamu yetu, kwani tutakuwa tukidondosha wimbo mmoja mmoja, kabla ya kuikamilisha na kuiachia mtaani, kabla ya kumalizika mwaka huu," alisema.
Msondo Ngoma imekuwa na desturi ya kutoa albamu kila mwaka, ila kwa mwaka jana haikuachia kazi yoyote, albamu yao ya mwisho ni ile ya mwaka juzi iitwayo 'Huna Shukrani'.

Siwezi kuchojoa nguo nicheze X-Skyner



MSANII wa filamu anayekuja juu nchini, Skyner Ally, amesema hata apewe kiasi gani cha fedha hawezi kucheza picha za watu wazima 'X' kwa madai kufanya hivyo mbali na kujidhalilisha, pia ni kwenda kinyume na mafundisho ya Mungu.
Akizungumza na MICHARAZO, Skyner, alisema ingawa yupo ndani ya fani ya uigizaji kwa nia ya kusaka fedha, lakini hayupo tayari kujivua utu wake, ili akubali kuchojoa nguo na kuigiza filamu za X.
Skyner, alisema anaamini kucheza filamu za namna hiyo ni kwenda kinyume na maadili na kukiuka mafundisho ya dini, mbali na yeye mwenyewe kujidhalilisha mbele ya jamii.
"Ingawa nasaka fedha kupitia kipaji cha uigizaji nilichonacho, lakini siwezi kukubali kucheza filamu za X hata nikiahidiwa kiasi gani cha fedha," alisema.
Kisura huyo, anayetamba kwenye filamu kama 'The Second Wife', 'Unpredictable', 'What is It', 'I hate My Birthday', 'Why I Did Love', 'Kizungumkuti' na nyinginezo, alisema kuwa msanii hakuna maana kujirahisisha na kufanya mtendo machafu, jambo alilolata wasanii wenzake kuepukana nayo ili kulinda heshima zao na fani zao kwa ujumla.
"Wasanii lazima tujiheshimu na kujithamini, kujiingiza kwenye skendo na matendo machafu ndiyo yanayotufanya tusiheshimike na kuichafua fani nzima ya sanaa, wakati imekuwa ikitusaidia baadhi yetu kumudu maisha na kuzisaidia familia zetu," alisema.
Skyner, anayetarajiwa kuolewa wiki ijayo, alisema wasanii wakijiheshimu na kuepuka skendo ni wazi jamii itawapenda na kuwathamini, hasa kama watajibidiisha kuboresha kazi zao.

Yanga sasa roho kwatu!


USHINDI mnono wa mabao 5-0 iliyopata kwa Coastal Union, umewafanya wadau wa klabu ya Yanga kuchekelea wakisisitiza kuwa hawana hofu ya kutetea taji lao msimu huu.
Yanga iliyokuwa ikichechemea katika ligi hiyo, iliishindilia Coastal mabao hayo katika pambano lilkilochezwa uwanja wa Taifa, na kuipandisha mabingwa watetezi hao hadi kwenye nafasi ya nne nyuma ya timu za Simba, Azam na JKT Oljoro zilizoitangulia.
Afisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu, alisema wanaamini ushindi waliopata kwa Wagosi wa Kaya ni salamu kwa watani zao na timu nyingine zilizokuwa zikiikejeli timu yao ilipoanza kwa kusuasua katika ligi hiyo.
Sendeu, alisema tangu awali walikuwa wakisisitiza kuwa, ligi bado mbichi na vigumu watu kuitabiria Yanga kwamba haiwezi kufurukuta msimu huu, bahati nzuri imethibitika kwa ushindi mfululizo ambao umewafanya wapinzani wao kuanza 'kuhema'.
Alisema anaamini mapumziko ya ligi kupisha pambano la Stars na Morocco itatumiwa vema na benchi lao la ufundi pamoja na wachezaji wao kuhakikisha wakirejea dimbani wanakuwa moto zaidi, ili kumaliza duru la kwanza katika nafasi stahiki.
"Nadhani waliokuwa wakitukejeli kwamba tumefulia, salama wamezipata na ninajua huko walipo presha zimeshaanza kuwapata, tunaombea tuendelee na mwendo huu huu ili tumalize duru la kwanza katika nafasi mbili za juu na kujiweka vema kulitetea taji letu," alisema.
Nao baadhi ya wadau wa klabu hiyo, wamedai pamoja na kuanza kuonyesha mwanga kwa timu yao, bado wachezaji hawapaswi kubweteka na badala yake waongeze juhudi ili kumaliza meechi tano zilizosalia kwa mafanikio.
"Tumefurahi mafanikio ya timu yetu, lakini naomba wachezaji na viuongozi wasibweteke, tuendelee kushinda mechi zijazo ikiwemo ile ya Simba Oktoba 29, ili turejeshe heshima yetu iliyopotea kwa matokeo mabaya ya mechi za awali," alisema Ramadhani Kampira.
Yanga kabla ya kuvaana na Simba katika pambano linalosubiriwa kwa hamu, itacheza na timu za Kagera Sugar, Toto Afrika na JKT Oljoro kabla ya kufunga dimba la duru la pili kwa kuumana na Polisi Dodoma mjini Dodoma Novemba 5.

Stewart ruksa kuinoa Zanzibar Heroes


UONGOZI wa klabu ya soka ya Azam, umekubali kwa moyo mmoja uteuzi wa kocha wao mkuu, Stewart Hall, kuinoa timu ya taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes kwa ajili ya michuano ya Kombe la Chalanji itakayofanyika Novemba, jijini Dar es Salaam.
Chama cha Soka Visiwani Zanzibar, ZFA, kilimtangaza Stewart kuwa ndiye atakayeinoa timu hiyo katika michuano hiyo, ikiwa ni mara ya pili kwa kocha huyo kupewa kibarua hicho cha kuinoa Zanzibar Heroes.
Katibu Mkuu wa Azam, Nassor Idrissa 'Father', alisema uongozi wao, hauna tatizo la kocha wao kwenda kuinoa Zanzibar Heroes, kutokana na ukweli kwa namna moja ni faida kwa Azam ambayo hutoa wachezaji wengi katika kikosi cha timu hiyo.
Idrissa, alisema pia kocha huyo ataenda kuinoa timu hiyo wakati klabu yao itakuwa imeshawapa likizo wachezaji wao kwa ajili ya mapumziko marefu kabla ya kuanza kwa duru la pili la ligi hiyo mapema mwakani.
Katibu huyo alisema pia ni vigumu kwa Azam kumzuia kocha huyo kwenda kutekeleza jukumu lake kwa timu ya taifa, ambayo ni sehemu ya Muungano wa Tanzania, labda kama angeteuliwa kwenda kuinoa Kenya au Uganda ndio wangweka pingamizi.
"Angekuwa ameteuliwa kuinoa Kenya au Uganda, hapo ingekuwa vigumu kumruhusu lakini kama ni Zanzibar au hata kama ingekuwa Tanzania Bara, tungemruhusu kwa vile ni faida kwa maendeleo ya soka letu, kwani Stewart ni kocha mzuri," alisema.
ZFA, ilisema kocha huyo angeungana na timu hiyo ya taifa, Novemba 10, siku tano baada ya duru la kwanza la ligi kuu kumalizika.
Kabla ya kutua Azam, Stewart anayetokea Uingereza aliletwa nchini kuinoa timu hiyo ya Zanzibar kupitia kampuni ya Future Century.

Skyner: Kisura anayetishia mastaa wa kike Bongo Movie





NI muda mfupi tangu Skyner Ally Seif, ajiingize kwenye fani ya uigizaji, ila tayari amekuwa na jina kubwa kutokana na umahiri aliouonyesha kupitia kazi alizoshiriki.
Mbali nba umahiri wa kisanii, pia mvuto wa sura na umbile vimemfanya msanii huyo, awe miongoni mwa wasanii wa kike wanaotamba nchini kwa sasa.
Sykner alikiri, licha ya kuwa na kipaji cha sanaa tangu utotoni, hakupata fursa ya kukionyesha hadi mwaka jana alipoibuliwa na Vincent Kigosi 'Ray' kupitia filamu ya 'The Second Wife'.
Alisema kabla ya 'shavu' la Ray, alishacheza kazi nyingine kama 'Mtumwa wa Mapenzi' na 'Johnson' ambazo hazikumtangaza sana.
Kazi nyingine alizoshiriki mara alipoibuliwa na Ray, ni 'What is It', 'Why I Did Love', 'I Hate My Birthday', 'Kizungumkuti', 'Unpredictable' na nyingine.
Skyner anayejiandaa kuolewa Ijumaa ijayo, alizaliwa mwaka 1992 jijini Dar, akiwa mtoto wa pili wa familia ya watoto watatu, alihitimu masomo ya sekondari Shule ya Cambridge, ya jijini Dar.
Nyota huyo, anayependa biriani na kunywa fanta, alisema licha ya kuwepo kwenye sanaa kwa muda mfupi, fani hiyo imemnufaisha mengi, akiota kuja kutamba kimataifa na mtayarishaji na muongozaji bora, akimiliki kampuni yake binafsi.
Kisura huyo, hutumia muda wake wa ziada kumuomba Mungu na kulala, pia ni shabiki wa
muziki akihusudu miondoko ya Arabian.
Juu ya madai ya rushwa na ngono katika sanaa, Skyner alikiri ni kweli amewahi kusikia, ila yeye hajawahi kukumbana nayo.
Ila, alisema wasanii wanaoombwa rushwa hiyo wana uhuru wa kukataa kwa kuringia vipaji vyao badala ya kujirahisisha na kudhalilika.
Skyner aliyewafiwa na wazazi wote mwaka 2006 wakipishana miezi mitano, akitangulia mama yake aliyefariki mwezi Aprili, kisha Septemba kufuata baba'ake, alisema licha ya kuwepo kwenye sanaa kusaka fedha, hayupo tayari kuchojoa nguo, ili acheze filamu za X.
Kimwana huyo, anayewazimia Irene Uwoya na Ray, alidai hawezi kucheza X hata akiahidiwa kiasi gani cha donge la fedha, kwa vile anajiheshimu na kujithamini kama mwanamke.
Aliwaasa wenzake, kujiheshimu na kuepukana na matendo machafu, aliyodai huwavunjia hadhi mbele ya jamii, na kusababisha sanaa yao kuonekana kama kazi ya wahuni wakati sio kweli.
Alisema, umaarufu wa msanii hupatikana kupitia ubora wa kazi zake na sio skendo chafu.
Skyner aliiomba serikali iwasaidie wasanii nchini kuweza kupambana na maharamia wanaowaibia kazi zao na kuwafanya wasanii wafe maskini tofauti na wenzao wa mataifa mengine.
Kadhalika, aliiasa jamii kuwa bega kwa bega na wasanii kwa kununua kazi zao halisi mara zitokapo, badala ya kukubali kuuziwa kazi feki, kitu kinachochangia wasanii kunyonywa na kuwafanya washindwe kusimama kimaisha na kiuchumi.

Mwisho

Azam yagomea nyota wake kwenda likizo, kisa...!

WAKATI nyota wa Simba na Yanga wakipewa likizo fupi ya kupisha mchezo wa timu ya taifa, Taifa Stars dhidi ya Morocco utakaochezwa ugenini mwezi ujao, uongozi wa Azam umewagomea mastaa wake, ukisisitiza kuwa timu yao itaendelea kujifua kama kawaida.
Simba kupitia Afisa Habari wake, Ezekiel Kamwaga, imetangaza kuwapa likizo ya wiki moja wachezaji wao, ili kupumzika kabla ya kurejea tena kujiandaa na pambano dhidi ya African Lyon litakalochezwa Oktoba 16, jijini Dar es Salaam.
Klabu hiyo imewapa likizo wachezaji hao baada ya kazi nzuri waliyofanya kwa kuiweka kileleni mwa msimamo timu yao ikiwa na pointi 18 kutokana na kucheza mechi nane bila kupoteza hata moja, ikishinda mechi tano na kutoka sare mechi tatu, .
"Wachezaji wetu tumewapa likizo ya muda mfupi, kabla ya kurejea tena kuanza maandalizi dhidi ya mechi yetu ijayo na zile zilizosalia katika ligi hiyo," alisema Kamwaga.
Hata hivyo timu inayoifukuzia Simba katika msimamo wa ligi hiyo, Azam imesema hawaendi mapumziko kama timu nyingine, bali wataendelea kujifua kujiandaa zaidi kwa mechi zao zijazo kabla ya kumaliza duru la kwanza mnamo Novemba 5.
Katibu wa Azam, Nassor Idrissa, alisema nyota wa timu yao wataendelea kufanya mazoezi kama kawaida, licha ya kwamba hawatakuwa na mchezo wowote hadi Oktoba 15 dhidi ya 'maafande' wa JKT Ruvu.
"Nyota wetu hawataenda likizo, wataendelea kujifua mazoezi kulingana na programu za kocha kwa nia ya kuwaweka sawa wachezaji kwa mechi zilizosalia za kumalizia duru la kwanza," alisema.
Idrissa maarufu kama 'Father' alisema yapo makosa ambayo yalikuwa yakifanyika katika kikosi chao, hivyo muda uliopo utatumiwa na benchi lao la ufundi kuweka mambo sawa kabla ya kurejea tena dimbani wakiwa moto kuliko hivi sasa.
Azam iliyopanda Ligi Kuu msimu wa 2008-2009, ndiyo inayoshikilia nafasi ya pili katika msimamo wa ligi ikiwa na pointi 15, tatu zaidi ya vinara Simba.

'Vijana wa Kova' wamsajili Mnigeria Ligi Daraja la Kwanza

MABINGWA wa Ligi ya TFF-Taifa, Central Stars (Polisi-Dar es Salaam), imetangaza kuwaongeza wachezaji sita wapya akiwemo Mnigeria kwa ajili ya Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara inayotarajiwa kuanza Oktoba 15 katika vituo vitatu tofauti.
Uongozi wa timu hiyo umedai, umewaongeza wachezaji hao kwa lengo la kuipa nguvu timu yao inayoendelea kujifua kwenye uwanja wa Chuo cha Polisi, Kurasini kuhakikisha inakuwa miongoni mwa klabu zitakazopanda Ligi Kuu msimu ujao.
Katibu wa timu hiyo, Ngello Nyanjaba, aliiambia MICHARAZO kuwa, wachezaji hao wapya waliongezwa ni Mnigeria, Felix Ameche, Msiba Joto, Paul Skazwe, Juma Sedege na Awadh ambao tayari wameorodheshwa kwenye usajili wa timu yao.
Nyanjaba, ambaye pia ni kocha wa timu hiyo ya Polisi, alisema wachezaji hao wapya wataungana na nyota 22 wa kikosi hicho waliopandisha daraja timu hiyo kwa ajili ya ligi hiyo, akisema walitarajia kuwasilisha usajili wao wakati wowote kuanzia leo.
"Tunaendelea vema na maandalizi ya ligi daraja la kwanza, ambapo tangu turejee toka Tanga tunaendelea kujifua kwa mazoezi, lakini kubwa ni kuongeza wachezaji wapya sita akiwemo Mnigeria kwa lengo la kufanya vema kwenye michuano hiyo," alisema.
Michuano hiyo itakayochezwa kwa mtindo wa nyumbani na ugenini itashirikisha timu timu 18 zilizopangwa katika makundi matatu, ambapo Polisi-Dar, imepangwa kundi A na timu za Mgambo-Tanga, Morani-Manyara, TMK United na Transit Camp za Dar na Burkina Faso ya Morogoro.
Kundi B lina timu za Majimaji-Songea, Mbeya City Council, Mlale JKT-Ruvuma, Polisi- Iringa, Small Kids-Rukwa na Tanzania Prisons ya Mbeya.
Timu nyingine zitakazoshiriki ligi hiyo ni pamoja na 94 KJ ya Dar, AFC-Arusha, Polisi-Morogoro, Polisi-Tabora, Rhino Rangers-Tabora na Samaria-Singida, zilizopangwa katika kundi C.

Mwisho

Kaseba, Oswald kumaliza ubishi kesho Dar


MABONDIA Japhet Kaseba na Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo', leo wamepima uzito tayari kumaliza ubishi katika pambano lao linalofanyika kesho jijini Dar es Salaam.
Kaseba na Oswald watapigana kwenye pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 la uzani wa Middle, litakalofanyika kwenye ukumbi wa Travertine Hoteli, Magomeni.
Pambano hilo lililoandaliwa na mratibu Gervas Muganda chini ya usimamizi wa Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Tanzania, PST, litasindikizwa na mapambano kadhaa ya utangulizi yakiwemo yale ya mchezo wa kick boxing.
Mabondia hao kwa nyakati tofauti wametambiana kila mmoja akitamba ni lazima aibuke mshindi katika pambano hilo kutokana na anavyomchukulia mpinzani wake, sambamba na maandalizi wanayofanya.
Oswald, alisema kwa uzoefu alionao ni wazi atammaliza Kaseba raundi za awali, huku Kaseba, licha ya kukiri mpinzani wake ni 'ngangari', ila anaamini atampiga.
"Ni kweli Oswald ni mzuri na mzoefu wa ngumi, ndio maana amesaini mapambano mawili dhidi yangu na la Rashidi Matumla, lakini kwa nilivyojiandaa nitamshinda tu," alisema Kaseba.
Oswald nae alisema anachotaka ni mashabiki wa ngumi kufurika ukumbini kuona namna Kaseba anavyorejeshwa kwenye kick boxing, kwa jinsi atakavyompiga.
Alisema anajiamini uwezo alionao katika ngumi ni vigumu kuzuiwa na Kaseba, akisisitiza kuwa atawathibitishia wadau wa ngumi kwa nini aliitwa 'Mtambo wa Gongo' na watu wa Malawi.
Michezo ya utangulizi itakayolisindikiza pambano la Kaseba na Oswald ni la bingwa wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini, Ernest Bujiku dhidi ya Mbukile Chuwa, Sweet Kalulu atakayepigana na Chaurembo Palasa na Venance Mponji kuzipiga na Jafar Majiha.

Villa kukutana J'pili, yamnyakua Habib Kondo

WAKATI wanachama wa Villa Squad wakitarajia kufanya mkutano wao mkuu keshokutwa, uongozi wa klabu hiyo umemnyakua kocha wa zamani wa Azam, Habib Kondo, ili kuokoa jahazi la timu yao linaloendelea kuzama katika Ligi Kuu Tanzania.
Makamu Mwenyekiti wa Villa, Ramadhani Uledi, aliiambia MICHARAZO kwamba klabu yao inatarajia kufanya mkutano wa wanachama kwa ajili ya kujadili mustakabali wa timu yao pamoja na mipango mingine ya kimaendeleo.
Uledi, alisema mkutano huo utafanyika Jumapili na kuwahimiza wanachama wake kuhudhuria kwa wingi kwa ajili ya kuisaidia klabu yao kuweka mikakati ya kuinusuru isishuke daraja.
"Tunatarajia kufanya mkutano wa wanachama siku ya Jumapili, kwa nia ya kujadili mustakabali wa timu yetu pamoja na mambo mengine ya maendeleo ya klabu yetu ikiwemo suala la uchaguzi mdogo wa kuziba nafasi zilizo wazi," alisema.
Aidha uongozi wa klabu hiyo umemnyakua aliyekuwa kocha wa timu ya Azam, Habib Kondo baada ya aliyekuwa kocha wao, Said Chamosi, kurejea kwao Kenya.
Kondo, alithibitisha kunyakuliwa kwake, akisema ameombwa na uongozi wa Villa kuisaidia timu yao, hadi atakapopatikana kwa kocha mpya mkuu wa kuinoa timu hiyo.
"Aisee ni kweli bwana, baada ya kufuatwa na viongozi wa Villa ili kuisaidia timu yao, nimekubali kuinoa kwa muda, wakati wakiendelea kusaka kocha mkuu wa kudumu, kwa wanamichezo kama sisi ni vigumu kukataa ombi kama hilo," alisema.
Kondo, alisema licha ya kuanza kuinoa timu hiyo kwa kupata sare ya 0-0 dhidi ya JKT Ruvu, bado itabidi afanye kazi ya ziada kuisaidia timu hiyo kutokana na ukweli nafasi iliyopo sio nzuri, ingawa ligi bado ipo katika duru la kwanza.
Nyota huyo wa zamani wa Reli-Morogoro na Sigara, ndiye aliyeipandisha daraja hadi ligi kuu timu ya Azam msimu wa 2008-2009 kabla ya kuwa msaidizi wa makocha wa kigeni walioinoa timu hiyo kwa vipindi tofauti akiwemo kocha wa sasa Stewart Hall.

Timu za 'Maafande' zaitisha Azam Ligi Kuu T'Bara


TIMU ya soka ya Azam, imedai inakoseshwa usingizi ndani ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu na kasi ya timu za jeshi, kuliko na vigogo vya Simba na Yanga.
Aidha klabu hiyo imeisifia safu yao ya ulinzi ambayo hadi sasa imeruhusu mabao mawili, ikiwa ndio timu pekee iliyofungwa mabao machache katika ligi hiyo.
Uongozi wa klabu hiyo, umesema mwenendo wa timu hizo za majeshi zilizopo katika ligi hiyo, umeifanya ligi ya msimu huu, kiasi cha kuwanyima raha wakizifikiria.
Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Nassor Idrissa 'Father', aliiambia MICHARAZO juzi kuwa, licha ya Simba na Yanga kuonekana tishio kwa klabu nyingine, wao Azam wanazihofu timu za JKT Oljoro, JKT Ruvu na Ruvu Shooting kwa jinsi zilivyo na upinzani mkali.
Idrissa, alisema timu hizo zimekuwa na upinzani mkali na kucheza soka la kusisimua na kutofungika kirahisi kitu kinachoifanya Azam zikiangalie kwa umakini timu hizo kuliko Simba na Yanga.
"Kwa kweli ligi ya msimu huu ni ngumu na yenye kusisimua na kati ya timu zinazotunyima raha ni timu za maafande ambazo zimekuwa na upinzania mkali na zenye kucheza soka la kusisimua," alisema Idrissa.
Alisema, timu hizo zimekuwa na matokeo bora zikiwa dimba la nyumbani au ugenini, na kudai uthibitisho wa ukali wao hata ukiziangalia kwenye msimamo zinafuata zikitofautiana kwa pointi chache na timu zilizopo juu.
Aidha Idrissa, aliipongeza safu ya ulinzi ya timu yake kwa kuruhusu kufungwa idadi ndogo ya mabao,ikiifanya iongoze kwa kuwa na ukuta mgumu hadi sasa nchini.
Azam katika mechi nane ilizokwishacheza hadi sasa imeruhusu mabao mawili, huku ikifuatiwa na Simba iliyoruhusu kufungwa mabao manne hadi hivi sasa.
"Kwa kweli tunaipongeza timu yetu na hasa safu ya ulinzi kwa kasi nzuri iliyofanya kwa kuruhusu mabao machache, naamini kwa mwenendo huu tunaweza kutimiza ndoto za kutwaa ubingwa au kuwa wawakilishi wa nchi kimataifa mwakani," alisema Idrissa.

Mwandido kuja nchini kuzindua kibao cha Assosa


MWANAMUZIKI nyota wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Ny'boma Mwandido anatarajiwa kuja nchini kutumbuiza kwenye uzinduzi wa kitabu cha gwiji la muziki wa dansi nchini, Tshimanga Kalala Assosa kiitwacho 'Jifunze Lingala'.
Uzinduzi wa kitabu hicho unatarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam, ingawa tarehe na jina la ukumbi, bado hazijawekwa bayana.
Akizungumza na MICHARAZO juzi, Assosa, alisema mipango ya uzinduzi wa kitabu chake yanaendelea vema ikiwemo kufanya mpango wa kumleta Ny'boma, aliyewahi kufanya naye kazi katika bendi mbalimbali nchini Congo, ili kushiriki uzinduzi huo.
Assosa alisema tayari wameshakubaliana na gwiji hilo linalotamba na nyimbo kama 'Double Double', 'Masua' na 'Abisina' kuja katika uzinduzi huo, kinachoendelea kwa sasa ni kumtafutia tiketi ya ndege ya kumleta na kumrejeshwa baada ya shughuli hiyo.
"Maandalizi ya uzinduzi wa kitabu changu yanaendelea vema, ambapo natarajia kuja

kushindikizwa na Ny'boma Mwandido, ambaye ameafiki mualiko wetu na kuhitaji tumtumie tiketi ya ndege," alisema Assosa.
Assosa, anayemiliki bendi ya Bana Marquiz, alisema umoja wao wa Wana 'Dar Kavasha Club', unafanya mipango ya kuisaka tiketi hiyo pamoja na ufadhili kwa ajili ya shughuli nzima ya uzinduzi wa kitabu hicho ambacho tayari kipo mtaani karibu miezi sita sasa.
"Kwa sasa tunasubiri majibu ya maombi yetu ya udhamini tuliotuma katika makampuni ya masharika mbalimbali ili kufanikisha uzinduzi huo utakaoenda sambamba na burudani ya muziki," alisema.
Aliongeza mbali na kitabu hicho cha 'Jifunze Lingala-Toleo la Kwanza', pia tayari ameanza maandalizi ya toleo la pili la kitabu hicho na na kile kinachohusu maisha yake binafsi.
Vitabu vyote vinafadhiliwa Klabu ya Dar Kavasha, umoja ambao Assosa ameomba mashabiki wa miondoko hiyo mikoani kuanzisha matawi yao, ili kuupanua zaidi.

Mwisho

Monday, September 26, 2011

Golden Boy, kuzinyuka na Miyeyusho

BINGWA wa UBO-Mabara, Mbwana Matumla 'Golden Boy' anatarajia kupanda ulingoni mwezi ujao kuzipiga na bondia Francis Miyeyusho katika pambano la kutetea taji lake litakalofanyika jijini Dar es Salaam.
Pambano hilo la uzani wa Bantam litakalokuwa la raundi 10, litafanyika Oktoba 30 kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee, likisindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Kwa mujibu wa kocha msaidizi wa kambi ya Kinyogoli Foundation inayowanoa mabondia watakaosindikiza pambano hilo la Matumla na Miyeyusho, Rajab Mhamila ni kwamba maandalizi ya pigano yanaendelea vema.
Mhamila, alisema pamoja na kwamba pambano hilo ni la kuwania taji la UBO, lakini pia limewagawa mashabiki wa ngumi kulingana na mahali wanapotoka mabondia hao nyota, ambapo Matumla yeye anatokea Temeke na Miyeyusho akitokea Kinondoni.
"Pambano la Matumla na Miyeyusho ni kama la watu wa Temeke na Kinondoni, huku yale ya utangulizi yatahusisha mabondia wa pande hizo mbili, hali inayofanya pigano hilo lijalo kuwa na msisimko wa aina yake," alisema Mhamila.
Mhamila, alisema pambano hilo la UBO limeratibiwa na Mood Bawazir wa kampuni ya Dar World Links na litasindikizwa na michezo ipatayo mitano ya utangulizi kati ya hiyo ni pigano linalosubiriwa kwa hamu kati ya Ramadhani Shauri wa Kinondoni dhidi ya Issa Sewe kutoka Temeke.
Pigano hilo la Matumla, linakuja miezi minne tangu bondia huyo alipopanda ulingoni na kulitetea taji lake hilo kwa kumchakaza Mkenya, Gabriel Ochieng katika pambano lililofanyika Mei Mosi, kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam.
Mabondia wote wawili yaani Matumla na Miyeyusho kwa sasa wapo kambini wakijifua kwa ajili ya pambano hilo, kila mmoja akitamba kuibuka na ushindi siku ya pigano hilo.

Mwisho

Maugo kuzichapa na Mkenya



BONDIA machachari wa ngumi za kulipwa nchini, Mada Maugo anatarajiwa kupanda tena ulingoni jijini Mwanza kuzipiga na Mkenya, ikiwa anatokea kuuguza kipigo toka kwa Francis Cheka.
Aidha bondia huyo amesema hayupo tayari kupigana tena na Francis Cheka, labda kama mwamuzi na majaji watakuwa ni wa kutoka nje ya nchi kwa kile alichodia waamuzi na majaji wa nchini humbeba mpinzani wake kila mara.
kizungumza na MICHARAZO, Maugo, alisema pambano hilo la Mkenya Mosses Odhiambo litafanyika Novemba kwenye uwanja wa CCM Kirumba.
Maugo, alisema pambano hilo lisilokuwa la ubingwa la raundi 10 na la uzani wa kati, ni maalum kwa maandalizi ya kwenda kupigana nje ya nchi katika pambano la kimataifa dhidi ya Mjerumani.
"Natarajia kupanda ulingoni mwezi Novemba kupigana na Mkenya katika pambano la raundi 10 la uzito wa kilo 72, lisilo la ubingwa kwa nia ya kujiweka fiti kabla ya kwenda kupigana ngumi za kimataifa dhidi ya Mjerumani," alisema Maugo.
Kuhusu kurudiana na Cheka, Maugo alisema atakuwa radhi kufanya hivyo kama majaji na waamuzi watatoka nje ya nchi kwa madai wa ndani humbeba mpinzani wake kama ilivyotokea kwenye mechi zao mbili ambapo zote alipigwa kwa pointi.
"Sintakuwa tayari kupigana tena na Cheka, labda kama waandaaji watawaleta majaji na mwamuzi kutoka nje, mpinzani wangu wamekuwa akibebwa ndio maana rekodi yake nje ya nchi ni mbovu tofauti na anavyotamba akicheza nyumbani," alisema.
Alisema wiki iliyopita akifuatwa na mmoja wa mapromota akiwataka wapigane na Cheka katika pambano la kusaka mbabe kati yao, na kuweka msimamo wake huo, hali iliyofanya muaandaji huyo kuamua kuachana na wazo la kuwapiganisha tena.
Maugo alipigwa kwa pointi na Cheka katika mapambano yaliyofanyika Januari Mosi, jijini Dar es Salaam na Septemba Mosi, mjini Morogoro, ambapo kote bondia huyo alikuwa akilalamikia 'kuchakachuliwa' matokeo.

Anti Fifi: Jimama linalotesa Bongo Movie, sasa ageukia utunzi wa vitabu







WAKATI mastaa wenye majina na umaarufu mkubwa kama wake nchini hupenda kuishi maisha 'bandia' ya kuhofia kujishughulisha na kazi au kujichanganya na watu
wengine wa kawaida, kwa Tumaini Biligimana au 'Anti Fifi', hali ni tofauti.
Licha ya umaarufu alionao kupitia sanaa aliyoanza kuifanya zaidi ya miaka 20 akianzia kama promota wa urembo, disko na muziki wa kizazi kipya, Anti Fifi anauza 'genge' la chakula eneo la Mwananyamala, alipika na kuuza mwenyewe.
Pia, nyota huyo haoni aibu kula 'chips dume' (mihogo ya kukaanga) au kupanda daladala katika mizunguko yake jijini Dar, licha ya kumiliki gari zuri la kisasa.
"Siwezi kuhofia kuishi nilivyozoea kwa sababu ya jina kubwa, kuishi 'bandia' ndiko kunakoponza mastaa wengi kuishia kwenye machafu wakitafuta mkato ya maisha ili waonekane bab'kubwa," alisema.
Alisema, tangu alipoanza kupata umaarufu hajawahi kuona aibu kujichanganya na watu wengine, jambo alilodai limemrahisishia mambo yake mengiu kimaisha na kisanii.
Anti Fifi, aliyefanya kazi na madansa wa nyota wa zamani kama Black Mosses, Master
Flash na wengine, alisema kitendo cha kupika na kuuza chakula katika mgahawa wake kumemfanya apate wateja wengi, baadhi wakienda ili kujiridhisha kama kweli ni yeye au wanamfananisha na mtu wanayemuona kwenye filamu.
Msanii huyo alisema anavyofahamu yeye, ustaa wa mtu kujizuia na matendo machafu na ya aibu mbele ya jamii, ila sio kuogopa kujichanganya au kuishi vile mtu apendavyo au alivyozoea.
"Ustaa ni kujiheshimu, kujithamini na kujichanganya na watu ili kujifunza mengi toka kwao yanayoweza kumsaidia msanii katika kukuza sanaa yake, sio kuishi maisha bandia ya hadhi ya juu, ilihali uwezo huo mtu hana," alisema.
Muigizaji huyo ambaye pia, ni mtunzi, mtayarishaji na mwandishi wa vitabu, alisema mbali na kuuga mgahawa, pia anajiuza mayai ya jumla katika nchi jirani, sambamba na nguo na vipodozi vya wanawake na watoto.
Alisema anaamini wasanii wakiamua kuishi jinsi walivyo kabla ya kupata umaarufu wanaweza kujiepusha na skendo chafu ambazo zimekuwa ni mazoea kwao na kuitia doa sanaa yao kwa ujumla.
"Sijisifii, ila mie ni baadhi ya wasanii wanaojiheshimu kwa vile naishi jinsi nilivyo, hivyo sikumbwi na skendo kwa kusaka umaarufu, bali kazi zangu ndizo zinazonipa 'ujiko' mbele ya jamii, kama unavyojua majuzi tu filamu niliyotunga ya 'Senior Bachelor' ilitwaa tuzo ZIFF."
Anti Fifi anayependa kula ugali kwa samaki na dagaa na kunywa juisi ya karoti na passion, alisema tangu atumbukie kwenye sanaa amenufaika kwa mengi, ikiwemo umaarufu, kujenga nyumba, kumiliki gari na kiwanja alichoanza kukijenga nyumba nyingine eneo la Mbezi.
"Najivunia sanaa pia, imenisaidia kuweza kutunga na kuuza hadithi za filamu, huku kwa sasa nikiwa nimetumbukia kwenye utunzi wa vitabu, nikijiandaa kutoa kitabu kiitwacho 'Migogoro ya Ndoa na Suluhisho Lake'," alisema.
Anti Fifi, aliyewahi kuishi maisha ya ndoa ya kiislam kuanzia mwaka 1989-2001 alipoachika, alisema matarajio yake ni kutaka kujitofautisha na wasanii wengine nchini akitaka kuwa mtunzi mahiri wa vitabu na filamu kwa ujumla.
Anti Fifi, aliyeokoka kwa sasa, alisema kama angekutana na Rais angemuomba asaidie kuiinua sanaa nchini na kukomesha uharamia, ili inawanufaishe wasanii.
"Hata mimi ningekuwa Rais ningeyafanya hayo, pamoja na kuondoa kero ya umeme nchini, kwani ni aibu kwa Tanzania yenye vyanzo vingi vya kuzalisha nishati hiyo kuwa na tatizo la ukosefu wa umeme na kuliingiza taifa kwenye hasara kubwa,: alisema.
Tumaini Biligimana, aliyezaliwa Julai 17, 1965 mjini Kigoma, akiwa mtoto wa sita kati ya 13 wa Mzee Biligimana, alisema hakuna tukio la furaha kwake kama aliposhiriki filamu ya Dar es Salaam akiigiza kama Jimama la Kikongo, linaloendesha genge la mabinti wahalifu, kiasi cha kufuatiliwa na Polisi, waliodhani huenda ndivyo alivyo.
"Huwezi amini nilifuatiliwa na Polisi kwenye duka na saluni yangu wakinipeleleza kwa kile walichokiona kwenye filamu hiyo niliyoiigiza mara nilipotua Dar nikitokea Kigoma," alisema.
Kisanii, Anti Fifi mwenye watoto watatu, Mohamed, 24 anayesoma kidato cha tano nchini Uganda, Omari, 21 anayesomea ufundi VETA na Zamda, 17 aliyepo kidato cha pili Shule ya Sekondari Kunduchi Beach, alianza tangu shuleni akicheza ngoma, kuimba na kupiga filimbi.
Alisema pia alikuwa mahiri wa kuchora, kubinuka sarakasi wakati wakisoma Shule ya Msingi Muungano na baadae Ujiji Sec, kabla ya kuajiriwa serikalini kama Mhasibu katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kigoma.
Baada ya miaka tisa ya utumishi wa umma, aliacha kazi hiyo na kujikita katika biashara akiwa promota wa fani ya urembo na disko, hadi mwaka 2001 aliposhiriki uzinduzi wa filamu ya Girlfriend na kupata kiu ya kuwa muigizaji baada ya kukutana na George 'Tyson' Otieno.
Alianza fani hiyo kwa kutunga na kuigiza filamu ya kwanza iitwayo Haraka ya Maisha ya mwaka 2002 kabla ya kuja Dar miaka miwili baadae kujiunga na kundi la Fukuto Arts na kushiriki filamu ya Dar es Salaam iliyomfungulia neema ya mafanikio.
Kazi nyingine alizoshiriki ni pamoja na Copy, Sound of Death, Senior Bachelor, I Deserve It, Kaburi la Mapenzi, Kizungumkuti, Fake Smile, Daddy, na nyinginezo baadhi akizitunga.
Anti Fifi anayechizishwa na rangi ya zambarau na pinki, alisema anawazimia Jacob Stephen 'JB', Irene Uwoya na Aunty Ezekiel, aliwaasa wasanii wenzake wajitume na kujichanganya kusaka maisha nje ya sanaa zao, kwa lengo la kuepusha kutumiwa ovyo.

Watanzania hawana utamaduni wa kusoma-EZAA





CHAMA cha Waandishi wa Vitabu Kanda ya Mashariki, EZAA, kimesema asilimia kubwa ya watanzania hawana utamaduni wa kupenda kusoma vitabu, jambo linalochangia kuwepo kwa ugumu wa soko la vitabu nchini.
Katibu Mkuu wa chama hicho, Jackson Kalindimya, aliyasema hayo wakati wa semina ya siku tatu ya watunzi wa vitabu vya hadithi za watoto, iliyofanyika kwenye ukumbi wa Msukuma, mjini Mlandizi, Pwani.
Kalindimya alisema Tanzania ina tatizo la watu kupenda kusoma, kitu ambacho kwa kiasi kikubwa kimekuwa kikiathiri soko la vitabu na maandishi mengi.
Hata hivyo, aliwaasa waandishi na watunzi wa vitabu kutokata tamaa badala yake kuzidi kuandaa kazi zenye mvuto ambavyo zitachochea wananchi kubadilika na kuanza kupenda kusoma kama ilivyo kwa mataifa mengi.
Kalindimya alisema tofauti na wananchi wa mataifa mengine ambao wawapo safarini au mahali popote hubeba vitabu au majarida kwa ajili ya kujisomea, kwa wananchi wa Tanzania ni wachache wanaofanya hivyo, kitu alichotaka watanzania wabadilike.
"Wananchi wanapaswa kubadilika na kujenga tabia ya kupenda kusoma kwani itawasaidia kuelimika, sambamba na kusaidia soko la kazi za waandishi," alisema.
"Licha ya hali hiyo, watunzi na waandishi msikate tamaa, muikabili changamoto hiyo kwa kuandaa kazi zenye mzuri zenye mvuto ambazo zitawabadilisha wananchi, pia ikirahisisha soko la kazi zenu," alisema.
Baadhi ya washiriki wa semina hiyo, ambao ni chipukizi katika utunzi na uandishi wa vitabu, waliwapongeza waandaaji wake kwa namna walivyowasaidia kuelewa mambo ambayo kabla ya hapo walikuwa hawana ufahamu nayo katika fani hiyo.

CBP yataka mrithi wa Shaaban Robert apatikane




WATUNZI na waandishi wa kazi za Fasihi nchini, wamepewa changamoto ya kujibidiisha katika fani zao, ili kumpata 'Shaaban Robert' mpya miongoni mwao atakayeendeleza na kudumisha fasihi katika kiwango alichokuwa nayo gwiji huyo.
Aidha jamii imeaswa kujenga utamaduni wa kuwanunulia na kuwasomea vitabu vya hadithi watoto wao kama njia ya kuchochea uwezo wao kuelewa na akili ambao utawasaidia katika masomo ya kitaaluma.
Katibu Mtendaji wa Mradi wa Vitabu vya Watoto Tanzania, CBP, Pili Dumea, ndiye aliyetoa wito huo kwa waandishi wakati wa ufungwaji wa semina ya siku tatu ya Waandishi wa Vitabu Kanda ya Mashariki, EZAA, iliyofanyika Mlandizi, mkoani Pwani.
Dumea, alisema watunzi na waandishi chipukizi wa kazi za fasihi wanapaswa kufanya kazi zao kwa umahiri, ili waweze kuja kumrithi Shaaba Robert, ambaye licha ya kufariki kitambo kirefu, bado amekosa wa kufikia umahiri wake katika fani hiyo.
"Semina na mafunzo haya yawe chachu kwenu katika kujibidiisha na kujituma katika fani hii mkiwa na lengo la kutaka kuwa warithi wa Shaaba Robert, ambaye licha ya kutokuwepo kazi zake zimeendelea kudumu milele," alisema Dumea.
Katibu huyo alisema CBP, ipo kwa ajili ya kuwasaidia watunzi na waandishi wa vitabu kufikia lengo la kuendeleza fasihi hasa vitabu vya hadithi vitakavyochochea maendeleo ya nchi kuanzia kwa watoto hadi watu wazima.
Pia, alisema jamii ni lazima iwe na utamaduni wa kuwasomea na kuwanunulia watoto vitabu kuwazoesha kusoma na kuchochea ufahamu wao na uwezo wao wa kimasomo darasani, akidai kusoma ni njia ya kusaidia uelewa na akili za mtu.
Naye Katibu Mkuu wa EZAA, Jackson Kalindimya, aliwaasa waandishi hao watumie vema uwezo wao wa 'kimungu' walionao katika kuchochea maendeleo ya nchi pamoja na kuijenga jamii katika maadili mema.
Kalindimya, alisema watunzi wa vitabu ambao wana uwezo wa kuumba dunia yao na viumbe wengine wakiwapa pumzi, tabia na uhusika unaoweza kuibadilisha jamii kutoka mahali pamoja hadi kwingine kimaendeleo na hata kimaadili kupitia kazi zao.
"Lazima mjivunie uwezo wa kimungu mlionao, kwa kuisaidia jamii kubadilika mahali ilipo hadi kwenye maendeleo, cha muhimu ni kutoa kazi nzuri zenye mvuto ambazo zitawafanya watu wazinunue na kuzisoma, kisha kuwabadilisha," alisema.

Mwisho

Wednesday, September 21, 2011

Kaseba amwinda Oswald


BONDIA mchachari nchini, Japhet Kaseba yupo katika maandalizi makali kwa ajili ya pambano lake dhidi ya mzoefu, Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo', akitamba kuwa anafanya hivyo ili kumzima mpinzani wake.
Kaseba na Oswald wanatarajiwa kupanda ulingoni kuzipiga katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 la uzani wa kati, litakalofanyika kwenye ukumbi wa Travertine, jijini Dar es Salaam.
Kila bondia amekuwa kwenye maandalizi ya pambano hilo, ambapo Kaseba, bingwa wa zamani wa dunia wa kick boxing, alikutwa na Micharazo kambini kwake, Mwananyamala Komakoma akijifua, huku akiapa kumshinda mpinzani wake.
"Kaka kama unavyoniona, nia yangu ni kutaka kurejesha heshima yangu katika ngumi kwa kutaka kumchakaza Oswald, siku tukikutana kwenye pambano hilo ambalo litasimamiwa na PST," alisema Kaseba.
Kaseba, alisema anaamini mazoezi anayofanya yatamwezesha kumnyuka Oswald ambaye kambi yake ipo Keko, ambapo amekuwa akisisitiza anataka kumshikisha adabu, muhimu mwamuzi amchunge Kaseba asirushe mateke yake.
Bondia huyo, alisema pambano lao na Oswald limeratibiwa na Gervas Muganda, litasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi ambapo aliyataja baadhi kuwa ni kati ya
Kaseba, alisema kabla ya pambano lake na Oswald ambaye amenukuliwa akitamba kumpiga akitaka waamuzi kumchunga asirushe mateke kwa kudhani yupo kwenye kick boxing, watasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Michezo hiyo ni pamoja na pigano la bingwa wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini, Ernest Bujiku dhidi ya Mbukile Chuwa.
Mapambano mengine ambayo yote yameandaliwa na mratibu, Gervas Muganda wa kampuni ya Babyface ni, Chaurembo Palasa dhidi ya Sweet Kalulu, Venance Mponji atapanda ulingoni kuzipiga na Jafar Majiha 'Mr Nice' na michezo miwili ya kick boxing.
Moja ya pambano hilo la Kick Boxing ni kati ya Ramadhani Mshana atapigana na Hamed Said na Kaseba alisema maandalizi yote kwa ajili ya michezo hiyo inaendelea vema.

Mwisho